Tuesday

NADHARIA ZA USHAIRI

0 comments



.

Nadharia ni dhana ambayo imeweza kufasiliwa na wataalamu mbalimbali. Mathalani, Wamitila (2003) anafasili nadharia kuwa ni mawazo, dhana au maelezo yanayotolewa kuelezea hali fulani; chanzo chake, muundo wake utenda kazi wake na mwingiliano wake wa ndani na nje.

Vilevile, Sengo (2009) anafasili nadharia kuwa ni wazo kuu, fikra kuu, muongozo mkuu wa mtu, watu au jamii ya pahala fulani. Kwa mantiki hiyo, nadharia ni dira na mwongozo wa kulikabili jambo kifalsafa, kidini, kimantiki, kijamii na kiutamaduni.

Hivyo, kwa ujumla tunaweza kufasili dhana hii ya nadharia kuwa ni dira inayomwongoza msomaji/mhakiki kuhusu dhana, asili au chanzo cha jambo fulani ili kulikabili jambo hilo kifalsafa, kimantiki, kijamii na kiutamaduni.

Dhana ya ushairi nayo imeweza kufasiliwa na wataalamu mbalimbali kwa mikabala miwili tofauti, ambayo ni mkabala wa kimapokeo na mkabala wa kimamboleo. Wataalamu mbalimbali wa mkabala wa kimapokeo wameweza kufasili dhana ya ushairi kama ifuatavyo;

Amri Abeid (1954) anafasili kuwa ushairi au utenzi ni wimbo, hivyo kama shairi haliimbiki halina maana.  Katika fasili hii kinachosisitizwa zaidi ni suala la ulinganifu au urari wa vina na mizani katika utunzi wa ushairi au utenzi. Hivyo basi, kwa mtazamo wake anaona kuwa shairi lisipokuwa katika muundo wa urari wa vina na mizani halina hadhi ya kuitwa shairi.

Massamba, (2002) akimnukuu Shaban Robert, anasema kuwa ushairi ni sanaa ya vina inayopambanuliwa kama nyimbo, mashairi na tenzi zaidi ya kuwa na sanaa ya vina ushairi unaufasaha wa maneno machache au muhtasari. Katika fasili hii linasisitizwa suala la vina na lugha ya mkato katika sanaa ya nyimbo, mashairi na tenzi.

Aidha, kuhusiana na mkabala wa kimamboleo pia wapo wataalamu ambao nao wameweza kutoa fasili zao kuhusu dhana ya ushairi mfano;

Kahigi na Mulokozi (1973) wanafasili ushairi kuwa ni sanaa inayopambanuliwa kwa mpangilio maalumu na fasaha na wenye muwala, kwa lugha ya picha, sitiari au ishara katika usemi, maandishi au mahadhi ya wimbo ili kuleta wazo au mawazo, kufunza au kueleza tukio au hisia fulani kuhusu maisha au mazingira ya binadamu kwa njia inayogusa moyo.

Aidha, Njogu na Chimerah (1999) wanafasili ushairi kuwa ni sanaa ya lugha inayoeleza jambo au wazo kwa njia ya mkato na kwa namna inavyoteka hisia za msomaji au msikilizaji. Waendelea kuelezea kuwa maneno ya mashairi huteuliwa kimaksudi ili yalete taswira maalumu akilini mwa msomaji au msikilizaji. Maneno hayo hupangwa ili yatoe mdundo fulani wa shairi linapoimbwa, linaposomwa, linapoghaniwa au linaposemwa.

Hivyo basi, kutokana na dhana hii ya ushairi kufasiliwa na wataalamu mbalimbali wa mikabala miwili tofauti yaani mkabala wa kimapokeo na mkabala wa kimamboleo tunaweza kutoa fasili ya ujumla ya ushairi kuwa  ni kazi ya sanaa yenye kuandikwa au kuimbwa kwa kufuata kanuni za ushairi au kutofuata kanuni za ushairi ikiwa na maana kuwa ushairi waweza kuwa wa kimapokeo au wa kisasa ilimradi ushairi huo uwe na ujumbe kwa jamii fulani.

Ushairi simulizi ni utanzu unaojumuisha tungo zote zenye mapigo ya kimziki, mawazo, hisia na hoja, katika utanzu huu huwasilishwa kwa njia ya mdomo. Aidha, ushairi simulizi hutumika kupitisha maarifa au mafunzo ya jamii fulani kwa mfano nyimbo za jandoni, za harusi, za dini hutumiwa kupitisha au kuwasilisha mafunzo katika jamii husika.

Baada ya kufasili dhana mbalimbali zilizojitokeza katika swali hili, kuna nadharia mbalimbali zinazoelezea kuhusu asili ya ushairi simulizi, nadharia hizo zimegawanyika katika makundi mawili ambayo ni mtazamo wa Kiulaya na mtazamo wa Kiafrika. Kwa kuanza na mtazamo wa kiulaya ni kama ifuatavyo.

Nadharia ya ubadilikaji taratibu, Wamitila (2012) anaeleza kuwa mwasisi wa nadharia hii ni Charles Darwin, huyu alikuwa mwanabaiolojia katika karne ya 19. Alifanya utafiti kuhusu viumbe hai akaona sifa ya kufanya hivo ni kuangalia sifa ya kibaiolojia ya viumbe hai na akaona viumbe wote wana sifa zinazofanana, kwa hiyo nadharia hii ya kibaiolojia ikahamishiwa  kwenye fasihi, mawazo ya utafiti wa Darwin yalianza kuathiriwa na wanafunzi wake ambao ni Edward Tylor na James George Frazer. Wanafunzi hawa waliona kuwa kuna ukoo mmoja na jamii moja ambazo zilizagaa ulimwenguni kote. Baadae mawazo yao yalishadadiwa na wanazuoni kama vile John Roscoe – alifanya uchunguzi katika jamii ya Baganda, Edwin Smith na Andrew Dale walichunguza katika jamii ya Ila huko Zambia. Wataalamu hawa walichunguza utamaduni wa binadamu katika utafiti wao walikusanya simulizi kutoka jamii mbalimbali za Kiafrika, Asia na Amerika ambapo baada ya kukusanya simulizi hizo ikiwemo ushairi waligundua zilikuwa na ufanano wa  kimaudhui, wanamabadiliko wanaamini kuwa ushairi simulizi tulionao leo una asili moja isipokuwa zimekuwa zikibadilika kutokana na mabadiliko ya wakati. Aidha, ubora wa nadharia hii ni kwamba fasihi ya Afrika sawa na ile ya Ulaya isipokuwa hubadilika kutokana na wakati na mazingira.

Upungufu wa nadharia hii ni kwamba wanamabadiliko waliamini kuwa kila kitu kilichokusanywa katika fasihi kilihesabika kama masalia ya zamani au mabaki ya fasihi iliyotangulia. Pia, walijikita katika kuangalia kipengele cha maudhui na kusahau fani.

Nadharia ya msambao, nadharia hii imeasisiwa na wataalamu Jacob na Wilhem Grimm ambao walitafiti fasihi kutoka India, Afrika na nchini kwao Ujerumani, na walihitimisha kuwa kuna kufanana kwa fasihi hizo wakatoa maamuzi kwamba fasihi za kiafrika ni chimbuko kutoka kwa wazazi wenye asili na utamaduni wa India na Ulaya. baadae mawazo yao yaliendeleza na Maxmuller na Stith Thompson (1946). Wataalamu hawa walikubaliana kuwa tanzu mbili au zaidi za fasihi kutoka katika jamii mbili au zaidi zikionyesha vipengele au sifa zinazofanana ni kwa sababu kuna kipindi fulani huko nyuma jamii hizi ziliingiliana. Mwingiliano ambao ulisababisha jamii moja kuchota baadhi ya vipengele vya utamaduni mwingine (Finnegan 1970). Mfano jamii A na jamii B, jamii A ni ile ambayo imeendelea na ipo juu kiuchumi na jamii B ni jamii ambayo ni duni hivyo, jamii hizi zikiingiliana jamii B huweza huchota vipengele vya fasihi kutoka jamii A. Utamaduni unaenezwa kutoka jamii A kwenda kwa jamii B. Wamitila (2012) anaeleza kuwa  kiini cha nadharia hii ni fikira kuwa chochote kinachopatikana kina chanzo chake na mahusiano ya karibu ndiyo yanaathiri misuko, wahusiaka, visa, mada au hata matendo ya fasihi simulizi. Kutokana na nadharia hii wanamsambao waliona kuwa asili ya ushairi simulizi ulitokana na kuathiriana kwa jamii za Kiulaya na ukasambaa katika jamii za Kiafrika.

Ubora wa nadharia hii kwa mujibu wa Finnegan (1970) wanamsambao waliipa hadhi fasihi simulizi kwa kuchunguza muktadha kwa undani. Vilevile, nadharia hii ilionekana kuwa ya kisayansi zaidi, hivyo inaweza kuchunguzika tofauti na wanamabadiliko kwa akili ya mtu haiwezi kuchunguzika. Aidha, Udhaifu wa nadharia hii ni kwamba imepuuza fasihi ya Afrika. Kwamba fasihi ilisambaa kutoka nchi zilizostaarabika (ulaya) kwenda nchi zisizostaarabika (Afrika).

Nadharia ya uamilifu, kwa mujibu wa Walles na Wolf (1980) nadharia ya Uamilifu iliasisiwa karne ya 20 na Bronslav Malinowski. Malinowski alizingatia fasihi simulizi kwa mujibu wa uamilifu au utenda kazi wake. Nadharia ya uamilifu huzingatia kuwa fasihi simulizi ina utenda kazi katika mfumo wa jamii ambapo huwa imo. Hali hii ni sawa kwa vitanzu vyake vyote zikiwemo nyimbo. Kwamba, ijapokuwa mwanafasihi hujihusisha na usanifu wa kazi fulani ya fasihi, sambamba na hilo hujaribu kubainisha utenda kazi wa utanzu katika jamii anayoifanyia uchunguzi. Kutokana na nadharia hii tunaona kwamba kila jamii ina utamaduni wake wa kuwaongoza katika maisha yao ya kila siku mfano; jando na unyago, matambiko, harusi, mazishi na  kusalia miungu kuwa ndio chanzo cha fasihi.

Ubora wa nadharia ni kwamba umesaidia kuondoa mawazo kuwa chimbuko la fasihi mbalimbali ikiwemo ushairi ni mahali fulani bali ni kila jamii imekuwa na simulizi ambazo zina sawiri uzoefu wao wa kila siku katika nyanja mbalimbali kama vile kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni na kijamii. Pia, nadharia hii inatusaidia kujielewa na kuzielewa jamii zetu vizuri kwa kuyaelewa mazingira ya mila na desturi zetu katika jamii.

Baada ya kuangalia nadharia ya asili ya ushairi simulizi kwa mtazamo wa Kiulaya, zifuatazo ni nadharia za ushairi simulizi kwa mtazamo wa Kiafrika

Nadharia ya Uhulutishi, hii ni nadharia ambayo iliasisiwa na wanazuoni wa Kiafrika wenye mtazamo kuwa hata wageni wamechangia sana katika ukuzi wa fasihi simulizi ya Kiafrika. Miongoni mwa waasisi na wafuasi hawa ni pamoja na Mulokozi, Johson na Ngugi wa Thiongo. Nadharia ya uhulutishi inaleta uwiano wa kitaaluma na kuona kwamba ingawa kwa kiwango kikubwa mawazo ya wanazuoni wa kigeni yalitawaliwa  na dosari kadhaa, si kila walichokinena kuhusu Afrika, hususani utamaduni wa fasihi ya Kiafrika si kibaya. Pia, kwa mujibu wa wanazuoni wa nadharia hii, yaliyosemwa na wageni yanahitaji kuchambuliwa na kufanyiwa ufafanuzi wa kina. Hii ni kwa sababu ndani mwake kuna uzuri na dosari ya namna fulani, hayapaswi kupuuzwa kabisa. Nadharia hii inasisitiza kuwa mbinu ya kupata nadharia bora ni kuchanganya nadharia zote mbili ya Kiafrika na Kiulaya.

Ubora wa nadharia hii ni kwamba, ilichunguza na nadharia mbalimbali mfano nadharia kwa mtazamo wa Kiulaya wakaona sio kila walichokinena kuhusu Afrika kilikuwa kibaya au kupuuzwa. Pia, Udhaifu wa nadharia hii ni kuwa hawakuelezea asili ya ushairi simulizi.

Nadharia ya Kitaifa, nadharia hii iliasisiwa na Adebayo Babalola, Daniel Kunene na Clark. Nadharia hii ilizuka katika vuguvugu la kudai uhuru barani Afrika. Mfano Adebayo Babalola katika kitabu chake cha The Content and Form of Yoruba Ijala (1966). Ijala ina maana ya ushairi wa wawindaji katika jamii ya Wayoruba, alibainisha mbinu za kimtindo katika Ijala (ladha ya kishairi) pia matini ya mashairi ya Ijala katika lugha ya Kiyoruba na tafsiri ya mashairi katika lugha ya Kiingereza. Wanautaifa wanadai kuwa wananadharia waliopita hawakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu lugha za Kiafrika, kwa kiwango kikubwa waliathiriwa na dhana ya ukoloni na upendeleo wa kibepari kuwa Afrika ni bara la giza na la washenzi wasiokuwa na aina yoyote ya ustaarabu na walistahili kustaarabishwa na Wazungu kupitia mlango wa ukoloni. Katika nadharia hii wamejaribu kuondoa dosari ambazo nadharia zilizopita zimeshindwa kuondoa. Kutokana na kwamba wananadharia waliopita mara baada ya kutafiti hawakuwa tayari kuchapisha matokeo yao halisi ya utafiti bali kuyahariri matokeo yao. Na wanaona ni kosa kubwa kufanya utafiti bila kuwahusisha wahusika wa eneo la utafiti. Hivyo, ili kufahamu vyema historia ya fasihi simulizi ya kiafrika ni lazima kuhusisha wataalamu na wanazuoni wa taifa au jamii hiyo.

Ubora wa nadharia hii ni kwamba wanazuoni wenyeji walifanikiwa kueleza na kufafanua ufanisi wa mbinu mbalimbali za kimtindo katika fasihi hasa katika ushairi simulizi. Pia, walirekodi hali na muktadha wote wa utendwaji wa fasihi simulizi.

Hivyo basi, baada ya kuangalia nadharia mbalimbali zinazoelezea ushairi simulizi kwa mtazamo wetu tunaona kuwa nadharia ya Kitaifa ndio nadharia iliyo bora na faafu. Hii kwa sababu kila jamii ina utamaduni wake na jamii ya Waafrika ina utamaduni wao ambao ulikuwepo hata kabla ya ujio wa wageni. Kupitia utamaduni wao huo, waliweza kuwa na ushairi simulizi wao ambao waliutumia katika shughuli mbalimbali za kijamii, kama vile katika harusi, jando na unyago. Aidha, ushairi huo ulikuwa unafungamana na muktadha na utendaji wa jamii hiyo katika kuwasilisha kazi iliyokusudiwa kwa jamii fulani.

Kwa ujumla, ushairi simulizi umekua na kuenea kwa kasi katika jamii za Waafrika kutokana na fani hii ya ushairi kutumika katika nyanja mbalimbali kama vile katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii. Ushairi unadhima mbalimbali kwa jamii, mathalani kuburudisha, kuelimisha, kuomboleza, kubembelezea watoto na kuhamasisha watu kutenda jambo fulani, hivyo basi, fani hii haiwezi kutenganishwa na maendeleo ya jamii husika kwani kila jamii inapobadilika na utanzu huu pia hubadilika kulingana na jamii hiyo.







MAREJELEO

Abedi, K. A. (1954) Sheria za Kutunga Mashairi na Diwani ya Amri. Nairobi: Kenya Literature  Bureau.

Finnegan, R. (1970) Oral Literrature in Africa. Nairobi: Oxford University Press.

Kahigi, K.K na Mulokozi, M. M. (1973) Mashairi ya Kisasa. Dar es Salaam: Tanzania Publishing  House.

Massamba, D. P. B. (2002) Historia ya Kiswahili: 50 BK Hadi 1500 BK. Nairobi: The Jomo   Kenyatta Foundation.

Mulokozi, M.M. na Sengo T. S. Y. M (1995) History of Kiswahili Poetry A.D. 1000-2000. Dar es Salaam: Institute of Kiswahili Research.

Njogu, K. na  Chimerah, R.  (1999) Ufundishaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

Sengo, T. S. Y. M. (2009) Sengo na Fasihi za Kinchi. Dar es Salaam: AKADEMIYA.

Walles, R. A. na Wolf, A. (1987) The Contemporary Socialogy Theory. New York: Prentice Hall Publishers.

Wamitila, K. W. (2003) Kamusi ya Fasihi, Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus Publication Ltd.

______________(2010) Kichocheo cha Fasihi Simulizi na Andishi. Nairobi: English Press.

No comments:

Post a Comment