Monday

DHANA YA KATEGORIA KATEGORIA ZA KILEKSIKA

0 comments

Dhana ya kategoria imejadiliwa kwa namna tofauti tofauti. Khamisi na Kiango (2002) wamegawa kategoria katika mitazamo miwili; Wanamapokeo na Wanausasa, ambapo Wanamapokeo walitumia dhana ya kategoria kumaanisha sifa bainifu ya vitu na wanausasa wanaona kategoria kuwa ni “zile aina za maneno kama vile nomino, vivumishi, vielezi, viunganishi, vihusishi na vitenzi”

Massamba, (2009) anatoa maana ya kategoria kwa kusema kuwa “Ni jumla ya maumbo, faridi au vipashio vingine ambavyo huchangia sifa fulani au ambavyo viko katika kiwango kimoja. Maana hii ni ya jumla kwani imeeleza dhana ya kategoria kwa ujumla bila kujikita katika kategoria miundo ambayo ndiyo sintaksia.

Massamba (khj)[1] anasema kuwa kategoria miundo ni“kategoria za mpangilio wa maneno ambazo ni muhimu katika tungo kama vile kirai nomino(KN), kirai kitenzi(KT), kirai kivumishi(KV) na kirai kielezi (KE).”

Fromkin na Rodman (1993) wanataja aina mbili za kategoria; phrasal categories and lexical categories (kategoria za virai na kategoria za kileksika-tafsiri ni yetu). Hivyo basi kulingana na nukuu hii kategoria za kisintaksia zinaweza kutazamwa katika viwango viwili; kategoria za kileksika na virai. Katika kazi hii aina zote mbili za kategoria za kisintaksia zitajadiliwa.

Kwa kuanza na kategoria ya kileksika, Kuna vigezo vya kiisimu ambavyo hutumiwa katika kuainisha aina za maneno. Besha, (2007) anasema kuwa “kumekuwa na mijadala mikali juu ya vigezo vinavyotumika kuainisha maneno ya lugha” hii inaonyesha kwamba hata vigezo ambavyo vipo sio vya kuaminika sana. Vigezo hivyo ni kama vile kigezo cha kifonolojia, kimofolojiakisintaksia na kisemantiki.

Kutokana na vigezo hivyo wataalamu mbalimbali wametofautiana katika idadi yake. Kwa mfano: “ Kapinga (1983), Nkwera (1978), Mohamed (1986), na Massamba na wenzake (1999) wameainisha aina saba ilhali Msokile (1992), Mgullu, R (1999), Mbaabu (2000), Rubanza (2003), Habwe na Karanje (2004) na Mdee na wenzake (2011) wameainisha aina nane za maneno katika lugha ya Kiswahili”(Matinde 2012:124).

Katika kazi hii aina za maneno ambazo zimejadiliwa ni: Nomino, Viwakilishi, Vitenzi, Vivumishi, Vielezi, viunganishi, vihusishi na viingizi.

Nomino (N) hii ni aina ya neno ambayo hutaja mtu,kitu, hali na dhana. Khamisi na Kiango(khj.28) wanasema kuwa “seti ya nomino iko wazi kwa kuwa milango yake iko wazi kupokea nomino mpya kadri zinavyojitokeza”.  Matinde, (khj.125) anathibitisha kuwa “kisintakisia nomino ni kategoria ya kileksika” nomino ziko za aina nyingi. Mfano wa nomino ni kama vile Tanzania, Juma, wadudu, kuimba na upendo.

Vivumishi (V), ni neno linalotokana na kitenzi ‘vuma’ kumaanisha kutoa sauti, kujulikana au kufahamika (Ndalu, A.E na wenzake 2014:760). Hivyo basi kivumishi ni neno linalotoa taarifa zaidi kuhusu nomino. Mifano ya vivumishi ni _refu, mamia, _angu na yupi.

Viwakilishi (W), Ndalu, A.E na wenzake (khj) wanasema kuwa maneno yote ambayo yanasimama badala ya nomino yanajulikana kama kiwakilishi, yaani yanawakilisha nomino fulani. Mfano wa maneno yanayosimama kama viwakilishi ni kama vile mimi, yule, wangapi, chake, kizuri, wengi na maelfu.

Vielezi (E), hii ni aina nyingine ya maneno ambayo huelezea zaidi kuhusu kitenzi. Katika lugha ya Kiswahili vitenzi hutokea katika sehemu ya kiarifu baada ya kitenzi. Kitenzi hujaribu kujibu maswali kama vile tendo lilifanyika wapi? Kivipi?Lini? Na mara ngapi.? Mifano yake ni kama vile; alfajiri, sanasana, harakaharaka, jana, nyumbani, mara kwa mara na polepole.

Vitenzi (T), hii ni aina nyingine ya maneno ambayo kazi yake ni kutoa taarifa ya tendeka kwa nyakati zote. Hii inamaanisha kwamba hutoa taarifa ya tendo linavyotendeka, lilivyotendeka na litakavyotendeka. Kwa mfano: kulima, kula, kulala, kusoma, kuimba, ni, aliyekuwa, alikuwa na si

Viunganishi (U), hii ni aina ya maneno ambayo yanaunganisha neno moja na lingine, kirai kimoja na kingine na sentensi moja na nyingine. Mara nyingi vimeundwa kwa mfumo ufuatao:-Viongezi, hivi ni viunganishi ambavyo huonekana kuongeza idadi na hutumika kuunganisha nomino, virai na sentensi. Kwa mfano: Maduhu anakula na kuongea.Viunganishi visababishi,hivi hudokeza usababisho wa hali fulani kwa mfano alifaulu kwa sababu alisoma sana.

Viingizi, ni aina ya maneno ambayo uamilifu wake huonyesha hisia za watu. Baadhi ya watalaamu wameviita vihisishi. Mfano Matinde (khj) yeye anatumia istilahi ‘vihisishi’. Viingizi hutofautiana kutegemea hisia za wazungumzaji na viko vya aina nyingi kutegemea na muktadha. Kuna vile vya mwitiko kwa mfano naam! Abee! Labeka! Vipo vinavyohusu shukrani kwa mfano alhamdulilah!Ahsante!, Kuna vingine vinahusu furaha kwa mfano oyeee! Haleluya!

Vihusishi (H), ni aina ya maneno ambayo huonyesha uhusiano baina ya matukio au matendo fulani ambapo tendo moja hukamilika baada ya lingine kutokea. Mifano yake ni kama vile; ‘walikimbia kwa amri ya jeshi.’

Kategoria ya virai,dhana ya virai imefasiriwa na wataalamu mbalimbali kwa namna tofauti tofauti. Baadhi ya wataalamu hutumia neno kikundi badala ya kirai. Mfano wataalamu kama Mohamed, M.A (1986:62), Mkude, D.J (2010:228-229) na Besha, R.M (2007:84) wametumia ‘kikundi’ badala ya ‘kirai’.  Hata hivyo kuna wataalam kama vile Massamba na wenzake (1999:84-118), Khamisi, A.M na Kiango, J.G (2002) na Matinde, R.S (2012:169) wametumia neno ‘kirai’ badala ya ‘kikundi’. Katika kazi hii neno ‘kirai’ litatumika kwa sababu kirai kinaweza kuwa neno moja au zaidi ilhali kikundi kinamaanisha neno zaidi ya moja.

Maana ya kirai imejadiliwa na wataalam mbalimbali, hata hivyo katika kazi hii maana ya Massamba na wenzake (khj)wanasema kuwa “kirai ni kipashio cha kimuundo chenye zaidi ya neno moja lakini ambacho hakina muundo wa kiimakiarifu”. Udhaifu wa tafsiri hii ni kwamba si lazima kirai kiwe zaidi ya neno moja bali kinaweza kuwa hata neno moja na kuendelea.

Kirai kimeundwa na sehemu kuu mbili: neno kuu ambalo ndilo linalotawala kirai chote, mfano ‘babu analima’ neno kuu ni ‘babu’ kwani ndilo linalotawala kirai na kijalizo ambayo ni maneno yanayojaliza neno kuu, kwa mfano ‘babu analima’ neno ‘analima’ ndilo kijalizo cha neno kuu.

Massamba na wenzake (khj) wanasema kuwa katika lugha ya Kiswahili kuna aina tano ya virai ambavyo ni virai-nomino, virai-vitenzi, virai- vivumishi, vira-vielezi na virai viunganishi. Hata hivyo Matinde, R.S (2012:169) ametabanaisha aina sita ya virai, ambapo kutoka kwa Massamba na wenzake ameongeza kirai kihusishi. Katika taaluma hii aina sita ya virai itajadiliwa:-

kirai-nomino, ni kirai ambacho ama kwa hakika muundo wake uko katika nomino. Hujengwa kwa nomino moja au zaidi au viwakilishi vya nomino, hudokeza taarifa inayohusu nomino au kiwakilishi cha nomino. Kirai nomino kina miundo tofauti tofauti:Nomino pekee kwa mfano;Mushi amekuja. Nomino mbili au zaidi zinazounganishwa na kiunganishi. Kwa mfano babanamama wanaishi.Nomino na kivumishi kimoja. Kwa mfano lori kubwa limeharibika.Kivumishi na nomino, kwa mfano;Yule jamaa aliumia. Pia kuna miundo mingine mingi ambayo ama kwa hakika si rahisi kuiweka yote katika kazi hii.

Kirai kivumishi, hiki ni kirai ambacho kimekitwa kwenye kivumishi, yaani neno kuu katika kirai hiki ni kivumishi. Muundo wake huwa ni wa kivumishi pekee yake au kivumishi na maneno mengine yanayoandamana nacho. mifano ya virai vivumishi ni kama vile: ile chai ni tamu sana, lile duka ni kubwa sana na Yule tajiri ni mkali vibaya!

Kirai kitenzi, hiki ni kirai ambacho huundwa kwa kitenzi na maneno mengine yanayohusiana na kitenzi chenyewe. Kirai kitenzi chaweza kuundwa na kitenzi kimoja kwa mfano; tumefika, kitenzi, nomino na kitenzi, kwa mfano; tunaomba wakuu kuwajibika, kitenzi na kielezi, kwa mfano; moto umewaka sana.

Kirai-kielezi, ni kirai ambacho muundo wake haukitwi kwenye neno kuu, yaani kielezi bali hukitwa kwenye baadhi ya maneno yanayofanya kazi pamoja na kielezi husika. Mara nyingi huchukuliwa kwamba kina miundo ya aina nyingi ambapo sasa si rahisi kuwa na kiini kimoja cha umiliki wa vipashio. Hivyo hakutakuwepo na miundo ya virai-vivumishi ila mifano yake ni kama ifuatavyo; leo asubuhi Sofia ataimba, Mzee hukoroma mara kwa mara.

Kirai-kiunganishi, hiki ni kirai ambacho muundo wake umekitwa kwenye uhusiano baina ya jina na kiunganishi. Neno kuu lake ni kiunganishi. Uhusiano wa kiunganishi na jina hudokezwa na matumizi ya: kwa,na, katikana kwenye. Katika lugha ya Kiswahili virai viunganishi huwa na muundo wa kiunganishi na kikundi jina. Kwa mfano: ilibidi aondoke kwa amri ya jeshi, walikula chakula katika hoteli ile, aliingia kwenye krabu, na alikamatwa na meno ya tembo.

Kirai-kihusishi, hiki ni kirai ambacho hudokeza uhusiano kati ya vitu vitu viwili au zaidi. Virai hivi hujikita zaidi katika vihusishi vya ‘a-unganifu. Hutumika pamoja na nomino ya mahali, nomino ya wakati au nomino dhahania. Kwa mfano: chukua simu juu ya meza, panya waliingia ndani ya shimo, hutaruhusiwa kuzungumza wakati wa kula

Kuna faida nyingi za kuwa na kategoria katika lugha; yaani kategoria za kisintaksia ambazo zimejadiliwa hapo juu kuwa ziko katika makundi mawili; kategoria za kileksika na virai. Mojawapo ya faida za kuwa na kategoria hizo ni pamoja na:-

Inasaida kupata sarufi inayojitoshereza kwa usahihi katika lugha. Lengo la uchambuzi wa kisitaksia ni kutafuta ukubalifu na usokubalifu wa tungo zisizo sahihi. Katika kujaribu kuchambua miundo ya lugha kwa kutumia mmilisi wa lugha fulani, mwanasarufi hujikuta ameshapata maarifa na kubaini ni miundo ipi iliyo sahihi na isiyo sahihi.

Vile vile inasaidia kuunda nadharia mbalimbali za kisintaksia. Kutokana na uchambuzi wa kategoria za kisintaksia kumepatikana nadharia kama vile sarufi miundo virai, sarufi geuza maumbo zalishi.

Inasaidia pia kujua aina za maneno. Mwanagenzi anapofanya uchambuzi wa kisintaksia inamsaidia kujua aina mbalimbali za maneno katika lugha husika. Kwa mfano nomino, Vitenzi, Vivumishi, vielezi, viunganishi na vihusishi ambayo pia anaweza kutumia katika taaluma nyingine za isimu.

Ukiachilia kujua aina za maneno faida nyingine ni kujua aina mbalimbali ya virai kwa mfano kirai nomino, kirai kitenzi, kirai kihusishi na kirai kiunganishi.

Kwa ujumla kategoria za kileksika na kategoria za virai zinahitaji kufanyiwa uchunguzi wa ndani zaidi na kuweza kubainisha vigezo vinavyotumika katika kuainisha. Hii inatokana na kwamba kuna baadhi ya maneno ambayo yanakuwa hayana maalum pa kuyaweka mpaka hapo tu utakapoyakuta katika tungo. Kwa mfano maneno yenye maana zaidi ya moja mfano ua linaweza kuwa kitenzi na linaweza pia kuwa nomino, hivyo inakuwa vigumu kwamba liwekwe katika kundi gani hasa linalositahili.

 

 

 

 

Marejeleo

Besha, R.M.(2007). Utangulizi wa Lugha na Isimu: Dar es salaam. Macmillan Aidan

Fromkin,V na Rodman, R (1993).An Introduction to Language: Florida. HBJC publisher

Khamisi, A.M na Kiango, J.G (2002). Uchanganuzi wa Sarufi ya Kiswahili. Dar es salam: Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.

Massamba, D.P.B. (2009). Kamusi ya Isimu na Falsafa ya Lugha. Dar es salaam: TUKI

Massamba, D.P.B. na wenzake (1999). Sarufi Miundo ya Kiswahili Sanifu (SAMIKISA): Dar es salaam: TUKI

Matinde, R.S (2012). Dafina ya Lugha: Isimu na Nadharia: Mwanza: Serengeti Educational publishers.

Mkude, D.J. (2010). Makala za Semina ya Kimataifa ya Waandishi wa Kiswahili: Uchambuzi wa Sentensi za Kiswahili.Dar es salaam: TUKI

Mohamed, M.A (1986). Sarufi Mpya: Dar es salaam: Press and publicity center.

 



[1] Khj-kama hapo juu


No comments:

Post a Comment