Tuesday

FASIHI YA WATOTO DHANA YA MTOTO

0 comments






a). Dhana ya mtoto ni pana na ina utata katika kuelezea maana yake kutokana na muktadha wa mtoa maana hiyo. Kwa mfano, wafuasi wa dini mbalimbali kama vile Wakristo, Waislamu, watu wazima, wazee kwa vijana hudai kuwa wao ni watoto wa Mungu, kwa maana hiyo mtoto hakui anabaki vilevile. Aidha, wapo wataalamu mbalimbali ambao wamefasili dhana hii ya mtoto.

TUKI (1981) wanafasili dhana ya mtoto kuwa ni mwanadamu au mnyama ambaye hajakomaa au ni jina analoitwa kiumbe ambaye amezaliwa na wazazi wawili. Fasili hii ina dosari kwani si kweli kuwa kila mtu ambaye amezaliwa na wazazi wawili ni mtoto bila kuangalia kigezo cha umri.

Ndalu na wenzake (2014) wanafasili kuwa mtoto ni kiumbe kizaliwacho hususani na mtu. Fasili hii ina mapungufu kwani hata kiumbe ambacho kimezaliwa na mnyama kama vile mbuzi anaweza kuwa mtoto wa mbuzi.

Kwa ujumla, mtoto ni mtu yeyote mwenye umri chini ya miaka kumi na nane (18). Aidha, Wafula (2010) katika kusaidia kuielewa dhana hii ya mtoto amewagawanya watu katika makundi makuu manne. Anadai kuwa rika la utoto ni miaka 0 – 17, rika la ujana ni miaka 18 – 34, rika la wazazi/utu uzima ni miaka 35 – 52 na rika la wazee ni miaka 53 nakuendelea. Hivyo basi, kwa mgawanyo huo mtoto ni mtu yeyote mwenye umri wa chini ya  miaka 18.

Pia, dhana hii ya fasihi ya watoto ni telezi kwani wataalamu wamepishana katika kuifasili. Aidha, Mpesha (1995) anasema fasihi ya watoto ni ile ambayo hulenga kuwafahamisha watoto kuhusu mambo mabaya, hisia na matarajio ya jamii hiyo. Dosari ya fasili hii kwamba imejikita katika kuangalia mambo mabaya tu hali ya kuwa fasihi ya watoto huweza pia kuburudisha, kuendeleza, kukuza na kurithisha utamaduni. Lakini pia, haijaweka wazi kuhusu hayo mambo mabaya ni yapi?

Hunt (1996), fasihi ya watoto ni ile inayolenga kiwango cha watoto kama msomaji wa fasihi hiyo. Kwahiyo, msomaji wa vitabu vya fasihi huwa ni watoto au mtoto aliyeandikiwa. Fasili hii pia ina dosari kwani fasihi ya watoto huweza kusomwa hata na watu wazima.

Weche (2002), anasema kuwa fasihi ya watoto ni kioo cha kumwongoza mtoto katika mambo yanayohusu  maadili. Pia anasema kuwa, fasihi hiyo inapaswa kukashifu tabia zisizo kubalika na kabainika katika jamii. Dosari ya fasili hii ni kwamba imezungumzia suala la kioo kama chombo cha kumwongoza mtoto lakini itambulike wazi kuwa kioo hakiwezi kumwonesha mtu kila sehemu ya mwili wake na akajirekebisha. Hii ikiwa na maana kuwa si kila maadili yanaweza kuzungumziwa katika fasihi ili kumwongoza mtoto.

NOUN (2010), wanasema fasihi ya watoto ni dhana ambayo inarejelea fasihi inayowalenga watoto pekee. Wanaendelea kusema, fasihi ya watoto huweza kuwa hadithi, ushairi, visakale na drama ambazo zimetungwa kwa ajili ya watoto wadogo. Fasili hii ina dosari kwani si kweli kuwa fasihi ya watoto ni lazima iwahusu watoto tu kwani kuna maudhui yanayopatikana katika kazi hizi lakini yanawahusu watu wazima.

Wamitila (2010), anasema kuwa suala la ufafanuzi wa fasihi ya watoto linaweza kueleweka kwa kukitwa katika mitazamo mikuu miwili. Mosi, fasihi ya watoto ni ile ambayo hadhira yake ni watoto. Pili, fasihi ya watoto ni ile ambayo msingi wa dhamira na kimaudhui huwarejelea watoto. Dosari ya fasili hii ni kuwa si kweli kwamba muda wote dhamira zake huwahusu watoto tu kwani wakati mwingine huwagusa hata watu wazima.

Kwa ujumla, tunaweza kusema kuwa fasihi ya watoto ni fasihi iliyoandikwa kwa kuwazingatia watoto kama hadhira lengwa. Hii ina maana kuwa hata mtu mzima anaweza akaisoma fasihi hii japo kuwa hadhira iliyozingatiwa zaidi ni watoto.

b).  Kwa kutumia kazi mbili za fasihi ya watoto ambazo ni Sababu mimi ni Mwanamke! iliyoandikwa na Ebraju (1999), pamoja na Kilio Chetu kilichoandikwa na Medical Aid Foundation (1995) tunaweza kueleza maana ya fasihi ya watoto kwa kurejelea kazi hizi kama ifuatavyo:

Kwa kumrejelea Mpesha (1995) anasema fasihi ya watoto ni ile ambayo hulenga kuwafahamisha watoto kuhusu mambo mabaya, hisia na matarajio ya jamii hiyo. Fasili hii inasawili na kile kilichozungumziwa katika vitabu hivi viwili. Mathalani, katika kitabu cha Sababu mimi ni Mwanamke! mwandishi anasema;

“Mwanangu” alisema baba, kwa upole, lakini bila shaka ni upole imara. “Mwanangu, wewe umekuwa mkubwa sasa. Mama yako anakuhitaji hapa nyumbani. Hana wa kumsaidia kuteka maji wala kuchanja kuni. Tena mtoto wa kike kutembeatembea kwenda shule si vyema sasa utabaki nyumbani! … Nenda ukaweke mkoba wako.” (Uk.12)

Haya ni miongoni mwa mambo mabaya ambayo yamezungumziwa kwenye fasili hii ambayo yamelenga kuwafahamisha watoto, ambapo inaonekana mtoto wa kike akakikatizwa masomo ili amsaidie mama yake kazi za nyumbani kwa kuwa tu yeye ni mwanamke. Vilevile, haya yanasawili kupitia kitabu cha Kilio Chetu ambapo mwandishi anasema;

“JUMBE: Siyo zamani akina mama utasikia: vibaya kuangalia magazeti ya mapicha ya uchi mtaota…sinema za “ X” ni kwa wakubwa tu siku hizi tunaangalia vyote, nani anaota?

WOTE: Hakuna

JUMBE: Twenzetuni tuwahi picha, senti zako tu (wanaondoka)”    (Uk.20).

Hii tunaona kuwa watoto wamekuwa wakifanya mambo mabaya ambayo hapo awali walikuwa wakikatazwa na wazazi wao.

Kwa kupitia vitabu hivi vya fasihi ya watoto tunaona kuwa vimeweza kufanikisha kufasili fasihi ya watoto kuwa ni ile ambayo hulenga kuwafahamisha watoto kuhusu mambo mabaya, hisia na matarajio ya jamii hiyo.

Lyimo (2016), anasema kuwa fasihi ya watoto ni fasihi ambayo walengwa wake wakuu ni watoto. Aidha, kwa kudhihirisha hili mwandishi wa kitabu cha Sababu mimi ni Mwanamke! anasema;



“Sara! Aisha! Dora! Mko wapi? mnanisikia?... wapi! Sauti yangu haifiki popote. Inachimbuka ndani kwenye nafsi yangu. Inanitambaa ndani ya mawazo yangu. Ina nguvu sana. Lakini wapi? Sauti ya mtoto tena mtoto wa kike! Kwanza ni aibu kutoa sauti. Pili haifiki popote.” (Uk. 2)

Kwa mfano huo, ni dhahiri kuwa fasili hiyo ya fasihi ya watoto ambayo walengwa wake wakuu ni watoto ambapo tunaona hata mhusika mkuu wa kitabu hiki ni mtoto. Vilevile, katika kitabu cha Kilio Chetu kinaonesha kuwa walengwa wake wakuu ni watoto, mwandishi anasema;

“ ANNA: Hivi wewe unakilimbilia wapi lakini? Soma kaka yangu. Mtoto mdogo hivi mambo haya ya nini? Mbona kutaka kujikomaza hivyo? Kisa cha kukimbilia suti na nepi hujavaa? Mambo hayo tutayakuta wakati ukiwadia. Wewe utaoa na mimi nitaolewa. Na nani aliyekueleza kuwa hii dunia itaisha kesho?” (Uk. 28).

Kutokana na mifano hii kutoka katika kazi hizi mbili tunaona kuwa inaenda sambamba na ile fasili inayosema kuwa fasihi ya watoto ni fasihi ambayo walengwa wake wakuu ni watoto.

Pia, Weche (2002), anasema kuwa fasihi ya watoto ni kioo cha kumwongoza mtoto katika mambo yanayohusu maadili. Fasili hii inaendana na kitabu cha Kilio Chetu pale ambapo mwandishi anasema;

“BABA ANNA: Haya wenzangu kurupushani za nini?

MJOMBA: Dada kakuta vidonge vya majira kwenye nguo za Suzi. Sasa kamdunda wee, mie nikamwambia hilo sio jibu la kumwokoa mtoto. Vyema basi aelimishwe madhara makubwa ya kufanya ngono kabla ya wakati wake. Akielimishwa kwa kina hawezi kuthubutu. Sasa nimekumbana na upinzani. Na jirani hapa alivyokuja ndio kabisaa.

BABA ANNA: Una maana kupewa elimu ya jinsia kama inavyoshauriwa?

MJOMBA: Hasaa.

BABA ANNA: Hilo ndilo mie nililofanikiwa mwenzenu. Nimemwambia mama Anna akae na mabinti zake nami nikae na vijana wangu wa kiume. Tumefanya kazi hiyo kwa makini sana. Tumewaelimisha juu ya madhara ya tabia hiyo kwao binafsi na kwetu sote. Hatukubakiza kitu. Dunia imeharika sasa bwana. Mzazi usipomfunza, walimwengu watamfundisha; Tena sasa si maadili bali ni njia potofu.

MJOMBA: Mzazi ndie mwalimu wa kwanza.” (Uk. 12 – 13)

Hapa tunaona kuwa katika mfano huu umeweza kuangazia suala zima la maadili hususani kwa watoto wadogo.

Kwa kuhitimisha tuaweza kusema kuwa fasihi ya watoto ina dhima mbalimbali katika jamii, dhima hizo ni kama vile kupata maarifa mapya, kuelimisha jamii, kufikirisha hadhira, kuedeleza, kukuza na kurithisha utamaduni pamoja na kusaidia kujielewa na kuwaelewa wengine.













                                                                                                                                                                                                                                               

                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                   



MAREJELEO

Ebraju, P. B. (1999). Sababu mimi ni Mwanamke!. Educational Books Publishers Ltd. Dar es Salaam.

Hunt, P. (ed.). (1999). Understanding Children’s Literature: Key Essays from the International Companion Encyclopidia of Children’s Literature. New York: Routledge.

Lyimo, E. B. (2016). Dhima na Mianzo na Miisho katika Nathari za Kiswahili na Fasihi ya Watoto: Mifano kutoka Riwaya na Hadithi za Watoto nchini Tanzania.

Medical Aid Foundation. (1995). Kilio Chetu. Tanzania Publishing House Limited. Dar es Salaam – Tanzania.

Mpesha, N. (1995). “Children’s Literature in Tanzania: A Literary Appreciation of its Growth and  Development.” Tasnifu ya PhD. Chuo Kikuu cha Kenyetta. (Haijachapishwa).

Ndalu, A. E, Babusa, H, na Suleiman, A. M. (2014). Kamusi Teule ya Kiswahili Kilele cha Lugha. East African Educational Publisher Ltd: Nairobi – Kenya.

NOUN (2010). Children’s Literature. Lagos: National Open University of Nigeria.

TUKI (1981). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Oxford University Press. Dar es salaam - Tanzania.

Wamitila, K. W. (2010). Kichocheo cha Fasihi: Simulizi na Andishi. Nairobi: Focus Books.

Weche, M. O. (2002). “Children’s Literature an Image Force. A Case Study of Ezekiel Alembi’s Books.” Tasnifu ya M. A, Chuo Kikuu cha Kenyetta. (Haijachapishwa).

No comments:

Post a Comment