USHAIRI
WA
KISWAHILI
Nadharia, Maendeleo, Mwongozo kwa Walimu wa Kiswahili
na DIWANI YA MEA
Method Samwel (PhD)
Amina J. Seleman
MEVELI PUBLISHERS (MVP) Akech J.Kabiero
2
USHAIRI WA KISWAHILI
Nadharia, Maendeleo, Mwongozo kwa Walimu wa Kiswahili
na DIWANI YA MEA
© MEVELI Publishers & Method Samwel
Toleo la kwanza 2013
Kitabu hiki kinapatikana kwa kuwasiliana moja kwa na waandishi au mchapishaji:
Dkt. Method Samwel
Simu:+255718165528
Baruapepe: method_samwel@yahoo.com
Akech Kabiero
Simu:+255685046179
Baruapepe: akeckabiero@yahoo.com na akabiero@gmail.com
Amina J. Seleman
Baruapepe: aminamikina@yahoo.com
ISBN: 978-9987-9735-0-7
Haki imehifadhiwa. Hairuhusiwi kuiga, kunakili, kutafsiri, kupiga chapa au kukitoa kitabu hiki
kwa jinsi yoyote ile bila idhini ya mchapishaji na Method Samwel. Hata hivyo, inaruhusiwa
kuchukua vipande vifupi vya kitabu hiki kwa minajili ya kufanya marejeo na nukuu au kufanya
mapitio.
3
SHUKRANI
Tunapenda kutumia fursa hii kuwashukuru watu, taasisi na mashirika mbalimbali
ambayo kwa namna moja au nyingine yamechangia katika kukamilika kwa kitabu hiki. Kwanza
tuanze kwa kumshukuru Mungu, ambaye, kwa mtazamo wetu, ndiye huwapa watu afya njema na
mawazo ya nini cha kufanya na nini cha kutofanya. Bila shaka Manani ndiye aliyetupa wazo la
kuandika kitabu hiki na kututia nguvu kulitimiza wazo hilo japo haikuwa kazi rahisi kutimiza
lengo letu kutokana na ugumu wa shughuli nzima ya uchapaji nchini Tanzania. Pia
tunawashukuru wazazi na walezi wetu ambao walitulea na kutusomesha hata tukapata maarifa
haya ambayo leo tunayaweka kitabuni kama kumbukumbu kwa vizazi vijavyo.
Zaidi ya hao, wapo ambao tumetumia maandiko yao katika kujielimisha juu ya ushairi
wa Kiswahili, wale ambao walihariri kazi hii katika ngazi mbalimbali na pia wale waliotoa fedha
kuhakikisha kitabu hiki kinachapishwa na kuwa na muonekano ulionacho. Hivyo tunawashukuru
wanazuoni wote ambao maandiko yao yamenukuliwa katika kitabu hiki. Kwa hakika maandiko
yenu ndiyo yametoa dira ya andiko hili. Tuwataje wachache kati ya hao kuwa ni Maprofesa
Mugyabuso Mlinzi Mulokozi, Kulikoyela Kanalwanda Kahigi, David Massamba, Kyalo
Wamitila, Fikeni Senkoro; washairi Shaaban Robert, Fumo Liyongo, Mwanakupona Binti
Mshamu, Mathias Mnyampala na wengineo mliotangulia mbele za haki. Mlale salama peponi na
Mola awape heri. Wengine tunaowashukuru hapa ni Prof. Yunus Rubanza, Dakta Shani Omari,
Dakta Selemani Sewangi, Dakta Aldin Mutembei na wanazuoni wote wa Taasisi ya Taaluma za
Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hawa ndiyo walitulea tukiwa tunajifunza taaluma
ya Kiswahili, ikiwa ni pamoja na ushairi wake.
Tungependa kumshukuru kipekee Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya MEVELI
Publishers, kwa kukubali kuuchapa muswada wetu uliozaa kitabu hiki. Yeye ndiye aliyetoa fedha
za kugharamia hatua kwa hatua uandazi wa kitabu hiki tangu uandishi na upangaji wa muswada,
uhariri na uchapishaji kwa ujumla. Tunakushukuru sana kwa mapenzi yako katika lugha hii. Ni
imani yetu kwamba tumekata kiu yako ya kuhakikisha ujuzi tulionao katika taaluma hii ya ushairi
unawafikia watu wengi.
Mwisho kabisa tuwashukuru wana familia wetu ambao kwa nyakati tofauti walitutia
moyo na kutuvumilia tulipotingwa na kazi hii ya uandishi. Andiko hili liwapoze machungu na
mjisikie kuhusika kipekee katika kuendeleza lugha hii adhimu ya Kiswahili. Tunapenda kusisitiza
kwamba tuliowashukuru hapa hawahusiki na udhaifu wowote utakaoonekana kitabuni. Udhaifu
huo, kama utaonekana, ni wetu wenyewe.
4
DIBAJI
Kitabu hiki kinashughulikia utanzu wa ushairi na hasa ushairi wa Kiswahili uliozagaa
katika nchi za Afrika Mashariki, Kati na Kusini mwa Jangwa la Sahara. Kinaanza kwa masuala
ya kidhana, kinadharia, historia na maendeleo ya ushairi wa Kiswahili, mbinu za ufundishaji wa
ushairi na Kiswahili kwa ujumla na kisha kumalizia kwa Diwani ya MEA. Katika sehemu ya
kwanza tumechambua kwa kina dhana ya ushairi, nadharia mbalimbali za chimbuko la ushairi,
historia na maendeleo ya ushairi wa Kiswahili na jinsi ya kuufundisha ushairi wa Kiswahili
pamoja na lugha yenyewe kwa ujumla. Tuseme wazi hapa kwamba sehemu hiyo ilikuwa na
changamoto kubwa kwani masuala kama hayo katika taaluma za sayansi ya Jamii, kama
anavyobainisha Madumulla (2009), hayana maelezo ya namna moja. Kuna maelezo mengi
yanayokinzana kuhusu dhana, nadharia na historia na maendeleo ya Kiswahili. Kitabu hiki
kimechunguza maelezo ya wanazuoni waliotangulia na kubainisha udhaifu wa maelezo hayo.
Udhaifu huo ndiyo uliweka misingi ya maelezo yetu katika kitabu hiki tukijaribu kuondoa
udhaifu husika.
Zaidi ya sehemu ya kwanza, kitabu hiki kina sehemu ya pili ambayo imepewa jina
Diwani ya MEA. Katika sehemu ya kwanza tuliyoieleza awali ambayo inaitwa Nadharia,
Maendeleo na Mwongozo kwa Walimu wa Kiswahili, tumetoa tu ufafanuzi wa dhana, nadharia,
historia na mbinu mbalimbali zinazoweza kutumika katika utunzi na uchambuzi wa mashairi. Ila
katika sehemu ya pili tumepiga hatua na kutunga mashairi kadhaa na Tumeiita Diwani ya MEA.
“Diwani ya MEA” ni kifupi cha “Diwani ya METHOD na AKECH,” waandishi wawili
waliotunga diwani hiyo. Zaidi ya kuwa kifupi cha majina ya waandishi, Diwani ya MEA inapanda
mbegu za mapinduzi katika mioyo ya kila msomaji ili ziweze kumea. Katika diwani hiyo kuna
mashairi mazito na mazuri ambayo yanakusudia kuielimisha na kuiburudisha jamii. Mashairi
hayo yanaakisi masuala mbalimbali ya kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni na kijamii. Aidha,
mashairi hayo yametumia miundo tofauti ikiwa ni mchanganyiko wa muundo wa kimapokeo na
wa kisasa. Kwa kufanya hivyo, sisi waandishi, tunajitambulisha kama wanausasa.
Diwani ya MEA imekusudia kupanda mawazo katika mioyo na vichwa vya wasomaji
wake ili yaweze kumea na hatimaye kuzaa matunda na matunda hayo yakapate kudumu ili
kwamba kila lifanyikalo likumbukwe kwamba linapandwa na litamea. Likishamea litahitaji
mvunaji makini na mwenye utayari ili ayavune na kuyapeleka sokoni kwa mauzo. Kutokana na
sifa hiyo, kitabu hiki kimekuwa cha aina yake katika historia ya ushairi wa Kiswahili. Diwani ya
MEA itamsisimua msomaji huku akipata mafunzo muhimu sana yatakayokuwa taa katika maisha
yake yote. Hata hivyo, diwani hiyo inapaswa kusomwa kwa tafakuri ya kiwango cha juu maana
ukweli kinzani umetumiwa sehemu nyingi.
yaliyomo/ content
Shukrani ................................................................................................................................ 3
Dibaji .................................................................................................................................... 4
Tabaruku ............................................................................................................................... 9
Vifupisho na Akronimu ........................................................................................................ 10
Sehemu ya Kwanza: Nadharia, Maendeleo na Mwongozo kwa Walimu wa .......
Kiswahili ................................................................................................................... 11
Sura ya Kwanza: Utangulizi .......................................................................................... 12
Ushairi kama Utanzu wa Fasihi Simulizi .............................................................................. 12
Uainishaji wa Tanzu za Fasihi Simulizi ................................................................................ 15
Nudhumu Simulizi ............................................................................................................... 20
Nyimbo ............................................................................................................................... 20
Uainishaji wa Utanzu wa Nyimbo kwa Kigezo cha Dhima ................................................... 20
Uainishaji wa Nyimbo Kimaudhui........................................................................................ 22
Uainishaji wa Nyimbo kwa Kifanani/Hadhira ....................................................................... 22
Uainishaji wa Nyimbo Kimuktadha ...................................................................................... 22
Maghani .............................................................................................................................. 22
Uainishaji wa Maghani kwa Kigezo cha Dhima .................................................................... 22
Uainishaji wa Maghani kwa Kigezo cha Utendaji ................................................................. 23
Ushairi kama Utanzu wa Fasihi Andishi ............................................................................... 23
Dhana ya Ushairi Andishi wa Kiswahili ............................................................................... 23
Mkabala wa Kimapokeo Juu ya Dhana ya Ushairi ................................................................ 24
Mkabala wa Kisasa/Kimamboleo Juu ya Dhana ya Ushairi ................................................... 27
Sifa za Jumla za Ushairi ....................................................................................................... 28
Sura ya Pili: Dhima za Ushairi wa Kiswahili .............................................................. 29
Dhima za Ushairi wa Kiswahili Kijamii ............................................................................ 29
Ushairi wa Kiswahili na Uhifadhi wa Historia ...................................................................... 29
Ushairi wa Kiswahili na Kukuza Ushujaa, Ujasiri na Uzalendo ............................................ 32
Ushairi wa Kiswahili na Kuendeleza Matabaka .................................................................... 32
Ushairi wa Kiswahili na Kuhifadhi na Kuendeleza Utamaduni ............................................. 33
Ushairi wa Kiswahili na Kuadilisha na Kuadibisha ............................................................... 34
Ushairi wa Kiswahili na Kuburudisha................................................................................... 35
Dhima za Ushairi wa Kiswahili Katika Fasihi .................................................................. 35
Ushairi wa Kiswahili na Kutambulisha na Kuwajenga Wahusika ......................................... 36
Ushairi wa Kiswahili na Kuhamisha na Kujenga Mbinu za Kifani ........................................ 36
Ushairi wa Kiswahili na Kuibua Maudhui ............................................................................ 37
Ushairi wa Kiswahili na Kukuza Tanzu za Fasihi ................................................................. 38
Sura ya Tatu: Chimbuko la Ushairi wa Kiswahili ..................................................... 41
Chimbuko la Ushairi wa Kiswahili ni Uislamu/Kiarabu ........................................................ 41
Chimbuko la Ushairi wa Kiswahili ni Ushairi Simulizi wa Kibantu ...................................... 45
Kufanana kwa Ushairi wa Kiswahili na Ushairi Simulizi wa Kibantu ................................... 46
Kufanana Kimaudhui ........................................................................................................... 46
Kufanana kwa Dhima ........................................................................................................... 51
Kufanana Kifani ................................................................................................................... 53
Sura ya Nne: Historia ya Ushairi wa Kiswahili ......................................................... 57
Ushairi Simulizi wa Kiswahili Wakati wa Ujima .................................................................. 57
Ushairi wa Kiswahili katika Karne ya 10 na 16 .................................................................... 58
Mchango wa Waarabu katika Ushairi wa Kiswahili .............................................................. 58
Ushairi wa Kiswahili katika Karne ya 17 na 18 .................................................................... 59
Ushairi wa Kiswahili katika Karne ya 19 .............................................................................. 59
Kuingia kwa Ukoloni na Athari Zake katika Ushairi wa Kiswahili ....................................... 59
Ukoloni wa Wajerumani/Wadachi ........................................................................................ 60
Ukoloni wa Waingereza ....................................................................................................... 60
6
Kupatikana kwa Uhuru na Hali ya Ushairi wa Kiswahili ...................................................... 61
Kipindi cha Uhuru na Azimio la Arusha ............................................................................... 61
Kipindi cha Vita vya Kagera na Ugumu wa Maisha .............................................................. 61
Ushairi wa Kiswahili Kipindi cha Utandawazi ...................................................................... 65
Sura ya Tano: Ushairi wa Bongo Fleva ...................................................................... 66
Dhana ya Muziki wa Bongo Fleva ........................................................................................ 66
Maudhui ya Ushairi wa Bongo Fleva ................................................................................ 67
Maudhui ya Uongozi na Utawala .......................................................................................... 67
Maudhui ya Kiuchumi .......................................................................................................... 67
Maudhui ya Kijamii katika Ushairi wa Bongo Fleva ............................................................. 68
Maudhui ya Kiutamaduni Katika Ushairi wa Bongo Fleva ................................................... 70
Fani ya Ushairi wa Bongo Fleva ........................................................................................ 72
Utungaji wa Ushairi wa Bongo Fleva ................................................................................... 72
Utendaji wa Ushairi wa Bongo Fleva ................................................................................... 77
Mandhari ya Ushairi wa Bongo Fleva ................................................................................... 84
Muundo wa Ushairi wa Bongo Fleva .................................................................................... 84
Mtindo wa Ushairi wa Bongo Fleva ..................................................................................... 88
Wahusika katika Ushairi wa Bongo Fleva .......................................................................... 110
Sura ya Sita: Uainishaji wa Ushairi wa Kiswahili ................................................... 111
Kigezo cha Aina ya Uwasilishaji ........................................................................................ 111
Kigezo cha Umbo ............................................................................................................... 111
Kigezo cha Mbinu za Kisanaa Zinazotumika ...................................................................... 112
Kigezo cha Maudhui Yabebwayo na Shairi ........................................................................ 112
Kigezo cha Idadi ya Mistari ................................................................................................ 113
Kigezo cha Bahari .............................................................................................................. 113
Bahari za Ushairi wa Kimapokeo ....................................................................................... 113
Upungufu wa Kigezo cha Bahari za Ushairi wa Kimapokeo ............................................... 119
Bahari za Ushairi wa Kimapokeo na Kisasa ........................................................................ 120
Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Beti, Mishororo na Vipande .......................................... 120
Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Aina ya Kiishilio ........................................................... 121
Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Urari wa Vina na Mizani ............................................... 121
Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Uradidi ......................................................................... 123
Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Madhumuni ya Utungaji (Lengo) .................................. 123
Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Muundo ........................................................................ 124
Hitimisho kuhusu Bahari za Ushairi ................................................................................... 125
Sura ya Saba: Uchambuzi wa Mashairi .................................................................... 126
Maudhui ............................................................................................................................. 126
Fani ................................................................................................................................. 127
Sura ya Nane: Ufundishaji wa Ushairi ...................................................................... 132
Ushairi kama Mbinu ya Kufundishia Masomo Mbalimbali ................................................. 132
Ushairi wa Kiswahili kama Somo ....................................................................................... 133
Silabasi na Ushairi wa Kiswahili ........................................................................................ 133
Kutafsiri Silabasi kwenye Vitendo...................................................................................... 134
Kufanya Mapitio ya Makusudi ya Ufundishaji wa Ushairi .................................................. 134
Kuchagua na Kupanga Mada za Ushairi Zitakazofundishwa ............................................... 134
Kutambua Vitabu vya Kiada na Kuteua Vitabu vya Ziada .................................................. 135
Kuandaa Mpangokazi wa Ufundishaji ................................................................................ 135
Kuteua na Kuandaa Mbinu ya Kufundishia Ushairi na Maandalizi Yake ............................ 139
Kuandaa Mwongozo wa Ufundishaji wa Ushairi Darasani .................................................. 143
Kuandaa Zana za Kufundishia ............................................................................................ 146
Kuingia Darasani na Kufundisha ........................................................................................ 147
Kufanya Tathmini (Upimaji) ya Ufundishaji wa Ushairi ..................................................... 147
Kutoa Matokeo ya Tathmini na Utoaji wa Motisha ............................................................. 148
7
Upangaji wa Ufundishaji Ujao ............................................................................................ 149
Hitimisho Kuhusu Hatua za Kutafsiri Silabasi kwenye Vitendo .......................................... 150
Sehemu ya Pili:Diwani ya MEA .................................................................................. 151
Lipaka ............................................................................................................................... 152
Hadithi ............................................................................................................................... 152
Mwatulinda? Mwatuua? ..................................................................................................... 154
…………Te. ...................................................................................................................... 154
Te!Te!TeTe! ....................................................................................................................... 155
Madhila Yako..................................................................................................................... 156
Kwaherini .......................................................................................................................... 157
Tangu Atoke Safari ............................................................................................................ 159
Maskini Afrika!! ................................................................................................................ 159
Kisabengo .......................................................................................................................... 161
Chakubimbi ........................................................................................................................ 162
Mchezo wa Maneno ........................................................................................................... 162
Barua Jukwaani .................................................................................................................. 163
Dunia Kambi ...................................................................................................................... 165
Ng’ombe Mmemmaliza ...................................................................................................... 165
Nyathiwa Woung Dala (Mwanetu Ondoka Nyumbani) ....................................................... 166
Naenda Kuitafuta ............................................................................................................... 167
Maji ya Kifo ....................................................................................................................... 170
Ulimi ................................................................................................................................. 171
Tukaogelee! ....................................................................................................................... 171
Akilamba Sabuni ................................................................................................................ 171
Umoja Wetu ....................................................................................................................... 172
Wegesa Mnyamongo (Wege/Penina) .................................................................................. 172
Panya Akimng’ata Chui ..................................................................................................... 173
Hata Kama! ........................................................................................................................ 174
Ksii!! Ksii!! ........................................................................................................................ 175
Mtakosa Kuthaminiana ....................................................................................................... 175
Pamoja Kwamba ................................................................................................................ 176
J.K.Nyerere Baba ............................................................................................................... 177
Sherehe Itakapoisha ............................................................................................................ 178
Rais Awaye Yeye! .............................................................................................................. 179
Barua ya Majibu ................................................................................................................. 180
Ya Nini Lakini? .................................................................................................................. 183
Chuny Piny (Roho Ya Nchi) ............................................................................................... 184
Na Tuvisome Vyote ........................................................................................................... 185
Safari Kuelekea .................................................................................................................. 186
Ndege si Ndege, Mnyama si Mnyama. ............................................................................... 189
Kizungumkuti .................................................................................................................... 190
Bunge la Wahuni. ............................................................................................................... 191
Karibu Mwanangu! ............................................................................................................ 193
Twende Tukawinde ............................................................................................................ 194
Kwa Jirani Yetu! ................................................................................................................ 194
Ni Lini na Wapi? ................................................................................................................ 195
Nyako Ma Ero Ainya ......................................................................................................... 196
Wimbo Ulio Bora ............................................................................................................... 197
Mafamba ............................................................................................................................ 198
Inapotokea .......................................................................................................................... 201
Mwanzo Mwisho ................................................................................................................ 203
Ngao ................................................................................................................................. 204
Tamati! .............................................................................................................................. 204
8
Marejeleo .......................................................................................................................... 205
Faharasa ............................................................................................................................. 211
9
TABARUKU
Tunakitabaruku kitabu hiki kwa washairi wote
waliotangulia mbele ya haki pamoja na marehemu
Prof. Yared Kihore. Mungu awajalie rehema zake na
siku moja tuonane akhera tukiimba na kughani ushairi
wa Kiswahili.
10
VIFUPISHO NA AKRONIMU
a.k.a Anajulikana kama (Also known as)
BAKITA Baraza la Kiswahili la Taifa
CD Compact Disc
CHAKA Chama cha Kiswahili Afrika
CHAKAMA Chama cha Kiswahili Afrika Mashariki
CHAKITA Chama cha Kiswahili cha Taifa
Dkt. Daktari
DVD Digital Video Disc
EATV East Africa Television
ht. Hakuna tarehe
ITV Independent Television
Khj. Kama hapo juu
PhD Daktari wa Falsafa
p.h.k Pia hujulikana kama
Prof. Profesa
TATAKI Taasisi ya Taaluma za Kiswahili
TAKILUKI Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni
TUKI Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili
TV Television
VCD Video Compact Disc
11
SEHEMU YA KWANZA:
Nadharia, Maendeleo na Mwongozo kwa Walimu wa
Kiswahili
12
SURA YA KWANZA
UTANGULIZI
Tanzu za lugha ni isimu na fasihi. Katika isimu, kuna tanzu kama vile isimujamii, isimu matamshi
(fonetiki/fonolojia), isimu muundo (Sintaksia), isimu maumbo (mofolojia) n.k. Kwa upande wa fasihi,
kuna aina mbili za fasihi ambazo ni fasihi simulizi na andishi. Ushairi ni utanzu wa fasihi unaopatikana
katika fasihi simulizi na pia andishi. Kitabu hiki kinapitia na kuchambua ushairi kama utanzu wa fasihi
simulizi na pia kama utanzu wa fasihi andishi.
1. USHAIRI KAMA UTANZU WA FASIHI SIMULIZI
Kabla ya kuzama katika kuchunguza ushairi kama utanzu wa fasihi simulizi, ni vema tuchunguze
dhana ya fasihi simulizi. Pamekuwepo na fasili mbalimbali za fasihi simulizi ambapo kila moja ina
jambo la muhimu inayolisisitiza. Suala la utata katika fasili ya fasihi simulizi linabainishwa vizuri na
Akivaga na Odaga (2011:1) wanaposema:
Until recently it was not possible to agree on the definition of oral literature. Different people
have come up with different definitions. Some people have even refused to accept the term “oral
literature,” arguing that it is a contradiction in terms. They argue that literature means the
written word and therefore it can not be oral.
Mpaka hivi karibuni haikuwa rahisi kukubaliana juu ya fasili ya fasihi simulizi. Watu
tofautitofauti wamekuja na fasili tofautitofauti za fasihi simulizi. Wengine wamefikia hatua ya
kuikubali dhana “fasihi simulizi,” kwa madai kwamba ni mkanganyiko wa dhana. Wanadai
kwamba kimsingi fasihi humaanisha maelezo yaliyoandikwa na kwa hiyo hayawezi kamwe kuwa
simulizi (Tafsiri yetu).
Maelezo haya yanatuthibitishia kwamba dhana fasihi simulizi ni yenye mkanganyiko mkubwa na japo
ni muhimu kuielewa kabla ya kuuelewa ushairi simulizi, jambo hilo halimaanishi kwamba litakuwa
rahisi. Ili kuuona ugumu huo unaodokezwa na Akivaga na Odaga (khj.) tuzipitie fasili chache za fasihi
simulizi. Kwa kuanza na Mulokozi (1996:24), tunaona anaiona fasihi simulizi kuwa ni fasihi
inayotungwa au kubuniwa kichwani na kuwasilishwa kwa hadhira kwa njia ya mdomo na vitendo bila
kutumia maandishi. Anaendelea kudai kwamba fasihi simulizi ni tukio linalofungamana na muktadha
(mazingira) fulani ya kijamii na kutawaliwa na mwingiliano wa mambo sita ambayo ni fanani (msanii),
hadhira (msikilizaji), fani inayotendwa, tukio, mahali na wakati. Naye Ngure (2007:1) kwa upande
wake, anasema kwamba fasihi simulizi ni ile ambayo inapitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine
kupitia neno la mdomo. Fasili hizi mbili (ya Mulokozi na ya Ngure), hata hivyo, zinaweka mkazo
katika utungaji na/au uwasilishaji na kupuuza masuala mengine ya kifasihi kama vile uhifadhi na
mabadiliko. Wakati ambapo fasili ya Mulokozi ni bora kuliko ya Ngure kwani inazingatia utungaji na
uwasilishaji, ya Ngure inazingatia tu uwasilishaji. Wamitila (2010a:2-3) anabainisha wazi kwamba
mgawanyo wa fasihi katika makundi (ya fasihi simulizi na andishi) unategemea (a) njia zinazotumiwa
kuhifadhi, kuwasilisha, kupokezana (b) nyenzo yake kuu. Kwa kutumia vigezo hivyo vya uainishaji wa
fasihi, ni wazi kwamba fasili ya Ngure (2007) ina mapungufu makubwa wakati ile ya Mulokozi
inaonekana kutimiza baadhi ya vigezo vya Wamitila. Aidha, fasili hizo mbili (ya Mulokozi, 1996 na
Ngure, 2007) zinachukulia kwamba fasihi simulizi husambazwa kwa njia ya masimulizi ya mdomo (na
kupuuza nafasi ya mbinu nyinginezo za usambazaji wa fasihi). Mawazo haya yanapingana na halisi.
Wamitila (2001b:13-14) akiandika kwa namna bora zaidi kwa wakati wa sasa anasema kwamba,
“katika tamaduni andishi ambazo zimeathiriwa na mfumo wa kimaandishi, hiyo inayojulikana kama
fasihi simulizi sio simulizi tena (haiwasilishwi kwa njia ya mdomo tu) bali inahifadhiwa kwa njia
mbalimbali kama kwa vinasa sauti, kanda za video na kompyuta” (ufafanuzi ni wetu). Bila shaka
waandishi wengi wa sasa wa fasihi watakubaliana na maelezo haya ya Wamitila na kuyapinga ya
Mulokozi na Ngure. Kutokana na hayo, Wamitila (2010a:3) anasema kwamba tofauti kuu kati ya fasihi
simulizi na andishi ni kwamba fasihi simulizi hutegemea zaidi kauli au usemi kuliko fasihi andishi
ambayo hutegemea maandishi kwa kiasi kikubwa. Wamitila anaendelea kwa kutahadharisha kwamba
“upo uwezekano wa fasihi andishi kupewa sura ya fasihi simulizi na fasihi simulizi kuwasilishwa
kimaandishi.” Hata hivyo, tungependa ieleweke kuwa hatubezi jitihada zilizofanywa na wataalamu wa
awali waliofafanua dhana hizi. Tunatambua kwamba wakati wataalamu wengi wa awali (na hasa
13
walioandika hadi miaka ya 1990) walipokuwa wanaandika juu ya fasihi simulizi, hakukuwa na
maendeleo makubwa ya kuiweka fasihi simulizi katika mbinu mpya za usambazaji kama vile
maandishi, kanda za video na kadhalika kama ilivyo leo. Hivyo, kwa wataalamu wa awali kuchukulia
kuwa fasihi simulizi inasambazwa kwa mdomo bila kutumia maandishi ni dai ambalo labda linatokana
na wakati walipokuwa wakiandika. Msingi wa pili wa dai hilo huweza kuwa sambamba na kile
anachokisema Wamitila (2010a:3) kuwa, fasihi simulizi hutegemea zaidi kauli kuliko maandishi.
Aidha, hata pale fasihi simulizi inapowekwa katika maandishi, bado ukweli unabaki kuwa palepale
kuwa kazi hiyo ilianza kwa kuwasilishwa kwa masimulizi ya mdomo na mbinu zingine za uwasilishaji
zikafuata baadaye. Vilevile, mawazo haya ya wataalamu wa awali huenda yametokana na ukweli
anaouwasilisha Wamitila (2010a:3) kwamba pale fasihi inapohifadhiwa na/au kuwasilishwa kwa njia
zingine ambazo si za kimasimulizi (inapohifadhiwa au kuwasilishwa kwa maandishi) hupoteza sifa
zake za msingi zinazoifanya kazi husika kuwa utanzu wa fasihi simulizi.
Hivyo, bado tusisitize hapa kwamba, fasihi simulizi inazalishwa kichwani mwa binadamu,
inawasilishwa kwa njia za midomo na matendo. Hata pale inapotokea fasihi simulizi ikahifadhiwa kwa
na kuwasilishwa kwa maandishi usimulizi asilia unakuwa ulifanyika katika masimulizi. Kwa mfano,
mtu anapoamua kuandika ngano ya sungura na fisi ina maana kwamba wakati anaandika anakuwa
anasimulia ngano hiyo kwa hadhira dhahania (hadhira ambayo haipo ila itaibuka baadaye na kusoma
kazi husika). Msanii anapoiandika ngano hiyo huwa haitungi maana ilishatungwa zamani, bali
anaisimulia hadhira yake. Aidha, mabadiliko haya ya fasili za fasihi simulizi yanadokeza jinsi
mabadiliko mbalimbali ya kisayansi na kijamii yanavyoweza kubadilisha mitazamo au dhana
mbalimbali za kitaaluma.
Mbali na utata katika suala la nyenzo ya uwasilishaji wa fasihi simulizi, jambo lingine
linaloonekana hapa ni kwamba fasihi simulizi inachukuliwa kuwa ni ile inayorithishwa kutoka kizazi
kimoja hadi kingine kwa njia ya masimulizi ya mdomo na matendo (Finnegan, 1977; Bukenya na
wenzake, 2000; King’ei na Kisovi, 2005; Kimani na wenzake, 2006 kwa kuwataja wachache). Samwel
(2012a) anafafanua kwamba kauli hii inaleta hisia kuwa fasihi simulizi haibadiliki, bali hubaki vile vile
toka kizazi hadi kizazi. Samwel anaendelea kueleza kwamba, kwa kuwa fasihi ni zao la jamii ni wazi
kwamba fasihi simulizi, pamoja na tanzu zake, zinabadilika kulingana na mabadiliko mbalimbali
yanayotokea katika jamii. Samwel (2012a) anamnukuu Rubanza (1994:1) kusisitiza juu ya hilo
anaposema kwamba, “si kweli kuwa fasihi simulizi ni masimulizi tu ya kale yarithishwayo kutoka kizazi
kimoja hadi kingine. Fasihi simulizi ni utanzu wa sanaa ulio hai na ambao hukua na kubadilika
kutokana na mabadiliko ya kiwakati na ya kimfumo jamii.” Aidha, Samwel anamnukuu pia Miller
(1984:151) anayeshadidia kuhusu mabadiliko ya fasihi simulizi kwa kusema kwamba hata idadi na
majina ya tanzu/vipera vya fasihi simulizi yataendelea kubadilika kulingana na mabadiliko yanayotokea
katika jamii. Hivyo, kuna uwezekano wa tanzu mpya kuzaliwa au tanzu zilizoainishwa awali kupotea.
Hata hivyo Samwel (2012a) akimnukuu Jamieson (1975:414), anasisitiza kwamba fasihi simulizi
inapobadilika na kuibua tanzu mpya, basi tanzu hizo mpya hujengwa katika msingi wa tanzu za awali.
Kutokana na hayo yote, tuseme fasihi simulizi ni nini hasa? Katika kitabu hiki labda tuseme
kwamba fasihi simulizi ni dhana inayochimbuka katika dhana ya Kiingereza “oral literature” ambayo
hasa inamaanisha aina ya fasihi ambayo msingi wake hasa ni masimulizi ya mdomo na matendo, japo
kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, inaweza pia kuhifadhiwa katika maandishi.
Zaidi ya utata katika dhana yenyewe suala lingine lenye utata katika fasihi simulizi ni uainishaji wa
tanzu na vipera vya fasihi simulizi. Uainishaji wa tanzu za fasihi simulizi umekuwa moja ya mambo
magumu sana katika fasihi hiyo. Ugumu wa uainishaji wa tanzu hizo unatokana na mambo kadhaa.
Miongoni mwa mambo hayo ni haya yafuatayo:
(i) Kuna vigezo vingi vinavyoweza kutumika katika uainishaji wa tanzu hizo. Vigezo hivyo,
hata hivyo, vinatofautiana kutoka mwanazuoni mmoja hadi mwingine. Kwa mfano, tunaona
Wafula na Njogu (2007:13) kwenye kitabu chao Nadharia za Uhakiki wa Fasihi wanabainisha
kwamba vigezo vinavyoweza kutumika katika kuainisha tanzu za fasihi simulizi ni pamoja na:
majina ya tanzu, miundo yake- kwa mfano mianzo na miishio yake, mitindo yake, wahusika
wake, wakati na mahali pa kutambia. Maelezo haya yanatofautiana na ya Mulokozi (1996:34)
katika Fasihi ya Kiswahili ambapo anabainisha kwamba vigezo vinavyoweza kutumika katika
14
kuainisha tanzu za fasihi simulizi ni pamoja na: umbile na tabia ya kazi inayohusika , vipengele
vya ndani na nje mfano lugha iliyotumika kama vile (lugha ya kishairi, kinathari, kimafumbo,
ki-wimbo, kighani, na kadhalika). Anataja vigezo vingine kuwa ni muundo wa fani, wahusika
(kama wapo), muktadha wa uwasilishaji, namna ya uwasilishaji wake kwa hadhira na dhima ya
fani hiyo katika jamii. Hivyo, vyovyote iwavyo, kutumia vigezo tofauti kutasababisha kuwa na
tanzu tofauti tofauti za fasihi simulizi.
(ii) Tanzu za fasihi simulizi ni nyingi na hutofautiana kati ya jamii na jamii. Kutokana na hili
inakuwa ni vigumu sana kueleza tanzu za fasihi simulizi ni zipi hasa. Kila jamii ina tanzu zake
za fasihi simulizi ambazo zinaweza kuwa tofauti na tanzu za jamii nyingine. Inawezekana tanzu
fulani ikawepo katika jamii fulani lakini isiwepo katika jamii nyingine au ikawepo katika jamii
nyingine lakini ikiwa na sifa tofauti kabisa. Kwa mfano, Samwel (2012a) anawasilisha kwamba
katika jamii za Wahaya na Wasukuma alizozitafiti, zina majigambo ya wanawake. Rejelea
anaposema:
...katika jamii za Kihaya na Kisukuma tulizozitafiti tumebaini kwamba walikuwapo
wanawake ambao walikuwa mashujaa na watawala. Mulokozi (2002:43) akithibitisha
kuwapo kwa mashujaa wa kike katika jamii ya Kihaya anasema kwamba tendi za nanga
zilikuwa za aina tatu, tendi za nanga za mashujaa (enanga z’emanzi), tendi za nanga za
wafalme (enanga z’abakama) na tendi za nanga za mizimu (enanga z’Abachwezi).
Anaendelea kusema kwamba katika tendi za nanga za ushujaa, shujaa kwa kawaida alikuwa
mwanamume jasiri au mwanamke jasiri. Hii ina maana kwamba enanga z’emanzi
zinatambua kuwapo kwa shujaa wa kike katika jamii za Wahaya. Jambo hili si la ajabu
kwani simulizi za Zanzibar pia zinatueleza kwamba Zanzibar hapo awali iliitwa Zinji la
Mwana Aziza ikipata jina hilo kutoka kwa mtawala wa kike aliyeitwa Mwana Aziza. Vivyo
hivyo, simulizi hizo zinatueleza kwamba huko Unguja alipata kuwapo mwanamke jasiri
aliyeitwa Bihole wa Unguja ambaye alimiliki watumwa wengi sana. Hivyo, kama
tunakubaliana kwamba walikuwapo wanawake mashujaa na watawala na kwamba
majigambo ni utanzu ulioghanwa na mashujaa na watawala basi ni wazi kwamba wanawake
mashujaa na watawala nao walikuwa na sababu ya kujigamba.
Hapa Samwel anapingana na dai la Bowra (1952) kwamba wanawake hawakuwa na sababu ya
Kujigamba. Hivyo, anathibitisha bila shaka yoyote kwamba jamii za Wahaya na Wasukuma
zina majigambo hayo ya wanawake. Hata hivyo, aina hii ya majigambo inaonekana kutowepo
katika jamii nyingi za Kitanzania na Afrika kwa ujumla (Taz. Rubanza, 1994; Mulokozi, 1996;
Peek na Kwesi, 2004). Jambo hili linafanya iwe vigumu sana kusema kwamba tuna aina hizi au
zile za tanzu za fasihi simulizi. Tunaweza kufanya hivyo tu kwa kuzingatia jamii moja mahsusi.
(iii) Tanzu hizo huingiliana. Katika fasihi simulizi ni kawaida kwa tanzu kuingiliana; methali
huweza kuwa hadithi na hadithi huweza kuwa methali na kadhalika. Hivyo, inakuwa vigumu
sana kuainisha tanzu. Jambo hili linafafanuliwa kwa kina na Mulokozi (1996) na Samwel
(2012a). Mulokozi (1996:37) anaelezea jinsi methali za Kihaya “obutelagaza bukaisa
Mashanda” (kutokujipangusa mikono kulimponza Mashanda) na ya Kimaragoli “Navolegwa
yita imbogo” (Navolegwa aliua mbogo (nyati)). Mulokozi (khj.) anafafanua kwamba methali ya
kwanza inadokeza hadithi moja ya mtu aliyeitwa Mashanda ambaye alimpa mfalme zawadi ya
buni za kutafuna bila ya kujipangusa mikono kwanza. Mfalme akakasirika na kuamuru auawe
(kwa kumlisha najisi). Methali inayofuata inadokeza hadithi ya Navolegwa ambaye alikuwa
mtu mnyonge sana na dhaifu aliyedharauliwa na kila mtu. Siku moja alikwenda kuwinda,
akamwua nyati, mnyama mkali ambaye hata wawindaji shupavu na wenye nguvu
walimwogopa. Huu ni mfano dhahiri wa kuingiliana kwa utanzu wa methali na hadithi. Samwel
(2012a) naye anatoa mifano iliyo dhahiri ya kuingiliana kwa tanzu ya nyimbo na maigizo (sanaa
za maonyesho) katika muziki wa Bongo Fleva. Katika muziki huu tunaona kwamba kuna
mwingiliano mkubwa baina ya utanzu wa nyimbo na utanzu wa maigizo. Tunaona kwamba
nyimbo za Bongo Fleva zinaporekodiwa katika kanda za video au sidii za kuona (DVD/VCD)
kuna namna fulani ya maigizo ya yale yanayoimbwa. Msanii anapoimba kuhusu kumfumania
mpenzi wake, kwa mfano, tunaona pia anaigiza zoezi zima la kufumaniwa na kuufanya wimbo
15
huo kuwa kama hadithi inayoimbwa. Kuingiliana huku kwa Bongo Fleva na Maigizo ndiko
kulimfanya Mahenge (2012) kuhoji ikiwa muziki wa Bongo Fleva ni utanzu wa nyimbo au
sanaa za maonyesho.
(iv) Tanzu za fasihi simulizi hubadilikabadilika kutegemeana na muktadha wa utendaji na
wakati. Kama tulivyoeleza hapo juu kwamba tanzu za fasihi simulizi hubadilika, tanzu mpya
huweza kuibuka na zamani kufa. Hivyo, ni vigumu kueleza kuna tanzu ngapi za fasihi simulizi
labda pia itajwe uainishaji huo ni kwa wakati gani? Tukitumia andiko la Samwel (2012a)
tunabaini kwamba anashughulikia utanzu wa fasihi simulizi wa nyimbo na kipera cha
majigambo ya Bongo Fleva. Kama anavyobainisha mwenyewe kwamba utanzu huu umeibuka
miaka ya 1980 na kushika kasi miaka ya 1990, hivyo utanzu huu haukuwapo kabla ya mwaka
1980. Kwa hiyo, kama mtu akitumia uanishaji wa tanzu za fasihi simulizi uliofanywa miaka ya
1960 ni wazi kwamba hatakuwa na aina hii ya utanzu maana haikuwapo wakati huo.
Kutokana na sababu hizo, na nyingine nyingi, imekuwa vigumu sana kubainisha tanzu za fasihi
simulizi. Hata hivyo, kwa minajili ya kurahisisha usomaji wa fasihi simulizi kwa wakati wa sasa,
tunachukulia hapa kwamba fasihi simulizi ina tanzu sita ambazo ni kama ifuatavyo:
UAINISHAJI WA TANZU ZA FASIHI SIMULIZI
1. NUDHUMU
(a) Nyimbo
· Uainishaji wa nyimbo kidhima
i. Tumbuizo
- Bembelezo
- Mbolezo
ii. Tukuzo
iii. Simango
iv. Chapuzo
- Nyimbo za uvuvi na ubaharia (Kimai)
- Nyimbo za makuli
- Nyimbo za kilimo (wawe)
- Nyimbo za kutwangia na kupepetea
- Nyimbo za michezo ya watoto
- Nyimbo za mapigano vitani n.k.
· Uainishaji wa nyimbo kimaudhui
i. Nyimbo za siasa
ii. Nyimbo za dini
iii. Nyimbo za kitamaduni
· Uainishaji wa nyimbo kifanani/hadhira
i. Nyimbo za wazee
ii. Nyimbo za vijana
iii. Nyimbo za watoto
iv. Nyimbo za wanawake
v. Nyimbo za wanaume
· Uainishaji wa nyimbo kimuktadha
i. Nyimbo za jandoni
ii. Nyimbo za unyagoni
iii. Nyimbo za kisimani
iv. Nyimbo za majumba ya ibada
(b) Maghani
· Uainishaji wa maghani kidhima
i. Maghani tumbuizo: haya ni maghani ambayo yanakusudia kutoa burudani kwa hadhira
husika.
16
ii. Maghani tukuzo/sifo: haya ni maghani ambayo dhima yake kuu ni kueleza sifa za mtu
binafsi au za mtu mwingine.
iii.Maghani simango: maghani ambayo dhima yake kuu ni kumsimanga mtu fulani juu ya
mambo aliyoyafanya au anayoaminika kuwa nayo. Kwa kawaida, mambo
anayosimangiwa mtu huwa ni mabaya na hayakubaliki katika jamii husika.
· Uainishaji wa maghani kiutendaji
i. Maghani nafsia
ii. Maghani simulizi
2. NATHARI
(a) Nathari za Kihistoria
i. Visasili: ni hadithi zinazoelezea kwanini viumbe wamekuwa na sifa, tabia au
maumbile ya namna fulani. Kwa mfano, kwanini kobe ana magambamagamba.
ii. Visaviini: ni hadithi zinazoelezea chimbuko la jamii ya watu, kabila, taifa au hata
miungu fulani ya jamii.
iii. Mighani (Visakale)
iv. Mapisi
v. Nasabu/ Shajari
vi. Tarihi
vii. Kumbukumbu
(b) Nathari za Kibunifu
i. Ngano
- Hurafa/ khurafa
- Hekaya
ii. Mbazi
iii. Istiara
iv. Michapo
3. TANZU FUPIFUPI
(i) Methali
(ii) Vitendawili
(iii) Shirikina: ni semi ambazo hutoa onyo kwa jamii juu ya jambo fulani la kiimani.
Hizi hujumuisha marufuku na makatazo ama miiko ya jamii husika. Shirikina
huweza kugawanywa katika makundi yafuatayo:
- Shirikina za matendo: ukinyoa nywele usiku unakaribisha msiba, ukinyooshea
kidole makaburi kidole kinapinda, kufagia nyumba usiku ni kufukuza baraka,
kuomba chumvi usiku ni kukaribisha misiba n.k.
- Shirikina za wanyama: bundi kulia karibu na nyumba ni ishara ya msiba, kondoo
kuangalia juu ni ishara ya mwisho wa dunia, jogoo kuwika usiku wa manane ni
kukaribisha nuksi n.k.
- Shirikina za jadi: mkono ukiwasha ni ishara kwamba utapokea fedha, macho
yakichezacheza ni ishara kwamba utaona jambo la ajabu sana na nyinginezo.
(iv) Mafumbo
(v) Simo/Misimu
(vi) Vichekesho
(vii) Lakabu
(viii) Misemo
(ix) Vitanza-Ndimi/ Kauli Tauria
4. MAZUNGUMZO
(i) Umbea (fasihi ya wanawake): ni mazungumzo ambayo kwa kawaida huwa ni kati
ya mwanamke na mwenziye yanayohusisha kuwasema watu juu ya mambo mabaya
17
waliyonayo. Mambo hayo huweza kuwa ya kweli au hata ya kubuni lakini pale yanapokuwa
ya kweli huongezewa chuku ndani yake. Kwa kawaida mtu anayesemwa katika
mazungumzo haya huwa hawepo wakati wa mazungumzo.
(ii) Hotuba
i. Hotuba za kimila
- Hotuba za matambiko: hotuba zinazotolewa katika shughuli ya kuwatambikia
mizimu, iwe makaburini, kwenye miti mikubwa au popote pale.
- Hotuba za kuposea: hotuba itolewayo na mshenga wakati wa kuomba kibali
cha kuoa kutoka katika ukoo fulani.
ii. Hotuba za kisiasa
iii. Hotuba za kidini
(iii) Soga
(iv) Mawaidha
(v) Mizaha
(vi) Utani
(vii) Mchongoano
(viii) Maombi
5. DRAMA SIMULIZI
(a) Komedia/Futuhi: ni drama za vichekesho ambapo fanani huiga tabia kadha wa
kadha ili kuichekesha jamii na kuifunza wakati huohuo. Mifano mizuri ya komedia
ni “Ze Orijino Comedy” inayorushwa na kituo cha televisheni cha TBC1, “Futuhi”
inayorushwa na Televisheni ya Star (Star TV) na “Ze Comedy” inayorushwa na
Televisheni ya Afrika Mashariki (EATV) nchini Tanzania. Pia inajumuisha vipindi
vya “Vioja Mahakamani” vinavyorushwa na televisheni mbalimbali nchini Kenya.
(b) Michezo ya Kuigiza
i. Maigizo ya watoto: mfano mzuri wa maigizo ya watoto ni michezo ya “cha
baba na mama” ambapo mtoto mmoja hujifanya baba, mwingine mama na
mwingine jogoo. “Baba” na “mama” huigiza matendo ya baba na mama halisi na
hata wanapoenda kulala, hulala pamoja. Kazi za jogoo huwa ni kuwika pindi
baba na mama wanapolala ili kuwaamsha.
ii. Maigizo ya msibani
iii. Maigizo ya sherehe
iv. Maigizo ya kidini
(c) Miviga
Kumekuwa na utata kuhusiana na ufasihi wa utanzu huu. Utata huo unatokana na
ukweli kwamba kuna baadhi ya mambo yanayotendeka katika miviga si fasihi hasa
bali huweza kuwa sanaa nyingenezo. Ikumbukwe kuwa fasihi ni sanaa itumiayo
lugha (maneno). Hivyo, kinachochukuliwa kuwa fasihi katika miviga ni matini na si
matendo yasiyo na maneno. Katika matambiko, kwa mfano, maneno, manuizo na
nyimbo zinazoambatana na tukio husika ndiyo fasihi simulizi lakini si matendo
yanayotendwa yasiyokuwa na maneno. Katika jando na unyago pia matini na
nyimbo na baadhi ya maigizo yenye maneno ndizo kazi za fasihi. Matendo ambayo
hayana maneno hayawezi kuwa fasihi. Hivyo, vipera vya utanzu huu vinapaswa
kuchunguzwa kwa tahadhari kubwa. Miongoni mwa vipera hivyo ni kama ifuatavyo:
(i) Matambiko
(ii) Jando
(iii) Unyago
(iv) Sherehe za kutolea majina
18
6. FASIHI NGOMA
Utanzu wa fasihi ngoma katika fasihi simulizi unasemwa kuwa ni miongoni mwa tanzu
kongwe sana kwani ulianza sambamba na uumbaji wa dunia. Ushe (2012) akimnukuu Melvin
(1975) anabainisha hili anaposema:
The Talking Drum is the cultural instrument which have endured and survived the test of
time up to the present generation. The history of the Talking Drum is as old as creation
itself. In many parts of Africa, the Talking Drum is used as means of notification,
alertness and entertainment of people in palaces or during ceremonies.
Ngomezi ni zana ya kitamaduni ambayo imepitia vizazi mbalimbali hadi kufikia kizazi
cha sasa. Historia ya ngomezi ni kongwe kama ilivyo historia ya uumbaji wenyewe.
Katika sehemu nyingi za Afrika, ngomezi hutumika kama njia ya mawasiliano, kutoa
tahadhari na kuburudisha watu katika makasri ya Wafalme na watawala au wakati wa
sherehe (Tafsiri yetu).
Nukuu hii inathibitisha kuwa utanzu huu umekuwapo katika jamii za Kiafrika kwa muda mrefu.
Hata hivyo, kwa upande mwingine, utanzu huu ni mchanga kuliko tanzu nyinginezo za fasihi
simulizi na si utanzu unaoeleweka vizuri sana miongoni mwa wanafunzi wa fasihi. Tunauchukulia
kuwa ni mchanga kutokana na ukweli kuwa ni utanzu ambao haujaanza kubainishwa zamani sana
japo umekuwapo katika jamii mbalimbali kwa muda mrefu. Labda kutotambulika kwake
kulitokana na wanafasihi kusita kuitambua ngoma kama kazi ya fasihi. Ngoma kwa uasili wake
huonekana kama aina ya sanaa za maonesho (Mhando na Balisidya, 1976:7), lakini si fasihi kwa
kuwa fasihi ni sanaa ambayo ni lazima itumie lugha kuwasilisha maudhui kwa jamii lengwa. Kwa
kuwa ngoma katika makabila mengi huwa ni midundo tu isiyokuwa na lugha yoyote itokayo katika
midundo hiyo, wanafasihi wengi waliacha kubainisha uwezekano wa kuwa na fasihi ngoma.
Ukweli ni kuwa upo uwezekano wa kuwa na ngoma ambayo inatoa lugha (maneno). Ngoma hizo
kwa kawaida huwa ni tofauti na ngoma za kawaida na ndiyo maana wanafasihi wengi huziita
ngomezi.
Sababu ya pili iliyosababisha utanzu wa ngoma kuchelewa kubainishwa na wanafasihi ni
kuwa aina hii ya fasihi haipatikani katika jamii nyingi sana kama zilivyo tanzu nyingine za fasihi
simulizi. Utanzu huu unasemwa kuenea sana katika jamii za Afrika Magharibi na tafiti za hivi
karibuni zimejaribu kubainisha kuwa upo uwezekano wa fasihi hii kuwapo katika jamii za Afrika
Mashariki (taz. Mulokozi, 1996).
Utanzu wa fasihi ngoma au ngomezi kama unavyoitwa na wengine, umeelezwa sana na
Kwabena Nketia katika maandiko yake mbalimbali. Nketia ni profesa na mtaalamu wa muziki
aliyefanya tafiti nyingi katika miziki asilia ya Kiafrika na kuandika vitabu mbalimbali kikiwemo
The Music of Africa (1974). Katika utafiti wake kuhusu ngoma, Nketia alibaini kuwa kuna aina
tatu za ngoma. Ambazo ni ngoma za ishara (signal drumming), ngoma za kuchezwa (dance
drumming) na ngoma za kifasihi/ngomezi (talking drums). Uainishaji huu unatupa ufahamu kuwa
si kila aina ya ngoma ni ngoma za kifasihi (ngomezi); zipo ngoma ambazo hazina ufasihi wowote.
Ufasihi wa ngomezi unatokana na ukweli kuwa ni ngoma ambazo hugeza vidatu na toni za lugha
ya mazungumzo. Milio ya ngomezi inaweza kurekebishwa kulingana na jinsi wapigaji
wanavyozipiga na kubadilisha nguvu wanayoitumia katika kupiga. Mapigo hayo, kwa hiyo, hugeza
sauti ya watu wanaoongea na ndiyo maana huitwa ngomezi (Ushe, 2010 na 2012). Fasihi ngoma
hutoa sauti za kimapokeo zilizozoeleka katika jamii kama vile methali au majigambo na hivyo
kueleweka kirahisi miongoni mwa wanajamii. Neno la Kiingereza la utanzu huu “talking drums”
linasawiri uhalisi wa kile ngoma hizi zinachokifanya; ngoma hizi zinaongea. Hivyo, ngomezi ni
tofauti na aina nyingine za ngoma ambazo haziongei bali hutoa midundo tu kwa maksudi maalum
kama vile kuburudisha, kutoa taarifa na kadhalika. Aidha, ngomezi hazikueleweka kwa mtu yeyote
bali kwa watu wenye ujuzi na lugha inayogezwa. Vilevile, ngoma hizi zilipigwa na wapigaji
maarufu waliobobea katika upigaji wake, si kila mtu aliweza kuzipiga ngoma hizi.
Nketia (1963) anabainisha kuwa katika historia ya Afrika, fasihi ngoma imekuwa ikitumika
kwa malengo mbalimbali. Malengo hayo, hata hivyo, yamekuwa yakibadilika kulingana na wakati
19
na jamii husika. Kwa mfano, tunaona anayataja malengo ya fasihi ngoma katika jamii za jadi za
Kiafrika kuwa ni pamoja na kutoa taarifa kwa vijiji vya mbali na kuwaleta watu pamoja kama vile
kuitisha mikutano. Malengo mengine anayoyataja ni kusaidia kusuluhisha migogoro miongoni
mwa wanajamii na kutunza kumbukumbu muhimu za kihistoria na hivyo kuwakumbusha watu
matukio hayo ya kihistoria pindi zinapopigwa. Mbali na matumizi hayo anayoyataja Nketia, Ebeze
(2002) naye kama anavyonukuliwa na Ushe (2012) anabainisha matumizi ya fasihi ngoma katika
jamii nyingine za jadi za Kiafrika kuwa ilitumika pia wakati wa sherehe, kama vile sherehe za
kusimika watawala na machifu, harusi, sherehe za kutoa majina au sherehe za mazishi ya watu
maarufu. Ushe anaendelea kueleza kuwa zilipopigwa wakati wa kusimikwa watawala na machifu,
ngomezi ziliwatahadharisha watawala na machifu hao kutofanya mambo yasiyokubalika
yatakayowafanya wajute. Akizungumzia matumizi ya ngomezi katika jamii za kisasa, Nketia
(1963) anasema kwamba fasihi ngoma inatumika kutukuza au kuwalaani watu wengine na
kuwakaribisha wageni, kuisifu miungu na watu katika jamii, kuita mizimu, wahenga na mizuka,
kusahihisha makosa ya wanajamii, kutoa mazungumzo ya kimethali ili kuwawezesha watu
kuwasiliana na wazee na pia ni sehemu ya sherehe za kifalme au majigambo ya wahenga (maelezo
haya yanabainika pia katika Ushe (2007) na (2012)). Hii inabainisha kuwa malengo na matumizi
ya fasihi ngoma, kama ilivyo kwa tanzu nyingine za fasihi simulizi, ni mambo
yanayobadilikabadilika kulingana na jamii na wakati.
Mbali na matumizi hayo yanayobainishwa na wataalamu hao, matumizi ya fasihi ngoma
yameendelea kupanuka kadri muda unavyozidi kwenda. Kwa mfano, kuanzia karne ya 20
imeshuhudiwa ngomezi zikitumika katika muziki pendwa wa Afrika Magharibi. Fasihi ngoma
imetumika katika aina mojawapo ya muziki wa Senegal uitwao Mbalaksi. Pia imetumika katika
miziki ya Nijeria iitwayo Fuji na Jùjú (katika miziki hiyo ngomezi huitwa dùndún). Aidha,
tunaona wanamuziki wakizitumia ngomezi kwenye miziki yao ya kisasa. Mfano wa wanamuziki
hao ni kama vile Tom Waits ambaye amezitumia ngomezi kwenye wimbo wake uitwao "Trouble's
Braids," iliyo katika albamu iitwayo Swordfishtrombones na Erykah Badu aliyezitumia ngomezi
kwenye wimbo wake "My People," katika albamu iitwayo New Amerykah Part One (4th World
War). Wanamuziki wengine waliotumia ngomezi kwenye miziki yao ya kisasa ni King Crimson
ambaye alizitumia ngomezi kwenye wimbo wake utwao, "The Talking Drum" katika albamu
iliyopewa jina Larks' Tongues in Aspic na mwanamuziki wa Kinijeria anayechukuliwa kuwa
mahiri katika ngomezi Sikiru Adepoju, aliyezitumia ngomezi katika nyimbo zake
alizowashirikisha wasanii maarufu wa Ulaya na Marekani kama vile Stevie Wonder na Carlos
Santana. Mbali na kutumika kwenye miziki ya kisasa, ngomezi pia zimetumika kwenye filamu na
tamthilia. Mfano mzuri wa matumizi haya tunayaona katika filamu ya The Nun's Story iliyotolewa
mwaka 1959.1 Mabadiliko haya ya matumizi ya fasihi ngoma yanaunga mkono madai ya Samwel
(2012a) kuwa si kweli kwamba tanzu za fasihi simulizi hurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi
kingine, bali hubadilika kulingana na wakati husika.
Kutokana na maelezo haya tunaungana na Samwel (2012b) kuwa fasihi ngoma huweza
kuainishwa katika aina kama vile fasihi ngoma za Taarifa, fasihi ngoma za Tahadhari, fasihi
ngoma za Uhusiano, fasihi ngoma za Tumbuizo. Fasihi ngoma za taarifa ni zile ambazo hupigwa
kwa lengo la kutoa taarifa fulani muhimu wakati ambapo fasihi ngoma za tahadhari hutoa onyo
kama tulivyoona hapo awali kuwa huweza kuwaonya watawala na machifu juu ya uongozi mbaya.
Aidha, fasihi ngoma za mahusiano ni zile zinazopigwa na vijana ili kuwasiliana na wazee wao
kama tulivyoona hapo awali. Fasihi ngoma za tumbuizo hujumuisha ngomezi zitumikazo katika
miziki na tanzu nyingine kwa lengo la kutoa burudani. Aina nyingine ambayo ni muhimu
kuiongeza hapa ni fasihi ngoma za miungu na mizimu. Hizi ni zile zinazopigwa ili kuwasifu na
kuwaabudu miungu na mizimu.
1 Maelezo haya kuhusiana na matumizi ya ngomezi kwenye tanzu mbalimbali za kisasa yamedondolewa katika mitandao
mbalimbali ikiwa ni pamoja na http://en.wikipedia.org/wiki/File:TalkingDrum.jpg
20
NB: Katika uainishaji huu tumefafanua/tumefasili dhana zile ambazo tunadhani ni ngeni au si maarufu
sana na kuziacha zile maarufu/zilizozoeleka. Aidha, tumefasili pia dhana ambazo uainishaji wetu ni
tofauti sana na uainishaji wa wataalamu mbalimbali waliotangulia na hivyo kama tusipozifafanua
zinaweza kufasiliwa zisivyostahili.
NUDHUMU SIMULIZI
Tanzu nudhumu simulizi ndiyo huitwa na wanafasihi wengine ushairi simulizi kwa kuwa
hapo awali haukuandikwa. Utanzu huu unaainishwa hapa kuwa ni wa kwanza. Tunauchukulia hapa
kuwa ni wa kwanza kwani wanafasihi wengi wanatoa madai ambayo tunayaunga mkono kwamba
ushairi au nudhumu kama tunavyouita hapa, ndiyo utanzu mkongwe zaidi katika historia ya fasihi
simulizi. Utanzu huu ulianza pale mwanadamu alipotoka kwenye uhayawani na kuanza kuzalisha
mali. Ili kuondoa machovu ya kazi, mwanadamu alianza kuimba tungo za kinudhumu ama nyimbo
na huo ndiyo ukawa mwanzo wa utanzu huu (Senkoro, 1988:1-2). Hivyo, nudhumu za kazi ndiyo
huchukuliwa kuwa ushairi wa mwanzo kabisa katika historia ya mwanadamu. Ushairi huu
uliwasilishwa kwa kutumia lugha mbalimbali za jamii husika. Utanzu huu unaonekana kuwa na
vipera viwili ambavyo ni nyimbo na maghani. Tuchambue baadhi ya nudhumu hizi simulizi kama
ifuatavyo:
I. NYIMBO
Nyimbo ni aina ya nudhumu ambayo huwasilishwa kwa toni ya uimbaji. Sauti hii ni tofauti na
vipera vingine vya fasihi simulizi ambavyo huweza kughanwa (maghani/ghani), kutongolewa
(tongozi) au kusemwa (masemezo). Hata hivyo wapo baadhi ya wanafasihi wanaodai kwamba upo
uwezekano wa nyimbo kughanwa, kutongolewa au kusemwa. Jambo hili kama tutalikubali basi
tunapaswa kujiuliza tofauti kati ya nyimbo, maghani na mighani ipo wapi sasa? Katika kitabu hiki
tutazijadili dhana hizo kuwa ni tofauti. Uainishaji wa utanzu wa nyimbo umekuwa na
mkanganyiko mkubwa sana miongoni mwa wanazuoni kwani kila mwanafasihi ameainisha utanzu
huu kwa kutumia mkabala wake. Katika andiko letu tutaainisha utanzu wa nyimbo kwa kutumia
vigezo vikuu vinne: kigezo cha dhima ya nyimbo, kigezo cha maudhui yabebwayo na nyimbo,
kigezo cha mahali/muktadha zinapoimbwa nyimbo na kigezo cha fanani/hadhira ya nyimbo husika.
(a) Uainishaji wa Utanzu wa Nyimbo kwa Kigezo cha Dhima
Dhima, kama inavyochukuliwa hapa, inarejelea kazi au jukumu. Hivyo, katika kigezo hiki
tunaainisha nyimbo kwa kuangalia kigezo cha kazi inayofanywa na nyimbo husika katika jamii.
Nyimbo huweza kuwa na kazi ya kutumbuiza, kutukuza au kuchapuza kazi. Pia nyimbo huweza
kutumika kubembelezea mtu, kuomboleza misiba na majanga mbalimbali na kadhalika. Hivyo,
kwa kutumia kigezo hiki, tuna aina kuu tatu za nyimbo ambazo ni tumbuizo, tukuzo na chapuzo.
(i) Tumbuizo
Neno “tumbuizo” linatokana na neno “tumbuiza.” Kitenzi kinapowekewa mofu “o” huashiria
matokeo kama ilivyo katika “piga” ambacho huzaa “pigo,” “imba” huzaa “wimbo” na kadhalika.
Hivyo, matokeo ya kutumbuiza ni tumbuizo. Tumbuizo ni nyimbo zinazotumbuiza yaani
zinazoburudisha na kusahaulisha machungu yaliyopo kwa wakati husika. Nyimbo hizi hutoa burudani
na kuliwaza. Tumbuizo huwa ni pamoja na bembelezo, yaani nyimbo za kubembelezea watoto na
mbolezo-nyimbo za misibani na katika majanga. Mtoto anapokuwa analia kutokana na sababu
mbalimbali anahitaji kitu cha kumtumbuiza ili aache kulia. Nyimbo huweza kufanya kazi hiyo na hivyo
kumtumbuiza mtoto hadi anyamaze na hata kulala. Vivyo hivyo panapotokea misiba mbalimbali watu
huimba nyimbo za kuliwazana na kujiliwaza ili kujisahaulisha misiba iliyowapata. Nyimbo hizi pia
huweza kutumika kupeana tumaini kwamba msiba uliotokea upo juu ya uwezo wa mwanadamu yeyote
na kwamba zaidi ya msiba husika bado kuna tumaini.
(ii) Tukuzo
Tukuzo ni neno linalotokana na kitenzi “tukuza.” Hivyo, tukuzo ni nyimbo ambazo zinakusudia
kumsifia na kumpa utukufu mtu binafsi au kikundi maalumu cha watu. Nyimbo za tukuzo huweza
21
kuwa zile zinazoimbwa kumsifia Mungu, mke na mume wakati wa ndoa, viongozi wa siasa na vyama
vyao, wapigania uhuru na vyama vyao na pia huweza kujumuisha nyimbo za uzalendo katika taifa
ambazo nyingine husifia taifa husika. Mfano mzuri wa nyimbo za tukuzo ni wimbo ufuatao wa dini ya
Kikristo:
Mwamba wenye imara
Kwako nitajificha
Maji hayo na damu
Yaliyotoka humu
Hunisafi na dhambi
Hunifanya mshindi
Kwa kazi zote pia
Siitimiza sharia
Nijapofanya bidii
Nikilia na kudhii
Hayaishi makosa
Ndiwe wa kuokoa
Sina cha mkononi
Naja msalabani
Nili tupu nivike
Ni mnyonge nishike
Nili mchafu naja
Nioshe nisijafa
Nikungojapo chini
Nakwenda kaburini
Nipaapo mbinguni
Na kukwona enzini
Roho yangu na iwe
Rahani mwako wewe
(Wimbo huu umenukuliwa kutoka katika Musoma Press (1998:58) Tenzi za Rohoni)
Wimbo huu unamtukuza Mungu wa Ukristo, “YEHOVA” kwamba ni Mungu mwenye nguvu. Nguvu
zake zinafananishwa na mwamba. Mwamba ni kitu kigumu ambacho mtu huweza kujificha na
asidhurike na jambo baya. Katika tukuzo hii ya dini tunaona kwamba Mungu anapewa uwezo mkubwa
sana kwamba yeye ndiye anayewasaidia wanadamu kushinda na ndiye mwokozi. Wakati ambapo
Mungu anatukuzwa namna hiyo mwanadamu anajidogosha kabisa na kujifanya kwamba ni kiumbe
kisichokuwa na uwezo wowote. Hii ni kawaida ya tukuzo nyingi, wakati ambapo kitu fulani kinasifiwa
kitu kingine hudogoshwa ili kukifanya kinachotukuzwa kionekane kikubwa zaidi (pawe na
mchomozo2). Hii inatokana na ukweli uliodhahiri katika lugha kwamba vitu vipo katika mfumo. Ili
tukijue kizuri hatuna budi kuwa na kibaya, vivyo hivyo ili tumjue mrefu hatuna budi kumjua mfupi.
Wakati wote tukiambiwa fulani ni mzuri tunajiuliza kuliko nani?
(iii) Simango
Maghani ambayo dhima yake kuu ni kumsimanga mtu fulani juu ya mambo aliyoyafanya au
anayoaminika kuyafanya na sifa alizonazo mtu au anazoaminika kuwa nazo. Kwa kawaida mambo
anayosimangiwa mtu huwa ni mabaya na hayakubaliki katika jamii husika.
(iv) Chapuzo
Chapuzo ni nyimbo zinazochapusha kazi. Aina za nyimbo hizi zilitegemea kazi iliyofanywa
na hivyo tulikuwa na nyimbo za uvuvi na ubaharia (kimai), nyimbo za kutwangia na kupepetea, nyimbo
za mapigano vitani na nyimbo za michezo ya watoto. Nyingine ni nyimbo za kilimo (wawe), nyimbo za
kusukia, nyimbo za upagazi, nyimbo za biashara na uchuuzi na kadhalika. Nyimbo hizi huweza kuwa
nyingi zaidi ya tulivyoziainisha hapa kwani kuna kazi za aina mbalimbali.
2 Mchomozo ni ile hali ya kitu kujitokeza au kujichomoza zaidi ya kitu kingine. Kitu chenye mchomozo huonekana zaidi ya
vingine visivyokuwa na mchomozo.
22
(b) Uainishaji wa Nyimbo Kimaudhui
Katika kigezo cha maudhui, nyimbo huainishwa kwa kuangalia yale yaliyomo ndani ya nyimbo
husika. Tunaangalia ikiwa wimbo husika unabeba maudhui ya kisiasa, kidini, kiuchumi, kijamii au
kiutamaduni. Hivyo, tunaweza kuwa na aina mbalimbali za nyimbo kama vile:
(i) Nyimbo za kisiasa: kama vile nyimbo za kishujaa na kizalendo
(ii) Nyimbo za kiuchumi: kama vile nyimbo za kilimo
(iii)Nyimbo za kijamii: kama vile nyimbo za mapenzi
(iv)Nyimbo za kiutamaduni: kama vile nyimbo za dini
(c) Uainishaji wa Nyimbo kwa Kifanani/Hadhira
Katika kigezo hiki tunaangalia fanani na/au hadhira wa nyimbo husika. Kinachozingatiwa ni
ikiwa fanani na/au hadhira ni wanawake au wanaume, ni vijana, wazee au watoto na kadhalika. Hivyo
kwa kutumia kigezo hiki tunaweza kupata aina zifuatazo za nyimbo:
(i) Nyimbo za wanawake
(ii) Nyimbo za wanaume
(iii)Nyimbo za wazee
(iv)Nyimbo za vijana
(v) Nyimbo za watoto
(d) Uainishaji wa Nyimbo Kimuktadha
Kigezo cha muktadha kinazingatia nyimbo husika huimbwa wapi na kwa ajili gani? Nyimbo
huweza kuimbwa jandoni na unyagoni, katika nyumba za ibada kama vile makanisani na misikitini,
katika harusi, katika tambiko na kadhalika. Hivyo kwa kigezo hiki tunapata aina zifuatazo za nyimbo:
(i) Nyimbo za tohara (nyimbo za jandoni na unyagoni)
(ii) Nyimbo za harusi
(iii) Nyimbo za tambiko
(iv) Nyimbo za kisimani
(v) Nyimbo za majumba ya ibada n.k.
II. MAGHANI
Maghani ni aina ya ushairi inayotumia sauti iliyo kati ya kuimba na kuongea, sauti hiyo huitwa sauti
ya kughani. Tofauti ya nyimbo na maghani ni kwamba wakati nyimbo hutumia sauti ya kuimba,
maghani hutumia sauti ya kughani. Maghani huweza pia kutongolewa. Uainishaji wa maghani
unatumia vigezo vikuu viwili ambavyo ni kigezo cha dhima na kigezo cha utendaji.
(a) Uainishaji wa Maghani kwa Kigezo cha Dhima
Kuainisha maghani kwa kuzingatia dhima ni kama tulivyoainisha nyimbo. Maghani, kama zilivyo
nyimbo, huweza kuwa na dhima ya kutumbuiza, kuburudisha na kadhalika. Hivyo, miongoni mwa aina
za maghani kwa kigezo hiki ni kama ifuatavyo:
(i) Maghani Tumbuizo
Haya ni maghani ambayo hulenga kutoa burudani. Hili ni kundi ambalo huweza kujumuisha pia
aina nyingine za maghani kwani maghani, kama kazi nyingine za fasihi, huwa na dhima kuu mbili
ambazo ni kuelimisha na kuburudisha. Katika kuburudisha ndipo kwenye dhima ya kutumbuiza.
(ii) Maghani Tukuzo/Sifo
Aina hii ya maghani huhusisha tungo ambazo hueleza sifa za mtu binafsi (majigambo) ama
tungo za mtu mwingine (tondozi). Katika majigambo, mjigambi hujitukuza mwenyewe juu ya mambo
mbalimbali ya kishujaa na kijasiri aliyoyafanya au anayoyaamini kuyafanya kwa uwezo wake au kwa
nasaba yake. Tondozi kwa upande mwingine, ni maghani ambazo hutukuza kwa kuelezea sifa za mtu
mwingine, kitu kingine au hata miungu na mizimu.
23
(iii) Maghani Simango
Hii ni aina ya maghani ambayo dhima yake kuu ni kumsimanga mtu fulani juu ya mambo
aliyoyafanya au anayoaminika kuyafanya na juu ya sifa alizonazo mtu au anazoaminika kuwa nazo.
Kwa kawaida, mambo anayosimangiwa mtu huwa ni mabaya na hayakubaliki katika jamii husika.
(b) Uainishaji wa Maghani kwa Kigezo cha Utendaji
Katika kigezo hiki tunaangalia ikiwa fanani anasema na nafsi yake au na nafsi ya mtu mwingine na
ikiwa anawasilisha kwa njia ya kusimulia au nyinginezo. Hivyo, katika kigezo hiki kuna aina kuu mbili
kama ifuatavyo:
(i) Maghani nafsia
(ii) Maghani simulizi
2. USHAIRI KAMA UTANZU WA FASIHI ANDISHI
Zaidi ya ushairi kuwa utanzu wa fasihi simulizi, ushairi pia ni utanzu wa fasihi andishi. Uainishaji
wa tanzu katika fasihi andishi, kama ulivyo katika fasihi simulizi, si suala jepesi. Kimazoea wataalamu
wengi wamekuwa wakidai kwamba fasihi andishi ina tanzu kuu tatu ambazo ni ushairi, tamthilia na
riwaya. Mtazamo huu huenda ndiyo uliowaathiri hata watunga mitaala katika shule na vyuo mbalimbali
nchini Tanzania na ndiyo maana katika nchi hii tanzu za fasihi andishi zinazosomwa katika shule na
vyuo vingi ni ushairi, tamthilia na riwaya. Kwa mfano, katika elimu ya sekondari, katika fasihi andishi
wanafunzi wanafundishwa tanzu hizo tatu. Hali kama hiyo inaonekana pia katika miongozo ya kozi ya
fasihi andishi ya vyuo vingi, ikiwa ni pamoja na chuo kikuu kikongwe kuliko vyote nchini Tanzania,
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo tanzu zinazofundishwa kwa msisitizo zaidi ni tatu tu, ushairi,
tamthilia na riwaya. Hii ina maana kwamba wataalamu hawa hawautambui utanzu wa hadithi fupi.
Aidha, nafasi ya utanzu wa novela katika fasihi andishi haiwekwi wazi, yaani ikiwa ni utanzu
unaojitegemea au ni sehemu ya utanzu wa riwaya. Kutokana na hilo tanzu za novela na hadithi fupi si
tanzu zinazoeleweka sana miongoni mwa watu wengi.
Hivyo, ili kurekebisha kasoro hizo, tunapendekeza kwamba fasihi andishi ichukuliwe kuwa na
tanzu kuu nne ambazo ni ushairi, tamthilia, hadithi fupi na riwaya. Novela tunaichukulia kuwa ni
sehemu ya riwaya. Hata hivyo, katika andiko hili msisitizo wetu ni katika utanzu wa ushairi na
hatutachambua tanzu nyingine za fasihi andishi.
DHANA YA USHAIRI ANDISHI WA KISWAHILI
Kabla ya kuzama katika dhana ya ushairi andishi, kwa kuwa tunashughulikia ushairi andishi wa
Kiswahili, hatuna budi kujiuliza ushairi wa Kiswahili ni upi? Swali hili si rahisi kulijibu kwani
linaturudisha katika swali lilelile la miongo mingi la Mswahili ni nani hasa? Je, Mswahili ni mtu wa
pwani, ni mtu wa Tanzania, ni mtu wa Afrika Mashariki au Mswahili ni nani? Vivyo hivyo katika
mawanda hayo twaweza kujiuliza fasihi ya Kiswahili ni ipi? Je, ni fasihi iliyoandikwa kwa lugha gani?
Je, kila kazi ya fasihi iliyoandikwa kwa lugha ya Kiswahili ni fasihi ya Kiswahili? Na kama
haijaandikwa kwa lugha ya Kiswahili si fasihi ya Kiswahili? Tukiweza kuyajibu maswali hayo,
tutaweza pia kufafanua ushairi wa Kiswahili ni upi. Ili kukwepa kuurudia mjadala ambao umekufa,
tuchukulie tu kwamba ushairi wa Kiswahili ni ule unaosawiri maisha, mila na utamaduni wa Waswahili
pwani na bara. Mtazamo huo umeathiriwa na fasili ya Senkoro (1988:10-11) katika kitabu chake
Ushairi: Nadharia na Tahakiki kuwa ushairi wa Kiswahili ni ule unaojitambulisha na kujihusisha na
utamaduni wa Waswahili (yaani wananchi wa Afrika Mashariki na kati – pwani na bara). Tukiichukua
fasili hii katika muktadha wa fasihi ya Kiswahili kwa ujumla, tutasema kwamba fasihi ya Kiswahili ni
ile inayojitambulisha na kujihusisha na maisha na utamaduni wa Waswahili. Utamaduni unasemwa
kuwa ni jumla ya mambo yote ya jamii husika. Hivyo, utamaduni wa Waswahili hapa tunahusisha mila
na desturi za Waswahili; Sanaa zao, siasa, sayansi na uchumi wao, na maisha kwa ujumla. Hata hivyo,
Senkoro (khj) anaongezea jambo lingine kwamba ushairi wa Kiswahili unapaswa kuwa katika lugha ya
Kiswahili. Rejelea nukuu hii anaposema:
Zamani sana lugha ya Kiswahili ilikuwa ya watu wa pwani ya Afrika Mashariki tu. Lakini leo
hii hutumika Afrika Mashariki yote pamoja na nchi za jirani kama vile Zaire (sasa Jamhuri ya
24
Kidemokrasia ya Kongo), Burundi, Somalia na Malawi. Kwa hiyo ni wazi kwamba
tukiongelea kuhusu ushairi wa Kiswahili mara nyingi tunamaanisha ule ushairi uliotungwa
kwa lugha ya Kiswahili.... (Ufafanuzi na msisitizo ni wetu).
Hapa tunaona kwamba Senkoro (khj.) anasisitiza kwamba ushairi wa Kiswahili unapaswa kutungwa
katika lugha ya Kiswahili. Hata hivyo tunadhani kwamba jambo hili si wakati wote kwani upo
uwezekano wa ushairi wa Kiswahili (na kwa hiyo fasihi ya Kiswahili) kuandikwa katika lugha
nyinginezo. Hili haliishii tu katika ushairi na fasihi bali pia katika vipengele vingine vya lugha.
Tunalithibitisha hili, kwa mfano, katika andiko la Ashton (1944) ambaye ameandika Swahili Grammar
Including Intonation. Kitabu hiki japokuwa kinaihusu sarufi ya Kiswahili, kimeandikwa kwa kutumia
lugha ya Kiingereza. Kutumia lugha ya Kiingereza hakuipotezei sarufi iliyoandikwa sifa ya kuwa sarufi
ya Kiswahili. Kwa kulifahamu hilo labda ndiyo maana Senkoro hapo juu anasema (... tukiongelea
kuhusu ushairi wa Kiswahili mara nyingi...). Bila shaka anatambua kwamba inaweza kutokea mara
chache ukatungwa kwa lugha nyinginezo. Jambo hili kwa sasa limeongezeka zaidi na kuwa si mara
chache tena bali ni mara nyingi tu inawezekana kuandika ushairi wa Kiswahili kwa lugha nyinginezo au
kuandika ushairi wa lugha nyinginezo kwa kutumia lugha ya Kiswahili.
Hivyo, tuhitimishe kwa kusema kwamba ushairi wa Kiswahili kama unavyochukuliwa hapa ni ule
ambao unahusu utamaduni wa Waswahili bila kujali lugha iliyotumika kuuandika. Jambo la kusisitiza
hapa ni kwamba mambo yanayosawiriwa katika ushairi husika yaihusu jamii ya Waswahili, maisha
yao, falsafa zao na itikadi zao. Dhana ya Waswahili inayotumika hapa inamaanisha watumiaji wa lugha
ya Kiswahili katika shughuli zao za kila siku.
Baada ya kufahamu fasihi ya Kiswahili ni ipi na ushairi wa Kiswahili ni upi sasa turudi kwenye
suala letu la msingi kuhusiana na dhana ya ushairi. Pamekuwapo na fasili mbalimbali juu ya dhana ya
ushairi. Shabaya na wenzake (2009:1) wanatuthibitishia hili kwa kunukuu fasili kadha wa kadha za
ushairi zilizokwisha kutolewa hadi sasa. Baadhi ya fasili wanazozinukuu ni kama ifuatavyo:
· Ushairi ni mfuatano wa hisia nzito zilizokumbukizwa kutokana na utulivu (William
Wordsworth)
· Ushairi ni sauti za lugha ya binadamu katika nyakati ambapo zinakuwa karibu sana na sauti
za malaika na sauti za wanyama (John Wain)
· Ushairi ni maneno bora katika mpangilio bora (Samuel Taylor Coleridge)
· Ushairi ni habari inayobaki kuwa habari (Ezra Pound)
· Ushairi ni ule utungo ambao ni wa kifalsafa zaidi na wa thamani kubwa kuliko historia
(Aristotle)
· Ushairi unaanza kwa uzuri na kuishia kwa busara (Robert Frost)
(Tafsiri zote hapo juu ni zetu)
Hizi ni baadhi tu ya fasili zinazotolewa na Shabaya na wenzake (2009) na hivyo kuthibitisha kwamba
kuna fasili nyingi sana za ushairi. Fasili hizo, hata hivyo, zaidi ya wingi wake, tunazigawa, na ndivyo
zilivyogawiwa pia na wanazuoni wengine, katika mikabala mikuu miwili, mkabala wa kimapokeo na
mkabala wa kimamboleo (Taz. Senkoro, 1988; Mulokozi, 1996 na Githuma, 2010). Dhana “mapokeo”
kama inavyotumika hapa inarejelea ujadi au ukongwe. Hivyo, mkabala wa kimapokeo ni ule ambao
umekuwapo kwa muda mrefu katika historia ya ushairi. Mkabala wa kimamboleo, kwa hiyo, ni ule wa
kisasa. Yaani mkabala ambao umeibuka baada ya mkabala wa kimapokeo.
A. MKABALA WA KIMAPOKEO JUU YA DHANA YA USHAIRI
Mkabala huu ndiyo ulioanza katika kutoa fasili ya ushairi. Unaitwa wa kimapokeo kutokana na
ukweli kwamba wafuasi wa mkabala huu waliupokea kutoka kwa wazee bila kuhoji ikiwa mambo
yanavyoelezwa ndivyo yalivyo au la. Wao waliurithi tu. Dhana hii ya umapokeo ni tafsiri ya ile dhana
ya Kiingereza “traditional approach.” Miongoni mwa wanamapokeo wanaojulikana zaidi ni kama vile
Amri Abedi, Shaaban Robert, Jumanne Mayoka, Amiri A. Sudi (Andanenga), Haji Gora Haji na
wengineo. Wanamapokeo hawa wamewaathiri wengi na hadi sasa pameshakuwapo na wanamapokeo
wengi tu. Hebu tupitie fasili chache za kimapokeo:
Gituma (2010) anafasili shairi kuwa ni mtungo wa kisanaa wenye mpangilio maalum wa lugha ya
mkato katika usemi, maandishi au wimbo unaoelezea wazi juu ya mawazo, hisi au tukio juu ya maisha
na ambao hufuata utaratibu wa urari na muwala maalum uliosheheni kanuni za utunzi wa mashairi…
25
Fasili hii inasisitiza kwamba “shairi ni wimbo, shairi huwa na urari (bila shaka wa vina na mizani),
shairi huwa na kanuni mbalimbali.” Maeneo haya anayoyasisitiza Gituma bila shaka yametokana na
athari za Abedi (1954:1) ambaye imani hiyo ilimfanya kuandika kitabu alichokiita Sheria za Kutunga
Mashairi na Diwani ya Amri. Jambo la dhahiri hapa ni kwamba Amri Abedi, kama alivyo Gituma,
anaamini kwamba utunzi wa mashairi una kanuni maalum. Aidha, wazo la Gituma kwamba shairi ni
wimbo linabainika pia humo katika Amri Abedi na anaongeza kwamba kama shairi haliimbiki basi
halina maana. Mtazamo huu kwamba shairi ni wimbo ndiyo unaotawala sana miongoni mwa
wanamapokeo wengi na tunauona pia kwa Mwaruka (1968) anaposema kwamba:
Mpaka miaka hii ya karibuni watunzi na waimbaji mashairi na tenzi katika nchi yetu
wameongezeka sana. Tena inafurahisha mno kuona kwamba utungaji wa mashairi unafundishwa
katika shule zetu za Tanzania. Kwa hivi, inadhihirika kwamba baada ya miaka michache
Tanzania itakuwa na watungaji na waimbaji wengi zaidi (msisitizo ni wetu).
Katika maelezo haya Mwaruka anasisitiza uimbikaji wa shairi na tenzi. Hii ni kusema kwamba
anachukulia kuwa shairi linatungwa ili liimbwe na hadhira husika. Wazo hili la Mwaruka linapewa
nguvu na fasili ya Uvetie (1976) anaposema kwamba, “napenda kuwafafanulieni kwamba mashairi ni
usemi usemwao kwa namna ya mafumbo, na pia ni nyimbo.” Yeye zaidi ya kusisitiza ushairi kuwa ni
wimbo, anaibua dhana nyingine kwamba shairi lazima liwe fumbo. Hii ni kusema kwamba kama shairi
si fumbo basi si shairi. Aidha, Mnyampala (1964:4) anabainisha kwamba mashairi ni nyimbo zenye
maghani ya mvuto wa madoido na vingorimbo bora. Hapa Mnyampala zaidi ya kuungana na
wanamapokeo wengine kwa kuuona ushairi kuwa ni wimbo, anaongeza suala la mvuto wa madoido na
vingorimbo bora. Anachokisema hapa ni kwamba ushairi lazima utumie lugha tamu yenye madoido.
Dhana ya ushairi kama utamu wa lugha inaonekana pia kwa Uvetie (1976) ambaye anachagua kukiita
kitabu chake cha mashairi Utamu wa Lugha. Anachokionesha hapa ni kwamba ushairi hubeba utamu
wa lugha.
Fasili hizi (za wanamapokeo) zinachukulia kwamba shairi lolote lile lazima liimbike. Fasili hizi
zinaweza kuonekana kuwa sahihi zaidi katika fasihi simulizi ambapo utanzu wa ushairi (na hasa ushairi
simulizi) unachukuliwa kuwa ni wimbo. Kimsingi tunapozungumzia utanzu wa ushairi katika fasihi
simulizi tunazungumzia nyimbo za aina mbalimbali za makabila ya Kiafrika. Hivyo, fasili hii haifai
tunapozungumzia ushairi andishi, ambao ndiyo hasa tunauzungumzia hapa (hata hivyo, dhana ya shairi
kuwa ni wimbo ni muhimu kama tutakavyoijadili hapo baadaye katika sura ya tatu). Ushairi kama
wimbo ulionekana sana katika miaka ya awali ya maendeleo ya taaluma ya ushairi wa Kiswahili (kabla
ya mwaka 1960-1970). Baada ya hapo dhana ya ushairi kama wimbo ilipingwa vikali. Hadi sasa
inakubalika miongoni mwa wanazuoni, na katika fasihi ya Kiswahili kwamba, shairi si lazima liimbike.
Shairi linaweza kughanwa, kutongolewa au hata kusemwa. Kwa kusema kwamba shairi lazima
liimbike, Abedi ana maana kwamba shairi lazima liwe na urari wa vina na mizani. Mashairi
yanayopishana sana vina na mizani ni vigumu sana kuyaimba. Dhana hii ya urari wa vina na mizani
kama sifa kuu ya shairi imepingwa vikali na hatimaye kubainika kwamba shairi linaweza kuwa na urari
wa vina na mizani au lisiwe nao na bado likabaki kuwa shairi. Jambo la kukumbuka ni kwamba shairi
linapokosa urari wa vina na mizani kuna uwezekano mkubwa wa shairi husika kutokuimbika. Hivyo,
dhana ya shairi kama wimbo si ya msingi japo hatuwezi kuipuuza kabisa kwani inajaribu kutupa
upande mmoja wa shilingi wa shairi.
Zaidi ya msisitizo katika kanuni na uimbikaji, fasili nyingine za ushairi zimejikita zaidi katika
dhima ya ushairi. Kwa mfano, tunaona Mnyampala (1975) kwenye dibaji yake anaufasili ushairi kwa
kuzingatia nguvu ya shairi kuiasa, kuiongoza jamii pamoja na uzuri na utamu wa lugha. Anauona
ushairi kuwa ni utungo wenye maneno ya hekima na kwamba ndiyo utungo ulio bora sana katika
maongozi ya dunia. Anaendelea kufafanua kwamba kuna aina tano za mashairi kwa kuzingatia
maongozi na mafunzo yanayotoa. Aina hizo ni mashairi ya kawaida, mashairi ya furaha, mashairi ya
huzuni, mashairi mazito na mashairi ya kuadibu. Mashairi ya kawaida ni yale ambayo yana mawaidha
ya dunia, visa na mikasa ya kawaida na mengine ya aina hiyo wakati mashairi ya furaha hushangilia
tamasha iliyopo, kutakia heri na mafanikio, ombi la kudumisha furaha hiyo na waadhi kwa ajili ya
tafrija hiyo. Kwa upande wa yale yaliyomo katika mashairi ya huzuni Mnyampala anayataja kuwa ni
rambirambi, maombezi kwa Mungu kwa ajili ya marehemu, maombezi kwa wale waliobaki
26
wanaomhusu, historia ya marehemu na kumbukumbu itakiwayo. Nayo mashairi mazito huwa ni
mashairi ya kuzama (kufumba), mashairi ya tambo, pigo kuu la ushairi, furaha ya ushairi na taaluma
zake na kuonyesha mbinu za lugha ya mshairi yule. Aina ya mwisho ambayo ni mashairi ya kuadibu
inajumuisha mashairi ya kumuonya mtu kinagaubaga bila kutumia utusi, kumtanabahisha ya hatima,
mashairi kuhusu maandiko matakatifu na yale yahusuyo uungwana na kadhalika. Tunachokiona hapa ni
kwamba Mnyampala (khj.), zaidi ya kushadidia wazo la wanamapokeo kwamba ushairi ni lazima uwe
na urari wa vina na mizani, anasisitiza kuwa shairi lazima litoe mawazo yenye hekima yenye
kumwongoza mwanadamu. Wakati ambapo tunakubaliana na wazo hili la Mnyampala kuwa shairi
linaweza kumwongoza mwanadamu, tunaona kwamba ushairi unapaswa kufasiliwa kwa kuzingatia
nduni bainifu na si nduni jumuishi kwani tanzu zote za fasihi huwa na jukumu hilo la kumwongoza
mwanadamu. Moja ya dhima kuu za fasihi ni kuelimisha, hivyo ndiyo kusema tanzu zote za fasihi
huweza kuelimisha. Hata hivyo izingatiwe kwamba si kila shairi hubeba mawazo ya hekima na
linakusudia kutoa maongozi kwa jamii. Yapo mashairi mengi ambayo yanapotosha jamii. Fasihi zaidi
ya uwezo wake mkubwa wa kuielimisha jamii, inaweza pia kuipotosha jamii hiyo. Samwel (2012a)
akifafanua jinsi fasihi inavyoweza kupotosha jamii, isipochukuliwa kwa tahadhari, anaonyesha jinsi
ushairi wa Bongo Fleva unavyoweza kuhamasisha ngono na matendo mengine yasiyofaa katika jamii.
Aidha, tukizama zaidi katika uainishaji wa Mnyampala tunabaini kwamba kuna upungufu mkubwa.
Kwa mfano, anaposema kwamba mashairi ya kuadibu ndiyo huwaonya watu na kuwaadibisha juu ya
uungwana na maandiko matakatifu ni kusema kwamba mashairi anayoyaita ya kawaida (na ya aina
nyinginezo anazozianisha) hayamwadibishi hadhira katika maeneo hayo. Jambo hilo kwa hakika
linaweza kupingwa na wengi kwani mashairi ya aina zote anazozianisha Mnyampala yanaweza
kuadibisha juu ya hayo. Kama hiyo haitoshi, majina ya aina za mashairi anayoyatumia ni telezi mno.
Kwa mfano, anapoyaita mashairi mazito twaweza kuhoji uzito huo ni wa nini? Tunaweza pia kuhoji juu
ya mashairi ya furaha kama ni ya furaha kwa kila mtu? Hoja hiyo pia twaweza kuiibua kwenye
mashairi ya huzuni.
Nayo fasili ya Robert (1968), zaidi ya kusisitiza vipengele kama urari wa vina na uimbikaji, inaibua
pia dhana ya ushairi kuwa ni utungo wenye kuvuta moyo kwa namna ya ajabu. Dhana karibu sawa na
hii inaonekana pia katika Mulokozi na Kahigi (1979). Hata hivyo dhana ya ushairi kuvuta moyo kwa
namna ya ajabu (kuburudisha moyo kwa namna ya ajabu, kama inavyodaiwa na wanazuoni wengine) ni
dhana telezi mno na iliyopingwa na wanazuoni wengine. Kwa mfano, Macgoye (2009:2) akipingana na
mtazamo huo anasema kwamba, “Poetry is a human creation. It can be attractive to some people and
repulsive to others. It can be fashionable or unfashionable,” yaani ushairi ni ubunifu wa binadamu.
Unaweza kuwa wa kuvutia kwa watu fulani lakini kuwa wa kuchukiza kwa wengine. Unaweza kuwa
mzuri au mbaya (tafsiri yetu). Hivyo, dhana kwamba ushairi huvuta moyo si sahihi sana na haitusaidii
kuufasili ipasavyo ushairi na labda kuutofautisha na tanzu nyingine maana hata hizo huweza kuwa na
sifa hiyo.
Udhaifu mkubwa unaoonekana katika fasili za wanamapokeo ni kule kudai kwamba shairi bora,
zaidi ya mambo mengine, lazima liwe na urari wa vina na mizani. Jambo hili limesababisha kuibuka
kwa mashairi mengi ambayo japo yanazingatia urari wa vina na mizani bado hayatimizi jukumu la
msingi la fasihi, kuelimisha na kuburudisha. Mashairi mengi hayana maana kabisa. Hoja hii
ilishadokezwa zamani na Abedi katika dibaji ya Akilimali (1971) kwamba:
Watungaji wenye ujuzi mdogo hujipangia tu mashairi muradi vina vipatane, wakaacha
kueleza sababu za mashairi zikifahamika. Lakini mafundi wengi wa mashairi ya
Kiswahili waliopo leo ni watu wanaoeleza falsafa ya maisha na mambo ya hekima sana,
na mahitaji yao…
Hii ina maana kwamba kuna haja ya mashairi kusisitiza maudhui kuliko fani ili ushairi wa Kiswahili
uweze kutimiza jukumu lake la kuielimisha jamii. Hata hivyo ieleweke kuwa hatusemi hapa kwamba
washairi waipuuze fani maana fani na maudhui hutegemeana, hufungamana na kuathiriana.
Tuhitimishe mjadala huu kwa kusema kuwa kwa wanamapokeo ili utungo uitwe shairi hauna budi
kuwa na urari wa vina na mizani na pia uwe unaielimisha jamii kwa namna ambayo hadhira
wanafurahia. Utungo wowote mwingine ambao hauna sifa hizo, kwao wao si ushairi. Japo tumeeleza
udhaifu wa mtazamo huu ieleweke tangu mapema kwamba hii haimaanishi kuwa wanamapokeo
27
hawakuwa na mchango wowote katika kufasili ushairi wa Kiswahili. Walikuwa na mchango mkubwa
na wao ndiyo hasa walioanzisha kutafuta ukweli juu ya ushairi wa Kiswahili hasa ni upi? Aidha,
ieleweke kwamba wanamapokeo wamewaathiri watu wengi na hata leo hii ambapo kuna mtazamo wa
kisasa wa kufasili ushairi (kama tutakavyoona katika sehemu inayofuata) bado watu wengi
wanachukulia kwamba ushairi lazima uende sambamba na urari wa vina na mizani, matumizi ya lugha
isiyokuwa ya kawaida na kuvutia moyo (kama tulivyoona kwa Mulokozi na Kahigi hapo juu). Katika
uzoefu wetu wa ufundishaji wa somo la ushairi, kila tulipowapa wanafunzi nafasi ya kutunga mashairi,
walitunga mashairi yenye urari wa vina na mizani na yenye beti na hivyo kudhihirisha kwamba
wameathiriwa sana na mtazamo huu. Labda kwa kuwa mtazamo huu ndiyo unaoonekana kufundishwa
katika ngazi mbalimbali za elimu ya awali na hasa elimu ya msingi na sekondari kama ilivyodokezwa
hapo awali na Mwaruka (1968).
B. MKABALA WA KISASA/KIMAMBOLEO JUU YA DHANA YA USHAIRI
Mtazamo huu ni wa hivi karibuni, katika miaka ya 1960 na 1970. Wanausasa hutunga mashairi
yanayoitwa masivina, yaani mashairi yasiyokuwa na vina ndiyo maana katika baadhi ya maandiko
mtazamo huu huitwa mkabala wa kimasivina. Wanazuoni wanaoupigia chapuo mkabala huu ni pamoja
na Theobald Mvungi, Fikeni Senkoro, Euphrase Kezilahabi, David Massamba, Kulikoyela Kanalwanda
Kahigi, Mugyabuso Mulokozi na wengineo. Kama tulivyodokeza awali, hawa kwa namna mbalimbali
wameathiriwa na wanamapokeo katika fasili zao na hivyo kimsingi hawatoi fasili tofauti sana na
tulizozipitia awali isipokuwa hawasisitizi urari wa vina na mizani wala uimbikaji wa shairi kama sifa
kuu ya shairi katika lugha ya Kiswahili. Hebu tujivinjari baadhi tu ya fasili za ushairi zinazotolewa na
wanausasa:
Tukianza na Wamitila (2010b:104), tunaona jinsi athari za wanamapokeo zinavyojibainisha kwa
wanausasa. Wamitila, akiathiriwa kwa namna fulani na mkabala wa kimapokeo, anaufasili ushairi kuwa
ni sanaa inayotambulishwa na mpangilio maalum wa sentensi au vifungu; mpangilio ambao una
mdundo maalum au ruwaza fulani inayounda wizani, lugha ya mkato, mafumbo na mpangilio usio wa
kawaida wa vifungu fulani. Fasili hii ya Wamitila, japo ni ya hivi karibuni, lakini bado inashindwa
kutatua matatizo katika fasili ya ushairi yaliyoanzishwa tangu zama za kutamalaki wanamapokeo.
Ingawaje Wamitila amejitahidi sana kubainisha sifa za ushairi (kama vile lugha ya mkato, wizani,
ruwaza n.k.) bado anaibua mjadala katika baadhi ya dhana anazozitumia. Kwa mfano, anaposema
kwamba ushairi una mpangilio usiokuwa wa kawaida wa vifungu fulani, dhana hiyo inaweza ikapingwa
na wengine. Upinzani unaweza kutokana na ukweli kwamba si kila mara sifa hii na hata zile nyingine
alizotangulia kuzitaja zinajitokeza. Au tuseme sifa hizi hazijitokezi katika mashairi yote na hivyo
hatuwezi kuzichukulia kama kigezo cha kutathmini ikiwa utungo fulani ni ushairi ama siyo.
Nao Kanuri na wenzake (2009:32-33) wanafafanua kwamba ushairi hutumia lugha ya mkato,
taswira, ishara na mbinu nyinginezo kuwasilisha maudhui mazito kwa hadhira lengwa. Wakiwa
wanazungumzia zaidi ushairi simulizi, wanasisitiza kwamba ushairi sharti usheheni mafunzo au
mawazo mazito ili msikilizaji aguswe kihisia na kwamba malenga huwa ni mabingwa katika kutoa
maneno ya busara. Kwa hakika fasili hii haitofautiani hata kidogo na ile ya Robert (1968) tuliyoipitia
hapo awali au za wanamapokeo wengine. Tofauti pekee hapa ni kwamba akina Kanuri hawasisitizi
urari wa vina na mizani kama sifa kuu ya ushairi. Suala la malenga kuwa bingwa wa kutumia lugha na
kutoa maneno ya busara linajitokeza pia katika Kezilahabi (1976) ambapo, zaidi ya mambo mengine,
anasisitiza kwamba, ushairi huwa na upangaji mzuri wa maneno ya fasihi yenye mizani kwa kifupi ili
kuonyesha ukweli fulani wa maisha. Dhana ya “upangaji mzuri wa maneno” inamchukulia malenga,
yaani mshairi kuwa mtu mwenye ujuzi mkubwa wa lugha na hivyo hupanga lugha yake vizuri. Hata
hivyo uzuri huu unaoelezwa hapa haupo wazi, uzuri katika nini hasa? Kwamba hatumii lugha mbaya?
Lugha mbaya ni ipi? Au tuseme mpangilio mbaya wa lugha huwaje? Aidha, dhana ya “ukweli”
anayoiibua Kezilahabi pia ina utata mwingi. Ukweli ni nini na ukweli hasa ni upi? Wanafalsafa wengi
wanakiri kwamba kila uongo ni ukweli fulani wa maisha na kwamba ukweli wa mtu mmoja au kundi
moja la watu huweza kuwa uongo kwa mtu au kundi jingine la watu.
Fasili ya Mulokozi na Kahigi (1979:25) haiendi mbali sana na tulizikwisha zipitia. Wao wanasema
kwamba ushairi ni sanaa iliyopambanuliwa kwa mpangilio maalumu wa maneno fasaha yenye muwala,
kwa lugha ya mkato, picha, sitiari au ishara, katika usemi, maandishi au mahadhi ya wimbo ili kuleta
28
wazo au mawazo, kufunza au kueleza jambo au hisi fulani kuhusu maisha na mazingira ya binadamu
kwa njia inayoburudisha na kugusa moyo. Suala la ushairi kuwa na mguso lilishadokezwa zamani na
Mnyampala (1970) anapodai kwamba shairi laweza kumliza mtu akatokwa na machozi kwa ajili ya
mchomo wa hanjari la kuukata moyo na maini kwa ule mchomo na mguso wa maneno ya shairi la
mshairi bora. Mnyampala anaendelea kudai kwamba shairi la mshairi bora linaweza kumfanya mtu
afurahi na kujiona kuwa anayo heri mithili ya mtu aliyeko peponi. Hapa tunaona kwamba zaidi ya
kupingana juu ya ulazima wa shairi bora kuwa na vina na mizani, wanamapokeo (wanaowakilishwa
hapa na Mnyampala) na wanausasa (wanaowakilishwa hapa na Mulokozi na Kahigi) wanakubaliana juu
ya ulazima wa shairi “kuwa na mguso” kwa hadhira yake. Dhana yao ya shairi “kugusa moyo”
tulishaieleza kwa kina wakati twawahakiki wanamapokeo. Hivyo, kuendelea kujitokeza kwa suala hili
kwa wanausasa makini kama Mulokozi na Kahigi tunaweza kuhusianisha na athari za wanamapokeo
katika fasili “bora” za kisasa. Wanaposema kugusa moyo ni kufanyaje hasa? Na je jambo likimgusa
moyo mtu mmoja litamgusa moyo mtu mwingine? bila shaka jibu ni hapana. Ni wazi kwamba hata
uainishaji wa Mnyampala (1970) tulioupitia hapo awali unaonyesha kwamba upo uwezekano mkubwa
wa shairi “kutokuugusa moyo.” Hoja hii imebainishwa kinagaubaga na Macgoye (2009) kwamba yapo
mashairi ambayo hayaburudishi bali yanakasirisha na kukera moyo.
Tuseme tu kwamba mapungufu katika fasili za ushairi yanaonekana tangu katika fasili za
wanazuoni wa zamani sana hadi wa kisasa. Hivyo, tukubaliane tu na Macgoye (2009:2) kwamba
ushairi, sawa na falsafa au dini au nishati au kazi, ni vigumu sana kuufasili kwa kutoa fasili moja fupi.
Labda ni kutokana na ukweli unaobainishwa na Senkoro (1988:3) kwamba [kutokana na ugumu wa
kufasili ushairi] kuwapo kwa pande mbili zinazovutana na kukinzana si jambo geni. Ni dalili ya kukua
kwa fasihi ya jamii inayohusika, pamoja na kupanuka kwa nadharia ya fasihi hiyo (ufafanuzi wetu). Hii
ni kusema kwamba juhudi hizi za kufasili dhana tete ya ushairi ndiyo usomi wenyewe na siku tukikoma
kufanya hivyo ndiyo mwisho wa usomi.
Tuhitimishe kwamba, ili kufasili vizuri dhana ya ushairi ni vema tukichukua vipengele
vinavyojitokeza kwa wanamapokeo na wanamamboleo na kuviunganisha ili kuwa na fasili bora
ambayo labda inaweza kupunguza ukakasi uliopo japo hatusemi kwamba ukakasi huo utakwisha.
Tukichunguza fasili za wanamapokeo na wanamamboleo tunaona kwamba wanakubaliana kuwa ushairi
lazima utumie lugha ya mkato au lugha fupi, mpangilio maalumu, lugha fasaha, lugha ya picha na
ishara na vipengele vingine vya ushairi. Wanachotofautiana hasa ni katika suala la matumizi ya urari
wa mizani na vina. Wakati wanamapokeo wanashikilia kuwa vipengele hivi ni lazima na ndiyo uti wa
mgongo wa ushairi, kama inavyobainika katika Abedi (1954), wanausasa kwa upande wao wanaona
kwamba ushairi unaweza kutumia urari wa vina na mizani au unaweza usitumie na bado ukawa na sifa
ya kuwa ushairi kama inavyobainika katika Mulokozi na Kahigi (1979).
Hivyo, katika andiko hili ushairi tunauchukulia kuwa ni utungo wa kisanaa unaoweza kusimuliwa
au kuandikwa ili kuwasilisha ujumbe fulani kwa jamii kwa kutumia lugha ya picha, mkato, taswira,
ishara na lugha ambayo kimsingi si ya kinathari kama ilivyozoeleka katika tanzu nyinginezo. Ushairi
ulioandikwa kwa maksudi ya kuifurahisha hadhira huweza kuifurahisha hadhira husika na shairi
lililoandikwa kwa maksudi ya kuibua huzuni huweza kuihuzunisha hadhira. Fasili hii inazingatia
ukweli kwamba ushairi huweza kuwa simulizi na pia andishi na kwamba unaweza kutumia vipengele
hivyo au isivitumie vyote kwa pamoja. Aidha, fasili hii inaanza kwa kusisitiza maudhui na kisha fani na
si fani na kisha maudhui kama ilivyofanywa na wengi waliotutangulia. Hata hivyo, hatusemi hapa
kwamba fasili hii ni bora zaidi ya zote zilizotangulia, kila fasili ni bora katika muktadha wake. Hatuna
shaka kwamba kila fasili ni sahihi katika kipindi ambacho ilitolewa ila kwa kuwa ushairi unakua ni
wazi kwamba fasili kadhaa huweza kupitwa na wakati.
SIFA ZA JUMLA ZA USHAIRI
Baada ya kupitia fasili za wanamapokeo na wanamamboleo tunabaini kwamba ushairi una sifa
muhimu kadhaa. Miongoni mwa sifa hizo ni ruwaza katika lugha, uwekevu, ubebaji wa hisia,
huonyesha tajiriba ya maisha, hufikirisha, huweza kuwa na mvuto na huweza kutumia ukiushi wa kaida
za lugha. Sifa nyingine ni zile zinazotajwa na Mulokozi (1996:100-) kuwa ushairi huwa na uteuzi mzuri
wa maneno, huwa na mpangilio maalumu wa maneno, huweza kutumia lugha ya mkato, tamathali za
semi, ishara na mafumbo na mengineyo kadha wa kadha.
29
SURA YA PILI
DHIMA ZA USHAIRI WA KISWAHILI
Neno dhima linatumika hapa kumaanisha kazi, umuhimu au majukumu. Hivyo,
tunapozungumzia dhima za ushairi wa Kiswahili, tunamaanisha kazi, umuhimu au majukumu ya ushairi
wa Kiswahili. Ushairi wa Kiswahili una dhima za namna mbili kuu: dhima za ushairi wa Kiswahili
kwenye jamii/kijamii na dhima za ushairi wa Kiswahili kwenye fasihi/kifasihi. Dhima za ushairi wa
Kiswahili kijamii ni zile kazi mbalimbali za ushairi husika kwenye jamii ya Waswahili. Katika dhima
hii tunaangalia ushairi wa Kiswahili unafanya kazi gani kwa Waswahili? Kwa upande wa dhima za
ushairi wa Kiswahili kifasihi tunazungumzia kazi zinazofanywa na ushairi kwa Kiswahili kwenye
fasihi. Hapa tunaangalia ushairi wa Kiswahili unafanya kazi gani kwenye fasihi ya Kiswahili na labda
kwenye fasihi nyinginezo? Katika sura hii tutafafanua kwa kina dhima hizo na kutoa mifano pale
inapobidi.
I. DHIMA ZA USHAIRI WA KISWAHILI KIJAMII
Ushairi wa Kiswahili una majukumu mengi kwenye jamii ya Waswahili. Miongoni mwa dhima
hizo ni pamoja na kutunza historia ya jamii, kukuza ushujaa, ujasiri na uzalendo na kuendeleza
matabaka. Aidha, ushairi wa Kiswahili huadibisha, huadilisha na pia huhifadhi amali na utamaduni wa
jamii husika. Zaidi ya yote hayo, ushairi wa Kiswahili huburudisha. Kwa ujumla, tunaweza kusema
kwamba, ushairi wa Kiswahili unatimiza dhima kuu mbili za msingi za fasihi ambazo ni kuelimisha na
kuburudisha.
1. Ushairi wa Kiswahili na Uhifadhi wa Historia
Suala la fasihi na uhifadhi wa historia limewashughulisha wanafasihi wengi na kuibua mjadala
mkubwa miongoni mwao. Wapo wanaoona kwamba kazi ya fasihi ipo mbali sana na ukweli wa
kihistoria. Kwa maneno mengine, hawa wanaona kwamba jamii inayosawiriwa na kazi za kifasihi na
jamii halisi ni vitu viwili tofauti kabisa. Dai hili linamaanisha kwamba kazi ya fasihi haibebi historia
halisi ya jamii husika. Wanaounga mkono dai hili wanaongozwa na Lord Raglan na G. Innes kama
inavyoonekana katika Raglan (1956:105-106) na Innes (1974:26). Wengine katika mkondo huu ni
pamoja na Jan Vansina na J.W. Johnson ambao wanaona kwamba historia inayosawiriwa katika kazi za
kifasihi si halisi bali ni historia yenye ukweli pendelevu (history with subjective truth) inayokusudiwa
kutimiza malengo ya jamii husika (Vansina, 1965:102, 160 na Johnson, 1978:193).
Hata hivyo, inakubalika miongoni mwa wanahistoria kwamba ni vigumu kuwa na historia yenye
ukweli thabiti (objective history) kwani kila mwandishi wa historia huweza kuathiriwa na itikadi au
mtazamo fulani anaoupendelea. Kutokana na hilo, wanahistoria wanazigawa kazi zinazohusu historia
katika makundi mbalimbali kulingana na itikadi au mtazamo kazi husika inaouelemea/iliyo athirika
nao. Makundi hayo huitwa mikabala ya uelezaji wa historia ya jamii (historiographies). Kwa mfano,
kuhusu historia ya Afrika kuna makundi mengi ya mikabala ya uelezaji wa historia yaliyobainika.
Miongoni mwa makundi hayo ni mkabala wa Kizungu wa kuieleza historia ya Afrika (Eurocentric
historiography), mkabala wa Kiafrika wa uelezaji wa historia ya Afrika (Africanist/nationalist
historiography), mkabala wa Kimaksi wa uelezaji wa historia ya Afrika (Marxist historiography) na
kadhalika. Mkabala wa Kizungu wa kuieleza historia ya Afrika huitwa pia mkabala wa kikoloni wa
kuelezea historia ya Afrika (Colonialist historiography). Huu ni mkabala unaoielezea historia ya Afrika
kwa kuzingatia mawazo ya Kizungu au ya kikoloni. Wakoloni wa Kizungu walidai kuwa walikuja
Afrika kuzistaarabisha jamii mbalimbali za Kiafrika. Wanafafanua kwamba, Afrika kabla ya ujio wa
Wazungu/wakoloni, ilikuwa haijastaarabika. Hivyo, wanadai kuwa ukoloni ulikuja Afrika ili
kuistaraabisha Afrika. Kutokana na mtazamo huo, vitu vingi vilivyoandikwa na wanahistoria
wanaoelemea mtazamo huu wa Kizungu “viliubeba” na kuusifia ukoloni kuwa ni kitu kilichokuwa na
faida kwa Waafrika. Udhaifu wa mkabala huu ni kuwa unakuza sana nafasi ya Wazungu katika
maendeleo ya Afrika. Aidha, unadogosha na kudunisha sana jamii za Kiafrika tofauti na hali halisi
ilivyokuwa. Pia unaficha ukweli halisi wa sababu za ukoloni Afrika.
Kwa upande wa mkabala wa Kiafrika wa uelezaji wa historia ya Afrika (nationalist
historiography), huu unaelezwa kuibuka ili kuupinga mkabala wa Kizungu/kikoloni. Kinyume na
mkabala wa Kizungu, huu “unawabeba” na kuwasifia Waafrika. Mkabala huu unawaona Waafrika
30
kabla ya ujio wa wakoloni kuwa walikuwa wamestaaribika na kupiga hatua kubwa katika maendeleo.
Aidha, mkabala huu unaulaumu ukoloni kuwa ndiyo chanzo cha umaskini wa Afrika kwani kabla ya
hapo, kiwango cha maendeleo kilichofikiwa na Waafrika kilikuwa kinafanana na kile kilichofikiwa na
Wazungu. Udhaifu mkuu wa mkabala huu ni kuwa unawakuza mno Waafrika na kupinga mchango
wowote wa Wazungu katika maendeleo ya Afrika. Hivyo, mkabala huu, kama ulivyo uliotangulia,
hauelezi ukweli usiokuwa pendelevu.
Mkabala wa tatu ni ule wa Kimaksi wa uelezaji wa historia ya Afrika (Marxist historiography).
Mkabala huu wa uelezaji wa historia ya Afrika unaelemea mawazo ya mwanahistoria aitwaye Karl
Marx. Mawazo ya Karl Marx yameunda kile kinachoitwa mtazamo wa Kimaksi au Umaksi ambao,
mbali na kubainika katika historia, unabainika pia katika nyanja mbalimbali. Kwa kuwa mtazamo huu
unabainika pia katika mawazo ya Fredrick Engles na wengineo waliofuata baadaye, mtazamo wa
Kimaksi huhusu falsafa ya kisiasa na kiuchumi inayohusishwa na Karl Marx (1818-1883) na Fredrick
Engles (1820-1895), pamoja na wafuasi wao. Mkabala huu unachukulia kuwa historia ya jamii imejaa
migogoro na mivutano kati ya matabaka mbalimbali. Mfano mzuri wa migogoro hiyo ni migogoro
baina ya watawala na wataliwa, wafanyakazi na waajiri, na kadhalika. Hivyo, kwa mujibu wa mkabala
wa Kimaksi, historia ya binadamu huwa ni mapambano au harakati za kitabaka. Tabaka ambalo
hudhibiti njia kuu za uzalishaji mali huitawala na kuidhibiti jamii lakini tabaka la wasio nacho
hupambana kuleta mapinduzi. Kwa mujibu wa Wamitila (2003) katika kitabu chake cha Kamusi ya
Fasihi Istilahi na Nadharia, dhana ya Umaksi (pia Umarx) inafafanuliwa kama ifuatavyo:
Umarx ni falsafa ya kipembuzi ambayo inasisitiza jinsi mazingira ya kuishi
yanavyochukua nafasi ya kimsingi yakilinganishwa na mawazo au imani katika maisha
ya binadamu. Umarx unaelekea kuwa na sifa ya umoja (Monism) na inahusu kila kitu
kuanzia uchumi, siasa, historia, jamii na mapinduzi.
Hivyo, tuseme mkabala wa kimaksi katika historia, huelezea historia ya jamii za Kiafrika ukiongozwa
na imani kuwa uchumi (uzalishaji mali) huathiri maisha ya mwanadamu na mtazamo wake kwa ujumla.
Kwa hiyo, historia inayoelezwa na wanaoelemea mkabala huu ni ile ihusuyo njia za uzalishaji mali
pamoja na miundo ya kiuchumi inayoathiri uzalishaji mali na ugawanyaji wa faida (nani anapata nini).
Aidha, historia inayoelezwa inaakisi harakati zinazoendelea baina ya matabaka ya kiuchumi-jamii.
Mabadiliko ya kihistoria yanaelezwa katika msingi wa uzalishaji mali unavyoathiri mabadiliko ya
muundo wa matabaka ya jamii na hivyo kutokeza tabaka tawala na tawaliwa ambayo huwamo katika
mapambano na harakati za kugombea uchumi, siasa na faida za kijamii.
Kutokana na kuwapo kwa mikabala mbalimbali ya kueleza jambo moja tunabaini kuwa ni
vigumu kuwa na historia ambayo haina ukweli pendelevu. Hivyo, tunaweza kudai kwa uhakika kuwa
mawazo ya Raglan (1956:105-106), Innes (1974:26), Vansina (1965:102, 160) na Johnson (1978:193)
kuwa historia inayosawiriwa katika kazi za kifasihi si halisi bali ni historia yenye ukweli pendelevu
(history with subjective truth) inayokusudiwa kutimiza malengo ya jamii husika ni madai ya ukweli
lakini si madai yenye nguvu sana. Hii inatokana na ukweli kuwa historia yoyote ile ni vigumu kuwa na
ukweli usio pendelevu. Aidha, mara nyingi kila jambo, hata mambo ya kawaida yasiyohusiana na
historia, huelezwa kwa mtazamo, imani na falsafa ya mwelezaji. Kwa mfano, inapotokea ajali ya gari
na kukawa na watu watatu, dreva, askari na fundi magari ambao walishuhudia ajali hiyo, kila mmoja
ataielezea ajali hiyo kulingana na mtazamo, imani na falsafa yake. Ni wazi kuwa kila mmoja ataielezea
ajali hiyo kwa kuzingatia taaluma yake. Dreva, kwa mfano, ataeleza jambo linalohusiana na udreva
analohisi kuwa lilisababisha ajali hiyo, polisi ataielezea ajali hiyo kwa mkabala wa kisheria zaidi wakati
ambapo fundi magari atazingatia matatizo ya kiufundi anayoamini ndiyo chanzo cha ajali hiyo. Itakuwa
vigumu kupata maelezo yasiyo na ukweli pendelevu.
Mbali na wataalamu hawa wanaopinga uwezo wa fasihi kusawiri historia, wapo pia wanaoamini
kuwa kazi za kifasihi zinaweza kusawiri historia halisi ya jamii husika. Hawa ni pamoja na Mugyabuso
Mulokozi kama inavyoonekana katika Mulokozi (1986 na 2002) na Samwel (2012a) miongoni mwa
wengi wengineo. Hata hivyo, mawazo haya yalianzishwa na Mwanahistoria Merrick Posnansky
ambaye alieleza kwamba kazi za fasihi zinaweza kuwa chanzo muhimu cha historia ya jamii husika
(Posnansky, 1966 na 1969). Mulokozi (2002:96) anatumia tendi za nanga kushadidia mkondo huu wa
mawazo kwa kusema kwamba:
31
For us, however, the legendary does not negate the historical. On the contrary, in enanga
epic, the two supplement each other and combine with a third element – fiction or artistic
imagination, to create epic…Many enanga epics are historical in the sense that their
heroes are usually based on historical verified prototypes and their episodes revolve
around known historical events…
Kwetu sisi, hata hivyo, usakale haupingani na historia halisi. Katika tendi za nanga ni
kinyume chake, mambo hayo mawili hukamilishana na kuungana na jambo la tatu –
ubunilizi au uumbaji wa kisanii, ili kuunda utendi…tendi nyingi za nanga ni za kihistoria
kwa maana kwamba mashujaa wake kwa kawaida ni wa kihistoria na matukio
yanayowazunguka yalitokea kweli katika historia... (Tafsiri yetu).
Aidha, Mulokozi anatumia tendi za nanga kuonyesha jinsi wahusika wa tendi hizo kama vile
Ruyobya, Mutesa, Kitekere3 na wengineo na matendo yao yanavyoonyesha ukweli wa kihistoria
(2002:98 -102). Jedwali alilolitumia kulinganisha wahusika wa tendi za nanga na uhalisia wao
linathibitisha jinsi fasihi inavyoweza kubeba historia halisi ya jamii husika. Hivyo anahitimisha
kwamba:
A comparison of dramatic personae in Table 12 reveals that there is a complete
agreement between the epic and the historical record on the names and the roles of the
principal personage.
Ulinganisho wa wahusika wa kifasihi katika Jedwali namba 12 unabainisha kwamba
kuna mlingano mkubwa baina ya tendi na kumbukumbu za kihistoria katika majina na
majukumu ya wahusika wakuu (Tafsiri yetu).
Naye Samwel (2012a) anatumia majigambo kushadidia mawazo ya Mulokozi na wengineo
kuwa kazi ya fasihi inaweza kusawiri ukweli wa kihistoria. Samwel (khj.) anaungana na Mulokozi
(2002) kudai kwamba kazi za fasihi, majigambo yakiwamo, hubeba historia ya mtu mmoja mmoja na
jamii kwa ujumla. Samwel katika (2012a:131-152) anatoa mifano ya majigambo mbalimbali ya jamii
za Wahaya na Wasukuma yanavyosawiri ukweli wa historia ya wajigambi wenyewe na jamii zao.
Anabainisha kuwa majigambo hayo yanaeleza mambo mbalimbali ya kihistoria ikiwa ni pamoja na
ukoo wa wajigambi, matukio ya kihistoria yaliyotokea katika jamii kama vile vita, matatizo ya kisiasa,
kiuchumi na masuala mbalimbali ya kiutamaduni. Anatoa mfano wa jigambo linaloelezea kilimo
kinachozingatia viwango vya Nyerere. Samwel anadai kuwa jigambo hilo ni halisi na linataja wahusika
kama Nyerere ambao ni halisi. Anaendelea kufafanua kuwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere
alikuwa Rais wa Tanganyika na hatimaye Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye alihimiza sana
kilimo chenye tija na si kilimo mradi kilimo. Anahitimisha kuwa jigambo hilo pia linaakisi sera za
ujamaa za miaka ya sitini na sabini zilizohimiza kilimo na kupinga ubepari (mirija) ambayo ilipata
kuwapo katika historia ya jamii husika.
Hivyo, tuhitimishe mjadala huu kwa kueleza kuwa ushairi wa Kiswahili, kama zilivyo tanzu
nyingine za fasihi kama vile tendi na majigambo zinazoelezwa na Mulokozi (2002) na Samwel (2012a),
husawiri historia ya jamii husika. Tunaona, kwa mfano, kuna mashairi mengi yanayosawiri historia ya
jamii mbalimbali za Waswahili. Miongoni mwa mashairi hayo ni pamoja na Utenzi wa Uhuru wa
Tanganyika (1967) ulioandikwa na Mwinyihatibu Mohamed Amiri; Utenzi wa Jamhuri ya Tanganyika
(1967) ulioandikwa na Ramadhani Mwaruka; Utenzi wa Uhuru wa Kenya (1972) ulioandikwa na Salim
A. Kibao na Utenzi wa Jamhuri ya Zanzibar. Tenzi hizi zinasawiri matukio ya kihistoria yanayohusiana
na uhuru wa Tanganyika, Kenya na Zanzibar. Mashairi mengine ni Mashairi ya Azimio la Arusha
(1971) yaliyohaririwa na Grant Kamenju na Farouk Topan na Ngonjera za UKUTA za Mnyampala
1970 ambayo yanasawiri siasa ya Ujamaa na Kujitegemea pamoja na Azimio la Arusha, matukio
ambayo ni ya kihistoria nchini Tanzania. Vilevile kuna Utenzi wa Vita vya Kagera na Anguko la Idd
Amini Dada (1981) ulioandikwa na Henry Muhanika ambao unazungumzia vita baina ya Tanzania na
Uganda iliyotokea kati ya mwaka 1978 na 1979.
3 Ruyobya ni shujaa mpinzani ambaye alikuwa mwana mfalme wa Kiziba. Mutesa alikuwa Kabaka wa Buganda na
Kitekere alikuwa mfalme wa Kyamutwala. Wahusika hawa watatu wanasawiriwa katika Utendi wa Mugangala na pia ni
wahusika ambao waliishi kweli na walikuwa na sifa hizohizo zinazosawiriwa katika utendi husika.
32
2. Ushairi wa Kiswahili na Kukuza Ushujaa, Ujasiri na Uzalendo
Zaidi ya kutunza historia ya jamii husika, ushairi wa Kiswahili pia hukuza ushujaa, ujasiri na
uzalendo miongoni mwa wanajamii. Kwa mfano, mashairi yanayoelezea harakati za kudai uhuru na
jinsi watu walivyojitoa muhanga, kama tulivyoona hapo awali, yanaweza kuwafanya wanajamii kuwa
wazalendo na kuenzi jitihada zilizofanywa na wazee wao katika kuleta uhuru na ukombozi miongoni
mwa jamii za Waswahili. Mashairi na nyimbo pia hutumiwa katika vita, kama inavyobainika katika
nyimbo za wanajeshi (nyimbo za vita) (taz. Samwel, 2012a), na hivyo kukuza ushujaa, ujasiri na
uzalendo. Aidha, yapo pia mashairi yaliyotungwa ambayo yanahimiza ushujaa, ujasiri na uzalendo.
Mfano mzuri wa mashairi ya aina hii ni shairi liitwalo “Upole Wachusha” katika Diwani ya Akilimali.
Katika shairi hilo Akilimali anawaonya wanajamii kutokaa kimya pale wanapoonewa na
kukandamizwa. Anawahimiza wanajamii kuwa mashujaa na majasiri na kupinga vitendo hivyo.
Anasema:
Ulimwengu huu wa leo, wataka kuchangamka
Sikaliye ndio ndio, radae utaumbuka
Si kazi pigwa kibao, ukaselea wacheka
Upole na kimya sana, ulimwengu wachusha
Kimya sana kikizidi, kila jambo kuitikia
Si kazi fanywa kuadi, na vitanda kutandika
Lisilopasa kaidi, ndivyo dunia yataka
Upole na kimya sana, ulimwengu wachusha
3. Ushairi wa Kiswahili na Kuendeleza Matabaka
Uhusiano baina ya fasihi na utawala au matabaka ni jambo lililojadiliwa kwa kina na wataalamu
mbalimbali. Mulokozi (2002), kwa mfano, zaidi ya mambo mengine, anajadili uhusiano uliopo baina ya
tendi za nanga na utawala. Anaeleza kwamba ushairi wa kishujaa, ukiwamo nanga na majigambo,
ulitumika katika jamii za jadi ili kuendeleza tabaka tawala na maslahi yao. Mulokozi (2002:17)
anasema:
These relations of domination and dependence were highly maintained and reproduced
through a superstructure that included a powerful, highly centralized state and
bureaucracy, as well as an ideological apparatus that included royal oriented religious
cults, mythology, heroic poetry, such as enanga epics and praise poetry, and a value
system that upheld the ‘virtues’ of heroism and ‘high birth’, and stressed the superiority
and sanctity of the ruling personages.
Mahusiano haya ya kiutawala na kitegemezi kwa kiasi kikubwa yaliendelezwa na
muundo wa kijamii uliojumuisha matumizi ya nguvu, dola imara na serikali, pamoja na
mbinu za kiitikadi zilizojumuisha mfumo wa dini, imani, ushairi wa kishujaa, kama vile
tendi za nanga na majigambo, na mfumo wa desturi ulioendeleza masuala ya ushujaa na
‘nasaba bora’, na kuhimiza ukuu na utukufu wa tabaka tawala (Tafsiri yetu).
Mtazamo kama huu umebainishwa pia na Vail na White (1984) walipokuwa wanaushughulikia
ushairi wa kusifu (sifo) wa jamii za Wandebele na Hodza na Fortune (1979) walipokuwa
wanashughulikia ushairi kama huo wa jamii za Washona. Hivyo, tunaweza kusema kwa uhakika
kwamba ushairi wa Kiswahili, kama ulivyo ushairi wa jamii nyingine, ni fasihi inayokuza na
kuendeleza tabaka tawala. Aidha, mtazamo huu unabainika pia katika Samwel (2012a)
anapozungumzia ushairi wa majigambo katika jamii mbalimbali za Kitanzania. Samwel (khj.) anadai
kuwa ushairi wa majigambo, zaidi ya dhima nyingine, ulikuwa na dhima hii. Anatoa mfano kuwa,
katika mengi kati ya mashairi ya majigambo ya jadi mjigambi alijikabidhi kwa mtemi, mkuu wa ukoo
au mtu yeyote wa tabaka tawala ambaye majigambo husika yalitendwa mbele yake. Anaendelea
kufafanua kuwa ushairi wa majigambo ulitendwa ili kuonyesha utii kwa tabaka tawala na utayari wa
kulitumikia tabaka hilo. Anahitimisha kuwa wajigambi wa jadi waliona fahari kujinasibisha na tabaka
tawala. Samwel (khj.) anatoa mfano wa ushairi wa majigambo unaokuza na kuendeleza matabaka kwa
kubainisha kuwa wajigambi, katika majigambo ya jadi, wanaanza kwa kutoa heshima kwa mfalme.
Anafafanua kuwa kwa kuanza hivyo, wajigambi walikusudia kusema kwamba “ingawa nitajigamba na
kueleza matendo makuu niliyoyafanya, sistahili heshima bali heshima ni ya mfalme wangu.”
Anabainisha heshima inayotolewa katika moja ya majigambo ambapo mjigambi anasema:
33
Mheshimiwa mtukufu
Akusemaye vibaya hulalia juu ya mwamba
Hujifunika ungo
Nakufananisha na Abahindakazi.
Samwel anaendelea kulifafanua jigambo hilo kuwa hata katika mistari inayofuata mjigambi bado
anaendelea kueleza kwamba ingawa yeye ameelezea matendo makuu aliyoyafanya, hastahili heshima
bali heshima apewe mfalme. Mwisho kabisa mjigambi anamkabidhi mfalme vifaa alivyovitumia
kuwinda, yaani mikuki. Mfalme anaonekana ndiye anayestahili kuvimiliki. Samwel anaendelea
kufafanua kuwa katika majigambo ya aina hii mjigambi hukabidhi pia na mawindo yake kwa mfalme,
na mfalme ndiye aliyemgawia mjigambi kiasi anachostahili kadri mfalme alivyoona inafaa. Aidha,
katika majigambo ya vita, mjigambi hukabidhi silaha za vita na mateka halafu ndipo mfalme
angemzawadia mjigambi sehemu ya ngawira aliyoona inafaa.
Hivyo, kama inavyobainika katika fasihi za jamii nyinginezo na pia katika tanzu nyingine za
fasihi, ushairi wa Kiswahili pia unakuza na kuendelea matabaka. Mashairi na tenzi mbalimbali
tulizozifafanua awali kama vile Utenzi wa Uhuru wa Tanganyika (1967), Utenzi wa Jamhuri ya
Tanganyika (1967), Utenzi wa Uhuru wa Kenya (1972), Utenzi wa Jamhuri ya Zanzibar, Utenzi wa
Vita vya Kagera na Anguko la Idd Amini Dada (1981), Mashairi ya Azimio la Arusha (1971) na
Ngonjera za UKUTA (1970), zaidi ya mambo mengine, yanasifia tabaka tawala na sera zao. Kwa
kufanya hivyo, mashairi na tenzi hizo zinakuza na kuendelea tabaka tawala.
4. Ushairi wa Kiswahili na Kuhifadhi na Kuendeleza Utamaduni
Ushairi wa Kiswahili unahifadhi na kuendeleza utamaduni wa jamii husika. Fasihi ni kioo cha
jamii na hivyo ni sehemu ya utamaduni wa jamii husika. Kwa hiyo, ushairi wa Kiswahili, kama kazi ya
fasihi, hubeba utamaduni wa jamii husika. Ushairi wa Kiswahili unahusu masuala mbalimbali ya
kitamaduni yanaihusu jamii ya Waswahili. Masuala hayo ni kama vile mila na desturi za ndoa, jando,
unyago, na mahusiano ya wanajamii, lugha ya Kiswahili na kadhalika. Mfano mzuri wa hili tunauona
katika shairi la “Utamaduni Kitu Gani” na “Kiingereza Lugha Nzuri?” katika Ngonjera za Ukuta
ambapo mshairi anafafanua dhana ya utamaduni na dhima ya utamaduni wa Kiafrika. Aidha,
anafafanua pia dhima ya lugha ya Kiswahili na kuwaelimisha watu kuwa Kiingereza si lugha nzuri
kuliko Kiswahili kama inavyobainika katika shairi la “Kiingereza Lugha Nzuri?” kama ifuatavyo:
Lo! Hata haya huoni, lugha ngeni kuipenda?
Lugha yao wakoloni, walojiita Kamanda
Tukawekwa utumwani, tukafanywa sisi punda…
Lugha nzuri Kiswahili, tuchezeacho kandanda
Lugha yetu ya asili, ya kunena na kutenda
Ya asili na fasihi, ya taifa twaipenda…
Kiswahili na Kigogo, na lugha nyingi zatanda
Kinyamwezi na kidogo, Kibantu hakina nyonda…
Lugha nzuri Kizaramo, hupendeza kwa Mganda
Huvuta muungurumo, Dogori hupiga panda
Ni wa Kibantu msemo, wananchi waipenda
Lugha nzuri ya kupenda, ni hii ya Kiswahili
Akizungumzia kuuenzi na kuuthamini utamaduni wa Kiafrika, Mnyampala katika shairi la “Utamaduni
Kitu Gani” kama linavyobainika katika Ngonjera za Ukuta. Anasema:
…tamaduni kutukuza, ni mila za kila fani…
Na ufinyanzi wa vyungu, nazo ngoma zetu nchini
Na nyimbo zetu za tangu, na sauti zetu ngomani
Mbali mila za Kizungu, ziwe kwao Uzunguni…
Kazi zetu za asili, silizofanywa zamani
Za mikono na fasili, sidharau tukuzeni…
Za asili zetu kunga. Za unyago na jandoni…
Ndoa zetu za kimila, na shangwe zake nyumbani…
Uchongaji wa sanaa, mapambo yetu nchini
Hadithi zetu zajaa, kuitwa ni utamaduni…
34
5. Ushairi wa Kiswahili na Kuadilisha na Kuadibisha
Kuadilisha ni kumpa mtu maadili wakati ambapo kuadibisha ni kumtia mtu adabu. Ushairi wa
Kiswahili, zaidi ya dhima nyingine, una dhima ya kutoa maadili pamoja na kuadibisha jamii. Tukianza
na kuadibisha tunaona kwamba kupitia ushairi wa Kiswahili, wanajamii hufanywa kuwa na adabu kwa
wakubwa wao, miungu yao, viongozi wao na kadhalika. Katika ushairi wa majigambo, na hasa
majigambo ya ukoo na ya miji na vijiji, kwa mfano, tunaona kwamba wanajamii hufunzwa kuyahusisha
mafanikio yao na vizazi vya ukoo. Samwel (2012a) anabainisha kuwa katika ushairi huo wa majigambo
mjigambi hutaja vizazi vyake vya kuumeni na kukeni na kuyahusisha na mafanikio aliyoyapata.
Wajigambi huona kwamba mafanikio waliyonayo na sifa za kishujaa walizonazo zinatokana na nasaba,
miji na vijiji vyao. Kwa namna hii, wajigambi hujengewa adabu na heshima kwa nasaba, miji na vijiji
vyao. Hivyo, wanajamii huamini kama si ukoo wao pamoja na miji na vijiji walivyotokea, wasingepata
mafanikio waliyonayo yanayowapa haki ya kujigamba. Maelezo haya yanathibitisha sifa za shujaa wa
Kiafrika zilizopendekezwa na Mulokozi (1999 na 2002) kwamba ili mtu awe shujaa katika jamii, zaidi
ya mambo mengine, anapaswa kupata uungwaji mkono kutoka kwa wanajamii wa jamii husika.
Wanajamii hao hupaswa kumsaidia na kumjenga, kinyume chake shujaa huyo ataanguka. Aidha,
mashujaa katika tendi za nanga, kama anavyofafanua Mulokozi, walianguka kutokana na kukosa
uungwaji mkono kutoka kwa wanajamii wa jamii zao. Turejelee Mulokozi (2002: 85-93) anaposema:
This in effect means that the hero needs and must enjoy the support and protection of his
group, which alone knows the source of his occult power, if he is to survive as a fighter.
Group support at the level of kinship and beyond, is obsolutely essential; it is the third
and final heroic trait of the enanga hero.
Hii ilimaanisha kwamba shujaa anahitaji na lazima apate uungwaji mkono na ulinzi
kutoka kwa watu wake, ambao pekee ndio hujua asili ya nguvu zake za ajabu, kama
anahitaji kuendelea kuishi na kushinda. Uungwaji mkono katika ngazi ya wanaukoo na
jamii kwa ujumla ni muhimu sana; ni sifa ya tatu na ya mwisho ya shujaa wa tendi za
nanga (Tafsiri yetu).
Kutokana na hilo, wanajamii walijengewa heshima na adabu kwa wanaukoo, na hasa mababu, na
wanajamii wengine kwa ujumla.
Aidha, yapo pia mashairi mbalimbali yanayowaadilisha watu juu ya mambo mbalimbali. Vile
vile yapo mashairi mengi yanayowaasa watu kuwa na adabu. Mashairi hayo, kwa mfano, huweza
kuwahimiza wanajamii kuwaheshimu wakubwa wao, wake kuwaheshimu waume zao, kuadilishwa juu
ya masuala mbalimbali ya kijamii na kadhalika. Tunaona mfano wa hili katika Diwani ya Akilimali
ambapo kuna mashairi kama vile “Asofunzwa na Wazazi,” “Aringae na Dunia,” “Akiba si Mbaya,”
“Jirani Yako ni Ndugu,” “Kila Mpenda Rushwa,” “Unapokosa Shukuru” na mengine mengi ambayo
huadilisha na kuadibisha. Katika shairi la “Asofunzwa na Wazazi” mshairi anawaonya wanajamii
kuwatii wazazi wao kwani kama hawatawatii na kuwasilikiza basi dunia itawafunza. Aidha, katika
shairi la “Aringae na Dunia” mshairi anawaonya wanajamii kutodharau wengine; katika shairi la
“Akiba si Mbaya” mshairi anahimiza wanajamii kuweka akiba; katika shairi la “Jirani Yako ni Ndugu”
msanii anahimiza wanajamii kupendana na kujaliana na katika shairi la “Kila Mpenda Rushwa” msanii
anaiasa jamii kuichukia rushwa. Tuchunguze ubeti wa kwanza na wa pili wa shairi la “Unapokosa
Shukuru” katika Diwani ya Akilimali kuona jinsi ushairi wa Kiswahili unavyoadilisha jamii kuthamini
kazi na pia kushukuru kwa kile kidogo walichonacho:
Kazi iwayo si mabaya, mabwana tieni nguvu
Kazi yoyote ni niya, bali usiwe mvivu
Mapesa huwa hidaya, hayataki uwerevu
Unapokosa shukuru, kupata kuna Rabuka
Shukuru unachopata, japo ukipata mbovu
Mungu mwenyewe taleta, nzima pasipo nguvu,
Bure pesa hutapata, pasipo uelekevu
Unapokosa shukuru, kupata kuna Rabuka
Mashairi ya kuadilisha na kuadibisha yanaonekana pia katika Malenga wa Mrima cha
Mwinyihatibu Mohamed. Mashairi hayo ni pamoja na “Maovu,” “Ushoga,” “Mmbeya” na mengineyo.
35
Katika shairi la maovu mshairi anawaadilisha wajamii kutambua maovu yao na kuyatubia kabla
hayajawaletea madhara; shairi la “Ushoga” mshairi anaiadilisha jamii kuepukana na tabia ya urafiki wa
kinafiki na katika shairi la “Mmbeya” mshair anaiadilisha jamii kuepukana na tabia ya umbea.
Kwa upande wa Diwani ya Amri tunaona kuna mashairi mengi ambayo yanawaadilisha watu
kuwa wacha Mungu na kuwaadibisha watu kumtii Mungu na wakubwa wao. Mashairi ya kuadilisha na
kuadibisha katika diwani hiyo ni kama vile “Wamchao Rahmani Ndio Wenye Mwisho Mwema,”
“Kheri Nirudi kwa Mola,” “Baba Shika Ushikapo, Muamuzi ni Jalali,” “Mali,” “Maovu Sigeukie” na
“Ahadi ni Deni.” Mashairi ya “Wamchao Rahmani Ndio Wenye Mwisho Mwema” na “Kheri Nirudi
kwa Mola” yanawaadilisha wanajamii kuwa wacha Mungu. Aidha, mashairi hayo yanawaadibisha
wanajamii kumuheshimu Mungu. Pia yanawahimiza wanajamii kuacha maovu na kumrudia Mungu ili
waweze kuishi maisha mazuri duniani na akhera. Shairi la “Baba Shika Ushikapo, Muamuzi ni Jalali”
linawaadibisha wanajamii kuwaheshimu wazazi wao. Mbali na hilo shairi hilo pia linawaadilisha watu
(hasa wazazi) kuheshimu dini za wengine maana mwenye uwezo wa kuhukumu ni Mungu na si
mwanadamu. Vilevile shairi hilo linawaadilisha wazazi kuwapa watoto wao uhuru wa kufanya
maamuzi bila kuingiliwa. Shairi la “Mali” linaiadilisha jamii kufanya kazi kwa bidii ili kupata mali.
Hata hivyo, shairi hilo linawaonya wanajamii kutojali mali kuliko utu. Hivyo, shairi hilo linawataka
wanajamii kuridhika na mali waliyonayo hata kama ni kidogo na kuwataka wasijiingize kwenye
vitendo visivyofaa vya kutafuta mali. Nalo shairi la “Maovu Sigeukie” linawaadilisha wanajamii
kutendeana wema wao kwa wao na kuepukana na maovu. Kwa upande wa shairi la “Ahadi ni Deni”
mshairi anawaasa wanajamii kuheshimu ahadi walizoziweka na kuzitimiza. Turejelee shairi la “Mali”
ili kuona jinsi linavyoadilisha:
Kupenda mno ukwasi, naona nitapotea
Mali ina wasiwasi, sikai nikatulia
Mali huzua maasi, mtu yakampotoa
Mali ni njema hidaya, hili kweli nalijua
Sura yangu iwe mbaya, watu wataisifia
Lakini naona haya, sifa hii kupokea
Mali ni nzuri hidaya, tena ninakariria
Lakini ina hekaya, ngumu kuizingatia
Hususa huwa kayaya, dunia kuizamia
6. Ushairi wa Kiswahili na Kuburudisha
Zaidi ya dhima za kuelimisha, kama vile kuadilisha, kuadibisha, kutunza historia na kadhalika,
ushairi wa Kiswahili, kama kazi zingine za kifasihi, huburudisha. Ushairi wa Kiswahili, na hasa nyimbo
za kazi, huweza kuimbwa wakati wa kazi ngumu na kumburudisha mwimbaji na msikilizaji pia.
Ikumbukwe kuwa nyimbo za kazi ndiyo ushairi wa awali kabisa wa Kiswahili. Ushairi huu ulipunguza
uchovu wa watu hasa katika kazi kama vile kilimo, vita, ufugaji, uwindaji na kadhalika. Vilevile yapo
mashairi andishi ambayo yanaposomwa huweza kumburudisha msomaji. Hii ni kusema kuwa baada ya
kazi nzito za kutafuta kipato watu huweza kusoma mashairi na kuburudika na hata kuwasahaulisha
madhila yao.
II. DHIMA ZA USHAIRI WA KISWAHILI KATIKA FASIHI
Mbali na dhima za ushairi wa Kiswahili katika jamii, ushairi wa Kiswahili pia una dhima kubwa
katika fasihi, simulizi na andishi. Ushairi wa Kiswahili umetumiwa sana katika tanzu mbalimbali za
fasihi, andishi na simulizi kwa sababu mbalimbali. Kwa mfano, ushairi wa Kiswahili, na hasa nyimbo,
zimetumiwa sana kwenye riwaya, tamthilia, novela na hata hadithi fupi. Zaidi ya mambo mengine,
matumizi hayo yana dhima kama vile kutambulisha wahusika wa kazi za fasihi, kujenga tamathali za
semi, ishara, taswira, kuweka urari wa vina na mizani na kuonyesha ushiriki wa hadhira katika kazi ya
fasihi. Aidha, dhima nyingine za ushairi wa Kiswahili katika fasihi ni pamoja na kodokeza na kuibua
maudhui na kukuza tanzu za fasihi ya Kiswahili. Katika sehemu hii tutawasilisha maelezo na
uchambuzi wa dhima hizi za majigambo ya jadi katika fasihi.
36
1. Ushairi wa Kiswahili na Kutambulisha na Kuwajenga Wahusika
Kwa kuanza na kutambulisha na kuwajenga wahusika tunaona kwamba ushairi wa Kiswahili
husaidia kujua kazi husika ya fasihi inatumia wahusika wa aina gani na wenye uwezo gani. Dhima hii
huonekana hasa pale ushairi wa Kiswahili unapotumika katika utanzu mwingine. Mulokozi (2002:354)
akielezea hili anabainisha kwamba, ushairi wa majigambo unapotumika katika tendi za nanga,
hutambulisha sifa mbalimbali za shujaa anayesimuliwa, maisha yake, matendo yake, chakula chake,
mavazi yake na kadhalika. Kwa mfano, katika Utendi wa Rukiza tunaona kwa kutumia ushairi wa
majigambo, shujaa anaeleza chakula anachokula, anavyopaswa kuitwa na hata alivyo tayari kufa.
Tuchunguze mstari wa 480-83 anaeleza alivyo tayari kufa.
480. Ndetela n’amata nganywe
481. Nakushohola Ebinyambo bindasha bimbona
obwamba!
482. Ai “Ndetela amajuta nyesiige
483. Nakushohola Ebinyambo bindasha bimbona
obwelu!”
480. Niletee maziwa ninywe
481. Nikitoka Minyambo isinifume mshale na kuona
damu yangu
482. Niletee na mafuta nijipake
483. Nikitoka Minyambo isinifume mshale na kukuta
nimepauka
Chanzo: Mulokozi (2002:354)
Vilevile katika mstari wa 16-18 katika utenzi huohuo wa Rukiza, tunaona kwa kutumia ushairi
wa majigambo, sifa ya shujaa ya kutokula ovyo inabainishwa. Shujaa wa tendi za nanga kama
anavyoeleza Mulokozi (2002:87) hali chochote bali hula chakula maalumu. Sifa hii inasawiriwa katika
utendi kwa njia ya majigambo. Hebu tuangalie, kwa mfano, manju anaposema:
16. Kulya ebyo ntalya nkeita!
17. Kulya omugobe n’eshwiga
18. Ningila eby’abazana bakahomboza!
19. Ai “Mawe Kachenkela”
16. Waama ninahamanika
17. Heri nijiue kuliko kula haramu
18. Kula mboga za majani ya kunde na mnavu (shwiga)
19. Kula takataka zisanywazo na wajakazi!
Chanzo: Mulokozi (2002:322)
Pia Mulokozi (khj.) anabainisha kuwa kwa kutumia ushairi wa majigambo, sifa ya shujaa ya kutoitwa
isivyopaswa inabainishwa. Shujaa anapaswa kuitwa kwa jina la majigambo la Mwinyi/Mheshimiwa
kama inavyobainika katika mistari ya 455-63 hapa chini:
455. Yaija nailuka Kinyampororo
456. Yayema aha nyumanju yamweta
457. Ati “Iwe Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza,
Rukiza, iwe kyamawe!
458. Rukiza, Rukiza, Rukiza!
459. [Aho abiita byabanza]
460. Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza,
Rukiza, iwe kyamawe!
461. Ai “Katule kalame!
462. Alikunyeta Rukiza nohai?”
463. Ai “Manti inye nkalagwa nyetwa ‘Waitu’?”
464. Ai “Niinye Kinyampororo
455. Kinyampororo akaja anakimbia
456. Akamwita Rukiza kutokea nyuma ya nyumba
457. “Ewe Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza, mtoto
wa mama
458. Rukiza, Rukiza, Rukiza!
459. [Hapo vita vimeanza]
460. Ewe Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza, Rukiza,
Rukiza, mtoto wa mama
461. Rukiza akaitika, “Na uishi maishi marefu!
462. Ni nani wewe uniitaye ‘Rukiza’?
463. Hujui kuwa mimi huitwa ‘Mwinyi’ (waitu)?
464. Kinyampororo akajibu “Ni mimi Kinyampororo”
Chanzo: Mulokozi (2002:352)
Hivyo, ushairi wa majigambo uliotumika katika mistari hii umesaidia kumtambulisha mhusika kuwa ni
shujaa na pia kutambulisha sifa za shujaa husika.
2. Ushairi wa Kiswahili na Kuhamisha na Kujenga Mbinu za Kifani
Dhima nyingine ya ushairi ni kujenga mbinu mbalimbali za kifani. Hili linathibitisha na
Mulokozi (2002:10) anaposema kwamba tabia ya tendi kutumia au kuazima mbinu za kifani kutoka
katika ushairi wa majigambo huhamisha sitiari na udokezi ambazo hutumiwa sana katika majigambo
kwenda kwenye tendi.
37
The tendency of the epic to incorporate or borrow material from praise poetry transfers a
lot of the rich praise poetry metaphors and allusions into the epics.
Tabia ya tendi kutumia au kuazima matini kutoka katika majigambo huhamisha sitiari na
udokezi ambazo hutumiwa sana katika majigambo kwenda kwenye tendi (Tafsiri na
msisitizo wetu).
Hapa tunaona wazi kwamba pale ushairi wa majigambo unapotumika katika utanzu wa utendi, labda na
tanzu nyinginezo za fasihi simulizi, hujenga mbinu za kifani kwa kuhamisha mbinu zile zinazotumika
katika ushairi wa majigambo na kuzipeleka katika utanzu husika ambao hutumia ushairi huo wa
majigambo. Zaidi ya kuhamisha sitiari na udokezi, ushairi wa majigambo pia huhamisha chuku na
ucheshi, mbinu ambazo hutumika sana katika majigambo. Vivyo hivyo nyimbo, kama ushairi,
zinapotumiwa katika riwaya, tamthilia au utanzu mwingine wowote, huhamisha mbinu za kifani
zilizopo katika wimbo kwenda katika utanzu husika.
Vilevile matumizi ya ushairi katika tanzu nyingine yanasaidia kuibua ushiriki wa hadhira.
Ushiriki wa hadhira ndiyo msingi wa kazi yoyote ya kifasihi simulizi. Sifa hii ni mojawapo ya sifa
zinazoifanya fasihi simulizi kuwa hai. Akielezea jinsi ushairi wa majigambo unavyoweza kuifanya
hadhira ishiriki katika kazi ya fasihi, na hasa tendi, Mulokozi (2002:60) anasema:
Another form of participation occurs when a performance of a given poem is so inciting
that a member of the audience becomes ‘possessed’ by the poetic muse, leaps up, and
begins reciting his ekyebugo ‘self praise’. At that juncture, the bard, pleased by the effect
of his performance on his listerners would usually postpone his singing without breaking
off his instrumental music while the ekyebugo performance lasts.
Namna nyingine ya ushiriki wa hadhira hutokea pindi utendaji wa shairi husika
unapovutia mno kiasi kwamba mmoja wa wasikilizaji (hadhira) huweza “kupagawa” na
munkari wa kishairi, na kuanza kughani majigambo binafsi. Katika hali hii, manju, huku
akifurahia athari ya utendaji wake kwa wasikilizaji wake, kwa kawaida atasimamisha
uimbaji wake bila kusitisha mapigo ya kimuziki wakati utendaji wa majigambo (wa
hadhira iliyogeuka fanani) ukiendelea (Tafsiri yetu).
Hivyo, tunaweza kusema kwamba ushairi wa majigambo na ushairi wa Kiswahili kwa ujumla husaidia
sana katika kuibua ushiriki wa hadhira katika tanzu nyingine za fasihi na hivyo kuzihuisha tanzu hizo.
3. Ushairi wa Kiswahili na Kuibua Maudhui
Kazi ya fasihi hujengwa na maudhui na fani. Kama tulivyofafanua katika sehemu nyingine za
andiko hili, maudhui ni jumla ya mawazo yaliyomo katika kazi ya fasihi wakati fani ni mbinu
zitumikazo kuwasilisha maudhui hayo. Ushairi wa Kiswahili unapotumiwa katika tanzu nyingine za
fasihi huweza kusaidia kuibua au kukazia maudhui yabebwayo na kazi husika ya fasihi. Kwa mfano,
ushairi wa Kiswahili unapotumiwa katika utanzu wa ngano (hadithi), riwaya, tamthilia au hadithi fupi
huweza kusaidia kudokeza au kukazia maudhui yabebwayo na kazi husika ya fasihi. Akifafanua dhima
ya nyimbo, ambao ni kipera cha ushairi, katika hadithi fupi Samwel (2012b:44-46) anaeleza kuwa
waandishi wa hadithi fupi huweza pia kutumia nyimbo. Anafafanua zaidi kuwa matumizi ya nyimbo,
ambacho ni kipera cha ushairi simulizi, katika hadithi fupi, ambacho ni kipera cha fasihi andishi
yanaonyesha jinsi tanzu zinavyoingiliana, kukamilishana na kutegemeana. Samwel (khj.) anaendelea
kueleza kuwa waandishi wa hadithi fupi hutumia mdokezo wa wimbo ili kuibua maudhui
wanayoyakusudia. Anatoa mfano wa matumizi ya nyimbo katika hadithi ya Maeko katika Damu
Nyeusi na Hadithi Nyingine ambapo nyimbo kadhaa zinatumika. Wimbo wa kwanza unatumika kama
kitangulizi cha hadithi hiyo ya Maeko katika ukurasa wa 50. Wimbo huu unaimbwa na Hamduni au
Duni. Huu ni wimbo wa taarabu njia, kwa maana ya kwamba inaimbwa njiani unaoimbwa kama
ifuatavyo:
Wengi wanakuuliza, lililokuweka, oo ‘kuweka
Hutaki kuwaeleza, kuwa meridhika, oo ‘ridhika
Pendo lina miujiza, ya kuajibika, oo ‘ajibika
Ndipo likawashngaza, kwani kunitaka, oo ‘nitaka
38
Samwel (khj.) anaeleza kuwa Duni katika wimbo huo anaangazia ukweli kwamba Jamila ametosheka
na pendo analompa. Pia anabainisha kuwa mapenzi hayo yamewastaajabisha Wanasebleni. Wimbo huu
umerudiwa tena katika ukurasa wa 57 (Takriri ya wimbo).
Samwel anabainisha pia kuwa wimbo wa pili umetumika katika ukurasa wa 51 na mwimbaji ni
yuleyule Hamduni. Katika wimbo huu Duni anamshauri Jamila awaarifu Wanasebleni kwamba
wasimsumbue kimapenzi. Wimbo wa tatu unaobainishwa na Samwel upo katika ukurasa wa 51.
Mwimbaji ni Hamduni vilevile. Katika wimbo huo Duni anamwakilisha mkewe Jamila kuhusu ndoa.
Anakiri kwamba anadumu katika ndoa hiyo kwa sababu ya yale anayofanyiwa na Hamduni. Samwel
anahitimisha kuwa matumizi haya ya nyimbo yana umuhimu mkubwa kwani yanadokeza maudhui.
Aidha, Samwel (khj.) anabainisha kuwa nyimbo zimetumika pia katika hadithi ya Ndoa ya
Samani katika kitabu hichohicho. Samwel anaeleza kuwa hapa nyimbo za harusi zikitumika katika
hadithi fupi. Anatoa mfano wa nyimbo zinazotumika kuwa ni pamoja na wimbo wa bwana arusi
unapoonekana katika uk. 85 kama ifuatavyo:
Yu wapi ee, yu wapi bwana arusi aje hapa!
Tuhangaike naye!
Yu wapi ee, yu wapi bwana arusi aje hapa!
Tuhangaike naye!
Aje hapa!
Tuhangaike naye!
Eeh aje hapa!
Tuhangaike naye!
Anaendelea kufafanua kuwa wimbo huu, zaidi ya mambo mengine, unaonyesha suala la mila na
desturi kwamba arusi ni tukio la shangwe na nderemo ambalo huambatana na nyimbo. Wimbo huu
pia unabeba maudhui yahusuyo majukumu ya ndoa. Unaeleza kwamba maisha ya harusi ni yenye
changamoto nyingi na hujumuisha kuhangaika kwa wanandoa katika kutimiza mahitaji muhimu.
Hivyo, wimbo huu unamjuza bwana arusi ukweli wa mambo.Wimbo wa pili anaoubainisha
Samwel unaonekana katika ukurasa huohuo na una maneno yafutayo:
Hongera mwanangu eeh hongera a!
Name nihongeree hongera!
Mama uchungu mama uchungu
Nyamala mwanangu oyee
Nyamala mwanangu tumbo la uzere linauma mno oyee!
Oyee linauma mno eeh!...
Anabainisha kuwa wimbo huu na unabeba maudhui ya kumpa hongera binti anayeolewa lakini pia
unamweleza matumaini ya jamii juu yake kwamba ndoa huimarika kwa kuzaa watoto. Hata hivyo,
bi arusi anatahadharishwa kwamba kujifungua si kitu rahisi. “Tumbo la uzere” hapa linamaanisha
tumbo la uzazi. Mama ajifunguapo hupongezwa kwa kupata mtoto lakini kuna maumivu ya
uchungu ayapatayo kabla ya kupewa hongera hizo. Suala la uzazi katika ndoa na umuhimu wake
linabeba falsafa halisi ya Kiafrika kwamba ndoa ni watoto (Van Pelt, 1971). Hivyo nyimbo hizi
zinapotumika katika hadithi fupi, hazina budi kuchambuliwa na kuhusishwa na maudhui ya hadithi
yenyewe. Zaidi ya kutumika katika hadithi fupi ushairi wa Kiswahili (nyimbo) huweza kutumiwa
katika riwaya, tamthilia na novela kwa maksudi hayohayo.
4. Ushairi wa Kiswahili na Kukuza Tanzu za Fasihi
Mbali na dhima hiyo ushairi wa Kiswahili, ushairi huo pia huweza kukuza tanzu za fasihi.
Inaelezwa na wataalamu mbalimbali kuwa matumizi ya nyimbo, pamoja na matumizi ya vipengele
vingine vya fasihi simulizi katika fasihi andishi, yanakuza tanzu za fasihi andishi. Matumizi haya ya
vipengele vya fasihi simulizi ndani ya fasihi andishi ambayo hayakuwapo hapo awali katika fasihi
andishi ya Kiswahili, yameibua kile kinachoitwa katika fasihi ya Kiswahili, majaribio katika fasihi na
yameibua dhana ya fasihi ya majaribio (Senkoro, 2011). Hivyo, matumizi haya yameibua riwaya ya
majaribio, tamthilia ya majaribi na kadhalika. Hivyo, matumizi ya tanzu za fasihi simulizi, ikiwa ni
pamoja na ushairi simulizi (nyimbo), yamekuza fasihi andishi ya Kiswahili. Matumizi haya ya nyimbo
katika tanzu za fasihi andishi yanabainishwa pia na Mutembei (2012). Mutembei (khj.) anabainisha
39
kuwa nyimbo zimetumiwa katika tamthilia ya Hatia (Muhando, 1972) ambapo wimbo unaanza katika
onyesho la kwanza kama ifuatavyo:
Sikilizeni, sikilizeni
Hapa si kijijini…ooh
Hapa ni mji mkubwa
tunayaona
Mutembei (2012) anabainisha pia kuwa kuna matumizi ya wimbo kwenye tamthilia ya
Nitaolewa Nikipenda (Ngugi na Ngugi, 1982), Nguzo Mama (Muhando, 1982), Lina Ubani (Muhando,
1984), Mashetani (Hussein, 1971) na Morani (Mbogo, 1993). Mutembei (2012) anaeleza kuwa, zaidi
ya mambo mengine, matumizi haya ya nyimbo hukazia maudhui yabebwayo na tamthilia husika na
kubadilisha mtindo wa uandishi wa tamthilia. Wimbo uliopo katika tamthilia ya Nguzo Mama
unabainisha jinsi jitihada za wanawake kujikomboa zinavyokwamishwa na wanawake wenyewe na pia
wimbo katika tamthilia ya Morani unadokeza maudhui ya uhujumu uchumi. Aidha, matumizi haya ya
nyimbo yanajenga picha, taswira na sitiari katika kazi ya fasihi. Hili linabainika katika wimbo
unaoimbwa kwenye tamthilia ya Lina Ubani, “Ngoma hii siiwezi,” unaibua sitiari ya ngoma katika
tamthilia hii. Ngoma hapa inatumika kumaanisha msiba au majanga.
Tuhitimishe sura hii kwa kufafanua kwamba ushairi wa Kiswahili una dhima kubwa sana kwa
jamii ya Waswahili na pia kwa fasihi yao na ya jamii nyinginezo. Hata hivyo, tuonye hapa kuwa, mbali
na dhima kubwa iliyonayo ushairi wa Kiswahili kwa jamii na fasihi, ushairi wa Kiswahili kama zilivyo
tanzu nyingine za fasihi ya Kiswahili na fasihi ya jamii nyinginezo isipochukuliwa kwa tahadhari
huweza kuipotosha jamii. Samwel (2013) akielezea uwezekano wa fasihi kupotosha jamii anabainisha
kuwa ni ukweli usiopingika kwamba utanzu wowote wa fasihi unaweza kupotosha kama
usipochukuliwa kwa tahadhari au kuzingatia mipaka yake ya utendaji. Katika utanzu wa semi, kwa
mfano, tunabaini wazi kwamba methali zinaelimisha sana. Methali kama vile “aliye juu mngoje chini”;
“sikio halizidi kichwa”; “wa mbili havai moja”; “haraka haraka haina baraka” na nyinginezo nyingi
zinatoa maadili muhimu sana katika jamii.
Samwel (khj.) anaanza na methali “aliye juu mngoje chini” ambapo anabainisha kuwa methali
hiyo inahimiza wanajamii kuwa wavumilivu na kwamba pale wanaponyanyaswa na kuonewa hawana
budi kuwa na subira maana ipo siku wanaowanyanyasa “watashuka chini.” Hata hivyo zaidi ya
kuelimisha huko methali hii inaweza kupotosha. Methali hii, kwa upande mwingine, inawahimiza
wanajamii kutochukua hatua pindi mabaya yanapofanywa katika jamii kwa imani kwamba kuna siku
mambo yatakaa sawa yenyewe. Mwelekeo huu kwa hakika ni wa upotoshaji kwani kama wazee wetu
wangeichukulia methali hiyo kwa mkondo huo hakuna shaka hadi leo ukoloni bado ungekuwa
waendelea kwani wasingepambana nao.
Hali kama hiyo inaonekana katika methali “sikio halizidi kichwa.” Methali hii ni muhimu sana
katika kuadilisha. Inajaribu kutoa onyo kwa watoto kwamba kamwe hawawezi kuwa na hekima kuliko
wazee wao. Hivyo, inahimiza watoto kuwaheshimu wakubwa wao. Hata hivyo, kama methali hii
isipochukuliwa kwa tahadhari inaweza kupotosha jamii. Upotoshaji unaweza kutokana na ufafanuzi
kwamba methali hii inadidimiza juhudi katika maendeleo. Methali hiyo inaweza kuchukuliwa kwamba
inawaonya watoto kutotia bidii katika kazi kwani kama wazazi wao ni maskini wao kamwe hawawezi
kuwa matajiri kuliko wazazi wao. Mtazamo kama huo unabebwa na methali “wa mbili havai moja.”
Kwa upande wa “haraka haraka haina Baraka,” Samwel anaeleza kwamba inafanana na methali
nyingine kama vile “polepole ndiyo mwendo,” “subira yavuta heri” na kadhalika. Methali hizi
zinaionya jamii kutofanya mambo kwa pupa. Kabla ya kufanya jambo lolote lile ni muhimu kutafakari
na kupanga mikakati ya kulifanya jambo husika. Hata hivyo, zaidi ya kuelimisha hii methali hii
inaweza kupotosha na hasa pale inapotumika katika mazingira yasiyofaa. Kwa mfano, kama mtu ana
mgonjwa na akatumia methali hii bila shaka mgonjwa huyo atakufa kwani mgonjwa anahitaji huduma
ya haraka. Vivyo hivyo kama mtu amevamiwa na majambazi au anakabiliwa na hatari na akazitumia
methali hizi hatuna shaka kwamba atapatwa na madhara makubwa kwani katika nyakati za hatari
maamuzi ya haraka huhitajika. Mbali na upotoshaji wote huu bado methali zitabaki kuwa tungo
fupifupi za hekima na za kimapokeo zinazotumika kurithisha falsafa ya jamii kutoka kizazi kimoja hadi
kingine (Mulokozi, 1996; Cuddon, 1998; Senkoro, 2011).
Samwel anaendelea kubainisha kuwa uwezekano wa utanzu fulani kupotosha jamii hauishii tu
katika semi, na hasa methali bali unaonekana pia katika tanzu nyinginezo, ushairi ukiwemo. Hivyo,
40
tuhitimishe kuwa utanzu wowote wa fasihi unatimiza majukumu makuu mawili ya kifasihi ambayo ni
kuelimisha na kuburudisha (Mulokozi, 1996). Katika kuelimisha ndipo tunaona kuna mambo kama
kuadilisha, kuadibisha, kuonya, kukosoa, kuhifadhi amali za jamii, kuendeleza historia na kadhalika.
Mbali na dhima hizo kuu mbili za fasihi, isipochukuliwa kwa tahadhari, fasihi huweza kuipotosha
jamii. Hivyo ni jukumu la wanajamii kuichukulia kazi yoyote ile ya fasihi kwa uangalifu mkubwa ili
iweze kuwafaidisha. Aidha, ni jukumu la washairi wa Kiswahili kuhakikisha kadri inavyowezekana
wanatoa kazi bora za kifasihi ambazo zitatimiza majukumu ya kuelimisha na kuburudisha na
kupunguza uwezekano wa kupotosha jamii.
41
SURA YA TATU
CHIMBUKO LA USHAIRI WA KISWAHILI
Chimbuko, kama tunavyolitumia katika andiko hili, tunamaanisha asili au chanzo cha jambo fulani.
Hivyo, kusema chimbuko la ushairi wa Kiswahili tunamaanisha asili au chanzo cha ushairi wa
Kiswahili. Katika sura hii maneno asili na chanzo yatatumika pia kumaanisha chimbuko.
Chimbuko la ushairi wa Kiswahili, kama ilivyo vipengele vingine tulivyoviangalia hapo awali, ni
suala telezi mno. Utelezi wa suala hilo unatokana na ukweli kwamba kuna nadharia mbalimbali
zinazoelezea chimbuko hilo. Nadharia kuu mbili kati ya hizo, zimeshika mizizi zaidi, kwanza ile
nadharia inayodai kwamba asili ya ushairi wa Kiswahili ni Uislamu na fasihi za Kiarabu na pili, ile
nadharia inayodai kwamba chimbuko la ushairi wa Kiswahili ni ushairi simulizi wa jamii mbalimbali za
Wabantu. Katika sehemu hii tutachambua nadharia hizi kwa kina na kuona ni ipi inayoweza
kutushawishi kama wanataaluma kukubali chimbuko la ushairi wa Kiswahili.
1. CHIMBUKO LA USHAIRI WA KISWAHILI NI UISLAMU/KIARABU
Dai hili ndilo la awali kabisa na linajibainisha vema katika andiko la Lyndon Harries (1962) liitwalo
Swahili Poetry. Harries anaeleza kuwa, chimbuko au asili ya ushairi wa Kiswahili ni “Uislamu na fasihi
ya Kiarabu.” Anaamini kuwa ushairi wa Kiswahili ulianza karne ya 17 na umetokana na Uislamu na
unafanywa sana na Waislamu. Anaendelea kudai kwamba ushairi wa Kiswahili ulianza pwani ya
kaskazini ya Kenya na hasa Lamu. Wafuasi wa mtazamo huu wa Harries wanauhusisha ushairi wa
Kiswahili na Uislamu na fasihi ya Kiarabu kutokana na mambo kama vile: ushairi wa Kiswahili kuanza
kipindi cha Waarabu, ushairi wa Kiswahili kutumia maneno ya Kiarabu, ushairi wa Kiswahili kubeba
maudhui ya Kiarabu, ushairi wa Kiswahili kuandikwa kwa hati za Kiarabu, ushairi wa Kiswahili
kutungwa sana na Waislamu, ushairi wa Kiswahili kuamini Uislamu na pia ushairi wa Kiswahili
kutumia kanuni za ushairi wa Kiarabu. Tuchunguze kwa makini hoja moja baada ya nyingine kati ya
hizi.
III. Ushairi wa Kiswahili kuanza kipindi cha Waarabu
Hoja ya kwanza inayotumiwa na wafuasi wa nadharia inayodai kwamba ushairi wa Kiswahili
chimbuko lake ni Uislamu ni kwamba ushairi huo ulianza katika kipindi ambacho Waarabu
walitamalaki katika upwa wa Afrika Mashariki. Kipindi kinachodaiwa kuwa ushairi wa Kiswahili
ulianza (karne ya 10-17) ni kipindi ambacho Waarabu walikuwa wameshakuja katika upwa wa Afrika
Mashariki na kufanya biashara na wenyeji. Katika karne ya 17 ndipo Waarabu walipoiteka ngome ya
Yesu kule Mombasa na kuhitimisha utawala wa Wareno waliokuja kuimiliki biashara kati ya Waarabu
na Waswahili (Coupland, 1938). Hivyo, kipindi hicho kiliiamsha upya biashara baina ya Waswahili na
Waarabu na hivyo tunaweza kukiita kuwa ni kipindi cha Waarabu kutamalaki. Kutokana na Waarabu
kutamalaki na kuwa na maendeleo ya kiuchumi, yaliyotokana na biashara mbalimbali walizozifanya,
mamwinyi wao walihitaji kitu cha kuwaliwaza. Hapo ndipo walipoingiza fasihi zao ili kujiliwaza na
ndiyo ukawa mwanzo wa ushairi wa Kiswahili. Uwezekano wa maendeleo ya kiuchumi kuibua kazi ya
fasihi umeelezwa pia na Mulokozi (1996:147) anapozungumzia maendeleo ya riwaya ya Kiswahili.
Anasema:
Kufikia karne ya 16, fani zilizotajwa hapo juu (visakale, visasili, sira n.k.) zilikuwa
zimekwisha enea na kufahamika katika mataifa mengi; kulihitajika tu msukumo wa
kijamii, kiteknolojia, na kiuchumi ili ziweze kuvyaza riwaya…Jambo la kwanza ni ukuaji
mkubwa wa shughuli za kiuchumi huko Ulaya. Ukuaji huo ulifungamana na biashara ya
baharini ya mashariki ya mbali, ‘kuvumbuliwa’ kwa mabara mawili ya Amerika, na
kukua kwa nyenzo za uzalishaji wa viwandani huko Uingereza, hasa viwanda vya nguo.
Malimbikizo ya ziada yaliyotokana na shughuli hizo yalipanda mbegu ya mapinduzi ya
viwanda yaliyotokea karne mbili baadaye. Aidha, mabadiliko haya yalizua tabaka jipya la
mabwenyenye waliohodhi viwanda na nyenzo nyingine za uchumi. Tabaka hilo lilihitaji
fani mpya za fasihi, lilikuwa na wakati wa ziada wa kujisomea, na uwezo wa kifedha wa
kujinunulia vitabu na magazeti.
Japo Mulokozi hakuwa akizungumzia kuhusu kuibuka kwa ushairi wa Kiswahili katika kipindi cha
Waarabu na kwamba yeye si mmoja wa wafuasi wa dai hilo lakini maelezo yake yanatusaidia kueleza
42
kwa nini ushairi wa Kiswahili unadaiwa kuibuka katika kipindi cha kutamalaki kwa Waarabu. Ni kwa
kuwa Waarabu walishajilimbikizia mali na walikuwa na muda wa kusoma na fedha za kujipatia kazi za
kishairi, hivyo kuibuka kwa ushairi wa Kiswahili.
Hata hivyo mtazamo huu kwamba ushairi wa Kiswahili uliibuka wakati wa Waarabu una kasoro.
Kasoro hiyo inatokana na ukweli kwamba ushairi simulizi umekuwapo miongoni mwa wakazi wa upwa
wa Afrika Mashariki na Bara kwa muda mrefu sana, hata kabla ya ujio wa Waarabu. Tukubali tu
kwamba huenda ni kweli kwamba ushairi andishi wa Kiswahili uliibuka baada ya Waarabu kuja,
kuhubiri dini ya Kiislamu na kuwafunza Waswahili hati za maandishi. Baada ya kujifunza hati hizo
ndipo walipoutia ushairi simulizi, uliokuwapo tangu enzi, katika maandishi na kuibua kile
kinachojulikana leo kama ushairi wa Kiswahili. Hivyo dai kwamba ushairi wa Kiswahili unatokana na
Uislamu na fasihi ya Kiarabu, linakosa mashiko.
IV. Ushairi wa Kiswahili uliibuliwa na wafuasi wa Waarabu
Hoja ya pili inayotumika kushadidia kwamba asili ya ushairi wa Kiswahili ni Uislamu na fasihi ya
Kiarabu ni kwamba ushairi huo uliibuliwa na kuenezwa na wafuasi wa Waarabu. Kwa kusema kwamba
ushairi wa Kiswahili uliibuliwa na wafuasi wa Waarabu ina maana kwamba washairi wengi wa
mwanzo wa ushairi wa Kiswahili walikuwa na mahusiano ya karibu na Waarabu. Mahusiano hayo
yanaweza kutokana na unasaba au mambo mengine ya kijamii kama vile dini na ndoa. Inadaiwa
kwamba washairi wengi wa mwanzo wa ushairi wa Kiswahili kama si kuwa na damu ya Kiarabu,
kuzaliwa kutokana na ndoa ya Mwarabu na Mswahili, walikuwa wafuasi wa dini ya Kiislamu au
walikuwa wamehusiana na Waarabu kindoa katika nasaba zao. Uhusiano huo unabainika kwa washairi
hao kuwa Waislamu au kuwa na majina ya Kiarabu. Tunaona, kwa mfano, washairi kama vile Shaaban
Robert, Amri Abedi, Sayyid Abdallah bin Ali, Mohamadi Kijumwa na wengineo wengi ni Waislamu,
wafuasi wa Waarabu kwa dini yao. Kutokana na hilo wafuasi wa nadharia ya Harries wanadai kuwa
hakuna shaka kwamba huenda Waarabu na Uislamu vilikuwa na nafasi katika ushairi wao.
Hata hivyo zaidi ya ukweli ambao unaweza kubebwa na hoja hii ni dhahiri kwamba hoja hii, kama
ile iliyotangulia, ni dhaifu pia. Udhaifu huo unatokana na ukweli tulioudokeza hapo awali kwamba
Waarabu waliwafunza wenyeji hati za maandishi ambazo hatimaye walizitumia kuuweka ushairi
simulizi, uliokuwapo tangu zama, katika maandishi na kuibua kile kilichokuja kuitwa ushairi wa
Kiswahili. Vilevile, zaidi ya kujifunza hati za Kiarabu, washairi hawa walijifunza ushairi wa Kiarabu
kupitia kaswida walizofunzwa katika Uislamu. Kaswida hizi, kwa kuwa nyingi zilikuwa katika
maandishi, ziliwaonyesha haja ya wao pia kuweka ushairi wao katika maandishi. Kutokana na hilo sasa
ushairi wa Kiswahili ukaibuka. Aidha, ifahamike pia kwamba wapo washairi wengine Wakristo
waliokuwapo karibu kipindi sawa na kuwapo kwa washairi wa Kiislamu. Miongoni mwa washairi hao
ni pamoja na Mathias Mnyampala.
V. Ushairi wa mwanzo wa Kiswahili ulihusiana na Dini ya Kiislamu na Uarabu
Jambo lingine linalotumika kushadidia kwamba ushairi wa Kiswahili unachimbuka katika Uislamu
na fasihi ya Kiarabu ni kwamba ushairi wa mwanzo wa Kiswahili ulihusiana sana na dini ya Kiislamu
na Uarabu. Hii ni kusema kwamba mashairi mengi ya mwanzo yalizungumzia Uislamu na Uarabu na
katu hayakuhusiana sana na masuala ya Waswahili. Ushairi mwingi ulioandikwa katika kipindi hiki
ulizungumzia mambo yanayohusiana na dini ya Kiislamu. Kwa mfano, utenzi wa Hamziyya ambao
unahusu maisha ya Mtume Muhamadi, ambaye ndiye mwanzilishi wa Uislamu; utenzi wa Tabuka
ambao unazungumzia juu ya vita kati ya Waislamu wa mwanzo na Mfalme Herekali wa dola ya
Warumi (Mulokozi, 1996:114). Ushairi mwingine wa Kiswahili uliobeba masuala yanayohusiana na
Uislamu na Uarabu ni Utenzi wa Al-Inkishafi na Utenzi wa Mwanakupona. Mulokozi (1999:71)
anabainisha kwa msisitizo kwamba:
Msingi wa maudhui ya Inkishafi ni Kurani Tukufu; mwandishi anachukua mafundisho ya
Kurani kuhusu maisha na mwenendo bora wa muumini, na kuyafafanua kwa vielezo
vinavyotokana na historia na mazingira ya Pate na Afrika Mashariki kwa
ujumla…Dhamira kuu ya Inkishafi ni kufafanua maana ya maisha: Je, maisha ni nini na
yana lengo gani? Maana anayoitoa ni ile ya kidini- ya Kiislamu.
43
Hapa tunabaini wazi kwamba utenzi huu umebeba maudhui mengi yanayohusiana na dini ya Kiislamu.
Tunaona hata maonyo yanayotolewa katika utenzi huu, falsafa ya maisha baada ya kufa inayoelezwa
humo na mengineyo yanaendana na mtazamo wa dini ya Kiislamu. Hali hiyohiyo inaonekana katika
Utenzi wa Mwanakupona ambapo maadili anayopewa binti wa kike ni maadili yanayotokana na Kurani
Tukufu. Ieleweke hapa, hata hivyo, kwamba hatuna kusudi la kudai kwamba tenzi husika ni za kidini
na hazina maana nje ya mpaka ya kidini. Kwa hakika tenzi husika zina maana pia nje ya muktadha wa
kidini kwani mambo mengine yanayoelezwa humo yanafaa katika maisha kwa ujumla wake.
Kama ilivyo kwa hoja zilizotangulia, hoja kuwa ushairi wa Kiswahili unatokana na Uislamu na
fasihi ya Kiarabu kutokana na uhusiano wake na Uislamu na Uarabu haina mashiko ya kitaaluma.
Ukosefu huo wa mashiko unatokana na hoja kwamba, kwa kuwa washairi wengi wa mwanzo (kama
ilivyobainishwa hapo awali) walikuwa Waislamu, hatuna shaka kwamba ingeshangaza sana ikiwa
washairi hao wasingetunga mashairi yanayohusiana na Uislamu. Fasihi ni zao la jamii na hubeba yale
yaliyomo katika jamii na uzoefu wa maisha ya msanii husika (Samwel, 2012a). Hivyo fasihi haiwezi
kujitenga na msanii na jamii yake. Aidha, ni jambo linalopaswa kukumbukwa kwamba wakati huu
ulikuwa ni wakati wa kutamalaki kwa dini ya Kiislamu na Uarabu, hivyo fasihi ilisawiri hali halisi.
Hali hiyo inaonekana pia katika vipindi vingine vya kihistoria miongoni mwa Waswahili ambapo
ushairi, na tanzu nyinginezo, zilisawiri matukio ya kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiutamaduni yaliyopo
katika jamii husika. Mulokozi (1996) anaonyesha jinsi ushairi na tanzu nyinginezo za fasihi ya
Kiswahili zilivyosawiri mambo kama ukoloni na harakati za kuuondoa, uhuru, azimio la Arusha, vita
vya Idd Amini na kadhalika.
VI. Ushairi wa Kiswahili ulishamiri sana katika maeneo yaliyokaliwa na Waarabu
Hoja nyingine ya msingi ni kwamba ushairi wa Kiswahili asili yake ni Uislamu na fasihi ya Kiarabu
kwa sababu ushairi huo ulishamiri sana maeneo yaliyokaliwa na Waarabu kama vile Kigoma, Tanga,
Tabora, Lamu, Pate na maeneo mengine. Maeneo haya ndiyo yanayotajwa kuwa njia kuu za biashara ya
Waarabu (Coupland, 1938). Aidha, maeneo haya pia ndiyo ambayo yalishuhudia ustawi mkubwa wa
ustaarabu wa Kiarabu pamoja na dini ya Kiislamu. Mifano ya washairi waliotoka katika maeneo tajwa
inabainishwa hapa chini:
·Kigoma: katika mkoa huu ndipo walipotoka washairi kama vile Amri Abedi, Issa Kitenge na
wengineo
·Tanga: mkoa wa Tanga ulitoa washairi kama vile Shaaban Robert, Hemed bin Abdallah el-
Buhry au maarufu kama Mzee Kibao, Ghulam Mabondo bin Mwinyimatano, Swalehe
Kibwana, Mwinyihatibu Mohamed Amiri n.k.
·Bagamoyo: huku alitoka Mahmoud M. Hamdouny bin Khalfan na wengineo
· Tabora: alikotoka Mwamshamu Yange na wengineo
· Lamu: alikotoka Muhamadi Abubakar Kijumwa, Ahmed Sheikh Nabhany, Zahid bin Mngumi
n.k.
· Pate: alikotoka Sayyid Abdallah bin Ali bin Nasiri, Mwanakupona Binti Mshamu Nabhany,
Fumo Liyongo, Ali Athmani Koti, Mohammad bin Sheikh Mataka n.k..
· Mombasa: huko alitoka Ahmad Nassir bin J. Bhalo n.k.
Historia hii ya washairi na mahali wanapotoka inaelezwa kwa kina katika Mulokozi na Sengo
(1995:28-60). Hivyo, kwa ufafanuzi wa kina kuhusiana na maeneo walikotoka washairi wa mwanzo wa
ushairi wa Kiswahili tazama andiko hilo muhimu.
Kwa ujumla, tuseme kwamba wakati ambapo hatupingi kushamiri kwa ushairi wa Kiswahili katika
maeneo yaliyokaliwa na Waarabu, tunaona kwamba kuchukua hiyo kama hoja ya kuitumainia katika
madai mazito kama haya ni udhaifu mkubwa. Tulishadokeza hapo awali juu ya nafasi ya Waarabu
katika kuibuka kwa ushairi wa Kiswahili, japo tumekanusha kwamba wao si waanzilishi bali wao ni
watia shime tu wa kuibuka kwa ushairi huu. Hoja hiyo pia inafanya kazi hapa.
VII. Ushairi wa Kiswahili kutumia maneno na hati za Kiarabu
Zaidi ya hoja hizo hoja nyingine ni kwamba ushairi wa Kiswahili unatokana na Uislamu na fasihi ya
Kiarabu kwa sababu ushairi wa mwanzo wa Kiswahili (na kwa sehemu hata ushairi wa sasa) unatumia
maneno mengi ya Kiarabu. Mulokozi na Sengo (1995:87), japo wao hawaungi mkono dai kuwa ushairi
44
wa Kiswahili unatokana na Kiarabu, wanabainisha kwamba hata dhana nyingi zinazotumika katika
ushairi wa Kiswahili kama vile shairi, mizani, ubeti, tathlitha, tarbia, takhmisa n.k. zinatokana na lugha
ya Kiarabu. Suala la maneno ya Kiarabu liliibuka pia wakati wa mjadala kuhusiana na chimbuko la
Kiswahili ambapo baadhi ya wanataaluma wakadai kwamba ushairi ni lugha inayotokana na Kiarabu
(Taz. Kitabu cha Historia ya Kiswahili cha Massamba, 2002 kuhusu watu waliotoa madai haya). Hata
hivyo, Massamba (2002) katika kitabu hicho ambacho kwa hakika kimechimba kwa kina anapingana na
madai kwamba Kiswahili ni Kiarabu japo hakanushi juu ya Kiswahili kuwa na maneno mengi ya
Kiarabu. Anasema:
Lakini hata kama ni kweli kwamba katika lugha ya Kiswahili asilimia kubwa ya maneno ya
mkopo ni yale yatokanayo na lugha ya Kiarabu hiyo peke yake haiwezi kuwa sababu ya kutufanya
tutoe kauli kwamba Kiswahili ni Kiarabu. Tunaweza tu kufikia hitimisho kama hilo iwapo
tutathibitisha, kwa kutumia vigezo kuntu, kwamba mfumo mzima wa kiisimu wa lugha hii ya
Kiswahili unashabihiana kabisa au zaidi na mfumo wa Kiisimu wa lugha ya Kiarabu....
(Massamba, 2002:17).
Hapa tunaona wazi kwamba Massamba anapinga madai kwamba Kiswahili ni Kiarabu. Hata hivyo,
anaonekana kukubali kwamba Kiswahili kina maneno ya Kiarabu. Hivyo, tuseme kuwa kwa sababu
lugha ya Kiswahili ina maneno mengi ya Kiarabu na ushairi tunaouzungumzia hapa ni wa Kiswahili,
basi ingeshangaza sana kama ushairi huo usingetumia pia maneno ya Kiarabu. Hata hivyo, matumizi
hayo hayamaanishi kwamba ushairi huo ni wa Kiarabu. Jambo lingine muhimu kujikumbusha hapa
(kama ilivyokwisha daiwa na wanazuoni wengine), Kiswahili hakina maneno ya Kiarabu tu, bali pia
kina maneno ya lugha nyinginezo kama Kiingereza (kwa neno kama shati, sketi, skuli n.k.), Kijerumani
(kwa maneno kama shule toka katika schule) na kadhalika. Inasemwa kuwa ni tabia ya lugha zote
duniani kukopa maneno kutoka katika lugha nyingine. Kukopa huko hakuifanyi lugha kopaji kuwa
lugha kopwaji.
Kuhusiana na matumizi ya hati za Kiarabu katika ushairi wa mwanzo wa Kiswahili pia ni jambo
linaloelezeka na ambalo hatuwezi kulitegemea kuhalalisha kwamba ushairi wa Kiswahili ni Uislamu na
Uarabu. Matumizi ya hati za Kiarabu yanatokana na Waswahili kujifunza hati hizo na kuuweka ushairi
katika maandishi. Matumizi ya lugha fulani hayatoi kibali cha jambo kuwa la lugha hiyo. Kwa mfano,
tulishadokeza awali katika kitabu hiki kwamba kuna vitabu vingi vya Kiswahili vilivyoandikwa kwa
lugha ya Kiingereza. Hata hivyo, matumizi ya lugha ya Kiingereza hayavifanyi vipengele
vilivyoandikwa kuwa vya Kiingereza. Tunaweza pia kutumia lugha ya Kiswahili kuandika ushairi wa
Kiingereza na wa lugha nyinginezo. Akipinga kuuhusisha ushairi wa Kiswahili na Kiarabu kwa
kuegemea katika matumizi ya hati za Kiarabu Mutua (2006:3) anasema:
na ieleweke kuwa Waswahili au herufi za Kiarabu kuliwawezesha washairi (wambuji, malenga,
nguli na manju) wa Uswahilini, kuandika tungo zao wakitumia herufi hizo. Lakini matamshi ya
nyimbo yalikuwa ya Kiswahili. Kuja kwa Wazungu, na mafunzo yao ya herufi za Kilatini
kuliimarisha hifadhi kubwa ya hazina hiyo ya lugha na fasihi ya Kiswahili
Hivyo, Mutua anabainisha wazi kwamba si ujio wa Waarabu wala wa Wazungu unaoweza kuhusishwa
na asili ya ushairi wa Kiswahili. Jambo hili linathibitisha pasipo shaka yoyote kwamba nadharia
inayochukulia kwamba ushairi wa Kiswahili chimbuko lake ni Uislamu na fasihi ya Kiarabu zaidi ya
kuwa na ukweli wa namna fulani ina udhaifu. Ukweli wa nadharia hii unaonekana karibu katika hoja
zote tulizozipitia; hata hivyo, ukweli huo hautoshi kuegemeza madai kwamba ushairi wa Kiswahili ni
Uislamu na fasihi ya Kiarabu. Hata hivyo, ni lazima tukubali kwamba ushairi wa Kiswahili umepiga
hatua kubwa kutokana na mchango mkubwa sana wa Waarabu. Hawa ndiyo walileta hati za Kiarabu
ambazo zilitumika kuuhifadhi ushairi wa Kiswahili katika maandishi. Pia hawa walileta kaswida na
fasihi za Kiarabu ambazo ziliwahimiza Waswahili kuandika kazi za fasihi zao. Zaidi ya hayo, si kweli
kwamba Waarabu ndiyo walioibua ushairi wa Kiswahili. Aidha, mchango mwingine wa nadharia hii
inayodai kuwa ushairi wa Kiswahili unatokana na Waarabu na Uislamu ni kuwa yenyewe ndiyo ya
kwanza katika kuchunguza asili ya ushairi wa Kiswahili. Hivyo, iliweka misingi ya uchunguzi wa
chimbuko la ushairi wa Kiswahili. Hii ina maana kwamba nadharia nyingine zilizofuata ziliibuka
kutokana na udhaifu wa nadharia hii. Vilevile, tuseme hapa kwamba mjadala wa ushairi wa Kiswahili
45
kuibuka kutokana na Uislamu na Uarabu ulianzia katika lugha yenyewe, yaani lugha ya Kiswahili
ambapo pia madai kama hayo yalitolewa kwamba asili ya lugha ya Kiswahili ni Uislamu na Uarabu.
Massamba (2002:18) anapoelezea kasoro iliyopo katika kuihusisha lugha ya Kiswahili na Uislamu
anabainisha kwamba:
Kigezo cha dini ya Kiislamu ndicho kigezo dhaifu zaidi kuliko kile cha kwanza. Si sahihi
kuitumia dini kama kigezo cha kuiainishia lugha ya Kiswahili. Huko ni kuitumia dini mahali
ambapo si pake. Kwa hakika huko ni kushindwa kutofautisha utamaduni wa Kiarabu, Uislamu na
utamaduni wa Kiafrika…
Kama si sahihi kuihusisha dini na lugha, hatuna shaka si sahihi pia kuuhusisha ushairi wa lugha hiyo
na dini ambayo si sehemu ya utamaduni wa jamiilugha inayotumia ushairi huo. Kutokana na upungufu
wa nadharia hii sasa ndipo wataalamu wengine walipoibua nadharia tutakayoipitia katika sehemu
inayofuata.
2. CHIMBUKO LA USHAIRI WA KISWAHILI NI USHAIRI SIMULIZI WA KIBANTU
Mbali na nadharia hiyo, nadharia nyingine inayoelezea chimbuko la Kiswahili ni ile inayodai
kwamba ushairi wa Kiswahili unatokana na ushairi simulizi wa Kibantu, hasa nyimbo za ngoma na
nyinginezo. Nadharia hii inabainika katika maandiko mengi ya wanamapokeo ambao walidai kwamba
ushairi ni wimbo kama tulivyoona katika sura iliyotangulia. Kwa kudai kwamba ushairi ni wimbo, kwa
maneno mengine, walikuwa wanaibua dai kwamba chanzo cha ushairi wa Kiswahili ni nyimbo simulizi
zilizokuwapo tangu zama miongoni mwa jamii za Kiswahili. Wengi wa wanamapokeo tuliowapitia
hawafikii hitimisho hilo moja kwa moja ila Mnyampala (1964:4-7) analisema hilo waziwazi. Anasema:
Mashairi ni nyimbo zenye maghani ya mvuto wa madoido na vingorimbo bora. Aina ya nyimbo
hizo zilianzishwa na mababu au manabii wa zamani za kale, nazo ziliimbwa nyimbo hizo kwa ajili
ya kumtukuza na kumsifu mwenyezi Mungu, kwa masujudu yaliyoimbwa kishairi, haidhuru kwa
kukosana na vina na mizani baina ya mashairi ya leo na hayo.
Hapa Mnyampala anabainisha wazi kwamba anaufasili ushairi kuwa ni wimbo (na kwamba kama
shairi haliimbiki halina maana yoyote) kutokana na hoja kwamba ushairi wa Kiswahili umetokana na
nyimbo simulizi zilizoimbwa na mababu tangu zama za kale. Mnyampala anajenga hoja ambayo
haijengwi na wanamapokeo wengi wanaodai kwamba shairi ni wimbo. Mtazamo huu wa Mnyampala
unashadidiwa pia na Mutua (2006:3) anaposema kuwa mashairi ni tungo zenye kanuni maalumu
ambazo zina asili yake katika nyimbo. Zaidi ya kuungwa mkono, udhaifu wa Mnyampala ni kwamba
anayaona mashairi simulizi (nyimbo) kuwa yalibeba ajenda ya dini kama ajenda kuu. Dini, na hasa
Ukristo na Uislamu anaouzungumzia hapa, zilianza karne ya kwanza na ya sita mtawalia. Hivyo kama
mashairi yanahusiana na dini hizo tu ina maana kwamba mashairi hayo yameletwa na Wakristo na
Waislamu walioleta dini husika. Labda ili kuiboresha hoja hiyo tuseme kwamba mashairi yalikuwapo
hata kabla ya ujio wa dini hizo, wakati huo yakiisifu miungu ya Kiafrika, ambayo inadaiwa kuwapo
mahali pengi (taz. kuhusu miungu na nyimbo za kuwasifu katika Mulokozi, 2002 na Samwel, 2012a).
Hata hivyo, kama tutaliweka dai hilo hivyo, hoja kwamba ushairi chimbuko lake ni kazi na kwamba
binadamu waliimba nyimbo ili kuchapuza kazi, nyimbo ambazo zilizua mashairi itakosa nguvu. Dai
hilo kwa sasa linakubalika miongoni mwa wanafasihi wengi na limekwishafanyiwa tafiti za kina
kulithibitisha (Mulokozi, 1996). Tuseme tu kwamba wazo tunalolichukua kwa Mnyampala kwa sasa ni
kwamba ushairi wa Kiswahili chimbuko lake ni nyimbo. Wazo hilo pia linaonekana katika maandiko
ya wanazuoni na watafiti wa chimbuko la ushairi wa Kiswahili kama vile Chiraghdin (1971:7); Shariff
(1988), Senkoro (1988), Mulokozi (1996), Samwel (2012a) miongoni mwa wengi wengineo.
Wataalamu hawa wanadai kwamba asili ya ushairi wa Kiswahili ni nyimbo simulizi zilizoimbwa na
jamii za Waswahili. Jamii za Waswahili kama inavyochukuliwa hapa ni jamii mbalimbali katika upwa
wa Afrika Mashariki na bara. Jamii hizo hujumuisha watu wa makabila mbalimbali. Nyimbo za
makabila hayo ndizo hatimaye zilizokuja kuvyaza ushairi wa Kiswahili. Nyimbo hizo zilikuwa
zikiimbwa katika shughuli mbalimbali kama vile, wakati wa kufanya kazi, katika sherehe za harusi,
katika jando na unyago, kubembeleza watoto, kuombolezea n.k. na si katika ibada na kuwasifu miungu
tu.
46
Mtazamo kwamba ushairi wa Kiswahili unatokana na tungo simulizi za Waswahili unaonekana
pia katika andiko la Chiraghdin (1977) Malenga wa Mrima: Tungo za Mwinyihatibu Mohamed, la
Knappert (1979) Four Centuries of Swahili Poetry na la Mulokozi na Sengo (1995) History of
Kiswahili Poetry: AD 100-2000. Aidha, mtazamo huu unaonekana pia katika maandiko mengi ya
kisasa na umeshafanyiwa tafiti za kina na kuthibitika kwamba una madai ya msingi. Wanazuoni
mbalimbali wanathibitisha kwamba tungo simulizi za Waswahili zinahusiana sana na ushairi wa kisasa
wa Kiswahili. Mfano mzuri wa wanazuoni waliofanyia utafiti wa kina wa hilo ni Samwel (2012a)
ambaye alifanya utafiti wa kulinganisha na kulinganua ushairi wa Kiswahili wa kisasa wa vijana
(ushairi wa Bongo Fleva) na ushairi simulizi wa jamii ya Wahaya na Wasukuma (majigambo ya jadi).
Matokeo ya utafiti huo yanathibitisha uhusiano wa karibu uliopo baina ya aina hizo mbili za ushairi.
KUFANANA KWA USHAIRI WA KISWAHILI NA USHAIRI SIMULIZI WA KIBANTU
Suala la kufanana kwa ushairi wa Kiswahili na ushairi simulizi wa Kibantu limewashughulisha
wanafasihi mbalimbali. Miongoni mwa wanafasihi hao ni Mmbaga (2004) na Samwel (2012a) kwa
kuwataja wachache. Mmbaga (khj.) analinganisha ushairi wa ngonjera na ushairi simulizi wa kijadi
uliokuwapo katika makabila mbalimbali likiwemo kabila ya Wapare. Anabainisha kuwa ngonjera
zilikuwapo katika jamii mbalimbali za Wabantu tangu kale na kwamba fani inayoibuka katika miaka ya
1960-1970 kama inavyoonekana katika Ngonjera za Ukuta si fani mpya. Naye Samwel (2012a)
anashughulikia kufanana baina ya ushairi simulizi wa Kibantu na ushairi wa kisasa wa Kiswahili.
Anabainisha kuwa ushairi wa majigambo ya Bongo Fleva (ambao anaubainisha kama aina mpya ya
ushairi wa Kiswahili wa kisasa) unafanana sana na ushairi simulizi unaojibainisha katika majigambo ya
jadi ya Wahaya na Wasukuma. Kufanana huko kunabainika kuwapo katika vipengele vyote, yaani
katika maudhui na pia katika fani. Tupitie mfanano huo ili kujenga hoja inayotolewa na nadharia
tunayoishadidia.
I. Kufanana Kimaudhui
Samwel (2012a) anabainisha kwamba ushairi wa majigambo ya jadi na ushairi wa Bongo Fleva
unafanana sana katika dhamira, ujumbe, falsafa, itikadi na mawazo ya kazi ya fasihi kwa jumla. Katika
utafiti wake ilibainika kwamba aina zote mbili za ushairi hubeba maudhui ya kisiasa, kiuchumi, kijamii
na kiutamaduni. Baadhi ya maudhui yanayofanana baina ya majigambo ya jadi na ya Bongo Fleva ni
yahusuyo vita/ushindani, utawala, kazi, mila na desturi, imani za kidini na kadhalika. Tupitie kufanana
huko katika vipengele mahsusi ili kubaini hoja ya msingi:
(a) Kufanana kwa Maudhui ya Kisiasa
Kwa kuanza na maudhui ya kisiasa, tunaona kwamba, ushairi wa Kiswahili na ushairi simulizi
wa Kibantu unabeba maudhui kama vile vita na utawala. Kuhusu maudhui ya vita, tunaona kuwa jamii
za Kibantu za jadi zilihitaji kujipanua, hivyo kukawa na vita vya kugombea ardhi, mifugo, vyakula na
kadhalika. Kutokana na hilo, kukawa na ushairi wa vita. Maudhui haya ya vita yanabebwa pia na
ushairi wa Bongo Fleva. Aidha, tunabaini wazi kwamba katika aina zote mbili za ushairi shujaa ni mtu
muhimu.
Kufanana kwingine anakokubainisha Samwel kupo katika sifa za shujaa. Mbali na shujaa kuwa
mtu muhimu sana katika vita vinavyosawiriwa katika aina zote mbili za ushairi, sifa za shujaa huyo
katika aina zote mbili za ushairi zinafanana. Katika ushairi wa jadi, shujaa ni mtu jasiri, asiye na woga
na anayepambana ili kuilinda jamii yake. Katika ushairi huo, shujaa anakubalika katika jamii na
anaungwa mkono na wanajamii walio wengi katika harakati zake za kuitetea jamii husika. Aidha,
shujaa ni mtu mwenye nguvu nyingi za kimwili na uwezo wa kisihiri na kimiungu. Shujaa huyu pia
huogopa aibu kuliko kifo na rijali kamili. Samwel (2012a) anatoa mfano mzuri wa sifa hizi katika
Utendi wa Rukiza katika mistari ifuatayo kama inavyonukuliwa kwa Mulokozi (2002:87-88):
Waama ninahamanika
Heri nijiue kuliko kula vya haramu
Kula mboga za majani ya kunde na mnavu
Kula takataka zisanywazo na wajakazi!
47
Hapa tunaona Rukiza, ambaye ni shujaa katika utenzi huu, anasawiriwa kwamba hali kitu chochote tu
bali hula vitu vya hadhi ya juu na kwamba yupo tayari kufa kuliko kuaibika kwa kula vitu duni.
Sifa nyingine ya shujaa wa jadi ni kutokuwa mwoga na kuwa rijali kamili. Shujaa huyu hakuwa
anaogopa chochote na hata kifo. Pia alikuwa na uwezo wa kufanya tendo la ndoa kwa kiwango
kisichokuwa cha kawaida ambacho wanajamii wengine hawawezi. Katika Utendi wa Rukiza, kwa
mfano, tunaona Rukiza anabainishwa kwamba haogopi kifo na ana uwezo wa kufanya tendo la ndoa
usiku kucha. Katika mstari wa 465-475 wa utendi huo tuliyoinukuu hapa chini tunaliona hili. Tafsiri
yetu ya Kiswahili ya mistari hiyo inasema:
Mteule, mara zote umepigana vita,
Amka upigane vita…
Rukiza akarudi kulala
Kulipopambazuka
Akamwambia Ruhunga wa Nshaiga
Akasema ‘Unajua kukumbatia!
Mke wangu umenikumbatia tangu nilipokuja kulala…
Dondoo hili linatuonyesha kwamba shujaa Rukiza kama kiwakilisha cha shujaa wa jadi hakuogopa
kufa. Hata alipoambiwa maadui wameshafika, yeye akarudi kulala. Aidha, hapa tunaona shujaa huyu
jinsi alivyo rijali kamili kwani amefanya tendo la ndoa na mke wake usiku kucha. Vilevile tunaona
katika utendi huo kwamba shujaa huyu ndiye ambaye mara zote amepigana vita kuitetea jamii yake.
Sifa hizi za shujaa wa jadi zinafanana sana na za shujaa wa kisasa anayesawiriwa katika ushairi
wa Bongo Fleva. Katika ushairi wa Bongo Fleva shujaa anatajwa kuwa mtu asiye na woga na kiongozi
wa wengine katika mapambano ya kuitetea jamii husika. Aidha, shujaa huyo ndiye mtetezi mkuu wa
wanajamii husika, ana uwezo mkubwa wa kimwili na kiakili na rijali kamili. Samwel anatumia wimbo
wa “Mchakamchaka” ulioimbwa na Mr. 2 (Joseph Mbilinyi) ambapo msanii anasawiriwa kuwa ni wa
kwanza na wa mwisho (alfa na omega) na kwamba ndiye kiongozi (kamanda) kwa wenzake. Vilevile
hana uoga, ni mwakilishi wa watu na mtetezi wao (super delegeto, yaani super delegate) na mtu
asiyechoka katika kupambana kama inavyobainika hapa chini:
1. Anha alfa na omega
2. Na ndo maana ni vigumu sana kuiga
3. Kwenye maisha mimi kamanda
4. Sina uoga
5. Na wanga wanavyochonga mimi sipigi nao kelele
6. Zangu mimi ni vita mbele
7. Babu asikwambie mtu kitu
8. Jasho la mtu haliendi bure
9. Na kwenye maiki bado naikamata bongo
10. Yaani mfano wa Koffi anavyoikamata bongo na bolingo
11. Na bado nasaka mingo anha
12. Ni mchakamchaka ni mchakamchaka anha
13. Hakuna kuchoka
14. Mie niite super delegeto ama deiwaka
15. Nalicheza hili gemu nnavyotaka
16. Ni albam ya kumi lakini hasira kama ndo kwanza natoka
17. Maisha ni kama soka kusongana
18. Haitakiwi kuchoka kupambana
19. Na ndo maana kama Sumaye alisoma na utu uzima
20. Basi na mimi ntasoma
21. Najua maisha mazuri
22. Nakataa kurudi nyuma
23. Na maisha ni kujituma anha
Samwel anabainisha nyimbo nyingine zinazosawiri hilo kuwa ni “Moto Chini” na “Veto.”
Hata hivyo, Samwel anabainisha kwamba wakati ambapo katika ushairi simulizi vita
vilivyosawiriwa ni vita baina ya kabila na kabila, jamii moja na nyingine au koo na koo, katika ushairi
wa Bongo Fleva kwa kiasi kikubwa, vita vilivyosawiriwa ni vya mapambano dhidi ya maisha na
ushindani wa kimuziki. Vita katika ushairi wa Bongo Fleva havikuhusisha sana matumizi ya silaha
halisi bali vilikuwa ni vita vya maneno katika kushindania udhibiti wa soko la muziki. Hivyo, katika
ushairi wa Bongo Fleva, vita ni sitiari tu inayotumika kuashiria ushindani.
48
Kufanana kwingine kwa kimaudhui baina ya ushairi simulizi wa Kibantu na ushairi wa kisasa
kunakobainishwa na Samwel (2012a) kunaonekana katika maudhui yahusuyo utawala. Ushairi simulizi
wa Kibantu ulisawiri suala la utawala ambapo wasanii walijibainisha kwamba wao ndiyo viongozi
wanaowaongoza wengine na hawastahili kuongozwa. Samwel ananukuu ushairi wa Kisukuma
ulionukuliwa na Gunderson (2010:175) kama ifuatavyo:
1. Nkanda, ntaale wa Bazinza
2. Basukuma, tumanile
3. Lyene ihanga lya makangi
4. Baluganda lwa Bazinza
5. Hubataale ba Sukuma
1. Nkanda, mtemi wa Bazinza
2. Wasukuma, tunamjua
3. Kwa hakika ni nchi inayotisha
4. Koo za Bazinza
5. (Kwa hakika) ndio viongozi wa Wasukuma
Katika wimbo huu msanii anajibainisha kuwa ametoka katika ukoo wa Bazinza, ambao ni ukoo wa
viongozi bora wa kabila la Wasukuma. Hivyo, anajigamba kwamba ni kiongozi bora.
Maudhui haya ya utawala yanaonekana katika ushairi wa Bongo Fleva pia ambapo washairi
wanajibainisha kwamba wao ni viongozi wa wengine, tena ni viongozi bora. Samwel anatumia mfano
wa wimbo wa “Veto” ambapo Mr. 2 anajibainisha kwamba yeye ndiye rais (president) wa wanamuziki
wa Bongo Fleva na kwamba anatakiwa kutatua matatizo ya wanamuziki wa muziki huu.
(b) Kufanana kwa Maudhui ya Kiuchumi
Zaidi ya kufanana katika maudhui ya kisiasa, kuna kufanana vilevile katika maudhui ya
kiuchumi. Katika ushairi simulizi wa Kibantu tunaona wasanii wakijibainisha juu ya mafanikio katika
kazi. Walibainisha kwamba ni wakulima hodari, wafugaji wazuri na hata wawindaji wazuri. Samwel
(2012a) akimnukuu Songoyi (2005) anatoa mfano wa wimbo wa Kisukuma anaoutafsiri mstari 1-4
kama ifuatavyo:
Sisi ndio tunaozilima nyasi ngumu
Wakulima wa mtama
Wapaliliaji wa palizi
Kwa viwango vya Nyerere.
Katika mistari hii tunaona wazi kwamba msanii anaeleza kwamba wao ndio wakulima wa nyasi ngumu.
Anaendelea kueleza kwamba wao ndio wakulima maarufu wa mtama na wapaliliaji wa mashamba na
kwamba wanalima kwa viwango vya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Huu ni
ushairi wa kazi ya kilimo.
Ushairi wa kazi unaonekana pia katika ushairi wa Bongo Fleva. Samwel anatoa mifano ya
wimbo wa “Mchakamchaka” ambapo Mr 2 (Joseph Mbilinyi) anaelezea juu ya kazi yake kwamba
ndiyo inamjengea heshima (CV) katika jamii na inamwingizia fedha nyingi. Kazi anayojigamba kwayo
ni kazi ya uimbaji kama inavyobainika hapa chini:
1. Anha baada ya dhiki faraja
2. Nimeamini mambo mema
3. Ni kwa yule anayengoja
4. Na wa mbili havai moja anha anha
5. Sasa ni mwendo wa dolali4
6. Ndani ya akaunti mtoni utadhani mtoto wa Balali
7. Sema vijisenti vyangu ni vya halali
8. Bongo mchaka mchaka tu
9. Mafisadi hawalali
10. Nina uhuru wa kusema
11. Na nitasema chochote ntakachoona kinafaa mimi kusema
12. Na nnakuja na falsafa za Obama
13. Tunatakiwa kuchange
14. Tusipochange maisha bora kwetu ndoto kama muafaka wa Zenji anha
15. Wacha niendeleze dozi
16. Maana leo kama balozi
17. Kama kazi ni kazi hakuna ubitozi
18. Na ni upuuzi kusema gemu haliuzi
19. Wakati we unangoja kuuza tepu tu na CD
4 Dolali ni msimu unaotumika kumaanisha dola (za Kimarekani).
49
20. Sisi tunauza mpaka jezi
21. Ni kwa sababu tuna CV
22. Na huu ndo mchakamchaka tunaoutaka
23. Na anha anha hakuna kuchoka
Ushairi huu wa kazi ya uimbaji unaonekana pia katika ushairi simulizi wa Kibantu kama anavyonukuu
wimbo wa Kisukuma kutoka kwa Songoyi (2005) katika mstari wa 1-2 na wa 5-6 anapoutafsiri kama
ifuatavyo:
Ninapokuwa katika uwanja wa ngoma
Mimi ni chifu…
Kwa haya yote nimejiimarisha
Na wachawi
Wamenifanya mkuu.
Katika dondoo hili msanii anaeleza kwamba anapokuwa katika uwanja wa ngoma huimba vizuri kuliko
wengine wote; anaposema yeye ni chifu ana maana kuwa anawaongoza waimbaji wengine. Hapa
tunaona wazi kwamba, maudhui ya ushairi simulizi wa Kibantu na ushairi wa Kiswahili yanafanana.
(c) Kufanana kwa Maudhui ya Kijamii
Vilevile ushairi simulizi wa Kibantu na ushairi wa Kiswahili, na hasa ule wa Bongo Fleva,
unafanana katika maudhui ya kijamii. Tunaona katika ushairi simulizi wa Kibantu kuna ushairi
unaoelezea koo ambapo mtu alielezea ukoo wake. Aidha, washairi katika ushairi huo wa koo walielezea
miji na vijiji walikotoka na kuvinasibisha na mafanikio waliyonayo. Samwel anatoa mfano wa shairi la
majigambo ya Fransisco Lwihula, anayeelezea kuwa ni wa kutoka Kanazi ya Bukiza na kwamba ni wa
ukoo wa Kayango aliyezaliwa na Byorugano anayetokea Kola Omwinoni Onabe. Vilevile msanii
anaelezea vijiji anavyohusiana navyo kama vile Kyanyonyi Kyamwiiga na Kafunjo Kamugoro kama
inavyobainika hapa chini:
1. Naimuka aansi ndi Franscisko eya Lwihula
2. Omuli Kanazi ka Bukiza
3. Naimuka ndi musinjaigulu amuzio rugeju
4. Ndi wa Kayango
5. Ndi wa Byorugana
6. Ndi wa Kola Omwinoni Onabe
7. Ndi wa Kyanyonyi Kyamwigwa
8. Ndi wa Kafunjo Kamugoro
9. Eibanga ntemba Kasiko elipango
10. Ninyija ninzarwamu ta Balingililaki eya Tiinaba
11. Okwo mawe narugayo
1. Nainuka ni miye Fransisko, mtoto wa Lwihula
2. Wa kutoka Kanazi ya Bukiza
3. Nainuka kama shujaa wa mashujaa
4. Ni wa ukoo wa Kayango,
5. Ni wa ukoo wa Byorugana
6. Ni wa kutoka Kola Omwinoni Onabe5,
7. Ni wa kutoka Kyanyonyi Kyamwigwa
8. Ni wa kutoka Kafunjo Kamugoro
9. Hupanda mlima mrefu wa Kasiko
10. Kule nazaliwa na Mzee Balingililaki, mtoto wa Tiinaba.
11. Huo ni ukoo wa mama
Chanzo: Rubanza (1994): (Tafsiri na msisitizo wetu)
Ushairi huo wa koo hautofautiani na ule unaoonekana ushairi wa kisasa wa Bongo Fleva hasa katika
wimbo wa Dogo Janja uitwao “Mtoto wa Uswazi” au wa Prof. Jay (Joseph Haule) uitwao “Ndiyo
Mzee.” Katika ule wa Dogo Janja, msanii anajitambulisha kuwa anaitwa Dogo Janja anayetokea katika
mji wa Arusha (A-Town) ambapo katika wimbo wa Prof. Jay anajitambulisha kuwa anaitwa Joseph
Haule mtoto wa Msolopagazi anayetokea katika nchi iliyopo Kusini mwa Jangwa la Sahara.
MTOTO WA USWAZI wa Dogo Janja Ft Godzilla
KIbwagizo
My name is Dogo Janja a.k.a Forty Seven
A town soldier
Stick to books not drugs
Ubeti wa 1
1. Jua lilipotoka ndo nikawa nimezaliwa
2. Wala sikuwa na nguo nikadhani nimevuliwa
3. Nimezaliwa huko kwenye baridi kali
4. Arusha Tanzania hakuna jua kali
5. Hospitali Mount Meru ndipo nilitokea
6. Thanks mummy and thanx daddy
7. Kila siku nawaombea
5 Kola omwinoni onabe maana yake ni “shika kwenye tope unawe.”
50
8. Muishi pamoja mimi nimewazoea...
9. Muziki nimechagua coz ndo kipaji changu
10. Arusha nitarudi nipo Dar ninatafuta...
11. Waambie walionuna kwamba washachelewa
12. Wape hi Arusha waambie nitakuja
13. Nimekuja kutake over hawa washachuja
14. Hongera mama kwa kunizaa kidume
15. Maisha ya hapo home yananifanya nijitume
16. Najitahidi kwenye mgongo nijikune
17. Na hii ndio sababu ukanizaa mwanamume
NDIYO MZEE wa Prof. Jay
1. Ok ok naitwa Joseph Haule mwana Msolopazi
2. Nadhani nimeletwa kuokoa hiki kizazi
3. Mimi ni mwanasiasa niliyebarikiwa na Mungu
4. Nimeletwa kwenu waungwana niwapunguzie machungu
5. Mimi ni mteule Kusini mwa jangwa la Sahara
6. Ndio maana nimetunukiwa cheti cha juu cha utawala
7. Nina hekima kuliko mfalme Sulemani msiwe na wasi
8. Na hii nitadhihirisha pindi mtakaponipa nafasi
9. Actually, nimedhamiria kuwasaidia
10. Taifa lenye nguvu duniani liwe Tanzania
Chanzo: Profesa Jay (2001), Machozi, Jasho na Damu
Katika aina zote mbili za ushairi, ushairi simulizi wa Kibantu na ule wa Kiswahili, wasanii
wananasibisha mafanikio yao na koo zao na mahali walikotoka.
(d) Kufanana kwa Maudhui ya Kiutamaduni
Kufanana kwingine baina ya ushairi simulizi wa Kibantu na ushairi wa Kiswahili upo katika maudhui
ya kiutamaduni. Katika ushairi simulizi kuna suala la imani juu ya kuwapo kwa Mungu. Wasanii wa
ushairi huu, huelezea kwamba wana mafanikio makubwa kwa kuwa wanapendwa na Mungu. Samwel
anatumia mfano wa jigambo liitwalo “Okwebuga kwa Mugasha” (Kujigamba kwa Mugasha)
kubainisha hili:
1. Nayebuga ndi kijuikanila-nda
2. Ky’omwa Lwamula ilembo,
3. Entale Lubologa nsindila omumalungu
4. Ngutula enyama ndaliila
5. Manya bakama bazo tibaija Kyamuyanje
6. Mba kishuma kyo’ Mugasha yahaile
7. Ekiyo mbanda kabugu, Lubaga
8. Nyitila enfulu abutumbi
9. Mba kyegile;
10. Mba lulabyo, ndabiza kabwela
11. Omubanyanga ilala itakamile
12. Abayebembeile nkaita
13. Abasigaile enyuma echuchu
14. Yabaigala amaisho
15. Nikwo kyunyeta eibala lya Tibandekile Lwabukaya
1. Najigamba Kijuikanila-nda
2. Kwa Lwamula ilembo6
3. Simba mkali angurumaye mwituni
4. Hukatakata nyama na kuila
5. Najua wenyewe hawaji Kyamuyanje
6. Mimi ni jizi aliyepewa kisu kikali na Mugasha,7
7. Kisu kitumikacho kuchinja
8. Huulia samaki kilindini
9. Mimi ni mtu asiyeogopa chochote
10. Mimi ni radi, humulika kabwela
11. Kwa wachezaji ngoma
12. Ng’ombe hulala bila kukamuliwa
13. Waliotangulia niliwaua
14. Waliobaki nyuma vumbi liliwaziba macho
15. Ndipo waliponibatiza jina la Tibandekile
Lwabukaya
Chanzo: Rubanza (1994:58-62)
Katika jigambo hili tunaona mshairi akielezea kwamba amefanikiwa kwa kuwa alisaidiwa (alipewa
kisu kikali) na muungu (aitwaye Mugasha). Ushairi wa aina hii, unaonekana katika ushairi wa kisasa
wa Kiswahili ambapo wasanii wanahusisha mafanikio yao na Mungu. Tunaliona hili katika wimbo wa
Bongo Fleva wa Sister P (Happiness Thadei) uitwao “Achana Nao” ambapo katika mstari wa pili wa
wimbo huo msanii anasema “kipawa chatoka kwa Mola wala sijatumia ubani.” Msanii anaamini
mafanikio aliyonayo katika kazi yake ya uimbaji yanatokana na kipawa alichopewa na Mungu kama
inavyobainika hapa chini:
6 Lwamula ilembo ni usemi wa Kihaya ambao unamaanisha mleta baraka
7 Mugasha ni muungu wa Wahaya anayehusika na ziwa. Katika jamii za Wasukuma huitwa Ngassa.
51
1.Nafungua ubongo natoa fikra za utumwa kichwani
2.Kipawa chatoka kwa mola wala sijatumia ubani
3. Sister P kupata chati watu wanadhani rap utani
4. Rap biashara bwana ila angalia usijepata hasara
5.Kuuza vitumbua, pipi maandazi zote biashara
6.Usidharau hizo biashara watu watakuangushia msala.
7.Wasomi wengi wamesoma kwa kutumia hizo biashara
8.Mashairi sibahatishi na nitauza nyingi nakala
9.Na siyo utani nyota kwangu imeonekana biashara
10.Wandago rafiki zangu tena wa kina
11.We uliza maswali mengi majibu mimi sina
12.Nakupa rap shule mashairi yangu yana vina
Vilevile kwa kutambua kuwapo kwa Mungu na uwezo alionao, wasanii katika ushairi simulizi
walijieleza kwamba wao ni wachamungu na washika dini. Wanaeleza kuwa wanatenda mema ili
kumfurahisha Mungu azidi kuwafanikisha. Samwel anatoa mfano wa wimbo wa “Mba Ilungu
Lyobuamila” (Mwito wa Wahamiaji):
1. Naimuka ndi Shelestini
2. Nikwo ichumu ly’obugingo
3. Ndi kalamulila
4. Nindamulila abo nkalala nabo
5. Omukambi ya tata
6. Aikwimka ati munyampara
7. Ii ati mwami
8. Nyowe ntumile, nzagira
9. Ekitebe kilio, omukeka guli ao
10. Enyomyo eyo tata yansigiile empango eliwo
11. Buli muntu nimuwa ekitinwakye
12. Nkokwo nkukiya tata na mae
13. Nti Katonda mbeela
14. Ayandesile abukama
15. Mungu amwebembele
1. Naingia ndimi Selestini
2. Mimi ni mkuki wenye ncha kali
3. Mimi ni msuluhishi
4. Husuluhisha ninaoishi nao
5. Katika kambi ya baba
6. Anayeamka huniita kiongozi
7. Ii asema mwami (mtemi)
8. Mimi nimejivimbisha kwenye kiti
9. Kiti kipo, mkeka upo
10. Nguzo kubwa niliyorithishwa na baba ipo
11. Kila mtu ninampa heshima yake
12. Kama ninavyomuheshimu baba na mama
13. Nasema kuwa Mungu nibariki
14. Aliyenisogeza mbele ya utemi
15. Mungu amwongoze
Chanzo: Rubanza (1994:50-52)
Ushairi wa aina hii wa kujisifia juu ya kutenda mema unaonekana pia katika ushairi wa Bongo Fleva.
Samwel anatoa mfano wa wimbo uitwao “Sisi Tulivyo” ulioimbwa na Sister P ambapo katika mstari wa
1 wa wimbo huo anasema “mimi nilivyo ni mchamungu kuliko ulivyo” na; katika mstari wa 6-7
anasema anapenda sana mambo ya Mungu na kwamba anatenda yote yaliyoandikwa katika biblia bila
kuchagua. Katika mistari mingine anabainisha jinsi alivyo mtenda mema na kwamba anawaheshimu
watu wote hata maadui zake na pia anapenda amani kama inavyobainika hapa chini:
1. Mimi nilivyo ni mchamungu kuliko ulivyo
2. Mimi nilivyo siyo bitozi wa kupenda sana mademu
3. Mimi nilivyo sina habari na adui asemavyo
4. Mimi nilivyo sasa ni peace hakuna uadui
5. Wote rafiki awe msichana awe mvulana
6. Mimi nilivyo napenda sana mambo ya Mungu
7. Sichagui kama inavyosema Biblia
8. Mimi nilivyo sinywi pombe sivuti brother
Chanzo: Omari (2009:295)
II. Kufanana kwa Dhima
Zaidi ya kufanana kwa maudhui kwa ujumla, Samwel (2012a) anabainisha pia kufanana katika
kipengele cha dhima. Anabainisha kwamba aina zote mbili za ushairi zinaweza kuhifadhi historia ya
jamii husika, kukuza ushujaa, ujasiri na uzalendo, kuendeleza matabaka na kuhifadhi na kuendeleza
utamaduni. Kufanana kwingine kwa dhima ni kwamba, aina zote mbili za ushairi zinaadilisha na
kuadibisha na pia zinaburudisha.
Kwa kuanza na dhima ya kuhifadhi historia ya jamii Samwel anabainisha kuwa kuna kufanana
kwingi kidhima. Ushairi simulizi wa Kibantu unaweza kuhifadhi historia ya jamii kuhusu vita,
52
migogoro, maendeleo ya jamii na kadhalika. Anatoa mfano kuwa, ushairi wa vita huweza kusimulia
vita vilikuwa kati ya nani na nani, vilipiganwa wapi na lini na pia nani alishindwa katika vita hivyo.
Ushairi huo ulihifadhi historia ya vita hivyo kwa vizazi vijavyo ambavyo havikuvishuhudia. Vizazi
hivyo vilihabarishwa juu ya vita hivyo kupitia majigambo haya. Anatoa mfano wa ushairi wa aina hii
kutoka katika wimbo wa Kisukuma uitwao “Barugaruga” (Warugaruga) kama unavyonukuliwa hapa
chini:
1. Balugaruga! (x2)
2. Balugaruga! (x2)
3. Tulikapumula nanali kwihala? (x2)
4. Kwihala!
5. Bamashima mashima
6. Ooh, kwihala! (x2)
7. Twiyagalule!
1. Warugaruga (x2)
2. Warugaruga (x2)
3. Tunakwenda lini kulipua kwenye uwanja wa vita?
(x2)
4. Kwenye uwanja wa vita!
5. Sisi watu tunaoheshimika, heshimika
6. Ooh, uwanja wa vita (x2)
7. Tujimwage!
Katika wimbo huo, Warugaruga wanaelezwa kwamba ni mabingwa wa vita na kwamba
wanaheshimika kwa sababu ya ushindi wao vitani. Wimbo huo unatunza historia ya Tanzania kwani
askari hao wa Kirugaruga kweli walikuwapo na walitumiwa na watawala katika vita (Gunderson,
2010).
Ushairi wa Bongo Fleva nao unahifadhi historia ya jamii. Ushairi wa Bongo Fleva kama ulivyo
simulizi wa Kibantu unahifadhi matukio mbalimbali. Katika wimbo wa “Veto” ulioimbwa na Mr. 2
mwanajamii anahabarishwa juu ya ufisadi mkubwa ulioibuka Tanzania miaka ya 2000. Kwa mfano
tunaona katika wimbo huo msanii anataja ufisadi wa EPA ambapo fedha zinazofikia bilioni 133
ziliibwa kutoka katika akaunti ya madeni ya nje. Hili linabainika katika mistari ifuatayo ya wimbo huo:
1. Mi ndo president wa kitambo nishaapa
2. Matatizo ya hili gemu katu siwezi kwepa
3. Kama serikali inavyokwepa ishu ya EPA
4. Hatuogopi kukipaka
5. Hatujali tunachojali ni kuzibana ukweli
Chanzo: Mr. 2 (2009), Veto
Kufanana kwingine katika dhima za ushairi kunaonekana katika dhima ya kukuza ushujaa,
ujasiri na uzalendo. Samwel anabainisha kwamba aina zote mbili za ushairi, zina dhima ya kukuza
ushujaa, ujasiri na uzalendo. Anatoa mfano kuwa katika ushairi wa majigambo ya jadi mjigambi
aliporudi kutoka vitani au katika uwindaji alijigamba na kupewa zawadi mbalimbali zikiwamo
mashamba, mke na mifugo. Waoga walipewa kinyesi wakawape wake zao. Kutokana na hili, wanajamii
wengine walitamani kwenda vitani ili watakaporudi wajigambe. Aidha, wake nao walikuwa
wakiwahimiza waume zao kuwa jasiri ili wasijeleta nyumbani kinyesi. Ushujaa, ujasiri na uzalendo
ulisawiriwa na kusisitizwa pia katika maudhui ya majigambo yenyewe. Ushairi huo ulikidhihaki kifo na
kukifanya kionekane si kitu cha kutisha, kiliudhihaki woga na kuhimiza moyo wa ushujaa.
Aidha, katika dhima ya kuendeleza matabaka ushairi simulizi wa Kibantu na ushairi wa
Kiswahili (Bongo Fleva) unaonekana kufanana. Hii ni kusema kwamba aina zote mbili za ushairi
zinakuza na kuendeleza matabaka katika jamii. Samwel anaeleza kwamba katika ushairi simulizi wa
Kibantu, msanii alikusudia kuonyesha utii kwa watawala waliopo. Ndio maana katika ushairi wa
majigambo tendo la mwisho lilikuwa ni kujikabidhi au kukabidhi mateka kwa mtemi au mkuu wa ukoo.
Hali hii pia inaonekana katika ushairi wa Bongo Fleva ambapo wasanii wake hutumiwa katika kampeni
mbalimbali za urais. Wasanii hawa hulazimika kuwapigia debe wagombea husika bila kujali kufaa na
kukubalika kwao kwa jamii. Kwa kufanya hivyo, majigambo ya Bongo Fleva, kama yalivyo ya jadi,
yanakuza na kuendeleza matabaka.
Kufanana kwingine katika dhima za ushairi kwa jamii ni kwamba aina zote mbili zinaweza
kuhifadhi na kuendeleza utamaduni. Ushairi simulizi wa Kibantu huweza kubeba masuala mbalimbali
ya mila na desturi na umuhimu wake na hivyo kuendeleza mila hizo. Mila kama kufanya zindiko, ibada
ya mizimu na umuhimu wake na mila nyinginezo huweza kusawiriwa katika ushairi simulizi wa
Kibantu. Kwa kufanya hivyo, jamii huweza kukumbushwa juu ya mila zao na jinsi zilivyozisaidia jamii
za jadi. Jambo hili linaweza kuziendeleza mila hizo.
53
Kufanana kwa mwisho kwa dhima baina ya ushairi simulizi wa Kibantu na ushairi wa Kiswahili
na hasa wa Bongo Fleva kupo katika dhima za kuadilisha, kuadibisha na kuburudisha. Samwel
anaendelea kudai kuwa aina zote mbili za ushairi zinatoa maadili, zinatia adabu na pia kumpa mtu
burudani. Anaeleza kuwa katika ushairi simulizi wa Kibantu wanajamii huhimizwa mambo kama
kuwaheshimu wakubwa, kuwaheshimu watawala, kuwaheshimu wazazi na kadhalika. Inaonekana, kwa
mfano, katika ushairi huu msanii hulazimika kuyahusisha mafanikio yake na ukoo wake wa baba na
mama. Ushairi wa aina hii ulikusudia kuadibisha wanajamii kuwaheshimu wazazi. Aidha, inaonekana
kuwa ushairi wa aina hii uliimbwa wakati watu wanaenda vitani au wakati wa vita ili kujiliwaza na
kujipa burudani na kadhalika. Samwel anahitimisha kuwa hali kama hiyo ndiyo iliyoonekana katika
ushairi wa Bongo Fleva ambapo wasanii huwaadilisha, kuwaadibisha na kutoa burudani. Hivyo, hakuna
shaka kwamba aina hizi mbili za ushairi zinafanana sana.
III. Kufanana Kifani
Mbali na kufanana kimaudhui, Samwel (2012a) anabainisha kwamba ushairi simulizi wa
Kibantu na ushairi wa Kiswahili unafanana pia kifani. Kufanana kifani kunaonekana katika utungaji wa
ushairi huo, utendaji, muundo, mtindo, matumizi ya lugha na kadhalika.
(a) Kufanana katika Utungaji
Kwa kuanza na suala la utungaji, Samwel anaeleza kuwa ushairi simulizi wa Kibantu na ule wa
Bongo Fleva, unafanana sana. Aina zote mbili za ushairi ziliweza kutungwa papo kwa papo, bila
kukaririwa wala kuandikwa (Hodza na Fortune, 1979; Mulokozi, 1996; Peek na Kwesi, 2004) na pia
ziliweza kutungwa, kukaririwa na hata kufanyiwa mazoezi kabla ya utendaji wake. Sifa hizi, zinafanana
sana na ushairi wa Bongo Fleva. Kuhusu utungaji wa papo kwa papo wa ushairi wa Bongo Fleva,
wasanii huweza kutunga papo kwa papo wakati wa utendaji. Samwel anaeleza kuwa utungaji huu
unaitwa mtindo huru. Kwa upande wa utungaji wa kabla ya utendaji katika ushairi huu, huchukua
muda. Katika utungaji huu, msanii hukaa na kufikiria jinsi anavyoweza kuliwasilisha wazo alilonalo
kichwani. Muda unaotumika hutegemeana na kipaji cha utunzi alichonacho msanii. Aidha, katika
utungaji huu mtu anaweza kutunga mwenyewe wimbo au kutungiwa na mtu mwingine. Sifa hii, ipo pia
katika ushairi wa Bongo Fleva ambapo msanii huweza kutungiwa na kisha yeye kuyaghani au
kuyaimba. Katika ushairi wa Kiswahili wa kisasa, kuna watu ambao kazi yao ni kutunga mashairi na
kuwauzia wasanii wa Bongo Fleva pamoja na hakimiliki yake. Vilevile wapo wasanii wa Bongo Fleva
ambao kutokana na vipaji walivyonavyo wanawatungia wasanii wengine na kuwapa kutokana na
mahusiano waliyonayo.
(b) Kufanana katika Utendaji
Kipengele cha utendaji kinahusisha fanani (mtendaji) na hadhira (msikilizaji/mshiriki).
Vipengele vingine ni pamoja na mavazi yanayovaliwa katika utendaji wa majigambo pamoja na vifaa,
malipo/zawadi zinazoambatana na utendaji huo, uchezaji na sauti inayotumika katika utendaji wa
majigambo. Samwel (2012a) anabainisha kuwa kuna kufanana kwingi baina ya ushairi simulizi wa
Kibantu na wa Bongo Fleva katika vipengele hivyo vya utendaji.
(i) kufanana kwa Fanani
Fanani ni kipengele cha kwanza kitakachochambuliwa katika kufanana kwa utendaji wa ushairi.
Ushairi simulizi na wa Bongo Fleva unafanana sana katika utendaji na hasa fanani wake. Katika ushairi
simulizi wa Kibantu kuna tanzu za wanawake (sifo), tanzu za wanaume (majigambo) na kadhalika
(Rubanza, 1994; Mulokozi, 1996; Peek na Kwesi, 2004). Katika ushairi wa Kiswahili pia hali ni hiyo
hiyo. Ushairi wa Bongo Fleva, kwa mfano, unaonekana kuwa wa wanaume japo pia wapo wanawake
wachache. Mwanamke anayeimba muziki huu haraka sana huweza kuonekana katika jamii kuwa ni
muhuni.
Kufanana kwingine katika kipengele cha fanani kunatokana na ukweli kwamba ushairi simulizi
wa Kibantu na ule wa Bongo Fleva unaweza kuwa na fanani wa aina mbili: msanii mmoja na kikundi
cha wasanii. Hivyo, Samwel anasema kuwa utendaji wa ushairi kwa jumla, huweza kuwa wa aina
mbili, utendaji wa ushairi wa mtu mmoja mmoja na utendaji wa ushairi wa vikundi.
54
(ii) Kufanana kwa Hadhira
Tukiachana na kipengele cha fanani Samwel anaelezea pia kuwa hadhira ya ushairi simulizi na
ushairi wa Kiswahili inafanana. Katika ushairi simulizi, hadhira ilikuwa ni shirikishi kwa kiasi
kikubwa. Vivyo hivyo hadhira ya ushairi wa kiswahili ni shirikishi. Hata hivyo, hadhira ya aina zote
mbili za ushairi inaweza isiwe shirikishi hasa pale unaporekodiwa kwa kutumia teknolojia mbalimbali
kama vile kanda za kaseti, sidii na kadhalika. Teknolojia hizi hazikutumiwa hapo awali ndio maana
wanafasihi wa awali walidai kwamba majigambo ya jadi ni utanzu simulizi si andishi (Mulokozi, 1996;
Peek na Kwesi, 2004).
(iii) Kufanana kwa Uchezaji
Ushairi simulizi wa Kibantu na ule wa Bongo Fleva unafanana pia katika suala la uchezaji.
Katika ushairi simulizi wa Kibantu, uchezaji ni suala muhimu sana. Katika ushairi wa Bongo Fleva pia,
uchezaji ni mojawapo ya nguzo za muziki huo (Omari, 2009). Aidha, uchezaji katika ushairi simulizi
wa jadi, unaenda sambamba na uigaji wa matendo mbalimbali yanayosimuliwa (Finnegan, 1970;
Mulokozi 1996, Peek na Kwesi 2004:358). Samwel alibaini kwamba, hata ushairi wa Bongo Fleva
unaenda sambamba na matendo ya mwili hasa matumizi ya vidole, mikono, kichwa na kadhalika. Hii
inathibitisha hoja ya msingi kwamba, matendo ni uti wa mgongo wa fasihi simulizi (Finnegan, 1970;
1977 na Mulokozi 1996). Philip na Kwesi (2004:357) wanaeleza kwamba “majigambo (kama ushairi
simulizi wa Kibantu) ni utanzu wa masimulizi na inapotokea ukawekwa katika maandishi, uhai wake
hupotea kutokana na ukweli kwamba matendo ambayo ni uti wa mgongo wa fasihi simulizi hupotea”
(Tafsiri na ufafanuzi wetu). Hali hiyo imeonekana pia katika ushairi wa Bongo Fleva ambapo ili kuuza
kazi zao, wasanii wa ushairi huu wametoa kanda za kaseti na sidii za kusikiliza (audio CD) ambazo
hazioneshi matendo. Ni wazi kwamba sayansi na teknolojia, zaidi ya faida zake, ina athari hasi kwa
maendeleo ya fasihi simulizi.
(iv) Kufanana kwa Sauti
Kufanana kwingine ni katika sauti. Katika ushairi simulizi wa Kibantu kuna tanzu ambazo
zilitumia sauti iliyo kati ya uimbaji na uongeaji, yaani sauti ya kughani (Ndamugoba, 1987; Rubanza,
1994). Hata hivyo, ushairi simulizi uliojitokeza katika tanzu nyingine kama vile nyimbo za ngoma na
kadhalika, huimbwa (Songoyi, 2005; Gunderson, 2010). Ushairi wa Kiswahili kama unavyoonekana
katika Bongo Fleva pia unaonekana kughanwa na/au kuimbwa. Sauti ya kughani ndiyo ya awali kabisa,
uimbaji katika Bongo Fleva ni dhana iliyokuja hivi karibuni. Hapo awali, muziki unaobeba ushairi huu
(muziki wa Bongo Fleva) uliitwa muziki wa rap, yaani muziki wa kughani (Mwanjoka, 2011). Aidha,
kama ilivyo kwenye ushairi simulizi wa Kibantu ambapo kwa kiasi kikubwa wanawake hutumia sauti
ya kuimba huku wanaume wakighani (Ndamugoba, 1987; Mulokozi, 1996), katika ushairi wa Kiswahili
hasa unaojitokeza katika Bongo Fleva sauti ya kughani hutumiwa zaidi na wanaume kuliko
inavyotumiwa na wanawake. Samwel anamnukuu Suriano (2007:2) kuthibitisha hili anaposema
kwamba, “wanawake katika gemu (muziki wa Bongo Fleva), na hasa wanaoghani, ni wachache…”
(Tafsiri na Ufafanuzi wetu).
(v) Kufanana kwa Mavazi na Vifaa Vinavyotumika
Kufanana kwingine kifani baina ya ushairi simulizi na ushairi wa Kiswahili unaojitokeza katika
muziki wa kizazi kipya, ni matumizi ya ala, mavazi maalumu na vifaa mbalimbali. Rubanza (1994:3) na
Mulokozi (1996:83) wanabainisha kwamba ushairi simulizi wa jadi, na hasa wa kabila la Wahaya, ulienda
sambamba na ngoma zilizoitwa amakondere/omutoro na mavazi maalumu (maleba). Vifaa vingine
vilivyotumika ni pamoja na mikuki, miundu na mapanga. Vifaa vingine vilivyosaidia uwasilishaji wa
ushairi wa jadi ni ngoma, njuga, nanga na vifaa vingine vya jadi. Ala hizi hutofautiana kutoka jamii moja
hadi nyingine. Katika ushairi wa Kiswahili na hasa wa Bongo Fleva, pia suala la vifaa na mavazi maalumu
ni muhimu. Samwel anaeleza kwamba, ingawa kwa sasa hakuna vazi maalumu la ushairi wa Bongo Fleva,
hapo awali yalikuwepo. Aidha, ushairi wa Bongo Fleva nao unatumia vifaa mbalimbali kama gitaa, vinanda,
tumba na kadhalika. Vifaa kama ngoma, nanga, zeze na kadhalika vilivyotumiwa na jamii ya jadi havina
tofauti na vifaa vinavyotumiwa na jamii kwa sasa katika ushairi wa Bongo Fleva. Kwa mfano, gitaa halina
tofauti kubwa na nanga au zeze; pia ngoma hazina tofauti kubwa na tumba. Hivyo, tunaweza kusema
utofauti uliopo ni wa majina na umbile la vifaa, lakini vinatoa sauti zinazofanana. Huu ni uthibitisho
55
kwamba, aina hizi mbili za ushairi zinafanana sana isipokuwa kuna mabadiliko ya aina fulani yaliyotokea
katika utendaji wa majigambo ya jadi yaliyosababishwa na maendeleo ya kiteknolojia na hivyo kuibua aina
mpya ya majigambo, majigambo ya kisasa, yanayotumia vifaa vya kisasa.
(c) Kufanana kwa Mandhari
Kama ilivyo kwa vipengele vingine vilivyotangulia, kipengele cha mandhari pia kina kufanana
baina ya aina hizi mbili za ushairi. Aina zote mbili za ushairi hutendwa katika mandhari yenye watu
(hadhira). Vilevile aina zote mbili za ushairi huweza kutendwa katika kumbi mbalimbali.
(d) Kufanana kwa Wahusika na Mtindo
Vipengele vingine vya kufanana baina ya ushairi wa jadi na wa Bongo Fleva ni wahusika na
mtindo. Ushairi wa jadi na ule wa Bongo Fleva unaonekana kufanana katika vipengele vya wahusika na
mtindo pia. Kwa mfano, katika wahusika tunaona aina zote mbili za ushairi zinatumia wahusika
binadamu, wasio binadamu na hata viumbe wa ajabu. Kuhusu mtindo, tunaona aina zote mbili za
ushairi zina mitindo mbalimbali ukiwemo wa majibizano. Majibizano hayo katika aina zote mbili za
ushairi tunayaona kuanzia katika majina ya wasanii hadi katika ushairi wenyewe. Mfanano mwingine
wa mtindo unaonekana katika vipengele vifuatavyo:
· Kufanana kwa Lugha Inayotumika
Aina zote mbili za ushairi zinaonekana kufanana pia katika lugha inayotumika. Ushairi wa simulizi
hutumia lugha ya picha, ishara na tamathali nyinginezo za usemi (Guma 1967:1-11; Rubanza 1994:22;
Philip na Kwesi 2004:358). Picha na tamathali hizi ndizo zilizojenga mantiki na vielelezo. Tungo hizo
hupewa mapigo maalumu yanayofuatana na kasi ya sauti iendayo kwa mfululizo wa hari (kuonesha ari
na uwezo) ili usimuliaji wake uwe na mori na hamasa (Rubanza, 1994). Baadhi ya picha zenye
kufanana zinazotumika katika ushairi wa jadi na ule wa Bongo Fleva ni pamoja na silaha kama vile
mikuki, mishale na kadhalika; vifaa vya kilimo kama vile jembe; wanyama kama vile dubu, simba,
tembo na kadhalika; watawala wenye nguvu na kadhalika. Picha nyingine zinazotumika ni pamoja na
mawe, majabali na miamba. Mfano wa matumizi haya katika ushairi wa Bongo Fleva unaonekana pale
msanii Inspector Haroun anapojiita Jabali la Rap Katuni na Joh Makini, Mwamba wa Kaskazini.
Matumizi ya dhana ya jabali yanaonekana pia katika wimbo wa “MaDJ” wa Sister P katika mstari wa 3
wa wimbo huo msanii anasema “sasa nije kwa hasira kama vile jabali.”
Kwa upande wa ushairi wa jadi matumizi haya ya lugha ya picha tunayaona katika nyimbo
mbalimbali. Tunaona, kwa mfano, msanii Fransisco Lwihula katika wimbo wake anasema kwamba
anatoka katika miamba ya Ruguta. Dhana ya jabali, mwamba na jiwe inaonekana katika majigambo ya
jadi ya Kisukuma ambapo msanii aitwaye Peter Mlangwa anajiita Jiganga (yaani jiwe). Hapa tunaona
kuna mfanano mkubwa wa falsafa zinazobebwa katika sitiari. Wasanii wa aina zote mbili za ushairi
wanatambua ugumu wa jiwe, mwamba na jabali na ndio maana wanajinasibisha na vitu hiyo.
Kwa upande wa picha ya vifaa vya kazi kama vile jembe, tunaona pia picha hii inatumika katika
aina zote mbili za ushairi. Kwa mfano, katika ushairi wa jadi wa Kihaya msanii Marko Petro
anajifananisha na jembe. Katika mstari wa 5 wa wimbo wake anasema “natonya ndi kafuka mutema
nkeke” yaani “naingia jembe mfyeka magugu.” Ushairi wa Bongo Fleva pia unatumia ishara na picha
kama hii. Msanii Khalid Mohammed au TID anajiita pia Jembe. Naye marehemu Mr. Ebbo alijulikana
kama Jembe la Rap Asili.
Kufanana huku kunaonekana hata katika matumizi ya ishara ya majina ya kiutawala na kishujaa.
Samwel anatoa mfano wa msanii wa ushairi wa jadi wa Kisukuma aitwaye Gumha Mang’ondi
akijitambulisha kwamba yeye ni Kilomanyangaki yaani chifu (Songoyi, 1987:17). Aidha, katika ushairi
wa jadi wa Kisukuma ulionukuliwa na Samwel msanii anasema yeye ni chifu (mstari wa 1-2). Sitiari
hii ya uchifu inatumiwa sana na wasanii wa ushairi wa Bongo Fleva. Miongoni mwao ni pamoja na
Anselm Ngaiza anayetumia jina la majigambo Chifu Rumanyika na Abubakar Katwila anayejulikana
pia kama Q. Chief. Vilevile tunaona msanii wa ushairi wa jadi wa Kisukuma aitwaye Balele Ngoya
akijitambulisha kwa jina la kishujaa la Masahi-o-Mbuga yaani Mmasai wa mbuga. Jina hilo hilo la
Mmasai linatumiwa na msanii wa Bongo Fleva Abel Motika a.k.a Mr. Ebbo kujitambulisha. Picha
nyingine ya kishujaa inayotumiwa pande zote ni picha ya kamanda au jemedari.
56
Kufanana pia kunaonekana katika picha na ishara zinazohusiana na wanyama. Kwa mfano,
tunaona katika shairi la jadi la Kihaya linalonukuliwa na kufafanuliwa katika Rubanza (1994:4-5),
inaelezwa kwamba Mtemi Mutatembwa anafananishwa na Simba wa Mwiko. Picha hii ya simba
inaonekana kutumika pia katika ushairi wa Bongo Fleva ambapo Afande Sele anajitambulisha pia kwa
jina la majigambo Simba Mzee.
Si hivyo tu bali pia kuna kufanana katika tamathali zinazotumika. Kwa mfano, tunaona katika
ushairi wa jadi ulionukuliwa na Samwel, msanii anasema “ninaingia kama radi.” Tamathali hii
inatumika pia katika jigambo la jadi la Kihaya lililonukuliwa na Rubanza (1994:4-5) ambapo zaidi ya
kumfananisha Mtemi Mutatembwa na Simba wa Mwiko anamfananisha pia na Radi Kuu. Tamathali
kama hii inatumika katika ushairi wa Bongo Fleva. Katika wimbo wa MaDJ ulioimbwa na Sister P
tunaliona hili. Katika mstari wa 8 wa wimbo huo msanii anasema “sauti yangu inatambaa kwenye beat
kama radi.” Hii haina tofauti na sitiari “mimi ni radi humulika kabwela” inayobainishwa na Rubanza
(1994) kuwa imetumika katika majigambo ya Kihaya.
· Kufanana kwa Matumizi ya Mapigo, Vina na Mizani
Pia kufanana kwingine kupo katika mapigo na suala la urari wa vina na mizani. Ushairi wa jadi
umebainika kwamba haukufuata kanuni ya urari wa vina na mizani kama sifa yake kuu ingawa ulikuwa
na mapigo. Kwa upande wa ushairi wa Bongo Fleva, ingawa yapo mashairi yanayofuata kanuni ya urari
wa vina na mizani, ushairi wa Bongo Fleva, haulazimiki kufuata kanuni hii. Aidha, ushairi huu nao una
mapigo. Kwa hiyo, tunawasilisha hapa hoja kwamba madai ya walioitwa wanausasa katika mgogoro wa
ushairi kwamba si lazima shairi liwe na urari wa vina na mizani yalikuwa ya msingi kwani yalilenga
kuurejesha ushairi wa jadi wa Kiafrika uliokuwapo tangu enzi katika jamii za Kiafrika katika mifumo
mbalimbali, ukiwamo ushairi wa majigambo. Kwa kuwa ushairi simulizi wa Kibantu haukuwa na urari
wa vina na mizani, hakukuwa na sababu ya kung’ang’aniza kuwapo kwa vina na mizani katika mashairi
yetu.
Samwel (2012a) anahitimisha kwa kusema kwamba, ushairi wa jadi na wa Bongo Fleva, unafanana
sana kifani ingawa pia kuna tofauti ndogondogo. Kufanana huku kifani, na kimaudhui kunaonesha wazi
kwamba ushairi wa Bongo Fleva umejengwa juu ya msingi wa ushairi wa jadi. Kwa maneno mengine
tunaweza kusema, kutokana na mabadiliko mbalimbali ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni,
utanzu wa ushairi ulilazimika kubadilika ili usipotee. Mabadiliko hayo ndiyo yakaibua ushairi wa
Kiswahili, ushairi unaojitokeza katika miziki mbalimbali ni mifano ya hiyo.
Aidha, anaendelea kudai kwamba kufanana huku ni uthibitisho kwamba wasanii wa ushairi wa
Kisasa wa Kiswahili wamechota mbinu za jadi (kutoka kwenye ushairi simulizi) na kuziingiza katika
ushairi wa kisasa wa Kiswahili. Peek na Kwesi (2004:358) wanaelezea uwezekano wa utanzu mmoja
kuazimwa na kutumiwa katika ushairi wa kisasa. Wanaeleza kwamba hiki si kitu kigeni kwani
kinaonekana katika nchi mbalimbali kama vile Zimbabwe ambapo nyimbo za kwaya za kudai uhuru za
miaka ya 1970 ziliazima na kutumia majigambo ya Nehanda, Kaguvi na Chiminuka ambao walikuwa
mashujaa wa kale. Sifa za mashujaa hao wakapewa wapigania uhuru wa Zimbabwe kama Mugabe,
Chitepo, Takawira na Nkomo. Rubanza (1994:22) akichangia jambo hili anasema:
Majigambo pia yanaweza kutumika katika senema na katika makundi ya maigizo. Vivyo hivyo, majigambo
yanaweza kutumika katika ushairi na riwaya. Matumizi haya yana kasoro zake…Kasoro hizo ni pamoja na
kukosa kuuona utendaji wa mjigambi na/au kundi lake. Kukosa ubora wa muziki unaoambatana na
ujigambi huo na pia kumnyima msikilizaji uwezo wa kushiriki kimatendo. Hata kati ya uchaguzi wa ama
majigambo kutoweka au kurekodiwa ni bora nusu shari kuliko shari kamili. Hivyo, ni vema kuyahifadhi
majigambo na kuyatumia kwa kila njia tutakayoweza.
Dondoo hili linatueleza tanzu zinazoweza kuazima utanzu wa majigambo (kama kielelezo cha ushairi
simulizi wa Kibantu) na kuutumia na pia madhara ya ushairi simulizi (majigambo) kutumika katika
tanzu hizo. Hata hivyo, dondoo hilo linahitimisha kwamba ni muhimu ushairi simulizi (majigambo)
kutumiwa katika tanzu nyingine. Tuhitimishe tu kwamba ushairi wa Kiswahili na ushairi simulizi wa
Kibantu vinahusiana sana na kwamba ushairi simulizi ndiyo umezaa ushairi wa Kiswahili.
57
SURA YA NNE
HISTORIA YA USHAIRI WA KISWAHILI
Ushairi wa Kiswahili una historia ndefu sana. Ushairi simulizi wa Waswahili unasemekana
kwamba ulikuwapo tangu lugha ya Kiswahili ilipoanza kutumika. Mulokozi na Sengo (1995:25)
wanakiri kwamba si rahisi kueleza ni lini hasa ushairi simulizi wa Waswahili ulianza. Kwa upande wa
ushairi andishi wa Kiswahili, ni vigumu pia kueleza ni lini hasa ulianza. Hali hii inatokana na sababu
kuu moja kwamba wataalamu mbalimbali wamekuwa na mitazamo tofauti juu ya jambo hilo. Mulokozi
na Sengo (1995:25) wanabainisha kuwa wakati Knappert (1979:66) anadai ushairi andishi wa mwanzo
wa Kiswahili ni Hamziyya ulioandikwa mnamo mwaka 1652, Harries (1962:5) anadai ushairi wa
mwanzo wa Kiswahili ni Tambuka (Tabuka) ulioandikwa mwaka 1728. Hata hivyo, utafiti wa
Mulokozi na Sengo unabainisha kwamba huenda wote wawili (Knappert na Harries) wamekosea na
kuwa ushairi andishi wa mwanzo wa Kiswahili umekuwapo tangu wakati wa Fumo Liyongo ambaye
anaaminika kuishi mnamo karne ya 13 huko Pate katika pwani ya Kenya. Aidha, utafiti huo
unabainisha ushairi andishi wa mwanzo wa Kiswahili ni “Swifa kwa Mwana Manga” unajulikana pia
kama “Tumsifu Yanga” ambao unahusianishwa moja kwa moja na Fumo Liyongo. Ushairi huo
umebainika uliandikwa mwaka 1532 B.K. Hata hivyo, Mulokozi na Sengo wanakiri huenda nyaraka
nyingi zitagundulika baadaye ambazo zitatufanya tubaini kwamba ushairi andishi wa Kiswahili
umekuwapo hata kabla ya hapo. Katika andiko hili, tunachukulia kuwa ushairi wa mwanzo wa
Kiswahili ulianza kuandikwa pale tu taaluma ya maandishi ilipoingia.
Tangu kuibuka kwa ushairi wa mwanzo wa Kiswahili hadi sasa, ushairi huo umepitia historia
ndefu sana na vipindi tofauti tofauti vya kihistoria. Tunaweza kuvigawa vipindi hivyo katika makundi
makuu mawili: kipindi cha kabla na wakati wa ukoloni (ushairi wa Kiswahili kabla na wakati wa
ukoloni) na kipindi cha baada ya uhuru (ushairi wa Kiswahili baada ya uhuru). Kipindi cha kabla na
wakati wa ukoloni tunaweza pia kukigawa katika makundi madogomadogo manne. Kundi la kwanza ni
kipindi cha ujima; kundi la pili ni kipindi cha ustawi wa miji, utamaduni na tawala za Waswahili; kundi
la tatu ni kipindi cha utawala wa Wareno na upinzani wa wananchi dhidi yao na; kundi la mwisho ni
kipindi kilichoasisiwa na utawala wa Waarabu wa Omani na kumalizikia na utawala wa Kiingereza na
Kidachi.
Kipindi cha kwanza, kipindi cha ujima kilidumu tangu binadamu alipopata urazini na kutoka
kwenye uhayawani hadi kama mwaka 600. Kipindi cha pili, kipindi cha ustawi wa miji, kilidumu kwa
kama miaka 600 hivi (yaani kuanzia mwaka wa 900 – 1500 BK). Kipindi hiki kilimalizwa na utawala
wa Wareno. Kipindi cha tatu kilianza kwa utawala wa Wareno na hatimaye wananchi wakaanza
kuupinga utawala huo. Kipindi hiki kilikuwa kati ya mwaka 1500 – 1730. Kipindi hiki, kiliishia kwa
kutekwa kwa Ngome ya Yesu (Fort Jesus) na kuingia kwa utawala wa Waarabu wa Oman (kama
mwaka 1730) na kumalizika wakati wa maingilio ya wakoloni wa Kidachi (kama mwaka 1890 baada ya
mkataba wa Berlin na Heligoland) na hatimaye ukoloni wa Kiingereza (kama mwaka 1918, baada ya
Wajerumani kushindwa katika vita kuu vya kwanza vya dunia).
USHAIRI SIMULIZI WA KISWAHILI WAKATI WA UJIMA
Inadaiwa kwamba binadamu anatokana na sokwe na alipitia hatua mbalimbali hadi kufikia
kuwa mtu kamili (homo sapiens). Kipindi cha ujima kinaanza pale binadamu alipopata urazini na
kuanza kuishi kama mtu kamili baada ya kutoka katika katika hali hiyo ya usokwe. Katika hatua za
awali za kipindi cha ujima, binadamu waliishi kwa uwindaji na ukusanyaji wa matunda. Taratibu
binadamu alipiga hatua na kuanza kuyatawala mazingira yake na kuanza kufanya kazi mbalimbali
ikiwemo kazi ya kilimo katika kile kinachoitwa mapinduzi ya kilimo (Neolithic Revolution). Mapinduzi
haya ya kilimo yalisababisha maendeleo makubwa katika maisha ya binadamu na binadamu sasa
wakaanza kuishi pamoja.
Katika kipindi chote hiki cha ujima, mwanadamu alishaibua ushairi kama njia mojawapo ya
kujiliwaza wakati wa kufanya kazi. Hakuna ushahidi kuwa katika kipindi hiki kulikuwa na kazi
nyingine za fasihi bali ushahidi uliopo unaonesha kwamba hiki kilikuwa ni kipindi kilichotawaliwa na
nyimbo za kazi. Hivyo, ushairi wa kazi unachukuliwa kuwa ndiyo ushairi wa mwanzo kabisa (Senkoro,
1988) na pia fasihi ya mwanzo kabisa. Mwanadamu aliimba nyimbo mbalimbali wakati wa shughuli
mbalimbali alizozifanya. Jukumu la nyimbo hizi lilikuwa ni kumliwaza na kumsahaulisha machovu ya
58
kazi husika. Senkoro (1988:2) anasema kuwa ushairi huu wa awali, ambao ulijitokeza zaidi katika
nyimbo za kazi, uliathiri hisia za mwimbaji na kumsukuma kufanya kazi kwa dhati zaidi na
kumsahaulisha ugumu wa kazi ile. Anaendelea kueleza kwamba jukumu hili la nyimbo la kufanya kazi
ngumu na nzito ionekane kutokuwa na hatari yoyote, ndilo linaloonyesha nguvu ya ushairi; na hata
wataalamu wengine wameipa nguvu hii sifa ya UCHAWI na kusema kuwa ushairi umetokana na
uchawi.8 Nyimbo za kazi ziliendelea kudumu kwa muda mrefu na hadi sasa, ingawa kuna mabadiliko
makubwa katika utanzu wa ushairi, nyimbo za kazi (ushairi wa kazi) bado umeendelea kuwa sehemu
muhimu ya ushairi wa Kiswahili.
USHAIRI WA KISWAHILI KATIKA KARNE YA 10 NA 16
Hiki kilikuwa kipindi cha ustawi wa miji, utamaduni na tawala za Waswahili. Kama tulivyoeleza hapo
awali (katika sura iliyopoita), ushairi wa Kiswahili unatokana na ushairi simulizi wa Kibantu. Ushairi huu
ulihusisha majigambo, tondozi, pembezaji, mbolezi, nyiso, chapuzo, na nyimbo nyinginezo kama vile nyimbo za
kazi na kadhalika. Mulokozi na Sengo (1995:75-76) wanabainisha kwamba kipindi hiki kilitawaliwa na tungo
zilizodaiwa kuwa za Fumo Liyongo. Kutokana na mapokeo tunaambiwa kwamba mshairi wa kale zaidi
anayefahamika ni Fumo Liyongo, ambaye inasemekana kuwa aliishi maeneo ya Shaka, Kipini na Pate huko
pwani ya Kenya katika karne ya 13 au kabla/baadaye. Hakuna hakika kama kweli Liyongo ndiye hasa mtunzi wa
tungo hizo, ila jambo la hakika ni kwamba nyingi zilimuhusu yeye mwenyewe. Iwapo Liyongo ndiye mtunzi,
yaelekea kuwa alitunga mashairi yake kwa ghibu bila kuandika. Tungo zake nyingi zilihifadhiwa kichwani hadi
zilipoandikwa katika miswada karne nyingi baadaye. Utungo wake wa kale zaidi uliotiwa katika maandishi
unaitwa “Swifa ya Mwana Manga” au “Kumsifu Yanga” (Mulokozi na Sengo, khj.; Mulokozi, 1996; Ridhiwani,
1996:22 – 32). Utungo huo unadaiwa kutungwa na Liyongo mwenyewe akimsifia mke wake na ulikuwa simulizi
hadi mwaka 937 H (sawa na mwaka 1531 BM) (Mulokozi, 1999). Kama tulivyoona hapo awali, kuna baadhi ya
wanazuoni, akiwemo Mulokozi na Sengo (1995), wanauchukulia huu kuwa ndiyo utungo wa kwanza wa ushairi
andishi wa Kiswahili.
Ingawa inaaminika kuwa Liyongo aliishi kabla ya karne ya 16, lakini tungo zinazomuhusu (zilizotungwa
na wengine) ambazo tunazo ziliandikwa mwanzoni mwa karne ya 19. Tungo hizo ni “Takhmisa ya Liyongo”
(Sayyid Abdallah bin Ali, kama mwaka 1800 BM) na “Utenzi wa Fumo Liyongo” (Muhamadi Kijumwa, 1913).
Hata hivyo, tungo hizi za baadaye, zilitokana na fasihi simulizi inayomhusu Liyongo na iliyotungwa zama za
Liyongo mwenyewe. Hivyo, kwa kiasi fulani kimaudhui na kihisia zinaakisi kipindi cha 900 – 1500 BK
tunachokizungumzia. Kwa hiyo, Utendi wa Fumo Liyongo ndiyo utenzi wa kale zaidi katika tenzi tatu za kale
(tenzi zingine mbili ni Utenzi wa Mwanakupona na Utenzi wa al-Inkishafi) ingawa umewekwa katika maandishi
karne ya ishirini (taz. Mulokozi (1999) Tenzi Tatu za Kale).
Tungo za Fumo Liyongo zinahusu ustawi wa miji ya pwani. Miji hiyo ni pamoja na Kilwa, Mombasa na
Pate. Miji hii ilisitawi kutokana na biashara ya Bahari ya Hindi (Indian Ocean Slave Trade) iliyoshamiri sana.
Utendi wa Fumo Liyongo, kwa mfano, unaelezea kusitawi kwa mji wa Pate alipoishi Liyongo. Utenzi huu
ulitungwa kutokana na hadithi za kimapokeo kuhusu Fumo Liyongo miongoni mwa Waswahili. Hata hivyo,
masimulizi ya maisha ya Liyongo kama yanavyotokea katika utendi huo si kamili, bali ni simulio mojawapo tu la
maisha yake. Masimulio mengine kama yanavyotokea katika nyimbo zake (zinazomuhusu) yameachwa (taz.
maelezo ya kina ya utenzi wa Fumo Liyongo katika Mulokozi, 1999:1-19).
MCHANGO WA WAARABU KATIKA USHAIRI WA KISWAHILI
Waarabu ndiyo wageni wa mwanzo kuja katika upwa wa Afrika Mashariki. Hawa walikuja na kuanza
kufanya biashara na wenyeji wa upwa huo ikiwamo biashara ya watumwa. Waarabu pia walileta dini ya
Kiislamu ambayo ilianza kuwa maarufu na watu wakaacha dini yao ya jadi. Aidha, Waarabu walileta hati zao za
Kiarabu. Dini hii na hati za kiarabu, zilikuwa na athari kubwa katika maendeleo ya ushairi wa Kiswahili. Ndipo
hapa sasa hati za Kiarabu zikaanza kutumika kuhifadhi ushairi wa Kiswahili. Aidha, kwa kuwa watunzi wengi
wa mashairi walishabadili dini na kuwa waislamu, hata maudhui ya mashairi yao yalisawiri dini hii. Vilevile,
kutokana na hilo hata aya za Korani na dua za Kiislamu zikaanza kuingizwa katika ushairi wa Kiswahili. Sio
hivyo tu, bali pia hata muundo wa mashairi ya Kiarabu ukaanza kutumika katika mashairi ya Kiswahili. Ndipo
hapa sasa ushairi wenye urari wa vina na mizani ulipoingia. Kasida ni mfano wa ushairi wa kisasa wa Kiarabu
8 Senkoro (1988:11) anafafanua kuwa wazo hili la kuwa ushairi chanzo chake ni uchawi limeelezwa kwa kirefu na George
Thomson katika Studies in Ancient Greek Society: The pre-historic Aegean. Senkoro (khj.) anaendelea kufafanua kuwa
katika Kiswahili, wazo hilo limeendelezwa na K.K. Kahigi katika makala yake, “Ushairi (Mtazamo wa Kisayansi)” katika
Kiswahili, Tol. 411 (Machi 1975). Kwa maelezo ya kina kuhusu haya taz. Senkoro (1988) Ushairi: Nadharia, Tahakiki na
Mifano.
59
ambao una vina na mizani na pia umeanza kutumika hata katika ushairi unaoonekana katika muziki wa Bongo
Fleva ambao katika andiko hili tumechukulia kuwa ni sehemu ya ushairi wa kisasa wa Kiswahili. Aidha, kama
tulivyodokeza katika sura iliyopita tukimnukuu Mulokozi na Sengo (1995:87) hata istilahi kadhaa za kishairi
zilitokana na ujio wa Waarabu. Istilahi hizo ni pamoja na shairi, mizani, ubeti, tathlitha, tarbia na takhmisa.
USHAIRI WA KISWAHILI KATIKA KARNE YA 17 NA 18
Baada ya kipindi cha ustawi wa miji kilichotokana na biashara baina ya wenyeji na Waarabu, kikaja
kipindi cha pili, kipindi cha uvamizi wa wakoloni wa Kireno. Hawa walikuja kutokana na safari zenye mafanikio
za Dkt. David Livingstone. Wareno walikuja wakiwa na lengo la kudhibiti biashara iliyokuwa inafanywa baina
ya Waswahili na Waarabu. Hivyo, ujio wao uliambatana na vita vya kudhibiti biashara hiyo na kupelekea miji
iliyositawi awali kuporomoka. Miji ya Kilwa, Mombasa na Pate ilipoteza udhibiti wa biashara ya Bahari ya
Hindi na hivyo ikaanza kuporomoka. Biashara hiyo ilichukuliwa na maharamia na wafanyabiashara wa Kireno
na pia ilididimia kutokana na kushambuliwa mara kwa mara na majeshi ya Kireno ambayo yaliwapora mali zao.
Kuporomoka huku kwa miji ndiko kunakosawiriwa katika Utenzi wa al-Inkishafi, utenzi ambao pamoja na
mambo mengine, unazungumzia kuporomoka kwa mji wa Pate (kwa maelezo ya kina ya utenzi huu na utenzi
wenyewe taz. Mulokozi, 1999:63 – 64, 69 -71).
Katika kipindi cha utawala wa Wareno, ushairi kwa kiasi kikubwa ulibaki kuwa simulizi uliokuwa katika
muundo wa nyimbo. Waswahili walitunga mashairi ya kisiasa yaliyowakashifu Wareno na kuibua moyo wa
ushujaa miongoni mwao ili kupambana nao na kuilinda miji yao ya pwani. Mulokozi na Sengo (1995:76)
wanabainisha kwamba kwa bahati mbaya ushairi mwingi simulizi wa kipindi hiki haukuhifadhiwa isipokuwa
vipande vichache kama kile cha Mzungu Migeli wanachokinukuu kama ifuatavyo:
Mzungu Migeli u mwongo
Mato yako yana chongo
Kwani kuwata mpango
Kwenda kibanga uwani?
Wimbo huu unaelezwa kuwahusu Wareno (ambao hapa wanapewa jina la Migeli) ili kuwaonya na vita
vitakavyofuata (Mulokozi, 1982:28 – 29; Mulokozi na Sengo, 1995:76).
Baada ya upinzani wa muda mrefu, hatimaye utawala wa Wareno ulipinduliwa na ndipo kikaanza kipindi
cha tatu, kipindi cha utawala wa Waarabu wa Omani. Katika kipindi hiki Uislamu na ushairi wao ulianza tena
kuwa maarufu na mashairi mengi ya kidini yaliandikwa. Kipindi hiki kilizua tungo nyingi za tendi za kidini
zilizorejelea katika historia ya kuasisiwa kwa Uislamu huko Arabia kama vile Mgeni bin Faqihi, Tabuka,
Hamziyya na Siri ‘lAsirari. Pia kipindi hiki kilishuhudia utendi wa kimawaidha wa Mwanakupona Binti
Mshamu (Utenzi wa Mwanakupona). (Kwa maelezo ya kina kuhusu Utenzi wa Mwanakupona na matini
yenyewe taz. Mulokozi, 1999:107 -109).
USHAIRI WA KISWAHILI KATIKA KARNE YA 19
Kama tulivyodokeza hapo awali, hiki kilikuwa kipindi cha utawala wa Waarabu wa Omani. Waarabu
hawa walihamisha makao yao toka Omani kuja Afrika Mashariki ambako walifungua mashamba. Aidha, kipindi
hiki pia kilikuwa na uvamizi baina ya miji ya Waswahili ambapo kila mji ulitaka kuutawala mji mwingine.
Utawala wa Waarabu wa Omani ulihusisha pia biashara za watumwa, ufanyaji kazi kwa lazima na kadhalika, na
hivyo, Waswahili wakaanza kuuchukia. Kwa hiyo, upinzani dhidi ya Waarabu hawa ukaanza. Washairi nao
walitunga kazi kuupinga utawala huo wa Waarabu na pia kuhimiza ulinzi wa miji yao dhidi ya uvamizi wa
Waswahili wengine. Mfano mzuri wa mashairi ya wakati huo yanaonekana katika wimbo wa Wakilindi
ulionukuliwa na Mulokozi (1982:33) na Mulokozi na Sengo (1995:76-77). Wimbo huo tunaunukuu pia hapa:
Wakilindi si watu ni pundamilia
Walikuza nti yao kwa reale mia (waliuza nchi yao)
Mulokozi (1982:33) na Mulokozi na Sengo (1995) wanafafanua kwamba wimbo huu unadaiwa kuwa
ulikuwa unawakebehi watu wa Kilindini kwa kuwakaribisha Waarabu katika maeneo yao.
KUINGIA KWA UKOLONI NA ATHARI ZAKE KATIKA USHAIRI WA KISWAHILI
Kufikia nusu ya pili ya karne ya kumi na tisa ukoloni ulikuwa umeshashika mizizi katika bara la
Afrika, maeneo ya Waswahili yakiwemo. Ukoloni huu unatajwa kusababishwa na maendeleo makubwa
ya viwanda yaliyotokea huko Ulaya kuanzia karne ya kumi na sita na hivyo kusababisha mahitaji
makubwa ya mali ghafi kwa ajili ya viwanda, mahitaji makubwa ya vibarua wa kufanya kazi
60
viwandani, ongezeko kubwa la idadi ya watu na mahitaji makubwa ya soko la kuuzia bidhaa
zilizozalishwa viwandani. Kutokana na hayo, watu kutoka bara Ulaya walikuja Afrika kutafuta mali
ghafi, vibarua, sehemu za kuishi ili kupunguza ongezeko la watu Ulaya na masoko kwa bidhaa zao.
Ukoloni huu ulipitia hatua mbalimbali. Hatua kubwa ya ukoloni ni ile iliyofikiwa baada ya mkataba wa
Berlin mwaka 1884-1885. Wakoloni waliotawala maeneo ya Waswahili ni pamoja na Waarabu,
Wareno, Wadachi na Waingereza. Kwa kuwa tumeshagusia kuingia kwa Waarabu na Wareno na athari
zao katika ushairi wa Kiswahili katika sehemu zilizotangulia, hapa tutajikita zaidi katika ukoloni wa
Wadachi na Waingereza.
1. UKOLONI WA WAJERUMANI/WADACHI
Wakoloni wa mwanzo wanaofahamika zaidi ni Wajerumani ambao wanaitwa pia Wadachi. Ujio wa
wakoloni ulienda sambamba na vita vya upinzani toka kwa Waswahili. Mulokozi na Sengo (1995:77)
wanabainisha kwamba miongoni mwa vita vya upinzani vya Waswahili ni pamoja na Vita vya Witu (1890-94)
vilivyoongozwa na Fumo Bakari na baadaye Fumo Omari; Vita vya Kismayu (1892); Vita vya Takaunga (1895 -
96) vilivyoongozwa na Mazrui na Sheikh Mbaruku Rashid na Mbarak Rashid na; Vita vya Abushiri (1888 –
1889). Aidha, Mulokozi na Sengo (khj.) na Mulokozi (1996) wanaeleza kuwa mashairi mengi yahusuyo vita hivi
hayajakusanywa bado isipokuwa Utenzi wa Vita vya Wadachi Kutamalaki Mrima (Hemed Abdalla, 1960) na
Utenzi wa Vita vya Majimaji. Inaelezwa kuwa, Hemed Abdalla aliyetunga Utenzi wa Vita vya Wadachi
Kutamalaki Mrima alishiriki katika vita vya Abushiri vilivyozaa utenzi huo na utenzi wake unabainisha mtazamo
wa Waswahili juu ya vita hivyo. Zaidi ya vita vyote hivi, hatimaye ukoloni ulianza rasmi katika upwa wa Afrika
mashariki.
Ukoloni uliambatana na mambo mengi ikiwa ni pamoja na kuanza kutumika kwa hati za Kirumi katika
mashairi, ufunguzi wa shule zilizowaelimisha watu kuhusu ushairi, kuanzishwa kwa magazeti yaliyokuwa na
safu maalumu za ushairi na kadhalika. Washairi wengi wa wakati huu ni wale waliopata elimu katika shule za
kikoloni na pia washairi wengi waliokuja kuwa maarufu kama vile Mathias Mnyampala na Shaaban Robert
waliibuka kupitia utunzi wa mashairi magazetini.
2. UKOLONI WA WAINGEREZA
Ukoloni wa Waingereza ulianza baada ya Wajerumani kushindwa katika vita kuu vya kwanza vya
dunia na hivyo makoloni yake kugawanywa miongoni mwa mataifa yaliyoshinda vita. Moja ya mataifa
hayo ni Uingereza. Katika kipindi hiki shule ziliendelea kutoa elimu ya ushairi na pia magazeti
yaliongezeka (kulikuwa na magazeti kama vile Msimulizi, Pwani na Bara na Mambo Leo). Aidha, katika
kipindi hiki palishuhudiwa pia kupiga hatua katika taaluma ya uchapaji wa vitabu. Ushairi wa Kiswahili
ulipiga hatua kubwa katika kipindi hiki na ndipo sheria na kanuni za utunzi wa ushairi zilitungwa na
Amri Abedi mnamo mwaka1954 katika kitabu chake Sheria za Kutunga Mashairi na Diwani ya Amri.
Katika kitabu hicho, Amri Abedi anaona kuwa kuenea kwa vitabu na magazeti kumewafanya watu
wengi watake kutunga mashairi. Anadai kuwa mashairi mengi yanayotungwa, yametungwa bila ujuzi
wa kutosha, nayo yanaelekea kupunguza thamani ya mashairi ya Kiswahili mbele ya mashairi ya lugha
nyingine. Hivyo, anaona ni vema kueleza kanuni za kutunga mashairi ili kuwarejesha watungaji katika
mipaka inayotakiwa. Abedi anafasili shairi au utenzi kuwa ni wimbo. Kwa hiyo, kama shairi haliimbiki
halina maana. Pia anaelezea kuwa utenzi ni ushairi wenye mizani chache kuliko kumi na mbili (12),
ambao mara nyingi hauna vina vya kati katika mstari, bali kila ubeti una vina vya namna moja katika
mistari yake isipokuwa mstari wa mwisho katika kila ubeti ambao unaendelea na kina cha namna moja
kinachoitwa bahari. Anaendelea kudai kuwa utenzi wa mizani nane (8) huimbika vizuri. Lakini pia
inawezekana kuwa na tenzi zenye mizani kumi na moja (11) kama vile al- Inkishafi, na pia kuna zenye
mizani sita (6).
Katika andiko hilo, Amri Abedi anabainisha mambo makuu manne ambayo ni muhimu katika
ushairi wa Kiswahili. Mambo hayo ni vina, mizani, kituo na utoshelevu. Abedi anadai kwamba shairi la
Kiswahili halina budi kuwa na urari wa vina na mizani. Anasisitiza kwamba vina na mizani ndiyo uti
wa mgongo wa shairi lolote lile la Kiswahili. Zaidi ya urari wa vina na mizani, anasisitiza umuhimu wa
kituo ambacho anakieleza kuwa ni mstari wa mwisho wa kila ubeti. Huo huwa ama ni kiini cha habari
(haubadiliki) ama kimalizio (hubadilika). Kituo kinapokuwa kimalizio, basi kinabadilikabadilika
ambapo kina cha mwisho huenda kati na cha kati huenda mwisho na kadhalika. Jambo la mwisho
analolisisitiza ni utoshelevu ambapo anadai kwamba kila ubeti ujitosheleze kadiri iwezekanavyo: yaani
61
uwe na maana kamili na maana hiyo isingoje kukamilishwa na ubeti mwingine unaofuata. Mambo
mengine anayoyaeleza Amri Abedi ni kwamba:
i. Kazi iliyo ngumu katika kutunga shairi hasa kwa anayejifunza ni kupata vina vilivyo sawa na
vizuri, vitoavyo maana, vyenye maneno mbalimbali. Kina cha “ni” ni chepesi zaidi. Kupata vina
kwa haraka inabidi ujizoeze kusoma sana mashairi mazuri ya watu mbalimbali.
ii. Watunzi wa mashairi wasiige ovyo bali wakuze vipaji vyao kwa kuwa na shauku ya kutunga na
kusoma mashairi ya watu wengine.
iii. Tunga iwapo haja: tunga shairi kwa jambo linalokusakama sana ndipo mashairi yatapenya
moyo, la sivyo yatakuwa chapwa kama mchuzi wa jogoo.
iv. Tumia lugha nyepesi ukizungumzia mambo ya kawaida. Usitunge mambo ya kihuni bali yale
yawafaayo, yaelimishayo, yafikirishayo, yafurahishayo watu.
v. Tumia lugha ya kizamani (ya wazee) unapotaka kuzungumzia shairi zito la fikra, tumia methali
katika kituo na pia dokeza na mafumbo.
vi. Lugha inayotumiwa na wanawake pia ni safi; huchapusha shairi.
KUPATIKANA KWA UHURU NA HALI YA USHAIRI WA KISWAHILI
Katika wakati wote wa utawala wa wakoloni, Waswahili hawakuwa kimya, bali waliendeleza
mapambano yao ya kutaka kujikomboa na kurudisha heshima yao. Wapo waliotumia njia za amani,
wapo waliotumia vita na mbinu nyinginezo kadha wa kadha. Penye nia pana njia, hatimaye kuanzia
miaka ya 1960 nchi za Afrika Mashariki zikaanza kujipatia uhuru wake. Tanganyika ilipata uhuru wake
1961, Kenya 1962, Zanzibar 1964 na Uganda 1964. Katika kuelezea historia ya Kiswahili baada ya
uhuru, ni vema tukigawe kipindi hicho katika vipindi kadhaa vidogovidogo:
i). KIPINDI CHA UHURU NA AZIMIO LA ARUSHA
Kipindi hiki kinaanza mwaka 1961 na kuishia mwaka 1970. Katika kipindi hiki mashairi mengi
yalikuwa ya kushangilia uhuru na kuwapongeza wapigania uhuru kwa kazi nzito. Mashairi ya aina hiyo
yanaonekana katika mashairi marefu kama vile Utenzi wa Uhuru wa Tanganyika (1967) ulioandikwa na
Mwinyihatibu Mohamed Amiri; Utenzi wa Jamhuri ya Tanganyika (1967) ulioandikwa na Ramadhani
Mwaruka; Utenzi wa Uhuru wa Kenya (1972) ulioandikwa na Salim A. Kibao na Utenzi wa Jamhuri ya
Zanzibar.
Mwaka 1967 Azimio la Arusha lililoambatana na siasa ya ujamaa na kujitegemea lilitangazwa na
hivyo kuleta sura mpya ya ushairi wa Kiswahili. Mashairi ya kijamaa-yaliyosifia Azimio la Arusha na
siasa ya ujamaa na kujitegemea yaliibuka. Miongoni mwa mashairi hayo ni Mashairi ya Azimio la
Arusha (1971) yaliyohaririwa na Grant Kamenju na Farouk Topan. Pia fani/mtindo mpya wa ushairi wa
kimajibizano ulianzishwa ambao ulipewa jina ngonjera. Mfano mzuri wa ushairi huo wa kimajibizano
unaonekana katika Ngonjera za UKUTA za Mnyampala 1970. Ngonjera hizi zilitumiwa sana na
wanasiasa kueneza siasa ya ujamaa na kujitegemea. Hata hivyo, Mbaga katika makala yake iitwayo
“Ngonjera: Historia yake Simulizi hadi Andishi” iliyopo kwenye jarida la Kiswahili na. 67 anaeleza
kuwa fani hii ya ngonjera imekuwepo katika jamii mbalimbali hata kabla ya wakati huo. Dai hili la
Mbaga linathibitisha tu kuwa ushairi andishi wa Kiswahili unachimbuka katika ushairi simulizi wa
Kibantu uliokuwepo tangu kale. Hoja yetu hapa ni kuwa, hata kama ngonjera simulizi zimekuwepo kwa
muda mrefu ngonjera andishi zilianza kuonekana katika wakati huu. Ushairi mwingi wa wakati huu
ulikuwa wa kikasuku. Kasuku ni ndege mwenye tabia ya kuiga kila sauti anayoisikia bila kujua maana
yake na madhara yake. Hivyo, kusema mashairi ya kikasuku tunamaanisha kwamba mashairi
yaliyosifia kila jambo lililosemwa na wanasiasa bila kujiridhisha kufaa kwake.
ii). KIPINDI CHA VITA VYA KAGERA NA UGUMU WA MAISHA
Kipindi hiki kinaanzia mwishoni mwa miaka ya 1960 na kuendelea hadi mwaka 1980. Kipindi hiki
kilishuhudia mambo mengi ikiwa ni pamoja na vita kati ya mataifa ya Waswahili, Tanzania na Uganda,
vita vilivyojulikana kama vita vya Kagera. Kutokana na vita hivi, pakaibuka mashairi yaliyobeba dhana
hiyo ya vita vya Kagera. Mfano mzuri ni Utenzi wa Vita vya Kagera na Anguko la Idd Amini Dada
(1981) ulioandikwa na Henry Muhanika.
62
Katika kipindi hiki palianza kuibuka hali ya kukata tamaa miongoni mwa watu kutokana na
matamanio na matarajio yao baada ya uhuru kutotimizwa. Baada ya uhuru, watu waliamini kwamba
maisha yao yangekuwa mazuri zaidi na kungekuwa na neema zaidi lakini hali haikuwa hivyo. Hapa
ndipo ulipoibuka ushairi wa kihakiki ambao uliikosoa jamii. Ushairi wa kipindi hicho ulionesha hali
halisi ya jamii katika nyanja mbalimbali kama vile hali ya kisiasa, hususani hali ya uongozi mbaya,
ukiritimba, kujilimbikizia mali, uhujumu uchumi na kadhalika. Washairi pia walianza kutathmini upya
kuhusu Azimio la Arusha na siasa ya ujamaa na kujitegemea kama vilikuwa na maana yoyote. Hapa
ndipo palipoibuka mashairi kama Miaka Kumi Baada ya Azimio la Arusha (1977) yaliyohaririwa na
Abdilatif Abdalla. Mashairi hayo yanaonyesha jinsi hali ya kiuchumi na kijamii ilivyokuwa mbaya,
kwa mfano, yanaonyesha jinsi wananchi walivyokuwa wanapata tabu kupata mahitaji muhimu.
Mashairi mengine ya mkondo huu ni ya Kezilahabi (1974) Kichomi na (1988) Karibu Ndani; ya Kahigi
na Mulokozi (1976) Malenga wa Bara na ya Mohamed Seif Khatib (1988) Fungate ya Uhuru.
Waandishi hawa walipendekeza mbinu mbalimbali za kuondokana na matatizo hayo ikiwa ni
pamoja na kuwahimiza wananchi kuungana ili kutatua matatizo yao na kuchukua hatua. Aidha,
yalipendekeza pia viongozi kuwajibika ama kuwajibishwa ili kuepusha matatizo zaidi. Hali hiyo
inaonekana katika mashairi ya Fungate ya Uhuru (1988) na ya Mochiwa (1988) Mvumilivu Hula
Mbovu. Mochiwa anasisitiza kwamba huu si wakati wa wananchi kuwavumilia viongozi wasiofaa
maana mvumilivu hula mbovu. Kwa ujumla, watunzi hawa wanataka Ujenzi wa jamii mpya ambayo
itakuwa na haki, uchumi imara, jamii iliyojikomboa kiutamaduni, yenye watu wazalendo, yenye umoja,
usawa na utu na ambayo ina viongozi bora. Kwa mfano, Kezilahabi katika kitabu cha Karibu Ndani
shairi lake la kwanza kabisa liitwalo “Chai ya Jioni” anabainisha maovu haya ya viongozi. Katika shairi
hili tunaona kuwa mshairi anaonyesha jinsi viongozi wanavyojisahau wakiwa madarakani.
Anawakumbusha kuwa wanapoona mambo yanaenda wajue na muda wa uongozi wao unaisha pia.
Hivyo, anawaasa kuwa ni vema wahakikishe kuwa kabla hawajaondoka madarakani wanafanya mambo
yanayokubalika katika jamii. Mashairi mengine ya mkondo huu katika diwani hii ni pamoja na shairi la
pili kitabuni “Mkesha,” la tatu “Matumaini” na mengineyo mengi. Katika shairi la “Mkesha”
mwandishi anabainisha kwamba wakati watu wanateseka wakisubiri maendeleo viongozi wanaishi
maisha ya kifahari; katika shairi la “Matumaini” mwandishi anabainisha jinsi Waafrika waliokuwa na
matumaini makubwa wakati nchi zao zinapata uhuru kuwa viongozi wa Kiafrika watawaletea
maendeleo, walivyokata tamaa na kukosa matumaini kabisa. Kwa ujumla, mshairi huyu amesawiri sana
hali ya kukata tamaa iliyokuwepo wakati huo. Hata hivyo, izingatiwe kuwa mashairi haya yanaweza
kuchambuliwa kwa namna nyingine na kupewa dhamira nyingine. Kwa mfano, Senkoro anaona kuwa
shairi la “Chai ya Jioni” linahusu mapenzi na wala si siasa kama tunavyodai hapa. Mtazamo huu wa
Senkoro unatuonyesha kuwa kazi ya fasihi huweza kuhakikiwa kwa namna tofautitofauti na kubainika
kuwa na dhamira tofautitofauti kulingana na mhakiki.
Kwa upande wa mashairi yanayohimiza ukombozi wa kiutamaduni yanaonekana katika vitabu
mbalimbali. Kwa mfano, katika Diwani ya Akilimali (1963) cha Akilimali Snow-White na Ngonjera za
Ukuta cha Mathias Mnyampala (1970) mashairi ya aina hii ni mengi sana. Katika Diwani ya Akilimali
tunaona katika shairi la “Kila Mdharau Chake” ambapo msanii anasisitiza watu kudhathamini vya
kwao, ikiwa ni pamoja na utamaduni wao. Aidha, katika Ngonjera za Ukuta msanii ameweka safu
maalumu yenye mashairi yanayohusu elimu na utamaduni. Katika safu hii, ametunga mashairi mengi
ambayo yanahimiza ukombozi wa kiutamaduni. Miongoni mwa mashairi hayo ni pamoja na
“Utamaduni Kitu Gani ” na “Kiingereza Lugha Nzuri?” Katika shairi la “Utamaduni Kitu Gani”
msanii anaielimisha jamii juu ya dhana nzima ya utamaduni wa Kiafrika na kuwataka wauheshimu
utamaduni wao maana ni bora. Katika shairi la “Kiingereza Lugha Nzuri” msanii anahoji uzuri wa
lugha ya Kiingereza. Katika shairi hilo, anawakejeli wanajamii wanaoona kwamba kujua Kiingereza
ndiyo usomi na ujuzi wa mambo na kuwakumbusha kuwa Kiswahili ni lugha inayojitosheleza na lugha
ya usomi pia. Kwa kusema hivyo, msanii alikusudia kuikomboa jamii kutokana na ukoloni wa
kiutamaduni.
KUIBUKA KWA USHAIRI WA KISASA NA MABADILIKO KATIKA USHAIRI
Tumeshuhudia kuwa kumekuwa na mabadiliko katika maudhui ya ushairi wa Kiswahili katika kila
kipindi tulichokieleza. Mbali na mabadiliko hayo ya kimaudhui tuliyoyaeleza katika vipindi
63
mbalimbali, katika kipindi hiki pia palishuhudiwa mabadiliko ya kifani yaliyotokana na kuibuka kwa
ushairi wa kisasa. Mabadiliko haya ndiyo yanayoitwa majaribio katika ushairi. Majaribio yamekuwapo
katika tanzu mbalimbali za fasihi pia. Mabadiliko katika ushairi wa Kiswahili yalianza tangu mwishoni
mwa miaka ya 1960 lakini yakashika kasi sana na kuwa bayana zaidi katika kipindi hiki. Kufikia miaka
ya 1970 kulikuwa na majaribio ya wazi ya kutunga mashairi yasiyozingatia kanuni za awali
zilizopendekezwa na akina Amri Abedi. Mashairi haya yanaonekana kwa wingi katika kazi za E.
Kezilahabi, K. K. Kahigi na M. M. Mulokozi, D.P.B Massamba, S.A Mohamed, M.S. Khatibu,
Mochiwa, Kithaka wa Mberia, F.E.M.K. Senkoro na wengineo. Majaribio haya yalipingwa na washairi
wengine wa kijadi na hapo sasa kile kinachoitwa katika fasihi ya Kiswahili mgogoro wa ushairi
kikaibuka. Wanaujadi wanaojulikana zaidi ni Andanenga, M. Mnyampala, J. Mayoka, S. Robert, Amri
Abedi, Said Karama, Abdilatif Abdala, Ahmad Nassir, Chiraghdin na S. Kandoro. Wanaujadi
wakayaita mashairi ya kisasa kuwa masivina, mapingiti na majina mengine yasiyofaa wakiwa katika
harakati za kuyadhalilisha. Mgogoro huu unafafanuliwa kwa kina na Jumanne Mayoka katika kitabu
chake kiitwacho Mgogoro wa Ushairi na Diwani ya Mayoka.
DHANA YA MGOGORO WA USHAIRI NA HALI ILIVYOKUWA
Mgogoro ni hali ya kutokukubaliana au hali ya mvutano baina ya watu wawili au makundi
mawili ya watu. Tunapozungumzia mgogoro wa ushairi tunamaanisha ile hali ya kutokukubaliana na
mvutano baina ya makundi mawili ya washairi na wanafasihi juu ya dhana ya ushairi wa Kiswahili.
Makundi haya yaliyokuwa yanakinzana ni kundi la washairi wakongwe, wanamapokeo, na kundi la
washairi wapya, wanausasa. Wanamapokeo huitwa pia wana ujadi na wanausasa huitwa pia
wanamamboleo. Makundi haya mawili yalihusisha washairi wenyewe pamoja na wataalamu wengine
wa fasihi ambao si washairi. Kila kundi lilikuwa na mtazamo wake juu ya dhana ya ushairi na kuamini
kuwa mtazamo wao ni bora zaidi na hivyo kutokuwa tayari kukubali kubadilika au kuukubali mtazamo
wa kundi lingine.
Mgogoro huu ulijibainisha katika midahalo, vyombo vya habari, mashairi na hata katika
maandiko mengine yasiyokuwa ya kishairi. Kwa mfano, katika midahalo iliyofanyika katika
makongamano mbalimbali mikinzano baina ya makundi hayo ilibainika waziwazi. Mingi ya midahalo
hiyo iliitishwa na idara ya Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Pia kupitia vyombo vya habari
mikinzano hiyo ilijibainisha ambapo washairi hawa walibishana juu ya dhana hasa ya ushairi wa
Kiswahili. Mashairi mengi yaliyoandikwa katika vyombo vya habari vya wakati huo na hasa magazeti
yalikuwa na majibizano baina ya wafuasi wa makundi haya. Aidha, majibizano hayo yalionekana hata
katika mashairi waliyoyatunga vitabuni. Mfano mzuri wa mashairi ya aina hiyo tunayaona katika
Diwani ya Andanenga, Diwani ya Karibu Ndani, Diwani ya Amri miongoni mwa nyingi nyinginezo.
Diwani ya Karibu Ndani ina shairi linalobeba anwani ya diwani hiyo liitwalo “Karibu Ndani” ambalo
linasawiri mgogoro huo wa ushairi. Katika shairi hilo, Kezilahabi anawaeleza wanamapokeo kuwa
ushairi wao unafikia mwisho na aina mpya ya ushairi, ushairi wa kisasa, inashika hatamu. Hili
linabainika katika ubeti wa kwanza anaposema:
Washairi wa mapokeo, sasa wacheza lalasalama
Katika mionzi hafifu, ya jua machweoni
Na mahadhi yagaagaa, juu ya bahari ya utenzi
Yameshindwa chini kuzama, kwenye kina cha urazini
Nao wahenga vibandani, nje tena hawatoki
Hakuna tena ngoma, ya kugeeana kani
Na ushairi umehama, umerudi peponi
Lakini majani makavu, sasa hayatingishiki
Nayo madirisha ya nyumba, imara yamefungwa
Waliomo ndani wahofu, hasira ya mizimu
Aidha, katika ubeti wa mwisho wa shairi hilo, anaufananisha ushairi wa kimapokeo na kibanda
kikuukuu ambacho kinakaribia kuanguka. Hii ina maana kuwa, anauona ushairi huo kuwa umefikia
mwisho na aina mpya ya ushairi, ushairi wa kisasa, unaonekana kutawala. Tazama anasema katika ubeti
huu:
Ni kibanda kikuukuu, kuanguka kimekaribia
Mhimili wake mmoja, umeanza kukatika
64
Nao mchwa walialia, paa si paa tena
Karibu na huu mhimili, katikati ya kibanda
Kuna kigoda kikubwa, ngozi ya chui pambole
Mbele yake pana moto, vijinga vyake mifupa
Mbali na kujibizana kupitia mashairi kwenye diwani zao, walijibizana pia kupitia maandiko
mengine yasiyokuwa ya kishairi. Majibizano ya aina hii yalioneka pia katika tangulizi za vitabu vyao
vya mashairi. Kwa mfano, Abedi (1954) katika dibaji yake anawashambulia washairi wa kisasa na
kuwaeleza kuwa hawajui kutunga mashairi na wanashusha thamani ya ushairi wa Kiswahili. Abedi
anadai kuwa kuenea kwa vitabu (elimu) na magazeti ndicho chanzo cha kuingia kwa fani hiyo mpya,
mashairi ya kisasa, “isiyofaa.” Hebu turejee katika maneno yake anaposema:
Siku hizi kuenea kwa vitabu na magazeti kumewafanya watu wengi watake kutunga mashairi. Mengi mno
katika mashairi yanayotungwa, yametungwa bila ujuzi wa kutosha, nayo yaelekea kupunguza thamani ya
mashairi ya Kiswahili mbele ya mashairi ya lugha nyinginezo…
Chiraghdin (1980:1) naye anatoa maelezo yanayofanana na Abedi (1954). Yeye anasema kuwa
washairi wa kisasa wanauona ushairi kuwa ni mgumu na hivyo hawawezi kutunga mashairi.
Anaendelea kusema kuwa, kwa kuwa hawawezi kutunga mashairi, wanatunga vitu vingine na kudai ni
aina mpya ya ushairi. Kwa maelezo haya Chiraghdin anaonekana wazi hakubaliani na wanausasa na
anauona kuwa ushairi wao si ushairi wa Kiswahili bali wa Kizungu, hasa wa Kiingereza. Hivyo,
Chiraghdin kama ilivyokuwa kwa Abedi (1954) anaonekana kuulaumu ujio wa wakoloni wa Kiingereza
pamoja na elimu kuwa ndiyo chanzo cha “kuharibiwa” kwa ushairi wa Kiswahili. Tazama kwa maneno
yake anaposema:
Hii leo ushairi umekuwa ni taaluma iliyoenezwa tangu mashule hata vyuo vikuu. Lakini mpaka Leo
wanafunzi husikiwa wakilalamika kuwa somo hili ni gumu kwao. Tuseme labda hata hao waliofunzwa
Kiswahili wakakishikilia na kuendelea nacho mpaka daraja za utaalamu wa lugha hii na adabu yake,
wameuona ushairi wa Kiswahili kuwa ni mgumu mno hata wakaona ni heri waukimbie na wakajizibezibe
katika kwapa za kudai kuwa wanauendeleza ushairi huu katika mkondo mpya. Maana kuvyaza kwao si
zaidi ya kufuata vipengee vya Kizungu vya kutunga mashairi kwa njia za nathari, na hali humohumo katika
fasihi za Kizungu, Kiingereza mathalan….
Kwa ujumla, tuseme kuwa, washairi wa wakati huo walikuwa na mgogoro mkubwa kuhusiana
na dhana ya ushairi, ushairi wa Kiswahili ni upi hasa? Ili kupata mwangaza zaidi kuhusiana na mgogoro
huu ni vema tuchambue mawazo ya kila kundi:
MADAI YA WANAMAPOKEO NA WANAUSASA KUHUSU USHAIRI WA KISWAHILI
Dai la msingi la wanamapokeo ni kuwa urari wa vina na mizani ni roho na uti wa mgongo wa ushari
wa Kiswahili. Wengi kati ya wanamapokeo hawakiri kuwa kinachotungwa na wanausasa ni mashairi
(taz. Utangulizi wa Chiraghdin, 1980). Hawa wanauchukulia ushairi wa kisasa kuwa si ushairi bali ni
insha au nathari tu. Kwa upande wa wale wachache wanaokiri kuwa ni ushairi, wanauona kuwa ni
ushairi usio bora na ushairi wa kigeni. Wanauchukulia kuwa ni ushairi uliotokana na kuiga ushairi wa
Kiingereza (taz. Dibaji ya Abedi, 1954). Kwa ujumla, wanamapokeo wanauchukulia ushairi wa kisasa
kuwa ni aina ya uandishi iliyotokana na elimu na ukoloni. Kwa hiyo, tuseme kuwa elimu inaonekana
kwao kuwa na mchango hasi katika maendeleo ya ushairi wa Kiswahili. Aidha, wanawachukulia
wanausasa kuwa ni watu walioshindwa kutunga mashairi ilhali wanatamani kuwa watunzi wa mashairi.
Matokeo yake ni kutunga vitu visivyokuwa mashairi na kudai kuwa ni mashairi ya kisasa jambo ambalo
wao, wanamapokeo hawalikubali.
Kwa upande wao wanausasa wanawalaumu wanamapokeo kwa kuzuia maendeleo ya ushairi wa
Kiswahili kwa kutoutambua ushairi “mpya” ulioibuka. Wanausasa wanabainisha kwamba ushairi
simulizi wa Kibantu, ambao ndiyo chimbuko la ushairi wa Kiswahili, kama wanavyokiri pia
wanamapokeo, haukufuata kanuni za urari wa vina na mizani. Kanuni ya urari wa vina na mizani kama
uti wa mgongo wa ushairi wa Kiswahili wanaiona kuwa ni kanuni iliyotokana na athari za Waarabu
katika ushairi huo na wala si kanuni ya jadi ya ushairi wa Kiswahili. Hivyo, wanausasa nao, kama
ilivyokuwa kwa wanaujadi, wanalaumu ujio wa wageni kama chimbuko la athari mbaya kwa ushairi wa
65
Kiswahili. Wanausasa wanaenda mbali na kukazia kwamba shairi liamuliwe na kufungamana na
mawazo, mtiririko wa hisia na makusudio ya mtunzi na si mbinu za kifani. Hoja ya msingi ya kusisitiza
hapa ni kuwa, wanausasa hawapingi uhalali wa urari wa vina na mizani katika ushairi wa Kiswahili,
bali wanataka aina “mpya” ya ushairi, ushairi usiofuata urari wa vina na mizani utambuliwe kuwa ni
ushairi wa Kiswahili pia. Kwa hiyo, wanausasa wanatambua mashairi yenye urari wa vina na mizani
kuwa ni mashairi ya Kiswahili lakini hawaoni kuwa huo ndiyo uti wa mgongo wa ushairi wa Kiswahili.
Mashairi ya Kiswahili yanaweza pia kutokuwa na urari wa vina na mizani.
(iii) USHAIRI WA KISWAHILI KIPINDI CHA UTANDAWAZI
Kwa dhana pana, kipindi hiki kinadaiwa kuanza zamani sana tangu ujio wa wakoloni waliovuka
mipaka yao na kuja Afrika. Hata hivyo, maelezo yetu yataelemea katika dhana finyu ambapo
utandawazi unaonekana kuanza miaka ya 1980 na kuendelea hadi sasa. Kipindi hiki kimeshuhudia
maingiliano makubwa baina ya mataifa mbalimbali ulimwenguni na dunia imekuwa kama kijiji kimoja.
Kimekuwa ni kipindi cha kubadilishana na kuathiriana kwa tamaduni baina ya mataifa ulimwenguni.
Maathiriano hayo yamejidhihirisha hata katika fani ya ushairi tunayoishughulikia. Hivyo, kipindi hiki
kimeshuhudia kunawiri kwa ushairi wenye athari kubwa ya kigeni. Kutokana na hali hiyo, ushairi wa
kisasa, ambao hapo awali ulipingwa sana na kuonekana wa kigeni, ukakubalika rasmi kama ushairi wa
Kiswahili, japo bado wapo wachache ambao hawautambui. Aidha, kipindi hiki kimeshuhudia kuingia
kwa aina mpya ya mashairi yanayojitokeza katika miziki mbalimbali kama vile Bongo Fleva, Taarabu
ya Mipasho na muziki wa Dansi. Ushairi huu unasemwa kuwa na athari kubwa ya ushairi wa kigeni.
Athari ya ushairi wa kigeni katika ushairi wa Bongo Fleva inabainishwa vizuri na Omari (2009) na
Samwel (2012a) miongoni mwa wengineo. Ushairi ulioibuka katika kipindi hiki una sifa kuu mbili:
kwanza, umejaa majigambo na pili, unazingatia kanuni za urari wa vina na mizani. Japo yapo pia
mashairi yasiyozingatia urari wa vina na mizani, suala la shairi kuwa na vina linaonekana ni suala
muhimu na ambalo washairi wanajisifia kwalo. Hii ni kusema kuwa, mashairi yasiyokuwa na urari wa
vina na mizani yanapungua thamani yake na kushusha hadhi ya msanii husika. Swali linaweza kuwa je,
msisitizo katika suala la urari wa vina na mizani katika ushairi wa kisasa ni aina mpya au kurejea upya
kwa mgogoro wa ushairi uliokuwapo miaka ya 1960 na 1970? Katika sura inayofuata tutachambua kwa
kina aina hii mpya ya ushairi wa Kiswahili. Kwa kuwa si rahisi kupitia aina zote za ushairi wa wakati
huu, tutajikita katika ushairi wa Bongo Fleva.
66
SURA YA TANO
USHAIRI WA BONGO FLEVA
Dhana ya Muziki wa Bongo Fleva
Ushairi wa Bongo Fleva ni ule unaobebwa na muziki wa Bongo Fleva. Hivyo, ili kuuelewa
ushairi wa Bongo Fleva, hatuna budi kuuelewa muziki wa Bongo Fleva kwa ujumla. Muziki wa Bongo
Fleva umepewa majina mengi sana miongoni mwa wanazuoni na wadau wa muziki huo. Majina hayo
ni pamoja na Bongo Flava na muziki wa kizazi kipya (Suriano 2006:1; 2007:207 na Omari 2009:5;
Samwel, 2012a). Muziki huu unaitwa wa kizazi kipya ikiwa na maana kwamba ni muziki unaopendwa
sana na vijana ambao ndio hasa huonekana kuwa kizazi kipya au kizazi cha leo. Dhana ya muziki wa
Bongo Fleva imekuwa na mkanganyiko mkubwa hasa katika jitihada za kuitofautisha na dhana ya Hip
hop (Suriano, 2006; Omari, 2009; Samwel, 2009; Samwel, 2012a). Wapo wanaouona muziki huu wa
Bongo Fleva kuwa ni aina mojawapo ya muziki wa Hip hop wa Kitanzania (Suriano, 2006:1 na
2007:207). Aidha http://spotistarehe.wordpress.com ikiwa na mtazamo kama huo inaeleza kwamba:
Muziki wa Bongo Flava unatofautiana na Genge (wa Kenya) kwani wao ni Commercial (wa
kibiashara) zaidi wakilenga kuchezesha (kuwaburudisha) watu na wakati mwingine hupati maana
kwenye wimbo mzima hata wakihojiwa wanashindwa kusema muziki ulilenga nini. Tofauti na muziki
wetu (Bongo Fleva) ambao unalenga kutoa ujumbe na kuburudisha na ndio maana utaona kila mtu
anajitahidi kumshirikisha mtu mwingine kwa ajili ya kuleta ladha tofauti ambayo pia inapatikana
kwenye makundi, na utaona nyimbo nyingi ambazo mtu amemshirikisha mwingine zimewatoa sana
(Ufafanuzi wetu).
Maelezo haya yanatudokeza kwamba Hip hop ni kundi kubwa la muziki duniani (universal)
ambapo kila nchi ina mtindo wake, Kenya-Genge, Afrika ya Kusini-Kwaito, Tanzania-Bongo Fleva na
kadhalika.
Aidha, wapo wanaoutofautisha muziki wa Bongo Fleva na Hip hop kwa vigezo vya midundo na
mapigo. Kwa mfano, Ramadhani Mponjika, katika mahojiano yetu, alitueleza kwamba muziki wa
Bongo Fleva ni “kapu” ambamo ndani yake kuna miziki ya aina mbalimbali ikiwemo zouk, rhumba,
reggae, RnB na kadhalika. Anadai kwamba mapigo ya muziki huu huwa ni mepesi, hakuna midundo
mizito (yaani bass). Akiielezea Hip hop anasema ni muziki unaofanana kote duniani na una mapigo
mazito (heavy beats) yanayoambatana na bass. Mawazo kama haya yametolewa pia na Suriano (2006
na 2007) na Omari (2009).
Mtazamo mwingine ni ule unaouona muziki wa Bongo Fleva kuwa ni muziki usio na nguzo
maalum. Muziki huu ni tofauti na muziki wa Hip hop ambao una nguzo zinazofahamika duniani kote.
Nguzo hizo ni pamoja na michoro inayowakilisha maudhui mbalimbali (graffiti), upangaji wa muziki
(deejaying), uchezaji wa kujinyonganyonga (breakdancing), mshereheshaji (MC) na ughani (rap)
(Suriano, 2006, 2007; Omari, 2009). Msanii Happiness Thadei (Sister P) anazitaja nguzo hizo katika
wimbo wake uitwao “MaDJ.” Hebu tuangalie ubeti huu:
1. Nazo nguzo tano za Hip hop weka akilini
2. Kwanza naanza na DJs kuweni makini
3. Pili MC jiheshimu wacha mapepe
4. Usilete mambo ya ajabu kuwafanya watu wacheke
5. Nayo ya tatu tungo zako sharti ujumbe zibebe
6. Zielimishe jamii ili utakacho waelewe
7. Tungo zako zikubalike zitumike hata kwenye mashule
8. Breakdance nayo mtindo wetu wakati ule
9. Hili ndilo darasa nakupa Hip hop shule
10. Hip hop nguzo ya tano michoro
Kundi la mwisho katika mkanganyiko huu ni la watu ambao wanauona muziki wa Bongo Fleva na
Hip hop kuwa ni kitu kimoja. Mtazamo huu unaona hakuna tofauti yoyote kati ya miziki hiyo miwili na
hivyo mwanamuziki fulani anaweza kutambuliwa kama mwanamuziki wa Bongo Fleva na pia anaweza
kutambuliwa kama mwanamuziki wa Hip hop. Mtazamo huu unaonekana hata miongoni mwa wasanii
wenyewe. Hili linathibitishwa na Samwel (2012a) ambaye anasema alipojaribu kuwauliza baadhi ya
wasanii ili kujua mtazamo wao juu ya wasanii fulanifulani kama ni wasanii wa Bongo Fleva au Hip hop
67
alipata majibu ya kutatanisha. Anatoa mfano kuwa, alipouliza kuhusu Joseph Haule (Profesa Jay/Prof.
Jay) na Selemani Msindi (Afande Sele), wengine walimwambia hao ni wanamuziki wa Bongo Fleva
wakati wengine walimwambia ni wasanii wa Hip hop. Samwel (khj.) anafafanua kuwa hii inatupa picha
kwamba muziki wa Bongo Fleva na Hip hop unaonekana kuwa kitu kimoja au kuna kutoelewa upi hasa
mpaka wa miziki hiyo.
Ili kuepuka mkanganyiko usio wa lazima, andiko hili halina lengo la kujiingiza katika mjadala huo
na hivyo katika andiko letu tutachukua mtazamo wa Samwel (2012a) ambaye muziki wa Bongo Fleva
anauita pia muziki wa Hip hop au wa kizazi kipya. Hivyo, katika andiko hili dhana za Bongo Fleva, Hip
hop na muziki wa kizazi kipya zitatumika kama visawe.
1. MAUDHUI YA USHAIRI WA BONGO FLEVA
Ushairi wa Bongo Fleva umebeba maudhui ya siasa, uchumi, utamaduni na maudhui ya kijamii.
Maudhui hayo, kwa hiyo, huhusisha masuala kama utawala, migogoro, kazi na umuhimu wake, dini,
mapenzi na ndoa na kadhalika. Mwanjoka (2011:34), akibainisha utokeaji wa maudhui haya katika
ushairi wa Bongo Fleva, anaeleza kwamba, “ujumbe katika nyimbo nyingi (za Bongo Fleva) za leo
umeegemea sana kwenye mapenzi, siasa, malumbano…” (Ufafanuzi wetu). Hapa tunaona anabainisha
kuwa ushairi wa Bongo Fleva unabeba maudhui ya kiutamaduni na kijamii (mapenzi) na pia kisiasa.
Aidha, Samwel (2012a) anaongezea kuwa ushairi huo huweza pia kubeba maudhui ya kiuchumi. Katika
sehemu ifuatayo tutachambua kwa kina maudhui haya na kuonyesha yanavyojibainisha.
Kwa kuanza na maudhui ya kisiasa tunaona kuwa ushairi wa Bongo Fleva umebeba maudhui
mengi yanayohusiana na siasa. Miongoni mwa maudhui ya mkondo wa kisiasa yanayoonekana katika
ushairi wa Bongo Fleva ni pamoja na maudhui yanayohusu utawala na uongozi.
(a) Maudhui ya Uongozi na Utawala
Uongozi na utawala ni mojawapo ya maudhui yabebwayo na ushairi wa Bongo Fleva. Uongozi
ni moja ya mambo ya msingi katika siasa za jamii yoyote ile. Ushairi wa Bongo Fleva umesawiri sana
maudhui ya kisiasa. Katika mashairi ya mkondo huu, wasanii wa Bongo Fleva wanaimba kuhusu wao
kuwa watawala na/au viongozi. Wasanii wanajipachika au kupachikwa majina kama rais, mfalme,
chifu, mheshimiwa na kadhalika ambayo kimsingi ni majina yanayotumiwa katika medani ya siasa.
Mfano mzuri wa mashairi ya Bongo Fleva yanayohusu siasa ni mashairi yanayoonekana katika
wimbo wa “Muhogo Andazi” wa msanii Rahim Nanji (p.h.k Bob Junior) ambapo msanii anaimba
akijieleza kwamba yeye ndiye rais wa masharobaro. Anafafanua kwamba masharobaro ni watu wasafi
na watanashati. Tunaweza kuthibitisha hili katika kibwagizo hiki anaposema:
1. Mimi ndiye Mr. Chocolate
2. Rais wa masharobaro dunia nzima
3. Ninaposema sharobaro
4. Namaanisha kijana msafi, mtanashati
5. Ninaposema mtoto wa Kitanzania
6. Namaanisha vidole gumba miamia…
7. Ninaposema rais wa wasafi
8. Namaanisha rais wa watanishati
9. Ninaposema sharobaro
10. Namaanisha kijana msafi, mtanashati
Chanzo: Bob Junior (2011), “Muhogo Andazi”
(b) Maudhui ya Kiuchumi
Zaidi ya maudhui yahusuyo siasa, ushairi wa Bongo Fleva umebeba pia maudhui ya kiuchumi.
Ushairi wa Bongo Fleva unaobeba maudhui ya kiuchumi umegawanyika katika makundi makuu
mawili, ushairi unaobeba maudhui ya ushindani na ushairi unaobeba maudhui ya biashara. Tuanze
kuangalia majigambo ya ushindani.
(i) Maudhui ya Ushindani
Ushairi wa muziki wa Bongo Fleva umebeba maudhui ya ushindani. Omari (2009:143) anaeleza
kwamba mashindano ni sifa moja kubwa inayoutambulisha muziki wa kizazi kipya. Mashindano haya
anayaeleza kwamba yamekuwa miongoni mwa wasanii wenyewe, watayarishaji wa muziki,
wasambazaji na hata wadhamini. Anaendelea kufafanua kuwa, mashindano haya yanahusisha kuibiana
68
mashairi, mapigo au mawazo yanayobebwa na nyimbo, kuhama kutoka kundi moja la muziki huu hadi
lingine, kutumia nyimbo za msanii mwingine na hata mapigano halisi baina yao. Ushindani huu na
migogoro inayoambatana nao vimepewa jina la bifu (Omari, 2009:78). Ushindani unaonekana katika
maneno ya wasanii wanapohojiwa na vyombo mbalimbali vya habari na hata katika mashairi yao.
Omari (2009:79) anabainisha kwamba miongoni mwa mabifu katika muziki wa Bongo Fleva
ambayo yaliwahi kufahamika ni pamoja na bifu baina ya Godfrey Tumaini (Dudu Baya) na Lucas
Mkenda (Mr. Nice); Filipo Nyandindi (O-Ten) na Selemani Msindi (Afande Sele); East Coast Team na
TMK Wanaume Family na bifu kati ya Happiness Thadei (Sister P) na Zainabu Lupangule (Zay B).
Zaidi ya mabifu hayo anayoyataja Omari, mabifu mengine ambayo yaliwahi kubainika ni baina ya
TMK Wanaume Family na TMK wanaume Halisi; Joseph Haule (Prof. Jay) na Selemani Msindi
(Afande Sele); Banana Zoro na Hafsa Kazinja; Naseeb Abdul (Diamond) na Mwingereza Athmani
Mwingereza (Tanzanite) na Naseeb Abdul (Diamond) na Raheem Nanji Rummy Rummy (Bob Junior).
(ii) Maudhui ya Kazi
Aina nyingine ya maudhui ya kiuchumi ya ushairi wa Bongo Fleva ni maudhui ya kazi. Ushairi
wa Bongo Fleva umebeba maudhui ya kazi za aina mbalimbali. Katika muziki wa Bongo Fleva wasanii
wanaelezea juu ya umuhimu wa kufanya kazi na faida zake. Mfano mzuri wa maudhui ya mkondo huu
unaonekana katika wimbo wa Mr. 2 “Mchakamchaka:”
1. Anha baada ya dhiki faraja
2. Nimeamini mambo mema
3. Ni kwa yule anayengoja
4. Na wa mbili havai moja anha anha
5. Sasa ni mwendo wa dolali9
6. Ndani ya akaunti mtoni utadhani mtoto wa Balali
7. Sema vijisenti vyangu ni vya halali
8. Bongo mchaka mchaka tu
9. Mafisadi hawalali
10. Nina uhuru wa kusema
11. Na nitasema chochote ntakachoona kinafaa mimi kusema
12. Na nnakuja na falsafa za Obama
13. Tunatakiwa kuchange
14. Tusipochange maisha bora kwetu ndoto kama muafaka wa Zenji anha
15. Wacha niendeleze dozi
16. Maana leo kama balozi
17. Kama kazi ni kazi hakuna ubitozi
18. Na ni upuuzi kusema gemu haliuzi
19. Wakati we unangoja kuuza tepu tu na CD
20. Sisi tunauza mpaka jezi
21. Ni kwa sababu tuna CV
22. Na huu ndo mchakamchaka tunaoutaka
23. Na anha anha hakuna kuchoka
Chanzo: Mr. 2 (2009), Veto
Hapa msanii anaonesha umuhimu wa kazi ambapo anaeleza kwamba yeye kazi ya muziki inamwingizia
fedha nyingi kama “mtoto wa Balali.” Daudi Balali alikuwa gavana wa Benki kuu ya Tanzania na
alifariki mwaka 2008 huko Marekani alikoenda kutibiwa.10Gavana wa Benki huaminika kuwa na fedha
nyingi sana na hivyo hata watoto wake hunufaika na fedha hizo. Kwa hiyo, msanii hapa anaeleza
kwamba muziki unamwingizia fedha nyingi sawa na anazoingiza gavana wa Benki Kuu ya Tanzania.
Aidha, katika mstari wa 17 msanii anasisitiza kazi ni kazi mradi mkono uende kinywani na pia kazi
yoyote lazima ifanywe kwa bidii.
(c) Maudhui ya Kijamii katika Ushairi wa Bongo Fleva
9 Dolali ni msimu unaotumika kumaanisha dola (za Kimarekani).
10 Taarifa hii imesomwa toka katika (http://bongocelebrity.com/2007/12/21/gavana-balali-ajiuzulu) tarehe 24/08/2011
69
Katika uchambuzi wa maudhui kijamii tunaangalia, zaidi ya mambo mengine, mahusiano miongoni
mwa wanajamii. Hivyo, aina kuu ya maudhui ya kijamii tutakayoyachambua hapa ni maudhui ya
mapenzi.
(i) Mapenzi
Mapenzi ni maudhui mengine yanayoonekana katika ushairi wa Bongo Fleva. Mapenzi ndiyo
maudhui yaliyopata umaarufu zaidi katika ushairi wa Bongo Fleva. Mwanjoka (2011:110) akifafanua
mapenzi katika Bongo Fleva, anaeleza kwamba:
Ni ukweli mapenzi huchukua sehemu kubwa ya maisha ya mwanadamu. Na imeandikwa hata
kwenye vitabu vya dini kwamba, (kuna hatua tatu muhimu), moja kuzaliwa, pili mapenzi, tatu ni
kifo. Na vyote hivyo havikwepeki ni lazima mwanadamu avipitie endapo atazaliwa na kuishi
miaka au muda fulani hadi kuja kujitambua. Katika muziki wa kizazi kipya (Bongo Fleva) zaidi ya
asilimia hamsini ni nyimbo zinazohusu mapenzi. Na asilimia zinazobaki ni ujumbe mchanganyiko
kama vile siasa na uchumi, majigambo, majibizano, starehe na maisha magumu ya jamii nzima ya
Mtanzania yanayozungumzwa kila kukicha.
Baadhi ya mambo ya mapenzi yanayosawiriwa ni pamoja na kujisifia kuwa na mume/mke bora au
mzuri, kuelezea ujuzi wa kupenda au kuelezea jinsi msanii anavyopendwa na wanawake. Vilevile
maudhui ya mapenzi huweza kuhusu kuelezea jinsi msanii alivyo na maumbile ya siri makubwa (na
hasa wanaume) au anavyojua kumridhisha mwenzi wake kimahaba, anavyochukua wake au wapenzi
wa watu wengine na kadhalika. Mfano wa ushairi wa mapenzi tunauona katika wimbo wa Sugu (Mr. 2)
uitwao “Moto Chini” kama tulivyounukuu hapa chini. Katika wimbo huo msanii anaeleza kwamba ana
mafanikio makubwa katika maisha kutokana na muziki anaoupiga na hivyo anachukua hadi wanawake
(maplayer) wa wenzake (mstari wa 13-14). Msanii anaendelea kudai kuwa anapendwa na wanawake
kutokana na umaarufu na mafanikio yake. Tazama wimbo huo:
1. Nimeshatoa ngoma UK sasa narudi tena
2. Nairobi na Kampala bado nawakilisha kwa sana
3. Maneno bado ni Yes
4. Naona kama hakuna noma
5. Sasa mechi ni international
6. Sugu ni chama kubwa kama Arsenal
7. Bado nipo dimbani
8. Na maiki ipo mkononi
9. Labda huku nilipo nifuateni
10. Maana inaonekana nitachelewa kushuka chini
11. Inashangaza kuona muda unazidi kwenda
12. Na mchezo wa Hip hop ndo kitu nnachokipenda
13. Check maplayer wenu jinsi ninavyowapiga denda
14. Ni VIP kila kiwanja ninachokwenda
15. Kwani hatari kitu gani
16. Kila wakati nipo bwana TBC extra quality
17. Na wachizi wangu wote sasa zidisheni hasira
18. Ni wakati wa kumaliza huu ni utungo wa kibiashara
19. Sasa ni muda mrefu wanatufanya mafara
20. Tunaingiza mabilioni wanahonga mademu vitara
21. Hamuwezi kunitisha
22. Katika kuthibitisha
23. Nawawasha na tafadhali sahauni kuhusu sugu
24. Maana atazidi tu kuleta mavurugu
25. Na kuwanyonga watu simo
26. Labda ganja zamani kidogo nilikuwemo
27. Na ndo mana mpaka leo bado inanipa misimamo
Chanzo: Mr. 2 (2009), Veto
Wimbo mwingine wa Bongo Fleva ambao unabeba maudhui ya mapenzi ni “Ananitesa” ulioimbwa
na Zay B akiwashirikisha Unique Sisters. Tazama mistari ifuatayo:
1. Nakupenda pia nakutaka pia
2. Mwenzio naumia
3. Unanipa machungu moyoni
4. Nikikutazama usoni
70
5. Jinsi ulivyo handsome
6. Nadata ukitabasamu
7. Nakuhusudu si mchezo
8. Ukinikubali utakula vya dezo
9. Usiogope kuitwa binti
10. Nitakutunzia siri
11. Nitakupa offer tutajivinjari
12. Viwanja hatari usione hatari
13. Limekuangukia zali
14. Mimi kwako nimenasa
15. Unanitesa nitajinyonga nikikukosa…
16. Nataka tushinde ndani ya jiji la Makamba
17. Ananitisha na pamba jinsi anavyotoka bomba…
18. Napata wendawazimu mapenzi hayana ugumu
19. Njoo tupate goodtime…
20. Sema unachotaka utapata
21. Ila usilete za kuleta kwangu utapeta
22. Sina ujanja nitakupa hata mkwanja
23. Twenzetu ukaben kiwanja
24. Mi sio mchunaji ukiwa nami utapata ulaji
25. Nina kiasi cha kumwaga tatizo utumiaji
26. Sio kama nachonga wanaume nawahonga
27. Unachotakiwa kwangu kutulia
28. Utakula raha zote za dunia
29. Na maisha utafurahia
Chanzo: Zay B (2002), Mama Afrika
Katika wimbo huu tunaona msanii anaelezea mapenzi ya dhati aliyonayo hata kuwa tayari kujinyonga
kwa sababu ya mapenzi. Anaendelea kueleza kwamba kwa mapenzi aliyonayo atatumia hata fedha zake
na mali nyingi alizonazo kumlisha na kumpa kila kitu mpenzi wake.
Aidha, naye mwanamuziki Bushoke anaelezea mapenzi ya dhati aliyonayo kwa mpenzi wake na
kwamba bado hajafika mwisho wa kumwonyesha mpenzi wake mapenzi yote. Turejelee wimbo wa
Jackline Ntuyabaliwe (K-Lynn) akimshirikisha Bushoke, uitwao “Machozi ya Furaha.” Tuchunguze
ubeti wa wimbo huo:
1. Na bado na bado sijafika mwisho
2. Na bado na bado sijamaliza kitabu
3. Vumilia maisha yangu, utakula vya kwangu
4. Mimi si wale wanaojisifu kwa ngono
5. Mapenzi si maneno, mapenzi ni vitendo
6. Na bado na bado nimesema bado
Chanzo: K - Lynn (2004), Machozi ya Furaha
Hapa msanii anaeleza kwamba mapenzi ni vitendo na si ya maneno matupu. Katika wimbo huu kama
ilivyo kwa ule wa Zay B msanii anaamini kwamba mapenzi ni kupeana vitu (tazama mstari wa 3).
Mapenzi katika ushairi wa Bongo Fleva yanahusishwa sana na vitu na mali alizonazo mtu.
Ujitokezaji mkubwa wa maudhui ya mapenzi katika nyimbo za Bongo Fleva ndio hutumika
kama kigezo kimojawapo cha kujaribu kuutofautisha muziki wa Bongo Fleva na Hip hop. Hivyo,
muziki wa Bongo Fleva unaonekana kuwa ni ule unaohusu zaidi mapenzi wakati Hip hop hauhusu sana
suala hilo bali mambo mengine “muhimu.” Akithibitisha hili Mwanjoka (2011:111) anaeleza kwamba:
Wapo wasanii wa Hip hop ambao wanaimba nyimbo za mapenzi pia, lakini sio mara kwa mara
kama wasanii wengine wa muziki wa kuimba (Bongo Fleva). Mfumo huu wa kutengeneza nyimbo
za mapenzi kwa wingi umejengeka hata kwa wasanii wapya wanaoanza muziki kwani wengi wao
huanza na nyimbo za mapenzi na wachache ndio huanza na nyimbo za kujisifia (nyimbo za
majigambo) (Ufafanuzi wetu).
(d) Maudhui ya Kiutamaduni Katika Ushairi wa Bongo Fleva
Zaidi ya majigambo ya kijamii, muziki wa Bongo Fleva pia unabeba maudhui ya kiutamaduni.
Miongoni mwa mambo yanayosawiriwa katika ushairi huo ni imani mbalimbali kama vile imani za
waganga na uchawi, masuala ya mila na desturi na kadhalika. Mfano mzuri wa mashairi ya kitamaduni
71
yanayozungumzia masuala ya mila na desturi ni yale yanayoonekana katika wimbo wa Abel Motika
(Mr. Ebbo) uitwao “Mi Mmasai” uliopo katika albamu ya Fahari Yako. Katika shairi hilo msanii
anaelezea mila za Wamasai. Anaeleza kwamba Wamasai wanazishika na kuzifuata mila na desturi za
Kiafrika. Aidha, anaeleza kwamba utamaduni wa Kimasai upo juu kuliko tamaduni zote za Afrika.
Anataja baadhi ya tamaduni hizo kuwa ni pamoja na mavazi ya Kimasai, dawa za asili na kadhalika.
Kujivunia utamaduni wa jamii husika ni moja ya mambo muhimu katika kujenga jamii endelevu (Ayisi,
1972; Mair, 1979).
Aina nyingine ya maudhui ya kiutamaduni ni maudhui ya imani. Wasanii wa ushairi wa Bongo
Fleva wana imani mbalimbali ikiwamo imani kwamba kuna Mungu ambaye ana uwezo wote.
Wanaoamini hili wanaamini vilevile kuwa kumcha Mungu na kujiepusha na uovu ni jambo la kujivunia
na jambo litakalompeleka mtu mbinguni. Tuthibitishe hili kwa kuangalia mfano kutoka kwa msanii
Sister P katika wimbo wa “Sisi Tulivyo” anapobainisha hili:
1. Mimi nilivyo ni mchamungu kuliko ulivyo
2. Mimi nilivyo siyo bitozi wa kupenda sana mademu
3. Mimi nilivyo sina habari na adui asemavyo
4. Mimi nilivyo sasa ni peace hakuna uadui
5. Wote rafiki awe msichana awe mvulana
6. Mimi nilivyo napenda sana mambo ya Mungu
7. Sichagui kama inavyosema Biblia
8. Mimi nilivyo sinywi pombe sivuti brother
Chanzo: Omari (2009:295)
Katika shairi hilo hapo juu msanii anaelezea jinsi yeye alivyo mchamungu na havuti sigara wala
hapendi ukahaba.
Aidha, wapo wanaoamini nafasi ya Mungu na uganga katika maisha. Wanaamini kwamba
uwezo wa kiganga na Kimungu unaweza kutumika kumwinua mtu na kumpa mafanikio na pia unaweza
kutumika kuwaharibia wengine. Vilevile, wanaonesha imani kwamba msaada kutoka kwa Mungu ndio
upo juu ya msaada mwingine wowote. Tuchunguze wimbo wa “Achana Nao” Sister P anaposema:
1. Kilichotoka kwa Mola kamwe hakitarubuniwa
2. Ni sawa na askari vitani habadili nia
3. Ongeza bidii kwenye steji safisha njia
4. Funga masikio fanya utakavyo Pondela
5. Sikiliza ushauri wa watu panapotakiwa
6. Ufikirie kwa kina kisha utunge ujumbe kwa kina
Chanzo: Omari (2009:292)
Hapa msanii anaonyesha uwezo mkubwa alionao Mungu katika kuwafanikisha wanadamu. Hata hivyo,
msanii anasisitiza nafasi ya juhudi na maarifa ili Mungu aweze kusaidia. Mawazo kama haya
yanaonekana katika ubeti ufuatao:
1. Nafungua ubongo natoa fikra za utumwa kichwani
2. Kipawa chatoka kwa mola wala sijatumia ubani
3. Sister P kupata chati watu wanadhani rap utani
4. Rap biashara bwana ila angalia usijepata hasara
5. Kuuza vitumbua, pipi maandazi zote biashara
6. Usidharau hizo biashara watu watakuangushia msala11.
7. Wasomi wengi wamesoma kwa kutumia hizo biashara
8. Mashairi sibahatishi na nitauza nyingi nakala
9. Na siyo utani nyota kwangu imeonekana biashara
10. Wandago12 rafiki zangu tena wa kina
11. We uliza maswali mengi majibu mimi sina
12. Nakupa rap shule mashairi yangu yana vina
Chanzo: Omari (2009:291)
Katika mstari wa pili (2) wa wimbo huo tuliounukuu anabainisha kwamba mafanikio aliyonayo
hayatokani na uganga bali amepewa na Mungu. “Ubani” hapo unawakilisha uganga kutokana na ukweli
11 Msala ni msimu unaotumika kumaanisha matatizo/kipigo.
12 Wandago anamaanisha Walume Ndago yaani kikundi cha Bongo Fleva cha TMK Wanaume.
72
kwamba ni vitu vinavyotumika sana katika fani hiyo. Hata hivyo, Zay B katika wimbo mwingine
uitwao “Hatari Kitu Gani” anaonesha kuwa Mungu na uganga vinaweza kusaidia tu kama mtu ataweka
juhudi binafsi. Aidha, anabainisha kuwa hata uchawi ukitumika kumkwamisha mtu lakini kama mtu
huyo atakuwa na juhudi, uchawi na uganga huo hautafaa kitu. Tuthibitishe hili katika ubeti huu:
1. Mimi komandoo tena nakuja kwa vishindo
2. Nasema njoo once again nawakilisha Tanzania
3. Wanga mtabana mtaachia lyrics nazidi kuwamiminia
4. Mimi mtaniambia sio kama najifagilia13
5. Mamia kwa mamia wamekiri kama mimi ndio concord…
6. Sauti yangu inasikika dunia nzima
7. Vigumu kuisahau kama Tupac na B.I.G
Chanzo: Omari (2009:342)
Katika wimbo huo msanii anabainisha kwamba zaidi ya “wanga” au wachawi kumbania mtu
(kumroga) bado kuna uwezekano wa mtu husika kufanikiwa. Hapa tunapata picha kwamba “wanga” au
uchawi hauleti maendeleo bali unatumika kuwakwamisha watu. Katika mstari wa tatu anabainisha wazi
kwamba kazi ya wanga ni kubana mafanikio ya watu wengine. Uchawi hapa unawekwa kundi moja na
tabia zenye sifa mbaya kama unafiki, uchoyo, kutopenda mafanikio ya mwingine na kadhalika.
Kutokana na hilo neno “wanga” huweza pia kutumika kumaanisha mtu yeyote asiyependa maendeleo
ya mwingine. Wasanii, kwa hiyo, wanaimba kuelezea jinsi wao wasivyorogeka kwa namna yoyote ile.
Hili linabainika pia katika wimbo “Maisha Uswahilini” wa Sister P:
1. Sister P nakuja wanga sasa mbona mtakwisha...
2. Sina papara katika fani nishatua...
3. Rudi nyuma kumbuka enzi za Mchonga14
4. Watoto wadogo wachawi mpaka skonga15
5. Tunashinda nao maskani nyumbani kwao
6. Tunacheka nao wachawi ni mama zao
7. Amka usiku ndugu zangu muone kazi
8. Walivyo uchi utafikiri radhi
9. Angalia cha moto akifa anavyotapatapa
10. Mchana watu, usiku wamegeuka paka
Chanzo: Omari (2009:303)
Hapa msanii anaonyesha uchawi ni jambo linalomchukiza Mungu, ni dhambi na hivyo mshika dini,
kama yeye, hapaswi kuwa mchawi. Vilevile, anabainisha kuwa uchawi hauwezi kuleta maendeleo bali
unarudisha nyuma maendeleo ya jamii husika. Uchambuzi wa kina juu ya suala la uchawi katika jamii
za Kitanzania na uhusiano wake na Mungu na maadili ya jamii unaonekana katika Mair (1979:218-
232).
2. FANI YA USHAIRI WA BONGO FLEVA
Tumeeleza hapo awali kwamba fani ni jinsi kazi ya kifasihi ilivyoumbwa. Fani hujumuisha
vipengele kama utungaji, muundo, mtindo, wahusika, mandhari na matumizi ya lugha. Katika sehemu
hii tutachambua mbinu mbalimbali za kifani zinazotumika katika ushairi wa Bongo Fleva tukianza na
utungaji.
(a) Utungaji wa Ushairi wa Bongo Fleva
Utungaji wa ushairi wa Bongo Fleva ni wa aina mbili: utungaji wa papo kwa papo na utungaji wa
kabla ya tukio/utendaji. Hebu tuchambue kwa kina aina hizi mbili za utungaji wa ushairi wa Bongo
Fleva.
(i) Utungaji wa Papo kwa Papo katika Ushairi wa Bongo Fleva
Wataalamu mbalimbali wameelezea kuhusu utungaji wa papo kwa papo wa kazi za fasihi.
Maelezo haya yanaonekana katika kile kinachojulikana katika fasihi kama nadharia ya fomula simulizi.
Nadharia hii ilianzishwa na Milman Parry (1928 na 1930) na mwanafunzi wake, Albert Lord (1981).
Parry alianza kwa kujiuliza ni kwa vipi tendi za Homer zilitungwa. Je, zilikuwa simulizi au andishi?
13 Kujifagilia ni msimu unaotumika kumaanisha kujisifia.
14 “Mchonga” hapa linatumika kumaanisha Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa sababu alichonga meno. Hivyo hapa
msanii anamaanisha enzi za Nyerere.
15 Skonga ni msimu unaotumika kumaanisha shule. Unatokana na neno la Kiingereza school (skuli)
73
Alihisi kuwa labda zilikuwa simulizi, na kuja kuandikwa baadaye. Ili kuthibitisha nadharia tete hiyo,
alifanya utafiti katika jadi hai ya tendi-simulizi nchini Yugoslavia (miaka ya 1920-1940). Ikumbukwe
kwamba jadi ya Yugoslavia ina uhusiano mkubwa na ile ya Wayunani (Homer). Kabla ya Parry,
wataalamu kama vile Robert Wood (1767) na F.A. Wolf (1775) walikwisha dokeza kuwa huenda tungo
za Homer hazikuandikwa, bali zilikuwa simulizi. Lakini uthibitisho wa kutosha wa dai hili ulikuwa
bado haujatolewa. Kadhalika, wataalamu wa Biblia walikwisha anza kuhisi kuwa huenda hata maelezo
ya Biblia, hasa Agano la Kale; yalikuwa simulizi za mdomo kabla ya kuandikwa.
Parry alianza kwa kuchunguza mishororo ishirini na tano (25) ya mwanzo ya Iliad na Ulisei
(Odyssey) ili kuona ni kwa kiasi gani tungo hizo mbili ni za kifomula. Parry (1971:272) anaielezea
fomula kuwa ni:
A group of words regularly employed under the same metrical conditions to express a given
essential idea.
Kundi la maneno linalotumika katika mazingira ya kinudhumu yanayofanana ili kueleza wazo
fulani mahsusi lililo muhimu (Tafsiri yetu).
Matokeo ya utafiti wake yalimshangaza: Aligundua kuwa takriban 70% ya mistari 27,000 katika
tendi hizo ilikuwa ya ki-fomula. Kutokana na hilo, Parry akahitimisha kwamba tungo hizo ni nudhumu,
ni simulizi (si andishi), na ni za kimapokeo.
Baada ya Parry kufariki mwaka 1935, mwanafunzi wake, Albert Lord, aliuendeleza utafiti wake
na kutoa mchango kubwa. Aliongeza kipengele cha “formulaic expression” – kauli ya kifomula – katika
nadharia ya fomula simulizi. Alisema, mbali na watendi kutumia fomula bila kuzibadilisha, wakati
mwingine huweza kubuni na kutumia kauli zenye muundo wa fomula. Alielezea kauli ya kifomula
kuwa ni “a line or half-line constructed on the pattern of fomula.” (mshororo au kipande chenye umbile
la fomula). Mchango mahsusi wa Lord ni katika kipengele alichokiita “theme.” Kipengele hicho ndicho
kilichokuja kuitwa topos (na kutoholewa kuwa topo kwa Kiswahili) na watafiti wengine. Lord anaeleza
kuwa “theme” ni “repeated incidents and descriptive passages” (Vitushi na vifungu vya maelezo
vinavyorudiwarudiwa). Tofauti na fomula, topo hailazimiki kufuata urari wa mizani, au kujirudia neno
kwa neno, bali huwa na umbo zalishi lenye kubadilika kulingana na mazingira ya usimulizi. Mifano ya
topo inayotolewa ni kupokea barua, kuitisha baraza, hotuba za ufafanuzi, kujibu barua, kujiandaa kwa
vita na kadhalika (taz Mulokozi, 2002, The Epic Contoversy). Topo husaidia kujenga mtiririko wa kazi
ya fasihi simulizi. Kadhalika, humsaidia fanani kuijenga na kuisimulia kazi yake kwa haraka wakati wa
utendaji, maana topo tayari zimo katika jadi na asili yake; anachohitaji ni kuziainisha, kuzirekebisha
kidogo na kuzitumia kulingana na mahitaji (taz. Samwel, 2012a).
Hata hivyo dhana za fomula na topo zikarekebishwa na wataalamu mbalimbali kadri
walivyoona inafaa kulingana na mitazamo yao (taz. Nagler, 1967 na 1974; Johnson, 1978; Okpewho,
1979; na Mulokozi, 2002:132-135). Kwa mfano, Mulokozi (2002:132-135) anaona kwamba maelezo ya
fomula ni bora yaanzie katika ngazi ya maana. Anasema:
Formula as it applies to enanga poetry is ana abstract, traditional recurrent core-idea, serving
primarily as a semantic and structural aid in oral composition-in-performance, and realized
concretely, as a phrase or clause, only in oral performance, and largely through the devices of
verbal repetition, derivation, transformation, and linguistic-contextual association.
Fomula kama inavyotumika katika tendi za nanga ni wazo-kiini radidi la kidhahania la kimapokeo
linalosaidia kuzalisha haraka maana na miundo katika utungaji wa papo kwa wakati wa utambaji,
na ambalo hujidhihirisha tu kama kipashio wakati wa utendaji-simulizi, hususan kwa kutumia
mbinu za uradidi-kauli, unyambuo, ugeuzi, na uhusishi wa kiisimu na/au kimuktadha (Tafsiri
yetu).
Mulokozi anaendelea kwa kusema kwamba fomula hudhihirika kwetu kupitia sura na maumbo
mbalimbali wakati wa uwasilishaji: maumbo hayo anayaita alomofu (< alloform-mulla). Dhana hii ya
fomula kwa mujibu wa Mulokozi, ndiyo iliyotumiwa pia na Samwel (2012a) na ndiyo inayotumiwa pia
katika andiko hili kwani inaboresha ufafanuzi wa awali wa akina Parry. Aidha, Mulokozi (2002:134)
anapendekeza dhana “topos” badala ya dhana “theme” iliyopendekezwa na Parry na Lord. Mulokozi
74
anaona kwamba kwa kuwa dhana ya “theme” tayari inatumika katika fasihi kumaanisha dhamira/wazo
kuu, “theme” katika nadharia ya fomula – simulizi iitwe topo. Anaifasili topo kwa kusema:
A traditional or conventional stock incident or description which is regularly reformulated in
different stories and contexts by the oral bards to build up oral narrative poems during
performance.
Kitushi au sawiri ya kikaida ya kijadi ambayo husimuliwa upya na watendi-simulizi katika hadithi
na miktadha mbalimbali ili kutunga tungo simulizi wakati wa utendaji.
(Tafsiri yetu).
Fasili ya Mulokozi ni bora kwani imeboresha maelezo ya waliomtangulia. Hata hivyo, kwa
kuwa Mulokozi (2002) alikuwa anashughulikia utendi ni wazi kwamba ili tuweze kuitumia fasili yake
katika ushairi wa Bongo Fleva tunaouelezea hapa, tunapaswa kuirekebisha fasili hiyo. Topo, kwa hiyo,
inafasiliwa katika andiko hili kuwa ni kitushi au sawira ya kikaida ya kijadi au kiada ambayo
husimuliwa upya na wasanii wa fasihi simulizi ili kutunga tungo simulizi, ukiwamo ushairi wa Bongo
Fleva, wakati wa utendaji wake. Topo ni moja ya zana zinazozalisha fomula katika usimulizi.
Kwa ujumla, msimamo wa Parry na Lord na wafuasi wao ni kwamba fomula na topo
hazihusishi kukariri. Hii ina maana kwamba kazi za fasihi simulizi, ukiwemo ushairi wa Bongo Fleva,
huweza kutungwa papo kwa papo wakati wa utendaji wake. Huu ndio umekuwa msingi unaotumiwa na
wanafasihi mbalimbali kueleza kwamba tanzu mbalimbali za fasihi simulizi zilitungwa papo kwa papo
wakati wa utendaji wake (taz. Finnegan, 1970; Mulokozi, 1996). Suala hili pia linabainika katika
ushairi wa Bongo Fleva ambapo tunaona kuna wasanii mbalimbali ambao huimba mashairi yao papo
kwa papo.
Baadhi ya wasanii wa ushairi wa Bongo Fleva hutunga mashairi yao wakati wa tukio husika la
utendaji. Wasanii huweza kuwa jukwaani katika maonyesho na baada ya kuimba au kughani nyimbo
zao kadhaa hupandwa na midadi na kuanza kughani au kuimba mashairi mapya papo kwa papo. Wakati
mwingine, huweza kubadilisha maneno ya mashairi ya awali na kuweka maneno mapya
wanayoyatunga papo kwa papo. Mtindo huu ni maarufu kwa jina la free style, yaani mtindo huru.
Profesa Jay katika mahojiano aliyoyafanya katika Samwel (2012a) alimwambia kwamba kuna
wanamuziki wanaojulikana kuwa maarufu kwa mtindo huu wa utungaji. Alimtajia baadhi ya
wanamuziki hao kuwa ni pamoja na Ibrahimu Mohamed (a.k.a Roma), Albert Ngwea (a.k.a Mangwea)
na John Sim Johon Mseke (a.k.a Makini). Kujua mtindo huu kunahusishwa na umahiri katika muziki
wa Bongo Fleva. Afande Sele katika wimbo wake uitwao “Mtazamo” anathibitisha hili anaposema,
“wanaitwa ma MC hawajui mitindo huru, huu mtazamo wangu naona vingi vioja.” Hapa tunaona wazi
kwamba mwanamuziki anayejua mtindo huru ndiye mwanamuziki bora. Hii inaurudisha muziki wa
Bongo Fleva katika sifa za msingi za fasihi simulizi, utendaji wa papo kwa papo.
Utungaji huu, hata hivyo, huongozwa na fomula na topo. Msanii anayetunga papo kwa papo
huongozwa na fomula na hasa ile ya urari wa vina na mizani. Fomula hii humfanya kila mara
kuhakikisha anapachika maneno mapya ambayo yana vina vinavyofanana na mstari uliopita. Kwa
mfano, tulihudhuria maonyesho ya Bob Junior ambaye alighani utungo huu ambao, kwa kuwa haupo
katika nyimbo zake zinazofahamika, tunachukulia kuwa aliutunga papo kwa papo. Hebu tuuangalie
utungo huo:
1. Bob Junior mzee wa mashati
2. Mimi ndiye Rais wa watanashati
3. Sasa naandaa mkakati
4. Mbona mimi mzee wa pati!
5. Sauti ya rojorojo za Chocolate
6. Wale wachawi tuwaweke kati
7. Watalia watajinyonga kwa wakati
Chanzo: Umenukuliwa katika onyesho la Bob Junior lililofanyika Mbeya Tarehe 13/4/2011.
Vivyo hivyo msanii Roma akiwa katika tamasha la Epiq Nation katika jiji la Mwanza alitoa
ghani za papo kwa papo kulingana na muktadha wa tukio lililolokuwa linaendelea. Ghani hizi hazipo
katika wimbo wake wowote na hivyo ni ithibati kwamba alizitunga papo hapo jukwaani. Ghani hizo
zinasema:
75
1. Mwanza, msishindane na mwanamke pedeshee atamuhonga noah16
2. Wanaume mjitahidi ipo siku mtatoboa
3. Mimi ni Rais wa ghetto
4. Sina kabisa mchecheto
5. Na wala sipigi punyeto
6. Namiliki mademu kwa kipato
7. Mwanza, sema oyee kwa Epiq Nation
Chanzo: Umenukuliwa katika onyesho la Epiq Nation Mwanza mwaka 2011.
Fomula hii ya urari wa vina na mizani wakati mwingine huwalazimisha kutumia maneno
ambayo kimantiki hayaendani na yale yaliyotangulia ila kwao lengo la msingi ni urari wa vina na
mizani. Vilevile, hufanya hata mawazo yabebwayo na ushairi husika kuwa hayana ushikamani. Mfano
wa hili tunauona katika wimbo wa Roma uitwao “Mathematics:”
Ubeti 1
1. Nimeshatikisa nyavu mi ndo MVP
2. Wakakimbia depo hapo nipo CCP
3. Niliwapigisha kuruta kwata la JKT
4. Nina kipaji mimi kushinda hata THT
5. Nawapangisha foleni kama benki ya NMB
6. Mi nimesoma PCM siyo PCB
7. So hata tufungwe mimi ni Asernal siyo Man U
8. Kibonde we ni member wa Loan Board au TCU
9. Nchi imeuzwa vigogo wanatuita ATM
10. Tuwakemee mafisadi wote wa CCM
11. Kuvua gamba haiwasafishi mbele ya CUF
12. CHADEMA mwone Makamba, JK kwa TFF
13. Sihitaji dancer wala mapanga yale ya TMK
14. Show zangu siyo longolongo zile za Y2K
15. Na siyo bandia ka Kontena lile la BOT
16. Situkuzi kilicho feki kama TOT
17. Mi ndio Roma ntasimama kama KKT
18. Ahsante Bongo, Macho juu, Nyamongo, TBC
19. Mistari yangu mitamu kama ya TPC
20. Na kwa hizo fomu MC utalazwa KCMC
21. Kodi ya Walalahoi pombe ya TRA
22. Miili yao ndio biashara ndani ya BBA
23. Fataki anatoa mkopo ndani ya TIA
24. Licha ya mimba haina uhakika mpaka DNA
Ubeti wa 2
25. Mwambieni hatukuogopa tabiri za Shekhe Yahaya
26. Mauti yangetufika bila kumpinga Jakaya
27. Sisaliti sirudishi kadi ya chama kama Nakaaya
28. Bado hainiingii akilini hukumu ya Babu Seya
29. (Mgonjwa anakufa mapokezi Doctor anakunywa valuer
30. Wazazi wanakufa labour wengine ICU) x2
31. Waambieni mi mzalendo na hii ndio mbiu ya mgambo
32. TANESCO wakizima umeme upitishe mzigo wa magendo
33. Harakati za Doctor Leakey katika kuinua michezo
34. Mama Terry wamemsaliti Mwasiti wamempa tangazo
35. Lady Pepeta hawavai msema kweli Semunge
36. Mipira hawaitumii eti kwa Babu kuna kikombe
37. Mafuta wanapandisha bei kisa wanaamini misheni
38. Wachina wanapewa tenda si tunanyimwa vibali
39. Gongo la Mboto wanalia misaada wamewatapeli
40. Wandugu bwaga manyama ayaokote Magufuli
41. Pesa za ujenzi wa shule kala na mkewe headmaster
42. Thamani ya mabango ya kampeni somesha watoto VETA
43. Wanajiuliza Doctor Slaa ni wapi anapata data
44. Hata kama nimevaa mlegezo ikulu napiga chata
45. Ikulu imejaa vibaka Manzese wanawakamata
16 Noah ni aina ya basi dogo (minibus) ambazo ni maarufu sana nchini Tanzania. Hutumiwa na watu mbalimbali kama gari
za kutembele. Aina hii ya magari huaminika kuwa ndio yanayotumika zaidi katika kuwahonga wanawake ili watoe penzi.
76
46. Makahaba wanaongezeka boom zinapokata
47. Wanauziana minada mali za serikalini
48. Mhasibu anacheck porno si tumepanga foleni
Ubeti wa 3
49. Ma MC wanapata stress Roma akitua Ubungo
50. Tanga nilifunga tatu nafunga tano hapa Bongo
51. Wanafuga rasta ili wapate mademu wa kizungu
52. We Mchaga kauze mitumba muziki ushakufunga pingu
53. Mistari yako myeusi unaipaka Carolite
54. Katiba siyo msahafu my people need copy...
55. Ndoto zangu kitambo zilikuwa nije kuwa padri
56. Zikayeyuka nilipopuliziwa moshi wa weed
57. Naenda church naanguka tena nasali
58. Na popote utakaponiona shingoni nimevaa rozali
59. Mi natafuta hela ya kula we unamcheck tu Alehandro
60. Unadhani utaandika nini kama siyo hadithi za Kemondo?
61. Kama hauna kipaji kamuone Babu wa Loliondo
Chanzo: Roma (2011), Mathematics
Katika wimbo huu unaoonekana wazi kuwa kabla ya kuurekodi ulitungwa papo kwa papo
kutokana na sifa simulizi zinazobainika, una utata mkubwa kimantiki na kiushikamani. Tunaona visa
anavyovisimulia vimetawanyika na havina ushikamani. Katika ubeti wa kwanza tunaona ni kama visa
hivyo vimepachikwa tu ili kuleta urari wa vina. Kwa mfano, visa vinavyoelezwa katika mstari wa 1-6
havihusiani na kisa kinachoelezwa katika mstari wa 8 na pia visa vyote hivyo havihusiani na kile
kinachoelezwa katika mstari wa 9-12. Pia kinachoelezwa katika mstari wa 9-12 hakina ushikamani
wala uhusiano na kinachoelezwa katika mstari wa 13-20. Hali hiyo inaonekana katika mistari mingine
na beti zingine za wimbo huu.
Mbali na aina hii ya utungaji kuongozwa na fomula na topo, tunaona kuwa hata utungaji wa
nyimbo nyingine zilizorekodiwa, wasanii hawa huongozwa na fomula ambayo huwasaidia kukariri
wakati wa uwasilishaji wa ushairi wao jukwaani. Msanii huweza kuwa na albamu kumi ambapo kila
albamu huwa na nyimbo hadi kumi na mbili lakini huwa na uwezo wa kuziimba nyingi kati ya nyimbo
hizo jukwaani bila kusoma mahali. Katika hali ya kawaida ni vigumu kukariri nyimbo nyingi kiasi
hicho. Vilevile, nyimbo hizo zina marudio mengi hata yasiyo ya lazima wakati mwingine, hivyo
tunadhani kwamba hata utungaji wa nyimbo hizo huongozwa na fomula simulizi. Mfano mzuri wa
nyimbo ambazo tunadhani kwamba zinaongozwa na fomula ni pamoja na wimbo wa Prof. Jay, “Jina
Langu” na wa Sister P “Sisi Tulivyo” kama inavyonukuliwa hapa chini:
WIMBO WA JINA LANGU
1. Jina langu linavuma, kwenye mitaa
2. Jina langu lina uwezo wa kisupastaa
3. Jina langu linaongeza idadi ya maadui
4. Wengine nawatambua wengine siwatambui
5. Jina langu
Chanzo: Prof. Jay (2003), Mapinduzi Halisi
WIMBO WA SISI TULIVYO
1. Sisi tulivyo kama utakavyoniona ndio nilivyo
2. Mimi nilivyo siko sawa na jinsi ulivyo
3. Mimi nilivyo hata unavyodhani sivyo nilivyo
4. Mimi nilivyo huwezi kunitambua jinsi nilivyo
5. Mimi nilivyo na huu ndio ukweli wa jinsi nilivyo
6. Mimi nilivyo siyo sawa na manabii jinsi walivyo
7. Mimi nilivyo nina hekima kuliko mtu mzima alivyo
8. Mimi nilivyo na hadhi zaidi ya wafalme jinsi walivyo
9. Mimi ni mchamungu kuliko ulivyo
10. Mimi nilivyo napenda mademu jinsi walivyo
Chanzo: Omari (2009:295-296)
Katika nyimbo hizo hapo juu tunaona kuwa kuna marudio mengi ambapo maneno, virai, vishazi na
sentensi vimerudiwa, kunyambuliwa au kupinduliwa. Katika wimbo wa “Jina Langu,” kwa mfano,
77
tunaona kirai “jina langu” kimerudiwa sana wakati katika wimbo wa “Sisi Tulivyo” tunaona kirai
“mimi nilivyo” kimerudiwarudiwa sana.
(ii) Utungaji wa Kabla ya Tukio katika Ushairi wa Bongo Fleva
Mbali na utungaji wa papo kwa papo, ushairi wa Bongo Fleva huweza pia kutungwa kabla ya
uwasilishaji wake. Ushairi wa Bongo Fleva huweza kutungwa kabla ya utendaji wake na kukaririwa,
kuandikwa au kurekodiwa. Utungaji huu ndio maarufu zaidi miongoni mwa wasanii wa ushairi huu.
Utungaji huu huchukua muda kutungwa na huandikwa na kukaririwa kabla ya kuimbwa. Kasonga
(2011:10) anabainisha wazi kwamba kutunga mashairi ya Bongo Fleva kunachukua muda mrefu sana
na kunahitaji umakini. Msanii huwa na wazo kichwani, halafu huanza kuliandikia mashairi yake na
hatimaye huyapeleka studio kwa ajili ya kutengenezewa mapigo (beats) na mtayarishaji wa muziki.
Kufikia mwaka 2011, gharama za kutengeneza wimbo studio zilikuwa ni kuanzia laki mbili na
kuendelea kutegemea na aina na ubora wa studio (Mwanjoka, 2011:14). Gharama kama hizi tulitajiwa
pia na Prof. Jay katika mahojiano yetu. Kazi hii ya kutunga mashairi ya Bongo Fleva huchukua muda
kulingana na uwezo wa msanii husika. Kwa mfano, katika mahojiano yetu msanii Kulwa Felician
Pongwa (a.k.a Black wa Uswazi) tuliyoyafanya tarehe 19/05/2011 alitueleza kwamba hutumia kati ya
siku tatu hadi wiki nzima kutunga wimbo ukakamilika. Lakini Adili Nkwera (a.k.a Hisabati) alidai yeye
huchukua kati ya siku moja hadi nne.
Vilevile katika utungaji wa mashairi ya Bongo Fleva kuna wasanii wanaotunga wenyewe na
kuna wale wanaotungiwa na watu wengine halafu wao huyanunua mashairi hayo pamoja na hakimiliki
yake. Ramadhani Mponjika katika mahojiano yetu alituambia kwamba wapo pia wasanii wanaotunga
wenyewe na kujiandalia na mapigo na hivyo kumwelekeza mtayarishaji wa muziki mapigo ya
kuyaweka katika nyimbo hizo. Mwanamuziki Abasi Hamisi (a.k.a Twenty Percent) akihojiwa na
www.Bongo Celebrity.com anathibitisha hili:
Mimi binafsi huwa napenda sana kufanya kazi na producer ambaye ananipa pia muda wa
kuzungumza na kuchangia katika uboreshaji wa kazi nzima kwa sababu mimi ninapotunga wimbo
huwa natunga pia kila kitu mfano beats, chorus, mpangilio wa ala nk. Kwa hiyo huwa napenda
kupata producer ambaye pia ananisikiliza. Nashukuru Mungu kwamba producers wangu
ninaofanya nao kazi tunashirikiana vizuri kabisa katika kuhakikisha kwamba kitu kinachotoka ni
katika kiwango cha kueleweka na kukubalika.
(b) Utendaji wa Ushairi wa Bongo Fleva
Kipengele kingine cha fani ni utendaji. Katika kipengele hiki tutachambua mambo kama fanani wa
ushairi wa Bongo Fleva, hadhira ya ushairi huo, mavazi na vifaa vinavyotumika katika utendaji wa
ushairi huu, malipo ya utendaji na sauti inayotumika katika utendaji wa ushairi wa Bongo Fleva.
Tuanze na kipengele cha kwanza, fanani wa ushairi wa Bongo Fleva.
(i) Fanani wa Ushairi wa Bongo Fleva
Ushairi wa Bongo Fleva huimbwa au kughanwa na wanawake na wanaume. Wasanii wa kike wa
ushairi huu ni pamoja na Happiness Thadei (Sister P), Zainabu Lupangule (Zay B), Judith Wambura
(Lady Jaydee), Estalina Sanga (Lina), Rehema Chalamila (Ray C) na Khadija Shaaban (Keysha) kwa
kuwataja wachache tu. Kwa upande wa wasanii wa kiume kuna Joseph Mbilinyi (Mr. 2), Selemani
Msindi (Afande Sele), Joseph Haule (Prof. Jay), Abdul Sykes (Dully Sykes) na wengineo.
Zaidi ya kubaini kwamba ushairi wa Bongo Fleva hutendwa na wanaume na wanawake, wasanii wa
kiume wanaoimba au kughani mashairi haya ni wengi kuliko wanawake. Kwa mfano, tunaona kuwa
hakuna msanii wa kike hata mmoja ambaye alikuwa maarufu katika muziki huu miaka ya 1990
mwanzoni. Wanamuziki wa kike wa awali walianza kuonekana mwishoni mwa miaka ya 1990 na
mwanzoni mwa miaka ya 2000 ambapo tuliona wanamuziki kama vile Zay B, Sister P, Dataz, Lady
Jaydee na Stara Thomas. Idadi hii ni ndogo sana ikilinganishwa na idadi ya wasanii wa kiume katika
kipindi hicho hicho (Mwanjoka, 2011:14).
Uchache wa wanawake katika muziki huu unatokana na ukweli kwamba wanawake
wanakabiliwa na changamoto nyingi ili waweze kudumu katika muziki huu. Katika mahojiano yetu na
msanii aitwaye Ramadhani Mponjika alitufahamisha kwamba kikwazo kikubwa cha wasanii wa kike
kudumu katika muziki huu ni watayarishaji wa muziki na mapromota. Anadai kwamba watayarishaji
78
wa muziki na mapromota huwataka kimapenzi wasanii wa kike ili waweze kuwasaidia kimuziki. Pindi
wanapokataa hufanyiwa fitina na hivyo nyimbo zao kutopigwa redioni na katika televisheni na pia
kutopata maonyesho. Hatimaye wanamuziki hao wa kike hupotea katika muziki. Mawazo kama haya
yametolewa na msanii Vumilia Abrahamu alipohojiwa na Fiesta (2011a:25-27). Anasema, “…wengi
wa wasanii wa kike wanakatishwa tamaa na kazi hii kwa sababu unapoanza muziki kila unayekutana
naye mbele yako anakutaka kimapenzi na kama utakuwa huna msimamo unaweza ukatoa ngono kwa
kila mtu.” Lakini kwa upande wake Vumilia anasema kwamba yeye anakuwa na msimamo, kwa
sababu, anapokwenda studio anakuwa na pesa yake mkononi na mtu anapomwambia suala hilo
anamwambia ukweli kuwa niko kazini sijafuata ngono. Mwanamuziki huyo anasema, “Unapotoa ngono
kwa kila mtu thamani yako inashuka sababu wanapokupata wote wanaenda kukutangaza kuwa wewe
hujatulia.” Zaidi ya kubainisha kuwapo kwa tatizo hilo, msanii huyu anatoa suluhisho kwa wasanii wa
kike kwenda studio wakiwa na hela zao za kurekodia ili kukwepa mtego huo.
Mbali na kikwazo hiki, kipo kikwazo cha kijamii. Wanajamii kwa kiasi kikubwa wanauona
muziki wa Hip hop kuwa ni muziki wa wanaume na hasa wahuni na hivyo mwanamke anapojiingiza
katika muziki huu huanza kuonekana kuwa ni muhuni na asiye na maadili. Kutokana na hilo, wanawake
wengi wenye uwezo na kipaji wameamua kutojiingiza katika muziki huu (Fiesta, 2011a:25-27). Hivyo,
tunaweza kusema kwa hakika hapa kwamba, ingawa kwa kiasi kikubwa fanani wa ushairi wa Bongo
Fleva ni wanaume wapo pia wanawake wachache ambao ni fanani wa ushairi huu.
Mbali na fanani wa kike kuwa wachache, jambo lingine linaloonekana ni kuwa fanani wa ushairi
wa Bongo Fleva anaweza kuwa mtu mmoja au kikundi. Katika sehemu hii tutapitia aina hizi mbili za
fanani wa ushairi wa Bongo Fleva, msanii mmoja kama fanani na kikundi cha wasanii kama fanani.
(ii) Msanii mmoja kama Fanani
Fanani wa ushairi wa Bongo Fleva, kwa kiasi kikubwa, ni msanii mmoja mmoja. Msanii huyo
huweza kutunga nyimbo zote mwenyewe au kutungiwa na watunzi wengine na yeye hununua mashairi
na hivyo hakimiliki ya nyimbo hizo hubaki kwa msanii huyo hadi atakapoamua vinginevyo. Msanii
huyu, kwa kawaida, anatumbuiza kwa mtindo wa kupiga sidii na kuimba kwa kufuatisha (playback).
Wasanii hawa hawawezi kupiga muziki moja kwa moja (live) kwani msanii mmoja hawezi kupiga
kinanda, gitaa, ngoma na vifaa vingine kwa pamoja. Wakati mwingine wasanii hawa hukodisha
wachezaji (dancers/shakers) ambao hucheza pamoja nao. Wengi wa wachezaji hawa si wa kudumu bali
hukodiwa kwa ajili ya shughuli maalumu na kisha kuwalipa. Mchezaji mmoja huweza kukodiwa na
wasanii mbalimbali wa ushairi huu kwa nyakati tofauti.
(iii)Kundi la Wasanii kama Fanani
Zaidi ya fanani wa ushairi wa Bongo Fleva kuwa msanii mmoja, kuna uwezekano wa kundi la
wasanii kuwa fanani. Kundi hili huweza kuwa mkusanyiko tu wa wasanii wanaoimba au kughani
ushairi wa Bongo Fleva kwa pamoja au msanii mmoja aliyeanzisha bendi na kuwakusanya wasanii
mbalimbali na kuwaajiri kama wafanyakazi wake. Miongoni mwa vikundi vya wasanii vilivyopo na
vilivyowahi kuwapo Tanzania ni pamoja na Kwanza Unit, Hard Blasters, Daz Nundaz, East Coast
Team, Wakilisha, Wateule, TMK Wanaume Halisi na TMK Wanaume Family. Vingi kati ya vikundi
hivi vilikufa na wanamuziki kuanza kuimba kwa kujitegemea. Kwa mfano, kuvunjika kwa Hard
Blasters ndiko kulimfanya Prof. Jay kujitegemea. Aidha, kuvunjika kwa Gangwe Mob ndiko
kulikomfanya Inspector Haroun kujitegemea na pia kuvunjika kwa Inafrika Group ndiko kulikowaibua
Banana Zoro, Bob Rudala na Bizman.
Baada ya makundi mengi kati hayo kuvunjika wasanii wakaanza kuimba mmoja mmoja kwa
kujitegemea. Hata hivyo, bado yalibaki makundi machache ambayo, zaidi ya migogoro ya mara kwa
mara miongoni mwa wasanii wake, yameendelea kudumu. Makundi hayo ni pamoja na TMK Wanaume
Family, TMK Wanaume Halisi na Tip Top Connection. Vilevile, wasanii, mbali na kuwa na makundi
yao, huweza kutoa albamu zao kwa kujitegemea. Zaidi ya makundi haya ya wasanii, katika siku za hivi
karibuni kumekuwa na uanzishaji wa bendi za muziki wa kizazi kipya. Miongoni mwa bendi za muziki
wa Bongo Fleva zilizoanzishwa ni kama vile Top Band inayoongozwa na Khalid Mohamed a.k.a TID
(Top In Dar), B-Band inayoongozwa na Banana Zorro na Machozi Band inayoongozwa na Judith
Wambura a.k.a Binti Machozi. Hii ni aina mpya ya fanani wa muziki wa Bongo Fleva ambayo imeanza
79
kuonekana miaka ya 2007 nchini Tanzania. Bendi ya Kwanza kuibuka ni Top Band. Kundi la wasanii
kama fanani wa ushairi wa Bongo Fleva, lina faida moja kubwa kwamba wasanii huweza kubadilishana
uzoefu na kuunganisha juhudi zao na kufanya kazi bora zaidi. Ikifafanua hili
http://spotistarehe.wordpress.com inasema:
Nakubaliana na kila mmoja wao kwenda solo (kuimba kwa kujitegemea) kwani inampa uwanja
mpana zaidi lakini tunatakiwa kukumbuka kuwa kwenye makundi siku zote kila mmoja ana nafasi
yake, kuna wengine wanajua sana kupanga sauti wengine kupanga vina na wengine kupanga
mpokezano. Mfano kwenye bendi ya Wenge Muzika wakati huo kulikuwa na mtu anaitwa Blaise
Bulla kwenye wimbo utamsikia akiimba verse (mstari) moja tu ila kazi yake kubwa ilikuwa
kupanga sauti na wakati mwingine hata kushauri kuwa beti hii haifai kuimbwa na wewe, ikiimbwa
na fulani italeta mguso zaidi (Ufafanuzi wetu).
Mbali ya kuwa na msanii mmoja au kikundi cha wasanii kama fanani, kwa kiasi kikubwa fanani
wa ushairi wa Bongo Fleva ni vijana. Ushairi huu, na muziki wa Bongo Fleva, kwa ujumla, ni wa
vijana (Suriano, 2006; 2007; Omari, 2009; Mwanjoka, 2011). Akielezea muziki wa Bongo Fleva na
vijana, Mwanjoka (2011:102 -103) anasema:
Muziki huu wa kizazi kipya umefanikiwa kwa kiasi fulani kuwakomboa vijana wengi wa
Tanzania waliokuwa kwenye hali mbaya kimaisha…kabla ya muziki huu vijana wengi walikuwa
hawana kazi na walikuwa wakishinda vijiweni na kupoteza muda wao kwa kuvuta sana
bangi…baada ya muziki huu wa kizazi kipya kushamiri nchini Tanzania …vijana hao waliokuwa
wanakaa mitaani bila ya shughuli maalumu walipata ajira za uhakika.
Kutokana na muziki huu kuwa na fanani vijana ndipo jina la muziki wa kizazi kipya, yaani muziki wa
vijana, lilipopatikana.
(iii) Hadhira ya Ushairi wa Bongo Fleva
Kipengele kingine cha utendaji wa ushairi wa Bongo Fleva ni hadhira. Hadhira ya ushairi wa
Bongo Fleva ni mwanajamii yeyote. Ushairi huu huimbwa au kughanwa katika vituo mbalimbali vya
redio na televisheni nchini Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla kupitia kanda na sidii
zilizorekodiwa. Miongoni mwa vituo maarufu vya redio vinavyopiga ushairi huu ni pamoja na vituo
vya redio vilivyopo katika jiji la Dar es Salaam kama vile Clouds Radio, Radio One, East Africa Radio,
Capital Radio, Times Fm, TBC Taifa, TBC Fm na Redio Uhuru. Vingine ni vituo vya redio vilivyopo
katika mikoa mbalimbali ya Tanzania kama vile Radio Free Africa, Kiss Fm (Mwanza), Bomba Fm
(Mbeya), Kashozi Radio (Bukoba), Aboud Radio (Morogoro) na kadhalika.
Aidha kwa upande wa vituo vya televisheni vinavyopiga muziki huu ni pamoja na vile
vilivyoko Dar es Salaam kama Clouds TV, East Africa TV, Capital TV, ITV, TBC1, C2C, CTN,
Channel Ten na DTV. Vituo vingine vya televisheni ni vilivyoko nje ya Dar es Salaam kama Star TV
(Mwanza), Aboud TV (Morogoro) na kadhalika. Kwa upande wa Kenya, kuna vituo vya televisheni
kama Citizen TV, KTV, KBC na kadhalika ambavyo hupiga muziki huu. Katika nchi ya Uganda na
nchi nyinginezo za Afrika Mashariki na hata nje ya Afrika Mashariki, pia kuna vituo vya redio na
televisheni mbalimbali ambavyo vinapiga muziki huu. Vituo hivi vya redio na televisheni husikika na
kutazamwa katika mahoteli, mabaa, magari ya usafiri kama vile madaladala/matatu na mabasi ya
mikoani na katika maeneo mengine. Kwa hiyo, hadhira ya muziki huu ni pana. Hata hivyo, hadhira hii
si shiriki, ni hadhira mfu. Hadhira ya ushairi wa Bongo Fleva, kwa kiasi kikubwa, haiwezi kushiriki
katika utendaji wa ushairi huo. Hii inatokana na ukweli kwamba kwa kiasi kikubwa ushairi wa Bongo
Fleva umerekodiwa katika kanda na sidii. Hadhira ya ushairi wa Bongo Fleva inaweza kushiriki iwapo
ushairi huo unatendwa katika maonyesho, ambapo mashairi hayo huimbwa au kughanwa katika kumbi
mbalimbali za muziki. Akifafanua juu ya ushiriki wa hadhira katika muziki wa Bongo Fleva, Omari
(2009:82) anasema:
An artist also involves his/her audience in singing or joining in the chorus by pointing out the
microphone to them, or s/he may pause the CD briefly for the audience to sing out loud. The
audience can also be required to jump…
Msanii huweza kuishirikisha hadhira yake katika uimbaji au kwa kuitikia kwa kuielekezea kipaza
sauti, au anaweza kuisimamisha sidii kwa muda mfupi ili hadhira ishiriki kuimba. Pia hadhira
inaweza kutakiwa kucheza... (Tafsiri yetu).
80
Hapa Omari alikuwa anazungumzia jinsi wasanii wa Bongo Fleva wanavyoishirikisha hadhira yao
katika maonyesho ya moja kwa moja (live performance).
(iv) Mavazi katika Utendaji wa Ushairi wa Bongo Fleva
Kipengele kingine muhimu katika ushairi wa Bongo Fleva ni mavazi. Suala la mavazi katika
ushairi wa Bongo Fleva ni jambo ambalo limezua utata mkubwa. Omari (2009:60-62) anaeleza
kwamba muziki wa Bongo Fleva umekuja na mavazi ya aina yake. Hapa anaibua dai kwamba muziki
huu una mavazi maalumu. Anaendelea kudai kwamba, kwa kuwa muziki wa Bongo Fleva unahusisha
zaidi vijana, mavazi yanayovaliwa zaidi ni yale yanayovaliwa na vijana. Anayataja mavazi
yanayovaliwa katika muziki wa Bongo Fleva kuwa ni pamoja na mavazi yanayofanana na yale
yanayovaliwa na wana Hip hop wa Kimarekani. Kwa mujibu wa Omari, mavazi hayo ni yale yenye
nembo mbalimbali kama vile FUBU (For Us By Us), Calvin Clein (CK), Timberland na kadhalika.
Mavazi hayo pia yanajumuisha makoti makubwa na makoti mazito bila kujali hali ya joto iliyopo nchini
Tanzania (Omari, 2009:61). Mavazi mengine yanayovaliwa na wanamuziki wa Bongo Fleva ni suruali
pana za jeans, mashati makubwa, mikufu, hereni, saa kubwa za mkononi, mavazi ya kijeshi, viatu
vikubwa na kadhalika. Zaidi ya mavazi hayo ya kuiga, Omari (2009:65) anabainisha kwamba wapo pia
baadhi ya wasanii ambao huvaa mavazi asilia ya Kitanzania. Anatoa mfano wa wasanii hao kuwa ni
Mr. Ebbo ambaye anavaa mavazi ya Kimasai. Msanii mwingine anayevaa mavazi ya asili ni Mrisho
Mpoto a.k.a Mjomba.
Ingawa imeelezwa kwamba muziki wa Bongo Fleva una mavazi maalumu, hata hivyo, suala
hilo lilikuwa muhimu wakati muziki huu unaanza. Wakati huo wanamuziki wa Bongo Fleva waliiga tu
kutoka nje bila kujua chimbuko la mavazi hayo. Haskins (2000:49) anathibitisha hili kwa kueleza
kwamba wanamuziki wa Bongo Fleva walivaa suruali “mlegezo”17 kutokana na kutojua kwamba uvaaji
huo unatokana na ukweli kwamba wasanii wengi wa Marekani walifungwa jela. Wakiwa magerezani
walivuliwa mikanda na hivyo suruali zao kuanza kushuka mpaka makalioni. Walipotoka jela
walionekana kama “wajanja” na hivyo, ili kujitambulisha kwamba wao ni “wagumu” waliotoka jela,
waliendelea kuvaa mavazi hayo. Baadhi ya wanamuziki wa Bongo Fleva walipobaini hili, uvaaji wa
aina hii ulipungua kutokana na ukweli kwamba kwenda jela si suala la kujivunia nchini Tanzania na
katika nchi nyingine za Afrika Mashariki. Ukweli huu unathibitishwa na msanii Black wa Uswazi
ambaye katika mahojiano yetu alisema:
wanamuziki wengi hawakujua kwamba ile style ya kuvaa mlegezo ilianzia gerezani kule
Marekani. Wanamuziki wengi wa Marekani walianza muziki baada ya kupambana na maisha ya
gerezani kwa kuwa walipotoka walionekana wajanja na wagumu. Walivuliwa mikanda ili
wasijiue. Kwa hiyo ilipojulikana hivyo wengi siku hizi wanaona milege (milegezo) siyo dili
(jambo la maana) (ufafanuzi wa kwetu).
Jambo hili linaonesha kwamba mavazi katika muziki wa Bongo Fleva ni jambo linalobadilika
badilika. Hadi sasa bado kuna wanaovaa mavazi hayo, ingawa tunakubali kwamba uvaaji huo
umepungua sana. Pia wapo wanaovaa mavazi mengine kama suti, nguo za kushona na kadhalika. Kwa
upande wa wanamuziki wa kike, wengi wao huvaa mavazi yanayoacha sehemu kubwa ya maungo yao
ya siri nje (nusu uchi) lakini wapo pia wanaovaa mavazi ya kujisitiri japo ni wachache. Katika
mahojiano yetu na baadhi ya wasanii walitueleza kwamba uvaaji huu hulenga kuwavutia wanaume.
Huu ni uthibitisho kwamba kazi za fasihi hubadilika kulingana na mabadiliko mbalimbali ya kisiasa,
kiuchumi, kijamii na kiutamaduni. Kwa ujumla, tunaweza kusema kwamba, muziki wa Bongo Fleva
kwa sasa hauna mavazi maalumu. Kila msanii anavaa anavyojisikia, labda pia kulingana na mahali
anapotumbuiza na hadhira iliyohudhuria.
(v) Vifaa vya Utendaji katika Ushairi wa Bongo Fleva
Vifaa ni kipengele kingine muhimu katika ushairi wa Bongo Fleva. Kuna aina mbili za utendaji
wa ushairi wa Bongo Fleva, utendaji wa kufuatisha (playback) na utendaji wa moja kwa moja (live
17 Mlegezo (au kifupi mlege) huitwa pia katakundu (au kifupi kata K). Huu ni mtindo wa uvaaji ambapo suruali huvaliwa
lakini ikiwa inaacha nusu ya matako nje. Hata hivyo matako hayo huweza kusitiriwa na bukta au chupi ambayo huvaliwa
ndani. Katika mtindo huu wa uvaaji chupi au bukta iliyovaliwa ndani huweza kuonekana.
81
performance). Katika utendaji wa kufuatisha kifaa ambacho msanii anahitaji kuwa nacho ni sidii (CD)
tu iliyorekodiwa nyimbo zake. Waandaaji wa matamasha na maonyesho ndio wana jukumu la kuandaa
vifaa vingine kama vipaza sauti, vicheza sidii (CD Players), spika (speakers), amplifaya (amplifiers) na
vifaa vingine vya aina hiyo. Katika utendaji huu msanii huweka sidii katika kicheza sidii na kisha
kuanza kuimba kwa kufuatisha kuimba wimbo ulioimbwa na sidii (Haskins, 2000:110-115; Omari,
2009:80). Kimsingi, sauti inayosikika katika spika ni ile ya sidii iliyorekodiwa na hivyo msanii
anachofanya ni kuigiza kuimba wakati kiuhalisia sauti yake haisikiki. Utendaji huu ndio asilia na
umetumika kwa muda mrefu zaidi. Katika utendaji huu msanii hakuhitaji wasaidizi wengi katika
utendaji wake, mara nyingi mtendaji alikuwa msanii mwenyewe. Haskins (2000:114) na Omari
(2009:80) wanabainisha kwamba utendaji wa aina hii unaufanya muziki wa Bongo Fleva na Hip hop
kuwa muziki wa gharama ndogo katika uzalishaji na uwasilishaji. Jambo hili ndilo limesababisha kuwa
na idadi kubwa ya wanamuziki wa Bongo Fleva kuliko idadi ya wanamuziki katika miziki kama
taarabu na muziki wa dansi. Aidha, jambo hili ndilo limewafanya wanamuziki wapya wa Bongo Fleva
kuibuka kila siku.
Hata hivyo, kutokana na maendeleo, utendaji wa ushairi wa muziki huu ukabadilika na
kumeibuka utendaji wa moja kwa moja (live performance). Ulianza kwa msanii kutengenezewa mapigo
tu na kuingiza sauti moja kwa moja akiwa jukwaani huku akisaidiwa kucheza na wachezaji (dancers)
na kukua hadi uanzishwaji wa bendi. Katika bendi, msanii/wasanii huwa na vyombo mbalimbali vya
muziki kama vile magitaa, vinanda, tumba, matarumbeta na kadhalika ambavyo hutoa mapigo ya
kimuziki na msanii/wasanii kutia sauti wakiwa jukwaani. Aidha, kunakuwa na wachezaji ambao
wananogesha utendaji huo. Utendaji wa moja kwa moja, kwa hiyo, unahitaji vifaa vingi zaidi kuliko
utendaji wa kufuatisha. Utendaji huu ni ghali na unahitaji uwezo mkubwa kifedha na kimuziki. Ili
msanii aweze kuanzisha bendi atahitaji vifaa na wasanii wa kuvipiga vifaa hivyo. Wasanii hawa
atapaswa kuwalipa mishahara ili waweze kuishi. Hii ni tofauti na utendaji wa awali. Hata hivyo, zaidi
ya gharama, utendaji huu ni bora kwani ushiriki wa hadhira ni mkubwa na pia kuna nafasi ya kufanya
mabadiliko kulingana na mazingira.
(vi) Malipo katika Utendaji wa Ushairi wa Bongo Fleva
Kipengele kingine cha utendaji kitakachojadiliwa hapa ni malipo katika utendaji wa ushairi wa
Bongo Fleva. Muziki wa Bongo Fleva umetoa ajira kwa vijana wengi. Vijana wengi wamejiingiza
katika muziki huu ili kupata kipato cha kuwawezesha kuishi (Mwanjoka, 2011:102-104). Kwa hiyo,
suala la malipo ni suala muhimu sana katika ushairi wa Bongo Fleva. Wasanii wa ushairi huu hughani
au kuimba nyimbo zao ili kujiingizia kipato. Hivyo, sehemu kubwa ya malipo wanayoyapata wasanii
hawa ni fedha. Fedha hizo huwawezesha kununua magari ya kifahari, nguo za gharama kubwa, vidani
vya thamani, pombe, madawa ya kulevya na wanawake (mademu) ambavyo vinaonekana kupendwa
sana na wasanii hawa (Omari, 2009; Mwanjoka, 2011).
Hata hivyo, matumizi haya ya vilevi kama pombe na madawa ya kulevya, katika ushairi wa
Bongo Fleva si kitu kigeni. Tunaona hata katika tanzu nyingine za fasihi simulizi na hasa majigambo ya
jadi mjigambi alikunywa pombe kabla ya kujigamba na baada ya kujigamba aliweza kupewa pombe
kama zawadi kwa ujigambi wake. Aidha, suala la wasanii wa Bongo Fleva kutumia fedha wanazozipata
kutafuta wapenzi si geni kwani hata katika majigambo ya jadi, msanii aliyejigamba vizuri aliweza
kupewa mwanamke (Rubanza, 1994; Mulokozi, 1996; Peek na Kwesi, 2004). Tofauti inayoonekana
hapa ni kwamba katika ushairi wa muziki wa Bongo Fleva wasanii wamesahau kunywa kiasi kidogo tu
ili wasiharibu kazi. Wamesahau Amarwa tigombeka,18 yaani pombe haijengi (Alipo, 2011; Musa,
2011).
Mbali na kupata fedha kama malipo ya utendaji wa ushairi wa Bongo Fleva, kuna unyonyaji
mkubwa katika utoaji wa malipo kwa wasanii wa ushairi huu. Mapromota na watayarishaji wa muziki
huwanyonya wasanii na hivyo wasanii wengi kuwa na hali ngumu kiuchumi (Omari, 2009; Abby na
Billy, 2011; Mwanjoka, 2011). Abby na Billy (2011:9) wakithibitisha hili wanasema:
Last week tulieleza jinsi magwiji wa Bongo Fleva walivyokwama nauli ya kurudi Dar wakitokea
Dodoma…..Inatia uchungu kwa sababu magwiji hao wameshafanya kazi kubwa ambayo ingetosha
18 Huu ni usemi maarufu katika majigambo ya Kihaya ambapo zaidi ya wasanii kupewa zawadi ya pombe, walizingatia
kuwa pombe haijengi. Hivyo walikunywa kiasi kidogo tu.
82
kuwapa utajiri na heshima. Walitakiwa kwenda Dom kwa ndege au wangeendesha magari yao,
ingeshindikana wangekodishiwa basi dogo ambalo lingewapeleka na kuwarudisha. Tukasema
muziki hauwalipi wasanii inavyotakiwa ndio maana hali hiyo ilitokea, kwani magwiji hao
wangepata chambi za kutosha hata mapromota uchwara wasingesogea. Mfano ni huyo wa Dom
(wa Dodoma) ambaye alilipa nauli ya kuwapeleka lakini akakosa ya kuwarudisha kwa sababu eti
geti halikutoa mavuno ya kutosha.
Hapa wanathibitisha hali mbaya za wasanii wa ushairi wa Bongo Fleva kiuchumi hadi kufikia kuwa
ombaomba. Hata hivyo, wanaona hali hiyo mbaya imetokana na wasanii kunyonywa na mapromota,
wasambazaji na watayarishaji wa muziki. Wasanii wenyewe wakihojiwa na Abby na Billy wanamtaja
mmoja wa mapromota kuwa mnyonyaji. Wanasema, “anatufanya tufikirie kazi nyingine wakati muziki
ndio ajira yetu. Sisi ndio tumepigana mpaka huu muziki ukawa biashara, sasa inakuwaje huu unyonyaji
uendelee?”
(vii) Uchezaji wa Ushairi wa Bongo Fleva
Kipengele kingine cha utendaji katika ushairi wa Bongo Fleva tutakachokijadili hapa ni
uchezaji. Ushairi wa Bongo Fleva ni utanzu wa fasihi simulizi. Kwa kuwa matendo ndio msingi wa
fasihi simulizi, kama tulivyoona hapo awali, ushairi huu una uchezaji unaoenda sambamba na matendo
ya mwili. Aidha, kama tulivyoeleza hapo awali, muziki wa Hip hop, ambao hapa tumeuchukua kama
sehemu ya Bongo Fleva, una nguzo zake. Mojawapo ya nguzo hizo ni breakdancing, uchezaji wa
kujinyonganyonga ambao huitwa pia kuruka majoka. Katika mtindo huu mchezaji hujinyonganyonga
mikono na miguu huku akifuatisha mapigo ya muziki husika. Mtindo huu umetumiwa sana na
mwanamuziki maarufu wa Pop duniani, marehemu Michael Jackson. Kwa hiyo, uchezaji ni mojawapo
ya nguzo za muziki wa Bongo Fleva. Zaidi ya mtindo wa kuruka majoka mitindo mbalimbali ya
uchezaji imeibuka ambayo inatumiwa pia na wachezaji wa majigambo haya. Miongoni mwa mitindo
hiyo ni ule mtindo wa kurusha miguu juu na kuipiga chini kwa nguvu, maarufu kama mtindo wa
timbatimba ambao ni mtindo wa kikundi cha TMK Majita (Omari, 2009:82). Mtindo huu ulianzishwa
na wasanii wa TMK Wanaume Halisi na kuigwa na wasanii wengine wa muziki wa Bongo Fleva na
hata miziki mingine ukiwamo muziki wa injili. Kwa mfano, msanii wa muziki wa injili aitwaye Rose
Muhando katika wimbo wa “Nibebe” ametumia mtindo huu wa uchezaji. Mtindo mwingine wa
uchezaji ni ule uitwao mapanga shaa (Omari, 2009:82) unaotumiwa na TMK Wanaume Halisi. Mtindo
huu hasa unahusisha uinuaji wa mikono na kuigiza kukata kama panga linavyokata mti huku mchezaji
akiwa amejikunja kulalia nyuma.
Mtindo mwingine ni ule uitwao kiduku ambao suala la mwanzilishi wake limezua mjadala
mkubwa. Wapo wanaomuona msanii wa Bongo Fleva Malima Lawrence (Marlaw) kuwa ndiye
mwanzilishi huku wengine wakimuona msanii wa taarabu ya mipasho, Mzee Yusufu wa kundi la Jahazi
Modern Taarabu, kuwa ndiye mwanzilishi (Mussa, 2010b; Michuzi, 2010). Marlaw anatajwa kuwa
mwanzilishi kwa kuwa katika wimbo wake wa “Pii pii” ndipo mtindo huu ulipoanza kuonekana kwa
watu wengi nchini Tanzania.
Kwa upande wa Mzee Yusufu anatajwa kuwa mwanzilishi wa kiduku kutokana na ukweli
kwamba, wapenzi wa taarabu ya mipasho, ambao ni wengi karibu sawa na wapenzi wa Bongo Fleva,
walianza kuuona mtindo huu kwa mara ya kwanza katika nyimbo zake. Aidha, uchezaji wa kiduku wa
Mzee Yusufu ndio unaonekana kuwa bora na kuwavutia watu wengi kuliko ule wa Marlaw. Katika
kundi la Jahazi Modern Taarabu kiduku huchezwa kwa mtu kuchuchumaa akitetemesha miguu huku
mikono imewekwa kama mtu aendeshaye pikipiki au baiskeli na huweza kushuka hadi akafikia kukaa
chini. Mtindo huu ni tofauti na ule unaoonekana kwa Marlaw ambapo wachezaji huchuchumaa na
kutetemesha miguu huku mikono ikiwekwa kama mtu anayeendesha pikipiki au baiskeli lakini
mchezaji hachuchumai hadi chini.
Hata hivyo, tunaona kwamba mwanzilishi wa mtindo huu ni mwalimu na uchezaji kutoka THT
(Tanzania House of Talent) aitwaye Msami Giovann. Mtazamo huu mpya unatokana na ukweli
kwamba katika mahojiano yetu na Msami tulibaini kwamba amekuwa akiutumia mtindo huu tangu
mwaka 2004. Alitufahamisha kwamba mtindo huu hapo awali ulikuwa unaitwa kidupu na ulikuwa
unatumiwa sana na wavuta bangi wa Temeke. Neno “kidupu” ni msimu ambao maana yake ni bangi.
Aidha, Msami alitueleza kwamba mtindo huu aliuona ukitumika sana kwenye ngoma ya mnanda,
83
mojawapo ya miziki ya jadi ya Kizaramo. Hivyo, Msami anasema aliupenda mtindo huo na akaanza
kuwafundisha wanafunzi wake. Maelezo haya ya Msami, yanafanana na maelezo tuliyopewa na Profesa
Jay alipokuwa anauzungumzia mtindo huu wa uchezaji. Profesa Jay anasema, “unajua mimi
nimeufuatilia sana mtindo huu wa kiduku na kugundua kwamba ulianzia kwa wahuni wa Temeke
kwenye ngoma za mnanda. Wewe waangalie wacheza mnanda utaona wanacheza staili ya kiduku.”
Vilevile Giovann alitufahamisha kwamba mwaka 2008 alikodiwa na Marlaw, pamoja na wachezaji
wengine wa THT, kwenda kucheza katika rekodi ya wimbo wa “Pii pii.” Ni hapo ndipo walipoutumia
mtindo huo, na tangu hapo Marlaw akatajwa kuwa ndiye mwanzilishi wa mtindo huo. Jambo hili
linawezekana kutokana na ukweli kwamba, nafasi ya wachezaji katika umiliki wa wimbo haijulikani.
Mchezaji hukodiwa na kulipwa kwa uchezaji wake na kisha msanii huwa na haki miliki ya wimbo,
mapigo, uchezaji na kila kitu katika wimbo husika. Hivyo, Marlaw kutajwa kuwa mwanzilishi wa
kiduku si kitu cha ajabu kwani wachezaji katika video yake, huonekana kama sehemu ya Marlaw.
Kuhusu uchezaji wa kiduku, Mussa (2010b:15) anasema:
Kiduku ni aina mpya ya uchezaji iliyoenea kwa kasi hivi sasa hapa nchini, hususan katika
vitongoji vya miji mikubwa kama lilivyo jiji la Dar es Salaam. Katika uchezaji wa staili hii,
mchezaji hulazimika kuchuchumaa huku akiwa kasimamia ncha za vidole vya miguu na kucheza
kwa kujitetemesha kiufundi akifuatisha mapigo ya muziki. Inasemekana chimbuko la uchezaji wa
mtindo wa Kiduku ni wa uchochoroni, kutoka kwa baadhi ya vijana wenye umri mdogo
walioamua kujifurahisha kwa kubuni staili hiyo ya uchezaji. Kutokana na ubunifu huo ulivyokuwa
unavutia wengi, makundi ya kushindana baina ya vijana kwa vijana yalianzishwa kwa wingi
ambako hadi sasa karibu kila mtaa kuna kundi la Kiduku. Unaweza kusema vijana wetu
wameharibika kila utakayebahatika kumfuma akinengua katika kipindi hiki ni lazima atakuwa
ananengua kwa namna hiyo tu. Hata hivyo kwa wale wanaomudu vilivyo kunengua katika staili
hiyo ya Kiduku, huonekana kivutio kikubwa kiasi cha watu hulazimika kuacha kazi zao na
kuwatazama. Kwa hakika ni uchezaji unaoonyesha dhahiri kuwa umejaa chembe za ufundi hasa,
kutokana na namna wachezaji wenyewe wanavyojinogesha kwa maringo ya kutupa mikono yao.
Aidha, mara nyingine wachezaji wa mtindo wa Kiduku hupindisha migongo yao pamoja na
kuyumbishayumbisha nyonga zao kiufundi huku shingo zao nazo zikinepa kistadi.
Hapa Mussa zaidi ya kueleza jinsi kiduku kinavyochezwa na kilivyo maarufu miongoni mwa
Watanzania, anatueleza pia mabadiliko mbalimbali ya uchezaji wa kiduku. Akifafanua juu ya
mabadiliko hayo na tofauti iliyopo katika uchezaji wa kiduku baina ya Marlaw na Mzee Yusufu, Msami
Giovann anasema:
Mimi nilipoanzisha kiduku kilikuwa hakichezwi vile. Bali mtu alikuwa anachuchumaa na
kutetemesha miguu huku ncha za vidole zimegusa chini na mikono kama mwendesha baiskeli.
Staili (mtindo) hiyo ilikuwa haimtaki mchezaji kuchuchumaa hadi chini. Kuchuchumaa hadi chini
ni staili (mtindo) mpya kwa kweli.
Kwa ujumla, uchezaji wa ushairi wa Bongo Fleva upo wa namna nyingi ikiwa ni pamoja na
kukata viuno, kurusha miguu, kuruka majoka (breakdancing), timbatimba, mapanga shaa, kiduku na
kadhalika. Hata hivyo, ipo mitindo mingine ya uchezaji ambayo bado haijapewa jina ingawa ni maarufu
katika uchezaji wa ushairi wa Bongo Fleva. Jambo la msingi hapa ni kwamba uchezaji katika ushairi
wa Bongo Fleva huigiza matendo yanayoimbwa katika wimbo husika. Hivyo tunaweza kusema
kwamba, uchezaji katika ushairi wa Bongo Fleva huhusisha matumizi ya viungo vya mwili kuiga
matendo. Hii ni sifa muhimu sana katika fasihi simulizi (Finnegan, 1970; Rubanza, 1994; Mulokozi,
1996). Ushairi wa Bongo Fleva, kwa hiyo, ni fasihi simulizi.
(viii) Sauti katika Utendaji wa Ushairi wa Bongo Fleva
Kipengele cha mwisho katika utendaji wa ushairi wa Bongo Fleva ni sauti inayotumika katika
utendaji. Mwanjoka (2011:51 -52) anaeleza kwamba ushairi wa Bongo Fleva, hasa ulikuwa ushairi wa
kughani. Lakini kutokana na mabadiliko na maendeleo, kwa sasa, kuna aina mbili za sauti zinazotumika
katika ushairi wa Bongo Fleva, sauti ya kughani na sauti ya kuimba. Hivyo, tunaweza kusema ushairi
wa Bongo Fleva umegawanyika katika makundi mawili, ushairi ulioghanwa na ushairi ulioimbwa.
Ushairi ulioimbwa hutendwa zaidi na wanawake wakati ambapo ushairi unaoghanwa hutendwa zaidi na
wanaume. Wanamuziki wa kike wa Bongo Fleva wanaoghani (wanaorap) ni kama vile Sister P, Zay B,
84
Nakaaya Sumari na Sarah Kaisi (Shaa). Wanamuziki wa kiume wanaoghani ni wengi na hawa ni
pamoja na Mr. 2, Prof. Jay, Joh Makini, Kala Jeremiah, TMK Wanaume Family, Afande Sele na
wengineo. Wapo pia wanamuziki ambao wanaimba na kughani kwa pamoja. Ushairi wa Bongo Fleva
wa kughani ndio ushairi asilia ya Bongo Fleva. Wanamuziki wanaoghani wanajiona wao ndio bora
kuliko wanaoimba na wamewapa wanaoimba jina la utani “wabana pua,” kwa maana ya kwamba ni
watu wasiojua kuimba ila wanachojua ni kubana pua tu ili kutoa sauti ya kuvutia. Ushairi wa Bongo
Fleva unaoimbwa na ule wa mchanganyiko wa kuimba na kughani ni wa hivi karibuni na ndio
umetokea kupendwa sana na kuwa na soko kubwa. Ushairi wa awali wa Bongo Fleva, katika miaka ya
1980 na 1990, ulikuwa unaghanwa. Sauti ya uimbaji mara nyingi ilijitokeza katika kiitikio tu.
Tunaweza kuthibitisha hili katika nyimbo za Mr. 2, Prof. Jay na wasanii wengine waliokuwepo wakati
huo. Suala la msingi hapa ni kwamba, aina ya sauti inayotumika hutumiwa pia katika kuitofautisha
Bongo Fleva na Hip hop. Wanaotumia kigezo hiki cha sauti kuitofautisha Bongo Fleva na Hip hop,
wanadai kwamba muziki wa Bongo Fleva hasa ni muziki unaotumia zaidi sauti ya kuimba wakati
muziki wa Hip hop unatumia zaidi sauti ya kughani (Suriano, 2006; Mwanjoka, 2011).
(c) Mandhari ya Ushairi wa Bongo Fleva
Mbali na vipengele vya utendaji tulivyovijadili, kipengele kingine cha kifani kinachojadiliwa hapa
ni mandhari. Utendaji wa ushairi wa muziki wa kizazi kipya kwa kawaida ni katika kumbi za starehe au
mandhari maalumu iliyoandaliwa kwa ajili ya shughuli hiyo. Katika kumbi hizo, mtazamaji (hadhira)
anapaswa kulipia gharama ya kiingilio mlangoni na ndipo anaweza kushuhudia maonyesho. Miongoni
mwa kumbi hizo jijini Dar es Salaam zinazotumiwa na wasanii hawa ni pamoja na Club Bilicanas, Club
San Sirro, Leaders Club, Maisha Club, Sigara TCC, Equator Grill, Mango Garden, Dar Live, Mango
Garden na kadhalika.
Vilevile muziki huu hutendwa katika hoteli mbalimbali maarufu ambapo wateja wa hoteli hizo
hutumbuizwa wakati wanapata vinywaji na vyakula. Karibu kila hoteli na baa maarufu jijini Dar es
Salaam ina siku maalumu ambapo wasanii wa muziki, wasanii wa Bongo Fleva wakiwamo, hualikwa
na kutoa burudani. Katika burudani hizo, wamiliki wa kumbi husika ndio hulipia maonyesho hayo.
Gharama ya wateja ni kununua kinywaji au chakula tu huku mmiliki wa hoteli au baa akiwalipa wasanii
hao. Kwa mfano, katika baa ya Nyumbani Lounge, Jaydee hutumbuiza kila Jumamosi. Banana Zoro na
Bendi yake ya B-Band hutumbuiza katika ukumbi wa Cine Club kila Jumamosi. Naye Vumilia
hutumbuiza katika ukumbi wa Triz Motel kila Jumapili wakati Top Band imekuwa ikitumbuiza katika
Nyumba ya Sanaa iliyopo karibu na Hotel ya Serena, zamani ilijulikana kama Movenpick, kila
Jumamosi na kadhalika. Hata hivyo, hoteli hizo huweza kubadilisha wasanii au hata siku za kuwaleta
wasanii na hivyo si jambo la kudumu.
Si hivyo tu, bali pia ushairi wa Bongo Fleva hutendwa katika mandhari maalumu ambapo kuna
shughuli maalumu. Kwa kawaida sehemu hizi huwa si mahsusi kwa ajili ya shughuli hiyo ila mandhari
ya muda kwa ajili ya kutenda ushairi huu huandaliwa ili kutimiza jukumu hilo. Baadhi ya sehemu hizo
ni viwanja vya mipira na viwanja vya mikutano na hasa wakati wa mabonanza au mikutano maalumu
ya kisiasa ya kuhamasisha vitu kama mapambano dhidi ya magonjwa kama vile UKIMWI na malaria,
kupiga kura, kuienzi amani na kadhalika. Sehemu hizi ni pamoja na viwanja vya Jangwani, Biafra,
uwanja wa Mwembeyanga, uwanja wa taifa na viwanja vya posta katika jiji la Dar es Salaam. Viwanja
hivyo katika miji mingine ni pamoja na CCM Kirumba (Mwanza), Sokoine (Mbeya), Kaitaba
(Bukoba), Jamhuri (Morogoro), Amri Abedi (Arusha) na kadhalika (Mwanjoka, 2011:94).
Pia mashairi ya ushairi wa muziki wa kizazi kipya hurekodiwa na kuhifadhiwa katika kanda za
kaseti, sidii za kusikiliza (audio CD), sidii za kuona (video CD) na hata kuwekwa kwenye simu kama
mlio wa kuitia (ringtones/caller tones). Vilevile, mashairi haya huhifadhiwa katika nakala tepe na
kupigwa kwenye kompyuta, simu za mkononi, magari na hata redio za kisasa ambapo wasanii hawapati
malipo yoyote ingawa waingizaji wa nyimbo kwenye nakala tepe hupata fedha.
(d) Muundo wa Ushairi wa Bongo Fleva
Kipengele kingine cha kifani ni muundo. Ushairi wa muziki wa kizazi kipya hauna muundo
maalumu isipokuwa tu mashairi mengi huwa na muundo wa kishairi wa kuwa na beti na mistari.
Muundo mwingine unaoonekana katika ushairi wa Bongo Fleva ni wa kuwa na beti na kiitikio chake na
85
pia muundo wa simulio. Katika sehemu hii tutachambua miundo hiyo tukianza na muundo wa beti,
mistari na kiitikio.
(i) Muundo wa Beti, Mistari na Kiitikio katika Ushairi wa Bongo Fleva
Matumizi ya istilahi “mistari” katika fasihi simulizi yameleta mkanganyiko mkubwa.
Wanafasihi wanaona matumizi ya neno hilo ni sahihi katika fasihi andishi na si katika fasihi simulizi.
Wanafasihi wengi akiwamo Mulokozi (2002) hawakubaliani na matumizi ya neno mstari katika ushairi
simulizi kwani katika usimulizi hakuna mistari. Wanafasihi wengine, kama Kunene (1971)
wakapendekeza dhana kikundi-mpumuo (breath group). Naye Mulokozi anapendekeza wakaa
(duration) kama kipimo cha urefu wa ushairi. Hata hivyo, kwa kuwa mashairi mengi ya Bongo Fleva
huandikwa kwanza kabla ya kughanwa, na hata pale yanapoghanwa kabla ya kuandikwa hatimaye
huandikwa, katika andiko hili tunaona matumizi ya istilahi mistari katika ushairi wa Bongo Fleva ni
sahihi. Ushairi wa Bongo Fleva unaonekana kuwa na muundo wa beti zanye mistari kadhaa. Idadi ya
mistari katika kila ubeti itategemea uamuzi wa msanii. Wakati mwingine, idadi ya mistari katika beti za
shairi moja hutofautiana. Aidha, mashairi mengi ya Bongo Fleva huwa na kiitikio. Mfano mzuri wa
mashairi ya aina hii unaonekana katika wimbo uitwao “Veto” ulioimbwa na Mr. 2 ambao una muundo
wa ubeti na mistari.
Ubeti wa 1
1. Nakupa kitu cha Veto
2. Muziki sio wa kitoto
3. Natambaa na beat19 nzito
4. Heshima ya huu muziki tunataka kuirudisha
5. Kwenye hili gemu ndo masela tuliobaki
6. Wengine wengi mafeki
7. Huwa wanachange wakikamata vilaki
8. Sie ni masela na zaidi si ndo mabora
9. Ndo mana tunapata mademu wa viwango bora
10. Niko around kitambo kama migomo ya chuo kikuu ah
11. Tukiacha gemu mnalipeleka pabaya
12. Mpaka mnasababisha tunashindwa kuretire
Ubeti wa II
13. Ni nani rapa wa kwanza kuwa na gari?
14. Wa kwanza kwa kila kitu hata kutoka nchi mbalimbali?
15. Na mpaka leo nipo mkali haya ndo maisha yangu
16. Kimbiza kama unaweza spidi yangu ni ya risasi
17. Mizuka ni ile ile ya Bob Marley
Ubeti III
18. Mi ndo president wa kitambo nishaapa
19. Matatizo ya hili gemu katu siwezi kwepa
20. Kama serikali inavyokwepa ishu ya EPA
21. Hatuogopi kukipaka
22. Hatujali tunachojali ni kuzibana ukweli
Chanzo: Mr. 2 (2009), Veto
Katika wimbo huu tunaona kwamba kuna beti tatu. Ubeti wa kwanza una mistari kumi na mbili wakati
ubeti wa pili na wa tatu ina mistari mitano mitano. Shairi hili halina kiitikio. Mfano mwingine ni shairi
la “Kiburi” lililoimbwa na Mr. 2 akimshirikisha Stara Thomas. Turejelee shairi hilo:
Kibwagizo
Sema mama
Anha hawataki
Kiitikio
Wanachotaka wao wewe upate tabu
Raha kidogo tu chuki bila sababu
19 Beat ni neno linalotumiwa na wasanii wa Bongo Fleva kumaanisha mapigo ya muziki.
86
Ubeti wa 1
1. Najua mama hili nitalikubali eh
2. Kwani najua jeuri dawa yake ni kiburi
3. Kwa wanaonijua tangu enzi za Hemenei
4. Au wakati bado mdogo mama aliponiita Mei
5. Miaka chini ya kumi tu nna jina mkali
6. Kila mtu alinijua mimi ni mtoto wa nani
7. Ni hivyohivyo mpaka walimu shuleni
8. Na ndo mana mpaka leo sishangai mimi kushine
9. Nilipoanza muziki sikujua mafanikio yangeambatana na chuki
10. Mara ngapi nachukua nawaita marafiki
11. Sasa nalala macho wanafiki siwataki
12. Maana kila nnachofanya wanaonekana hawataki
13. Anha na sijali wanachosema baba alinifundisha kutazama mbele daima
14. Na moto ni ule ule tu hakuna wa kuuzima
15. Na najua wanachotaka kuona sugu kachoka ili wapate kucheka
16. Watasubiri watachoka watapanda watashuka
17. Mie nabaki vilevile kila siku kila mwaka
18. Na bado nawakilisha chama la deiwaka
19. Mimi ni fighter nafight bila kuchoka
Rudia Kiitikio
Ubeti wa II
20. Kweli jeuri dawa yake kiburi
21. Nami nitabaki mbishi mpaka nilione kaburi
22. Wako wapi walionicheka shuleni nilipofeli
23. Pilika zangu mtaani zimenifikisha mbali
24. Tisini na tatu nipo boda naitafuta South Africa
25. Na kila ninapotaka naenda zangu Amerika
26. Ndivyo maisha yanavyoweza kuchange
27. Leo nipo na terrano kesho VX or range
28. Na bado nikiwa bar nadai chenji
29. Ah pata picha sugu angekuwa ameshachoka
30. Hakika historia ingekuwa imeshafutika
31. Mabwana wadogo wangeongea kuhusu game wanavyotaka
32. Ningeaibika kama wastaafu wa soka
33. Kumbuka niliacha muziki fan wakasema wamenimiss
34. Nimerudi kwa kishindo wengine wanapata stress
35. Wanabaki tu wanasema
36. Nasema waseme watakavyosema
37. Ndivyo watasema mchana na usiku watalala
38. Na wakiamka asubuhi mi naendeleza bakora
Rudia Kiitikio
Ubeti wa III
39. Maisha yangu yote mimi nimepata sana tabu
40. Nashangaa raha kidogo tu chuki bila sababu
41. Sijawafanya madhambi vipi mnataka nitubu
42. Wanasema nikisema wanasema mi nna gubu
43. Najua bado nipo juu kwenye listi
44. Sina mchezo na life ila siogopi kulost
45. Haya siyo maisha yangu ni masuala
46. Haya ni mambo tu ya hela
47. Siku nikikosa mchuma niko ndani ya daladala
48. Hata kama ni kweli mimi sikuzaliwa Gheto
49. Nimekulia street na nimeshazoea misoto20
50. Hadi ndugu zangu machizi waliniita msela ngoto
51. Na kwa DJ sitoi rushwa za kitoto
52. Hata uendelee kubana hautazuia ndoto
53. Au niende PCB21 niwapelekee za moto
20 Misoto ni msimu unaomaanisha matatizo.
87
54. Kama noma na iwe noma na ikibidi iwe kinoma
55. Bora niache muziki ni kwanini nione huruma
Rudia Kiitikio
Chanzo: Mr. 2 (2009), Veto
Katika shairi hili tunaona pia kuna beti tatu zenye kiitikio cha aina moja, kiitikio bahari. Idadi
ya mistari katika beti inatofautiana. Ubeti wa kwanza una mistari 19 wakati ubeti wa pili una mistari 18
na wa tatu mistari 16. Aidha, shairi hili lina kibwagizo ambapo msanii hughani maneno na kuchombeza
ushairi wake kabla ya shairi lenyewe. Hata hivyo, muundo uliozoeleka zaidi katika ushairi wa Bongo
Fleva ni ya kuwa na beti tatu katika shairi. Mashairi ya beti tatu ndiyo mengi zaidi katika muziki wa
Bongo Fleva kuliko aina nyingine za mashairi. Idadi ya beti hizo hufanya nyimbo husika kuwa si fupi
sana kiasi cha kwisha huku hadhira bado inatamani kuusikiliza na si mrefu sana kiasi cha hadhira
kuchoka kusikiliza.
Muundo huu wa beti, mstari na kiitikio katika Bongo Fleva una dhima ya kulifanya shairi
husika liimbike. Vilevile, huweza kuchochea ushiriki wa hadhira ambapo hadhira huweza kushiriki kwa
kuimba kiitikio. Nacho kiitikio bahari huweza kuwa na dhima ya kusisitiza maudhui.
(ii) Muundo wa Simulio katika Ushairi wa Bongo Fleva
Aina ya pili ya muundo wa ushairi wa Bongo Fleva ni muundo wa simulio. Muundo huu
unaonekana kutokea katika mashairi kama yale yanayoonekana katika wimbo wa “Usiniseme”
ulioimbwa na Ali Kiba. Katika wimbo huo msanii anasimulia matatizo mbalimbali aliyoyapata
kutokana na kula kupita kiasi. Katika ubeti ufuatao anasema:
Kibwagizo
Yo lilele yoyo lilele
Ali K, Ali K, Ali Kiba
Yo lilele yoyo lilele
Kiitikio
Usiniseme x3
Usiniseme kama napenda kula
Usinishangae x3
Usinishangae kama napenda kula
Usiniseme x3
Usiniseme kama napenda kula
Usinitenge x3
Usinitenge kama napenda kula
1.Basi hivi juzijuzi
2.Kulikuwa na shughuli
3.Mtaa wa pili tena si mbali
4.Kulikuwa na pilau na wali
5.Basi mimi nikajiunga
6. Palepale kupiga mpunga
7.Watu wakajipanga
8.Nikaanza kwa tonge na nyama
9.Nina matonge x4
10.Mpaka wakanifukuza
11.Nikasema sijali
12.Nikatoa pesa mfukoni
13.Nikanunua mayai
14.Kilichofuata watu hawakai
Rudia kiitikio
21 PCB ni kifupi cha Taasisi ya Kuzuaia Rushwa (Prevention of Corruption Bureau) kwa sasa inaitwa PCCB, Prevention
and Combating of Corruption Bureau (Tume ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa)
88
15. Ilikuwa Jumapili
16. Siku ya watu wenye ufahari
17. Kujirusha sehemu mbalimbali
18. Nami nikasema leo sikubali
19. Wacha niende x3
20. Ila sina pesa nataka nikale
21. Nikapita sokoni
22. Nikaomba embe sokoni
23. Nikaelekea baharini
24. Nikawaona wengi ufukweni
25. Hakika na embe kiutani
26. Nakula ili watamani
27. Mate yaliwajaa midomoni
28. Basi wote wakaanza kuniomba
29. Usiniombe x3
30. Si unasema mimi napenda kula
Rudia kiitiko
Chanzo: Ali Kiba (2010), Mapenzi Yanarun Dunia
Katika wimbo huu msanii anasimulia jinsi alivyokwenda kwenye shughuli/karamu na kula
kupita kawaida na pia alivyokwenda ufukweni. Masimulizi hayo yote yanalenga kujenga majigambo
yake ya yeye kupenda kula kupita kawaida na anawataka watu wasimseme, kumcheka, kumshangaa
wala kumtenga.
Muundo wa simulio unaonekana pia katika nyimbo nyingine za Bongo Fleva kama vile “Tilalila”
wa Mr. Blue na “Mikasi” wa Mangwea. Katika wimbo wa “Tilalila” Mr. Blue anaimba kwa kusimulia
jinsi alivyokwenda baa na kunywa pombe nyingi kiasi cha kulewa kupita kiasi. Msanii katika wimbo
huo, hachukulii kulewa kuwa kitu kibaya bali anaeleza kwamba baada ya kulewa ndipo alipokuwa jasiri
zaidi na alipoweza kufanya mambo ambayo awali hakuweza. Kwa upande wa wimbo wa “Mikasi,”
msanii anaimba kwa kusimulia jinsi alivyokwenda kupata starehe na marafiki zake hata wakatumia
fedha nyingi. Starehe anazoziimba ni kunywa pombe kupita kiasi, kula na kustarehe na wanawake.
(e) Mtindo wa Ushairi wa Bongo Fleva
Zaidi ya muundo, kipengele kingine cha ushairi wa Bongo Fleva kinachojadiliwa hapa ni mtindo.
Cuddon (1998:872) anabainisha kwamba mtindo unajumuisha vipengele vingi ikiwa ni pamoja na
ujitokezaji wa kazi husika ya kifasihi, uteuzi wa maneno, matumizi ya lugha, tamathali za semi, mbinu
za kisanii, muundo wa sentensi, muundo wa aya na kadhalika. Vipengele tutakavyovieleza katika
sehemu hii ni ujitokezaji wa ushairi wa Bongo Fleva, matumizi ya lugha, tamathali za semi, na mbinu
za kisanii. Kipengele cha kwanza tutakachoanza nacho ni ujitokezaji.
I. Ujitokezaji wa Ushairi wa Bongo Fleva
Ushairi wa Bongo Fleva unajitokeza katika majigambo na majibizano. Majigambo na majibizano
haya huonekana katika namna kuu mbili: majigambo na majibizano katika majina ya wasanii na
majigambo na majibizano katika mashairi yao. Hivyo, tunaweza kusema kwamba kuna ushairi wa
majigambo na majibizano ya majina na majigambo na majibizano ya mashairi. Katika sehemu ifuatayo
tutachambua aina hizi za ujitokezaji tukianza na majigambo na majibizano ya majina.
(i) Majigambo ya Majina katika Ushairi wa Bongo Fleva
Mangesho (2003), Omari (2009), (2010) na (2011) wanabainisha kwamba moja ya mitindo ya
Bongo Fleva ni majigambo katika majina ya wasanii. Omari (2009:56) anabainisha wazi kwamba moja
ya sifa muhimu ya muziki wa Bongo Fleva ni matumizi ya majina ya majigambo, majina ya usanii
kama anavyoyaita. Anaendelea kueleza kwamba mengi ya majina haya yana asili ya lugha ya
Kiingereza na yanafanana sana na yale ya wanamuziki wa Hip hop wa nchi za Ulaya na Marekani.
Anatoa ushahidi wa hili katika wimbo ya Prof. Jay uitwao “Bongo Dar es Salaam.” Anasema:
1. Wabongo wanatamani wangezaliwa Brunei wamwage radhi
2. Mabrothermen majina yao ya asili hawayataki
89
3. Bitozi Nyangema anataka aitwe Tupac
Chanzo: Omari (2009:56)
Majina haya ya majigambo yanatumiwa sana na wasanii kiasi cha majina yao rasmi kutojulikana.
Akithibitisha hili, Mtemwa (2011:17) anabainisha kuwa wasanii hawa huweza hata kuyasahau majina
yao rasmi kutokana na kuzoeleka kuitwa kwa majina haya ya majigambo. Akieleza kuhusu msanii John
Simon kusahau jina lake anasema:
Joh Makini ni kichwa kikali (msanii maarufu) cha Hip hop Bongo (Tanzania). Jina lake halisi ni
John Simon a.k.a Joh Makini. Jamaa mmoja aliwahi kukomaa (kuamua) kumuita John lakini
hakugeuka na alipomuita Joh Makini ndipo akashtuka. Hii inatokana na kulizoea zaidi jina hilo
kuliko John (Ufafanuzi wetu).
Nalo Kitangoma (2011c:22) linashadidia hoja hii kwa kusema kwamba “Mwanaisha Said
Nyange ndio jina lake la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (Jina lake rasmi), ni msanii wa muziki
wa kizazi kipya japo wengi hawalifahamu, lakini kwa jina lake la kujitafutia mkate wa kila siku (jina
lake la majigambo) anaitwa Dayna” (Ufafanuzi wetu).
Hata hivyo, majina ya majigambo katika muziki wa Bongo Fleva hayaishii tu kwa wasanii bali
huendelea hadi kwa watayarishaji wa muziki, studio na hata watangazaji wanaozipiga nyimbo hizi.
Mfano wa majina hayo ni kama TID (Top in Dar), Studio ya Wasafi (Sharobaro Records), Rais wa
Wasafi, Dhahabu Records, Master J Rercords na kadhalika.
Wasanii wanatumia majina haya ya majigambo ili kuonyesha uwezo wa kimuziki walionao na
ili kujiimarisha kimuziki. Jina lina uwezo mkubwa sana katika muziki na sanaa nyinginezo. Prof. Jay
katika wimbo wake wa “Jina Langu” anathibitisha uwezo wa jina anaposema:
1. Jina langu linavuma, kwenye mitaa
2. Jina langu lina uwezo wa kisupastaa
3. Jina langu linaongeza idadi ya maadui
4. Wengine nawatambua wengine siwatambui
5. Jina langu
Chanzo: Prof. Jay (2003), Mapinduzi Halisi
Majina ya majigambo, au majina ya utani kama yanavyoitwa na wengine, katika fasihi hujulikana
kama lakabu na kwa kawaida huwakilishwa kwa herufi A.K.A, yaani “Anajulikana Kama” (Also
Known As) au P.H.K yaani “Pia Hujulikana Kama.” Mulokozi (1996:42) anafasili lakabu kuwa “ni
majina ya kupanga ambayo baadhi ya watu hupewa au hujipatia kutokana na sifa zao za kimwili,
kinasaba, kitabia au kimatendo.” Mwanjoka (2011:14) anaeleza kwamba majina ya majigambo, lakabu,
ya wasanii wa Bongo Fleva yanaonesha mahali atokapo msanii, uwezo wake kimuziki na kadhalika.
Kwa ujumla, majigambo ya majina yanayopatikana katika ushairi wa Bongo Fleva yana nduni
mbalimbali za kimaudhui na kifani.
Tukianza na nduni za kimaudhui, tunaona kwamba majina ya majigambo ya wasanii wa Bongo
Fleva yanaweza kuwa ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na hata kiutamaduni. Miongoni mwa maudhui hayo
ni kama vile utawala na uongozi, utajiri, usomi na heshima. Majina ya majigambo ya Bongo Fleva
yanayobeba maudhui mbalimbali ya kisiasa ni kama yale yanayoonyesha uwezo wa kiutawala. Majina
ya kiutawala kama vile chifu (chief), mfalme (king) na rais (president) yametumika sana katika
majigambo ya majina. Miongoni mwa wanamuziki wanaotumia majina haya ya kiutawala ni pamoja na
mwanamuziki wa kikundi cha kwanza cha muziki wa Hip hop Tanzania, Kwanza Unit¸ Ramadhan
Mponjika ambaye anajulikana kama Chief Rhymson. Wengine ni Anselm Ngaiza anayejulikana kama
Chief Rumanyika na Abubakar Katwila aliyejulikana kama Q. Chief. Wengine ni pamoja na John
Simon Mseke ambaye anajulikana pia kama Mfalme wa Kaskazini na pia mtayarishaji wa muziki wa
Bongo Fleva na promota maarufu Mohamed Abdallah Kiumbe anayejulikana kama Chief Kiumbe
ambaye ni mmiliki wa kampuni ya burudani iitwayo Respect Entertainment. Wengine ni Abdul Nasibu
anayejulikana pia kama Rais wa wasafi na Raheem Nanji anayejulikana pia kama Rais wa
Masharobaro.
Wasanii na watayarishaji wa muziki wanajitambulisha kwa majina ya mkondo huo, kuonyesha
uwezo wa kiuongozi walionao. Wanajitambulisha kwamba katika muziki wa Bongo Fleva, wao ni
watawala wanaowatawala watu wengine (wanamuziki na watayarishaji wengine) (Omari, 2010:4).
90
Tumeeleza hapo awali kuwa machifu ni viongozi wa asili katika jamii nyingi za Kiafrika ambao
walikuwa wanaongoza koo na makabila mbalimbali (Koponen, 1988 na 1995). Aidha, wafalme na
malkia ni watawala wa kijadi katika nchi mbalimbali duniani. Tumetoa mfano wa nchi kama
Uingereza, Saudi Arabia na Jordan ambazo bado zina viongozi wanaotumia vyeo hivyo.
Vilevile, wapo wasanii wa Bongo Fleva wanaojitambulisha kwa majina ya kijeshi. Jeshi ni moja
ya nguzo muhimu ya kiutawala ambayo inatumika kuendeleza tawala mbalimbali. Zipo dola nyingi za
Kiafrika zilizoibuka kutokana na kuwa na jeshi imara (Koponen, 1988; 1995). Kuwa na jeshi dhaifu
kunaweza kusababisha kuanguka kwa utawala (Koponen, 1988:191). Hivyo, watawala katika jamii
mbalimbali na katika vipindi mbalimbali, wamekuwa wakiwaheshimu sana wanajeshi. Wasanii wa
Bongo Fleva wanatumia majina ya kijeshi ili kuonyesha uwezo walionao katika vita (ushindani wa
kimuziki) na pia heshima waliyonayo katika jamii. Kama tulivyotaja hapo awali, miongoni mwa
wanamuziki wanaotumia majina haya ya kijeshi ni pamoja na Afande Sele (Selemani Msindi),
Commander Mullah (Karama Masoud), Inspector Haroun (Haroun Kahena) na Komandoo (Judith
Wambura). Matumizi ya majina haya, yanatupa picha kuwa katika muziki wa Bongo Fleva kuna vita
(ushindani mkubwa) na hivyo ili kuweza kumudu ushindani huo, msanii inampasa kuwa imara kama
mwanajeshi alivyo imara vitani (Omari, 2010, 2011; Mwanjoka, 2011).
Aidha, yapo majina kama “gaidi” na mheshimiwa ambayo yanabeba dhamira ya kisiasa. Katika
miaka ya mwishoni ya 1990 kuliibuka wimbi kubwa la “ugaidi” duniani likiongozwa na Osama bin
Laden na mtandao wa al-Qaeda. Magaidi hawa wameongoza vita dhidi ya nchi za Magharibi na
washirika wao na kusababisha maafa makubwa ikiwa ni pamoja na vifo vingi. Tunakumbuka jinsi
“magaidi” walivyolipua jengo la World Trade Centre na Pentagon nchini Marekani tarehe 11/9/2001,
na treni iendayo kasi Uingereza na Hispania na kadhalika. “Magaidi,” kwa hiyo, wanatambulika kwa
kutokuwa na huruma kwa yeyote. Hivyo, msanii kama Zainab Lupangule anapojiita Mwanadada Gaidi
anamaanisha kwamba yeye ni zaidi ya askari na kwamba hana huruma katika vita vya ushindani wa
kimuziki vinavyoendelea. Nalo jina la Mheshimiwa ni jina linalowakilisha kada fulani ya kisiasa kama
vile mbunge, waziri au Rais. Kwa hiyo, kwa wasanii kujitambulisha kuwa waheshimiwa,
wanajitambulisha kwamba ni wanamuziki wa ngazi za juu. Nchini Tanzania, na katika nchi nyingi za
Afrika Mashariki, wanasiasa wanaongoza kwa kulipwa zaidi na hivyo kufanya watu wengi kuacha kazi
zao na kujiingiza katika siasa ili kupata faida kubwa zaidi. Mfano mzuri wa wasanii wanaotumia jina
hili la mheshimiwa ni pamoja na Amani Temba a.k.a Mheshimiwa Temba.
Mbali na maudhui ya kisiasa, majigambo ya majina pia yanabeba maudhui ya kiuchumi.
Wajigambi wanajitambulisha kwamba ni matajiri, watu wa thamani, wenye uchumi uliotengemaa na
wenye uwezo mkubwa kiuchumi. Mfano wa wasanii wanaotumia majina yenye maudhui ya kiuchumi
ni pamoja na Naseeb Abdul anayejulikana kama Diamond (Almasi), Mwingereza Athumani
Mwingereza anayejulikana kama Tanzanite (Tanzanaiti) na Joseph Raymond anayejulikana kama Black
Rhino (Kifaru Mweusi). Almasi ni madini ya thamani sana duniani. Nayo Tanzanaiti ni madini ya
thamani ambayo hupatikana katika nchi ya Tanzania tu. Aidha, kifaru mweusi, zaidi ya nguvu zake, ni
mnyama wa thamani ambaye anatajwa kuwa adimu sana duniani. Hivyo, wasanii hawa kujitambulisha
kwa majina hayo, wanaonyesha kwamba wao ni watu wa thamani sana na adimu duniani.
Wanaonyesha jinsi walivyo ghali katika kukodiwa na uwezo mkubwa wa kiuchumi walionao.
Aidha, yapo majigambo ya majina yanayobeba maudhui ya kijamii. Kwa mfano, tunaona
wasanii wakijitambulisha kwa majina ya kisomi, yanayoonyesha uwezo wa kitaaluma, kama vile
Daktari (yaani daktari wa falsafa), profesa na mwanafalsafa. Majina haya yanaonekana kwa
wanamuziki John Simba (Doctor John), Hemed Suleiman (PhD, yaani Daktari wa Falsafa), Joseph
Haule (Profesa Jay) na Hamisi Mwinjuma (Mwana FA, yaani mwanafalsafa). Madaktari, maprofesa na
wanafalsafa ni watu wanaoheshimika katika jamii kutokana na ujuzi walionao. Hivyo, wasanii
kujitambulisha kwa majina haya wanataka jamii iwatambue na kuwaheshimu kama inavyowatambua na
kuwaheshimu madaktari, maprofesa na wanafalsafa.
Si hivyo tu, bali pia kuna matumizi ya majina kama CPWAA/C.P, yaani Critical Personmkosoaji
(Illunga Khalifa) na Babu (Haroun Kahena) ambayo pia yanabeba maudhui ya kijamii.
Critical Person ni mtu anayeogopwa katika jamii kutokana na uwezo wake wa kukosoa. Aidha, Babu ni
mtu anayeheshimika kutokana na hekima na busara alizonazo. Katika jamii mbalimbali kuna methali
nyingi zinazowataka watu kuwaheshimu watu wakubwa, kama mababu na mabibi. Kwa mfano,
91
asiyesikia la mkuu huvunjika guu; sikio halizidi kichwa; kuishi kwingi kuona mengi; ukubwa dawa, na
kadhalika. Hivyo, jamii inatambua uzee kuwa chanzo cha hekima na busara. Kwa kujitambulisha kwa
jina la Babu, msanii anataka jamii iamini kwamba yeye ana hekima na busara kama babu alivyo.
Msanii mwingine anayetumia majina ya kizee ni pamoja na Joseph Haule anayeitwa Mzee wa
Mitulinga na Mzee wa Red Carpet; Selemani Msindi anayeitwa Mzee wa Darubini Kali na Abdul
Naseeb anayeitwa Mzee wa Mbagala. Wasanii hawa wamepewa majina hayo kutokana na nyimbo zao
maarufu walizowahi kuzitoa au wenyewe kujitambulisha hivyo. Joseph Haule, kwa mfano, katika
nyimbo zake nyingi anajitambulisha kama J wa Mitulinga, hivyo wanajamii wakampa jina la Mzee wa
Mitulinga. Naye msanii Abdul Nasibu anaitwa hivyo kutokana na wimbo wake maarufu uitwao
“Mbagala.” Selemani Msindi pia anaitwa Mzee wa Darubini Kali kutokana na wimbo wake maarufu wa
“Darubini Kali.”
Aina nyingine ya maudhui yabebwayo na majigambo ya majina ya wasanii wa Bongo Fleva ni
maudhui ya kiutamaduni. Majina ya majigambo yanayobeba dhamira ya kiutamaduni ni pamoja na
TMK Wanaume Family, TMK Wanaume Halisi na Kiuno Bila Mfupa. Jamii ya Kitanzania inatambua
nafasi ya juu aliyonayo mwanamume katika jamii. Kutokana na mfumo dume ulioota mizizi katika
jamii jinsia ya kiume huonekana ndiyo bora zaidi ya jinsia ya kike. Mwanamume anaonekana kuwa
mtu shupavu, shujaa, mwenye nguvu na mvumilivu kuliko mwanamke (Mair, 1979; Basow, 1992). Hii
inathibitika hata katika misemo kama vile “jikaze kiume,” “unalia kama mwanamke” na “uanaume
kazi.” Misemo hii inaonyesha kwamba mwanamume anatakiwa awe mvumilivu kwani kuwa
mwanamume si kazi ndogo. Aidha, msemo “mwanamume suruali” kumaanisha mwanamume
asiyekuwa na kitu unaonyesha jinsi jamii inavyotambua wajibu wa mwanamume kutafuta fedha za
kumlisha mwanamke. Mwanamke asiye na kitu haitwi “mwanamke sketi” kutokana na ukweli kwamba
jamii inaamini kwamba mwanamke anapaswa kuhudumiwa. Hivyo, kwa wasanii hawa kujiita
“Wanaume,” wanataka kutambulika kama watu wavumilivu, watafutaji, watu wa hadhi ya juu na
wajasiri. Vilevile kujitambulisha kama “Wanaume halisi,” maana yake ni kwamba wao ni zaidi ya
wanaume wa kawaida. Mtazamo huu wa udume unaonekana pia katika majina kama Baba Violeth
linalotumiwa na Seif Shaban (Matonya), Baba Willy linalotumiwa na Godfrey Tumaini (Dudu Baya) na
Mr. Chocolate linalotumiwa na Raheem Nanji (Bob Junior). Baba ni kiongozi wa familia mwenye
jukumu la kulea familia na kuwarekebisha watoto wanapokosea. Hivyo, kwa kutumia jina hili bila
shaka wasanii wanakusudia kujitambulisha kwamba wao ndiyo viongozi wa wasanii wengine wa
Bongo Fleva na kwamba wanapaswa kujifunza muziki kwao.
Nalo jina la Kiuno Bila Mfupa ni jina linaloonyesha jamii inavyopendelea wanawake wanaojua
kukata viuno. Katika jamii nyingi za Kitanzania, kukata viuno ni ishara ya umahiri katika tendo la ndoa.
Jamii mbalimbali huwapeleka watoto wao wa kike wa umri fulani unyagoni ili wafundishwe mambo
mbalimbali ya kinyumba, ikiwa ni pamoja na kukata viuno. Pia kuna ngoma kama msondo na sindimba
ambazo hutumiwa kuwafundisha wanawake kukata viuno. Aidha, katika jamii mbalimbali kuna mila ya
wanawake kuwekwa ndani na kufundwa kabla ya kuolewa. Miongoni mwa mambo wanayofundishwa
ni pamoja na kumridhisha mume katika tendo la ndoa na hasa kukata viuno (Mosha, 2010). Hivyo,
kukata viuno ni suala muhimu katika tendo la ndoa. Kwa hiyo, Rehema Chalamila anapojitambulisha
kama Kiuno Bila Mfupa, anajitambulisha kwamba yeye ni mtu aliyehitimu katika mafunzo ya kimila ya
kukata viuno.
Mbali na nduni za kimaudhui za majigambo ya majina, majigambo hayo yana nduni za kifani
pia. Katika kipengele hiki tutawasilisha nduni hizo za kifani. Nduni hizo zimegawanywa katika
vipengele kama vile utungaji, utendaji, wahusika, muundo, mtindo, matumizi ya lugha na kadhalika.
Tuanze kwa kuchambua kipengele cha utungaji wa majigambo ya majina.
· Utungaji wa Majigambo ya Majina
Majigambo ya majina au lakabu kama anavyoyaita Mulokozi (1996:42), huweza kutungwa na
mhusika mwenyewe au mhusika kupewa jina hilo na wanajamii kulingana na sifa zake. Majigambo ya
majina ya wasanii wa Bongo Fleva yanathibitisha maelezo hayo ya Mulokozi kwani nayo hutungwa
kwa namna mbili. Kwanza, msanii mwenyewe huweza kujipa jina, na pili msanii huweza kupewa jina
na wanajamii wanaomzunguka. Alipo (2011:4-7) akithibitisha uwezekano wa mwanamuziki kujipa jina
mwenyewe anasema:
92
...mwenyewe anajiita ‘Heavyweight Mc wa Bongo flava’ Professor Jay ameshinda mtihani wa
kukaa kwenye game la Bongo Flava (muziki wa Bongo Fleva) kwa zaidi ya miaka 10. Prof. Jay
anaweza kuwa mwanamuziki pekee aliyeweza kupindua muono kuhusu muziki huo kwa nyimbo
zake zilizokwenda shule (zilizo bora) kama ‘Bongo Dar es Salaam’ na ‘Ndiyo mzee’ (Msisitizo na
Ufafanuzi ni wetu).
Hapa mwandishi anatambua jina mojawapo la majigambo la msanii Joseph Haule ni Prof. Jay. Hata
hivyo, anatudokeza kwamba mwenyewe anajiita pia “Heavyweight Mc wa Bongoflava.” Jina hili
msanii mwenyewe amejipa ili kujitofautisha na wasanii wengine. Katika jina hilo anajigamba kwamba
yeye ni mshereheshaji (MC) mkuu katika muziki wa Bongo Fleva.
Aidha, Kitangoma (2011b:20) nalo linatupa mfano mwingine wa msanii aliyejipa mwenyewe
jina la majigambo. Linamnukuu msanii Abbas Hamisi (a.k.a Twenty Percent), anasema:
...jina langu halisi ni Abbas Hamis......Hili jina la Twenty Percent nililipata kutokana tu na jinsi
mimi mwenyewe nilivyokuwa najiona (nimejipa mimi mwenyewe kwa jinsi nilivyojiona). Hata
wewe mwenyewe kama utabahatika kusimama na mimi, utajua mimi kweli ni Twenty Percent
kutokana na kimo na maumbile. Halafu pili mimi najitambua kama Twenty Percent kimatendo
kwa sababu, tofauti na labda watu wengine mashuhuri au matajiri duniani ambao wanaishi kwa
kutegemea utajiri waliourithi au akili nyingi walizopewa na Mungu na mambo kama hayo, mimi
natumia akili yangu ndogo kuishi na kufanya mambo yangu kitu ambacho mimi nakiona ni
Twenty Percent, yaani kulinganisha akili yangu na labda za wale manabii wa hapo zamani
(Ufafanuzi wetu).
Hapa tunaona msanii mwenyewe anathibitisha kwamba jina alijipa mwenyewe.
Akizungumzia uwezekano wa msanii kupewa jina na wanajamii, msanii Adili Nkwera a.k.a
Hisabati alipokuwa akihojiwa katika Samwel (2012a) alisema, “Jina la Hisabati nilipewa na mashabiki
kwa kuwa waliona nyimbo zangu zinatungwa kimahesabu zaidi tofauti na wanamuziki wengine.
Nyimbo zangu zina viwango vya hali ya juu.” Naye Profesa Jay akielezea jinsi alivyopewa jina hilo na
wanajamii, alieleza kwamba jina la Prof. Jay alipewa kupitia kipindi cha Radio One ambacho DJ
Dilinga alikuwa anakiongoza. Kupitia kipindi hicho Prof. Jay aliufahamisha umma kwamba anataka
kubadilisha jina la Nigga J na akawaomba wanajamii wampe jina jingine. Hapo ndipo alipopewa jina la
Profesa Jay. Wazo la wasanii wa Bongo Fleva kupewa jina na wanajamii linathibitishwa pia na
Mwanjoka (2011:14) anaposema, “pia wapo waliotungiwa majina na watu kutokana na tabia zao au
aina yao ya kughani...”
· Muundo wa Majigambo ya Majina
Kipengele kingine cha kifani cha majigambo ya majina ya wasanii wa Bongo Fleva ni muundo.
Majigambo ya majina yana miundo mbalimbali. Mulokozi (1996:42) akifafanua hili anasema kwamba,
“Lakabu ni majina ya kupanga...majina haya huwa ni maneno au mafungu ya maneno...” Hapa
Mulokozi anatudokeza kuwa majina ya majigambo huweza kuwa neno moja au fungu la maneno (kirai,
kishazi na hata sentensi). Hivyo, majina ya majigambo ya Bongo Fleva yana miundo ya neno, kirai,
kishazi na sentensi. Tukianza na majina yenye muundo wa neno moja tunaona majina kama Babu,
Inspector, yaani Inspekta (Haroun Kahena), Diamond, yaani Almasi (Abdul Naseeb), Mfalme (Afande
Sele), Komandoo (Judith Wambura), Mkoloni (Fredrick Mariki) na Sugu (Joseph Mbilinyi).
Kwa upande wa majina yenye muundo wa kirai ni pamoja na TMK Wanaume Halisi, TMK
Wanaume Family, Wachuja Nafaka na Wagosi wa Kaya. Mengine ni Heavyweight MC, Mzee wa
Mitulinga (Joseph Haule), Komando Binti Machozi (Judith Wambura), Mwanadada Gaidi (Zainabu
Lupangule), Mzee wa Misifa (Abdul Sykes) na Kiuno Bila Mfupa (Rehema Chalamila). Aidha, kuhusu
majina ya watayarishaji wa muziki na studio yenye muundo huu ni Master J (Joseph Kimario),
Dhahabu Records (Dully Sykes Records) na Wasafi Records (Sharobaro Records/Raheem Nanji
Rummy Records). Majina yenye muundo wa vishazi na sentensi ni pamoja na jina la Gerald Mwanjoka
anayetumia jina la G SOLO ambalo kwenye jalada la kitabu cha Mwanjoka (2011) anafafanua kuwa ni
kifupi cha vishazi na sentensi zifuatazo: G ni Gerald, S ni Saying, O ni On, L ni Lyrics na O ni Only,
yaani Gerald is Saying On Lyrics Only. Sentensi hii, ingawa inatumia Kiingereza kisicho sahihi,
inamaanisha kuwa Gerald anaongea kupitia mashairi tu. Jina jingine lenye muundo wa sentensi ni Jay
Tunakuzimia linalotumiwa pia na Joseph Haule (Prof. Jay).
93
· Mtindo wa Majigambo ya Majina
Mbali na muundo, kipengele kingine cha kifani ni mtindo. Kama tulivyoeleza hapo awali, mtindo
unajumuisha vipengele vingi. Vipengele vya mtindo vya majigambo ya majina tutakavyovijadili hapa
ni pamoja na matumizi ya mafumbo, taswira na ishara, matumizi ya lugha na tamathali za semi.
Tukianza na matumizi ya mafumbo, ishara na taswira tunabaini kwamba huu ndio mtindo muhimu
uliotumika katika majina ya majigambo. Majina kama vile Afande Sele (Selemani Msindi),
Commander Mullah (Karama Masoud), Inspector Haroun (Haroun Kahena) na Komandoo (Judith
Wambura) ni majina ya kijeshi ambayo yanakusudia kutujengea taswira ya uaskari na kuihusisha na
muziki wa Bongo Fleva. Majina hayo yanatupa taswira kuwa katika ushairi wa Bongo Fleva, wasanii
husika ni mahiri kama walivyo mainspekta, makomandoo na makamanda katika jeshi. Omari (2010:4)
akifafanua hili anasema kwamba sitiari ya majina ya kijeshi inatumiwa na wasanii hawa ili kusawiri
(taswira ya) nguvu za kimwili walizonazo wanajeshi. Omari anafafanua kwamba nguvu hizi zinaashiria
wasanii husika wana uwezo wa kuhimili mikikimikiki ya ushindani katika soko la muziki kama
wanajeshi wanavyoweza kuhimili mikikimikiki ya vita.
Mfano mwingine, ni majina ya kiutawala kama vile chifu, mfalme na malkia. Miongoni mwa
wanamuziki wa mkondo huu ni pamoja na mwanamuziki wa kikundi cha kwanza cha muziki wa Hip
hop Tanzania, Kwanza Unit¸ Ramadhan Mponjika ambaye alijulikana kama Chief Rhymson, Anselm
Ngaiza aliyejulikana kama Chief Rumanyika na Abubakar Katwila aliyejulikana kama Q. Chief.
Wengine ni pamoja na John Simon ambaye anajulikana kama Mfalme wa Kaskazini na wengineo.
Kama ilivyo kwa majina tuliyoyaeleza hapo awali, haya pia ni ya kitaswira. Majina haya yanaonesha
majigambo kwa njia ya taswira. Omari (2010:4-5), anasema kuwa wasanii wa Bongo Fleva wanatumia
majina haya ili kujitambulisha kwamba wao ni watawala katika muziki huu na wanamuziki wengine ni
raia wa kawaida katika himaya zao za ufalme.
Zaidi ya majina ya kiutawala, wanamuziki wa Bongo Fleva wanajigamba kwa kutumia majina
yanayoonesha uwezo wa kitaaluma (Omari 2010:6) ambayo pia yana taswira. Majina hayo ni pamoja
na Daktari (yaani, daktari wa falsafa), profesa na mwanafalsafa. Majina haya yanaonekana kwa
wanamuziki John Simba (Doctor John), Hemed Suleiman (PhD), Joseph Haule (Profesa Jay) na Hamisi
Mwinjuma (Mwana FA, yaani mwanafalsafa). Omari (khj.) anaeleza kwamba wasanii hawa walitumia
majina haya ili kujitambulisha kwamba ni watu wenye ujuzi wa kutosha katika muziki kama madaktari,
maprofesa na wanafalsafa walivyo na ujuzi mwingi katika taaluma zao. Majina haya yanatuchorea
akilini taswira ya madaktari, maprofesa na wanafalsafa kitaaluma na kuwafananisha na wao.
Aidha, aina nyingine ya majina ya majigambo yanayotumiwa na wasanii wa majigambo ya Bongo
Fleva ni yale yanayoonesha vitu vya thamani katika jamii. Mfano mzuri ni majina kama Naseeb Abdul
anayejulikana kama Almasi (Diamond), Mwingereza Athumani Mwingereza anayejulikana kama
Tanzanaiti (Tanzanite) na Joseph Raymond anayejulikana kama Kifaru Mweusi (Black Rhino). Majina
haya yanatupa taswira ya madini hayo ya thamani na mnyama huyo adimu na kutufanya tuvilingishe na
nyimbo na uwezo wa wasanii husika.
Vilevile, yapo majina ya majigambo yanayotupa taswira ya watu wa kada bora katika jamii.
Miongoni mwa majina hayo ni pamoja na Mheshimiwa Temba, CPWAA/ C.P Critical Person (Illunga
Khalifa) na Babu (Haroun Kahena) kama tulivyokwishaona. Jina la C.P (Critical Person)
linamtambulisha msanii huyu kama mkosoaji na hasa katika mambo yasiyokubalika katika jamii.
Majina mengine ya mkondo huu ni pamoja na jina la Babu linalotumiwa na msanii Haroun Kahena.
Babu ni mzee anayeheshimika katika jamii.
Aidha, kama inavyoelezwa na wataalamu, majigambo yana pande mbili - kusifia na kukashifu (taz.
Rubanza, 1994; Mulokozi, 1996; Samwel, 2012a). Hivyo, zaidi ya majina ya majigambo yanayochora
taswira nzuri ya kusifia, yapo majina yenye kuchora taswira mbaya, inayokashifu. Majina hayo
yanaonekana kubeba taswira mbaya lakini ikiwakilisha uzuri. Miongoni mwa majina ya majigambo ya
mkondo huo ni pamoja na Mzungu Kichaa (Espen Sorensen), Matonya22 (Seif Shaaban), MB Dog
(Mohamed Ali), Dudu Baya (Godfrey Tumaini), Mwanadada Gaidi (Zainabu Lupangule), Crazy G.K.
22 Matonya ni ombaomba maarufu sana aliyepata kuvuma nchini Tanzania miaka ya 2000. Ombaomba huyu, zaidi ya
kurudishwa kwao Dodoma mara kadhaa, alirudi tena Dar es Salaam na kuendelea na kazi yake ya kuombaomba barabarani.
Kazi ya kuombaomba barabarani ni kazi inayodharauliwa sana na ombaomba huonekana kuwa watu duni. Hivyo, msanii
kujiita jina hilo ni namna fulani ya kujikashifu kama upande wa pili wa majigambo yake.
94
(Gwamaka Kihaula) na Mchizi Mox (Taikun Ali). Majina haya kwa hakika hayana sifa nzuri katika
jamii. Jina kama “Kichaa” si zuri, linawakilisha mtu asiyekuwa na akili timamu. Nalo jina la
“Matonya” ni la ombaomba mashuhuri ambaye alikuwa akiomba katika jiji la Dar es Salaam, wakati
MB Dog lina jina “dog’ ambalo lina maana ya mbwa. “Dudu Baya” ni jina linalotupa taswira ya
kiumbe kisichopendeza, kiumbe chenye ubaya wa sura na/au matendo. Nalo jina “mchizi” halina tofauti
na neno kichaa tulilolieleza hapo awali. Majina haya yanatuchorea taswira mbaya kichwani kuwakilisha
kitu kizuri. Majina haya yanatuonyesha upande wa pili wa majigambo, upande wa kukashifu. Zaidi ya
kusifia, majigambo pia huweza kukashifu (Hodza na Fortune, 1979; Rubanza, 1994; Mulokozi, 1996;
na Peek na Kwesi, 2004). Matumizi ya majina haya ya kukashifu yanaonyesha uasi au athari za kigeni.
Kipengele kingine cha kimtindo katika majigambo ya majina ni matumizi ya lugha. Kwa kiasi
kikubwa, majigambo ya majina yanatumia lugha ya Kiswahili. Miongoni mwa majigambo ya majina ya
wasanii wa Bongo Fleva yanayotumia lugha ya Kiswahili ni pamoja na majina kama Mwanadada
Gaidi, Kiuno Bila Mfupa, Komandoo, Afande Sele, Sam wa Ukweli, Mzee wa Mitulinga, Binti
Machozi, Mchizi Mox, Sugu na Kamanda Mullah. Akizungumzia matumizi ya majina ya majigambo ya
Kiswahili, Mangesho kama anavyonukuliwa na Omari (2009:57) anasema kwamba matumizi haya
yanatokana na majina ya lugha ya Kiingereza yaliyotumika hapo awali kuonekana hayana mantiki
katika muktadha wa Kitanzania. Maelezo haya yanatupa picha kwamba majina ya lugha ya Kiingereza
ndiyo yalianza kutumika. Lakini majina hayo yakabadilika na wasanii wakaanza kutumia majina ya
Kiswahili. Miongoni mwa majina ya majigambo yanayotumia lugha ya Kiingereza ni kama vile King
Crazy G.K., Mr. Ebbo, Mr. Blue, Heavyweight MC, G SOLO (Gerald is Saying On Lyrics Only) na
TID (Top In Dar). Matumizi haya ya majina ya Kiingereza yalianza sambamba na kuibuka kwa muziki
huu. Omari (2009) anaeleza kwamba katika hatua za mwanzo za muziki wa Bongo Fleva, kulikuwa na
athari kubwa za utamaduni wa nje katika muziki wa Bongo Fleva. Matumizi ya majina ya majigambo
yaliyo katika lugha ya Kiingereza, ni moja ya athari hizo. Lakini athari hizi zinaendelea kupungua kadri
muda unavyopita. Mabadiliko haya ndiyo yamesababisha kuwa na matumizi ya majina ya majigambo
yaliyo katika lugha ya Kiswahili. Chachage (2002) anatoa maelezo ya kina ya athari za utamaduni wa
nje, ikiwamo athari ya matumizi ya lugha ya Kiingereza, katika muziki wa Bongo Fleva. Chachage
(2002) anabainisha kwamba matumizi haya yanatokana na athari za utandawazi na yana nafasi kubwa
katika kuleta mgongano wa kitamaduni.
Zaidi ya matumizi ya majina ya majigambo ya Kiswahili na Kiingereza, kuna majigambo ya majina
ambayo yana asili ya lugha za kikabila za Tanzania. Majina hayo ni kama vile Wagosi wa Kaya, na
Mnyalu (Michael Mwakatundu ak.a Mike Tee). “Wagosi” ni neno/jina lenye asili ya Kibondei ambalo
linamaanisha “ndugu,” na “mnyalu” ni neno/jina lenye asili ya kabila la Wahehe (Iringa) ambalo
linamaanisha “mwenyeji” (wa Iringa), au mtu wa kabila la Wahehe/ndugu yao. Jina la Wagosi wa Kaya
ni jina la kikundi cha muziki kinachojumuisha wanamuziki kadhaa ambao wanaishi Tanga. Nalo jina la
Mnyalu linatumiwa na msanii aitwaye Mike Tee. Aidha, yapo majina yenye mchanganyiko wa lugha za
makabila na lugha ya Kiingereza. Jina la Chief Rumanyika ni mchanganyiko wa Kiingereza “Chief”
(chifu) na la Kinyambo, “Rumanyika” (mtu mashuhuri, anayejulikana sana).
Mbali na matumizi hayo ya lugha, majigambo ya majina ya wasanii wa Bongo Fleva hutumia pia
tamathali za semi. Kazi za fasihi hutumia tamathali za usemi ili kuweka mkazo katika maana na mtindo
(Cuddon, 1998; Alembi, 1999; Senkoro, 2011). Miongoni mwa tamathali za usemi zilizotumika katika
majigambo ya majina ni pamoja na sitiari, tashihisi na chuku. Katika sehemu hii tutazipitia tamathali
hizi na kuona jinsi zilivyotumika.
· Sitiari katika Majigambo ya Majina
Tukianza na sitiari tunabaini kwamba majigambo ya majina ya wasanii wa Bongo Fleva yametumia
sana tamathali hii. Hii ndiyo mbinu iliyotumika zaidi katika majigambo ya majina ya Bongo Fleva.
Miongoni mwa majina ya kisitiari ni pamoja na Mwamba wa Kaskazini, Diamond, Tanzanite,
Komandoo, Inspector Haroun, Babu na kadhalika. Katika jina la Mwamba wa Kaskazini, msanii
anakusudia kujilinganisha yeye na mwamba. Mwamba ni jiwe imara ambalo kwa kawaida ni gumu
kuvunjika. Mwamba pia huweza kutumika kuviegemeza vitu vingine dhaifu ili navyo viwe imara.
Msanii, kwa hiyo, anajiona kwamba kwa jinsi alivyoiva katika ushairi huo, yeye ni kama tegemeo la
mikoa ya Kaskazini mwa Tanzania. Kwa kiasi kikubwa na kwa kipindi kirefu, wasanii wa muziki wa
95
Bongo Fleva wamekuwa wakitokea Dar es Salaam. Aidha, msanii Diamond, anakusudia kujilinganisha
na almasi. Anajiona kwamba ni mwanamuziki wa thamani na ghali kama ambavyo almasi ilivyo ghali
na ya thamani.
Vivyo hivyo kwa jina la Tanzanite, msanii anajitambulisha si tu kwamba ni msanii ghali na wa
thamani, bali anajitambulisha kwamba ni ghali kiasi ambacho hakuna msanii kama yeye duniani.
Madini ya Tanzanaiti yanapatikana katika nchi ya Tanzania tu duniani kote. Matumizi ya sitiari hii
yanaweza pia kumaanisha kwamba msanii anajitambulisha kwamba ni Mtanzania halisi au
anatambulisha chimbuko lake kuwa ni Tanzania. Nalo jina la Komandoo msanii anajilinganisha na
komandoo wa kijeshi. Komandoo katika jeshi huwa ni askari ambaye zaidi ya kupitia mafunzo ya
kawaida ya askari, yeye hupewa mafunzo ya ziada. Huwa ni askari mwenye uwezo mkubwa sana wa
kijeshi na uvumilivu wa hali ya juu pindi anapokutana na mateso. Marekani baada ya kumtafuta gaidi
wa kimataifa kwa miaka zaidi ya kumi bila mafanikio, waliwatuma makomandoo ambao walifanikiwa
kujua alipo na kumuua tarehe 2/5/2011. Kwa hiyo, kwa Judith Wambura kutumia jina hilo,
anamaaniisha kwamba ameiva sana kwenye muziki wa Bongo Fleva na mvumilivu.
Jina la Inspector Haroun, kwa upande mwingine, linamlinganisha msanii na askari polisi mwenye
nyota moja na kuendelea (afisa wa jeshi la polisi). Askari polisi mwenye cheo kama hicho kwa kawaida
hukaa ofisini na ni mara chache hufanya kazi ngumu wanazofanya askari wengine kama makoplo na
kadhalika. Inspekta wa polisi hawezi kwenda doria, na kama akienda atakuwa msimamizi wa askari
wengine, hawezi kwenda lindoni kulinda mabenki, maofisi na kadhalika. Vilevile, hata malipo
(mshahara) ya inspekta wa polisi hutofautiana na polisi wa vyeo vya chini. Kwa hiyo, kwa
kujitambulisha kama inspekta, Haroun Kahena, alikuwa anajigamba kwamba ni askari (msanii)
anayeheshimika miongoni mwa askari wengine (wanamuziki wengine) na kwamba anafanya kazi
ndogo isiyotoa jasho sana lakini kwa malipo makubwa.
· Tashihisi katika Majigambo ya Majina
Mbali na matumizi ya sitiari, majigambo ya majina yanatumia pia tashihisi. Miongoni mwa majina
ya kitashihisi ni Mwamba wa Kaskazini analolitumia John Simon, Diamond, Tanzanaiti na Mbwa. Ni
wazi kwamba mwamba, madini ya Tanzanaiti, almasi na mbwa haviwezi kuimba wala kuongea. Hivyo,
kwa wanamuziki kujipa majina haya, wanavipa uwezo vitu hivyo kuongea na kutenda kama binadamu.
Tamathali hii ndio huitwa tashihisi (Abram, 1981; Akivaga na Odaga, 1998).
· Chuku katika Majigambo ya Majina
Chuku imetumika pia katika majina ya majigambo yanayotumiwa na wasanii wa muziki wa Bongo
Fleva. Majina ya aina hiyo, ni kama vile Profesa Jay, PhD, yaani Daktari wa Falsafa (Hemedi
Suleiman) na Mwana FA. Majina haya ni ya wataalamu waliobobea katika eneo fulani la kitaaluma.
Lissah (2007:7) anabainisha kwamba wasanii wengi wa Bongo Fleva wameacha shule na kujiingiza
katika muziki huu. Kama hivyo ndivyo, ni wazi kwamba wasanii wengi hawana elimu hii
wanayojinasibisha nayo. Utafiti wa Samwel (2012a) unabainisha kuwa wasanii wengi wa Bongo Fleva
wana elimu ya sekondari na wachache sana wamefikia elimu ya Chuo Kikuu na kupata walau digrii
moja. Miongoni mwa wasanii wenye digrii moja ni Roma, mwanaFA na K-Basil. Utafiti wake, kwa
wakati huo, haukumpata msanii hata mmoja mwenye digrii ya uzamili achilia mbali uzamifu (PhD)
wanayojinasibisha nao. Hivyo, majina wanayoyatumia ya Profesa na Daktari wa Falsafa ni chuku.
· Wahusika wa Majigambo ya Majina
Mbali na vipengele hivyo, kipengele kingine cha majigambo ya majina ya wasanii wa Bongo Fleva
ni wahusika. Wahusika wa majigambo ya majina ni kama wahusika wengine wa kifasihi simulizi.
Kama tulivyodokeza hapo awali, wahusika wa fasihi simulizi huweza kuwa watu, wanyama, miti,
mizimu, mahoka na viumbe wengine wasio binadamu. Kwa hiyo, wahusika wa aina hizo pia ndio
wanaotumika katika majigambo ya majina katika Bongo Fleva. Kwa mfano, katika jina la Chief
Rumanyika mhusika hapo ni mzimu/mtu aliyekufa. Omukama Rumanyika aliyekuwa akiitwa Mfalme
Rumanyika Orugundu alikuwa mtawala wa Karagwe nchini Tanzania kati ya mwaka 1853-1879
(Koponen, 1988; 1995). Kwa msanii huyu kujiita Rumanyika, anajitambulisha kwamba yeye ni
marehemu aliyefufuka. Hivyo ni mzimu wa Mfalme Rumanyika.
96
Pia kuna matumizi ya wahusika wasio binadamu. Kwa mfano, jina la “Mwamba wa Kaskazini” ni
matumizi ya jina la kiumbe asiye binadamu. Majina mengine ni kama Diamond (Almasi), Tanzanite
(Tanzanaiti) na mbwa (Mb Dog na Soggy Doggy). Wahusika wengine ni Vichaa (King Crazy GK,
Mchizi Mox, Mzungu Kichaa) na kadhalika.
· Majigambo ya Majibizano katika Bongo Fleva
Zaidi ya mtindo wa majigambo ya majina, mtindo mwingine wa ushairi wa Bongo Fleva ni
majigambo ya majibizano. Omari (2009:195) anabainisha kwamba majibizano au malumbano ni moja
ya sifa muhimu katika muziki wa Bongo Fleva. Majigambo ya majibizano katika muziki wa Bongo
Fleva yanaonekana katika makundi makuu mawili: majibizano katika majigambo ya majina na
majibizano katika mashairi ya majigambo. Katika sehemu inayofuata tutachambua aina hizo mbili za
majigambo ya majibizano tukianza na majibizano yanayojitokeza katika majina ya majigambo ya
wasanii wa Bongo Fleva.
· Majigambo ya Majibizano katika Majina
Majina ya majigambo ya wasanii wa Bongo Fleva wakati mwingi yamekuwa katika hali ya
majibizano – msanii mmoja anatumia jina fulani ili kumjibu msanii mwingine. Kama tulivyoona hapo
awali, wasanii mbalimbali wa muziki wa Bongo Fleva wanajipa au kupewa majina ili kujitambulisha
kwamba ni watu wenye uwezo kimuziki, wasanii wanaoongoza katika muziki huu, wasanii wenye
kuhimili ushindani katika soko la muziki, wasanii wenye mashairi yenye hekima na busara na sifa
nyinginezo zinazofanana na hizo. Hata hivyo, imekuwa ni kawaida kwa wasanii kutumia majina ili
kujibu sifa aliyojipa au aliyopewa msanii mwingine. Majibizano hayo yapo katika kila mkondo wa jina
la majigambo, yaani tangu majina ya kijeshi, majina yanayoonesha vitu vya thamani, majina
yanayoonesha utawala na kadhalika.
Kwa kuanza na majina ya majigambo ya kijeshi, tunaona wazi kwamba kuna majibizano baina ya
wasanii. Kijeshi cheo cha Inspekta kinatumiwa na askari polisi wenye kuanzia nyota moja hadi tatu.
Hawa ndio huitwa mainspekta. Mwanamuziki Haroun Kahena anatumia jina la Inspector Haroun
kujitambulisha kwamba yeye katika muziki wa kizazi kipya, ni kama askari polisi mwenye nyota
(mwenye cheo). Haroun Kahena hapa anaufananisha muziki wa Bongo Fleva/Hip hop na jeshi la polisi
lenye askari wasio na vyeo, wenye vyeo vya chini na hata wenye vyeo vya juu. Yeye anajitambulisha
kwamba ni askari mwenye nyota – mwenye cheo cha juu na hivyo anapaswa kuheshimiwa na askari
polisi (wanamuziki) wengine.
Kutokana na ukweli kwamba nchini Tanzania majeshi ya ulinzi yanaheshimika zaidi ya majeshi ya
usalama,23wanamuziki wengine wakajitokeza kumjibu Haroun Kahena (Inspector Haroun).
Wanamuziki hao wakaanza kujitambulisha kwa majina ya vyeo vya majeshi ya ulinzi (JKT na JWTZ).
Kwa mfano, mwanamuziki Karama Bakari anajitambulisha kwa jina la Luteni Karama. Cheo cha
Luteni hutumiwa na askari wa majeshi ya ulinzi. Luteni ni askari jeshi mwenye nyota mbili au moja.
Mwenye nyota moja huitwa luteni usu na mwenye nyota mbili huitwa luteni. Ni wazi kwamba Karama
Bakari anajitambulisha kwamba yeye si polisi bali ni mwanajeshi mwenye nyota.
Aidha, wanamuziki wengine wakiongozwa na Karama Masoud wakajitambulisha kwamba wao ni
Kikosi cha Mizinga. Jeshi la Tanzania linagawanyika katika vikosi mbalimbali na vyenye majukumu
tofauti. Kuna kikosi cha anga, kikosi cha majini, kikosi cha mizinga na kadhalika. Wanamuziki hao
wanajitambulisha kuwa ni kikosi cha jeshi lakini si kikosi cha kawaida bali ni kile cha mizinga
ambacho kina mafunzo ya hali ya juu katika kurusha makombora. Kikosi cha mizinga huwa ni
maalumu kwa ajili ya kushambulia ngome ngumu na kujibu mashambulizi ya silaha nzitonzito. Bila
23 Majeshi ya ulinzi nchini Tanzania yanajumuisha JWTZ (Jeshi la Wananchi wa Tanzania) na JKT (Jeshi la Kujenga Taifa).
Majeshi haya yapo chini ya Wizara ya Ulinzi na jukumu lake kuu ni kulinda usalama wa nchi ikiwamo mipaka. Majeshi ya
usalama ni pamoja na polisi – ambalo ni jeshi linaloshughulikia usalama wa raia na mali zao - na jeshi la magereza. Majeshi
haya yapo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Nchini Tanzania majeshi ya usalama yanaheshimika sana machoni
pa raia na hata machoni pa serikali. Wananchi wengi huwaogopa wanajeshi kuliko wanavyowaogopa polisi au askari
magereza. Mara kadhaa wanajeshi wamewapiga polisi kutokana na mwanajeshi mwenzao kukamatwa au kucheleweshwa na
polisi katika foleni pale ambapo askari polisi wanaongoza magari barabarani. Serikali nayo inatoa mishahara mikubwa kwa
wanajeshi kuliko kwa polisi na magereza.
97
shaka kwa kutumia jina la Kikosi cha Mizinga wanajitambulisha kwamba wana uwezo wa kiwango cha
juu kujibu mapigo pale wanaposhambuliwa. Kwa kuwa moja ya sifa ya muziki wa Bongo Fleva ni vita,
au bifu wanachofanya wanamuziki hawa ni kuwatahadharisha wengine kwamba wao wapo tayari
kujibu mashambulizi.
Majibizano hayaishii hapo, wanamuziki wengine wanajitambulisha kwa majina ya vyeo vya juu
zaidi vya kijeshi kuliko Luteni. Bila shaka wakifahamu kwamba Luteni ni mwanajeshi mwenye nyota
moja au mbili, Mwanamuziki Albert Mangwair katika wimbo wake wa Speed 120 Shaa
anajitambulisha kama Meja Jenerali. Meja Jenerali ni cheo cha juu sana katika Jeshi la Tanzania, ni
askari anayekaribia kufikia cheo cha mwisho kijeshi, Jenerali. Anachokifanya Ngwair hapa ni
kujitambulisha kwamba yeye si tu mwanajeshi bali ni mwanajeshi wa cheo cha juu sana. Bila shaka
anakusudia kuonyesha kwamba yupo juu zaidi ya “wanajeshi” wengine katika muziki wa Bongo Fleva.
Hata hivyo, wanamuziki wengine wakitambua mafunzo ya kiwango cha juu ya kijeshi wanayopata
makomandoo, wanajitambulisha kwa majina hayo ili kuwajibu wenzao. Wanamuziki wanaotumia
majina kama hayo ni pamoja na Judith Wambura anayejiita Komandoo na Karama Masoud anayejiita
Kamanda Mullah.
Majibizano hayapo tu katika majina ya majigambo ya kijeshi bali pia katika majina ya majigambo
ya kiutawala. Wanamuziki wengi wa muziki wa Bongo Fleva hapo mwanzo walijitambulisha kwa jina
la Chief/Chifu. Kama tulivyoeleza hapo awali, machifu walikuwa watawala wa Kiafrika waliotawala
jamii za Kiafrika wakiwasaidia wafalme kabla ya ukoloni kuingia. Katika jamii za Kihaya, kwa mfano,
waliitwa bami b’enshozi (Mulokozi, 2002:17). Kwa hiyo, kwa kutumia jina la Chief/Chifu, wanamuziki
hawa wanajitambulisha kama watawala wa muziki wa Bongo Fleva. Miongoni mwa wanamuziki hao ni
pamoja na Ramadhani Mponjika (Chifu Rhymson), Abubakar Katwila (Q. Chief) na Peter Kiwinga
(Chifu Kiwinga). Lakini, Ansleim Tryphone Ngaiza akijua wapo wanamuziki wanaojiita machifu,
akajiita Chifu Rumanyika. Neno “Rumanyika” ni la Kinyambo lenye maana ya “mtu
maarufu/mashuhuri” au “anayefahamika sana.” Hivyo, msanii kwa kulitumia jina hili, zaidi ya mambo
mengine, alikuwa anawajibu “machifu” waliomtangulia kwamba yeye si tu kwamba ni chifu bali pia ni
chifu anayefahamika zaidi yao.
Hata hivyo, baadhi ya machifu katika jamii za Kiafrika walitumiwa na wakoloni, hasa wa
Kiingereza, kuwatawala Waafrika ukoloni ulipoingia (Koponen, 1988 na 1995; Rubanza, 1995; Omari,
2010). Hivyo, machifu wakaonekana mbele ya wengi kama wasaliti. Si hivyo tu bali pia katika nchi
nyingi za Kiafrika baada ya uhuru machifu na watawala wengi wa kijadi walipoteza mamlaka zao za
asili. Badala yake, uchifu ukabaki kuwa jina tu la kiongozi asiye na mamlaka. Hali ilikuwa hivyo pia
nchini Tanzania (Rubanza, 1994). Ili kuwajibu wanamuziki wenzao waliojiita machifu, wanamuziki
wengine walijigamba kwamba wao ni kiboko cha machifu au ni zaidi ya machifu. Msanii Frederick
Mariki anajitambulisha kwa jina la Mkoloni, hii ikiwa na maana kwamba anawatumia machifu
kutawala kwa niaba yake. Kwa jina hili, Frederick Mariki anajitambulisha kwamba machifu wote wako
chini yake kama machifu wa Kiafrika walivyokuwa chini ya Wakoloni wa Kiingereza. Naye Mr. 2
katika wimbo uitwao “Veto” anajiita Rais (president). Jina la Rais pia linatumiwa na wasanii Diamond
na Bob Junior. Marais wengi ndio walioupiga marufuku utawala wa machifu (Rubanza, 1994:16).
Hivyo, kujitambulisha kama Rais inamaanisha wanatangaza mwisho wa utawala wa machifu katika
Bongo Fleva.
Wanamuziki wengine waliojitokeza kuwajibu wanamuziki waliojiita machifu ni pamoja na John
Simon anayejitambulisha kama Mfalme (King) na Gwamaka Kahaula anayejitambulisha pia kama
King Crazy GK, yaani Mfalme Kichaa GK. Kama tulivyoeleza hapo awali, katika jamii za Kiafrika
kabla ya ukoloni, machifu walikuwa wasaidizi wa wafalme. Kwa kujitambulisha kwa jina la Mfalme,
wasanii hawa wanawajibu wale wanaojiita machifu kuwa wapo chini yao kimuziki. Aidha, kwa upande
wa nje ya Afrika kulikuwa na wafalme. Nchi za Ulaya na Asia ambazo zina maendeleo makubwa,
zilikuwa na zingine bado zina utawala wa kifalme. Kwa wanamuziki hawa kujitambulisha kama
wafalme, kwa upande mwingine, inaweza kuonekana kwamba wanawajibu wale wanaojitambulisha
kama machifu kwamba wanaongoza mataifa tajiri.
Majina mengine ya majigambo yaliyotumiwa na wasanii hawa pia yalikuwa na majibizano. Kwa
mfano, mwanamuziki Tanzanaiti alijipa jina hilo ili kumjibu mwenzake, Diamond (Almasi).
Kinachoonekana hapa, ni kwamba wakati ambapo Diamond ni madini ya thamani sana, Tanzanite ni
98
madini ya thamani zaidi na ambayo hupatikana katika nchi moja tu, Tanzania. Kwa hiyo, msanii huyu
kujiita Tanzanite, alikuwa anamjibu Diamond kwamba yeye si tu ni madini ya thamani bali
yanapatikana katika nchi moja tu, Tanzania.
Hata majina ya majigambo ya kukashifu, yalikuwa na majibizano. Majina kama Gaidi, Dudu Baya
na kadhalika, ni wazi kwamba yalikuwa yanawajibu wasanii wengine. Gaidi ni tishio kwa utawala
wowote ule, uwe wa chifu, mfalme, malkia au hata Rais. Kwa hiyo, kujitambulisha kama Gaidi
kunawaeleza wanamuziki wengine kwamba huyu ni kiboko yao. Hali ni hiyohiyo hata kwa jina Dudu
Baya. Dudu baya linaweza kumshambulia mtawala yeyote, askari yeyote au hata raia mwema. Kwa
kujitambulisha kwa jina hilo kunamaanisha yeye ni kiboko yao.
Majibizano haya ya majina ya majigambo yaliendelea hadi katika mashairi waliyoyatunga. Sister P
na Zay B wametunga mashairi na kujibizana juu ya majina yao. Kwa mfano, katika wimbo wa Zay B
“Gado” anajitambulisha kuwa ni Mwanadada Gaidi. Hili linabainika katika shairi lifuatalo:
1. Zay to the B Mwanadada Gaidi
2. Sitaki ushahidi nini cha ziada
3. Mimi ni danger usinichezee ntakuchinja
4. Niko gado24 tena bado
5. Huwezi kucheza na anga hizi
Chanzo: Omari (2009:333)
Ili kumjibu Zay B, Sister P anajitambulisha kuwa ni “Bush” na Kijukuu cha NATO, kwa hiyo,
hatishiki na Gaidi. Tunaliona hili katika wimbo wake uitwao “Maisha ya Uswahilini:”
1. Sina papara katika fani nishatua
2. Bush nakuja magaidi mtanitambua
3. Mtoto mdogo kifani sasa nishakuwa…
4. Nenda Milembe kawape call machizi
5. Sister P kiburi gaidi kashamdhibiti
6. Kijukuu cha NATO sasa nakula kiulaini
Chanzo: Omari (2009:197)
Hapa Sister P anamwambia Zay B kuwa kama yeye ni gaidi basi yeye ni Bush hivyo ameshamdhibiti.
George W. Bush alikuwa Rais wa Marekani kati ya mwaka 2000-2008 na alikuwa Rais aliyepambana
sana na ugaidi. Huyu ndiye mwanzilishi wa vile vinavyoitwa “Vita vya Ugaidi Duniani” ambapo
aliivamia Afghanstan kwa lengo la kumsaka “gaidi namba moja duniani,” Osama Bin Laden (Wade na
Almir, 2011). Nalo NATO ni Shirika la Kujihami la Mataifa ya Magharibi ambalo nchi wanachama ni
pamoja na Marekani, Uingereza, Ujerumani, Ufaransa na Italia. Shirika hilo liko mstari wa mbele
kupambana na “ugaidi” duniani.
Jambo la kukumbuka hapa ni kwamba wasanii wengine wa muziki wa Bongo Fleva wamekuwa
na jina zaidi ya moja la majigambo kwa nyakati mbalimbali au hata kwa wakati mmoja. Kwa mfano,
Joseph Mbilinyi alijitambulisha kwa jina la 2 Proud wakati anaanza muziki, lakini baadaye akabadili
jina na kuitwa Mr. 2 na Sugu ambayo yanatumika kwa pamoja hadi sasa. Vivyo hivyo, Judith Wambura
alitambulika kama Lady Jaydee na kisha Komandoo na Binti Machozi, majina yote hayo yanatumika
hadi sasa. Joseph Haule anatambulika kama Prof. Jay, Jay Arosto, Mzee wa Mitulinga na kadhalika na
Ansleim Ngaiza alijulikana kama Soggy Doggy Hunter na kisha Chief Rumanyika. Naye Abubakar
Katwila alijulikana kama Q. Chief na hatimaye Q. Chila na pia Savimbi. Haroun Kahena
anajitambulisha kama Inspector Haroun, Jabali la Rap Katuni na pia Babu, na Zainab Lipangule
alijulikana kama Zein B lakini akabadilisha na kuitwa Zay B na hatimaye Mwanadada Gaidi (Omari
2010:4, 9). Zaidi ya majina hayo pia tunaweza kuona katika mashairi yake majina mengine aliyowahi
kujipa kama vile Komandoo, Bongo First Lady na Concord. Wengine waliobadilisha majina ni pamoja
na Dudu Baya anayeitwa Dudu Zuri, Hemed Suleiman anayeitwa PhD, TID anayeitwa pia Jembe na
kadhalika. Kubadilisha huku kwa majina au kuongeza jina jipya kuna dhima ya kumpa msanii sifa
mpya ya majigambo anayodhani au ambayo mashabiki wake wanadhani anayo. Kwa mfano, kutokana
na Dudu Baya kuona tabia yake ya ugomvi inahusishwa na jina lake akaamua kubadili jina ili kujaribu
24 Gado ni msimu ambao unamaanisha niko imara.
99
kuwashawishi wapinzani wake kwamba kwa sasa amebadilika na hivyo si Dudu Baya tena bali ni Dudu
Zuri. Hali ni hiyo hiyo kwa Hemed Suleiman ambaye hakuwa na jina la majigambo alipoamua kujiita
PhD ili kuonesha jinsi alivyoiva katika fani ya muziki kwa sasa.
Aidha, wapo baadhi ya wasanii ambao hawana majina ya majigambo. Hawa ni pamoja na Ali
Kiba, Banana Zorro, Ferouz Mrisho, Nakaaya Sumari na Stara Thomas. Wapo walioendelea kutumia
majina yao ya asili kama yalivyo na pia wapo walioyafupisha majina yao ya asilli. Walioyafupisha
majina yao ni kama vile Faridi Kubanda (Fid Q), Ambwene Yesaya (A. Y), Rehema Chalamila (Ray C,
huyu anaitwa pia Kiuno bila Mfupa) (Omari 2010:2-3). Vilevile wapo waliofupisha jina moja kati ya
majina yao. Hawa ni pamoja na Dully Sykes (Abdul Sykes), Angeris Faber a.k.a Angie, Bakari
Abdallah (Beka) na Estalina Sanga (Lina). Majina haya hata hivyo si ya majigambo.
(ii) Majigambo ya Majibizano katika Mashairi ya Bongo Fleva
Mbali na majibizano katika majina yao, wanamuziki wa muziki wa kizazi kipya walijibizana
katika mashairi ya nyimbo zao. Mambo waliyojibizana, ni ujumbe, anasa, ndoa, dini na kadhalika.
Mfano mzuri wa majibizano ni kati ya msanii Hamisi Mwinjuma (Mwana FA) na Haroun Kahena
(Inspector Haroun). Mwana FA alitunga wimbo wa “Bado Niponipo Kwanza” ambamo anapinga suala
la ndoa. Turejelee ubeti huu:
1. Japo natokea Tanga mapenzi yalipozaliwa
2. Sijiviki maufundi nikajifanya najua
3.Mi nna akili timamu naona mnavyorukia
4.Ukiniona na demu haimaanishi ndio nitamuoa
5.Napata wakati mgumu washkaji wanapolia kwa uchungu
6.Kwani nami nna maumivu yangu nasema tu na moyo wangu
7.Watu wanalalamika wanavyoteswa na ndoa zao
8.Wengine wanaficha wanakufa na maumivu yao
9. Sioi leo sioi kesho kutwa wala mtondogoo
10. Sioi mchana sioi usiku wala majogoo
11. Morali niliyonayo sasa siwezi kukubali kuibiwa
12. Ngoja nizeekezeeke kwanza pengine nitakuja elewa
13. Wengine nifumbe macho, wengine nizibe masikio
14. Nisione wakati naibiwa
15. Hamuwezi kuwa hamjalewa
16. Mi nkiona mtu anaibiwa naona kama naibiwa mimi
17. So mpaka miaka kadhaa ijayo ndo mniulize naoa lini
Chanzo: Mwana FA (2011), Yalaiti
Katika wimbo huo msanii anajigambo kwamba yeye anatokea Tanga mapenzi yalipozaliwa na
hivyo anajinadi kwamba anajua mapenzi. Zaidi ya ujuzi huu wa mapenzi anaojinasibisha nao
anaonyesha jinsi ndoa inavyoweza kuleta matatizo kwa mtu kutokana na kusalitiwa na ampendaye.
Anabainisha wazi kwamba wanawake katika ndoa si waaminifu na hivyo ili kukwepa matatizo hayo,
msanii anabainisha kwamba ni vema asioe kwa sasa. Akimjibu Mwana FA, Inspector Haroun, ambaye
ameoa, akatunga wimbo wa “Tamu ya Ndoa.” Katika wimbo huo anamjibu Mwana FA kwamba ndoa
ni tamu na ni kitu cha hekima. Inspector anajigamba kwamba anaheshimika kwa kuwa ameoa na
kwamba asiyeoa huonekana muhuni na anayeogopa majukumu.
Aidha, majibizano mengine yanaonekana baina ya Sister P na Zay B. Wasanii hawa kwa muda
mrefu walikuwa kwenye malumbano kutokana na kila mmoja wao kutaka kuonekana ndiye mahiri
katika muziki huu kwa upande wa wanawake. Majibizano kati ya wawili hawa yanabainishwa vizuri na
Omari (2009:195). Kwa mfano, tunaona wanajibizana juu ya suala la biashara. Tuangalie wimbo wa
Zay B uitwao “Mama Afrika”:
1.Msipende kutembea na wazee
2. Fuateni wosia hiyo tabia isiendelee...
3. Tumeumbika ulimwengu mzima tunakubalika...
4.Weusi asilia ndio zetu kujivunia...
5.Watoto wa kike tusikae nyuma na tuzingatie elimu
6.Ukijifanya unajua shauri yako utaishia kuuza vitumbua
Chanzo: Omari (2009:336)
100
Sister P alijibu mashairi hayo katika wimbo uitwao “Achana Nao.” Anasema:
1.Nafungua ubongo natoa fikra za utumwa kichwani
2.Kipawa chatoka kwa Mola wala sijatumia ubani
3. Sister P kupata chati watu wanadhani rap utani
4. Rap biashara bwana ila angalia usijepata hasara
5.Kuuza vitumbua, pipi maandazi zote biashara
6.Usidharau hizo biashara watu watakuangushia msala.
7.Wasomi wengi wamesoma kwa kutumia hizo biashara
8.Mashairi sibahatishi na nitauza nyingi nakala
9.Na siyo utani nyota kwangu imeonekana biashara
10.Wandago rafiki zangu tena wa kina
11.We uliza maswali mengi majibu mimi sina
12.Nakupa rap shule mashairi yangu yana vina
Chanzo: Omari (2009:291)
Vilevile wanajibizana juu ya uwezo wao kimuziki. Rejelea katika wimbo wa “Gado” ulioimbwa na Zay
B:
1. Zay B sasa yuko gado
2.Mashairi yamejaa kisadosado
3.Zay B sasa yuko gado
4.Yote kumi tisa mambo bado bado
Sister P akimjibu katika wimbo wa “MaDJ” anasema,
1.Ya nini visado? Watu tumejaza lumbesa
2.Na bado katika fani tunazidi kutikisa
3. Sister P, Mnyamwezi Hamisi na Prado
4.Hatuogopi vishindo vyenu eti kwamba mko gado
5.Na bado mimi Sister P ni damudamu Thadeo
6. Pumbavu unauliza ningeimba nini Sister P asingekuwepo Zay B...
7. Swali linarudi kwako sasa eh eh
8.Ungeimba nini Mwanafalsafa tusingekuwepo wasanii?
9.Au ungekuwepo wewe bubu katika fani hii?
Chanzo: Omari (2009:196)
Majibizano haya ni aina ya majigambo kwani msanii mmoja anapomjibu mwingine lengo lake hasa
huwa kuionyesha jamii na msanii huyo kwamba msanii anayejibiwa si mwanamuziki aliyebobea na
kwamba anatunga nyimbo ambazo hazina ujumbe mzito unaokubalika katika jamii.
(f) Matumizi ya Lugha katika Ushairi wa Bongo Fleva
Baada ya kuangalia ujitokezaji wa ushairi wa Bongo Fleva kipengele cha kimtindo ni matumizi ya
lugha. Ushairi wa Bongo Fleva, kwa kiasi kikubwa, hutumia lugha ya Kiswahili, ambayo ndio
inaeleweka kwa Watanzania walio wengi. Matumizi haya ya lugha ya Kiswahili huenda
yanasababishwa na ukweli kwamba Kiswahili ndio lugha ya taifa nchini Tanzania na lugha
inayoeleweka kwa wengi. Kwa hiyo, kutumia lugha hii kunatokana na msanii kuilenga hadhira pana
zaidi.
(i) Matumizi ya Lugha Iliyotoholewa
Zaidi ya matumizi ya lugha ya Kiswahili kuna matumizi makubwa ya lugha iliyotoholewa na
kuchanganya lugha hasa Kiingereza na Kiswahili. Majembe (1998), Chachage (2002) na Omari (2009)
wakielezea hili wanasema kwamba muziki wa Bongo Fleva/ Hip hop kwa kiasi kikubwa umeathiriwa
na muziki wa Hip hop wa Kimarekani. Hivyo wanaeleza kwamba kuna mchanganyiko wa lugha ya
Kiswahili na Kiingereza. Lugha ya Kiingereza ndio inayotumiwa na wasanii wa Hip hop wa Marekani.
Mfano mzuri wa nyimbo inayotumia lugha yenye utohozi ni “Mchakamchaka” wa Mr. 2 kama
ifuatavyo:
1. Mie niite super delegeto ama deiwaka
101
2. Nalicheza hili gemu nnavyotaka
3. Ni albam ya kumi lakini hasira kama ndo kwanza natoka
4. Sasa ni mwendo wa dolali
5. Ndani ya akaunti mtoni utadhani mtoto wa Balali
6. Sema vijisenti vyangu ni vya halali
7. Bongo mchakamchaka tu
8. Mafisadi hawalali
9. Nina uhuru wa kusema
10.Na nitasema chochote ntakachoona kinafaa mimi kusema
11.Na nakuja na falsafa za Obama
12.Tunatakiwa kuchange
13.Tusipochange maisha bora kwetu ndoto kama muafaka wa Zenji anha
14.Wacha niendeleze dozi
15.Maana leo kama balozi
16.Kama kazi ni kazi hakuna ubitozi
17.Na ni upuuzi kusema gemu haliuzi
Chanzo: Mr. 2, (2009), Veto
Hapa tunaona anatumia neno super delegeto (super delegate), deiwaka (day worker), gemu (game),
albam (album), dolali (dollar), kuchange (to change), akaunti (account) na dozi (dose). Maneno haya ni
ya Kiingereza yaliyoswahilishwa. Hii inaonesha athari za lugha ya Kiingereza katika Kiswahili na
mchango wake katika kukuza msamiati wa Kiswahili. Aidha, lugha inayotumiwa hapa inasawiri lugha
inayotumiwa na vijana, ambao ndio hasa fanani na hadhira ya ushairi wa Bongo Fleva.
(ii) Matumizi ya Lugha za Mchanganyiko
Mbali na matumizi ya lugha ya Kiswahili na lugha iliyotoholewa, ushairi wa Bongo Fleva unatumia
pia lugha mchanganyiko. Mchanganyiko wa lugha unaotumika ni ule wa Kiswahili na lugha za
makabila na mchanganyiko wa Kiswahili na Kiingereza. Katika vipengele vinavyofuata tutaelezea
matumizi haya ya lugha mchanganyiko na kuthibitisha kwa mifano. Tuanze na mchanganyiko wa
Kiswahili na lugha za makabila.
Ushairi wa Bongo Fleva una matumizi ya mchanganyiko wa lugha ya Kiswahili na lugha nyingine
za makabila. Hii inatokana na ukweli kwamba wasanii wa ushairi huu wana makabila yao ambayo
wangependa kujitambulisha kwayo. Uchanganyaji wa aina hii unaonekana katika wimbo wa “Walimu”
ulioimbwa na Wagosi wa Kaya kama unavyonukuliwa katika data namba (106) hapa chini:
1. Goodmorning teacher, goodmorning sir
2. Monika zeze mwalimu hicho ni Kisambaa
3. Nimechanganyikiwa mpaka naongea Kisambaa darasani
4. Na hii ni kwa sababu sina kitu mfukoni
Chanzo: Wagosi wa Kaya (2003), Ripoti Kamili
Hapa tunaona zaidi ya uchanganyaji wa Kiswahili na Kiingereza katika mstari wa 1, kuna
uchanganyaji wa Kisambaa na Kiswahili katika mstari wa 2. Kirai Monika zeze kina maana ya habari za
asubuhi katika lugha ya Kisambaa. Uchanganyaji unaonekana pia katika wimbo wa Suma Lee,
“Hakunaga” ambapo msanii anaanza kwa ghani za kikabila. Aidha, hata neno “hakunaga” analolitumia
mara kwa mara ni neno lenye asili ya lugha za makabila na hasa Kisukuma. Matumizi haya ya lugha za
kikabila yana lengo la kupata soko katika mikoa na maeneo makabila hayo yanamotumika. Sababu
nyingine ya matumizi hayo ya lugha, inaweza kuwa harakati za kujinasua kutoka katika athari za
kutoka nje (ukoloni mamboleo) na hasa athari za kiutamaduni. Likithibitisha haya Fiesta (2011:27)
linasema:
Mwanamuziki wa Bongo Fleva ambaye anatumia lafudhi ya Kimasai katika kuimba nyimbo
zake, Abel Loshilaa Motika maarufu kwa jina la Mr. Ebbo amewataka wanamuziki wa Bongo
Fleva kujivunia lugha yao sio kupenda kutumia lugha za wenzetu katika nyimbo zao.
Akizungumza na Fiesta, mwanamuziki huyo mkongwe katika fani hiyo alisema kuwa utamkuta
mwanamuziki wa Kitanzania anaimba lugha ya kigeni katika nyimbo zetu bila aibu. Msanii huyo
anajivunia kila kilicho chake na pia hapendi kuiga bali anapenda kubuni na anapobuni
anatoka na vitu vya ukweli. Mr. Ebbo anasema tatizo la wasanii wa Bongo Fleva ni kuigana, kila
msanii angekuwa na ubunifu wake basi ingekuwa rahisi kuuzika sokoni lakini wanapoigana
kunakuwa hakuna kitu kipya kwa wasikilizaji (Msisitizo wetu).
102
Katika dondoo hili mwandishi anatueleza kwamba msanii huyu si tu anatumia lugha ya Kimasai, bali
pia anatumia lafudhi ya Kimasai.
Zaidi ya matumizi ya lugha yenye mchanganyiko wa lugha ya Kiswahili na lugha za makabila,
kuna matumizi ya mchanganyiko wa lugha ya Kiswahili na Kiingereza. Aina hii ya mchanganyiko wa
lugha, imetumika sana katika ushairi wa Bongo Fleva. Maneno yote tuliyoyawekea hati za mlalo
(italic) katika mashairi ya Bongo Fleva tuliyoyanukuu, yanaonyesha matumizi ya lugha hii
mchanganyiko.
Hata hivyo, kumekuwa na harakati za wasanii kupinga uigaji wa tamaduni za nje yakiwamo
matumizi ya lugha ya Kiingereza katika muziki wa Bongo Fleva. Likisisitiza jinsi matumizi ya lugha
ya Kiingereza katika muziki wa Bongo Fleva yanavyopingwa, Kitangoma (2011a:7) linamnukuu
msanii Dayna anaposema, “ …nawashangaa baadhi ya wasanii wenzetu ambao wamekuwa
wakikimbilia kuimba Kizungu (Kiingereza) na kutukuza lugha za nchi nyingine na kukiacha Kiswahili
ambacho kwa sasa kimeanza kutambulika duniani” (Ufafanuzi wetu).
Matumizi haya ya mchanganyiko wa lugha ya Kiswahili na Kiingereza, ingawa yanaonekana
kupingwa na baadhi ya wasanii na wanajamii, yanaakisi hali halisi ya jamii. Yanaonyesha athari ya
ukoloni mamboleo katika lugha. Mchanganyiko huu wa lugha hauonekani tu katika ushairi wa Bongo
Fleva lakini unaonekana pia katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na bungeni na kadhalika.
Hivyo, huu ni uthibitisho kwamba fasihi ni kioo cha jamii husika.
(g) Matumizi ya Tamathali za Semi
Mbali na matumizi ya lugha ya Kiswahili, lugha iliyotoholewa, lugha ya Kiswahili
iliyochanganyika na lugha za makabila na lugha ya Kiswahili iliyochanganyika na lugha ya Kiingereza,
ushairi wa Bongo Fleva unatumia pia tamathali za semi. Baadhi ya tamathali za semi zinazotumika sana
ni sitiari, tashbiha, tashtiti, udokezo na chuku. Katika sehemu inayofuata tutachambua tamathali hizi
kwa kina. Katika kipengele hiki tutapitia tamathali hizo za usemi.
(i) Tashbiha katika Ushairi wa Bongo Fleva
Aina hii ya tamathali imetumika sana katika mashairi mbalimbali ya ushairi wa Bongo Fleva.
Matumizi ya aina hii yanaonekana katika wimbo wa Sister P uitwao “MaDJ” kama inavyonukuliwa
katika ubeti ufuatao:
1.Kwamba mimi sitishiki hata ukishika kisu kikali
2.Nilikutana na Halifani track ya kwanza ilikuwa kali
3. Sasa nije kwa hasira kama vile jabali?
4.Au nije kikakamavu kama vile jemedari?
5.Kutoa vishindo vikuu na sauti za ukali
6. Ili waelewe Bongo Records label yenye nembo kali
7.Najipa cheo kwenye rap mi ni stadi
8. Sauti yangu inatambaa kwenye beat kama radi
9.Usiniulize ovyoovyo jina langu linanipa chart
Chanzo: Omari (2009:190)
Katika ubeti huu tunaona kwamba msanii anatumia tashbiha tatu, “nije kwa hasira kama vile jabali,”
“kikakamavu kama vile jemedari” na ya mwisho “sauti inatambaa kwenye beat kama radi.”
Vilevile, matumizi mengine ya tashbiha yanaonekana katika wimbo wa “Jina Langu”
ulioimbwa na Prof. Jay. Katika ubeti ufuatao mstari wa 5 anatumia tashbiha isemayo “jina langu
mahiri kwenye giza kama kandili.” Turejelee ubeti huo ambapo msanii anasema:
1. Jina langu linavuma kwenye mitaa
2. Jina langu lina hadhi ya kisupa staa
3. Jina langu linaongeza idadi ya maadui
4.Wengine nawajua wengine siwatambui
5. Jina langu mahiri kwenye giza kama kandili
Chanzo: Prof. Jay (2003), Mapinduzi Halisi
103
Matumizi haya ya tashbiha yanaweka msisitizo katika maana inayokusudiwa. Wasanii wanatumia
vitu vilivyozoeleka kufafanua vitu ambavyo wanadhani havifahamiki vema. Kwa mfano, tunaona
msanii Sister P, ili kufafanua ukakamavu alionao, anatumia picha ya jemedari (askari wa jeshi). Katika
jamii majemedari wanafahamika sana kwa ukakamavu wao. Vivyo hivyo anapotaka kufafanua mapigo
(beats) ya nyimbo zake anatumia sauti ya radi ambayo wanajamii wamezoea kuisikia.
Kwa upande wa Prof. Jay, anatumia picha ya mwanga wa taa ya kandili unavyoweza kufukuza
giza hata liwe nene kiasi gani. Hapa anafananisha uwezo wa jina lake na wa taa ya kandili. Picha hii
imezoeleka kwa Watanzania walio wengi kwani wanatumia taa hizo kila siku. Zaidi ya asilimia 80% ya
Watanzania hawapati nishati ya umeme na hivyo taa walizozizoea ni kandili, vibatari na kadhalika.
Akithibitisha hili Msuya (2011:1) anamnukuu Sir George Kahama mmoja wa wanasiasa maarufu
Tanzania anaposema:
Bila kubeza mafanikio makubwa yaliyopatikana, ni vema pia tukiri kwamba, safari yetu ya kufikia
lengo la kuwa na maisha bora kwa kila Matanzania bado ni ndefu. Asilimia 36 ya Watanzania
bado hawajaweza kumudu kupata mahitaji yao ya msingi. Asilimia 86 ya wananchi hawapati
umeme wa gridi ya taifa. Wote tunajua ya kwamba, wananchi wengi bado wanaishi katika nyumba
zilizojengwa kwa kuta za miti, fito na matope na kuezekwa kwa makuti au nyasi.
Hivyo matumizi ya tashbiha yanafanya maudhui kufika kwa njia bora zaidi kuliko kama zisingetumika.
(ii) Sitiari katika Ushairi wa Bongo Fleva
Aina nyingine ya tamathali ya semi iliyotumika kwa kiasi kikubwa katika ushairi wa Bongo
Fleva ni sitiari. Sitiari ni uchoraji wa picha katika akili ya hadhira. Ingawa tashibiha pia huchora picha,
ina tofauti na sitiari kwani sitiari huchora picha kana kwamba ndio ukweli. Sitiari huchora picha kwa
kulinganisha vitu viwili tofauti bila kutumia vifananisho kama: kama, kama vile, mithili ya na
kadhalika. Hivyo, picha inayochorwa huonekana kama ndio uhalisia wenyewe. Mtu anaposema,
“Mariam ana uzuri kama malaika,” anakuwa ametumia tashibiha kuchora picha ya malaika kichwani
mwa hadhira. Watu wengi huamini kwamba malaika ni kiumbe mzuri sana. Hata hivyo, picha hii
huonekana kama mfano tu na si uzuri halisi wa Mariam. Lakini fanani anaposema, “Mariamu kwa uzuri
wake ni malaika” (sitiari), hadhira hupata picha ya uzuri halisi. Picha hii huwa na nguvu na kuaminika
zaidi kuliko ile ya kitashibiha. Hivyo, majigambo ya Bongo Fleva hutumia sitiari ili kujenga picha
halisi na za kuaminika zaidi na hivyo kuweka mkazo katika maana.
Mifano ya matumizi ya sitairi inaonekana katika nyimbo mbili zifuatazo zilizoimbwa na Zay B.
Katika wimbo wa kwanza, “Siwezi Kuacha” anatumia sitiari mbili ambazo ni “mimi ndo Bongo First
Lady” (mstari wa 2) na “wanaotaka ushindani wote takataka” (mstari wa 3) kama inavyojibainisha
katika data ifuatayo:
1.Nacharaza mijeledi na wale wote wapinzani wa jadi
2.Wamekiri mimi ndo Bongo First Lady…
3.Wanaotaka ushindani wote takataka
4.Unanigwaya hatari kuliko miwaya…
5.Katika madada mi kiboko
Chanzo: Omari (2009:348)
Katika wimbo wa pili unaoitwa “Hatari Kitu Gani” msanii anatumia sitiari mbili pia. Sitiari ya
kwanza ni “mimi ni komandoo tena nakuja kwa vishindo” (mstari wa 1) na ya pili ni “mamia kwa
mamia wamekiri kama mimi ndio Concord.” Turejelee ubeti huu:
1.Mimi kamandoo tena nakuja kwa vishindo
2.Nasema njoo once again nawakilisha Tanzania
3.Wanga mtabana mtaachia lyrics nazidi kuwamiminia
4.Mimi mtaniambia sio kama najifagilia
5.Mamia kwa mamia wamekiri kama mimi ndio Concord…
6. Sauti yangu inasikika dunia nzima
7.Vigumu kuisahau kama Tupac na B.I.G
Chanzo: Omari (2009:192)
Katika data namba nyimbo mbili hapo juu tunaona Zay B anafananisha umaarufu wake katika muziki
na umaarufu wa first lady (mke wa Rais) na anawafananisha wapinzani wake na takataka. Vilevile
analinganisha anavyowasumbua wapinzani wake na kuwatesa kama vile mtu anayechapa wengine
104
mijeledi. Pia anajifananisha na komandoo na ndege ya concord. Hapa hatumii vifananisho kama ilivyo
kwenye tashbiha na hivyo anachora picha halisi zaidi na zinazoaminika.
Aidha, zaidi ya kuchora picha za kuaminika na zilizo halisi zaidi, tumeeleza hapo awali kwamba
sitiari ndio huufanya utungo kuwa na sifa ya kishairi kwani ni moja ya sifa muhimu ya utanzu wa
ushairi (Mulokozi, 2002; Songoyi, 2005). Hivyo, tunaweza kusema kwamba matumizi ya sitiari hapa,
zaidi ya mambo mengine, yameyafanya majigambo ya Bongo Fleva kukidhi vigezo vya utanzu wa
ushairi.
(iii) Tashihisi katika Ushairi wa Bongo Fleva
Ushairi wa Bongo Fleva mbali na kutumia tamathali zingine, umetumia tamathali hii ya usemi.
Mfano mzuri ni wimbo uitwao “Nawakilisha” ulioimbwa na Prof. Jay anaposema:
1. Beti kamili zenye mizani thamani zaidi ya madini...
2.Weka mbali malenga mnaosifia huu ubongo ni Shakespeare...
3.Wenyewe mnajuta tena nina uwezo zaidi ya kompyuta
Chanzo: Omari (2009:193)
Katika shairi hili msanii anaupa ubongo wake uwezo wa kuimba na kutunga kazi za kisanii kama
Shakespeare alivyokuwa mahiri katika utunzi. William Shakespeare alikuwa mshairi na mtunzi
maarufu wa mashairi na tamthiliya aliyeisha kati ya mwaka 1564 hadi 1616. Msanii huyu alitunga
mashairi zaidi ya 154 na tamthliya 38 na kazi zake zimetafsiriwa na kutumiwa katika nchi mbalimbali.
Msanii huyu anajulikana kama sheha wa malenga wa taifa la Uingereza (Gibbons, 1980 na 1993;
Grady, 2001a na b). Hivyo, msanii anaufananisha ubongo wake na ule wa Shakespeare. Anachokisema
hapa ni kwamba ubongo wake unaweza kutunga, kuimba na kutenda kama Shakespeare. Katika hali ya
kawaida ubongo hauwezi kutenda hayo.
Tashihisi, kama zilivyo tamathali nyingine, zimetumiwa na wasanii wa ushairi wa Bongo Fleva
ili kukazia maana. Kwa mfano, katika shairi tulilolinukuu msanii anatumia tashihisi ili kuweka mkazo
katika uwezo mkubwa alionao katika ushairi wa Bongo Fleva.
(iv) Udokezi katika Ushairi wa Bongo Fleva
Tamathali nyingine ya usemi ambayo imetumika katika ushairi wa Bongo Fleva ni udokezi.
Tumeeleza hapo awali kwamba udokezi au mdokezo ni tamathali ambayo inatumika katika kazi
mahsusi ya kifasihi ili kurejelea kazi nyingine ya fasihi au ya sanaa, au mtu au hata tukio. Aidha,
tumeona kwamba tamathali hii inatumika katika ushairi wa majigambo kwa dhima ya kuhusianisha kazi
za fasihi, vitu, watu au matukio kwa lengo la kuyapa uzito maudhui ya kazi husika na/au kuupa ushairi
huo upekee (Johnson, 1978: 14; Cuddon, 1998:27). Katika ushairi wa Bongo Fleva udokezi umetumika
sana. Mfano mzuri wa matumizi ya mbinu hii unaonekana katika wimbo wa “Ndiyo Mzee” ulioimbwa
na Profesa Jay ambao tumeunukuu hapa chini.
1. Ok ok naitwa Joseph Haule mwana Msolopazi
2. Nadhani nimeletwa kuokoa hiki kizazi
3. Mimi ni mwanasiasa niliyebarikiwa na Mungu
4. Nimeletwa kwenu waungwana niwapunguzie machungu
5. Mimi ni mteule Kusini mwa jangwa la Sahara
6. Ndio maana nimetunukiwa cheti cha juu cha utawala
7. Nina hekima kuliko mfalme Sulemani msiwe na wasi
8. Na hii nitadhihirisha pindi mtakaponipa nafasi
9. Actually, nimedhamiria kuwasaidia
10. Taifa lenye nguvu duniani liwe Tanzania
Chanzo: Profesa Jay (2001), Machozi, Jasho na Damu
Katika mstari wa kwanza wa uberi wa kwanza msanii anasema “ok ok naitwa Joseph Haule
mwana Msolopagazi.” Katika mstari huo msanii anatumia mbinu ya udokezi kwa kuturejesha katika
hadithi za Ridder Haggard za Mashimo ya Mfalme Selemani, na mhusika wake wa Kiafrika aitwaye
Msolopagazi (Umsolopagaas) anayeambatana na wahusika Wazungu, Allan Quarteman, Sir Henry
Curtis na John Good (taz. Haggard, 1885). Hapa msanii, zaidi ya mambo mengine, huenda pia
anakusudia kutuonyesha kwamba yeye ni mwanamuziki wa Kiafrika ambaye hadhi yake ni sawa na ya
105
wanamuziki wa Kizungu na kwamba anawasaidia hata katika tungo zao. Ikumbukwe kwamba kwa
kipindi kirefu muziki wa wanamuziki Wazungu ndio umechukuliwa kuwa bora na wa kiwango cha juu.
Lakini Profesa Jay ameshirikiana kuimba na wanamuziki kadhaa wa nje ya Tanzania wakiwamo
Wazungu. Miongoni mwa alioshirikiana nao ni Jaguar na Amani (kutoka Kenya), Jose Chamellion
(kutoka Uganda), P Square (kutoka Nigeria), Heavy D (kutoka Marekani) na kadhalika.
Udokezi katika wimbo huo unatumika pia katika mstari wa 7 anaposema “nina hekima kuliko
mfalme Sulemani msiwe na wasi.” Hapo anaingiza katika ushairi ngano ya Kiyahudi inayomuhusu
Mfalme Sulemani. Katika ngano hiyo Mfalme Sulemani, ambaye alikuwa mtoto wa Daudi aliyezaliwa
katika ukoo wa Yese, anatajwa kwamba alimpendeza sana Mungu kiasi cha Mungu kumwambia
amuombe chochote atakacho. Ndipo mfalme huyo akaomba hekima. Baada ya kutoa ombi hilo
kinyume na matarajio ya Mungu aliyetegemea angeomba utajiri, Mungu akamwambia atamuongezea
na vingine vyote. Hivyo, Sulemani akawa na hekima kuliko wanadamu wote duniani na hata wafalme
wengine na watawala wa dola nyingine kama vile Malkia wa Sheba wakasafiri umbali mrefu kuja
kushuhudia hekima ya Sulemani (Tanzania Bible Society, 1997:377-379). Udokezi huu unatumiwa na
msanii kwa lengo la kukejeli viongozi wa Kiafrika jinsi wanavyotaka waonekane wana hekima sana
wakati kimsingi hawana hekima yoyote.
(v) Kejeli katika Ushairi wa Bongo Fleva
Zaidi ya kutumia udokezi ushairi wa Bongo Fleva unatumia pia kejeli. Senkoro (2011:13)
anafasili kejeli kuwa ni tamathali ambayo maneno yake huwa kinyume kabisa na maana inayotakiwa
kutolewa. Anaendelea kusema kwamba kejeli huweza kuchanganya tamathali nyingine kama vile
ubeuzi uliofichika, kinyume, tabaini na msisitizo bayani. Nao Kahigi na Mulokozi (1979:37)
wanafafanua kuwa kejeli ni usemi wa kebehi ambamo kisemwacho sicho kikusudiwacho na msemaji,
kisemwacho kumbe ndicho kinachobeuliwa. Tamathali hii imetumika sana katika ushairi wa Bongo
Fleva. Matumizi ya mbinu hii yanaonekana katika wimbo wa “Ndiyo Mzee” tuliounukuu hapo awali.
Wimbo huo umebeba dhana ya unyume. Msanii anawakilisha majigambo ya uongo ya wanasiasa
wakati wa kampeni za uchaguzi. Kwa hiyo, majigambo hayo ni ya kikejeli.
(vi) Chuku katika Ushairi wa Bongo Fleva
Aidha, tunaona matumizi ya chuku katika mashairi ya Bongo Fleva. Mbali na matumizi ya
chuku katika majina ya wasanii wa uushairi wa Bongo Fleva, kama tulivyojadili hapo awali, pia kuna
matumizi ya chuku katika mashairi haya. Kwa mfano, katika wimbo wa Dogo Janja uitwao “Anajua”
tunaona matumizi haya ya chuku. Tunathibitisha hilo katika ubeti ufuatao:
1. Tunainama
2. Tunameza tunatema
3. Mtaipata fresh ya mwaka mpaka mnatetemeka
4. Kuona kwa bei tunamakeup tupo full mzuka...
5. Dogo Janja mimi sirushi ngumi nawachapa tu na ulimi
6. Kwa michano hunichomi
7. Kama ulikuwa hunisomi
8. Nakufunika Ommy
9. Huwezi kukabiliana utemi
10.Dogo Janja sikwami
11.Eh basi nina army
12.Tupo japo hatuvumi
13.A town siyo Miami
14.Dogo Janja kamanda...
Chanzo: Dogo Janja (2009), Ngarenaro
Hapa tunaona msanii anasema hakwami na kwamba ana jeshi (army) na yeye ni kamanda. Katika hali
ya kawaida hakuna binadamu ambaye hakwami. Pia nchini Tanzania hairuhusiwi mtu kuwa na jeshi
lake binafsi. Hivyo, msanii hapa kwa kusema ana jeshi ni chuku zinazotumika kujenga lugha ya picha.
Lugha hii ya picha huwa na mchango mkubwa katika kuweka mkazo katika maudhui. Kwa mfano,
katika shairi hili kwa msanii kusema kwamba ana jeshi anakazia maudhui kwamba yeye hawezekani
maana ana mashabiki wengi wanaomuunga mkono.
106
(vii) Takriri katika Ushairi wa Bongo Fleva
Ushairi wa Bongo Fleva pia unatumia takriri. Takriri ni mbinu iliyotumika zaidi katika ushairi
wa muziki wa kizazi kipya. Dunleavy (1992:23) anaeleza kwamba takriri ni moja ya sifa kuu katika
lugha ya kimuziki na pale takriri zinapotumika, kunakuwa na msisitizo katika maana. Tunaliona hili
anaposema:
We are familiar with the three Rs associated with music – rhythm, rhyme and repetition. When
lyrics are repeated, an idea or concept is reinforced. The repetition of the consonant can
punctuate the rhythm of a piece of music. Letter, words, phrases, lines, refrains, choruses, and
verses can all be repeated.
Tunafahamu kwamba muziki una sifa tatu za msingi ambazo ni mapigo, vina na marudio. Wimbo
unaporudiwa, ujumbe husisitizwa zaidi. Marudio ya konsonanti katika mstari yanaweza kuleta
mapigo ya kimuziki. Herufi, maneno, virai, mishororo, viitikio na hata beti nzima huweza
kurudiwa (Tafsiri yetu).
Katika ushairi wa kizazi kipya, zaidi ya aina nyingine ya takriri, kuna takriri kiitikio. Haya ni marudio
ya kiitikio kizima katika ushairi. Katika muziki wa kizazi kipya marudio ya kiitikio yanaonekana karibu
katika kila wimbo. Tunalithibitisha hilo katika wimbo wa Mr. 2 uitwao “Mchakamchaka,” “Veto” na
ule wimbo uitwao “Moto Chini” ambapo tunaona msanii anarudia kiitikio kizima. (Taz. Nyimbo
mbalimbali tulizozinukuu).
Mbali na takriri kiitikio, pia ushairi wa Bongo Fleva unatumia takriri mstari, takriri neno, takriri
kirai, takriri kishazi, takriri silabi na kadhalika. Kwa mfano, katika wimbo uitwao “Sisi Tulivyo”
ulioimbwa na Sister P:
1. Sisi tulivyo kama utakavyoniona ndio nilivyo
2. Mimi nilivyo siko sawa na jinsi ulivyo
3. Mimi nilivyo hata unavyodhani sivyo nilivyo
4. Mimi nilivyo huwezi kunitambua jinsi nilivyo
5. Mimi nilivyo na huu ndio ukweli wa jinsi nilivyo
6. Mimi nilivyo siyo sawa na manabii jinsi walivyo
7. Mimi nilivyo nina hekima kuliko mtu mzima alivyo
8. Mimi nilivyo na hadhi zaidi ya wafalme jinsi walivyo
9. Mimi ni mchamungu kuliko ulivyo
10.Mimi nilivyo napenda mademu jinsi walivyo
Chanzo: Omari (2009:295-296)
Hapa kuna takriri neno ambapo neno “nilivyo” au sehemu yake limerudiwa karibu wimbo mzima. Pia
kuna marudio ya neno “mimi” (mstari wa 9 na wa 10) na marudio ya kishazi “mimi nilivyo” (mstari wa
2 hadi wa 8). Takriri hii, zaidi ya kukazia maneno yaliyorudiwa, inafanya kazi ya kuleta mapigo katika
ushairi na kushadidia maudhui.
(h) Mbinu za Kisanii
Zaidi ya vipengele hivyo vya mtindo kipengele kingine ni mbinu za kisanii. Kama tulivyomnukuu
Senkoro (2011:25-51) hapo awali mbinu za kisanii tunazozizungumzia hapa ni pamoja na ishara,
picha, ucheshi, vina na mizani, mapigo, methali na, usambamba. Mjadala unaofuata utahusu vipengele
hivi vya kimtindo.
(i) Matumizi ya Picha na Taswira
Picha na taswira zimetumika sana katika ushairi wa Bongo Fleva. Picha na taswira zimetumika
kuanzia katika majina ya wasanii wa ushairi huu, hadi katika mashairi yao. Kwa mfano, majina ya
Komandoo, Chifu na Inspekta ambayo tumeyaeleza matumizi yake huko nyuma, ni majina ya
kitaswira. Maelezo ya kina ya lugha ya ishara na picha tazama kipengele kinachohusu majina ya
wasanii wa ushairi wa Bongo Fleva tulichokieleza hapo awali.
(ii) Ucheshi katika Ushairi wa Bongo Fleva
Mbinu nyingine inayotumika katika ushairi wa Bongo Fleva ni ucheshi. Ucheshi ni mbinu
ambayo hulenga kuchekesha au kuifanya hadhira walau itabasamu (Senkoro, 2011:26). Mbinu hii
huundwa kwa kutumia maneno na sentensi ambazo zinastaajabisha na hivyo kuifanya hadhira ishangae
107
na iishie kucheka au kutabasamu. Pia wakati mwingine msanii huweza kutumia kejeli ili kujenga
ucheshi. Matumizi ya ucheshi katika wimbo wa Bongo Fleva uitwao “Ndiyo Mzee” wa Profesa Jay
kama inavyoonekana katika ubeti ufuatao:
1. Wafanyakazi serikalini nashangaa hamna magari
2. Yaani hata mikweche, ha! ha! ha! hii ni hatari
3. Na nina mpango wa kuongeza mishahara iliyo minono
4. Mara mia moja ya ile ya mwanzo iliyowafanya mfanye migomo
5. Nitawapa nyumba nzuri na magari ya kifahari
6. Watu watashangaa mtakapopita kila mahali
7. Mkulima kila mmoja nitampatia trekta
8. Nadhani hiyo kidogo itasaidia kuinua sekta
9. Mtauza nafaka zenu bilioni kwa mabailioni
10.Watu midomo wazi kama wamekamatwa ugoni
11.Walimu zawadi yenu mh nimezificha moyoni
12.Nadhani mtazimia siku mkizitia machoni
13.We acha tu, mtafurahi nyinyi
14. Ila hapa hapamfai mtu mwingine niwekeni mimi
15. By the way polisi mi nawasifu
16. Jinsi mnavyokwenda sahani moja na wahalifu
17. Sasa kila mmoja nitampatia helkopta
18.Nadhani hiyo ndoto wote hamjawahi kuota
19.Raia wa Tanzania mtalala milango wazi
20. Infact nina uhakika wa kudhibiti ujambazi
21.Nitajenga barabara tano tano juu na chini
22.Nitajenga kumbi nyingi sana za starehe baharini
23.Ninapenda kuitwa mshumaa kumulikia wenzangu
24.Na mtakaoyumba kiuchumi tutagawana vya kwangu
Chanzo: Omari (2009:266 -268)
Katika wimbo huu tunaona msanii anaeleza kwamba ataongeza mishahara ya wafanyakazi mara mia
moja, atawapa wafanyakazi wote magari ya kifahari, atawapa wakulima matrekta na kwamba atajenga
kumbi za starehe baharini. Aidha, msanii anaeleza kwamba kila askari polisi atampatia helkopta na
kadhalika. Mambo haya anayoyasema ni chuku zinazojenga ucheshi kwa hadhira. Hapa msanii
anatumia chuku kujenga kejeli na kejeli hiyo inajenga ucheshi.
(iii)Vina na Mizani katika Majigambo ya Bongo Fleva
Zaidi ya ucheshi mbinu nyingine ya kimtindo inayotumika katika ushairi wa Bongo Fleva ni urari
wa vina na mizani. Katika ushairi wa muziki wa kizazi kipya kuna matumizi makubwa ya vina na
mizani. Utumiaji wa vina na mizani katika muziki huu ndio huonekana kuwa ujuzi wa kuimba na
ubobezi katika fani ya Bongo Fleva. Kwa mfano, katika wimbo uitwao “Nawakilisha” ulioimbwa na
Prof. Jay, msanii anajigamba kwamba mashairi yake yana vina na hivyo yeye amebobea katika muziki
huu. Anasema:
1. Beti kamili zenye mizani thamani zaidi ya madini...
2.Weka mbali malenga mnaosifia huu ubongo ni Shakespeare...
3.Wenyewe mnajuta tena nina uwezo zaidi ya kompyuta
Chanzo: Omari (2009: 193)
Hapa msanii anabainisha kwamba mashairi yenye beti kamili na mizani ndio yenye thamani kubwa
kuliko madini. Kwa maneno mengine, mashairi ambayo hayana sifa hizo hayana thamani yoyote.
Jambo la ajabu ni kwamba, ingawa anajigamba kwamba shairi lake lina urari wa mizani lakini ukweli
ni kwamba shairi hilo, kama yalivyo mengine ya wasanii wa Bongo Fleva, halina urari wa mizani.
Tunaona mstari wa 1 una mizani 20 wakati mstari wa 2 una mizani 25 na mstari wa 3 una mizani 21.
Vilevile tunaona pia msanii Sister P akijigamba kwamba mashairi yake yana urari wa vina. Katika
wimbo wa “Achana Nao” msanii anabainisha hilo kama anavyosema katika ubeti huu:
1. Nafungua ubongo natoa fikra za utumwa kichwani
2. Kipawa chatoka kwa mola wala sijatumia ubani
3. Sister P kupata chati watu wanadhani rap utani
4. Rap biashara bwana ila angalia usijepata hasara
5. Kuuza vitumbua, pipi maandazi zote biashara
108
6. Usidharau hizo biashara watu watakuangushia msala.
7. Wasomi wengi wamesoma kwa kutumia hizo biashara
8. Mashairi sibahatishi na nitauza nyingi nakala
9. Na siyo utani nyota kwangu imeonekana biashara
10. Wandago rafiki zangu tena wa kina
11. We uliza maswali mengi majibu mimi sina
12. Nakupa rap shule mashairi yangu yana vina
Chanzo: Omari (2009:291)
Hapa msanii anabainisha kwamba atauza nakala nyingi na mashairi yake yanakubalika kwa sababu
yana vina (mstari wa 12). Wasanii wengine wanaojigamba kwamba mashairi yao yana vina ni pamoja
na Zay B, Afande Sele, Mr. 2 na Dully Sykes. Hivyo, urari wa vina ni moja ya sifa muhimu
inayoonekana katika mashairi ya Bongo Fleva. Mfano mzuri wa mashairi yenye urari wa vina na
mizani unaonekana katika wimbo uitwao “Moto Chini” ulioimbwa na Mr. 2 kama inavyobainika katika
ubeti ufuatao:
1. Nimeshatoa ngoma UK sasa narudi tena
2. Nairobi na Kampala bado nawakilisha kwa sana
3. Maneno bado ni Yes
4. Naona kama hakuna noma
5. Sasa mechi ni international
6. Sugu ni chama kubwa kama Arsenal
7. Bado nipo dimbani
8. Na maiki ipo mkononi
9. Labda huku nilipo nifuateni
10. Maana inaonekana nitachelewa kushuka chini
11. Inashangaza kuona muda unazidi kwenda
12. Na mchezo wa Hip hop ndo kitu nnachokipenda
13. Check maplayer wenu jinsi ninavyowapiga denda
14. Ni VIP kila kiwanja ninachokwenda
15. Kwani hatari kitu gani
16. Kila wakati nipo bwana TBC extra quality
17. Na wachizi wangu wote sasa zidisheni hasira
18. Ni wakati wa kumaliza huu ni utungo wa kibiashara
19. Sasa ni muda mrefu wanatufanya mafara
20. Tunaingiza mabilioni wanahonga mademu vitara
21. Hamuwezi kunitisha
22. Katika kuthibitisha
23. Nawawasha na tafadhali sahauni kuhusu sugu
24. Maana atazidi tu kuleta mavurugu
25. Na kuwanyonga watu simo
26. Labda ganja zamani kidogo nilikuwemo
27. Na ndo mana mpaka leo bado inanipa misimamo
Ah moto chini
Chanzo: Mr. 2 (2009), Veto
Hapa tunaona msanii anatumia kina cha mwisho -na (mstari wa 1 na wa 2); kina cha mwisho -nal (no)
katika mstari wa 5 na wa 6; kina cha mwisho -ni katika mstari wa 7 hadi wa 10. Vina vingine
vinavyotumika, ni kina cha mwisho -nda katika mstari wa 11 hadi 14; kina cha mwisho -ra katika
mstari wa 17 hadi wa 20; kina cha mwisho -sha katika mstari wa 21 hadi wa 22; -gu katika mstari wa
23 na 24 na kina -mo katika mstari wa 25 hadi wa 27. Hata hivyo, kuna mistari kama vile mstari wa 3
na 4 na mstari wa 15 na 16 ambayo haina urari wa vina. Mistari hii isiyokuwa na urari wa vina
hutumika kama mistari ya mpito inayomwezesha msanii kubadilisha sauti na kuingiza vina vipya
ambavyo ni tofauti na vina vya awali. dhima kubwa ya matumizi haya ya vina ni kwamba yanalifanya
shairi liimbike. Pia vina huweza kuleta mapigo ya kimuziki.
(iv)Matumizi ya Mapigo katika Ushairi wa Bongo Fleva
Aidha, ushairi wa Bongo Fleva unatumia pia mapigo. Mapigo ndio sifa inayoufanya muziki
utofautiane na maongezi mengine ambayo si muziki. Mapigo husababishwa na marudio ya sauti au
sauti zilizopangwa kwa mpangilio maalumu. Dunleavy (1992:9) anaeleza kwamba mapigo ndio msingi
109
wa muziki wowote ule. Ushairi wa Bongo Fleva kwa kuwa ni sehemu ya ushairi nayo yanatumia
mapigo. Mapigo haya zaidi ya kuufanya utungo husika kuweza kuimbika au kughanwa, yanaufanya
utungo huo kutimiza sifa za kuwa ushairi, na hivyo kazi ya fasihi simulizi.
Hata hivyo, kumekuwa na mjadala miongoni mwa wanafasihi kama Bongo Fleva ni ushairi au
sanaa za maonyesho. Mahenge (2009) anaushughulikia kwa kina mjadala huo. Kwa kuwa utafiti huu
hasa unachunguza matini, yaani Bongo Fleva kama ushairi (taz. mawanda ya utafiti katika 3.2.7),
tunaona kwamba Bongo Fleva ni ushairi kama nyimbo za miziki mingine. Hii inatokana na ukweli
kwamba sifa tulizozijadili hapa nyingi zinaufanya uwe na sifa nyingi za kishairi kuliko za sanaa za
maonyesho. Mtazamo huu unaungwa mkono na Omari (2009), Suriano (2006 na 2007) na wasanii
waliohojiwa katika utafiti huu.
(v) Matumizi ya Methali katika Ushairi wa Bongo Fleva
Zaidi ya matumizi ya mapigo, ushairi wa Bongo Fleva unatumia pia methali. Methali kwa mujibu
wa Mulokozi (1996:36) ni usemi mfupi wa kimapokeo unaodokeza kwa muhtasari fikra na mafunzo
mazito yaliyotokana na tajriba (uzoefu wa maisha) ya jamii husika. Matumizi ya methali katika ushairi
wa Bongo Fleva, yanamaanisha kwamba ushairi huu unakusudia kutoa mafunzo. Maelezo haya
yanaweza kupinga madai yaliyoelezwa hapo awali kwamba ushairi wa Bongo Fleva hupotosha jamii.
Ushairi wa Bongo Fleva, kama tanzu zingine za fasihi simulizi, una dhima ya kuielimisha jamii. Mifano
ya matumizi ya methali yanaonekana katika wimbo wa Zay B uitwao “Siwezi Kuacha.” Anasema:
1.Hii fani jamani haihitaji kiwewe
2.Dua la kuku halimpati mwewe
3.Wacha kupiga mayowe
4.Na kama unaota aliyeko juu mngoje chini
5.Utaingia kaburini bado sijashuka chini
6.Game nalinyaka siyo kama najaribu
7.Vichwa vya kuku hapa mmegonga mwamba
Chanzo: Omari (2009:348)
Methali “dua la kuku halimpati mwewe” na “aliyeko juu mngoje chini” zinasaidia kufikisha maudhui
yake kwa njia. Kwa mfano, katika methali ya kwanza, msanii anaeleza kwamba yeye yupo juu ya
wengine na kwamba wenzake wanamuombea mabaya lakini hayatamfika. Anajifananisha na mwewe na
kuwafananisha adui zake na kuku.
Vilevile matumizi ya methali yanaonekana katika wimbo uitwao “Niko Gado” ulioimbwa na
Zay B. Hebu tuangalie ubeti ufuatao:
1. Domo kama chai jaba makelele mtindo mmoja
2. Mtoto hunyamazi usiniletee pose mambo huyawezi
3. Kama pikipiki basi we batavuzi
4. Kama msichana we kiluzi
5. Huwezi kucheza na anga hizi
6. Kubwa zima kikojozi
7. Ukiulizwa eti oh nilipitiwa na njozi
8. Kumbuka akunyimae mbaazi akupunguzia mashuzi
9. Nakuja live kwako full dose
10.Mimi ndio nyakanga tayari kukupa kozi
11.Bado mpaka mtu atoe machozi
Chanzo: Omari (2009:333)
Kwa kutumia methali “akunyimae mbaazi akupunguzia mashuzi” msanii anakusudia kuwaeleza
wapinzani wake na hasa Sister P ambaye alikuwa anamtenga na kukwepa kushirikiana naye kwamba
anampunguzia “mashuzi.” Methali hii kwa hakika inasaidia kuwasilisha ujumbe wake kwa njia ya
majigambo.
(vi)Matumizi ya Misimu katika Ushairi wa Bongo Fleva
Ushairi wa Bongo Fleva vilevile unatumia kwa kiasi kikubwa lugha za misimu (Omari, 2009:162).
Misimu ni maneno yanayozuka katika kipindi fulani cha kihistoria na kutumiwa na kikundi maalumu
cha watu na hatimaye huweza kupotea. Mulokozi (1996:42) anabainisha kwamba misimu inaweza
kushika mizizi na ikaingizwa katika methali au misemo ya jamii husika. Pia misimu huweza kuingizwa
110
na kuwa msamiati rasmi wa lugha husika. Kuna misimu ya makundi mbalimbali ya wanajamii: misimu
ya wanafunzi, misimu ya wanajeshi, misimu ya madreva, misimu ya wasanii wa Bongo Fleva na
kadhalika. Misimu hii hueleweka na kundi maalumu la watu lakini wakati mwingine huweza
kueleweka kwa jamii pana zaidi.
Ushairi wa muziki wa kizazi kipya umesheheni hazina kubwa ya misimu. Moja ya sababu
zilizoufanya muziki huu hapo awali usikubalike na uonekane wa kihuni ni matumizi ya misimu.
Misimu mingi inayotumika katika muziki huu ni misimu ya vijana ambao wengi wao ndio
wameathirika na suala la ukosefu wa ajira na hivyo kuishia kukaa vijiweni na kutumia madawa ya
kulevya. Aidha, kutokana na ukosefu wa ajira vijana wengi wameishia kuwa wevi, vibaka,
machangudoa, na kujiingiza katika vitendo vingine vinavyoonekana katika jamii kama uhuni. Kutokana
na hili hata misimu inayotumiwa na vijana inaonekana katika jamii kama misimu ya kihuni. Kwa hiyo,
matumizi ya misimu hii yaliufanya muziki huu nao uonekane wa kihuni.
Matumizi ya misimu, hata hivyo, hayapaswi kuchukuliwa kuwa ni kitu hasi bali ni chanya kutokana
na ukweli kwamba misimu ina dhima kubwa katika lugha. Baadhi ya dhima za misimu katika lugha ni
pamoja na kukuza msamiati wa lugha, kupunguza makali ya maneno na kuonesha hisia za watumiaji
wake. Pale misimu inapokua na kusanifiwa, inasaidia kukuza lugha husika. Vilevile matumizi ya
misimu huweza kutunza historia ya jamii husika kutokana na ukweli kwamba misimu husawiri kipindi
cha kihistoria ilipoibuka. Kwa ujumla matumizi ya misimu yanafanya ushairi wa Bongo Fleva kuwa na
dhima kubwa katika jamii. Miongoni mwa misimu iliyotumika katika ushairi wa Bongo Fleva ni
sharobaro (kijana msafi), demu (mpenzi/mwanamke), gemu (muziki), Bongo (Tanzania/Dar es
Salaam), dolali (dola) na kadhalika.
(vii) Usambamba katika Ushairi wa Bongo Fleva
Zaidi ya matumizi ya misimu, ushairi wa Bongo Fleva, hutumia pia usambamba. Kahigi na
Mulokozi (1979:49) wanafasili usambamba kuwa ni takriri ya sentensi au vifungu vya maneno vyenye
kufanana kimaana au kimuundo. Wanaendelea kwa kueleza kwamba usambamba ni sifa muhimu katika
ushairi simulizi. Hivyo, tunaweza kusema kwamba kuna aina mbili za usambamba, usambamba wa
kimuundo na ule wa kisemantiki/kimaana. Matumizi ya usambamba katika fasihi simulizi yanasaidia
kuunda fomula itakayomsaidia fanani kutunga jigambo lake papo kwa papo bila kukariri (Lord,
1981:54). Mfano mzuri wa usambamba tunauona katika wimbo uitwao “Sisi Tulivyo” ulioimbwa na
Sister P:
1. Sisi tulivyo kama utakavyoniona ndio nilivyo
2.Mimi nilivyo siko sawa na jinsi ulivyo
3.Mimi nilivyo hata unavyodhani sivyo nilivyo
4.Mimi nilivyo huwezi kunitambua jinsi nilivyo
5.Mimi nilivyo na huu ndio ukweli wa jinsi nilivyo
6.Mimi nilivyo siyo sawa na manabii jinsi walivyo
7.Mimi nilivyo nina hekima kuliko mtu mzima alivyo
8.Mimi nilivyo na hadhi zaidi ya wafalme jinsi walivyo
9.Mimi ni mchamungu kuliko ulivyo
10.Mimi nilivyo napenda mademu jinsi walivyo
Chanzo: Omari (2009:295-296)
Kutokana na matumizi haya ya usambamba, msanii anawezeshwa kuendelea kuimba ushairi wake bila
kulazimika kukariri shairi zima. Msanii anakariri fomula ya msingi inayojirudiarudia na kisha
kuongezea maneno katika fomula hiyo na hivyo kuunda mstari mpya.
(i) Wahusika katika Ushairi wa Bongo Fleva
Mbali na kipengele cha mtindo, kipengele kingine cha kifani cha ushairi wa Bongo Fleva ambacho ni
muhimu kukijadili hapa ni wahusika. Kama tulivyoona katika majigambo ya majina ya wasanii wa
Bongo Fleva, wahusika wa ushairi wa Bongo Fleva kwa ujumla ni binadamu, wanyama, viumbe wasio
binadamu au hata viumbe wasiokuwa na uhai. Maelezo ya kina kuhusu wahusika wa ushairi wa Bongo
Fleva yametolewa katika kipengele cha majigambo ya majina ya wasanii wa Bongo Fleva hapo awali,
hivyo, hatuna haja ya kukirudia kwa kina hapa.
111
SURA YA SITA
UAINISHAJI WA USHAIRI WA KISWAHILI
Uainishaji ni neno lililozaliwa kutoka katika dhana “aina” yaani namna mbalimbali ya vitu. Hivyo
uainishaji ni kupanga vitu katika aina, namna au makundi. Uainishaji wa ushairi wa Kiswahili pia ni
eneo lingine ambalo ni gumu kulieleza kwa maneno mawili matatu. Ugumu huu unatokana na ukweli
kwamba zipo namna mbalimbali za kueleza aina za ushairi wa Kiswahili. Uainishaji wa awali kabisa
wa ushairi wa Kiswahili ni ule uliofanywa na Mnyampala (1975) ambapo, kama tulivyobainisha awali,
anataja aina tano za mashairi kwa kuzingatia maongozi na mafunzo yanayotoa. Uainishaji kama huu wa
kuzingatia maongozi na mafunzo unaonekana pia kwa El Kaiim (1985:33-44). Yeye anabainisha
kwamba aina za mashairi ni pamoja na mashairi ya kusifu, kutukana, kuomba dua, kutoa shukrani,
kuapiza, kulaumu na kusimanga. Hapa tunabaini jambo moja kwamba El Kaiim anatambua uwezekano
wa shairi kutumia lugha ya utusi ambapo Mnyampala alidai kwamba hauwezi kuitumia. Zaidi ya hawa,
wapo pia wanaoona kwamba kuna aina kuu mbili za ushairi wa Kiswahili ambapo wanaanisha ushairi
wa kimapokeo (huitwa pia ushairi wa jadi) na ushairi wa kisasa (huitwa pia ushairi wa kimamboleo).
Wanazuoni wengine wanaanisha ushairi katika aina kuu tatu ambazo ni mashairi ya simulio, mashairi
ya kidrama na mashairi ya kiwimbo (taz. Shabaya na wenzake, 2009:7).
Jambo moja tunaloliona hapa ni kwamba kila uainishaji unaweza kuwa sahihi kwa namna yake
kwani kila mmoja kati yao ametumia vigezo vyake. Kwa mfano, tunaona uainishaji wa Mnyampala na
El Kaiim unazingatia zaidi kigezo cha dhima ya shairi husika. Kwa namna fulani, Mnyampala pia
anazingatia kigezo cha uhodari na ubora wa shairi husika na hasa anapoainisha aina kama mashairi
mazito, yaani yenye maudhui ya msingi, bila shaka akiyatofautisha na mashairi mepesi, ambayo hayana
maudhui muhimu au ya msingi. Shabaya na wenzake (khj.) wao wanaonekana kuelemea zaidi kigezo
cha mtindo. Hivyo tuhitimishe kwamba kuna vigezo vingi sana vinavyoweza kutumika kuainisha
ushairi na mashairi kwa ujumla. Vifuatavyo ni baadhi ya vigezo vinavyoweza kutumika katika
kuainisha ushairi wa Kiswahili:
· Kigezo cha aina ya uwasilishaji
· Kigezo cha umbo
· Kigezo cha mbinu za kisanaa zinazotumika
· Kigezo cha maudhui yabebwayo na shairi
· Kigezo cha idadi ya mistari
· Kigezo cha bahari
1. Kigezo cha Aina ya Uwasilishaji
Katika kigezo cha uwasilishaji kinachoangaliwa ni jinsi utanzu husika ulivyowasilishwa, yaani
ikiwa umewasilishwa kwa maandishi au kwa masimulizi. Hivyo katika kigezo hiki cha uainishaji kuna
aina kuu mbili za ushairi ambazo ni ushairi simulizi na ushairi andishi. Ushairi simulizi ni ule ambao
unawasilishwa kwa njia ya masimulizi ya mdomo na mara nyingi huambatana na matendo. Ushairi huu
unahusisha nyimbo mbalimbali kama vile nyimbo za kubembelezea watoto, nyimbo za jandoni na
unyagoni, mbolezi na aina nyinginezo. Aina hii ya ushairi tumeieleza kwa kina katika tanzu za ushairi
wa fasihi simulizi. Aina ya pili ni ushairi andishi. Huu ni ule ushairi ambao unawasilishwa kwa kutumia
hati za maandishi. Mpaka sasa katika lugha ya Kiswahili kuna diwani nyingi zilizokwisha kuandikwa.
Tahadhari haina budi kuchukuliwa hapa kwamba upo uwezekano wa mashairi simulizi kuwekwa katika
maandishi na pia mashairi andishi kusimuliwa. Hata hivyo, mashairi simulizi yanapoandikwa
hayapotezi sifa zake za kisimulizi hali kadhalika na mashairi andishi yanapokuwa simulizi hayapotezi
sifa zake za kuwa andishi.
2. Kigezo cha Umbo
Kigezo cha umbo cha uainishaji wa mashairi kinategemea umbo la shairi husika. Mashairi huweza
kuwa na maumbo mbalimbali ambapo yanaweza kuwa na umbo la kinathari (kisimulizi), umbo la
kitamthilia (kimajibizano) au umbo la kiwimbo. Mashairi ya kisimulizi ni yale yanayosimulia kitu kwa
112
namna ya hadithi. Mashairi haya hufuata kanuni za usimuliaji wa hadithi. Tendi nyingi huwa ni aina hii
ya mashairi maana hubeba hadithi fulani inayosimuliwa.
Zaidi ya aina hiyo, aina nyingine ya ushairi kwa kigezo cha umbo ni ushairi wa kimajibizano.
Ushairi huu huitwa pia ushairi wa kitamthilia au kidrama kwa maana kwamba unafuata kanuni za
kimajibizano. Mashairi haya huwa na wahusika ambao wanajibizana kwa kutumia kauli zao ambazo ni
tofauti na kauli ya mshairi. Wakati mwingine aina hii ya mashairi huweza kuwa na mhusika mmoja tu
ambaye anajibishana na nafsi yake au mhusika anayejibishana na hadhira. Hadhira hiyo inaweza kuwa
dhahiri au ya kufikirika. Sifa kubwa ya mashairi haya ni kuwa na mgogoro, mgogoro ambao unamfanya
mhusika kujibishana na mhusika mwenziye, nafsi yake au hadhira.
Aina ya mwisho ya ushairi kulingana na umbo ni ushairi wa kiwimbo. Ushairi huu huwa na beti na
mistari iliyopangwa vema katika urari wa vina na mizani ili liweze kuimbika. Aina hii ya ushairi ndiyo
iliyokuwa maarufu sana kabla ya kuibuka kwa mashairi ya kisasa miaka ya 1960. Hivyo, hoja ya Amri
Abedi kwamba shairi ni wimbo na kama haliimbiki halina maana yoyote huenda ilitokana na kutawala
kwa aina hii ya mashairi.
3. Kigezo cha Mbinu za Kisanaa Zinazotumika
Kigezo cha tatu cha uanishaji wa ushairi ni kigezo cha kuzingatia mbinu za kisanaa zilizotumika
katika shairi husika. Mbinu za kisanaa tunazozizungumzia hapa ni vina na mizani, miongoni mwa
nyinginezo. Shairi laweza kutungwa kwa kuzingatia urari wa vina na mizani au lisizingatie kanuni hiyo.
Mashairi yanayozingatia kanuni hiyo huitwa ya kimapokeo na mashairi yasiyozingatia huitwa ya
kisasa. Hivyo kwa kutumia kigezo hiki tunapata aina kuu mbili za ushairi: ushairi wa kimapokeo na
ushairi wa kisasa.
Ushairi wa kimapokeo, kama tulivyoeleza awali ni ule wa kijadi, yaani uliokuwapo katika jamii
kwa muda mrefu. Ushairi huu, zaidi ya mambo mengine, unazingatia urari wa vina na mizani kama sifa
yake kuu. Shairi ambalo halizingatii kanuni hiyo huchukuliwa na wanamapokeo kuwa si shairi ama ni
shairi lisilokuwa na ubora wowote. Ushairi wa kisasa kwa upande mwingine ni ule ulioibuka baadaye
na hauzingatii urari wa vina na mizani. Katika aina hii ya ushairi, urari wa vina na mizani si kanuni ya
lazima, shairi laweza kutumia au lisiitumie kanuni hiyo. Kwa kuwa wanausasa hutambua pia mashairi
yenye urari wa vina na mizani kama aina mojawapo ya ushairi wa kisasa, ila si aina pekee, njia bora ya
kumjua mshairi wa kisasa ni kwa kusoma mashairi yake kadhaa na kuona ikiwa yote yanatumia kanuni
hiyo au la. Kama kanuni hiyo haionekani katika mashairi yote basi tunasema kwamba mshairi husika ni
mshairi wa kisasa, lakini kinyume chake tunamchukulia kwamba ni mshairi wa kimapokeo. Mashairi ya
kisasa yasiyozingatia kabisa urari wa vina na mizani huitwa pia mashairi huru, mashairi guni, masivina
na istilahi nyingine kadha wa kadha.
Japokuwa dhana hizi za usasa na umapokeo zimetumika sana katika ushairi wa Kiswahili na kuota
mizizi lakini Samwel (2012a) alihoji usahihi wa dhana hizo ikiwa kweli ni sahihi kuwaita washairi
wanaozingatia kanuni ya urari wa vina na mizani kwamba ni wanamapokeo na wale wasiozingatia
kanuni hiyo wanausasa. Hoja ya Samwel ni kwamba, ushairi usiozingatia urari wa vina na mizani ndiyo
mkongwe kwani hata ushairi simulizi wa Kibantu uliojibainisha katika nyimbo mbalimbali kama vile
mbolezi, nyimbo za jandoni na kadhalika haukuzingatia kanuni hiyo. Hivyo, kwake yeye wanaoitwa
wanamapokeo si wajadi hasa bali ni washairi wa kisasa kwani mtazamo wao si mkongwe bali
ulikuwapo tangu zamani katika jamii mbalimbali. Wanausasa ndiyo wanaostahili kuitwa wanamapokeo
kwani wao wanaturudisha katika ujadi. Mashairi ya Kiswahili yanayozingatia urari wa vina na mizani
uliibuka baada ya Waarabu kuja na kuuathiri ushairi wa Kibantu uliokuwapo. Mtazamo huu wa Samwel
ni muhimu kwani unatoa changamoto kubwa katika mambo ya kinadharia yaliyoonekana kuwa sahihi
kwa muda mrefu.
4. Kigezo cha Maudhui Yabebwayo na Shairi
Kigezo cha maudhui cha uainishaji wa mashairi kinazingatia nyanja ya maisha iliyoangaziwa na
shairi husika. Shairi huweza kubeba maudhui ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni. Hivyo,
tunaweza kusema kwamba kwa kutumia kigezo hiki kuna aina nne za ushairi ambazo ni ushairi wa
kisiasa, ushairi wa kiuchumi, ushairi wa kijamii na ushairi wa kiutamaduni. Hata hivyo, kigezo hiki ni
telezi mno kwani upo uwezekano wa kuwa na shairi ambalo linasawiri nyanja zaidi ya moja ya maisha.
113
Kwa mfano, shairi laweza kusawiri masuala ya kisiasa lakini wakati huo huo likigusia mambo
mbalimbali ya kijamii na kadhalika.
5. Kigezo cha Idadi ya Mistari
Uainishaji huu huyagawa mashairi katika makundi kulingana na idadi ya mistari katika kila ubeti
wa shairi husika. Shairi huweza kuwa na mstari mmoja katika ubeti hadi mistari kumi na kuendelea,
kila shairi lina jina lake kulingana na idadi ya mistari. Miongoni mwa aina za mashairi tulizonazo kwa
kutumia kigezo hiki ni: tathmina, tathnia, tathlitha, tarbia, takhmisa, tasdisa, tasdia, naudia, telemania
na ukumi.
(i) Tathmina: hili ni shairi lenye mshororo mmoja katika kila ubeti.
(ii) Tathnia: ni shairi lenye mistari miwili katika kila ubeti. Aina hii ya mashairi huitwa pia uwili.
(iii)Tathlitha: aina hii ya ushairi huitwa pia utatu kutokana na ukweli kwamba ni aina ya mashairi
yenye mishororo mitatu katika kila ubeti. Kwa kuwa inadaiwa kwamba bahari ya wimbo huwa
na mistari mitatu kwa kila ubeti mashairi ya utatu huitwa pia wimbo.
(iv)Tarbia: mashairi ya tarbia huitwa pia unne kwa sababu yanakuwa na mistari minne kwa kila
ubeti.
(v) Takhmisa: hili ni shairi lenye mistari mitano katika kila ubeti. Mashairi haya huitwa utano.
(vi)Tasdisa: tasdisa huitwa pia tashilita, sudusia na usita. Haya ni mashairi yenye mishororo sita
katika ubeti.
(vii) Tasadia: ni aina ya mashairi ambayo huwa na mistari saba katika kila ubeti. Hivyo, huitwa pia
usaba.
(viii)Naudia: ni shairi lenye mishororo nane katika ubeti. Huitwa pia unane.
(ix) Telemania: ni shairi lenye mishororo tisa. Huitwa pia utisa.
(x) Ukumi : ni shairi lenye mishoro kumi.
6. Kigezo cha Bahari
Kwa muda mrefu kigezo cha bahari kimetumika kuainisha mashairi ya kimapokeo. Hii inatokana na
ukweli kwamba waandishi wengi wa awali walizingatia kwamba katika kigezo hiki cha uainishaji wa
mashairi kwa kutumia bahari kinachozingatiwa zaidi ni idadi ya mistari iliyopo katika beti na jinsi
mistari hiyo ilivyogawanywa katika vipande. Sifa ya shairi kuwa na beti na mistari inaonekana katika
mashairi ya kimapokeo tu. Kutokana na hilo uainishaji huu kwa muda mrefu umeitwa bahari za
mashairi ya kimapokeo au bahari za mashairi ya kijadi (taz. Mulokozi, 1996:125-135).
BAHARI ZA USHAIRI WA KIMAPOKEO
Kumekuwa na mvutano miongoni mwa wanazuoni na wataalamu wa ushairi juu ya dhana hii ya
bahari na hasa katika kueleza idadi ya bahari zilizopo na bahari hizo ni zipi hasa? Wapo wanaodai
kwamba kuna bahari tatu, wengine tano na kadhalika. Aidha, wapo wanaoona kuwa bahari hizi
zinahusisha aina za mashairi kimuundo kama tulivyoeleza katika kigezo cha idadi ya mstari na wapo
wanaopinga hilo. Kwa mfano, uainishaji wa bahari wa Mutua (2006:18-20) unahusisha pia tathmina,
tathnia, tathlitha, tarbia, takhmisa, tasdisa, kikai, msuko, sarakani na kadhalika. Uainishaji huu unaweka
pamoja uainishaji wa mashairi kwa kuzingatia idadi ya mistari na kwa kuzingatia kile kinachoitwa na
wengine bahari. Lakini bila kujiingiza katika mjadala wa idadi ya bahari na uhakika wa bahari hizo,
tutapitia hapa bahari zote zinazotajwa kuwapo katika ushairi wa kijadi. Kwa kuwa “bahari” za ushairi
kwa kuzingatia idadi ya mistari tumeshazibainisha hapo awali, katika sehemu hii bahari tutakazozipitia
ni shairi, wimbo, utenzi/utendi, ngonjera, kikwamba, zivindo, ukawafi/kawafi, ukara, wajiwaji,
Hamziyya, Mandhuma, msuko, wawe, sarakani, kimai na kikai.
(i) Shairi
Ni utungo wenye mishororo minne kila ubeti na vipande viwili vya mizani nane nane kila kipande.
Hii ndiyo bahari maarufu zaidi katika utunzi wa mashairi ya Kiswahili na watunzi wengi wa ushairi wa
Kiswahili wamezingatia sifa hii. Mfano ni shairi liitwalo “Tukomesheni Ajira za Watoto” katika Mutua
(2006:32):
Natunga nikiwaasa, watoto kutowajiri
Nawaelezea hasa, ya mambo yalivyojiri
114
Ni kinyume shika sasa, huo ukweli mukiri
Komeni tena komeni, watoto kuwaajiri
Wa ubwana kupigia, nyingi mali kuzalisha
Migongo wamedandia, ya wana kutumikisha
Damuyo kujinyonyea, ili kujitajirisha
Komeni tena komeni watoto kuwaajiri
Katika shairi hili tunaona kuwa kila ubeti una mistari minne iliyogawanyika katika vipande viwili na
kila kipande kina mizani nane (jumla mizani kumi na sita). Kwa mfano, mstari wa kwanza wa ubeti wa
kwanza “Natunga nikiwaasa, watoto kutowajiri,” kipande cha kwanza ni “natunga nikiwaasa” na
kipande cha pili “watoto kutowajiri.” Kipande “natunga nikiwaasa,” kina mizani nane (na-1, tu-2, nga-
3, ni-4, ki-5, wa-6,a-7,sa-8) na kipande “watoto kutowajiri,” kina mizani nane (wa-1, to-2, to-3, ku-4,
to-5, wa-6, ji-7, ri-8)
(ii) Wimbo
Kwa mujibu wa wanamapokeo bahari ya wimbo inahusisha utungo wenye mishororo mitatu katika
kila ubeti. Kila mshororo huwa na vipande viwili. Wimbo unaweza kuwa na vina au la. Bahari hii ni ya
kijadi na imekuwapo kwa muda mrefu sana katika historia ya ushairi wa Kiswahili. Mfano mzuri wa
wimbo tunauona pia katika Mutua (2006:30). Wimbo huo umepewa jina “Haki za Binadamu:”
Kwa jina lake Jalia, muumba wa nchi na mbingu
Aloumba nisia, na wengi viumbe chungu
Rabi mola metimia, kwake hakuna tewengu
(iii) Utendi/Utenzi
Ni shairi refu lenye beti nyingi ambazo zina mizani chache au mishororo mifupi ambayo kwa asili
haina vina vya kati kama yalivyo mashairi ya kawaida. Tenzi/tendi kwa kawaida huwa na maudhui ya
kidini, vita, ushujaa, tukio la kizamani au la historia. Utendi huweza kugusa pia maisha ya mashujaa:
kuzaliwa, shida zao, vita na matendo yao ya kishujaa, vifo vyao, nk. Matukio haya huwa ya kihistoria
ila huweza kuchanganya na visakale na visasili. Mifano mizuri ya tenzi ni: Utenzi wa Nyakiiru Kibi,
Utenzi wa Adamu na Hawaa, Utenzi wa Fumo Liyongo, Utenzi wa Vita vya Maji Maji na Utenzi wa
Vita vya Mau Mau.Kwa mfano, Utenzi wa Nyakiiru Kibi unaelezea historia ya ukoo wa Babito na
kiongozi wao aitwaye Nyakiiru Kibi. Utenzi huu una beti mia nane tisini na mbili (892). Utenzi wa
Adamu na Hawaa ni mrefu pia na unaelezea maudhui ya kidini ambayo pia yanaaminika kuwa ya
kihistoria na kadhalika.
Bahari ya utendi/utenzi imezua mjadala miongoni mwa wanafasihi kwa muda mrefu. Ruth Finnegan
(1970) alidai kwamba utendi haupo katika bara la Afrika. Finnegan alielemea vigezo vikuu vinne vya
utendi Kiaristotle. Sifa hizo ni:
a) Nudhumu (verse): utendi uwe ni utungo wa kishairi na si wa kinathari
b) Urefu (length): ni utungo mrefu wa kutosha
c) Uunganifu (unity): ni utungo wenye visa/hadithi vilivyounganika kimantiki katika mtiririko
na msuko wake wa matukio na si matukio mparaganyiko yasiyohusiana.
d) Maudhui (subject matter): husimulia juu ya maisha na matendo ya kishujaa ya mbabe wa
utendi, kwa mfano kuzaliwa, masaibu yake, safari zake, uongozi wake kwa watu wake na kifo
chake.
Baada ya kuchunguza matini kadhaa zilizodaiwa na wahariri wake kuwa ni tendi akafikia
hitimisho kwamba tendi hazipo katika bara la Afrika kwani hizo si tendi. Nyingi kati ya matini hizo
wahariri wake hawakuzitoa katika muundo wa kishairi hivyo kuishia kuwa masimulizi ya kinathari.
Miongoni mwa matini hizo ni Sundiata, Mugasha na Mwindo. Kauli hii ya Finnegan ilizua mjadala
mzito na kama anavyosema Mulokozi (2002:2) miaka ya 1970 ilichukuliwa kuwa ni ya mjadala wa
kauli hiyo. Hata hivyo, kwa sasa mjadala huu umefikia mwisho kwani wataalamu wanakubaliana
kwamba Afrika ina tendi. Mjadala uliosalia sasa ni tendi hiyo ya Kiafrika ipoje?
Tunaona utendi tuuchukulie kwa Mtazamo wa Mulokozi (2002) kwamba una sifa zifuatazo:
(a) Ni masimulizi
(b) Hutolewa kishairi
(c) Huhusu matukio muhimu ya kihistoria na kijamii
115
(d) Huelezea habari za ushujaa na mashujaa
(e) Huwasilishwa kwa kughanwa (au kuimbwa) pamoja na ala za muziki
(f) Hivyo, utendi hutawaliwa na muktadha wa utungaji na uwasilishaji wake kwa jamii.
Zaidi ya kuchukua mtazamo wa Mulokozi (2002) kuwa ndiyo bora, tunaona sifa moja kati ya saba
alizozitaja hatutaitumia, matini (maneno) yake kwa kawaida hutungwa papo kwa papo, japo kisa au
hadithi yenyewe huwa ya kimapokeo. Sifa hiyo ni ile isemayo, “utendi haukaririwi (hautungwi kabla na
kuhifadhiwa kichwani kwanza ili baadaye utolewe kwa ghibu).” Tunaiacha sifa hii kutokana na ukweli
kwamba kutokana na mtazamo wetu, utendaji wa utendi na fani nyingi za fasihi simulizi (zilizodaiwa
kutendwa papo kwa papo) huhusisha kukariri kwa namna fulani.
Mulokozi (2002:127-170) anabainisha kwamba fanani wa utendi (na tanzu mbalimbali za fasihi
simulizi) hakariri bali hutunga kazi yake papo kwa papo wakati wa utendaji wake, kinachomsaidia
fanani kufanya hivyo ni topo na fomula iliyomo kichwani kwake. Mulokozi (khj.) anadai kwamba
fanani anakariri topo ambazo huzijazia maneno anayoyatunga wakati wa utendaji. Topo hizo huwa ni
hadithi nzima. Hata hivyo, tunaona kwamba topo hizi hukaririwa na hivyo bado kuna kukariri kabla ya
utendaji wake. Hii inatufanya tuone kwamba inaweza isiwe sahihi sana kusema kuwa tendi
hazikukaririwa.
(iv)Ngonjera
Mmbaga (2004:43) anafasili ngonjera kuwa ni utanzu wa ushairi ambamo twakuta mahojiano au
malumbano kati ya mhusika na mhusika, mhusika na wahusika au wahusika kwa wahusika. Hivyo,
twaweza kusema kuwa ngonjera ni ushairi wa majibizano ambao hutolewa baina ya watu wawili au
vikundi viwili vya watu kwa kupokezana. Mmbaga (khj.) anaendelea kubainisha kuwa ngonjera, tofauti
na nyimbo na mashairi, huwa haziimbwi bali husemwa. Katika ngonjera kunakuwa na majibizano
kuhusu mada fulani inayowatatiza wahusika au mmoja wa wahusika katika majibizano hayo na
mhusika mwingine hujaribu kumpa ufafanuzi juu ya mada hiyo. Kwa kawaida majibizano haya huwa ni
ubeti kwa ubeti ambapo mhusika mmoja hutoa ubeti mmoja na mwingine humjibu katika ubeti
unaofuata. Mfano mzuri wa ngonjera za aina hii tunaziona katika Mmbaga (khj.) kama anavyomnukuu
Muyaka:
MDENI
Nilime mnda Ngozini, ule wangu mjuawo
Pata kata ishirini, na mbili zipungushewo
Hawauza hutendani, nionyani zitendwawo
Mke yu ataka nguo, name nawiwa kikanda
RAFIKI
Karejee ngozi mbamba, winike yako mamungo
Mpiga n anti yembe, huinua nililo kongo
Mke mrari au membe, kwa kweli au kwa uwongo
Deni uongeze kiwango, mwenye deni takulinda
Katika ngonjera hii tunaona kuna wahusika wawili ambao wanajibizana juu ya suala la deni. Mmbaga
anaeleza kuwa mtindo huu wa ushairi ni mkongwe zaidi na ulionekana pia kwa malenga wa kale. Mbali
na majibizano kuwa katika ubeti kunaweza kuwa na majibizano katika mistari ambapo mhusika mmoja
anasema mstari mmoja na mwingine kumjibu katika mstari wa pili. Mfano mzuri wa ngonjera hizi pia
tunauona kwa Mmbaga (khj.) anapotoa ngonjera ya jadi ya Kipare:
Msimulizi
Ichua ne mvu velahane
Mvu
Uiao kidoho na singo wesina?
Ichua
Hanini weghereke ghati?
Mvu
Nihala nesila nicho neghereke ghati
Tafsiri:
Msimulizi
Chura na nyigu walishtakiana
Nyigu
116
Unalia bure wala shingo huna
Chura
Mbona wewe u mwembamba kiunoni?
Nyigu
Ni kwa vile mie sili ndio maana ni mwembamba kiunoni
Mifano mingine ya ngonjera tunaiona katika Mnyampala (1970) Ngonjera za UKUTA na Wamitila
(2005) Tamthilia ya Maisha miongoni mwa vingi vingine. Kwa mfano, shairi la “Kuhalalisha Maovu”
katika Wamitila (2005) lililoandikwa na Kineene wa Mutiso ni la kingonjera ambapo kuna majibizano
baina ya tajiri na mnyonge. Katika shairi hilo tunaona kuna majibizano baina ya tajiri na mnyonge
kuhusu utajiri unavyopatikana. Suluhisho la majibizano hayo linapatikana katika ubeti wa mwisho.
(v) Kikwamba
Hii ni bahari ambayo mashairi yake hutumia neno moja mwanzoni mwa kila mshororo. Hii ni
kusema kwamba mashairi haya huanza na neno lilelile katika mistari yake yote. Lengo la msingi la
takriri hii ni kusisitiza na pia kulipendezesha shairi husika kwa kuweka usambamba. Mfano mzuri wa
mashairi ya aina hii tunaona katika Muzale (2009) kwenye shairi la “Kifo” katika Diwani yake iitwayo
Nakuomba. Katika shairi hilo tunaona kuwa mshairi ameanza na neno “kifo” katika mistari yote ya beti
zake zote ishirini na mbili (22). Tazama, kwa mfano, ubeti wa kwanza na wa pili:
Kifo ninakuimbia, sauti kali hewani,
Kifo ninakulilia, chozi hadi miguuni,
Kifo ninakutungia, shairi lenye thamani,
Kifo ninakuinamia, bila kofia kichwani.
Kifo naomba tulia, sikio nalitamani,
Kifo nakusimulia, majonzi ya duniani,
Kifo sote tunalia, huzuni tele rohoni,
Kifo unatusumbua, hatuna tena amani.
(vi)Zivindo
Ni bahari ya kishairi ambayo mashairi hutungwa kwa lengo la kufafanua maana mbalimbali za neno
moja katika lugha ya Kiswahili. Kila lugha duniani, Kiswahili kikiwemo, ina maneno ambayo huwa na
maana mbalimbali. Maneno ya aina hii huweza kuwachanganya watumiaji wa lugha husika. Hivyo,
mashairi haya hukusudia kufafanua maana hizo na kukuza ujuzi wa lugha wa hadhira husika. mfano wa
zivindo tunaziona katika Muzale (2009:74-78) ambapo anafafanua maana za maneno “ulevi” na “utu”
katika mashairi aliyoyaita “Ulevi” na “Utu” mtawalia. Katika shairi la ulevi, mshairi anabainisha kuwa
kuna maana mbalimbali za neon ulevi. Anazitaja maana hizo kuwa ni ulevi wa pombe, bangi na hata
wanawake na kadhalika. Kuhusu utu anafafanua kuwa utu ni mtu kuwa na heshima kwa kusalimia
watu, kuwa na akili timamu, kufanya kazi kwa bidii na kadhalika. Tuchunguze shairi la “Ulevi:”
Kuna wa pombe ulevi, na wengi wake walevi,
Alobobea mlevi, aenda kama kiwavi,
Atalala kwenye jamvi, jamala yake ugomvi,
Hana heshima mlevi, hakosi kuwa mchimvi.
Moshi ulevi wa pili, kazi kuharibu mwili,
Mapafu yakihimili, wavuta bila kujali,
Sigara sumu ya mwili, tumbaku ni sumu kali,
Tumia yako akili, usitafute ajali.
Kulewa televisheni, hiyo nayo ni balaa,
Wanashinda barazani, macho wakiyakodoa,
Kabumbu peke kichwani, mengine wameyaondoa,
Ni ulevi si utani, ushabiki usiofaa.
(vii) Ukawafi au kawafi
Aina hii ya bahari huhusu shairi lenye mistari mitatu au zaidi na wenye vipande vitatu kila
mshororo huku kila kipande kikiwa na kina chake. Katika ushairi vipande hivi vina majina; kipande cha
117
kwanza huitwa ukwapi, cha pili utao na cha tatu mwandamizi. Muundo wa msingi wa bahari hii ya
ushairi huwa kama ifuatavyo:
Ukwapi utao mwandamizi
_________ ___________ ____________
Mfano mzuri wa mashairi yanayoingia katika bahari hii ni shairi la “Biashara” lililopo katika Mbarwa
(2000:11) kama linavyonukuliwa hapa chini:
Biashara ni hasara, huwaka moto, ni kujitolea
Haitaka fikara, ila mvuto, inaweza kolea
Mbiashara busara, impa mapato, na kuendelea
Inahitaji upangaji, ugunduzi, na uvumilivu
Ukaribishaji, utii utumizi, na utulivu
Awe mlipaji, mkakamizi, haitaki ulegevu
(viii) Ukara
Bahari hii mashairi yake huwa na vipande viwili katika kila mshororo, utao na ukwapi, huku
kipande cha pili, ukwapi, kikiwa na vina ambavyo ni irabu. Vina hivyo katika ukwapi, hata hivyo,
hubadilikabadilika katika kila mshororo. Mfano wa kufikirika wa ukara huweza kuwa kama
inavyooneka hapa chini:
Ubeti wa 1: ___________________ni, ________________a
___________________ni, ________________e
___________________ni, ________________i
___________________ni, ________________u
Ubeti wa 2: ___________________ni, ________________u
___________________ni, ________________i
___________________ni,________________e
___________________ni, ________________o
Ubeti wa 3: ___________________ni, _________________o
___________________ni, _________________e
___________________ni, _________________a
___________________ni, _________________u
___________________ni, _________________i
(ix)Wajiwaji au Takhmisa
Hii ni bahari ambayo huwa na mashairi yenye mistari mitano katika kila ubeti. Kutokana na hilo,
mashairi yote yenye mistari mitano huitwa takhmisa. Kwa kawaida mashairi haya huwa na mizani kumi
na tano (15) kila mshororo ambapo si lazima yawe na vina vya kati lakini una vina vya mwishoni.
Mfano mzuri wa aina hii ya mashairi ni “Takhimisa ya Liyongo” ambayo kimsingi yalikuwa yakimsifu
Fumo Liyongo, shujaa wa Kiswahili anayeaminika kuishi huko Pate. Mashairi haya yaitwayo
“Takhmisa ya Liyongo” yalitungwa na Sayid Abdalla Bin Ali bin Nasir. Tazama ubeti ufuatao:
Nabudi kawafi takhmisi kidiriji,
Niwathihishe izagale kama siraji,
Ili kufuasa ya Liongo samba wa miji,
Ai wanji nazawanji kisiza wanji; na
Kadiliza kasiliza, mwanangu mema
Mfano mwingine wa takhmisa unaonekana katika shairi la “Mkulima” katika Mbarwa (2000:36):
Hubarikiwa Mola na jasho lake
Yeye huwa saa zote shambani lake
Hujuwa vizuri ukubwa wa soko lake
118
Amejiajiri tayari shambani lake
Mkulima huwa na bidii na mpango kanuni
Hupata mkopo benkini ya washiriki
Huwa anapo kadri benkini ya ushiriki
Huwapo usahibu na wengine washiriki
Hupatia ananapo misaada na washiriki
Mkulima huwa na bidii na mpango kanuni
(x) Hamziya
Bahari hii ilipewa jina kutokana na utenzi maarufu wa Kiarabu ulioitwa Utenzi wa Hamziyya
ulitungwa na Mmisri Muhammad bin Said Al- Buswiri/al-Busiri ambao ulikuwa ni simulizi ya maisha
ya Mtume Mohammad (S.A.W). Utenzi huo ulipewa jina la Hamziya kutokana na ukweli kuwa ulikuwa
na urefu wa mizani thelathini (30) na uliishia na herufi ya 29 ya lugha ya Kiarabu. Katika herufi za
Kiarabu kuna herufi thelathini na herufi ya 29 huitwa hamza. Hivyo, kwa kuwa utenzi huu uliishia na
herufi ya ishirini na tisa (hamza) ndiyo ukapewa jina kutokana na herufi hiyo. Utenzi huu ulitafsiriwa
katika Kiswahili na Said Aidarus bin Athman kutoka Pate-Kenya mwaka 1652/1749. Hata hivyo,
izingatiwe kuwa tafsiri ya utenzi huo katika Kiswahili, kwa kuwa hautumii herufi za Kiarabu, hauishii
tena na herufi hamza ya Kiarabu (kama ilivyokuwa katika utenzi asilia) (Maelezo mengi kuhusu bahari
hii tumeyadondoa katika Mulokozi, 1996 na Kineene wa Mutiso, 2005). Kwa hiyo, katika Kiswahili
utenzi wowote wenye mizani thelathini, kama ilivyokuwa kwa Utenzi wa Hamziyya, unaingia katika
bahari hii ya ushairi.
(xi)Mandhuma
Mandhuma ni aina ya bahari ambapo mashairi yake huwa na ukwapi na utao isipokuwa ukwapi
hutoa wazo ambalo ni fumbo na kisha fumbo hilo linafumbuliwa katika utao. Mfano mzuri wa shairi
linaloingia kwenye bahari hii ni shairi la “Moyo” lililopo katika Wamitila (2005) Tamthilia ya Maisha
kama linavyonukuliwa katika ubeti ufuatao hapa chini:
Moyo waniambia ota, kuwa mwizi usiote, siwe kaini,
Moyo wanambia kata, mirija yote ikate, mizizini,
Moyo wanambia teta, penye dhuluma patete, andikoni,
Moyo wanambia woga, ndiyo mwanzo wa maafa.
(xii) Msuko
Msuko ni bahari ya ushairi ambayo huwa na kibwagizo, kibwagizo hicho, kwa kawaida huwa ni
kifupi (kina maneno machache) kuliko mishororo mingine katika ubeti husika. Mfano wa msuko
tunauona katika shairi la Mahiri Mwita liitwalo “Nimo” lililomo katika Wamitila (2005). Tazama ubeti
huu:
Nimo ndimo mi nilimo, simo simostahili,
Nimo niwajibikamo, simo mwenye ujahili,
Nimo nikusudiamo, simo wanamodhalili,
Nimo na nitakikamo, simo name kwa thakili,
Nimo kwa kina na kimo, simo mwa wasiobali
Nilimo nimo.
(xiii) Wawe/ Vave
Matamshi tofauti baina ya wawe au vave ni ya kilahaja. Wawe ni bahari ya ushairi inayohusisha
tungo za kishairi ambazo huimbwa wakati wa kufanya kazi, hasa kilimo (kufyeka, kulima, kukata
magugu, kuchoma moto magugu na kadhalika). Tungo hizi zinaweza kuwa na urari wa vina na mizani
au zisiwe nao. Mifano ya tungo hizi inapatikana katika Mulokozi (1996).
(xiv) Sakarani
Bahari hii ni mchanganyiko wa bahari kadhaa katika shairi moja. Hii ni kusema kwamba katika
bahari hii kuna aina mbalimbali za mashairi katika ubeti mmoja au katika shairi moja. Shairi linaweza
kuwa kikwamba na wakati huohuo likawa msuko, au shairi likawa wimbo na wakati huohuo likawa
119
kikwamba na kadhalika. Aidha, shairi moja linaweza kuwa na mashairi ya mistari mitatu, mistari
minne, mistari mitano, mistari sita na kadhalika. Mfano mzuri wa shairi la aina hii ni shairi la Mahiri
Mwita la “Nimo” tulilolinukuu hapo awali. Hebu tuchunguze tena ubeti huu:
Nimo ndimo mi nilimo, simo simostahili,
Nimo niwajibikamo, simo mwenye ujahili,
Nimo nikusudiamo, simo wanamodhalili,
Nimo na nitakikamo, simo name kwa thakili,
Nimo kwa kina na kimo, simo mwa wasiobali
Nilimo nimo.
Kwa hakika ubeti huu unakidhi sifa za kuwa katika bahari ya kikwamba, kwa maana ya kwamba shairi
linaanza na neno moja “nimo” katika kila ubeti, na pia unakidhi sifa za kuwa katika bahari ya msuko,
kwa maana ya kuwa lina kibwagizo kilichofupishwa. Vilevile shairi la Nyambari Nyangwine liitwalo
“Kilio cha Paka” katika Wamitila (2005) linaonekana kuwa na beti mchanganyiko, kuna beti zenye
mistari mitatu, beti zenye mistari mitano, beti zenye mistari sita, beti zenye mistari saba na kadhalika.
(xv) Kimai
Bahari ya kimai inahusu nyimbo zinazoimbwa katika shughuli mbalimbali za baharini. Hizi
hujumuisha nyimbo za mabaharia, wavuvi na wasafiri wa vyombo vya baharini. Nyimbo hizi hazina
idadi kamili ya vina na mizani na pia suala la urari wa vina na mizani si la lazima. Mifano mizuri ya
ushairi unaoingia katika bahari hii tunaiona katika Mulokozi (1996) na King’ei na Kisovi (2005)
miongoni mwa wengi wengineo. Kwa mfano, katika King’ei na Kisovi (2005:145) tunaona wimbo
ufuatao:
Mwana wa maji wa kale, mjuzi wa kazi yangu
Kufa maji nizowele, kufunda kazi yangu
Mwana wa maji na maji, maji yatanitendani?
(xvi) Kikai
Bahari hii, kwa kawaida, huwa na mishororo yenye vipande viwili, ukwapi na utao, ambapo kwa
asili yake huwa na mizani kumi na mbili (12), ambapo ukwapi huwa na mizani nne na utao mizani
nane. Bahari hii pia huhusisha mikondo mingine ya ushairi ikiwa ni pamoja na mashairi yenye mizani
nane kwa sita, nane kwa tatu na tano kwa nane (Mutua, 2009:19). Mutua (khj.) anatoa mfano wa shairi
la bahari hii lenye mizani tano kwenye ukwapi na nane kwenye utao kama ifuatavyo:
Likichomoza, jua liote haraka,
Likiangaza, mapema kazi rauka,
Likikoleza, hifadhi zako nafaka
Likituliza, basi nenda pumzika
UPUNGUFU WA KIGEZO CHA BAHARI ZA USHAIRI ZA KIMAPOKEO
Uainishaji wa ushairi kwa kigezo cha bahari umesemwa kuwa na mapungufu mengi. Mapungufu hayo
yamebainishwa kwa kina na Mulokozi (1996). Katika mjadala wetu tutabainisha udhaifu huo ili tufike
mahali na kuwa na muainisho ambao labda utakuwa bora kiasi cha kuondoa upungufu huo:
1. Kigezo hiki kinatumika kuainisha aina moja tu ya ushairi: ushairi unaoainishwa kwa kigezo
hiki, hadi sasa, ni ushairi wa kimapokeo. Hii ina maana kwamba kwa kutumia kigezo hiki
ushairi wa kisasa hauainishwi. Hii, kwa maana ya urejezi ni kwamba ushairi wa kisasa si ushairi
na hivyo haupaswi kuainishwa.
2. Kigezo hiki kinachanganya sana vigezo vingi vidogovidogo (bila kuvifafanua). Kuna baadhi ya
fasili za bahari ambazo zinatudokeza kwamba kigezo kidogo kilichotumika ni idadi ya mistari
lakini bahari nyingine zinadokeza kigezo cha urefu na aina ya mistari, nyingine ni maudhui,
muktadha na kadhalika. Hivyo, kuna mkanganyiko mkubwa sana hapa.
3. Bahari hizi zina ukomo wake, zipo aina nyingi za ushairi wa kijadi zinazoweza kutungwa
ambazo zinaweza zisiingie katika bahari yoyote kati ya hizo. Hatari iliyopo ni kwamba kuna
120
uwezekano wa ushairi wa aina hiyo kuonekana kuwa si ushairi kwani hauingii katika bahari
yoyote.
Kutokana na upungufu huu tunaona kwamba kuna haja ya kuainisha bahari kwa namna ambayo
itapunguza ama kuondoa kabisa kasoro hizo. Hivyo katika uainishaji wetu tumeainisha bahari kwa
kuzingatia aina zote za mashairi (mashairi ya kimapokeo na kisasa) na kwa kuzingatia vigezo
vilivyobainishwa wazi ili ijulikane wapi tunatumia kigezo gani kupata aina gani ya bahari.
BAHARI ZA USHAIRI WA KIMAPOKEO NA KISASA
Katika andiko letu tunachukulia kwamba uainishaji wa kutumia kigezo cha bahari ni uainishaji wa
ushairi unaoweza kutumika katika aina zote za ushairi. Aidha, tunachukulia kwamba kigezo hiki kina
vigezo vidogo vidogo vingi. Miongoni mwa vigezo hivyo ni kigezo cha vipande vya mishororo, kigezo
cha aina ya kiishilio, kigezo cha urari wa vina na mizani, kigezo cha uradidi, kigezo cha madhumuni ya
utungaji na kigezo cha muundo.
· Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Beti, Mishororo na Vipande
· Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Aina ya Kiishilio
· Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Urari wa Vina na Mizani
· Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Uradidi
· Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Madhumuni ya Utungaji
· Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Muundo
Kwa kuwa katika sehemu iliyopita tulishafafanua kwa kina bahari mbalimbali na kutoa mifano
ilipobidi, katika sehemu hii hatutoa maelezo marefu wala mifano mingi ya bahari hizo, isipokuwa pale
tu kutakapokuwa na haja ya kufanya hivyo.
1. Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Beti, Mishororo na Vipande
Katika kigezo hiki ushairi unaainishwa kwa kuzingatia shairi husika lina mishororo mingapi katika
beti na kila mshororo una vipande vingapi? Kwa kutumia kigezo hiki, kwa hiyo, tunapata aina zifuatazo
za mashairi:
(i) Shairi
Shairi ni dhana pana inayobeba aina nyingine za bahari. Bahari hii inajumuisha tungo zote ambazo
si za kinathari kwa uasili wake. Inajumuisha tungo zenye lugha ya mkato, lugha ya kishairi, na nduni
nyingine bainifu za ushairi kama tulivyobainisha hapo awali. Kwa hiyo, hata wimbo huweza kuwa na
mashairi, utendi huweza kuwa na mashairi na kadhalika.
(ii) Wimbo
Hii ni bahari ambayo inahusisha tungo zenye mishororo katika kila ubeti. Hata hivyo, idadi ya
mishororo katika ubeti inategemea uwezo wa mtunzi husika. Aidha, si lazima idadi ya mishororo katika
kila ubeti wa shairi husika ilingane, inaweza kutofautiana. Kwa kawaida kila mshororo katika bahari hii
huwa na vipande viwili, lakini yapo mazingira ambapo kaida hiyo huweza kukiukwa. Vilevile, wimbo
unaweza kuwa na vina au la.
(iii) Utendi/utenzi
Utendi ni shairi ambalo huwa na kipande kimoja cha mshororo na mizani chache katika mshororo
(kwa kawaida kati ya mizani nne hadi kumi na mbili). Utendi huwa na vina vya mwisho pekee na
huwa ni simulio (hadithi) ndefu kuhusu matukio ya kihistoria, mashujaa, dini na mambo mengineyo
mbalimbali.
(iv)Tumbuizo
Bahari ya tumbuizo huhusu tungo ndefu zenye mishororo mingi lakini si lazima ziwe na urari wa
mizani na vina. Kwa asili yake, tumbuizo zilikuwa na kina kimoja tu cha mwishoni au vina tofauti
katika mistari tofauti.
121
(v) Ukawafi au kawafi
Hii ni aina ya bahari inayojumuisha mashairi yenye mistari mitatu au zaidi na yenye vipande vitatu
kila mshororo huku kila kipande kikiwa na kina chake. Vipande hivyo ni: ukwapi, utao na
mwandamizi. Maudhui ya kawafi nyingi kuhusu dini ingawa zipo chache zizonahusu masuala ya
kidunia.
(vi)Wajiwaji au Takhmisa
Hii ni bahari ambayo huwa na mashairi yenye mistari mitano katika kila ubeti. Kutokana na hilo,
mashairi yote yenye mistari mitano huitwa takhmisa. Kwa kawaida mashairi haya huwa na mizani kumi
na tano (15) kila mshororo ambapo si lazima yawe na vina vya kati lakini una vina vya mwishoni.
(vii) Gungu
Hii ni aina ya ushairi ambao una mizani zaidi ya kumi na mbili katika kila mshororo na hali huwa
hivyo katika mishororo yote. Kwa hakika gungu ni aina mojawapo ya utenzi ila tofauti iliyopo baina ya
tenzi na gungu ni kwamba utenzi huwa na mizani michache katika mshororo wakati katika gungu
mizani huwa mingi zaidi. Tenzi huwa na mizani kati ya 4-12 wakati gungu huwa na mizani 12.
(viii) Mathnawi/ Mathinawi
Mathnawi ni aina ya bahari inayohusu mashairi ambayo kila mshororo huwa na vipande viwili:
ukwapi na utao na kwa hiyo huwa na vina viwili: vya kati na vya mwisho.
Ukwapi utao
____________________na _________________li
____________________na _________________li
____________________na _________________li
(ix)Bantundi
Bahari hii hujumuisha aina ya mashairi ambayo huwa na vipande vinne katika kila mshororo, yaani
ukwapi, utao, mwandamizi na ukingo. Kwa mfano:
Utao ukwapi mwandamizi ukingo
____________lo ______________ma ___________ni _____________mba
2. Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Aina ya Kiishilio
Katika kigezo hiki tunaainisha mashairi kwa kuzingatia kuwapo au kutokuwapo kwa kiishilio
(kituo), urefu au ufupi wa kiishilio na kadhalika. Kiishilio kama kinavyotumika hapa ni mshororo wa
mwisho katika ubeti ambao hujirudiarudia (kituo bahari). Kama mshororo husika haujirudii huitwa
kimalizio. Hivyo, kwa kutumia kigezo hiki tunapata aina zifuatazo za ushairi:
(i) Msuko
Msuko ni aina ya ushairi ambao kiishilio kimefupishwa, yaani kimesukwa kwa namna ambayo
kimekuwa kifupi zaidi kuliko kilivyopaswa kuwa kama kingetumia maneno ya kawaida. Mfano
unaonekana katika shairi la Mahiri Mwita litwalo “Nimo” tulilolinukuu hapo awali.
(ii) Sabilia
Sabilia ni aina ya ushairi ambao kwa kawaida hauna kiishilio bali huwa na kimalizio. Mshororo wa
mwisho katika aina hii ya ushairi huwa hakirudiwi bali kinabadilikabadilika na hivyo huwa kama
kimalizio tu lakini si kiishilio/kituo. Mfano mzuri wa mashairi haya unaonekana katika mashairi mengi
yaliyomo katika sehemu ya pili ya kitabu hiki.
3. Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Urari wa Vina na Mizani
Katika kigezo hiki ushairi huainishwa kwa kuzingatia kuwapo au kutokuwapo kwa urari wa vina,
urari wa mizani au vyote pamoja. Aidha, katika aina hii ya ushairi tunazingatia pia aina ya vina na
122
mizani iliyotumika katika shairi husika pamoja na namna vina na mizani hiyo ilivyopangwa. Kwa
kutumia kigezo hiki tunapata aina zifuatazo za ushairi:
(i) Wajiwaji au Takhmisa
Hii ni bahari ambayo huwa na mashairi yenye mistari mitano katika kila ubeti. Kutokana na hilo,
mashairi yote yenye mistari mitano huitwa takhmisa. Kwa kawaida mashairi haya huwa na mizani kumi
na tano (15) kila mshororo ambapo si lazima yawe na vina vya kati lakini una vina vya mwishoni.
(ii) Wawe/ Vave
Kama tulivyodokeza hapo awali, matamshi tofauti baina ya wawe au vave ni ya kilahaja. Wawe ni
bahari ya ushairi inayohusisha tungo za kishairi ambazo huimbwa wakati wa kufanya kazi, hasa kilimo
(kufyeka, kulima, kukata magugu, kuchoma moto magugu na kadhalika). Tungo hizi zinaweza kuwa na
urari wa vina na mizani au zisiwe nao.
(iii)Kimai
Bahari ya kimai inahusu nyimbo zinazoimbwa katika shughuli mbalimbali za baharini. Hizi
hujumuisha nyimbo za mabaharia, wavuvi na wasafiri wa vyombo vya baharini. Nyimbo hizi hazina
idadi kamili ya vina na mizani na pia suala la urari wa vina na mizani si la lazima.
(iv)Ukara
Hii ni bahari inayohusu mashairi ambayo vina vya kati huwa vinafanana katika mishororo ya beti
zote za shairi husika, huku vina vya nje vikibadilika kutoka mshororo hadi mshororo au ubeti hadi
ubeti. Wakati mwingine mshororo wa mwisho wa kila ubeti huweza kuwa na vina vinavyohitilafiana au
hata kuwa na kituo bahari au kimalizio lakini tu iwe na kina cha kati ambacho ni bahari na kina cha
mwisho kinachobadilikabadilika.
(v) Ukuraguni
Hii ni aina ya mashairi ambapo kuna vina vya kati na vya mwisho vinavyofanana. Hata hivyo vina
hivyo vinabadilikabadilika kutoka ubeti mmoja hadi mwingine
Ubeti wa 1: ___________________ni, ________________a
___________________ni, ________________a
___________________ni, ________________a
___________________ni, ________________a
Ubeti wa 2: ___________________sa, ________________ma
___________________sa, ________________ma
___________________sa,________________ma
___________________sa, ________________ma
Ubeti wa 3: ___________________po, _________________la
___________________po, _________________la
___________________po, _________________la
___________________po, _________________la
___________________po, _________________la
(vi)Mtiririko
Haya ni aina ya mashairi ambayo kwa kawaida vina vyake vya kati hufanana/hutiririka katika beti
zake zote na pia vina vya mwisho hufanana/hutiririka katika beti zake zote. Kuna baadhi ya maandiko
ambapo dhana ya mashairi ya mtiririko hutumika kumaanisha mashairi yasiyokuwa na urari wa vina na
mizani na ambayo hayana beti bali hutiririka tu mwanzo hadi mwisho. Hata hivyo dhana hiyo siyo
inayotumika hapa.
123
(vii) Masivina
Masivina ni aina ya mashairi ambayo hayana urari wa vina lakini yanaweza kuwa na urari wa
mizani. Neno “masivina” ni kifupi cha “mashairi yasiyokuwa na urari wa vina.” Hii haimaanishi
kwamba ni mashairi yasiyokuwa na urari wa mizani. Kuna baadhi ya wanazuoni huyachukulia
masivina kuwa ni mashairi yasiyokuwa na urari wa vina na mizani, bali dhana hii si sahihi. Masivina
huitwa pia mapingiti, yakitumia dhana kwamba kama ilivyo kwa vipingiti vya vitu mbalimbali kama
vile muwa huweza kufanana lakini si lazima vipingiti vyote vifanane. Vina na mizani hufananishwa na
vipingiti hivyo ambapo katika mashairi haya vina havifanani bali mizani hufanana.
(viii) Kisarambe
Kisarambe ni mashairi yanayokaribiana sana na masivina. Tofauti baina ya masivina na kisarambe
ni kwamba wakati ambapo masivina ni mashairi yasiyokuwa na urari wa vina lakini yanayoweza kuwa
na urari wa mizani, kisarambe ni mashairi ambayo hayana urari wa mizani bali yana urari wa vina.
(ix)Guni
Mashairi guni yanahusiana sana na masivina na kisarambe. Tofauti pekee ni kwamba masivina
hayana urari wa vina bali yanaweza kuwa na urari wa mizani, kisarambe hayana urari wa mizani bali
yana urari wa vina na mashairi guni yenyewe hayana urari wa vina wala mizani. Mashairi haya pamoja
na masivina ndiyo huitwa mashairi ya kisasa.
(x) Upeo
Upeo ni aina ya ushairi wenye idadi tofauti ya mizani katika mishororo ya ubeti mmoja. Hii ina
maana kwamba mshororo wa kwanza unaweza kuwa na mizani kumi na mbili, unaofuata ukawa na
mizani kumi na kadhalika.
(xi)Kikai
Ni aina ya mashairi ambayo huwa na mizani kumi na mbili katika kila mshororo ambapo mizani
nne huwa katika ukwapi na nane katika utao. Hata hivyo bahari hii yaweza kuwa pia na mizani sita au
nane kwa tatu au tano na kwa nane. Jambo la msingi hapa ni kwamba mizani katika upande mmoja wa
mshororo huwa michache sana kuliko katika sehemu nyingine.
4. Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Uradidi
Uradidi ni ile hali ya kujirudiarudia kwa jambo. Uainishaji wa ushairi kwa kutumia kigezo cha
uradidi, kwa hiyo, kinazingatia kurudiarudia kwa neno moja au kifungu cha maneno katika shairi kwa
lengo la kusisitiza wazo au kuweka mkazo katika maana. Kwa kutumia kigezo hiki tunapata aina
zifuatazo za mashairi.
(i) Kikwamba
Kikwamba ni mashairi ambayo neno moja hurudiwarudiwa katika kila mshororo au hata ubeti
mzima. Neno linalorudiwa laweza kuwa lile linaloanza katika kila mshororo au linaweza kujitokeza
katikati ya mshororo. Shairi lililopewa jina “Dini” lililopo katika sehemu ya pili ya andiko hili ni mfano
mzuri wa mashairi ya bahari hii ya kikwamba.
(iii)Pindu
Pindu ni aina ya ushairi ambapo neno au fungu la maneno lililo mwishoni mwa ubeti (linalomalizia
ubeti) linarudiwa kama kianzio cha ubeti unaofuata. Ni mashairi yenye uelekeo wa kitathlitha.
5. Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Madhumuni ya Utungaji (Lengo)
Katika bahari hii uainishaji hufanywa kwa kuzingatia madhumuni ya utungaji wa shairi husika. Kila
mshairi huwa na lengo au madhumuni mahsusi anapotunga shairi lake. Aidha, shairi husika lililotungwa
huwa linatimiza majukumu kadhaa, iwe ni kuelimisha, kuburudisha, kuzindua moyo na kadhalika.
Hivyo, kigezo hiki kinazingatia mambo hayo. Kwa kuzingatia kigezo hiki tunaweza kupata aina
zifuatazo za ushairi:
124
(i) Zivindo
Ni utungo wa kishairi ambapo mshairi hutunga ili kufafanua maana tofauti za neno moja kama vile
paa, kaa, ala, panda, shuka, na kadhalika. Kila mshororo huelezea matumizi au maana tofauti za neno
linalofafanuliwa. Kazi yake ni kufunza lugha kwa kutoa maana tofauti ya neno moja au yenye
matamshi yanayokaribiana.
(ii) Tumbuizo
Ni shairi linaloimbwa au kughanwa ili kutumbuiza na kuwaliwaliza watu. Lengo kuu la utungo huu
ni kutoa burudani.
(iii)Tiyani Fatiha
Ni bahari ya ushairi wa kidini wa kuomba toba. Ni utungo wenye mishororo tisa (9) kila ubeti
ambao una vina vya kati na mwisho. Mbali na uwezekano wa kuwa na urari wa vina vya kati na
mwisho tiyani fatiha huweza pia kakosa sifa hiyo katika baadhi ya mistari.
(iv)Inkishafi/Dura Mandhuma
Bahari hii imepata jina lake kutokana na Utenzi wa al-Inkishafi wa Sayyid Abdalla Bin Ali bin
Nasir (1720-1820) pia kutokana na utungo wa Sheikh Umar bin al-Ahdaly (1798-1869) uitwao Dura
Mandhuma. Ni tungo za kishairi za zamani zilizokuwa na mishororo yenye mizani kumi na moja (11).
Maudhui yake yalikuwa ya kidini, hasa dini ya Kiislamu, na yenye mafunzo ya maadili kama vile
kuusia, kuonya, kufunza mwenendo wa kidini na kuelekeza. Hii ina maana kuwa japo, kwa kiasi
kikubwa bahari hii ilihusu tungo za kidini lakini ilihusu pia tungo zenye maudhui ya kidunia.
(v) Taabali
Ni aina ya ushairi ambao hutungwa ili kuwaenzi marehemu. Utungo huu hukusudiwa kuwasifia
watu walioaga dunia kama njia ya kuwaenzi na kuihamasisha jamii kuwa na matendo mema kama wao
ili watakapokufa na wao wakumbukwe kwa mema.
6. Bahari za Ushairi kwa Kigezo cha Muundo
Kigezo cha muundo kinazingatia umbo la ushairi husika (ikiwa ushairi una umbo la majibizano au
la na kama una majibizano, majibizano hayo yapoje). Kwa kutumia kigezo hiki tunapata aina zifuatazo
za ushairi:
(i) Ngonjera
Haya ni mashairi ya majibizano yanayohusisha fanani wawili au zaidi. Fanani mmoja huimba au
kughani ubeti mmoja au hata mshororo mmoja na wakati mwingine hata kipande kimoja na kisha
fanani mwingine hujibu.
(ii) Sarakani
Sarakani ni aina ya ushairi ambao una muundo wa beti usiolingana, ubeti mmoja unaweza kuwa
na mishoro miwili, unaofuata mitatu na mwingine minne na kadhalika. Aidha, katika bahari hii pia
ubeti wa kwanza huweza kuwa una mishororo mitano, unaofuata minne na kadhalika. Tunaweza
kusema kwamba ushairi wa aina hii unachanganya bahari tofauti tofauti katika beti zake ambapo beti
moja inaweza kuwa utano, nyingine ukumi na kadhalika.
(iii) Mandhuma
Mandhuma ni aina ya shairi ambalo huwa na sehemu mbili, sehemu ya kwanza huwa ni swali na
sehemu ya pili ni jibu. Wakati mwingine sehemu ya kwanza huweza kuwa wazo na sehemu ya pili ni
msisitizo wa wazo husika au ufafanuzi wake. Mgawanyo huu unaweza kuwa baina ya beti moja na
nyingine au hata katika mshororo mmoja ambapo kunakuwa na ukwapi (unaotoa swali) na utao
(unaojibu swali hilo).
125
HITIMISHO KUHUSU BAHARI ZA USHAIRI
Tuhitimishe kwa kusema kwamba uainishaji wa mashairi kwa kuzingatia bahari ni telezi mno na
bado kuna mwingiliano mwingi. Swali la kujiuliza hapa ni je, bahari hizi zipo ngapi hasa na ni lazima
tuainishe mashairi katika bahari mbalimbali? Bila shaka jibu la swali la pili ni rahisi. Ni lazima
tuainishe ushairi katika bahari, kwa uainishaji wa ushairi hurahisisha usomaji wa ushairi na hata
ufafanuzi wake.
126
SURA YA SABA
UCHAMBUZI WA MASHAIRI
Uchambuzi wa mashairi ni uhakiki wa mashairi mbalimbali. Wanafasihi wengi wanabainisha
kwamba uchambuzi wa mashairi huhusisha vipengele vikuu viwili ambavyo ni maudhui na fani. Hata
hivyo kumekuwa na utata wa kipengele gani kinapaswa kuanzwa katika uhakiki wa mashairi na kazi za
wa fasihi kwa ujumla. Wapo wanaoona kwamba uhakiki wa kazi ya fasihi hupaswa kuanza kwa
kuchambua vipengele vya maudhui na pia wapo wanaoshadidia kuanza na vipengele vya kifani. Hata
hivyo katika andiko hili tutaendeleza mkabala unaopigiwa chapuo sana na Samwel katika maandiko
yake kwamba tunapaswa kuanza na uchambuzi wa maudhui na kisha fani. Hoja ya Samwel ambayo
tunakubaliana nayo ni kwamba maudhui ndiyo huanza katika kichwa cha mwanafasihi na kisha
hutafutia fani ya kuyawasilisha maudhui hayo (taz. Samwel, 2012a, Mabadiliko katika Majigambo:
Uchunguzi wa Mabadiliko ya Jadi na Bongo Fleva na Samwel, 2012b, Hadithi Fupi: Nadharia, Mbinu
na Mifano). Hivyo uchambuzi wetu katika sehemu hii utaelemea mkabala huo.
Jambo la msingi la kukumbuka ni kwamba japokuwa katika uhakiki wa kazi za fasihi ukiwemo
ushairi, maudhui na fani hutenganishwa, vipengele hivi ni kitu kimoja. Maudhui na fani huathiriana,
hutegemeana na kukamilishana na hivyo ni vitu ambavyo havipaswi kuchukuliwa kuwa ni tofauti. Kila
mara ni vema kuvihakiki vipengele vya maudhui na kuvihusisha na fani. Maudhui huweza kuathiri fani
na fani kuathiri maudhui. Kwa mfano, pindi mashairi yanapotumia lugha ngumu sana isiyoeleweka
kirahisi hufanya hata maudhui yake yasieleweke. Vivyo hivyo pale mashairi yanapoweka mkazo katika
maudhui na kusahau fani mashairi hayo huweza kuwa chapwa ama yasiyofurahisha kuyasoma na kwa
hivyo maudhui yake kutowafikia wahusika. Hivyo, maudhui na fani ni sawa na sura mbili za sarafu
moja, sura moja inapoharibika sarafu hiyo inapoteza uhalali wake.
1. MAUDHUI
Wanafasihi wengi huyafafanua maudhui kwamba ni umbo la ndani la kazi ya fasihi. Maudhui ni
mawazo yanayojitokeza katika kazi ya fasihi. Ni jumla ya mambo yote yanayobebwa na kazi husika ya
kifasihi. Kwa minajili ya andiko hili, maudhui tuchukulie kuwa ni jumla ya mawazo au mambo
yanayobebwa katika ushairi wa Kiswahili. Maudhui hujumuisha dhamira, ujumbe, migogoro,
masuluhisho, falsafa, fundisho na msimamo.
I. Dhamira
Dhamira ni mada, lengo, kusudi, wazo kuu linalozungumzwa na shairi/kazi ya sanaa. Mashairi
huweza kuwa na dhamira za kisiasa, kiuchumi, kijamii na hata kiutamaduni. Mifano ya baadhi ya
dhamira zinazoonekana katika mashairi ni pamoja na uongozi bora, mapenzi, dini, ndoa, elimu, kazi na
ukombozi. Dhamira hizi huweza kuelezwa kwamba mwandishi anakusudia kuielimisha jamii juu ya
dhana na sifa za kiongozi bora, kuionya jamii juu ya madhara ya mapenzi shuleni, kuielekeza jamii juu
ya umuhimu wa dini katika jamii, kuiasa jamii kuwa na uaminifu katika ndoa na kadhalika.
II. Ujumbe
Ujumbe ni yale mambo ambayo mshairi angependa hadhira ijifunze ili kuweza kufanikisha
misimamo iliyojengwa na msanii huyo. Kwa mfano, kama shairi linahusu mapenzi ujumbe unaweza
kuwa “mapenzi yanaua, mapenzi yanapofanywa shuleni huweza kuathiri ujifunzaji na ufundishaji,
mapenzi huweza kuwa faraja katika kipindi cha matatizo” na kadhalika.
III. Falsafa
Falsafa ni imani ya mshairi. Kipengele hiki huhusisha vipengele vya ujumbe, maadili na
msimamo wa mshairi ambao hutokana na dhamira za kazi hiyo. Mara nyingi falsafa hujitokeza katika
namna mshairi anavyotoa masuluhisho ya migogoro inayojitokeza au mahitimisho anayoyatoa juu ya
masuala mbalimbali. Falsafa inaweza kuwa “pindi wema na ubaya vinapopambana wema hushinda,
malipo ya ubaya ni aibu, tamaa mbele mauti nyuma, asiyesikia la mkuu huvunjika guu, maisha hayana
maana yoyote (kufa leo au kesho vyote ni sawa tu)” na kadhalika.
127
IV. Fundisho
Fundisho huitwa pia mafunzo. Fundisho, kwa hiyo, ni yale mambo ambayo tunajifunza kupitia
shairi husika. Fundisho huhusiana na falsafa na mtazamo wa jamii kwa ujumla jinsi inavyoyaona
mambo. Mara nyingi fundisho huwa ni juu ya mambo mema, hatutarajii mhakiki aseme mshairi
anaifundisha jamii juu ya umuhimu wa wizi katika kipindi cha matatizo. Wizi ni kitu kibaya na katika
jamii hakuna namna ya kuhalalisha wizi. Hivyo, fundisho huweza kuwa, kwa mfano, mwandishi
anaifunza jamii kwamba ni muhimu kuvumilia matatizo kwani mvumilivu hula mbivu.
V. Msimamo
Msimamo wa mshairi huitwa pia mtazamo wa mshairi. Msimamo ni jinsi mshairi
anavyoyachukulia mambo katika ulimwengu au jamii husika anayoisawiri. Msimamo si lazima kila
wakati ukubalike na wanajamii wote japokuwa mafundisho yanayotolewa katika ushairi yanaweza
kukubaliwa na jamii yote. Kwa mfano, msimamo wa Kezilahabi katika kazi zake nyingi ni kwamba
maisha hayana maana yoyote. Msimamo huu unatokana na falsafa ya kidhanaishi inayoaminiwa na
Kezilahabi. Misimamo mingine huweza kuwa “kiongozi mbaya anapaswa kuondolewa kwa nguvu
madarakani na kuuawa, wanyonge wanaokandamizwa watumie vita kujikomboa maana njia ya amani
huchukua muda mrefu, ili kujilinda na UKIMWI wanajamii hawana budi kujiingiza katika dini na
misimamo mingineyo.”
VI. Mgogoro
Mgogoro ni hali ya kutoelewana baina ya watu wawili au makundi mawili ya watu. Kwa mfano,
kunaweza kuwa na mgogoro baina ya wenyenacho na wasionacho ambapo wasionacho wanataka njia
kuu za uchumi zimilikiwe na wote ilhali wenyenacho hawataki hali hiyo. Kunaweza kuwa na mgogoro
baina ya binti na wazazi wake ambapo binti anataka kuolewa na kijana maskini lakini wazazi wake
hawataki na pia kunaweza kuwa na mgogoro baina ya wachungaji na waumini ambapo wachungaji
wanataka waumini watoe sadaka kubwa zaidi ili wao wazitumie katika anasa lakini waumini
wanaamini kwamba kutoa sadaka ni kumpa chochote Mungu ambaye ni tajiri hivyo hata kidogo
chamtosha. Upo pia uwezekano wa mtu mmoja kuwa na mgogoro baina yake na nafsi yake. Mgogoro
huu huitwa mgogoro wa kinafsia na huwa unatokana na mhusika kuwa na mambo mawili
yanayomsonga ambapo kila jambo linamvuta kuliamua. Mhusika huyo, kwa hiyo hujikuta akiwa
kwenye mgogoro ikiwa aamue hili au lile lingine. Kwa mfano, mhusika binti huweza kuwa na mgogoro
nafsia ikiwa ashikilie nia yake ya kuolewa na kijana maskini hata kama wazazi wake wamemkataa ama
akubaliane na wazazi wake na aolewe na kijana tajiri aliyechaguliwa na wazazi wake.
VII. Masuluhisho
Masuluhisho kwa kawaida huenda sambamba na migogoro. Panapotokea mgogoro, msanii
huweza kupendekeza usuluhishi wa mgogoro huo. Kwa mfano, katika mgogoro wa wazazi na binti
mshairi huweza kutoa suluhisho kwamba binti aliolewa na kijana maskini na waliishi kwa amani na
furaha na mwishowe kijana (mume) alikuja kuwa tajiri kuliko tajiri aliyechaguliwa na wazazi wa binti
ili aolewe naye. Hivyo, suluhisho hapa ni kwamba wazazi wawaache watoto wao waolewe na mtu
yeyote wanayempenda maana la msingi katika ndoa ni upendo na amani bali mali hutafutwa. Hata
hivyo mara nyingine washairi huamua kutotoa masuluhisho ya migogoro wanayoiibua na kumwachia
msomaji nafasi ya kuamua lipi linafaa kuwa suluhisho bora.
2. FANI
Fani huelezwa kwamba ni umbo la nje la kazi ya fasihi. Hii ina maana kwamba fani ni mbinu
mbalimbali azitumiazo mshairi katika kuwasilisha fikra na mawazo (maudhui) anayoyakusudia kwa
hadhira lengwa. Vipengele vya fani vilivyozoeleka ni pamoja na muundo, mtindo, matumizi ya lugha,
mandhari na wahusika.
I. Muundo
Muundo hudhihirika kwenye umbo la shairi. Umbo ni sura ya nje ya shairi au kazi ya sanaa, ni jinsi
shairi husika linavyoonekana. Muundo (umbo) la shairi hutegemea na mkabala wa mshairi, ikiwa ni
mwanamapokeo au mwanausasa. Lakini kwa ujumla muundo wa shairi hujumuisha yafuatayo:
128
a) Beti: ni mkusanyiko wa mistari/mishororo na kwa kawaida huwa na wazo moja kamilifu.
Katika uchambuzi, tunaangalia ikiwa shairi husika lina beti au halina na beti hizo zimeundwaje?
b) Mshororo: ni mistari ambayo inapowekwa pamoja huunda beti. Katika kipengele hiki
tunaangalia ikiwa beti za shairi linalochambuliwa zimegawanyika katika mishororo na pia
mishororo hiyo ipoje? Je mishororo imegawanyika katika vipande?
c) Vipande: ni sehemu ya mshororo wa shairi. Mshororo huweza kuwa na sehemu kadhaa,
sehemu hizo ndizo huitwa vipande. Mshororo huweza kugawanyika katika sehemu mbili, tatu
au hata nne na kadhalika. Kipande kikigawanyika katika sehemu mbili sehemu ya kwanza
huitwa ukwapi na ya pili utao; kikigawanyika katika sehemu tatu, sehemu ya kwanza huitwa
ukwapi, ya pili utao na ya tatu mwandamizi; na kikigawanyika katika sehemu nne sehemu ya
kwanza huitwa ukwapi, ya pili utao, ya tatu mwandamizi na ya nne ukingo.
d) Mizani: ni jumla ya salabi katika mshororo mmoja. Kila mshororo huundwa na maneno
yaliyoundwa na silabi. Kila silabi moja ni mizani moja, hivyo, jumla ya silabi katika mshororo
ndizo huunda mizani ya mshororo husika.
e) Vina: ni silabi zinazofanana katika mshororo wa shairi au beti. Kuna aina mbalimbali za vina
ambazo ni pamoja na kina cha kati, kile kinachotokea katika kipande cha mshororo ambacho si
cha mwisho na kina cha mwisho ambacho hujitokeza katika kipande cha mwisho cha mshororo.
f) Kibwagizo: ni mshororo wa mwisho wa ubeti unaorudiwarudiwa, huitwa pia kiitikio.
Kipengele hiki kiliigwa kutoka tungo simulizi. Hasa zenye mwimbaji mkuu mmoja. Kazi ya
kibwagizo katika shairi ni kumalizia ubeti na kushadidia dhamira au wazo la shairi. Upo
uwezekano pia wa kuwa na vibwagizo ambavyo si viitikio. Hivi huwa ni ghani
zinazochomekwa mwanzoni mwa shairi ili kumtambulisha msanii, maudhui yake au shairi
lenyewe. Aina hii ya vibwagizo ni maarufu sana katika ushairi wa Bongo Fleva.
g) Mkarara: ni mshororo wa mwisho ambao unajirudiarudia katika kila ubeti. Neno mkarara
linatokana na dhana ya kukariri, yaani kurudiarudia kwa jambo fulani.
h) Kituo/kimalizio: ni mstari wa mwisho katika ubeti. Iwapo mstari huo unabadilikabadilika
kutoka ubeti mmoja hadi mwingine basi mstari huo ni kimalizio lakini kama mstari huo
haubadiliki basi huitwa kituo (kituo bahari).
II. Mtindo
Mtindo ni upangaji wa fani na maudhui kwa namna ambayo inampambanua mshairi mmoja na
mwingine. Mtindo huhusisha kuchunguza ikiwa shairi ni la tathlitha, tarbia, telemania au mtindo
mwingineo. Mtindo pia huhusisha maneno aliyoyateua mtunzi, je ni magumu au ni rahisi? Ni ya
kilahaja au yanatumia lahaja sanifu? Yanatumia lugha ya wazee, vijana au watoto? Ya wanaume au ya
wanawake? Je mashairi hayo ni ya kimajibizano au ni monolojia? Je, mshairi ametumia lugha ya
Kiswahili pekee au amechanganya lugha? Anatumia lugha fasaha na sanifu au ya mitaani? Mambo
mengine ya mtindo ni pamoja na matumizi ya lugha ya picha, ishara na taswira. Kwa hakika mtindo
hujumuisha pia mambo mengi ikiwa ni pamoja na matumizi ya lugha, lakini ili kurahisisha usomaji na
uchambuzi wa mashairi, matumizi ya lugha hupewa kipengele chake kinachojitegemea.
III. Matumizi ya Lugha
Katika kipengele hiki kinachohusiana sana na mtindo tunaangalia vipengele vile ambavyo
hatujavichambua katika mtindo. Hapa tunaangalia mambo kama vile matumizi ya tamathali za semi,
matumizi ya methali, misemo, misimu, mafumbo na vipengele vingine vya aina hiyo.
129
a) Matumizi ya Tamathali za Semi
Samwel (2012b) anabainisha kwamba dhana ya tamathali za semi imekuwa ikichanganywa sana
na wahakiki pamoja na walimu wengine ambao wamezijumuisha methali, misemo na misimu katika
tamathali za semi (Kanuri na Wenzake, ht.). Uchanganyaji huu unaonekana pia katika Msokile
(1993:60). Samwel anaendelea kubainisha kwamba tamathali za semi, methali, misemo na misimu ni
vitu tofauti. Tamathali za semi ni maneno au miundo inayotumika katika lugha ili kutia msisitizo na
mkazo katika maana, kwa kawaida huwa na idadi kamili na zinajulikana. Tamathali za semi
zinazojulikana kutumika katika ushairi ni pamoja na tashbiha/tashbihi, sitiari, tashihisi, takriri, tasifida,
na chuku. Hata hivyo bado kuna mjadala juu ya tamathali hizi kama itakavyobainishwa katika mjadala
utakaofuata.
(i) Tashbiha: huitwa pia tashibihi au mshabaha. Hii ni aina ya tamathali ambayo hufananisha vitu
viwili tofauti kana kwamba ni kitu kimoja. Tamathali hii hutumia vifananisho kama vile: kama,
kama vile, mfano wa, mithili ya na nyingine za aina hiyo. Mifano ifuatayo itatusaidia kuielewa
dhana hii ya tashbiha:
- Vero ni mrembo kama malaika
- Gilo ni mrefu kama mti wa mwanzi
- Nilimuona kijana mwenye sura mithili ya mwanamke
- Maziwa yana rangi mfano wa chokaa
(ii) Sitiari: huitwa pia istiara, istiari au jazanda. Hii ni tamathali ya usemi (maneno, kirai au
miundo) inayotumika kuumba picha fulani akilini inayotoa athari fulani kwa, au inayoamsha
mwitikio fulani kutoka kwa hadhira. Cuddon (1998:507) anasisitiza kwamba sitiari ni tamathali
muhimu sana katika ushairi. Mifano ya sitiari inaweza kuwa kama ifuatavyo:
- Vero kwa urembo wake ni malaika
- Gilo ana urefu wa mti wa mwanzi
- Asha ana weusi wa mkaa
(iii)Tashihisi: tamathali hii huitwa pia uhaishaji na pia uhuishaji. Kuhaisha ni kuvipa uhai vitu
visivyokuwa na uhai na kuhuisha ni kuvipa hadhi vitu vilivyokuwa duni. Hivyo tunaweza
kusema kwamba tashihisi ni aina ya tamathali ambapo viumbe visivyokuwa na uhai hupewa
uhai (Kahigi na Mulokozi, 1979:33-34; Alembi, 2000:36). Vilevile tashihisi huhusisha viumbe
visivyo binadamu kupewa uwezo wa kiutendaji kama binadamu. Dhana hii ya pili ndiyo
inayobebwa na neno lenyewe “tashihisi” ambalo linamaanisha nafsi. Hivyo, ni mbinu ya kuvipa
nafsi ya binadamu vitu ambavyo havina nafsi hiyo. Cuddon (1998:661) anabainisha kwamba
matumizi ya tamathali hii zaidi ya kuweka mkazo katika maana, inaupa utungo sifa ya kuwa
kazi ya fasihi. Ifuatayo ni mifano ya tashihisi:
- Kiza kinene kilitawala usiku ule kabla mayowe hajaanza kutembea
- Taratibu usingizi ulianza kunichukua huku mawazo yakinibembeleza
- Vumbi lilikimbia njia nzima
(iv)Takriri: huitwa pia inadi au uradidi. Dhana hii inakaribiana sana na dhana ya usambamba.
Kahigi na Mulokozi (1979:40) wanaieleza takriri kuwa ni uradidi, yaani urudiaji wa sauti, neno,
kirai, kishazi na hata sentensi katika kazi ya kifasihi. Takriri hutumika kuweka mkazo katika
maana na pia huleta ushikamani na muunganiko katika ushairi. Katika ushairi kuna aina
mbalimbali za takriri kama vile: takriri irabu, takriri konsonanti, takriri silabi (huitwa pia takriri
mizani), takriri neno, takriri mstari/mshororo, takriri ubeti, takriri vina na takriri kituo na takriri
ridhimu. Takriri pia huweza kuwa katika ngazi ya maudhui ambapo kunakuwa na takriri wazo.
(v) Tasifida: ni aina ya tamathali ambayo inayafanya maneno ambayo hayapaswi kutamkwa
hadharani, kuweza kutamkika kwa mbinu nyingine mbadala (Cuddon, 1998:292; Senkoro,
2011:18).
130
(vi)Udokezi/mdokezo: Cuddon (1998:27) na Mulokozi (2002:187) wanafasili mdokezo kuwa ni
tamathali ambayo inatumika katika kazi mahsusi ya kifasihi ili kurejelea kazi nyingine ya fasihi
au ya sanaa, au mtu au hata tukio.
(vii) Chuku: huitwa pia chukwu au udamisi. Chuku ni mbinu ya kisanii ambapo kitu, mtu au
jambo hukuzwa zaidi ya uwezo wake (Kahigi na Mulokozi, 1979:36; Alembi, 2000:44). Katika
mbinu hii kitu, jambo au mtu anapewa uwezo ambao katika hali ya kawaida hawezi kuwa nao.
Mara nyingi chuku huelezwa kuwa ni kutia chumvi kwa jambo ambako kunaweza kuwa chanya
au hasi.
(viii) Balagha: ni ile hali ya mshairi kuuliza swali ambalo linakuwa la kikejeli kwa kuwa mshairi
anauliza jambo ambalo jibu lake analifahamu fika.
(ix) Ucheshi: Senkoro (2011:26) anafasili ucheshi kuwa ni mbinu ya kifani ambayo wasanii
huitumia katika kazi zao za fasihi kuzichekesha hadhira zao, au walau kuzifanya hadhira hizo
zitabasamu. Lengo la kutumia mbinu hii ili kuwafurahisha wasomaji, wasikilizaji au watazamaji
wa kazi zao, kuiepushia uchovu hadhira ya kazi zao na kujenga kejeli katika kazi zao.
b) Matumizi ya Methali
Methali ni semi fupifupi zinazobeba uzoefu wa jamii kuhusu maisha na hivyo kuadilisha na
kuihekimisha jamii. Kazi kubwa ya methali ni kuitajirisha fani na maudhui ya kazi ya fasihi na
hutumika kama daraja la kupitishia maadili kwa jamii husika. Hivyo, tunaweza kusema kwamba
methali ni tungo za kimapokeo ambazo hubeba falsafa ya maisha katika jamii husika.
c) Matumizi ya Nahau
Nahau ni fungu la maneno ambayo maana yake haipatikani kwa kufasili neno moja moja. Hizi
ni tungo za kimapokeo ambazo maana yake huwa ni tofauti na maana ya neno kwa neno. Samwel
(2012b) anatoa mifano ya nahau kuwa ni kama vile:
- Ana mkono wa birika (mchoyo)
- Ana roho ya korosho (mchoyo)
- Ana mkono mrefu (mwizi)
- Amevunja ungo (amebalehe hasa msichana)
d) Matumizi ya Misimu
Misimu ni maneno yanayoibuka katika kipindi fulani cha kihistoria na huweza kupotea. Wakati
mwingine misimu huweza kusanifiwa na kuwa msamiati. Mifano ya misimu ni kama vile njagu (polisi),
mshkaji (rafiki), changu (kahaba), zali (bahati) na kadhalika.
e) Vipengele Vingine katika Matumizi ya Lugha
Zaidi ya vipengele tulivyovieleza, matumizi ya lugha katika ushairi hujumuisha pia vipengele kama vile
inksari, mazda, tabdili, ritifaa, lugha ya mkato .Ufafanuzi wake ni kama ifuatavyo:
(i) Inksari: kufupisha maneno katka shairi ili kupata ulingano wa vina na hata mizani. Kwa
mfano, aliyekuja ( inafupishwa kuwa alokuja), mwana wako (inafupishwa kuwa
mwanao), mama yako (inafupishwa kuwa mamayo) na kadhalika.
(ii) Mazda: ni kinyume cha inksari. Ni hali ya kurefusha neno kwa nia ya kupata mizani
inayohitajika. Mifano mizuri ya mazda ni kama vile: nenda (inarefushwa kuwa
enenda), ajapo (inarefushwa kuwa anapokuja), nipo (inarefushwa kuwa nimekuwepo)
na kadhalika.
(iii) Tabdili: kubadilisha mpangilio wa herufi au vitamkwa katika neno ili kupata urari
(ufanano) wa vina vinavyotakikana. Mfano mzuri unaweza kuwa kama unataka
131
kutumia kina “hi” bahari (itabadilishwa na kuwa barahi), au kama unataka kutumia
kina “si” basi sukari (itabadilishwa na kuwa karusi).
(iv) Ritifaa: mbinu hii hutumika kwa kuelekeza ujumbe wake kwa kitu kisicho na uhai kama
vile sanamu, maiti. Hutumika kutoa hisi za ndani za huzuni/majonzi makali.
(v) Tanakali Sauti: ni mbinu ambapo mshairi huiga sauti ya kitu halisi kwa kutumia
maneno. Mfano mzuri wa maneno ya ainaa hii ni kama vile churuzika, tiririka,
tetemeka, bandubandu na kadhalika.
(vi) Lugha ya mkato: shairi huzungumza mambo kwa ufupi kwa kutumia taswira na
tamathali
IV. Mandhari
Ni mazingira ya kijamii na kihistoria yaliyozua utungo. Mazingira ambayo kazi ya fasihi imeandikwa.
Mandhari ni dhana inayoonekana rahisi lakini ni pana na yenye mijadala mingi. Kumekuwa na utata juu
ya dhana yenyewe ya mandhari, aina za mandhari zilizopo na hata dhima ya mandhari katika kazi ya
fasihi. Kuna wanafasihi wanaofasili mandhari kwa kuzingatia eneo (mahali) kazi ya fasihi inapotendwa
lakini wapo pia wanaofasili mandhari kwa kuangalia wakati, wengine wanazingatia muktadha na
wengine wanachanganya vyote kwa pamoja.
Wanaofasili mandhari kwa kuzingatia eneo kazi ya fasihi inapotendwa wanajumuisha Msokile (1992),
Njogu na Chimerah (1999), Madumulla (2009) na Samwel (2012b). Kwa upande wa wanaofasili
mandhari kwa kuzingatia wakati na muktadha ni pamoja na Cuddon (1998) na Wamitila (2008). Nao
Sunkuli na Miruka (1990) wanafasili mandhari kwa kuzingatia muktadha. Katika andiko hili, tunaona
kuwa mtazamo bora wa kufasili mandhari ni kwa kuunganisha mitazamo yote. Hivyo, mandhari ni
wakati, mahali na muktadha ambamo kazi ya fasihi inatendwa. Hivyo tuseme ili kufasili mandhari
tunapaswa kujibu maswali yafuatayo: kazi ya fasihi inatendeka wapi? Lini? Inatendwa na nani? Na
inatendwa vipi?
Kuhusu aina za mandhari za kazi za fasihi tunaweza kusema kwamba ni eneo lingine lenye utata
mwingi. Wapo wanafasihi wanaoona kuwa aina za mandhari ni tatu, mandhari ya kijiografia, kijamii na
kihistoria (Sunkuli na Miruka, 1990); wapo pia wanaoona kuwa mandhari ya kifasihi ni ya aina mbili,
halisi na ya kibunifu (Wamitila, 2008; Madumulla, 2009 na Samwel, 2012b). Katika andiko hili
tunaonelea kuwa kuna aina kuu mbili za mandhari, mandhari halisi na ya kibunifu. Mandhari halisi
inajumuisha maeneo ya kweli yanayojulikana katika jamii husika lakini mandhari ya kibunifu
huhusisha maeneo ya kufikirika ambayo hayapo katika ulimwengu halisi. Mandhari pia huweza
kuhusisha wakati halisi uliopo au mwandishi anaweza kurudisha wakati nyuma au kwenda mbele ya
muda. Mwandishi, kwa mfano, anaweza kutunga shairi akielezea hali ilivyo mwaka 2100 kana kwamba
mwaka huo umeshafika.
V. Wahusika
Wahusika ni watu, wanyama au viumbe ambao hutumika katika kazi ya fasihi. Mashairi mengi
hayana wahusika ila mashairi ya masimulizi huwa nao. Mfano mzuri wa hili ni tenzi/tendi mbalimbali
kama inavyobainika katika Utenzi wa Vita vya Wadachi Kutamalaki Mrima, Utenzi wa Adamu na
Hawaa ambamo tunaona kuna wahusika. Kwa ujumla, tenzi nyingi hutumia wahusika. Katika uhakiki
wa ushairi tunajiuliza wahusika hao wana tabia/sifa gani? Je, wahusika hao wanaingiliana vipi?
Kutokana na meneno/matendo yao tumepata taswira gani? Je kuna wahusika wengine wa kiishara kama
vile “ua” kumaanisha “mpenzi” na kadhalika? Na je, ipi nafasi ya wahusika hao katika kuibua
maudhui?
132
SURA YA NANE
UFUNDISHAJI WA USHAIRI
Ushairi wa Kiswahili ni moja ya mada za lazima zinazopaswa kufundishwa katika ngazi
mbalimbali za elimu katika ukanda wa Afrika Mashariki. Katika nchi za Tanzania na Kenya, ushairi wa
Kiswahili unafundishwa katika shule za msingi, sekondari, vyuo vya ualimu na vyuo vikuu. Katika nchi
nyinginezo za Afrika Mashariki pia Kiswahili kinafundishwa katika ngazi mbalimbali. Vilevile, ushairi
wa Kiswahili unafundishwa katika vyuo mbalimbali ulimwenguni ambavyo vinafundisha lugha ya
Kiswahili na fasihi yake. Kutokana na kupanuka kwa ufundishaji wa ushairi wa Kiswahili ni muhimu
kupitia namna ushairi wa Kiswahili unavyoweza kufundishwa kwa ufanisi. Hata hivyo, kwa kuwa si
rahisi kupitia ufundishaji wa ushairi wa Kiswahili katika ngazi zote za elimu katika nchi zote, tutapitia
ufundishaji wa ushairi wa Kiswahili kwa ujumla bila kuelemea ngazi yoyote mahsusi ingawa tutatumia
mifano ya ufundishaji wa ushairi wa Kiswahili katika shule za msingi, sekondari na vyuo vya ualimu
katika nchi mbalimbali za Afrika Mashariki.
USHAIRI KAMA MBINU YA KUFUNDISHIA MASOMO MBALIMBALI
Ushairi wa Kiswahili, zaidi ya kuwa somo, ni moja ya mbinu muhimu ambayo inaweza
kutumika kufundishia somo la Kiswahili na masomo mengineyo. Kama mbinu ya kufundishia, ushairi
hujibainisha katika nyimbo zinazotumika kufundishia. Hivyo, mbinu ya nyimbo inahusiana moja kwa
moja na ushairi wa Kiswahili kwani, kama tulivyoeleza hapo awali, nyimbo ni ushairi simulizi wa
Kiswahili. Kwa hiyo, mbinu ya kufundisha kwa kutumia ushairi huitwa pia mbinu ya nyimbo. Katika
mbinu hii, nyimbo hutumiwa kufundisha masomo mbalimbali. Masomo hayo huweza kuwa ya sanaa au
hata ya sayansi. Kwa mfano, wanafunzi wengi wa sayansi nchini Tanzania wanapoanza kujifunza
elementi za kikemia katika somo la kemia hutumia wimbo. Katika shule nyingi nchini Tanzania,
mwanafunzi anapotakiwa kufundishwa elementi hizo, hufundishwa kwa kutumia wimbo maarufu
uitwao “Halo Helena,” ambao kila neno la wimbo husika huwakilisha elementi fulani ya kemia. Wimbo
huo huimbwa kama ifuatavyo:
Halo Helena Lile Beberu Bora Chinja na Ondoa Figo Nene Na yule Mzungu Aliye Simama Pale Serengeti
Club Aende Kwao Canada.
Elementi zinazowakilishwa na kila neno la wimbo huu ni kama ifuatavyo:
Halo (Hydrogen), Helena (Helium), Lile (Lithium), Beberu (Belium), Bora (Boron), Chinja (Carbon), Na
(Nitrojen), Ondoa (Oxygen), Figo (Florin), Nene (Neon), Na (Sodium), Mzungu (Magnesium),
Aliyesimama (Alminium), Simama (Silicon), Pale (Phosphorus), Serengeti (Sulphur), Club (Chloride),
Aende (Algon), Kwao (Potasium), Canada (Calcium)
Mbali na kutumika kufundishia kemia, nyimbo pia hutumika kufundishia kufundishia masomo
ya lugha, ikiwa ni pamoja na Kiswahili na Kiingereza. Kwa mfano, katika shule mbalimbali za
chekechea na shule za msingi katika nchi kadhaa za Afrika Mashariki, kuna ule wimbo wa “Mabata
Wadogo Wadogo” uimbwao kama ifuatavyo:
Mabata wadogowadogo wanaogelea, wanaogelea
Katika shamba zuri la bustani
Wanapenda kuli kwa kwa kwa kwa kwa kwa, kwa kwa kwa kwa kwa kwa
Katika shamba zuri la bustani
Wimbo huu unawafundisha wanafunzi kutamka konsonanti ambatani kwa ambazo kwa umri wao huwa
ni ngumu sana kuzitamka. Hivyo, hapa wimbo unatumika kama mbinu ya kufundishia muundo KKI
(Konsonanti, Konsonanti, Irabu) wa silabi za Kiswahili. Kwa hiyo, hapa tunaona jinsi ushairi wa
Kiswahili unavyoweza kutumika kama mbinu ya kufundishia masomo mbalimbali. Mbinu hii
inasemwa kuwa, zaidi ya faida nyinginezo, husaidia kuwafanya wanafunzi kuchangamka darasani na
hivyo kuwafanywa wasichoke wakati wa zoezi la kufundisha na kujifunza. Hii ni kutokana na dhima
mojawapo ya ushairi wa Kiswahili ya kuburudisha. Kwa hiyo, somo hueleweka vizuri mbinu hii
inapotumika. Pia, mbinu hii huwasaidia wanafunzi kukariri mambo mbalimbali ambayo wasingeweza
kuyakariri kirahisi kwa namna nyingine.
133
USHAIRI WA KISWAHILI KAMA SOMO
SILABASI NA USHAIRI WA KISWAHILI
Ufundishaji wowote ule huanzia kwenye silabasi na kuongozwa na silabasi hiyo. Tunatumia
neno “silabasi” badala ya neno “muhtasari” ambalo hutumiwa na wengine kwa sababu kuu mbili:
kwanza, neno muhtasari tayari linatumika katika lugha ya Kiswahili kumaanisha ufupisho wa maelezo
fulani. Kanuni ya lugha inasisitiza kuepa matumizi ya maneno ambayo yameshatumika kumaanisha
dhana nyingine. Aidha, dhana ya muhtasari kutumika kumaanisha silabasi inachanganya kwani
inawafanya walimu na wanafunzi kuichukulia silabasi kama ufupisho wa zoezi la ufundishaji. Dhana
hii si sahihi hata kidogo kwani silabasi si ufupisho wa zoezi la ufundishaji. Pili, neno silabasi
linatumika ili kutunza uasili wa dhana yenyewe. Neno silabasi linalotumiwa hapa linatafsiri neno la
Kiingereza syllabus linalotumika kumaanisha mwongozo wa ufundishaji (TUKI, 2001:295 husisha na
TUKI, 2004:896). Hivyo, kulitohoa neno hilo kutalifanya neno silabasi linalozaliwa kuweza kuhifadhi
maana ya msingi ya dhana hiyo kama ilivyorejelewa na walioileta dhana hii kwetu. Wataalamu
wanakubaliana kuwa dhana ya silabasi, kama lilivyo zoezi zima la utoaji wa elimu rasmi (formal
education), ililetwa na wakoloni. Kabla ya ukoloni, sehemu kubwa ya Afrika haikuwa na mfumo rasmi
wa elimu bali mfumo usio rasmi uliojibainisha katika jando na unyago kwa kutaja baadhi tu (Coupland,
1938; Mair, 1964; Van Pelt, 1971; Ayisi, 1972; Rodney, 1975).
Hivyo, silabasi tunaweza kuifasili kuwa ni mwongozo mkuu unaomwelekeza mwalimu namna
ya kufundisha somo husika. Silabasi hii, kwa kawaida, hutokana na malengo na sera za elimu katika
nchi husika. Kila nchi ina malengo yake ya kutoa elimu katika ngazi husika, yaani kila nchi ina
malengo yake ya kutoa elimu ya chekechea, elimu ya msingi, elimu ya sekondari, elimu ya vyuo vya
kati na hata malengo ya elimu ya juu. Wanafunzi katika kila ngazi ya elimu wana mahitaji na matarajio
yao na ya jamii pia. Hivyo, katika kila ngazi kunakuwa na malengo mahsusi ambayo huamua masomo
ya kufundishwa, mada za kufundishwa na mbinu za ufundishaji kulingana na mahitaji na matamanio ya
wanafunzi na jamii. Silabasi hueleza yote hayo ili kuwawezesha walimu kufanya kazi yao ya
kufundisha kwa namna bora. Aidha, zaidi ya hayo, silabasi pia huelezea vitabu vya kiada, ziada na vya
rejea vya kutumika katika kila mada pamoja na zana za kufundishia. Silabasi hubainisha pia namna ya
kumpima mwanafunzi katika kila mada inayofundishwa.
Tangu nchi za Afrika Mashariki, ambazo ndizo hutumia na kufundisha zaidi Kiswahili, zipate
uhuru kumekuwa na silabasi mbalimbali. Wakati wa uhuru nchi hizo zilirithi silabasi za kikoloni
zilizokuwa zinatumika kufundishia shule za kikoloni. Ingawa silabasi hizo zilikusudiwa kutoa elimu
itakayowanufaisha wakoloni na kuendeleza utawala wao, lugha ya Kiswahili pamoja na ushairi wake
pia vilifundishwa (Mulokozi, 1996). Tulieleza katika sura zilizotangulia kuwa wakoloni walikuwa na
nafasi kubwa sana katika ukuzaji wa lugha ya Kiswahili na ushairi wake. Ni kupitia shule hizi za
kikoloni ambapo washairi wengi maarufu wa mwanzo waliibuka. Vilevile, wakoloni waliwafundisha
watu wa Afrika Mashariki ushairi wa nchi nyinginezo ulimwenguni na hivyo kuanza kuchochea
mabadiliko katika ushairi wa Kiswahili. Mabadiliko ambayo hatimaye yaliishia kuibua ushairi wa
kisasa wa Kiswahili, ushairi ambao hauamini kuwa urari wa vina na mizani ndiyo uti wa mgongo wa
mashairi ya Kiswahili. Ushairi ambao unasisitiza maudhui kuliko fani.
Baada ya uhuru, silabasi hizo za kikoloni zilibadilishwa. Tangu wakati huo silabasi zimeendelea
kubadilishwabadilishwa kulingana na mabadiliko ya sera ya elimu pamoja na malengo ya elimu katika
nchi mbalimbali za Afrika Mashariki. Nchini Tanzania, kwa mfano, kumekuwa na mabadiliko katika
sera ya elimu ambapo tangu kupatikana uhuru, sera ya elimu imekuwa ikibadilikabadilika. Sera ya
elimu inayotumika sasa ni ya mwaka 1995 ambayo, hata hivyo, imeonekana kuwa haiendani na
mabadiliko mbalimbali yaliyotokea katika jamii na hivyo kumekuwa na jitihada, ambazo labda zitazaa
matunda karibuni, za kuibadilisha sera hiyo. Kutokana na mabadiliko hayo ya sera ya elimu, hata
silabasi imekuwa ikibadilikabadilika.
Mbali na kubadilika kwa sera ya elimu, sababu nyingine inayoweza kusababisha silabasi
kubadilika ni mabadiliko ya kisiasa. Katika mabadiliko haya, tunazungumzia kubadilika kwa utawala
wa kisiasa katika nchi husika. Utawala unapobadilika, unaweza kuja utawala mpya wenye itikadi
tofauti na ile ya watawala waliotangulia na hivyo kuona kuna haja ya kubadilisha silabasi ili kuisukuma
mbele ajenda ya itikadi wanayoipigia chapuo.
134
Pia, silabasi huweza kubadilika kutokana na mabadiliko ya kiuchumi na kijamii. Nchi husika
huweza kupiga hatua kubwa kiuchumi kiasi ambacho silabasi iliyopo kuonekana haiwezi kuendana na
maendeleo yaliyofikiwa na nchi husika. Hivyo, kuonekana kuna haja ya kubadilisha silabasi iliyopo ili
iendane na maendeleo hayo.
Kutokana na sababu mbalimbali, kwa mfano, silabasi nchini Tanzania imekuwa
ikibadilishwabadilishwa. Silabasi inayotumiwa sasa katika shule za sekondari ni ya mwaka 2010
ambayo imetokana na kurekebishwa kwa silabasi ya mwaka 2005 ambayo na yenyewe pia ilitokana na
mabadiliko yaliyofanywa katika silabasi ya mwaka 1997.
Silabasi zinazotumika kufundishia hivi sasa katika nchi za Afrika Mashariki katika ngazi
mbalimbali za elimu, zinamtaka mwalimu kufundisha fasihi ya Kiswahili, ushairi ukiwemo. Katika nchi
ya Tanzania, silabasi ya Kiswahili sekondari inamtaka mwalimu kufundisha tanzu tatu za fasihi andishi:
riwaya, tamthilia na ushairi. Nchini Kenya, silabasi ya Kiswahili sekondari inamtaka mwalimu
kufundisha riwaya, tamthilia, hadithi fupi na ushairi. Katika nchi nyinginezo za Afrika Mashariki pia,
ushairi unabainishwa kama mojawapo ya tanzu za fasihi zinazopaswa kufundishwa. Kwa hiyo, silabasi
za Kiswahili zinazotumiwa sasa katika nchi mbalimbali za Afrika Mashariki, na kwingineko duniani,
zinabainisha haja ya kufundisha ushairi wa Kiswahili.
KUTAFSIRI SILABASI KWENYE VITENDO
Tunapozungumzia kutafsiri silabasi kwenye vitendo tunamaanisha namna silabasi inavyoweza
kutekelezwa katika zoezi zima la ufundishaji au utumiaji wa silabasi katika ufundishaji. Utafsiri wa
silabasi katika ufundishaji wa ushairi wa Kiswahili hauna tofauti na utafsiri wa silabasi katika
ufundishaji wa masomo mengine. Kuna hatua kadhaa ambazo mwalimu huzipitia katika kutafsiri
silabasi kwenye vitendo. Hatua zinazofahamika zaidi ni hizi zifuatazo:
1) Kufanya mapitio ya makusudi ya ufundishaji
2) Kuchagua na kupanga mada
3) Kutambua vitabu vya kiada na kuteua vitabu vya ziada vya kuvitumia
4) Kuandaa mpangokazi wa ufundishaji
5) Kuteua na kuandaa mbinu ya kufundishia
6) Kuandaa mwongozo wa ufundishaji darasani
7) Kuandaa zana za kufundishia
8) Kuingia darasani na kufundisha
9) Kufanya tathmini na upimaji
10)Kutoa matokeo ya tathmini na utoaji wa motisha
11)Upangaji wa ufundishaji ujao
Ni vema tuchambue hatua moja baada ya nyingine ili tuone jinsi ambavyo tunaweza kufundisha ushairi
wa Kiswahili kwa mafanikio makubwa na kuufanya utanzu huu kupiga hatua na kurithisha amali kwa
vizazi vijavyo.
1) Kufanya Mapitio ya Makusudi ya Ufundishaji wa Ushairi
Mara baada ya mwalimu kukusudia kufundisha ushairi wa Kiswahili au kupangiwa kufundisha
ushairi wa Kiswahili, anapaswa kuirejelea silabasi na kuona jinsi inavyoelekeza kufundisha ushairi wa
Kiswahili katika ngazi husika. Katika kuirejelea huko, mwalimu anapaswa kufanya mapitio ya
makusudi ya ufundishaji, yaani anapaswa kujua kwa nini ushairi wa Kiswahili unafundishwa katika
ngazi husika (iwe shule za msingi, sekondari au vyuo vya ualimu). Anapaswa kujiridhisha ikiwa
makusudi yanayobainishwa katika silabasi yanaendana na sera ya elimu ya taifa na sera ya elimu ya
ngazi husika (kama ni sera ya elimu ya msingi, sekondari na kadhalika).
2) Kuchagua na Kupanga Mada za Ushairi Zitakazofundishwa
Baada ya kuchambua makusudi ya kufundisha ushairi yanayobainishwa katika silabasi na kuona
kuwa yanaendana na sera ya elimu, hatua inayofuata ni kuchagua mada na kuzipanga. Ni wazi kuwa
uchambuzi wa silabasi ukifanywa kwa makini kuna mada ambazo zitabainika kutofaa, mada hizo, kwa
hiyo, zitaondolewa. Pia, kuna uwezekano wa kubaini kuwa mada zimepangwa katika mpangilio
135
usiokuwa na ushikamani. Hivyo, mada zitapangwa kwa namna ambayo italeta mantiki katika
ufundishaji wake na ina ushikamani. Aidha, kuna uwezekano wa kubainika kuwapo kwa mada radidi na
hivyo kuona haja ya kuondoa uradidi huo. Katika hatua hii, mwalimu atachagua mada zinazofaa
kufundishwa na kisha atazipanga, ipi itaanza kufundishwa na ipi itafuata, kwa namna ambayo anadhani
itawasaidia wanafunzi kuelewa. Njia bora ya upangaji wa maudhui inayopendekezwa zaidi ni kwa
kuanza kufundisha mada nyepesi na kisha kufuatiwa na mada ngumu na pia kufundisha mada
inayojulikana zaidi na kisha isiyojulikana (Samwel, 2012b).
3) Kutambua Vitabu vya Kiada na Kuteua Vitabu vya Ziada
Katika hatua hii mwalimu anapaswa kutambua vitabu vya kiada na kuteua vitabu vya ziada
atakavyovitumia katika ufundishaji wake. Kwa kawaida, vitabu vya kiada huidhinishwa na wizara
inayoshughulikia elimu kupitia taasisi mahsusi zinazohusika na zoezi hilo. Hivyo, mwalimu hana
chaguo katika vitabu hivi. Hata hivyo, mwalimu mzuri husoma na kuelewa mwenyewe kabla ya
kupanga ufundishaji wowote uwao. Hivyo, katika hatua hii mwalimu atasoma mada husika katika
vitabu vya kiada pamoja na vile teule vya ushairi. Vitabu teule vya ushairi hubadilishwa kila baada ya
miaka kadhaa ili kuondoa vitabu vilivyopitwa na wakati na kuingiza vitabu vipya. Pia, vitabu teule
hubadilishwa ili kuingiza vitabu vingine vyenye maudhui yanayopaswa kusisitizwa kwa wakati huo.
Kwa mfano, wakati wa harakati za ukombozi wa bara la Afrika, vitabu vya ushairi vyenye mrengo huo
vilikuwa muhimu sana, lakini nchi za Afrika zilipopata uhuru, vitabu hivyo vikapungua umuhimu wake
na hivyo kulazimu kubadilishwa na kuingizwa vitabu vingine vinavyobeba maudhui mengine kama vile
ukombozi wa wanawake na kadhalika. Mwalimu anapaswa kuvitambua vitabu hivyo kabla ya kuanza
zoezi la ufundishaji.
Mbali na hilo, mwalimu atachagua na kuvisoma vitabu vya ziada ambavyo atavirejela na kuvitumia.
Jambo la kukumbuka ni kwamba kuna vitabu vingi vinavyoelezea ushairi wa Kiswahili. Vingine ni
dhaifu sana na vimeandikwa bila kufanyika utafiti wa kutosha na vingine hata vina makosa katika
ufafanuzi wa dhana mbalimbali. Kwa hiyo, ni jukumu la mwalimu kutumia vitabu vifaavyo ambavyo,
kadri inavyowezekana, vinawasilisha mawazo sahihi kuhusiana na ushairi wa Kiswahili. Kwa mfano,
kama mwalimu atatumia kitabu cha Harries (1962) Kiswahili Poetry kufundishia chimbuko la ushairi
wa Kiswahili, ni wazi kuwa atawapotosha wanafunzi kwa kuwafundisha kuwa ushairi wa Kiswahili
chimbuko lake ni Uislamu na fasihi ya Kiarabu. Japo kitabu hiki kinasaidia kuelewa chimbuko la
ushairi wa Kiswahili, kinapaswa kutumiwa sambamba na vitabu vingine. Mwalimu, kwa hiyo, hana
budi kusoma vitabu hivi ili kubaini vile vilivyo bora na kuwaongoza wanafunzi kubaini na kuvitumia
vitabu wanavyofaa kuvisoma.
4) Kuandaa Mpangokazi wa Ufundishaji
Baada ya kuchagua mada za kufundisha na kuzipanga ipi itaanza kufundishwa na ipi itafuata na
kusoma vitabu vinavyoelezea mada hizo, hatua inayofuata ni kuandaa mpangokazi wa ufundishaji.
Katika ualimu, mpangokazi wa ufundishaji huitwa azimio la kazi. Azimio la kazi ni mwongozo
ulioandaliwa na mwalimu unaoonesha mpangilio wa mada na mgawanyo wake katika ufundishaji
kwenye muda maalum. Azimio la kazi huandaliwa na mwalimu wa somo husika kama namna ya
kupanga ufundishaji wake utakavyokuwa katika kipindi fulani. Azimio la kazi huweza kuonyesha
ufundishaji katika kipindi cha juma moja, mwezi mmoja, muhula mmoja na kadhalika. Kwa kawaida,
azimio la kazi linaloonyesha ufundishaji katika muhula mmoja ndilo linaloonekana kutumiwa zaidi
kwani linamsaidia mwalimu kupanga ufundishaji utakavyokuwa katika kipindi kirefu. Azimio la kazi la
juma moja halitumiki sana kutokana na ukweli kuwa kama mwalimu atatumia utaratibu huo, atapaswa
kuandaa azimio la kazi kila juma na hivyo kupoteza muda mrefu. Aidha, azimio la kazi la muda mfupi
linaweza kumfanya mwalimu kushindwa kuwa na mipango ya muda mrefu kwa ajili ya darasa lake.
Hata hivyo, azimio la kazi linaloonyesha muda wa zaidi ya mwaka mmoja halifai kutumika kwani, kwa
kawaida, wanafunzi hubadilisha madarasa kila mwaka. Hivyo, azimio la kazi likizidi mwaka mmoja
litakuwa linashughulika na wanafunzi tofauti na labda tuseme haliwezekani kutekelezwa.
Azimio la kazi huwa na vipengele mbalimbali kama vile mwezi mada itakapofundishwa, juma
mada itakapofundishwa, idadi ya vipindi katika juma husika vitakavyotumiwa kufundishia na mada
kuu. Vipengele vingine ni mada ndogo, shughuli za mwalimu zitakazofanywa katika ufundishaji wa
136
mada husika, shughuli za mwanafunzi anazopaswa kuzifanya katika ushiriki wake kwenye zoezi la
kujifunza, vitabu vya rejea vitakavyotumika katika mada husika, vifaa na zana za kufundishia na maoni
yatakayotolewa baada ya zoezi la ufundishaji. Vipengele vyote katika azimio la kazi vinajazwa wakati
wa kuliandaa azimio la kazi husika isipokuwa kipengele cha maoni ambacho kitajazwa mara baada ya
ufundishaji kufanyika. Katika kipengele hicho cha maoni, mwalimu atajaza kile kilichotokea katika
ufundishaji, ikiwa mada imefundishwa kama ilivyopangwa au mada haikufundishwa kutokana na
jambo lolote lililotokea. Miongoni mwa mambo yanayoweza kutokea na yakasababisha wanafunzi
kutofundishwa mada husika katika muda uliopangwa ni kama vile misiba, maafa kama mafuriko na
kadhalika, wanafunzi kuingizwa katika shughuli nyingine badala ya shughuli ya msingi ya kujifunza
kama vile kufyeka, kulima na kadhalika. Kwa ujumla, si kila kilichopangwa na mwalimu katika azimio
la kazi lazima kitokee kwa namna ileile, upo uwezekano wa mambo kutoenda sawa na yalivyopangwa.
Aidha, mwalimu anaweza kubadilisha kipengele chochote kulingana na hali ilivyo wakati wa
ufundishaji. Kwa mfano, mwalimu anaweza kubadilisha shughuli za mwalimu na mwanafunzi
kulingana na hali ilivyo, anaweza kubadilisha kitabu cha rejea kutokana na kupata kitabu bora zaidi cha
rejea, anaweza kubadilisha zana za kufundishia kutokana na kuona kuwa hali ya wanafunzi ilivyo
hairuhusu kutumika kwa zana aliyoibainisha katika azimio la kazi au labda uwezo wa kiuchumi wa
shule kununua zana hiyo ni mdogo na kadhalika. Tunachosema hapa ni kuwa azimio la kazi ni mpango
wa kazi utakavyokuwa na mwalimu anapaswa kujitahidi kadri awezavyo kuutekeleza lakini pale
inapolazimu kubadilisha jambo fulani, mwalimu anaweza kufanya hivyo. Hata hivyo, kwa kuwa azimio
la kazi limeshaandaliwa, mabadiliko yoyote yale hayataingizwa katika azimio la kazi bali mabadiliko
hayo yataonekana katika andalio la somo la siku husika. Katika shule mbalimbali kuna karatasi
maalumu za kuandalia azimio la kazi. Karatasi hizi huwa ni pana zaidi ya karatasi za kawaida. Katika
shule nyingine karatasi hizi hazipo na hivyo ni jukumu la walimu kutafuta karatasi watakazoandalia
azimio la kazi. Mfano wa azimio la kazi unabainishwa hapa chini:
137
SHULE YA SEKONDARI SINGINO
IDARA YA KISWAHILI
AZIMIO LA KAZI LA SOMO LA KISWAHILI KWA MUHULA WA KWANZA, 2013
KIDATO CHA TANO HKL
MWEZI
JUMA
VIPINDI
MADA KUU MADA
NDOGO
SHUGHULI
ZA
MWALIMU
SHUGHULI
ZA
MWANAFUNZI
VITABU VYA
REJEA
VIFAA NA ZANA
ZA KUFUNDISHIA
MAONI
YA MWALIMU
J A N U A R I
1
2 FASIHI KWA
UJUMLA
DHANA ZA
FASIHI
Kuwaongoza
wanafunzi
kuelewa dhana
ya fasihi
ikiwemo
ushairi kwa
kubainisha kazi
mbalimbali za
fasihi
Kushiriki katika
kujifunza kwa
kubainisha dhana za
fasihi kutoka katika
kazi mbalimbali za
fasihi
Samwel
(2012b)
Hadithi
Fupi:
Nadharia ,
Mbinu na
Mifano,
Iringa:
Kasenyenda
Tanzania
Chati za kazi
mbalimbali za fasihi Mada imefundishwa
2 FASIHI KWA
UJUMLA
AINA ZA
FASIHI
Kuwaongoza
wanafunzi
kubaini aina za
fasihi kwa
kutumia kazi
mbalimbali za
fasihi
Kushiriki katika
kujifunza kwa
kubainisha aina za
fasihi kutoka katika
kazi mbalimbali za
fasihi
Mulokozi, M.M.
(1996) Fasihi ya
Kiswahili, Dar es
Salaam: OUT
Chati za kazi
mbalimbali za fasihi
Mada
haikufundishwa
kwani iliingialiana
na michezo ya
UMISSETA. Mada
itarudiwa katika
muda wa ziada
2
2 FASIHI KWA
UJUMLA
DHIMA ZA
FASIHI
Kuwaongoza
wanafunzi
kubaini dhima
za fasihi kwa
kutumia kazi
mbalimbali za
fasihi
Kushiriki katika
kujifunza kwa
kubainisha dhima za
kazi mbalimbali za
fasihi
Mulokozi, M.M.
(1996) Fasihi ya
Kiswahili, Dar es
Salaam: OUT
Chati za kazi
mbalimbali za fasihi
Mada ilifundishwa
ingawa wanafunzi
wachache
walihudhuria.
Wasiohudhuria
walipewa msaada
2 FASIHI KWA
UJUMLA
TANZU ZA
FASIHI
ANDISHI
Kuwaongoza
wanafunzi
kubaini tanzu
za fasihi
andishi
Kushiriki katika
kujifunza kwa
kubainisha tanzu za
fasihi andishi
Mulokozi, M.M.
(1996) Fasihi ya
Kiswahili, Dar es
Salaam: OUT
Chati za ushairi,
riwaya, tamthiliya na
hadithi fupi
Mada ilifundishwa
138
3
4
UCHAMBUZI
WA MASHAIRI
MAUDHUI
YA Diwani
ya MEA
Kuwaongoza
wanafunzi
kusoma na
kubaini
maudhui
yanayojitokeza
katika Diwani
ya MEA
Kushiriki katika
kusoma na
kubainisha maudhui
yanayojitokeza
katika Diwani ya
MEA
Samwel, M. na
Akech, K. (2013)
Diwani ya MEA,
DSM: DZT
Publishers
Chati za ukutani za
mifano ya maudhui ya
kazi za kifasihi
Mada imefundishwa
UCHAMBUZI
WA MASHAIRI
DHAMIRA
ZA
Diwani ya
MEA
Kuwaongoza
wanafunzi
kusoma na
kubaini
dhamira
zinazojitokeza
katika Diwani
ya MEA
Kushiriki katika
kusoma na
kubainisha dhamira
zinazojitokeza
katika Diwani ya
MEA
Samwel, M. na
Akech, K. (2013)
Diwani ya MEA,
DSM: DZT
Publishers
Chati za ukutani za
mifano ya dhamira za
kazi za kifasihi
Mada imefundishwa
4
4
UCHAMBUZI
WA MASHAIRI
FANI YA
Diwani ya
MEA
Kuwaongoza
wanafunzi
kusoma na
kubaini fani
iliyotumika
katika Diwani
ya MEA
Kushiriki katika
kusoma na
kubainisha fani
iliyotumika katika
Diwani ya MEA
Samwel, M. na
Akech, K. (2013)
Diwani ya MEA,
DSM: DZT
Publishers
Chati za ukutani za
mifano ya mbinu za
kifani za kazi za
kifasihi
Mada imefundishwa
UCHAMBUZI
WA MASHAIRI
MATUMIZI
YA LUGHA
KATIKA
Diwani ya
MEA
Kuwaongoza
wanafunzi
kusoma na
kubaini lugha
iliyotumika
katika Diwani
ya MEA
Kushiriki katika
kusoma na
kubainisha lugha
iliyotumika katika
Diwani ya MEA
Samwel, M. na
Akech, K. (2013)
Diwani ya MEA,
DSM: DZT
Publishers
Chati za ukutani za
mifano ya tamathali za
semi
Mada imefundishwa
1 M I T I H A N I Y A N U S U M U H U L A
K U F U N G A S H U L E K W A L I K I Z O Y A N U S U M U H U L A
139
5) Kuteua na Kuandaa Mbinu ya Kufundishia Ushairi na Maandalizi Yake
Baada ya kuandaa azimio la kazi, hatua inayofuata ni kwa mwalimu kuchagua mbinu muafaka
atakayoitumia darasani. Kuna mbinu nyingi ambazo mwalimu anaweza kuzitumia darasani katika
ufundishaji wa ushairi wa Kiswahili. Kuna mbinu kuu mbili zinazoweza kutumiwa katika ufundishaji
darasani. Mbinu hizo ni mbinu shirikishi na mbinu zisizo shirikishi. Mbinu shirikishi ni zile ambazo
mwalimu anampa mwanafunzi nafasi kubwa ya kutoa mchango wake katika mchakato wa kufundisha
na kujifunza. Katika mbinu hii matakwa na matarajio ya wanafunzi yanazingatiwa na hivyo
mwanafunzi ndiye anakuwa mtendaji mkuu katika mchakato wa kufundisha na kujifunza. Jukumu la
mwalimu katika mbinu hii linakuwa lile la mwezeshaji. Mbinu zisizo shirikishi ni kinyume chake.
Katika mbinu zisizo shirikishi mwalimu huwa ndiye mtendaji mkuu na kwamba zoezi la utoaji wa
maarifa linamilikiwa na mwalimu. Mbinu zisizo shirikishi zina hasara nyingi sana katika matumizi
yake kwani zinamchukulia mwalimu kuwa ndiye mjuzi wa kila kitu na kwamba mwanafunzi hajui
lolote. Mbinu hizi huwanyima wanafunzi nafasi ya kuonesha hisia na uwezo wao. Katika ulimwengu
wa sasa, mbinu shirikishi ndizo zinazopigiwa chapuo zaidi kutokana na ubora wake. Hata zile mbinu
ambazo si shirikishi kwa asili yake, zinashauriwa zirekebishwe katika matumizi yake na kumshirikisha
mwanafunzi kwa kiasi kikubwa ili ziwe shirikishi pia kwa namna fulani. Hivyo, ili kufanikisha
ufundishaji wa ushairi wa Kiswahili, mbinu shirikishi zinafaa zaidi. Uteuzi wa mbinu ya kufundishia
inategemea mambo kadhaa. Miongoni mwa mambo hayo ni haya yafuatayo:
(i) Mada: mada itaamua mbinu ya kutumika kufundishia. Kila mada inaweza kufundishika vizuri
kwa kutumia mbinu yake mahsusi na kwamba si kila mbinu inaweza kutumika katika kila mada.
Kwa mfano, itakuwa vigumu sana kutumia mbinu ya nyimbo kufundishia mada ya ushairi
kwani ushairi wenyewe ni nyimbo pia.
(ii) Malengo: uteuzi wa mbinu ya kufundishia pia utategemea malengo mahsusi ambayo mwalimu
anakusudia yatimie katika mada fulani. Kama lengo la mwalimu ni kuwafanya wanafunzi
wakumbuke jambo hilo ni wazi kuwa atatumia mbinu ambayo inaamsha kumbukumbu ya
wanafunzi; kama lengo ni kuwafanya wanafunzi wathamini, au wachanganue au waweze
kufanya kwa vitendo na kadhalika, mbinu inayopaswa kuteuliwa ni ile ambayo inaweza
kutimiza malengo husika.
(iii) Ukubwa wa darasa: kama darasa ni kubwa sana (lina wanafunzi wengi) kuna mbinu hazitafaa
kutumika na pia kama ni dogo sana (lina wanafaunzi wachache) kuna mbinu hazitafaa
kutumika. Kwa mfano, kama darasa ni kubwa sana ni wazi kuwa mbinu ya majadiliano katika
vikundi haitafaa sana kwani makundi hayo hayatapata muda wa kutosha kuwasilisha yote na
yakaisha. Aidha, kuna uwezekano wa kuibuka zogo kubwa sana wakati wa majadiliano.
(iv)Hali ya wanafunzi: wanafunzi wanaweza kuwa katika hali ambayo hairuhusu utumizi wa
mbinu fulani. Kwa mfano, kama wanafunzi wana uwezo mdogo sana kiakili kuna mbinu
hazitafaa kabisa kuzitumia maana zinahitaji wanafunzi wenye uwezo kiasi. Aidha, kama
wanafunzi wamepatwa na msiba wa mwenzao ni wazi kuwa mbinu ambazo si shirikishi
hazitafaa kwani watakuwa wamejaa hofu na huzuni. Njia bora katika mazingira kama hayo ni
mbinu shirikishi ambayo itawashirikisha na wao na hivyo kuwaondolea hofu na mawazo.
(v) Hali ya mwalimu: mwalimu pia anaweza kuathiri uteuzi wa mbinu ya kufundishia. Mbinu
inayoteuliwa inapaswa kuendana na mwalimu, yaani mwalimu awe na umahiri katika kuitumia
ili iweze kuwa na manufaa makubwa. Mwalimu lazima aelewe namna ya kuiandaa mbinu
husika, namna ya kuitumia, faida na hasara zake ili matumizi ya mbinu hiyo yafanikishe somo
lake. Mbinu ambayo mwalimu haimudu vema hapaswi kuitumia. Vilevile, kuna wakati
mwalimu kama binadamu, anaweza kuwa katika hali inayomzuia kutumia mbinu fulani. Labda
hana amani, hana furaha, ana matatizo binafsi na kadhalika. Akiwa katika hali kama hizo ni
dhahiri hataweza kuwa msemaji mkuu darasani. Ni vema msemaji mkuu awe mwanafunzi na
mwalimu awe mwezeshaji tu. Hii ni kusema kuwa katika hali kama hizo, mbinu shirikishi ni
bora zaidi.
(vi)Gharama ya mbinu husika: kila mbinu ina namna yake ya kuiandaa na inahitaji gharama zake.
Kuna mbinu nyingine ni ghali sana na nyingine ni nafuu. Hivyo, uteuzi wa mbinu uzingatie
uwezo wa shule au/na wazazi kuimudu mbinu husika. Mbinu kama ziara, kualika mgeni na
nyinginezo ni gharama sana. Gharama hii huweza kuwa si tu katika fedha bali pia muda.
140
Hivyo tuseme kuwa kuna mbinu nyingi ambazo mwalimu anaweza kuteua kuzitumia katika
ufundishaji, si tu wa ushairi wa Kiswahili bali pia mada nyinginezo. Miongoni mwa mbinu ambazo
mwalimu anaweza kuzitumia ni kama hizi zifuatazo:
a) ZIARA: hii huweza kuwa ziara halisi au ziara zisizo halisi. Ziara zisizo halisi ni zile ambapo
wanafunzi husafirishwa kimawazo kwenda katika maeneo yanayohusu kile kinachofundishwa.
Ziara halisi, kwa upande wake, ni zile ambazo wanafunzi husafiri kwa dhahiri kwenda maeneo
yanayohusu kile kinafundishwa. Ziara zisizo halisi hufanywa sana katika zoezi la kufundisha na
kujifunza kiasi kwamba inapozungumziwa mbinu ya ziara inaonekana ni ziara halisi tu kwani
ziara zisizo halisi ni kitu kilichozoeleka. Katika ziara halisi, wanafunzi wanaweza kuchukuliwa
kupelekwa katika sehemu halisi zinazohusiana na ushairi wa Kiswahili. Kwa mfano,
wanapojifunza kuhusu ushairi simulizi wa Kibantu, wanafunzi wanaweza kusafiri na kwenda
kwenye mikoa ambapo shughuli za jando na unyago hufanyika ili wakajionee utendaji wa
nyimbo za jandoni na unyagoni, ama wanaweza kusafiri kwenda katika jamii ambazo bado
zinatenda majigambo na pia wanafunzi wanaweza kutembelea maeneo waliyoishi wasanii
maarufu wa ushairi wa Kiswahili kama vile Shaaban Robert na kadhalika.
Mbinu hii ina ubora na udhaifu wake. Ubora wa mbinu hii ni kama ifuatavyo: kwanza,
inabadilisha mazingira ya kufundisha na kujifunza na hivyo inakuwa na nafasi kubwa ya
kuwasaidia wanafunzi kuelewa. Kwa kawaida, binadamu hupenda mambo tofautitofauti na
hivyo kujifunza katika mazingira yaleyale kila siku miaka nenda rudi kunaweza kumfanya
mwanafunzi kutoelewa somo kutokana na kuyachoka mazingira. Huweza pia kumfanya
mwalimu kutopenda kufundisha kutokana na kuyachoka mazingira. Pili, mbinu hii huweza
kuwafanya wanafunzi kujifunza katika mazingira halisi. Wataalamu wa elimu wanakubaliana
kuwa kujifunza kwa kutumia mazingira halisi husaidia sana wanafunzi kuelewa vizuri somo.
Hivyo, mbinu hii inaweza kuwasaidia wanafunzi kuelewa somo. Tatu, mbinu hii huweza
kusaidia wanafunzi kutunza kumbukumbu. Kwa kuwa wanafunzi wanajifunza katika mazingira
halisi, nafasi ya wanafunzi kukumbuka somo walilojifunza huwa ni kubwa sana.
Mbali na ubora huo mbinu hii ina udhaifu ufuatao: kwanza, mbinu hii ni ya gharama
sana na hivyo haiwezi kutumika katika shule zisizokuwa na uwezo mkubwa kifedha (kama
shule ndiyo hugharamia) au katika jamii ambazo wazazi hawana uwezo mkubwa kifedha (kama
wazazi ndiyo wanagharamia). Kwa kawaida, katika shule nyingi wanafunzi huchangia kiasi cha
fedha kumudu gharama ya usafiri, malazi na chakula wakati wa ziara. Hivyo, wanafunzi ambao
wazazi wao hawana uwezo wa kugharamia ziara wanaweza kushindwa kushiriki katika
ujifunzaji kwa kutumia mbinu hii. Pili, mbinu hii huweza kuathiri vipindi vya masomo mengine.
Hii ni kutokana na ukweli kuwa kama ziara inafanyika katika sehemu ya mbali na shuleni,
itahitaji muda zaidi. Jambo hilo litaathiri vipindi vya masomo mengine shuleni. Namna bora ya
kukabiliana na hili ni kwa kufanya ziara katika kipindi cha likizo au wakati wa mapumziko ya
mwisho wa juma. Hata hivyo, changamoto inaweza kuwa kwa mwalimu kuiacha mada husika
hata kama wakati wa kuifundisha umefika hadi likizo itakapofika ili autumie muda huo
kufundisha mada hiyo. Changamoto ya pili ni kuwa muda wa likizo ni kwa ajili ya wanafunzi
kupumzisha akili ili ziweze kurudi katika hali ya kawaida kabla ya kuendelea na ujifunzaji.
Akili ambayo haina muda wa kupumzika hukosa ufanisi katika zoezi la kujifunza. Likizo pia
humsaidia mwalimu kujiandaa kwa ajili ya ufundishaji ujao. Hivyo, kuitumia likizo kwa ajili ya
ziara za kitaaluma kunaweza kuwaathiri wanafunzi na walimu pia.
Udhaifu wa tatu ni kuwa ziara zinaweza kuchochea tabia mbaya miongoni mwa
wanafunzi. Kama shule inahusisha wanafunzi wa kike na kiume waliokwisha kubalehe na
wanafunzi hao wakaruhusiwa kusafiri kwenye gari moja kwenda kwenye eneo la ziara huku
wakiwa wamekaa kiti kimoja kwa muda mrefu usiku na mchana, mahusiano ya kimapenzi
huweza kuibuka. Aidha, ziara zinapofanywa katika maeneo ya miji mikubwa inayowavutia
wengi, wanafunzi huweza kutumia muda huo wa ziara kama sehemu ya matembezi na si kama
sehemu ya kujifunza na hivyo kuathiri maana nzima ya ziara. Ili kudhibiti haya ni jukumu la
mwalimu aliyeambatana na wanafunzi katika ziara kuwaeleza wanafunzi kwa kina dhumuni la
safari yao, yale wanayotarajiwa kuyafanya na yale ambayo hawatarajiwi kuyafanya. Pia, wakati
141
wote wa safari na wakati wa ziara, mwalimu anapaswa kudhibiti mienendo na tabia za
wanafunzi na kuwapanga kwa namna ambayo haitaibua tabia zisizofaa.
b) KUALIKA MGENI: katika mbinu hii mtu ambaye si mwalimu anayefundisha somo hilo kila
siku hukaribishwa ili kuja kutoa mada husika. Mgeni huyu anaweza kuwa mwalimu wa somo la
ushairi wa Kiswahili kutoka darasa lingine la shule hiyo, mwalimu wa ushairi wa shule nyingine
au mtaalamu wa ushairi kutoka taasisi zinazojishughulisha na ushairi na Kiswahili kwa ujumla
kama vile TATAKI, BAKITA, CHAKITA, CHAKAMA, CHAKA, UKUTA na kadhalika. Kwa
kawaida, mgeni husika huandikiwa barua rasmi ya mwaliko na kuelezwa mada na yale
anayokusudiwa kuyafanya. Mwaliko huo lazima uoneshe siku na saa mada hiyo itakapotolewa.
Kwa kawaida, ni jukumu la waalikaji kumgharamia mgeni usafiri, chakula na masuala mengine
muhimu japokuwa zipo baadhi ya taasisi ambazo huweza kuwagharamia wataalamu wao
wanapoalikwa katika shughuli kama hizo. Wakati mgeni anapokuwa anatoa mada husika kwa
wanafunzi, mwalimu lazima awepo ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wanapata kile
alichokikusudia na kwamba wanafunzi wanafuatilia kwa makini mada hiyo.
Ubora wa mbinu hii ni kuwa wanafunzi wanapata nafasi ya kufundishwa na mtu tofauti
na yule anayewafundisha kila siku. Hivyo, kunakuwa na uwezekano wa wanafunzi kuelewa
somo na kuondoa uwezekano wa wanafunzi kumchoka mwalimu wa somo husika. Faida
nyingine ni kuwa kama mgeni atakuwa mbobezi katika mada husika, wanafunzi watakuwa na
uwezekano wa kuelewa zaidi kuliko kama mada hiyo ingefundishwa na mwalimu wa somo.
Zaidi ya ubora huo, mbinu hii ina udhaifu pia. Udhaifu mkuu wa mbinu hii ni gharama.
Mbinu hii ni ghali mno na hasa pale mgeni anapotoka mbali. Pia kama mgeni atakuwa si
mwalimu kuna uwezekano wa kushindwa kuwasaidia wanafunzi kuelewa mada husika.
Walimu, zaidi ya kujua masomo husika, wamefundishwa pia masuala kama saikolojia ya
wanafunzi, mitaala, namna ya kufundisha na kadhalika. Mambo yote kwa ujumla huwasaidia
sana katika kuwasilisha ujuzi walionao. Mtaalamu wa ushairi ambaye si mwalimu atashindwa
kuwasaidia wanafunzi wenye matatizo binafsi ya kisaikolojia au kitaaluma ambao ili
kuwatambua ni lazima mhusika ajue masuala ya saikolojia na mbinu za ufundishaji.
c) MAJADILIANO: hii ni mbinu ambapo wanafunzi huachwa wajadiliane wao kwa wao juu ya
mada mahsusi. Majadiliano pia huweza kuwa baina ya mwalimu na mwanafunzi. Kuna aina kuu
mbili za majadiliano, majadiliano ya darasa zima na majadiliano katika vikundi vidogo vidogo.
Majadiliano ya darasa zima huhusisha darasa lote juu ya mada fulani ya ushairi. Mbinu hii hufaa
sana kama darasa halina idadi kubwa sana ya wanafunzi, maana darasa likiwa na idadi kubwa
sana mjadala huweza kugeuka na kuwa zogo. Kwa upande wa majadiliano ya vikundi,
wanafunzi hugawanywa katika vikundi vidogovidogo na kuachwa wajadiliane. Katika
majadiliano ya vikundi ni muhimu kuzingatia uwiano wa jinsia kama darasa linahusisha
wanafunzi wa kike na kiume. Si jambo la busara kuwa na kikundi chenye wanafunzi wa kike
pekee au wa kiume pekee; ni vizuri kuwachanganya ili kuwapa uzoefu na kuwafanya wajihisi
kuwa sawa. Pia ni muhimu kuzingatia uwezo wa wanafunzi, si busara kuwa na kikundi chenye
wanafunzi wanaojiweza sana kitaaluma na kuwatenga na wale wasiojiweza. Ni vizuri wanafunzi
kuchanganywachanganywa ili kuwasaidia wale wasiojiweza na kuwafanya wasijisikie vibaya.
Vikundi hivyo pia visiwe vikubwa sana kwani kama wanafunzi wakiwa wengi sana kwenye
kundi kuna uwezekano wa wanafunzi wengine kutoshiriki katika mjadala. Aidha, ni muhimu
kwa kila kikundi kuwa na viongozi kama vile mwenyekiti wa kundi, katibu, mtunza muda,
muhamasishaji na kadhalika. Viongozi hao watasimamia shughuli nzima ya majadiliano na
uwasilishaji wa matokeo ya mjadala wao.
Faida ya mbinu hii ni kuwa wanafunzi wanashiriki katika zoezi la kujifunza na
kufundisha na hivyo ni mbinu bora. Wanafunzi wanaposhiriki katika mchakato wa kujifunza na
kufundisha hujihisi kuwa wamethaminiwa na huongeza uwezekano wa wanafunzi kuelewa.
Faida nyingine ni kuwa mbinu ya majadiliano hupunguza uwezekano wa wanafunzi kuchoka
wakati wa mchakato wa kufundisha na kujifunza na hivyo kuboresha mchakato huo. Vilevile,
142
mbinu hii huwajengea wanafunzi hali ya kujiamini, kushindana kwa hoja na kujenga hoja.
Mambo hayo ni muhimu sana katika maendeleo ya kitaaluma ya wanafunzi.
Kwa upande wa udhaifu wa mbinu hii ni kuwa kama zoezi la kujadiliana
halitasimamiwa vema kuna uwezekano wa kuibua zogo miongoni mwa wanafunzi. Pia
majadiliano huweza kuwafanya wanafunzi kutoka nje ya mada na kuanza kujadiliana mambo
mengine yasiyohusiana na mada. Mijadala kuhusiana na mambo ya michezo kama vile mpira
na kadhalika huweza kuibuka. Vilevile mbinu hii huweza kuwabagua baadhi ya wanafunzi, hasa
wale wenye uwezo mdogo kitaaluma na hivyo kujihisi kama wametengwa na mjadala mzima
kutawaliwa na watu wachache. Mambo haya, hata hivyo, yanaweza kudhibitiwa kwa usimamizi
mzuri wa mwalimu na viongozi wa vikundi.
d) MDAHALO: hii ni mbinu ambapo wanafunzi hugawanywa katika pande mbili na kujibizana
juu ya mada fulani kuhusu ushairi wa Kiswahili. Kwa kawaida pande hizo mbili huwa upande
unaounga mkono na ule unaopinga dai lililotolewa. Mwalimu huandaa mada na kuwaacha
wanafunzi wakijibizana juu ya mada hiyo na wakati huohuo wakijifunza mada fulani ya ushairi
ambayo mwalimu ameikusudia. Kwa mfano, mada inaweza kuwa Vina na Mizani ni Uti wa
Mgongo wa Mashairi ya Kiswahili, Chimbuko la Ushairi wa Kiswahili ni Ushairi wa Kiarabu,
Ushairi wa Bongo Fleva si Ushairi Asilia wa Kiswahili n.k. na wanafunzi wanajibizana,
wengine wakiunga mkono huku wengine wakipinga. Ili mbinu hii ifanikiwe panapaswa kuwa na
viongozi wa mdahalo, yaani mwenyekiti, katibu, mtunza muda na wachangiaji wakuu. Jukumu
la mwenyekiti ni kusimamia zoezi zima la majibizano na ndiye anayetoa nafasi kwa
wachangiaji. Katibu yeye huwa mtunza kumbukumbu na mwandishi wa hoja zinazotolewa.
Naye mtunza muda ana jukumu la kuhakikisha kila mchangiaji anatumia muda uliopangwa na
anayezidisha muda anagongewa kengele ili aweze kukaa chini na kutoa nafasi kwa mchangiaji
mwingine. Nao wachangiaji wakuu hugawanyika katika makundi mawili, wachangiaji wakuu
kwa upande wa utetezi wa mada na wachangiaji wakuu kwa upande wa upinzani. Kwa kawaida
baada ya mwenyekiti kutambulisha mada na kufafanua, wachangiaji wakuu hukaribishwa
kwanza kabla ya wachangiaji wengine. Wachangiaji wakuu hupewa muda mwingi zaidi ya
wachangiaji wa kawaida. Kwa mfano, mchangiaji mkuu anaweza kupewa dakika tano wakati
mchangiaji wa kawaida anapewa dakika tatu na kadhalika. Baada ya mdahalo kwisha hoja
zilizotolewa huhesabiwa na mshindi hutangazwa.
Ubora wa mbinu hii katika ufundishaji wa ushairi wa Kiswahili ni kuwa wanafunzi
hushiriki katika mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji. Pili, mbinu hii huwajengea wanafunzi
hali ya kujiamini, kushindana kwa hoja, upangaji wa hoja na pia uwezo wa kushawishi. Katika
kujiamini tunaona kuwa ili kutoa hoja mwanafunzi lazima asimame mbele ya wenzake inajenga
ile hali ya kujiamini na kuongea mbele za watu. Pia kwa kuwa mdahalo ni kushindana kwa hoja,
wanafunzi wanajengewa uwezo wa kushindana kwa hoja. Vilevile wanafunzi wanawezeshwa
kuweza kupanga hoja za muhimu kwanza na zingine baadaye na uwezo wa kuwashawishi
wenzao kukubali uzito wa hoja wanayoitoa.
Mbali na ubora huo mbinu hii inaweza kuwa na udhaifu. Udhaifu mkuu ni kuwa kama
mdahalo usipodhibitiwa vizuri na wanafunzi kuelezwa kwa kina malengo yake unaweza
kushindwa kutoa maarifa ya mada iliyokusudiwa na kuishia kuwa kama sehemu tu ya
mabishano. Aidha, huweza kuishia katika ugomvi na uhasama wa kudumu miongoni mwa
wanafunzi.
Zaidi ya mbinu hizi tulizozifafanua hapa, mbinu nyingine zinazoweza kutumiwa na
walimu wa ushairi wa Kiswahili ni pamoja na maswali na majibu, igizo na bungua bongo.
Katika maswali na majibu mwalimu huandaa maswali yake ambayo atawauliza wanafunzi
katika kukamilisha ujifunzaji wa mada fulani ya ushairi. Katika igizo, mwalimu huwataka
wanafunzi kuigiza jambo fulani la kishairi. Mbinu hiyo huweza kufaa sana kufundishia ngonjera
ambazo huonekana kuwa na namna fulani ya uigizaji.
143
6) Kuandaa Mwongozo wa Ufundishaji wa Ushairi Darasani
Baada ya mwalimu kuandaa mpangokazi wa ufundishaji (azimio la kazi) unaoonyesha ushairi
utafundishwa lini na kuteua mbinu atakayoitumia katika ufundishaji wa mada anayokusudia
kuifundisha katika siku husika, jambo linalofuata ni kuandaa mwongozo wa ufundishaji wa ushairi
darasani. Mwongozo wa ufundishaji wa darasani huitwa andalio la somo. Andalio la somo ni
mwongozo wa mwalimu juu ya zoezi la ufundishaji darasani. Kwa kawaida, andalio la somo huonyesha
jinsi ufundishaji utakavyokuwa darasani katika kipindi husika. Nchi mbalimbali za Afrika Mashariki
zinatofautiana dakika kwa kila kipindi, na hata shule katika nchi moja huweza kutofautiana katika
dakika kwa kila kipindi. Zipo shule ambazo kipindi kimoja huwa ni dakika arobaini, nyingine ni dakika
arobaini na tano, hamsini na kadhalika. Somo la Kiswahili huweza kuwa na idadi tofautitofauti ya
vipindi katika shule mbalimbali. Zipo shule ambazo Kiswahili hupewa vipindi vitatu kwa wiki, yaani
vipindi viwili kwa pamoja (double periods) na kipindi kimoja (single period). Kwa hiyo mwalimu
katika shule kama hizo atapaswa kuandaa maandalio ya somo mawili, moja kwa ajili ya vipindi viwili
na lingine kwa ajili ya kipindi kimoja. Zipo shule ambazo, kama ilivyo kwa azimio la kazi, zina
madaftari maalumu ya kuandalia maandalio ya somo. Madaftari hayo yamegawanywa katika vipengele
mbalimbali vya andalio la somo na jukumu la mwalimu ni kujaza tu nafasi zilizoachwa katika
vipengele hivyo kulingana na kile anachokusudia kufundisha katika siku husika. Katika shule ambazo
hakuna madaftari ya aina hiyo mwalimu atatakiwa kutafuta karatasi zifaazo na kutengeneza andalio la
somo. Hata hivyo utaratibu wa kuwa na madaftari maalumu ya andalio la somo ni mzuri kwani
unawapunguzia walimu kazi kubwa ya kuandaa andalio la somo na pia husaidia katika kuleta uwiano
miongoni mwa walimu wa shule husika katika sura ya andalio la somo.
Andalio la somo lina vipengele mbalimbali. Vipengele hivyo ni pamoja na tarehe, idadi ya
wanafunzi na jinsi zao, idadi ya vipindi vitakavyotumika kufundisha, mada kuu, ujuzi unaotegemewa
kupatikana, mada ndogo, lengo kuu, malengo mahsusi, vitabu vya kiada, ziada na rejea, zana za
kufundishia, hatua za utoaji wa somo (ufundishaji), shughuli zitakazofanywa na mwalimu na
mwanafunzi, mbinu ya tathmini itakayotumika na maoni ya mwalimu kuhusu ufundishaji husika.
(a) Tarehe: katika kipengele hiki mwalimu atabainisha tarehe atakayofundisha somo husika.
(b) Idadi ya wanafunzi na jinsi zao: katika kipengele hiki mwalimu atabainisha idadi ya
wanafunzi aliowakuta darasani katika ufundishaji wake (waliohudhuria) na pia idadi ya wale
ambao hajawakuta (wasiohudhuria). Mwalimu mzuri atafuatilia idadi ya wanafunzi
wanaohudhuria darasani na wale ambao hawahudhurii ili kubaini tatizo linalowafanya
wengine wasihudhurie na kutafuta namna ya kuwasaidia. Mwanafunzi asiyehudhuria
darasani ana nafasi kubwa ya kushindwa mtihani. Aidha, ni vizuri kujua mahudhurio kwa
jinsi (wanafunzi wa kike na kiume) ili kuweza kubaini matatizo ya kijinsia yanayokwamisha
jinsi fulani kuhudhuria darasani na kutafuta ufumbuzi wake. Kuna baadhi ya jamii katika
nchi za Afrika Mashariki ambazo hazioni umuhimu wa kumpatia mtoto wa kike elimu,
hivyo mtoto wa kike huweza kuachwa nyumbani akifanya shughuli kama vile kupika,
kuchota maji na kadhalika wakati mtoto wa kiume akiwa shule. Kutokana na hilo, ni vizuri
kwa mwalimu kufuatilia mahudhurio kwa jinsi ili kuweza kuyabaini matatizo ya aina hiyo.
(c) Idadi ya vipindi: katika kipengele hiki mwalimu atabainisha kipindi chake ni cha ngapi na
kina muda gani. Muda kipindi kilipopangwa kinaweza kuathiri kueleweka kwa somo. Kwa
mfano, vipindi vingi vilivyo karibu na muda wa mapumziko huathiriwa sana kwani
wanafunzi huwa wanawaza mapumziko na hivyo wakati mwingine kushindwa kuelewa
masomo. Pia vipindi vinavyofuata baada ya chakula huambatana na kulala kwa wanafunzi
wengi kutokana na mchakato wa umeng’enyaji wa chakula. Aidha, idadi ya vipindi
alivyonavyo mwalimu vitaamua uwingi wa mambo atakayoyafundisha mwalimu. Hivyo ni
vema kubainisha idadi ya vipindi ili kupima ikiwa yale anayokusudia kuyafundisha
yatatosha katika muda husika wa kipindi.
(d) Mada kuu na mada ndogo: kwa kawaida mada kuu na ndogo hutoka katika silabasi na
kuchukuliwa katika azimio la kazi. Hata hivyo, mwalimu huweza kuamua mada ndogo
kulingana na muda alionao na upana wa mada husika.
144
(e) Ujuzi: katika kipengele hiki mwalimu anapaswa kubainisha ujuzi anaotaka wanafunzi
husika waupate mara baada ya kumaliza kufundisha na kujifunza mada kuu na mara baada
ya kumaliza kufundisha na kujifunza mada ndogo.
(f) Lengo kuu: hutokana na mada kuu na kwa kawaida huwa ni pana na haliwezi kufikiwa
katika ufundishaji wa kipindi kifupi bali baada ya ufundishaji wa mada nzima. Hivyo, lengo
kuu huwa la jumla na haliwezi kupimwa kirahisi. Maneno yanayotumika katika kuandaa
lengo kuu huwa hayapimiki, ni maneno ya jumla. Maneno hayo huweza kuwa kuelewa,
kujua, kutambua, kufahamu, kuzingatia na kadhalika. Kwa mfano, tunaweza kuwa na lengo
kuu: Kufikia mwisho wa mada wanafunzi waweza kuelewa chimbuko la ushairi wa
Kiswahili. Lengo hili kwa hakika halipimiki. Swali linaweza kuwa je, unawezaje kujua
kuwa wanafunzi wameelewa?
(g) Malengo mahsusi: huitwa pia madhumuni mahsusi. Haya hutokana na mada ndogo na,
kwa kawaida, huweza kupimwa mara baada ya kipindi kwisha. Maneno yanayotumiwa
katika kuandaa malengo mahsusi ni sharti yawe yanayoweza kupimika. Maneno hayo ni
kama vile kutaja, kueleza, kuorodhesha na kadhalika. Hivyo, lengo mahsusi linaweza kuwa:
Kufikia mwisho wa kipindi kila mwanafunzi wa kidato cha tano aweze kueleza kwa usahihi
hoja tatu kati ya tano za Harries zinazoeleza kuwa chimbuko la ushairi wa Kiswahili ni
Uislamu na fasihi ya Kiarabu. Madhumuni haya ni mahsusi na yanapimika; mwisho wa
kipindi mwalimu anaweza kumwambia mwanafunzi aeleze na akiweza kueleza atajua kuwa
malengo mahsusi ya somo yamefikiwa.
(h) Vitabu vya kiada, ziada na rejea: hivi ni vile vitabu ambavyo mwalimu amevitumia katika
uandaaji wa somo. Mwalimu mzuri ni yule ambaye anasoma kabla ya kuingia katika
ufundishaji darasani. Jambo likieleweka vizuri kwa mwalimu linaweza pia kueleweka kwa
mwanafunzi. Vitabu vya kiada ni vitabu vya lazima katika mada husika, vitabu vya ziada ni
vile ambavyo hutumiwa kuongeza maarifa na vitabu vya rejea ni vitabu vinginevyo
vinavyozungumzia mada husika. Katika kipengele hiki mwalimu anaonyesha mahali
ambapo amejiegemeza katika mada husika.
(i) Zana za kufundishia: kuna tofauti kati ya zana za kufundishia na vifaa vya kufundishia.
Vifaa vya kufundishia ni dhana pana inayojumuisha vitu vyote vinavyoenda sambamba na
zoezi la utekelezaji wa mtaala wowote uwao. Ni vitu vyote vinavyosaidia mchakato wa
kufundisha na kujifunza ikiwa ni pamoja na silabasi, vitabu vya ziada, kiada na rejea, zana
za kufundishia, vifaa kama vile chaki, ubao, hata jengo lenyewe la darasa na kadhalika.
Zana za kufundishia, kwa upande wake, ni vielelezo ambavyo mwalimu ataona vinafaa
kufundishia mada husika ili kumsaidia mwanafunzi kuelewa. Kwa kawaida mwalimu ndiye
huteua zana za kufundishia, huziandaa na kuzitumia darasani katika mchakato wa
kufundisha na kujifunza. Vielelezo hivi huweza kuwa vitu halisi, picha, matukio
yanayosawiri mada na hata sehemu huweza kuwa zana ya kufundishia.
Katika kipengele hiki mwalimu hubainisha zana za kufundishia atakazozitumia. Zana
mbalimbali ambazo mwalimu huzitumia katika ufundishaji wake. Matumizi ya zana za
kufundishia yana dhima kubwa sana katika mchakato wa kufundisha na kujifunza. Miongoni
mwa dhima hizo ni kama ifuatavyo:
· Zana za kufundishia humshirikisha mwanafunzi katika zoezi la ufundishaji na
kujifunza
· Humsaidia mwalimu kulifanya somo kuwa halisi kuliko kuwa la kufikirika
· Humsaidia mwanafunzi kuzingatia anayojifunza
· Husaidia kumbukumbu ya mwanafunzi
· Huchochea udadisi kwa wanafunzi
· Huondoa uchovu kwa wanafunzi
· Husaidia wanafunzi kuelewa mada husika
(j) Hatua za utoaji wa somo: katika kipengele hiki mwalimu atabainisha hatua za ufundishaji
atakazozifuata darasani. Kwa kawaida utoaji wa somo darasani huwa na hatua tano:
utangulizi, utoaji wa maarifa mapya, kukazia maarifa, matumizi na hitimisho la somo.
Katika utangulizi, kwa kawaida mwalimu huwaandaa wanafunzi wake kwa ajili ya mada
145
mpya. Kwanza, mwalimu hupima kumbukumbu ya wanafunzi katika mada iliyopita na kisha
kuhusisha mada iliyopita na mada mpya. Baada ya hapo mwalimu hutaja na kufafanua
malengo mahsusi ya somo. Kumekuwa na mjadala ikiwa malengo ya somo ni kwa ajili ya
mwalimu au mwanafunzi. Hata hivyo, inakubalika kuwa malengo ya somo ni kwa ajili ya
mwalimu na mwanafunzi. Kwa mwalimu, malengo ni muhimu kwani humsaidia kujua nini
akifundishe, akifundisheje na pia atumie mbinu gani kutathmini. Kwa mwanafunzi, malengo
ni muhimu kwani humsaidia kujua kwa nini anafundishwa na ategemee nini na pia mwisho
wa kipindi au mada atatarajiwa kuwa na uwezo wa kufanya nini. Hii humfanya mwanafunzi
wakati wote wa mchakato wa kufundisha na kujifunza awe anatafuta kutimiza malengo
hayo. Kwa kuwa malengo haya ni muhimu kwa mwalimu na mwanafunzi, ni muhimu kwa
mwalimu kuyasoma malengo haya darasani na kuyafafanua kabla ya kuendelea na
ufundishaji wake ili kuwaandaa wanafunzi.
Baada ya utangulizi, hatua inayofuata ni utoaji wa maarifa mapya. Katika hatua hii
mwalimu ataanza utoaji wa maarifa mapya aliyoyakusudia. Hatua zinazofuata ni kukazia
maarifa mapya aliyoyatoa na matumizi ya maarifa hayo mapya. Katika hatua hizi mwalimu
atatumia vifaa na zana mbalimbali za kufundishia kutimiza malengo ya somo husika na
kuwawezesha wanafunzi kuyatumia maarifa hayo. Hatua ya mwisho ni hitimisho. Katika
hatua hiyo, mwalimu atatoa muhtasari wa yale aliyoyafundisha na kisha atapima ikiwa
madhumuni mahsusi ya somo husika yametimizwa. Upimaji wa madhumuni mahsusi ya
somo huenda sambamba na kipengele kinachofuata, upimaji wa kutimia kwa malengo
mahsusi. Katika kipengele hiki cha utoaji wa somo darasani, mwalimu atabainisha kazi
zitakazofanywa na mwalimu na zile zitakazofanywa na mwanafunzi katika kila hatua.
(k) Maoni na tathmini: katika kipengele hiki mwalimu atajipima mwenyewe na ufundishaji
wake kuona ikiwa amefanikiwa au la. Mwalimu katika kipengele hiki atabainisha wanafunzi
wangapi wameelewa na wangapi hawakuelewa na wale ambao hawakuelewa, hata kama ni
wachache, aliwasaidiaje. Katika kipengele hiki mwalimu huweza kuandika, kwa mfano,
mada imefundishwa na kueleweka kwani asimilia tisini ya wanafunzi walipata zaidi ya nusu
katika zoezi nililowapa na wale walioshindwa nilitenga muda wa ziada kuwaelewesha vizuri
zaidi.
(l) Saini ya mwalimu: Katika kipengele hiki mwalimu atapaswa kuweka saini yake ili
kuthibitisha kuwa aliyoyasema huko juu katika vipengele vingine ni kweli. Kipengele hiki
huitwa pia kipengele cha ithibati, yaani kipengele cha kuthibitisha maelezo ya huko juu.
Saini hutumiwa mahali pengi kama njia ya kuthibitisha ukweli wa mambo mbalimbali. Kwa
mfano, saini hutumika benki kuhakikisha kuwa malipo yaliyofanywa ni sahihi, saini
hutumiwa pia katika mikataba na kadhalika.
MFANO WA ANDALIO LA SOMO
SHULE YA SEKONDARI SINGINO
ANDALIO LA SOMO LA KISWAHILI
TAREHE KIDATO VIPINDI MUDA MAHUDHURIO
WALIOFIKA
W/WAKE: 40
W/UME: 20
1/5/2013 V HKL
2
DAKIKA 80
(Saa 6.00-7.20)
WASIOFIKA: 2
MADA KUU: UHAKIKI WA MASHAIRI
MADA NDOGO: DHAMIRA KATIKA DIWANI YA MEA
LENGO KUU: Wanafunzi waweze kutambua dhamira mbalimbali zinazoibuliwa na waandishi wa
Diwani ya MEA.
UJUZI: Wanafunzi waweze kusoma kazi ya fasihi na kubainisha mawazo makuu yaliyomo katika kazi
husika
MADHUMUNI MAHSUSI: Kufikia mwisho wa kipindi cha dakika 80 wanafunzi wa kidato cha tano
146
HKL kwa kutumia Diwani ya MEA waweza kutaja na kuzieleza kwa usahihi dhamira
angalau tano zinazojitokeza katika Diwani ya MEA huku wakitoa mifano katika nchi za
dunia ya tatu.
MAREJEO: Samwel, M. na Akech Kabiero (2013) Diwani ya MEA, Dar es Salaam: DZT Publishers
ZANA ZA KUFUNDISHIA: Chati za ukutani za dhamira za kazi za kifasihi na uhusiano wake na
uhalisia.
UTOAJI WA SOMO:
HATUA
NA
MUDA
SHUGHULI
ZA
MWALIMU
SHUGHULI
ZA
MWANAFUNZI
UTANGULIZI
(Dakika 10)
-Kuwajengea wanafunzi utayari
-Kupima maarifa ya awali juu ya
nadharia ya fasihi
-Kuhusisha nadharia ya fasihi na
uchambuzi wa mashairi
-Kueleza madhumuni mahsusi
ya somo jipya
-Kuwa tayari kwa ajili ya
kujifunza
-Kujibu maswali wanayoulizwa
kuhusiana na maarifa ya awali
-Kuuliza maswali kuhusu
maeneo ambayo hawajayaelewa
vizuri
-Kusikiliza
KIINI (Utoaji wa maarifa
mapya, kukazia maarifa,
matumizi)
(Dakika 60)
-Kuwaongoza wanafunzi
kubainisha dhamira
zinazojitokeza katika Diwani ya
MEA
-Kuwaongoza wanafunzi
kutumia chati za dhamira
kuhusisha dhamira hizo na
uhalisia wake katika dunia ya
tatu
-Kuwashirikisha wanafunzi
katika zoezi zima la kujifunza
-Kushirikiana na mwalimu
katika kubainisha dhamira
zinazojitokeza katika Diwani ya
MEA
-Kutumia chati za ukutani
kubainisha dhamira na kueleza
zinavyohusiana na hali halisi
-Kujibu maswali wanayoulizwa
na mwalimu na wao kuuliza
maswali wasipopaelewa
HITIMISHO
(Dakika 10)
-Kutoa muhtasari wa mambo
muhimu yaliyofundishwa
-Kupima kufikiwa kwa malengo
mahsusi ya somo
-Kusikiliza, kuuliza maswali na
kujibu maswali
-Kufanya zoezi walilopewa ili
kupima kufikiwa kwa malengo
mahsusi ya somo
MAONI NA TATHMINI: Mada imeeleweka kwani wanafunzi wameweza kutaja dhamira kama vile
rushwa, uongozi mbaya n.k. na kuzihusisha na hali halisi. Asimilia 98 ya wanafunzi wamepata
zaidi ya alama 60 kati ya 100 katika zoezi nililowapa. Wachache ambao hawakufanya vizuri
nimepanga kuwasaidia katika muda wa ziada ili kuhakikisha wanaelewa pia.
SAINI YA MWALIMU: Jasinta.
7) Kuandaa Zana za Kufundishia
Baada ya andalio la somo kukamilika, mwalimu anapaswa kuandaa zana za kufundishia mada
husika. Kama tulivyobainisha katika kipengele kilichopita, kwa kawaida, mwalimu hubainisha, katika
andalio la somo, zana za kufundishia mada husika. Baada ya kuzibainisha, hatua inayofuata ni
kuziandaa kwa kuzingatia sifa tulizozieleza hapo awali kwamba zana hizo ni muhimu ziwe zenye
kuvutia, zenye rangi nzuri na pia zinazoonekana vizuri hata kutokea mwisho wa darasa. Aidha, zana za
kufundishia lazima zitumie maandishi makubwa. Maandalizi ya zana hizo hutegemea aina ya zana
husika. Jambo lingine la muhimu ni kuwa zana zinapaswa kuendana na mada husika.
147
8) Kuingia Darasani na Kufundisha
Kuingia darasani na kufundisha huitwa pia ufundishaji halisi darasani. Ufundishaji halisi darasani ni
matokeo ya andalio la somo aliloliandaa mwalimu. Jambo la kukumbuka hapa ni kuwa andalio la somo
ni mwongozo tu ambao mwalimu anautumia na kwamba mwalimu hapaswi kuwa mtumwa wa andalio
la somo. Mwalimu anaweza kurekebisha jambo lolote lililopo katika andalio la somo kulingana na hali
ya wanafunzi au hali halisi aliyoikuta darasani. Kwa mfano, mwalimu anaweza kurekebisha muda
alioutenga kuutumia katika kila kipengele, mwalimu anaweza kurekebisha mbinu ya ufundishaji na
kadhalika. Mfano mzuri ni kuwa kama mwalimu amepanga kutumia dakika kumi katika utangulizi na
akabaini kuwa asilimia kubwa ya wanafunzi hawako tayari kwa ajili ya maarifa mapya na kwamba
maarifa ya awali hayajaeleweka vema, ni wazi kuwa mwalimu huyo atalazimika kutumia muda mrefu
zaidi katika utangulizi akifafanua maarifa ya awali kabla ya kuanza maarifa mapya. Pia kama mwalimu
amepanga kutumia mbinu ya muhadhara mfupi, kwa mfano, lakini akakuta wanafunzi hawapo katika
hali nzuri kutokana na msiba walioupata ni wazi kuwa mwalimu atalazimika kubadilisha mbinu yake ili
atumie mbinu shirikishi zaidi itakayowafanya wanafunzi kushiriki na kusahau madhila yao. Aidha,
mwalimu hapaswi kila mara kulirejelea andalio la somo kuangalia aliandika katika hatua fulani
atafanya nini. Mwalimu anapaswa kuelewa yale aliyoyaandika katika andalio la somo na kulirejelea
andalio la somo pale tu ambapo ni muhimu kufanya hivyo.
9) Kufanya Tathmini (Upimaji) ya Ufundishaji wa Ushairi
Kuna aina mbili za tathmini zinazoweza kufanywa katika ufundishaji. Kuna tathmini ambayo
mwalimu huifanya wakati zoezi la ufundishaji likiendelea na kuna tathmini ambayo mwalimu huifanya
baada ya ufundishaji kukamilika. Katika tathmini ya wakati zoezi la ufundishaji likiendelea, mwalimu
wakati wote wa ufundishaji wake darasani huuliza maswali mbalimbali kupima uelewa wa wanafunzi
juu ya mambo mbalimbali anayoyafundisha. Wakati wa tathmini hii inashauriwa kwa mwalimu
anayefundisha ushairi wa Kiswahili kuwauliza maswali wanafunzi tofautitofauti na si wanafunzi
wachache tu. Kuna baadhi ya walimu huwa na wanafunzi wao ambao huwauliza maswali mara kwa
mara. Ni vema kuwasaidia hata wanafunzi ambao hawako tayari kujibu maswali haya ili na wao
washiriki kujibu. Pia tathmini hii izingatie jinsi za wanafunzi, mwalimu anapaswa kuwauliza maswali
wanafunzi wa kike na kiume na si wa kiume pekee au wa kike pekee. Kuwauliza maswali wanafunzi
wa jinsi moja inaweza kujenga hisia kuwa mwalimu anaichukia jinsi fulani au mwalimu ana upendeleo.
Aina ya pili ya tathmini, tathmini inayofanywa baada ya kukamilika kwa zoezi la ufundishaji, nayo
imegawanyika katika sehemu kadhaa. Kuna tathmini inayofanywa kama kazi za nyumbani na kuna
tathmini inayofanywa kwa njia ya mitihani, majaribio na mazoezi. Kazi za nyumbani, mara nyingi
hutolewa mara tu baada ya zoezi la ufundishaji kukamilika. Wanafunzi wanapewa kazi ambazo
wanazifanya nyumbani na kuzirudisha shuleni kwa mwalimu siku inayofuata kwa ajili ya usahihishaji.
Mazoezi, majaribio na mitihani hutolewa na walimu katika kipindi fulani. Kwa mfano, kuna mitihani ya
wiki (weekly tests), mitihani ya mwezi (monthly tests), mitihani ya nusu muhula (mid-term tests),
mitihani ya mwisho wa muhula (terminal tests), mitihani ya mwisho wa mwaka (Annual tests) na
mitihani ya taifa (national examinations). Mitihani yote hii ina uzito wake kwa mwanafunzi, mwalimu
na jamii. Kwa kawaida ushairi wa Kiswahili huwa sehemu ya mtihani wa somo la Kiswahili katika
ngazi mbalimbali za elimu. Katika ngazi nyingine mtihani wa ushairi huweza kutenganishwa na
mtihani wa jumla wa Kiswahili na hivyo kuwa somo linalojitegemea au kuwekwa katika mtihani wa
fasihi ya Kiswahili. Kwa kawaida upimaji ni moja ya kipengele kinachobainishwa katika muhtsari na
kuna malengo kadhaa ya kufanya tathmini.
MALENGO YA KUFANYA TATHMINI
(i) Kupima uwezo asilia wa mwanafunzi na uwezo utokanao na kufundishwa na kujifunza
(ii) Kupima maendeleo ya mwanafunzi katika mchakato wa kufundisha na kujifunza kutokana na
malengo mahsusi
(iii) Kupima uwezo wa mwalimu kufundisha na mbinu za ufundishaji anazozitumia
(iv) Kupima ubora wa silabasi inayotumika
(v) Kutathmini ubora wa mazingira mwanafunzi anayojifunza
148
Kutokana na malengo haya ya upimaji tunabaini kuwa zoezi la kufanya tathmini linahusisha
kupima mafanikio ya ufundishaji kwa kuangalia matatizo ya mwanafunzi, mwalimu, silabasi na hata
mazingira ya kujifunzia. Hivyo, kushindwa kwa mwanafunzi katika mtihani ni kushindwa kwa
mwalimu, silabasi na hata mazingira ya kujifunzia japo si wakati wote hali inaweza kuwa hivyo. Kuna
wakati mwanafunzi anaweza kufanya vibaya kwenye mtihani kutokana na uzembe wake lakini mara
nyingi kufanya vibaya kwa mwanafunzi kunatokana na matatizo ya mwalimu, silabasi na hata
mazingira ya kutolea maarifa. Kama mwalimu atakuwa hajafunzwa na kufuzu vema ni wazi kuwa
wanafunzi wake watafanya vibaya maana hata Waswahili husema mwanafunzi hamzidi mwalimu
wake. Hivyo, kuna haja ya kuwekeza kwa walimu kwa kuwapa mafunzo bora na kuhakikisha fani ya
ualimu inatolewa kwa watu waliofanya vizuri na sivyo ilivyo sasa katika baadhi ya nchi za Afrika
Mashariki ambapo kozi ya ualimu (na hasa ualimu wa shule za awali, msingi na sekondari) inatolewa
kwa watu waliopata madaraja ya chini na kwamba ualimu ni fani ya watu walioshindwa kukubalika
katika fani nyinginezo. Kwa hakika, mwalimu anapaswa kuwa mtu aliyepata daraja la juu zaidi
kutokana na umuhimu wake katika jamii. Pia, walimu hao wanapaswa kupewa motisha ambayo itawapa
utulivu katika ufundishaji wao ili kuinua kiwango cha kufaulu. Aidha, mishahara na maslahi mengine
ya walimu hayana budi kuboreshwa. Jambo la kukumbuka ni kuwa kama mwalimu atafundisha akiwa
na furaha na amani, ana nafasi kubwa ya kufanikisha zoezi la utoaji wa maarifa.
Vilevile, hatuna budi kuhakikisha kuwa silabasi unakuwa bora ili kufanikisha zoezi zima la
kujifunza na kufundisha. Zaidi ya yote, wanafunzi wanapaswa kujifunza katika mazingira mazuri yenye
madarasa, viti vya kukalia na kadhalika. Mwanafunzi anayepata elimu chini ya mti ana nafasi kubwa
sana ya kufanya vibaya katika mtihani.
AINA ZA TATHMINI NA UPIMAJI
Kuna aina mbalimbali za tathmini na upimaji zinazoweza kufanywa katika ushairi wa Kiswahili.
Aina hizo za maswali ya kutathmini ufundishaji na kujifunza hujumuisha hizi zifuatazo:
(i) Kuchagua jibu sahihi/sahihi zaidi (multiple choice questions)
(ii) Kweli/Si kweli (True/False questions)
(iii)Kuoanisha (Matching items questions)
(iv)Kujaza nafasi zilizo wazi (Fill in the blanks questions)
(v) Majibu mafupimafupi (Short answers questions)
(vi) Insha (Essay type questions)
10)Kutoa Matokeo ya Tathmini na Utoaji wa Motisha
Baada ya kufanya tathmini, hatua inayofuata ni kutoa matokeo na motisha. Hatua hii ni muhimu
sana lakini walimu na wataalamu wa elimu hawaiwekei mkazo unaostahili. Inapaswa kukumbukwa
kwamba, kama isivyokuwa na maana kupiga kura ya kuchagua viongozi na kutotoa majibu kwa wakati,
ndivyo isivyokuwa na maana kutoa zoezi, kazi ya nyumbani, jaribio, mtihani na kadhalika bila kutoa
matokeo ya upimaji huo (kwa wakati). Wanafunzi wanapofanya zoezi, kazi ya nyumbani, jaribio,
mtihani au aina nyingineyo ya tathmini, hutarajia majibu. Kwa kawaida, wanafunzi (na hata wakati
mwingine wazazi na walezi na jamii kwa ujumla) husubiri kwa shauku kubwa matokeo ya tathmini
iliyofanyika. Mwanafunzi anapofanya mtihani wa taifa, kwa mfano, husubiri kwa hamu majibu hayo ili
(w)ajue ikiwa ataweza kuendelea na ngazi ya elimu inayofuata ama la. Vilevile, tathmini huweza
kumsaidia mwanafunzi, mwalimu, mzazi na jamii kwa ujumla kubaini maendeleo ya elimu kwa mtu
binafsi, shule na hata taifa kwa ujumla. Hivyo, tunaweza kusema kuwa kuna sababu nyingi
zinazosababisha utoaji wa matokeo ya tathmini kuwa muhimu. Miongoni mwa sababu hizo ni:
(a) Kumpa taarifa mwanafunzi juu ya hatua aliyofikia katika kujifunza
(b) Kumweleza mwanafunzi nini anakimudu vema na nini hakimudu vema katika vitu
alivyojifunza
(c)Kuwafahamisha wazazi na walezi maendeleo ya mwanafunzi
(d) Kuweza kuchagua wanafunzi wa kuendelea na ngazi inayofuata ya elimu
(e)Kutoa motisha kwa wanafunzi waliofanya vema na kama ikibidi adhabu/ushauri kwa
waliofanya vibaya.
(f)Kumwezesha mwalimu kujua maeneo ambayo hakuelewa vema wakati wa zoezi la ufundishaji
149
(g) Kuweza kutoa taarifa juu ya kiwango cha elimu kilichofikiwa na shule, wilaya, mkoa hata taifa
kwa ujumla.
(h) Kuweza kuthibitisha usahihi wa maamuzi yaliyofanywa kwa kutumia matokeo hayo. Kwa
mfano, kama mtihani husika ndiyo uliotumiwa kama kigezo cha kuwachagua wanafunzi wa
kuendelea na ngazi nyingine ya elimu au darasa lingine ni vema matokeo ya mitihani hiyo
yakatolewa ili wanafunzi waweze kujua kwa nini walichaguliwa au hawakuchaguliwa.
Kwa kuwa walimu wengi na taasisi zinazohusika na upimaji na tathmini hawaipi hatua hii ya kutoa
matokeo ya tathmini iliyofanyika umuhimu unaostahili, huchukua muda mrefu kwa wanafunzi kupata
matokeo hayo. Wakati mwingine walimu na taasisi zinazohusika na utoaji wa matokeo hutumia muda
mrefu kutoa matokeo hayo na hivyo kuwaweka wanafunzi katika hali ya taharuki kwa muda mrefu. Ni
jambo muhimu sana kusisitiza kuwa wanafunzi wanapaswa kupewa matokeo ya zoezi, kazi ya
nyumbani, jaribio, mtihani au aina nyingineyo yoyote ya upimaji iliyofanyika, mapema kadri
inavyowezekana. Wanafunzi wanapopewa matokeo hayo mapema, kunakuwa na uwezekano wa
kurekebisha makosa yaliyofanywa na mwanafunzi kwani bado mwanafunzi anakuwa anakumbuka
makosa hayo. Matokeo yanapochelewa, mwanafunzi husahau mtihani ulivyokuwa na majibu
anayoyatarajia, kwa hiyo, ni vigumu kuweza kubadilisha tabia ya mwanafunzi. Vilevile, utoaji wa
mapema wa matokeo mapema humwondolea mwanafunzi hofu ambayo huweza kuathiri afya yake.
Aidha, kuna baadhi ya mitihani na tathmini walizopewa wanafunzi hazirudishwi. Kuna baadhi ya
walimu, kwa maksudi kabisa, hawarudishi mitihani ya wanafunzi ingawa kwa mujibu wa taratibu,
walipaswa kuirudisha. Walimu wa aina hii wanadidimiza maendeleo ya elimu kwani wanafunzi
wanakosa fursa ya kutambua makosa yao na kuyarekebisha. Hata hivyo, kuna mitihani ambayo kwa
mujibu wa taratibu, huwa hairudishwi. Mitihani hiyo ni pamoja na mitihani ya kitaifa ya kumaliza
masomo katika ngazi mbalimbali. Ingawa kuna sababu za msingi za kufanya hivyo, tunaona kuwa kuna
haja ya kuwarudishia wanafunzi mitihani hiyo ili waweze kubaini makosa yao. Japokuwa hawawezi
kuyarekebisha makosa hayo katika ngazi husika kwani wanakuwa wameshamaliza masomo, inaweza
kuwasaidia kujirekebisha katika ngazi za mbele kama watabahatika kuendelea na masomo. Aidha,
katika nchi inayozingatia uwazi na ukweli, kurudisha mitihani hiyo linaweza kuwa jambo zuri la
kujenga imani kwa wadau wa elimu na kuwapa fursa ya kutathmini zoezi la usahihishaji lilivyokuwa.
Wasahihishaji, kama binadamu, huweza kufanya makosa. Makosa hayo yanaweza kurekebishwa kwa
wanafunzi kurudishiwa mitihani yao na kuipitia. Tukiri tu hapa kuwa kurudisha mitihani ya namna hiyo
kunaweza kuwa na changamoto na gharama kubwa.
Kwa kawaida, zoezi la kutoa matokeo ya tathmini iliyofanyika huenda sambamba na utoaji wa
motisha kwa waliofanya vizuri au adhabu na ushauri kwa wanafunzi waliofanya vibaya. Mazoezi, kazi
za nyumbani, majaribio, mitihani na aina nyinginezo za tathmini zinazofanywa katika ngazi ya shule au
darasa husika huweza kuwasaidia walimu kutoa motisha kwa wanafunzi waliofanya vizuri. Motisha hii
huweza kuwa zawadi mbalimbali kama vile vitabu, madaftari, kalamu, pesa au zawadi nyinginezo. Hata
kumwandikia mwanafunzi vizuri sana katika daftari la mazoezi ni motisha. Katika ngazi za mitihani ya
kitaifa, motisha hii huweza kuwa kuchaguliwa kwa ajili ya kuingia ngazi nyingine ya elimu au darasa
lingine. Motisha ni muhimu sana katika kukuza ufaulu wa wanafunzi.
11)Upangaji wa Ufundishaji Ujao
Baada ya hatua zote, hatua ya mwisho kabisa katika kutafsiri muhtasari kwenye vitendo ni upangaji
wa ufundishaji ujao. Katika hatua hii mwalimu na shule hufanya tathmini ya zoezi zima la ufundishaji
lilivyokuwa, matokeo ya tathmini yalivyokuwa na sababu za matokeo mazuri au mabaya
yaliyopatikana. Walimu na shule wanapaswa kuyajadili matokeo yaliyotolewa ili kubaini ikiwa kuna
udhaifu wowote. Hilo linaweza pia kuwasaidia kufahamu udhaifu uliobainika umetokana na wanafunzi
wenyewe, mazingira ya kujifunzia, walimu, shule, jamii au sababu nyingineyo. Baada ya sababu
kujulikana, walimu wanapaswa kuandaa mikakati ya kutatua tatizo hilo ili kuhakikisha hali hiyo
haijirudii siku zijazo. Tathmini hii itamsaidia mwalimu kuboresha zana za kufundishia, mbinu za
kufundishia, vitabu na ufundishaji kwa ujumla ili aweze kutoa matokeo bora zaidi katika mwaka
unaofuata. Kwa bahati mbaya sana, kuna shule nyingi ambazo haziweki kipaumbele katika hatua hii.
Shule kama hizo itakuwa vigumu kujinasua kutoka katika ufaulu mdogo waupatao. Shule hazina budi
kukaa na walimu na kuyajadili matokeo na kujua namna ya kufanya. Baada ya hatua hii, mzunguko
150
unaanza tena kwa kurudi katika hatua ya kwanza ya kufanya mapitio ya makusudi ya ufundishaji.
Mapitio ya sasa yatatilia maanani sababu za kufeli na kufaulu zilizobainika kutokana na matokeo ya
tathmini yaliyotolewa.
HITIMISHO KUHUSU HATUA ZA KUTAFSIRI SILABASI KWENYE VITENDO
Hatua hizi ni muhimu sana kwa mwalimu anayetaka kufundisha si tu ushairi wa Kiswahili bali
pia lugha ya Kiswahili kwa ujumla. Hatua hizi hufuatwa pia na walimu wanaofundisha masomo
mengineyo. Hatua hizi zinapaswa kufuatwa na mwalimu anayeanza kufundisha darasa husika kwa mara
ya kwanza. Kwenye baadhi ya shule, mwalimu hupangiwa darasa husika na hulifundisha miaka nenda
miaka rudi. Kwa mfano, mwalimu huweza kupangiwa kufundisha ushairi wa Kiswahili kidato cha nne;
kinachobadilika ni wanafunzi tu wa kidato cha nne ila mwalimu wa ushairi huwa ni yuleyule miaka
yote. Kwa mwalimu wa aina hiyo aliyekwisha kufundisha darasa husika, hatua nyingi huweza kurukwa.
Kwa mwalimu huyo, hakutakuwa na sababu ya kupitia upya makusudi ya kufundisha kwani alishafanya
hivyo mwaka uliopita. Aidha, hatakuwa na sababu ya kuchagua upya vitabu vya kufundishia au
kuandaa mpangokazi wa kufundishia kwani alishafanya mwaka uliopita. Hata hivyo, ni muhimu kwa
mwalimu kujiridhisha ikiwa kweli hakuna haja ya kupitia mojawapo ya hatua hizi hata kama mwalimu
huyo alifundisha somo hilo katika darasa hilohilo mwaka uliopita. Hii ni kwa sababu vitabu vipya
hutungwa kila siku na hivyo kuwa na haja ya kuchagua upya vitabu vya kufundishia ambavyo ni vya
kisasa zaidi na kuachana na baadhi ya vya zamani. Pia, mbinu za ufundishaji hubadilikabadilika
kutokana na tafiti mbalimbali zilizofanywa. Mabadiliko haya huweza kuathiri hata muundo wa azimio
la kazi na andalio la somo. Kwa mfano, nchini Tanzania hapo awali, hatua za ufundishaji zilikuwa tatu:
utangulizi wa somo, utoaji wa somo na hitimisho la somo lakini kutokana na tafiti mbalimbali
ikabainika kuwa kuna haja ya kuingiza vipengele vya matumizi na kukazia maarifa na hivyo Serikali
ikaanzisha kile kilichokuja kuitwa muhamo wa ruwaza, yaani kuhama kutoka kwenye muundo wa
zamani wa andalio la somo lenye sehemu tatu hadi muundo mpya wenye sehemu tano.
Vilevile, mapitio haya ni muhimu kwani tathmini iliyofanywa wakati wa hatua ya upangaji wa
ufundishaji ujao inaweza kubainisha kuwa mpangilio wa mada haukuwa mzuri na ndiyo maana
wanafunzi hawakufaulu kwa kiwango kizuri. Aidha, kwa kuwa wanafunzi wanaokuja ni wapya na
wana matamanio tofauti na wale waliopita, mambo mengi huenda yakahitaji kubadilishwa na hivyo
kuwa na haja ya kupitia upya hatua zote hizi.
Jambo la mwisho, ambalo ni muhimu kusema hapa ni kwamba hatua hizi ni muhimu kufuatwa
kwa mwalimu anayeanza na wanafunzi tangu mwanzo wa kuanza darasa husika. Kama mwalimu
anakabidhiwa darasa katikati ya muhula hataweza kupitia hatua hizi. Mwalimu huweza kupewa darasa
katikati ya muhula kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuanza kazi kipindi hicho,
mwalimu wa somo kufariki, kuhama au kuacha kazi na sababu nyinginezo. Mwalimu anapokabidhiwa
darasa katikati ya muhula ni imani yetu kuwa mwalimu anayepokelewa alikwisha fuata hatua zote hizo
hapo awali. Hivyo, mwalimu mpokeaji atapaswa kurithi azimio la kazi la mwalimu anayepokelewa.
Anaweza kurithi pia vitabu vilivyokuwa vinatumiwa na mwalimu anayepokelewa kama
vinavyobainishwa kwenye azimio la kazi. Hata hivyo, mwalimu mpya kuanza kufundisha katikati ya
muhula kuna madhara makubwa kwa wanafunzi. Hii inatokana na ukweli kuwa mwalimu husika
hakuhusika kupanga zoezi la ufundishaji na hivyo inakuwa vigumu kufuata mipango ya mtu mwingine,
anaweza akawa hajavisoma vitabu vilivyochaguliwa kutumiwa na mwalimu aliyepokelewa na pia
wanafunzi hupata shida kuzoea mbinu mpya za ufundishaji kutoka kwa mwalimu mpya. Inashauriwa
hapa kuwa, kadri inavyowezekana, walimu wazuiliwe kuliacha darasa katikati ya muhula ili kukwepa
uwezekano wa haja ya kubadilisha mwalimu.
151
SEHEMU YA PILI:
DIWANI YA MEA
152
LIPAKA
Nyauu! Nyauu! Utasikia linalia
Usilijali, usilihangaikie hata likilia
Ni liongo, halifai, huhitaji kulivumilia
Paka yake adabu, kaiweka mkiani
Lipaka hili, lisikupe presha moyoni.
Utu na nidhamu limepungukiwa
Fadhila lifadhili lakini bado litakwibia
Utunze mboga mahala pema likiipata linabwia
Kwa hakika udokozi ndiyo yake tabia
Lipaka mlijue, ni chanzo cha umaskini.
Tazama dharau na masimango yake
Ye’ kuishi ndani awadharau wenzake
Jirani zake mbwa na ng’ombe wakilala nje
Lenyewe lawazomea na kuwaona vibwete
Hili lipaka jamani, liache dharau.
Yote hayamsujudu huyu paka mikasa
Uaminifu, utiifu, wema kwake ni tasa
Ufisadi, wizi, udokozi, kwake layatakasa
Lafuzu zote na sasa laturudisha nyuma kimaisha
Lipaka hili wandugu, haya halioni.
Busara zake ni za kutengeneza
Hazina tija bali ni jeneza
Zinachosha kweli, vema kulipuuza
Panya litakula, samaki litakwibia ukihisi chunguza
Lipaka hili lipige bunduki likafie mbali.
HADITHI
Navuta kiti na meza. Nakaa
Japo hamjanikubalia lakini ntakaa
Hata kwa nguvu ilimradi nimekaa
Kaeni kitako kimakundi na kwa pamoja
Hodi naipiga kila mmoja malangoni pake
Napenda kuileta hadithi hii isiyo ya makeke
Inamhusu yeye, wao na watu wake
Hii ni kwa wote.Waume na wake
Yasikieni mambo haya kwa dhati yote.
Namkumbuka bwana huyu
Kwa zake busara mithili ya mkuyu
Alizozaliwa nazo chini ya mbuyu
Na kupelekea kufahamika kama Kibuyu
Aliipenda sana nchi yake
Ni mzalendo wa kweli
Sikieni sifa za maisha yake
Aliichukia dhambi ya hongo kwa maisha yake
Tangu awali hadi tamati ya uongozi wake
153
Mafisadi kuringa walikoma enzi zake
Walikoma hadi wakaacha makeke
Zavutia sana habari za baba Kibuyu
Zake falsafa, zilivuka ukomo wetu
Aliiona nchi ng’ambo ya mawazo yetu
Kwa kututaka tuwe wazalendo wa taifa letu
Kwa wote waume kwa wake wajifunge mikanda
Tayari kwa vita ya kikamanda.
Taifa kulipigania na kulilinda
Dhidi ya magonjwa, umaskini na ujinga
Ambao ni maadui sugu wa taifa letu changa
Kwa pamoja mapambano walishiriki
Bila hofu wala hamaki
Ilimradi taifa halizimiki
Halifi wala kupotea bila mantiki
Wazawa, wazalendo wakaitikia mikikimikiki
Ya kuwaondoa wasaliti, mafisadi na wazandiki.
Namnukuu alivyosema.“Yatubidi kuukata mbuyu hata kama shetani ni damu na nyama yetu”
Unajua alimaanisha nini?
Alimaanisha hivi fahamu
Sikilizeni kwa zenu timamu
Iwapo ndugu awaye yeye ana hila za kutia sumu
Amani na mustakabali wa taifa si timamu
Hivyo sheria ya nchi ipite katikati ya damu
Iondoe mizizi ya watu hao sumu
Tusikumbatiane sababu sote tuna damu
Taifa likiungua wapi utaitwa binadamu?
Fikara zake ni zaidi za wanadamu.
Ni wajibu wetu kumkumbuka
Shujaa Kibuyu kwa zake hulka
Zilizo amilifu zikachochea kukurika
Taifa likasimama na kuimarika
Uzembe, uongo na ubabe ukatoweka
Tuzienzi jitihada zake si kwa dhihaka.
Yaniuma upepo unapovuma
Taifa liso mhimili sasa limechuchumaa
Maovu yaendeleayo sasa hakika nitasema
Taifa linaumia maumivu yazidi komaa
Wenye dhamana, wasaliti dhamana
Urithi mkuu wa taifa wautia dhahama
Wengi wabakia kurarua ngozi ya mnyama
Wachache wajifungia shingoni nyama
Uchungu huu sasa basi!!
154
MWATULINDA? MWATUUA?
I
Si mnijibu swali hilo…………Alaaaha!
Nawauliza nyie Mabwana Magwanda!
Mnaona aibu kwa vile mnajua uonevu wenu?
Maumivu mwatuachia, familia zetu zaparaganyika
Hivi majuzi mlimpiga hadi kifo rafiki yangu, kosa hatulijui.
II
Haki ya kuishi
Ni haki ya kila kiumbe chenye damu
Kuwa na familia ni msingi wa maendeleo ya kijamii
Furaha ya familia ni uwepo wa ndugu wote ndani yake
Lakini mnavotuua familia hizi mnaziganga vipi na maumivu?
III
Haki yetu kuihoji serikali inapokosea
Haki yetu kuiwajibisha serikali inapobabatiza ukweli
Haki yetu kuandamana kutoa malalamiko yetu kikatiba
Tukifanya hayo mnatujia juu
Na mabomu mazito ya kutishia amani
Tukiomba ushirikiano wenu mnakuwa kizuizi cha hitaji letu
Ngoja niulize, Bwana Magwanda hivi nyie wa akina nani?
IV
Ngoja niwageukie, mna maisha duni kama yetu
Tukipigania ahueni yetu mnatupiga
Mna mishara mibovu twajua
Twakusanya nguvu kuhoji kwa ajili yenu
Mwatusukasuka kwa mabomu na virungu
Mna watoto wenu wanasoma shule hizi za pipijojo
Hawajui kusoma wala kuandika insha, walimu wapo tu
Tukifanya mageuzi ya hali hizo mwatufyatulia mabomu
Hivi nyie ni wa akina nani?
Niambieni nami nijue.
…………TE.
Si haba ila yameshasemwa yote
Hadharani na pengine pote
Wachungaji, maaskofu na mashekhe wote
Si wao tu hata wanasiasa wote
Wamejaribu na watajaribu kote
Kupambana ili kuondoa adha hii kokote
UKIMWI umesambaa pande zote
Hakika ni janga letu sote
Tujihadhari nao na tutapona wote
Hizi ni dalili zake zote
Zitupasazo kuzijua sote
Kuharisha, kutapika kwa mara zote
Kukondeana na kupukutika nywele zote
Baridi kutawala kwa nyakati zote
Si hizo tu nyingine mzitafute
155
Hamu huisha hata ya kumeza mate
Ugonjwa huu si wa nani,ni wetu sote
Utatuua na kututesa sote
Tukiendekeza michezo hatari yote.
Umang’aa na ukahaba upingwe kote
Mahaba nje ya ndoa yatengwe na wote
Heshima na uadilifu uhimizwe kwa wote
Wanandoa, wapenzi heshimianeni pote
Hiyo ndo ngao muishikeni nyote
Vimini na matiti wazi tuzikemee sote
Milegezo na ulevi ni vyanzo vyake vyote
Tukicheka tutateketea sote
Ujane na uyatima vitatawala pote
Si kwa matajiri tu bali kwa watu wote
Masikini na vigogo nao wamo wote
Ni waathirika na tusiaminiane sote
Jiamini wewe kwanza, usimuane yeyote
Tukifanya hayo tutapona siku zote
Lakini yasisahulike na mengine yote
Sindano na mkasi ni hatari zote
Zina ncha kali tukizichangia sote
Ngono zembe iogopwe na watu wote
Na biashara ya uroda itokomezwe kote
Sheria na amri za Mungu tuzikamate zote
Na hizo ndizo hazina za kutuokoa siku zote
Te!Te!TeTe!
Kicheko hiki msikilete
Kimejaa haramu kama ugoro wa mate
Kitatuponza tukikatae sote
Usaliti unapokithiri ni athari kwetu sote
Uzembe, ubadhilifu na uongo ni kansa kwa wote
Wapendeao maendeleo na sio mateteWanasiasa hawa uchwara si budi kuwatema wote
Tuwatemee makohozi wala si mate
Watatuponza na zao zile Disloyalty
Utasikia wakijiita ni watu wa watu wote
Wa matajiri, masikini na wa wengine wote
Lakini cha ajabu hatamu imeenda fungate
Msiba umekuwa mzito kwa makabwela wale wote
Wachangishwa na kukamuliwa kile chao chote
Kidogo wakipatacho kwa mioyo yao yote
Harusi wagharamikia maakuli yao ni mate
Minofu na Michele ya taifa waifungia matete
Ulinzi wauimarisha wazamiaji wasijivute
Kuja kula malipo ya jasho lao lote
Virungu watachezeshewa hadi wakome wote
Shutuma watatupiwa na hukumu iwafuate
Eti kakosa ni kauasi dhidi ya mtawala wa yote
Aaa!Usaliti sasa basi na udhalimu wake wote
156
Miaka mitano nayo ipite
Usaliti wao wapanga eti waufute
Kwa kurudi nyuma na msemate
Wajitetea na kuulaani uchumi kwa yale yote
Eti ndio chanzo cha mambo hayo yote
Kauli zao ni za uoga na zinatishia uhai wa wote
Walowapa dhamana ya miaka mitano wajikitekite
Madarakani wakiwa na dhamira ya awaye yeyote
Sasa tuseme basi juu ya huu umbutete
Na kadhia hii ya nipe nipite
Sasa tunaangalia vipi tumeremete
Tunataka taifa jipya la kwetu sisi sote
La mwalimu kufaidi uchu wa yake mate
La daktari kufanya kazi kwa uledi wake wote
La mkulima kupanda mahindi avune shamba lote
La wanafunzi kusemea jamii msipite
Nje ya ubia wa walalahoi wote
Waliojikota nje ili kuwapa hii mpite
Hili ndilo taifa la ndoto zetu sote
MADHILA YAKO
Magomeni Mwananyamala Tandika nakufuata
Kwa kuikwepa jakala nyumbani nitakukuta
Kabla hata hujalala ili tukaile bata
Asilani naumia na haya madhila yako.
Nakiri nilikusihi, hima ufike nyumbani
Mapema asubuhi ungenikuta uani
Hukuja hata kunisabahi nikavunjika moyoni
Abadani nakusihi jaribu pengine pakufaapo.
Sikia! Sikia mpenzi sikia! Tena sikia
Shida kichwa cha panzi foleni zilinizuia
Sikukusudia habari hizi hata pia kuzinuia
Asilani naumia na haya madhila yako.
Usijitetee hukunijali ulinifanyia hila
Ni heri ungenambia, foleni ipo Mwananyamala?
Ulipita kando ya njia, ukaondoka na vibwambala
Mi nakusibiria, kumbe na mwengine mwagalagala
Asilani nakusihi jaribu pengine pakufaapo.
Umeniacha mimi umempa moyo Kajale
Yeye si kama mimi wasema hana machepele
Mmekula yamini mimi niondoke nikalale
Ulonitendea mimi madhila yako si ya pole
Asilani naumia na haya madhila yako.
Jiheshimu nikuenzi kama wangu wa zamani
Sina tena ncha ya mapenzi kuwa nawe ni msibani
157
Kajale ni wangu mtetezi popote hata vitani
Tafadhari tupe uwazi na huyu wangu mwandani
Asilani nakusihi jaribu pengine pakufaapo.
KWAHERINI
Baba!
Mwanao nakereketwa moyoni
Najua nimevuruga maisha yangu
Lakini uyafanyayo si jema ndani ya taifa
Aibu nimekutia nawe ni rais unapiga kelele
Asubuhi, mchana na usiku
UKIMWI unaua.Jihadhari
Mwanao nimelikwaa gonjwa hilo.
Mi pia ni raia ya nini kunificha ughaibuni?
Kunificha haipaki rangi ukweli huu
Ni aibu kwako na kwa taifa
Lakini usifanye hivyo.
Kifo chaningoja
Kwaheri baba yangu!
Kwaheri mama yangu!
Kwaheri taifa langu!
Kwaheri wanazuoni!
Kwaherini mashekhe na makasisi
Dunia naiacha.
Jamani msiniige mwenzenu
Nilofanya ni tokeo la mimi kuwa kitandani
Mtoko uso pungua na lundo la wasichana
Mapenzi dhaifu bila kinga
Ubabe na dharau zimeniponza
Napandisha kenchi bila mjenzi
Nahara natapika hadi uchu wote
Msijione mkadhani
Gonjwa ni letu sote
La kwenu mbavu za mbwa
La mabosi kizani na vitambi
La kwangu mimi mwana wa Rais
Nawaageni Kwaheri
Tabia isipobadilika hamponi.
Baba najua ntakufa hivi punde
Lakini
Yasikie na ujue mtandao ulivyokuwa
Thabita ni mpenzi wangu
Aliyekuwa kimada wa Mheshimiwa Macheche
Nyuma ya saluni ana kabuzi kake kanafunzi
Usiku Mheshimiwa Macheche hutoka na Zaina
Zaina yasemekana ni kipozeo cha dereva lori
Liendalo nje ya nchi mara mbili
Kwa wiki.
Likifika mpakani dereva ana hawala yake
Ajishughulishaye na kuuza vyakula mpakani
158
Huko ana pedeshee limfanyialo
Mipango ya kuvusha na kuingiza chakula kinyemela
Na baada ya kazi ni dawa. Kazi na dawa
Pedeshee anajishindia gesti naye.
Balaa
Ni kwa Waziri wa Afya na Uhai
Mmiliki wa Kasino nzito jijini
Naye chini ya sakafu habari zaruka
Anakata kiu kwa Zaina.
Mheshimiwa Macheche kuona hayo
Si kagonga hodi kwa mpinzani wake
Kimahaba atoka na Bi Zeituni Masaka
Mke wa Waziri wa Afya na Uhai
Yule mchungaji mseja unamjua
Si naye anamega kwa waziri
Ziara zikianza nyumbani huibukia
Maombezi ndo hoja kumbe
Nyuma anakula asali.
Mtandao ukakua
Hata Dokta Shija alikula kwa Zaina
Siku kadhaa baada ya kumtoa ujauzito
Profesa Kisu si akamvizia Weisiko
Yule binti wa Waziri wa Ujenzi
Miss Chuo Kikuu
Weisiko ni kisu kuliko Profesa Kisu
Nyuma alishadata na pedeshee la mji
Ambaye naye alishafuta jasho kwa Thabita.
Mama!
Nalia siwezi malizia.
Rai yangu baba ni moja
Tangaza hadharani tangu sasa
Nimeukwaa UKIMWI na wote wajue
Usiogope aibu.Aibu ni nguvu ikipita
Usiposema
Orodha hiyo utaificha vipi?
Usiwahukumu bila sheria watakaonong’ona
Mwana wa Rais afariki kwa UKIMWI
Usiwatupe gerezani bali wasifu kwa kuhoji
Gonjwa hili si la wa maskini tu
Si la mapeshee tu
Si la walimu tu
Si la wao tu bali hata mimi
Ni letu sote
Vunja ukimya na sema jambo
Nami ntapumzika kwa amani.
Kwaherini walenga!
Kwaherini wenzangu!
Kwaheri nchi yangu!
159
TANGU ATOKE SAFARI
Mchana homu nimekaa, nikiwa sina hili na lile
Kwa mbali nikasikia simu inaita, furaha ikanijaa kedekede
Mpenzi Nana kuja Daa, kuanzia saa moja mbele
Kan’ita n’ende kumfata, kwa haraka ilioje
Ukweli nilimpenda, hata ninyi muelewe.
Sasa ni mwaka umepita, mpenzi amekuwa mbogo
Nikisema neno pata, ye analeta songombingo
Nakuuliza hivi ni wazimu, mbona hukuwa hivi huko?
Au kuna mme mwenzangu, nieleze ukweli wako
Ukweli nilimpenda, hata ninyi muelewe.
Nahisi nilipenda fuvu, yangu maisha ni udongo
Kuzikwa na sanda langu, wakati mbele ni pigo
Likaushalo damu yangu, nikaja kufa kwa pengo
Kwa hatia ya uchungu, ya kubariki hiki kigongo
Ukweli nilimpenda,hata ninyi muelewe.
Mpenzi umebadilika, tangu utoke safari
Dunia inanicheka, mapenzi yawa lamri
Chini nimeterereka, maumivu yakithiri
Naomi umesimika, kisu bila adhiri
Kiukweli nilikupenda, hata wewe uelewe
Ni heri niwe kapela kuliko huu msumari
Unanigongea bila kuangalia yote mazuri
Nilichimba hata jalala, ili we upate nawe hariri
Nikamkopa hadi Kalala mtaani naitwa taperi
Ukweli nilikupenda, tamaa usaliti vimetawala.
Nenda nenda nakutakia salama mbeleni
Daima nilikupenda weye ukatia kisarani
Umenitenda ukanitenda, sasa nakutupa mgongoni
Nitakiganga kidonda, ili niwe salama salimini
Ukweli nilikupenda, sasa nabwaga manyanga.
MASKINI AFRIKA!!
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio cha ukabila nchini Rwanda
Ya Watutsi na Wahutu mauaji ya Kimbari
Maskini Afrika! Ndugu wakachinjana wao kwa wao.
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu magonjwa ya kutisha Kusini Jangwa la Sahara
UKIMWI, Ebola, Saratani, Maleria na Kifua kikuu
Maskini Afrika! Ni lini tiba zitatosha, magonjwa yasishamiri
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu udini Somalia na Nigeria
Uislamu na Ukristo,vinanyonya amani ya mataifa hayo
Maskini Afrika! Amani yako inadidimizwa kila kukicha.
160
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu maasi ndani ya mataifa
RUF, LRA, M23, Boko Haram na Al-Shabab.
Maskini Afrika! Raia wasio na hatia dhamana yao i’ wapi?
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu ukiukwaji wa demokrasia ya kweli
Ung’ang’anizi wa madaraka na tawala za kimabavu
Maskini Afrika! Mizizi ya udikteta yazidi shamiri.
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu mabadiliko ya sayanasi na teknolojia
Uzinduzi na utengenezaji silaha za kinyuklia
Silaha, Ulaya zizalishwe, yanini Afrika ulingo wa vita?!
Maskini Afrika! Vijana wadogo nao waingizwa vitani.
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu ukiukwaji wa haki za binadamu
Mauji ya Albino, vikongwe na vichanga visivyo na hatia
Maskini Afrika! Imani potofu zachafua taswira ya uzuri wako.
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu majanga ya asili ndani ya mataifa
Mafuriko,baa la njaa na magonjwa ka Ebola.
Maskini Afrika! Wakazi wako walia na kuwa wakimbizi.
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu utitiri wa wakimbizi kila pembe
Mutabila kila mmahali hadi Bonde la Ufa
Maskini Afrika! Sera za uongo majukwaani na ubabe wa wanasiasa pelekeo la ukimbizi.
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu unyonyaji wa rasilimali ya mataifa yetu
Dhahabu, Almasi, Fedha, pembe za ndovu na ardhi ya rutuba
Maskini Afrika! Wazawa wanabakia na kitu gani kujivunia?.
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu sera sirini za uwekezaji
Wazawa wavuurumshwa kupisha uwekezaji, tija hawaioni
Huduma zadorora, malighafi inachotwa, makombo yabakia nchini.
Maskini Afrika! Twajivunia nini kuwa na keki inayoliwa na wageni?
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu uingiliwaji wa kinguvu wa dola za Magharibi
Akina Komesa kimya mwanyamaza,
Uingizaji majeshi hamuhoji,wahanga wananyonywa.
Maskini Afrika! Hujiulizi mbona wao hawakuiti uwaingilie?
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu rushwa, ufisadi na ubadhirifu umeota miguu
Huduma zimepooza hadi chochote kikutoke mfukoni
Wenye nacho wafaidi, wa majalala huzuni tupu maishani
Walalahai uhondo mdomoni, walalahoi miungurumo tumboni
161
Maskini Afrika! Matabaka ya kijamii yazidi kushamiri
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu matumizi ya siasa chafu
Zimetopea chuki, vinyongo, masimango na hongo
Ashindaye si chaguo la wengi
Aliyepaswa kanunuliwa kwa milungula
Wajaleo, waenda leo kutwa kituoni kupiga kura
Huzuni imewaingia kila kukicha
Maskini Afrika! Huruma kwanza kwa mpiga kura wako
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu manyanyaso ya kijinsia
Mikong’oto mizito, mahaba ya nguvu wabinti kuwafanyia
Ukeketaji, maumivu yasoisha mwilini kuwaachia
Msomi wa kike tasa, wa kiume yake ni zalishi
Maskini Afrika! Utu wako umeutundika wapi?
Kilio! Kilio! Kilio barani Afrika!
Kilio chetu utitiri wa magenge na vijiwe vya vijana
Kazi wamekosa, matunda ya elimu yao yaozea jalalani
Bangi wavuta, madawa ya kulevya msimari mtindio’ ubongo
Maskini Afrika! Taifa la kesho linakufa.
KISABENGO
Jogoo hajawika asubuhi
Nyumba ya majirani waibukia
Kwako kumenuna njaa kali
Unaporoja uongo asubuhiasubuhi
Hicho ni kisabengo!
Umeniona na msichana
Koridoni twazungumza
Humjui ni nani na twaongea nini
Unasambaza kwa mwandani wangu
Umefuma koridoni na hawala
Hicho ni kisabengo!
Umekuja kuomba kura yangu
Nakuchagua hutimizi uloniahidi
Unasingizia mtikisiko wa uchumi
Lakini kwako nyumbani na familia yako
Mtikisiko unaouhubiri hakuna!
Hicho ni kisabengo! Adilika.
Unamdharau mama yako
Sababu nawe una matiti
Sababu nawe una sauti nzitonzito
Unamtangaza barabarani kwa mabaya
Hukumbuki alipokutoa
Hicho ni kisabengo! Badilika.
Unawaunganisha watu
162
Mnalenga kuhatarisha amani ya wengi
Mnajua nini thamani ya amani ilivyo
Mnajitia kiburi mnatimiza njama yenu
Usalama unakufa machafuko yanazaliwa
Hicho ni kisabengo! Hatari kinaua.
CHAKUBIMBI
Chakubimbi jamaa mkimuona muogope
Ana meno manne yanauma kotekote
Macho yake tochi mithili ya mtoto wa kenge
Msimualike hata bure kwenye lenu genge
Chakubimbi muone na kumsikia kwa bomba tu.
Muyasemayo yote jueni atayaanzishia kijiwe
Sasa nikumsusia kijiwe hadi akome mwenyewe
Asishiriki hata kukunja nne. Hadi akielewe
Mwaka huu siyo wake tumeijua siriwe
Siri zetu ni zetu na zake akawalishie mwewe
Chakubimbi tumekuzibia hadi ukome kuringa
Kama mkizembea niyasemayo, mtaumia
Sikieni chakubimbi alichonifanyia
Nilimtonya kistaraabu ya kuwa nahamia
Mtaa wa pili toka ule wa Makororo Nehemia
Alaalaa!Si kaanza udaku kusambazia
Mtaani, majirani, mwenye nyumba na kule napohamia
Nyumba nayokaa nikatimuliwa kabla sijajipangia kuhamia
Chakubimbi jamani huna neno moyoni.
Chakubimbi kumbuka urafiki wetu
Haukuchipuka hivihivi bali kwa utatu
Nilikuheshimu na kukujali kama mtu
Wewe si mimi lakini mbona huna utu?
Tabia yako kuniunguzia utambi kwa bosi wetu,
Kazi nimetemwa sasa naishi kwa matumaini tu
Jamani Chakubimbi jua dunia ni mviringo kuna kesho pia.
Hivi majuzi uliyonifanyia nakusamehe bure
Ulinivurugia penzi langu kwa yule wangu wa milele
Ulimpumbaza kwa uongo na chako kijino pembe
Ulimtongoza ukanikandia eti mie nashika pembe
Njiwa wangu ukamrusha na kuniacha mi pekee
Chakumbi nakujua una meno manne unauma kotekote!
MCHEZO WA MANENO
Ni mchezo mzuri kwa vijana na wazee
Namaanisha kwa mtu wa asili-damu pekee
Mchezo huu ni wangu utoto kama kinda pekee
Basi natuuimbe na kucheza wote
Katika maisha haya
Mganga wa jadi anaitwa Kalumanzila
163
La………..Lala salama
Ma……….Mama mzazi
Zi…………Zizi la ng’ombe
Mbe……...Mbele ya nyumba
Mba………Mbali na wewe
We……….Wembe wa kucha
Cha……….Chakula kitamu
Mu…………Mungu mkubwa
Bwa……….Bwawa la samaki
Ki………….Kingi Majuto
To…………Tone la maji
Ji……………Jitu la kale
Le…………Lenye mandevu
Vu…………Vumbua dhahabu
Bu…………Bubu hasemi
Mi…………Mimi mdogo
Go…………Gogo la Mti
Ti………….Tina na Mjuba
Ba………….Baba mkali
Li……….....Taa ya umeme
Me…………Meli imezama
Ma………...Maji mabaya
Ya…………Yai la kuku
Ku…………Kuku mweusi
Si………….Simu inalia
A………….Alimwiba bata
Ta………..Tanzania nchi yangu
Ngu………Ngumi ya Onyango
Ngo……...Ngome ya Yesu
Su………Sungura Mjanja
Nja……..Njaa inauma
Ma……..Mama mzazi
Zi……….Zizi la ng’ombe
Mbe……Mbele ya nyumba
Mba…… Mbali na wewe
We………Wembe wa kucha
Cha……..Chakula kitamu
Mu………Mungu mkubwa
Bwa……..Bwawa la samaki
Ki……….Kiswahili lugha yangu
Najitukuza kujifunza hazina ya lugha hii
Mchezo huu hushitua akili na hata bidii
Kufikiria kwa undani si hayo hata kutalii
Kunako fikra na zile zinazoitwa mvii
Nawasihi watoto rudisheni nyumbani mchezo huu
BARUA JUKWAANI
Pazia nalifungua, jukwaani najivinjali
Kwa manjonjo, madaha na hata sabili
Kuziturufu na hata kuzisoma barua zenu amali
Zichocheazo lakini zichomazo moyo na akili
Basi nami ntazisasambua jukwaani nikitalii
164
Yako barua ni wewe Mashauri Mashishanga
Wa sanduku la barua 111 Mjini Shinyanga
Unasema unataka kupasua jipu hata kwa upanga
Ili ubakie huru na ahueni ije Mjini Shinyanga
Gadhabu yako ni juu ya tabia chafu iliyojivika Shinyanga
Wanaume kupotoka na kufanya ushoga
Kuoa na kuoana wao kwa wao bila uoga
Mji kuuchafua hata aibu kwa wahenga na vitoto vichanga
Japo ni makinda lakini waweza ng’amua huu ujinga
Inakera na kuchukiza nafsi bila kupinga
Unazidi kuhoji juu ya uhalali wa Mji wa Shinyanga
Kuvaa miwani myeusi wakati mji unadokolewa na Kipanga
Unahitimisha kwa kuomba upenyo wa kuvaa gwanda
La ujasiri na uamuzi mgumu ili kuwatilia ngumu na inda
Tabia hii kuimaliza na kuirudisha pahala pake Shinyanga
Kusema hayo nami na kushusha kwa madaha yote
Jukwaani ili ukapumzike na kuujenga upya mjini wenu wote
Nakushukuru kwa barua yako il’ojaa busara potepote
Ni wewe Salome Tainyo wa Temeke, Daresalaama
Sanduku lako la barua ni 099 Daresalaama
Waomba kukwea taratibu vidato ili upande salama
Jukwaani na kuanza kurusha zako hasira na lawama
Juu ya viongozi, wasimamizi na wakazi wa jiji la Daresalaama
Kwa kuzembea na hata kudharua usafi wa jiji la Daresalaama
Unahoji kwa tashtiti iwapo maana halisi ya “Darisalaama
Ni mji wa bandari salama?”
Kama ni hivyo mbona ni aibu na chukizo kwa usalama
Wa raia, wageni na hata wawekazaji wa Daresalaama
Niseme, huenda natoa tu lawama zisizo na mashiko
Lakini zungukia mitaa yote muone vituko
Huko Kariakoo, Tandika, Magomeni, Boko na hata Keko
Kunatisha mithili ya msuguano ulojaa sokomoko
Uchafu, uharibufu na hata magonjwa yamejaa huko
Daresalaama si pepo salama tena ila ni jehanamu ya Kiko
Inacheza mchezo wa uongo na wavutaji wa hiyo Kiko
Wakazi wamefutiwa hisa ya afya njema isiyo na masumbuko
Wanaishi kwa“Angalau ya leo ipite, kesho itakuaje huko?”
Unahitimisha kwa kuzihoji mamlaka husika
“Je wamesau kitu wanachotakiwa kufanya ili kufikika
Kwa maendeleo ya afya ya watu na hata kuimarika
Kwa Mji wa Darisalaama?”
Kusema hayo unaomba nikushushe jukwaani kwa makeke
Nami bila ajizi nakusindikiza hadi chini kwa upweke
Kuifunga barua yako ndo mwanzo wa kufungua nyenzake
Kilio chako kitasikilizwa kote Ilala, kinondoni na pia Temeke
Afya, mazingira safi na uadilifu ni lazima kwa wakazi wake
Viongozi, watendaji na wasimamizi ndivyo inapaswa kieleweke
Barua jukwaani inazidi pasua anga na sasa ni wanawake
We’ hutaji jina na wapi ulipo
Lakini wanivuta shati kwa upepo
165
Unashusha ghadhabu yako kwa mila iliyopo
Hususani barani Afrika huko uishipo
Unasema tabia ya koo kuvunja utu wa mwanamke
Ni unyanyasaji na dhuluma kwa mwanamke
Unahoji mke akiolewa, anaolewa na mume na ndugu zake?
Kwanini mume akifa ndugu purukushani kwa mke wake
Ung’ang’anizi wa mali na hata mke wake
Mwataka kumrithi kikao kikali kumuwekea
Watoto hamkumbuki, mali, mke tu mwaongelea
Unazidi kurusha dongo lako kama tsunami
Unauliza huo ni utu au ufisadi hata wa ndimi
Kaka atafute, afapo chake chenu
Kaka afanye kazi uroho wa mali kwenu
Una hitimisha kwa kusema
Mila hizo zifungwe kwenye dema
Wenye tabia’zo wapelekwe pasipo pema.
Nafunga barua yako nakushusha kwa heshima.
DUNIA KAMBI
Ni kambi ya mkusanyiko wa kila aina
Imekusanya takataka na maua ya kila aina
Tunakaa humo sote kama wakimbizi
Twazikimbia shida lakini kambini napo zipo
Hakika dunia kambi vaa gwanda tayari.
Kambi ya dunia imekusanya wengi
Tunaishi nao ndani ya kambi
Wezi wa mifugo kijijini
Wafitini, wavunja nyumba za watu
Waongo ukweli kwao ni sumu
Wasaliti madhara hawayajui
Dunia kambi vaa shika bunduki mkononi.
Ndani ya kambi kuna mengi
Kuchomeana utambi kazi wafukuzwa
Kusalitiana ndoa inavunjika
Kuasiana taifa linayumba
Kuoneana wasio na hatia waumia
Kunyonyana ukoloni mpya wa Kiafrika
Dunia kambi vaa gwanda tayari.
Hadi sasa kambi ya dunia
Haina kamanda anayetulinda
Kama yupo basi ni dhaifu mithili ya uyoga
Ugomvi unatawala kati yetu hatuongei
Chuki twachukiana hakemei
Uasi twaasiana aunga mkono
Kambi hii ya dunia
Kaa chonjo!
Fumbua macho usijiliwe kekundu!
NG’OMBE MMEMMALIZA
Huruma mmeipeleka likizo nyie wazandiki
166
Mbona mshipa wa aibu mmeuziba kwa matope
Tuliwaamini lakini mmeimeza kwa tindikali imani yetu
Ng’ombe wetu alikuwa mnene na mwenye afya tele
Yako wapi maziwa na nyama zake?
Mmemmaliza halafu mwatuletea makombo!
Hamfai hata bure.
Kila aliyemtegemea ng’ombe huyu sasa analia
Ng’ombe amekamuliwa bila huruma
Usaha wa maumivu yasiyoisha yazidi kumtoka
Yamtoka na kumuachia vidonda visivyopona
Sasa watoto wamegeuka kumlamba vidonda ili apone
Wanawake wamegeuka kuwa waganga wa jadi
Wanalia usiku kucha dawa haipatikani, ngombe anaumia
Kwa hali hii hamfai tena kumfuga ng’ombe wetu
Hivi ndivyo mlivyokuja mkihubiri jukwaani.
Kwa sauti ya ushawishi kisiasa, mkapaza mkisema
“Niaminini mimi kwa mioyo yenu, ng’ombe huyu nitamchunga vizuri na kumfanya anawiri tele. Nyote
mtafaidika kwa maziwa, nyama, na ngozi kupitia kwa watoto wake”
Lakini haijawa hivyo.
Ng’ombe hajazaa sasa yasemekana ni tasa
Ng’ombe hatoi maziwa sasa anatoa usaha wa uongo wenu
Ng’ombe amekonda sasa anaishi kwa matumaini
Ng’ombe amevunjika mguu zizini hatoki tena anasubiri kufa
Ng’ombe ni hazina na rasimali yetu na fanaka kwa wanetu
Lakini sasa ni mwiba na moto moyoni mwetu
Ng’ombe tuliyewapa mmemmaliza pyeee!
Ng’ombe mali ya wazawa wote
Ng’ombe ni rasilimali ya awaye yeyote
NYATHIWA WOUG DALA
(Mwanetu Ondoka Nyumbani)
Okumu mwanetu sasa umekuwa kijana
Umri umekuwa na akili zako zimebeba utimamu sasa
Umejua jema na baya, we si kinda tena
Mimi baba yako na mama yako tuna neno kwako
Lipokee, lifanyie kazi, litakuwa hazina yako maishani.
Tumetafakari kwa kina utukufu wa maisha yako,
Ujenzi wa maisha yako ya sasa na ya baadaye,
Uhalali wa maendeleo yako na neema yako
Hazitoki nyuma ya viganja vyetu bali nje ya dunia yako
Nje ya nyumba ya baba na mama yako.
Kumbuka maandiko na vitabu vitakatifu,
Vya manabii na mitume walivyoandikiwa wanadamu,
Ondoka katika nyumba ya baba yako na uende katika nchi nitakayokuambia……
Kulijua hilo nasi wazazi wako tunakueleza sasa
Umekuwa, nenda ukajijenge uwe baba wa kaya yako
Tena dunia siyo pepo ya amani bali ni jalala la tabu
167
Wanadamu si watu ila usijitenge nao wakujiapo
Tafuta amani ya moyo kwani huko duniani ni kwenu sasa
Washukuru wakusadiao, waombee kwa Mola wakuchukiao
Mwanetu ondoka nyumbani, umekuwa mkubwa sasa
Mimi baba yako sikuwa hivi bila kujituma
Fanya kazi, usidharau kikupacho mkate wako kila siku
Jitenge na magenge hayana tija ni shimo la umaskini
Nilipoyajua hayo nikayamezea moyoni
Sikuwahi kumtemea mtu zaidi yako wewe mwanetu
Nawe yameze hata kama ladha imechujwa kwa teknolojia
Mwanetu kumbuka hili daima
Maisha ni leo tu kesho usiingoje
Ukiisubiri ije mwana hatokua wako tena
Nyumbani usiogope rudi utakapo
Nasi ni lulu yako na wanao ukiwaleta
Mikononi tuwashike mapajani tuwapakate
Mwanetu ondoka nyumbani, umekuwa mkubwa sana.
NAENDA KUITAFUTA
Baba,mama na Mjomba wote nawaiteni jamvini
Msimsahau shangazi,kaka na binamu nao waiteni
Fikeni kwa pamoja jamvini bila kinyongo rohoni
Mwanenu na neno ndani kabisa moyoni
Nataka kuwaageni
Naenda zangu safarini
Mbali kabisa kuitafuta Nyota ile ya Amani
Iloshushwa toka angani na kuzikwa ardhini
Huko nendako mwanenu ni ugenini
Iwe mashariki,magharibi,kusini au kaskazini
Sina ndugu yeyote huko duniani kama nyumbani
Japo ni safari yenye dhoruba,niendapo ntafika kwa imani
Nikifika nitahoji na kujua kulikoni nyota ile ya Amani
Ipotee angani na kuruhusu giza totoro duniani?!
Ni nani haswa aliyeizima nyote ile ya Amani?!
Naam! Ni asubuhi na mapema nipo njiani
Naenda safari ya mbali huko kunakoitwa duniani
Nguvu yangu i moyoni,mlinzi wangu ni yangu imani
Njiani nang’amua wasaliti waliyoishusha nyota angani
Ni dharau ninayemkuta ameketi katikati porini
Amezingirwa na maswahiba wake chuki,uongo na mfitini
Uoga waniteka nyara na kunipokonya ile imani
Najikuta ni mbabe na mwenye kujaa kisirani kichwani
Sikumbuki nilipotoka na safari yangu ni ya ugenini.
Kisirani na ubabe vinanifanya niidondoshe imani
Uongo,usaliti,dharau na majivuno ni adui wa amani
Narithishwa mikoba hiyo katikati safarini
Hata niendako sijapaona nimepokonywa imani
Hazina na mlinzi wangu waliyonipa wazazi nyumbani
168
Imepotea sijijui asilani
Wolololoo! Nakuwa mtumwa njiani wa kuiua imani duniani
Mizimu ya nyumbani mko wapi? Muje munioke utumwani?
Usiku wa siku ya thelathini na dakika ya sitini
Tangu ilipotimia saa sita kamili hapo porini
Najihisi ni mwepesi mithili ya hereni sikioni
Minyororo ya utumwa imenitoka mikononi
Akilini nawa timamu nagundua nimepoteza imani
Mizimu toka nyumbani imenifungua na kunihoji kulikoni
Nashindwa kujitetea.Najikuta natetemeka sana mapajani
Acha usoni,mikononi na hata pia mwilini
Nilikuwa natetemeka hoi bin taabani
Najikusanya upya toka ardhini
Tayari nimeshapoteza ngao yangu ya imani
Ya kunilinda muda wote niwapo safarini
Navuta pumzi nzito yenye muwasho mkali ndani
Naanza safari kulekea mbele zaidi huko duniani
Mizimu inaniacha na kupotelea angani
Najipa moyo nikiamini wapo nami abadani
Hawataniteleza japo nimekosea nikamezwa tena asilani
Nalivuka pori salama bila kadhia njiani
Nafika salama nchi ya watu wa chini
Natangatanga mtaani kutafuta eneo nikajipumzishe chini
Mitaa imechanganyana kila mtu anawaza lake kichwani
Lugha ya mtaani ni kali na inachusha sana moyoni
Matusi,masimango na vijino pembe ni asili ya lugha ya mitaani
Ikichanganyia sana jamii yote hii mashakani
Nalijua hilo na siku zote napita zangu pembeni
Nani atanijua nikijitetea nipo safarini?
Nuru ikiwa haijajizika chini tena ardhini
Pembezoni kabisa mwa nchi hii ya watu wa chini
Katikati ya mji wa Kingelemkeni
Sauti kali mithili ya vurumai inanijia masikioni
Natulia na kutega mlango wa fahamu kwa makini
Kuitambua vema asili ya sauti hiyo Kingelemkeni
Natambua kuwa imejaa ishara kama kitu kimatatani
Naondoka naenda kujionea mwenyewe kulikoni?
Asalale! Macho yangu nchi hii ya ugenini
Watu wamelazwa wakiwa nyang’anyang’a ndivyo natabaini
Wamepewa mkong’oto takatifu-Ondoa mtu duniani
Yasemekana ni majizi tishio Kingelemkeni
Wanakingelemkeni wadai eti tamaa zimewaponza asilani
Navutika kutega matundu yangu ya sikio kwa makini
Kusikiliza madai yao yenye ukali ya kusimumua mwilini
Wazidi kupayuka zaidi bila kusita mioyoni
Walitaka kupokonya akina mama hawa sokoni
Fedha zao,hereni zao na cheni zao shingoni zenye madini
Siyo mara ya kwanza ni wazoefu sana hapa sokoni
169
Wamekubuhu kuliko hata bidhaa za hapa sokoni
Huja na kupokonya tukawajua leo tumewatia mtegoni
Akafunga hotuba yake mzungumzaji huyu makini.
Moyoni nikatamani wasulubiwa wapewe hata ncha ya ahueni
Waitumie kujitetea huenda wanahoja makini
Si mbuzi hawa kana kwamba hawana akili kichwani
Wanayo na wanajua kimbembe cha kutiwa mashakani
Ikigundulika ni kung’atwa na kuondolewa duniani
Huruma chini ya kiatu wanadamu wamevaa miwani
Wanaikanyaga bila kujali,hawaoni kitafuata nini
Jamani hatupendi kuwa hivi ila ni Kingelemkeni
Imetuzaa na kutufanya tuwe na hivi hapa mjini
Tumejitahidi kufanya kazi ila tumetiwa vikwazoni
Tumefanya kazi hali kujipatia kipato mfukoni
Tumeuza mitumba na kuwa machinga hapa mjini
Lakini Kingelemkeni na serikali yake imetuweka vizuizini
Haturuhusiwi kufanya kazi zetu hadi tuhamie eti zizini
Huko ndiko halali kufanyia biashara hadi kileleni
Tumekaa huko wiki inayeyuka hakuna kitu mfukoni
Nami niwaulizeni nani kati yenu anayeenda zizini?
Hamuendi huko kumekufa mithili ya maiti makaburini
Yazikwa kisha waombolezaji watawanyika kurudi nyumbani
Kama ndiyo hivyo tumekosa nini?
Nikashusha pumzi taratibu mithili ya gari mteremkoni
Amejitetea vizuri japo sijui ukweli wa Kingelemkeni
Nikaamini
Kama mimi nawaza jambo akilini
Basi wananchi-vinyongo watakuwa wanawaza makini
Lakini haikuwa hivyo.Nikasikia akisema“wamwagieni mwilini
Astakafili petroli mwilini”
Kiberiti kikawashwa na kudondoshwa chini
Watuhumiwa wao wakaanza teketea chini kwa chini
Moyo ulijikunja kwa huruma nikakumbuka nyumbani
Ya kuwaita mizimu ya ukombozi waje hapa ugenini
Kuwasaidia vijana hawa wanaoteketea ardhini.
Nikajiondokea huku nikimlaumu aliyeishusha nyota ya amani
Yuko wapi Jamani niambieni.
Nikaondoka polepole uchungu ukiwa moyoni
Furaha ikiwa imejizika chini kabisa ardhini
Nikaenda kutafuta nyumba ya kujiegesha wageni
Wawe wasafiri au hata ndugu wa mtaa wa jirani
Huko nikashusha pumzi hofu nikaitia mfukoni
Nikawa mpya kuliko nilivyoingia Kingelemkeni
Namuomba Rabana anijalie bwerere usingizini
Ni saa kumi na moja jogoo aniwikia dirishani
Navuta shuka naamini nimemkwepa asalini
Hiyo haisaidii kwani sauti yake inanizidi usingizini
Kuona hivyo nakoma,naamka nawaza jambo akilini
170
Ni wapi ntafika,nani nimuulize anijibu swali kwa amani
Ni nani aliyeishusha nyota ile ya Amani?
Swali hili nitajibiwa lini?
Kelele inanijia nahisi ni sauti ya wageni
Kusikiliza kwa makini nang’amua ni vurumai chumbani
Sintofahamu inaninyonga ujasiri wangu unapita pembeni
Nafikiria kimapana natafakari akilini
Ni waungwana gani hao,hakujakucha wana yao chumbani
Nifikiriavyo kumbe napotoka wenye mali washikana ugoni
Mume kamsaliti mke bila kujua athari yake ni nini.
Mke naye kamsaliti mume bila kujua balaa lake ni nini
Sasa siwamefumaniana vitaulo viunoni,aibu machoni
Daaa! Duniani jamaa,kuna mengi mengine nyamazeni
Wiki tatu zinayumba nikiwa Kingelemkeni
Kazi niliyoifata kufanya nimeimaliza mimi maskini
Navunja kibubu,basini nakwea narudi nyumbani
Wazazi na ndugu zangu simameni pale barabarani
Mwanenu nimejua nani aliyeishusha nyota ya amani
Kusanyeni kuni baridi ikizidi washeni moto muoteni
Hapo tuchome mahindi,punje tuzirushe mdomoni
Majibu ya kazi yangu nitayatoa kwenye shairi B mbeleni
Tumuombe Mola atutie nguvu zaidi mwilini
Tuonane hapo bila ya vinyongo moyoni.
MAJI YA KIFO
Maji ya kifo hayafai kuoga
Yananyofoa uhai wa mtu
Yanaunguza amani ya mwilini
Yaepuke usiyaoge.
Maji ya kifo
Hayafugi samaki
Yananuka uvundo wa mauti
Yakwepe
Usiyatumie hata kunywa!
Maji ya kifo
Yagadhabisha sana
Yaunguza maua ukiyanyunyiza
Ndege hawayanywi kiu wakiona
Yanatisha!
Yanaogopesha!
Usiyazoee!
Maji ya kifo
Yachemshwe yapoe yachujwe
Hayafai kwa kunywa
Yanavimelea hatarishi
Kioo kikizidi
Vumilia hadi mwisho
Yakwepe kama ukoma.
171
ULIMI
Ulimi nyama laini,sumu iuayo sana
Wengi wako hatarini,amaniyo yagongana
Hofu i tele moyoni,dunia yasalitiana
Ulimi kitu kidogo,chaangusha hata dunia.
Machafuko mitaani,vijana watadundana
Neno lotoka mdomoni,gonjwa linaoteana
Lakomaa hadi ndani,visasi vyazaliana
Ulimi kitu kidogo,chaangusha hata dunia.
Ulimi hata chumbani,wazazi hutifuana
Maneno ya mitaani,yaingiapo chembana
Heshima ’dondoka chini,kwenye ndoa hutengana
Ulimi kitu kidogo,chaangusha hata dunia.
Ulimi nyama laini,laua hata dubwana
Giza tete maishani,amani kama dafina
Imejizika ardhini,magomvi ni yake mnuna
Ulimi ni sumu kali,inayoua taratibu
TUKAOGELEE!
Tukaogelee!
Wapi?! Ndani ya tope zito
Lenye kunatisha nyama ya machungu yetu
Tusivue nguo tukiogelea!
Tuogelee macho wazi mbwa mwitu asijeiba
Tumaini tulolivua kando ya mto
Tukaogelee!
Tukaogelee ndani ya wimbi zito la tafakuri
Lirutubishacho mpito wa kinadharia
Zo dumu zenye utasa ulokubuhu
Manyang’au yatakwama ng’amnoni
Kinani tikielea.
Tukaogelee!
Tukaogelee!
Tukipiga mbizi juu ya ya nyayo ndefu
Katikati ya kina chenye wimbi zito
Pumzi zikichoka
Giza tete la msisitizo bainifu
Litatushukia mbele tukiibuka!
Hekima,busara ni kina cha uvumilivu
Tukishaogelea.
Tukishaogelea!
Tutakuwa?!
Tumeshinda dhoruba ya maisha
Tumechoka tunarudi salama.
AKILAMBA SABUNI
Mate yashamiri ugwadu
172
Radha hufifia mdomoni
Ulimi huteleza pasipo kikomo.
Mbuzi akilamba sabuni!
Utamu huchokocha
Koromeo hukereketa koo hutii
Udenda mzito uso mwisho
Humvuja bila yake hiari.
Kuna wakati nao upo
Binadamu akailamba sabuni.
UMOJA WETU
Kong’ai! Kong’ai!
Ndo yetu dira itupayo nguvu
Isikikapo dunia yatambua moja
Wakuu wa anga hao wakatiza
Furaha yetu safarini kughani
Kong’ai! Kong’ai!
Dhoruba angani nzito ipe moyo
Si wote twafika kwa wakati pangwa
Vunjika mbawa,kosa nguvu ni vikumbo
Hufiki bila kuvikabili na dhati yote.
Akumbwapo mwenzetu si twasonga
Kudra zetu kuziweka kwa kundi la pili lijapo
Nalo hufika kumchota na kumsindikiza nyumbani
Furaha yetu moja
Kughani umoja wetu
Kong’ai! Kong’ai!
Makazi yetu makutini
Minazini kujistiri na baridi kali
Wanana kuwalea na kuwaepushia mbali na dhahama
Tishio mtikisiko wa kimaslahi na ndege wachafu
Bundi na watoao miziki dhalimu
Songombingo!
Minazi kuhimili mikikiki
Maslahi yetu kujilindia
Dira yetu ni moja
Kong’ai! Kong’ai!
WEGESA MNYAMONGO
(Wege/Penina)
Nakueleza kinagaubaga Wegesa Mnyamongo
Kwa beti hili moyoni nakuimbia.Elewa!
Nilidadisapo kutano letu Tarime
Nakiri wazi hata penye mvua pana uwazi
Sitolisahau bali nitalihifadhi kwa pendo kuu
Naamini ni wewe hakika nilofunuliwa na Manani
Nashukuru!
Ni wewe uliye sura ya wanangu
Ukanizalia!
Ni wewe uliye damu na nyama ya wanangu
Ukanilelea!
173
Ni wewe uliye pumziko langu moyoni
Nimetulia!
Kwa hilo nakutabaruku maneno haya
Mapenzi ni mchuzi ulopikwa ukapika
Viungo linganifu ladha yetu tusipoteze.
Nasi tuupike mchuzi wetu juu ya figa letu
Kani ya upepo ni majaribu ya dunia
Mchuzi wetu tukikosa kuunga vyema
Ladha yake ikawa shubiri mioyoni mwetu!
Kumbuka hata wale mbwa mwitu walotupania
Wakakuta kiambaza kikubwa penzi letu ni fupa
La mzimu fisi alisalimu amri na iweje wao?
Nakusihi tusukumize sayari yetu mbele
Lifike salama jalali tunaomba
Hata katika misukosuko ya dhoruba
Agano letu litimie ndoa tuifunge
Na familia yetu isimame kwa jina letu
Nikupendaye ni mimi wengine mafamba.
Moyoni watakutoboa mibani wakikupitisha
Nakuomba yasikie niyasemayo!
Wewe sabuni yangu ya roho!
Penina Mnyamongo!
PANYA AKIMNG’ATA CHUI
Panya akimng’ata chui kilio husikika
Makucha huyatoa kwa sauti huunguruma
Hasira hubeba kisasi hulipiza
Panya na chui si wajamii moja
Urafiki wao ni wa mashaka sana
Chui hujiweka kimbele kama mtawala
Hulinda na kuvizia vitoweo vipitavyo jiraniye
Hajali ujuzi gani atumie kudaka kitoweo hicho
Kukwaruza,kung’ata au hata kunyonya damu
Ubongo wake unajali kitoweo tu na si kingine
Ujane,uyatima na upweke huwatia wenzake
Panya na chui hakika si wa jamii moja
Chui hakumbuki utu na haki za wenzake
Kuwalinda wake na kuwapa ulinzi ndo yake tija
Panya akithubutu kumng’ata kilio utakisikia
Pori litakuwa jehenamu,upende usipende.
Chui akigundua kekiye ipo rehani kuliwa
Huja juu na kumtishia panya
Chuki huionesha ulinzi huimarisha
Kimya hukaa upepo ausome
Hasira zikimzidi pori hulichafua
Panya wote mashakani huishia.
Panya wakikosa umoja wamekufa tayari
Chui hukaa kando kushuhudia vurumai mpya
Paka na panya hii ni vita mpya darini
174
Msako huwa endelevu,chui azidi chekelea
Pori likichafuka mtini hujipandia
Panya akipata mwanya
Humng’ata kwa hasira mkiani
Kilio cha chui utakisikia
Kweli chui na panya si wa jamii moja.
KUNGUNI
Hebu niache ewe kunguni
Usafi nimefanya bado hutaki
Nguo nimefua lakini hutoki
Rangi ukutani nimepaka bado unaning’inia
Kunguni we ni wa aina gani?
Kunguni unaninyonya damu,nakonda!
Unaniaziili hata mbele ya watu
Naonekana mchafu
Tabia gani ulonayo?
Kunguni tafadhali!
Kunguni nakiri nilikukaribisha kwangu
Uishi nami nawe ni kiumbe
Umesahau fadhili zangu
Umekula vyote sasa hadi damu yangu unataka
Kunguni we ni wa aina gani?
Kunguni muda utafika
Kikomo kitashika hatamu
Dawa nitakunyunyizia kwangu unitoke
Niishi kwa amani kama mwanadamu
Kunguni siku itafika!
HATA KAMA!
Hata kama jua litakoma kuangaza leo mchana
Sitagota kuisubiria miale ya penzi lako
Iniangaziayo na kunipa sababu ya furaha moyoni
Hata kama baridi itausukasuka mwili wangu
Sitokufa kwa ganzi maana sauti yako ni koti langu la baridi
Sitoyumba moyo wala kutetemeka meno
Hata kama mawimbi ya bahari yatakoma kuimba
Sitoacha kuwashinikiza ndege na wadudu waimbe badala
Miti na upepo nazo zitaughani wimbo huu wa “Nakupenda”
Hata kama penzi lako litakuwa mwiba kwangu
Nitajifanya siyasikii maumivu yake ili nifike
Nitaliona kama ua zuri la kunidekia machungu hayo
Hata kama mwili wako si blanketi yangu ya baridi
Sitonunua shuka zito kuutelekeza uwepo wako
Nitajikunja hata ngumi kujilinda na baridi kali
Hata kama nikifa kwa kupenda kwa dhati
Pepo haitonifariji kama sauti yako ifanyavyo
Kuzimu haitonitisha kwani sauti yako ni ngao yangu.
Hata kama mvua itaijaza dunia kwa mafuriko
175
Nitajipa moyo kupiga mbizi maana we ni boya langu
Nitaiokoa dunia ili ijue navyokupenda kwa niaba yake
Hata kama kitanda kitanisaliti usiku nikilaliapo
Sitowaza tena,hata chini nitajilaza ukiwa pembeni yangu
Sakafu itanibariki kwa ubaridi mwepesi wa mahaba yako
Tena nawaambia hivi hata kama! Hata kama! Hata kama!
Maswahibu hayataisha,sitakufa moyo
Visa vitazidi,Akech nitavisherehekea
Na hiyo ndiyo fanaka ya pendo langu kwake
Hata kama majangiri yataniwinda usiku kucha
Mwili wangu nautoa rehani kwako
Roho ipumzike kwako
Moyo wangu upoe ndani ya pendo lako
Hata kama! Usipolilea abadani penzi langu!
Nitakupenda!
Ksii!! Ksii!!
Nakupa ujauzito
Twanyofoa mimba
Kiumbe twakinyima uhai
Asubuhi naranda mtaani
Kwa mbali mtu aita simjui
Ksii! Ksii! Ksii
Nageuka nyuma simuoni
Kushoto kulia simuoni
Ksii! Ksii! Aita tena
Natambua ni mwanangu nilemwangamiza
Anililia kwa uchungu!
Namtengeneza mwalimu
Namuajiri vijijini
Maji,umeme hakuna
Nami nalitambua napuuza
Anilalamikia napuuza
Nakunywa chai mjini nasikia
Ksii! Ksiii! Ksiii! Nasimama
Natizama kila kona.Hakuna mtu
Ksii! Ksii! Aita kwa ghamu
Nabaini kwa kina ni mwalimu nilemsaliti
Nakuja kwa wananchi
Naomba kura kwa ghamu nyingi
Naahidi maisha bora
Mwanichagua nashinda
Napuuza jukumu langu kwenu
Nasinzia bungeni.Nasikia
Ksii! Ksii! Nashtuka
Nang’amua ni kilio cha wapiga kura yangu
Wanililia kwa usaliti wangu!
MTAKOSA KUTHAMINIANA
Tabia mliyoanza nasema siyo njema
Kutupiana vijembe mitaani siyo njema
176
Kuchomeana utambi kwa marafiki si njema
Ikikithiri tabia hii
Itatunga mimba ya mauti
Mkizidi kulea hiyo mimba
Mtakosa kuthaminiana
Kamchezo kanakojitokeza si kazuri
Kamchezo ka kujivinjari na wanenu kimahaba
Kamchezo kachohatarisha hadhi zenu
Kaacheni kabla hata jua halijazima
Mkikaendeleza
Mtakosa kuthaminiana!
Mnapotupiana ngumi nanyi mu ndugu haifai
Mnapoingiza ukabila kwenye hakuna mnakosea
Mnapopandikiza udini kwenye hakuna ni dhahama
Tufani likizidi hasara hujitokeza
Mkikomalia hayo
Mtakosa kuthaminiana!
Mnapanga nyumba moja ninyi ni majirani
Shida ya mmoja iwe yenu nyote
Lakini mnapopikiana chokochoko,hafai!
Mnapotupiana tuhuma za kuchafua ujirani,haifai
Msipobadilika!
Mtakosa kuthaminiana!
Mnaponyimana ndani ya nyumba ni laana hiyo
Mliridhiana na kuuvunja umbali ili mfaidiane
Mnapojijengea vikwazo vya uchoyo ikiwa hamu mnayo
Mnapowekeana amri nzito za kukomoana
Mwajikosea wenyewe
Mnajihatarisha wenyewe!
Mtakosa kuthaminiana!
PAMOJA KWAMBA
Pamoja kwamba pendo lako laniacha
Nitalituma langu lilirudishe kwangu
Pamoja kwamba kwaheri inanijongelea
Nitatizama milima,kushindwa kwangu kunatoka wapi?
Anga linafifia na jua halionekani tena
Siku hii ikipambwa na mhemko
Naapia mbingu nitaikabidhi kwako
Ntaisihi mbingu itutakie lakheri hadi dahali.
Najiuliza kama utaondoka tena?
Utarudi lini?
Moyo wangu unazama kwenye zahama
Hofu yangu inazidi kukomaa bila sababu
Pamoja kwamba nimetawaliwa na miujiza
Lakini nyuma ya kumbukumbu zangu
Nakiri sina ujasiri wa kuishi maisha haya bila wewe
Natazama nyuma yako nahisi utakuwa mwisho wetu
Kuonana! Hata kama moyo wangu utapata ganzi
177
Hu,sawa na mshumaa kwenye ukingo
Upulizwao na upepo mkali
Ngoja ya muda mrefu,yanichimbia maumivu yasiyovumilika
Lakini bado…………bado….
Nashauku na wewe kila siku
Hivyo tusitengane turudianapo
Nahitaji pendo lako!
Nakuhitaji!
Nakuhitaji kwa huba lako!
Sina chozi zaidi la kumwaga
Sa tafadhali usiseme kwaheri,usilie bali tabasamu
Sa kwaheri kwa wale waishio gizani kwa upweke
Muda wote nisimamapo kando ya mto ulipo’ndokea
Naikumbuka taswira yako kwa mara nyingine
Nahemka kukukumbatia tena
Nitayaficha machozi yangu katikati ya mvua
Huku nikipunga mkono wangu kwa ukimya
Uendapo na urudipo akutangulie Maulana
Pamoja kwamba! Tunatengana tena.
Bado nakupenda!
J.K.NYERERE BABA
Nyerere baba
Mwana wa Afrika
Mwamba wa mataifa ya Afrika
Twakukumbuka siku zote maishani.
Uliteketeza umimi
Ukavaa uzalendo wa Afrika
Wanyonge ulisimama badala yao daima
Leo haupo nasi
Twakukumbuka siku zote maishani.
Nyerere baba
Kauli zako kali zilileta hamasa
Wezi waliogopa,mafisadi walitetemeka
Hukuwa na mzaha asilani
Leo haupo nasi
Twakukumbuka siku zote maishani.
Ulianzisha umoja wa kitaifa
Ulivunja udini na ukabila kwa maneno
Undugu akauzalisha miongoni mwetu
Thamani ya umoja ilionekana
Leo haupo nasi
Twakukumbuka siku zote maishani.
Hukuwa mchoyo na mroho
Madaraka kuyakumbatia milele
Kwa ridhaa ya moyo wake
Akayakabidhi kwa wananchi
Uamuzi wakauridhia
Nyerere baba!
178
Mfano hai wa kuigwa
Leo haupo nasi
Twakukumbuka siku zote maishani.
SHEREHE ITAKAPOISHA
Sherehe itakapoisha
Tutarudi kwenye msoto
Pesa mpapatiko
Chakula mpapatiko
Maisha thakili
Na gharama za kujikumu
Angani zitapaa.
Sherehe itakapoisha
Kumbukumbu nazo hufifia
Walokufa tunawasahau
Walopigania na kulijenga taifa
Walohatarisha tija ya maisha yao
Tunawafuta pia kumbukubuni
Hakika hatufai!
Thamani ya utu tumeidondoshea kutu.
Sherehe itakapoisha
Fungate litajongea
Ndoa itashika hatamu
Wafadhili wetu watarudi mpapatikoni
Mapesa walitumwagia
Familia zao zapaliwa na ukata.
Sherehe itakapoisha
Taifa litakuwa huru
Makafiri wataishi bwerere
Kwa kidogo chao.Chao na nyumba zao.
Michango ya sherehe zitakoma.
Sherehe itakapoisha
Makinda yatalia sana
Yatakumbuka furaha yaliyoipata
Asalale! Haitojirudia.
Hasira,chuki na vinyongo watazichonga
Kwa wazazi na ndugu.Hasara hawaioni.
Mahusiano yao hatimaye hudidimia.
Sherehe itakapoisha
Ndege angani wata’budu haleluya!
Watarandaranda jalalani kudonoa makombo
Mabaki na makombo ya wahafidhina.
Jasho la makabwela,walilofanyia mafambo
Huzuni tele kwa wakamuliwaji.
Sherehe itakapoisha
Mataji tuliyovishwa tutayavua
179
Sifa tulizovalishwa zitadidimia na sherehe
Maisha yataparara!
Vituko vitakithiri
Utu utatokomea gizani
Mahusiano yatadorora tena nyumbani.
Sherehe itakapoisha
Viziwi watapata kusikia tena
Vipofu watapata kuona tena
Wafu watapata kuishi tena
Wataduwaa kwa maajabu ya sayari hii
Watapinga kuvaa vazi la karne mpya
Uongo ni rangi ya kupendeza
Inatishia uhai wa ukweli
Lakini ukweli ukidhihiri,uongo hujifia.
Sherehe itakapoisha
Maisha yalokuapo yatasonga
Yote yapita,kesho haitokuja
Malengo,maarifa,jitihada na mikakati itatekelezwa
Adha ya kuchangia sherehe zitapotea
Furaha itajipandikiza upya.
RAIS AWAYE YEYE!
Asiwe kipanga
Awe na kauli chanya
Ajue dhamana ya aliyonayo begani
Asijikweze ila atambue makundi yote
Huyo ndiye Rais awaye yeye!
Awe na chachu ya mabadiliko
Asiwe na mgando wa kutambua
Avunje mizizi ya undugu na uswahiba madarakani
Asione aibu kukosoa na kukosolewa
Aseme nipeni ushauri akikwama
Huyo ndiye Rais awaye yeye!
Aishi pamoja na maskini
Ajue ni watu tisa kati ya kumi wanaounda taifa
Awafariji mabalaa yakiwakuta
Machozi awafute asichoke kuwahani
Atatue matatizo na siyo kuyakimbia
Huyo ndiye Rais awaye yeye!
Akemee kwa mshindo mkuu
Azibe mianya rushwa inapotoboa
Amwage razi wasaidizi wake wanapompotosha
Asiwaone haya usoni
Huyo ndiye Rais awaye yeye!
Awe ni sauti ya wengi
Asiwe moyo wa faraja kwa wachache
Azunguke kila kona na ncha ya nchi kuona hali halisi
180
Asiwe wa kuletewe nakala na kupitisha bila kuhoji
Awe ngangari wa uzalendo na si bendera ya uasi
Huyo ndiye Rais awaye yeye!
BARUA YA MAJIBU
Mpenzi!
Udondoshapo macho yako juu ya barua hii
Tambua mimi ni mzima na buheri wa afya.
Nilifurahi,nikaimba,nikatabasamu nilipoisoma
Barua uloniandikia siku ile!
Ni barua nzuri yenye virutubisho vyote
Inanifanya ninenepe kila niisomapo muda nikipata.
Nami usiku huu natembea juu ya kurasa huu mkubwa
Kukuandikia barua.
Barua ya jibu la barua yako!
Ulihoji iwapo nimepata ajira!
Nasikitika kukwambia sijaajiriwa bado
Tangu nihitimu chuo sasa ni miaka miwili
Ofisi zote nilizunguka visigino vikauma
Maajabu nikayaona!
Wapo walioniambia vigezo miaka mitatu ya uzoefu
Jiulize miaka hiyo mitatu nitaipata mimi
Wengine wakadiriki kupinga ufaulu wangu
Eti kwa ufaulu huo,hawawezi kunilipa
Sikutia inda.Nikakata tamaa sasa nimepoa tu
Hakuna kazi! Sina kazi!
Oooh! Kuhusu rafiki yangu K.
Ye’ ameajiriwa sasa ni mwalimu
Huko kijijini nyumba ya kuishi hakuna
Kamshahara kake kaduchu ayavumilia mateso
Marupurupu hakuna
Mazingira ya kazi ni adui wa afya yake
Nawasiliana naye mara kadhaa
Ntamtumia muhtasari wako
Tuliza moyo sasa.
Uliniulizia kuhusu baba!
Ni mzima si kama ulivomuacha
Alilitupa jembe na kutimkia mjini
Kilimo kwake ni sumu-alisema
Huko mjini hana kazi fununu zilisambaa
Aliumizwa na mgambo wa jiji
Alipoanzisha ujasiriamali wa umachinga
Eneo lilipigwa mkasi kumfanyia biashara
Natamani kujua mengi
Nasikitika ni hayo niyajuayo.
Haaa!
Usicheke! Tafadhali nakuomba
X siku hizi ni Mheshimiwa nchini
Unamkumbuka alivyokuwa fakiri?
181
Tulimchagua sababu fakiri huenda angetuona wenzie
Duuu! Uamini usiamini tulichagua msiba
Alifunga ndoa ya mkataba na mzungu pua mbaya
Mkataba wao wa siri wazawa hatuujui
Ndege zatua kila dakika zapakia na kupotea
Malighafi yetu ardhini imenyonywa
Sasa tumebakishwa kabishishi ya mashimo makubwa
Hakuna tunachofaidi!
Ngoja nikutibue moyo
Pili alipokosa kazi japo rushwa aliombwa
Alikataa kutoa,majukumu yakamuandama
Dunia ilipomtelekeza twasikia ana biashara mahsusi
Ana vaa vichupi usiku kwenda kujitafutia chochote
Mtaani aitwa Kahaba machachari
Niliumia,nikasikitika mwisho nikaomboleza
Siku nilipomuona.
Dunia mbaya
Walimwengu nao wachochezi
Tumuombee.
Mpenzi!
Unaikumbuka hospitali yetu takatifu
Si takatifu tena ila ni domo la jehanamu
Kisa kilichotukia hivi majuzi kimetuacha vinywa wazi
Dokta makini,msomi wa nyanja zote
Amfanyia binadamu mwenzie upasuaji
Alipomaliza kamshona kwa nyuzi nzito
Tumboni kamuachia mkasi mgonjwa
Ajabu gani ya dokta huyu msomi?
Tukajua maajabu yameisha hapa duniani
Miezi kadhaa mbele kubwa kuliko likajiri
Mgonjwa wa mguu,mgonjwa wa kichwa!
Aliyepaswa kupasuliwa mguu apasuliwa kichwa
Wa kichwa ye apasuliwa mguu
Tukajiuliza!
Alitaka tibu nini?
Naumwa kichwa watibu mguu
Naumwa mguu watibu kichwa
Akili kweli hiyo?
Dada Aisha uliyemuulizia
Hana raha tena ya maisha baada ya ujauzito
Tabu alizozipata kumzaa mwanae Tabu ni tabu kweli
Alijifungulia chini pamoja na kuwa alikuwa hospitalini.
Mnuna tangu atupokee kwenye unga
Maisha yake ni heri na jehanamu
Ni mlevi amechoka sasa ni teja
Dunia iko kulia,yeye kushoto
Maisha yameganda
Ni huzuni kwetu.
182
Na ukata ule tangu upange kwetu
Amani ya maisha hakuna
Asubuhi njaa! Mchana miayo! Usiku nikulala
Siku zinaenda,zikipita tunasahau
Pesa hakuna! Kazi zimeota mabawa.
Ni kama ulivyotuacha laazizi wangu!
Nimaliziapo kujibu barua hii
Nakiri utakuwa mwendelezo wa barua kadhaa toka kwako
Nipe nikupe,
Uonapo inakidhi nitumie nyingine
Wako katika mapenzi.
Akech!
MKULIMA WA MKONO
Kumekucha!
Kokolikoo!
Jimbi limeshawika
Mkulima damka ukajichimbie shambani
Fanya kazi usikumbuke nyuma
Nyuma.Nyuma kabisa enzi za kampeni
Mwanasiasa alikuambia………..
Mwanasiasa?! Ha! Ha! Ha
Wote ni uchwara tu.
Kheri yako iko kwenye mpini
Uliong’atana na jembe lenye mapengo
Lima asubuhi.Lima mchana.Lima tu
Fanya kazi mavuno yatakufata yenyewe
Ukikumbuka kuna mbolea
Tumia ya ng’ombe wako.
Usisubiri ya siasa.Siasa inachosha subira
Subira nyingi yaumiza moyo
Jua likipoa ardhi imeshika mbolea
Tia mbegu
Palilia shamba
Vuna mwenyewe,usimsubirie mwanasiasa.
Soko lijenge mwenyewe
Soko la serikali ni unyanyasaji
Lina dhamira ya watu wachache.
Nyie wengi umoja wenu ni nguvu
Gumba lenu litamvunja chawa mnyanyasaji
Mkulima wa mkono.Pole sana.
Kumekucha!
Kokolikoo!
Jimbi lawika tena.
Uchaguzi unajivinjari tena
Mwanasiasa mpya na mkongwe wanapigana vikumbo
Wanakujia.Akili yako waiduwaza.
183
Watakupumbaza.“Nipitishe mimi ntakuletea tingatinga la kulimia”
Waongo wakubwa!
Tema ondoka usiwasikilize
Wapaza sauti jukwaani,wakipata ofisini wajichimbia
Ninyi ndugu zangu,
Tena wa damu,
Nilipokuwa navyo,
Niliwasaidia toka moyoni,
Leo nimeishiwa,
Mwanidhihaki,
Wampe ridhaa wewe chini ya jua
Kwenye msururu mrefu wa kupiga kura
Akishinda!
Humuoni tena.Si shambani,jukwaani na wapi……
Amekipata alichokitaka yanini kujisumbua?
Ndiyo falsafa yao mpya
Mpya kabisa nawabainishia.
Miaka mitano unarudi kwenye msoto.
Mkulima wa mkono.Sahau yote
Jua uko mwenyewe bila mkombozi
Jembe lako ndio silaha yako
Imeshasemwa:Jembe halimtupi mkulima.
Lakini:Trekta la mwanasiasa ndio umaskini wako.
Likatae hata bure!
YA NINI LAKINI?
Na kunikejeli,
Ya nini lakini?!
Mwanisomesha nimesoma,
Narudi kwetu nyumbani,
Nyie ni wazazi wangu,
Nanyi ni binadamu,
Mnakosea,mnakandamiza,
Napowakosoa,
Mnanijia juu na kulaani,
Sina nidhamu napotoka!
Ya nini lakini?!
Unatangaza kazini,
Dada yangu anataka kazi,
Anakuja kutafuta,
Unamtongoza na kumlaghai,
Penzi akupe,
Kazi umpe,
Eti mfumo mpya,
Nipe nikupe!
Ya nini lakini?!
Unatuhubiria kanisani,
184
Tutoe tulichonacho,
Twajikamua twatoa,
Sadaka unakula,
Kesho unahubiri tutoe tena,
Tumboni umeshiba,
Umetuibia kidogo chetu!
Ya nini lakini?!
Wanifata haraka,
Wanidokeza lako moyoni,
Wanipenda toka moyoni,
Nakujibu kistaarabu,
Naye wangu wadhati,
Anipenda kwa dhati,
Huamini waning’ang’aniza,
Nimteme nikuchukue weye!
Ya nini lakini?!
Naolewa kwenu
Mume kanitoka
Matanga hayajaanuka
Mmeanza gawana
Mali za ndugu yenu
Watoto hamuwaoni
Uchu wenu ni mali
Mnafikiri nini
Nitaenda wapi mimi?
Ya nini lakini?!
CHUNY PINY
(Roho Ya Nchi)
Ni kiungo laini mwilini mwangu
Kikinikimbia natambua sitoishi
Anajua Manani mwenyewe umbo lake
Aliniwekea mwilini nje ya utambuzi wangu
Naishi sababu ni injini yangu
Je,roho ya nchi nini?
Nchi ni mwili si wa mtu mmoja
Ni mwili wangu,wako,wake na wote
Ni mateso yetu ya nyuma
Adha za utumwa na unyanyasaji tulizovuka
Jana nzima enzi za Berlin
Leo hii twapandikiza roho moja
Nchi inapumua.
Tunaishi kwa furaha
Je,roho ya nchi ni nini?
Amani,umoja,upendo na mshikamano
Ukweli,uadilifu na usawa wa haki
Ndizo zatengeneza mshipa mmoja wa roho ya nchi
Nchi itapumua kwa usawa
Nchi itavuta hewa ya heshima na demokrasi ya kweli
Roho ya nchi,jibu mmeelewa?
185
Rai yangu kwenu wazalendo wa dunia ya tatu
Nchi inapopumua ndo raha yako
Nchi ikifa jua ukimbizi utakuwa subi
Hakuna atakayetupa hifadhi ya maisha
Tumeiua yetu atuamini nani?
Eti yake tutailinda na kuienzi?
Tujiulize hayo bila kudhania.
Roho ya nchi mustakabali wetu.
NA TUVISOME VYOTE
Wosia wangu kwenu
Tuamke twende maktaba tukajisomee
Vitabu ni chemchem ya maarifa isokauka
Vitabu ni dawa ya matatizo yako
Vitakupa nguvu na mwangaza mpya kusoma ukimaliza
Viliandikwa,vimeandikwa na vitaandikwa na wataalamu
Njooni tuvisome vyote,
Hadithi,ushairi na tamthilia
Hadithi!
Mfalme Ndevu na Mmaskini Mkata Kuni
Ya Abdallah Khalfani.
Jipatie elimu juu ya dhuluma,urasimu na tamaa
Ukimaliza kusoma utajihoji mwenyewe
Abed Mehta ni katika Anaona Anasikia
Somo la kujifunza ni athari ya Ukimwi
Ukimwi ni sumu ya maendeleo ya taifa na jamii
Na kitabu cha Mtego Kabambe
Kitakuachia elimu na mafunzo anuani
Kuku Njiwa Kicheche na Hadithi Nyingine
Ya Athumani Abassi.
Ni mahususi kukupa maadili ya kutosha
Chatu cha Bata,A.A
Kinatufundisha thabiti juu ya mapenzi kabla ndoa
Athari zake na ukinzani katika malezi baina-
Ukristo na uislamu
Bwana Jemes, H kupitia Mganga Pazi
Atakuonya juu ya ulaghai katika kupata mali
Balisidya Ndyanayo anasema Ushindi wa Majeruhi
Na Hadithi nyingine
Atakuangazia kwa kina juu ya matatizo
mazitomazito katika maisha
Hao na wengine wengi
Natuitike kuvisoma vyote!
Ushairi!
Zipo tele Kama mvi za babu
Diwani Ya Akilimali cha Akilimali.K.H.A
Chadhamiri kwenye mawaidha mema
Na maadili mbalimbali kama wema na upendo
Utenzi wa Mwanakupona cha Alen .J.W.T
Chenye kudhamiri kwenye maadili mema
186
Na wosia juu ya wanawake-Pwani na Afrika Mashariki
Frenk Wiliam na Diwani Yangu
Mahsusi katika dhamiri ya Mawaidha mbalimbali
Ya kijamii kama siasa safi,adabu,heshima na upendo
Liwazo la ujamaa cha Kandoro,S,A
Chenye dhamiri ya Mapigano dhidi ya unyonyaji,
Na mawaidha juu ya siasa,ujamaa na kujitegemea
Na vingine vingi.
Tamthilia
Ni kama hivi vifuatavyo!
Zimwi la Mrima cha Fawah F
Kinachojadili juu ya dhuluma na uonevu katika jamii
Mashetani cha Hussein E
Kinazungumzia juu ya mapinduzi ya kiafrika
Jitihada za ndani ya bara la Afrika
Kaptula la Marx cha Kezilahabi E
Chazungumzia Utawala wa Kiitikadi hasa wa mafunzo ya Usoshalisti na Ubepari.
Na Mpaka lini? Chake Mariam S M
Alichokiandika kujadili
Madhara ya Rushwa,UKIMWI na Udanganyifu
Naradidi tena na tuvisome vyote
Elimu haina mwisho na ni bahari isokauka
Kujisomea ni chanzo cha maarifa
Ni muda sasa tufunge makazi tukajisomee vitabu
Tusije kuwa vichwa vya wendawazimu
Kwani maono ya vitabu yameandaliwa kwa kina
Twendeni!
Tuvisomeni tusiogope!
SAFARI KUELEKEA
Naitwa Kabiero
Anaitwa Habiba
Namuita Mahabibi!
Ananiita Mahabuba
Raha ya penzi,mpende mpendene.
Na hakika tukashibana mithili ya samaki na maji.
Naivuta taswira nyuma kabisa ya mambo
Ya saa na siku ile
Tulipokutana,tukapanga tarehe ya dibaji yangu
Wazazi na ndugu zake wanitambue
Kisha watutunuku fanaka na ndoa tuifunge
Pingu zituunganishe mwilini hadi moyoni
Si hilo likapita!
Siku ya siku.Ni Jumamosi nifike
Mama mkwe,Habiba na mashemeji wapo CMG Motel
Waningojea
Nimeshavunja kabati suti nyeupe zaningoja
Ngriii! Ngriii! Simu inaita kwa nguvu ikitetemeka
Jina lasomeka-RohoYangu!
187
Napokea.Haloo! Naongea
“Bado upo wapi Laazizi wangu? Mama na ndugu wakutamani.Wahi!”sauti laini ya Habiba yanidekea
Bila kujua hakuna aliye na kesho yake mkononi
Nikajibu kwa mikogo“Nipe lisaa limoja.
Watulize munkari.Aibu sitokutia!”
Laazizi atabasamu kicheko chanitekenya sikio.
Simu nakata.Haraka najivalia viwalo vyangu
Furaha inanisukuma hadi nje
Tabasamu limechanua usoni
Habiba ameamua kunitoa kimasomaso
Kunifungulia hazina ya pendo lake
Halali ya ndoa safi yatoka kwa wazazi
Manani hubarikia wenye malengo yalotimia.
Kisirani ni mjomba wa kiburi.
Najiona nimefika
Furaha imenifura moyoni
Nasahau bado siku haijaisha
Na laiti ningelijua aibu itayonipata ningeihonga
Ikanikalie mbali.
Nisijetoswa majini kwa kumkosa Habiba
Lakini digrii hiyo sina.
Nachunia usafiri wa teksi
Nadandia bodaboda, si nami nionekane nipo.
“Elfu tatu”dereva bodaboda anambia
“Kamua mafuta twende”naamuru kwa mikogo
Safari inazaliwa akilini namuwaza Habiba
CMG Motel ni mita mia saba toka nilipo
Mita mia kabla ya kujivinjari CMG Motel
Bodaboda kajisahau pikipiki kaitumbukiza dimbwini
Yalaa! Maji machafu,mvua ya jana yatwama hapo
Suruali na viatu vyaloa,rangi yabadilika
Balaa gani lanipata mimi.
‘Asalale!’ nang’aka kwa hasira
Pikipiki inakongojwa pembeni
Amani yangu yatumbikia tope la hasira
“We mpumbavu hivi…”najikuta tusi navurumisha
Sijui nifanyeje sasa! Nirudi au niende?
Najipapasa mfukoni kwa hamu simu kuitoa
Taarifa nimjuze Habiba atambue
Napo ndege ni mbaya kwangu
Simu ilishaniponyoka mfukoni
Wazo lanipandia-Imezama majini.
Daaa! Nashtuka kwa ghamu
Jaribu gani lanipata mimi
Mwana wa upendo mjukuu wa amani
Yanibidi kuifata hata kama kuzama dimbwini
Najitosa.Nimekubali hasara sasa.
Kabla sijatia maguu yangu majini
188
Ghafla gari‘Corola’ lilipotoka sijui
Liendapo hata sijichoshi kujua
Lisivyo na utu wala heshima
Lapita kwa kasi dimbwini
Maji machafu lanirushia.Mwili na nguo zalowa
Maji yanikogesha bila kunivua nguo
Sitamaniki.Nipo nyang’anyang’a.
“Kichwa kama gonkone!”namtusi mwenye gari
Uchungu umenikaba.Hasira zimenijaa
Mama mkwe siwezi muona sasa
Mashemaji siwezi waona pia
Ntawajibu nini?
Nitamwambia nini Habiba?
Simu ishapondwapondwa na gari dimbwini
Jameni nambieni.
Aibu hii nimpe nani mimi?
Najiresha nyumbani.Aibu yangu yote
Dunia imenihujumu nisiweze muona Habiba
Wizara ya ujenzi imenitia majaribuni
Halmashauri ya Tarime imedharau utu wangu
Miundo mbinu ya barabara imeraruka
Waona lakini wamejaa porojo kila leo!
Natupa laana yangu kwenu
Mmehujumu dibaja yangu kwa shemeji zangu
Dibaji yangu kwa mama mkwe wangu!
Haipo tena imekufa!
Nimtonye Habiba? Hapana.
Nitamjibu nini? Sijui.
Kesho yake asubuhi si mwenyewe kajivinjari
Kwangu na hasira zimemjaa pomoni
Hataki kunisikiliza
Nilidhamiria kuchuna anasadiki hivyo
Si wake msimamo akaubwaga
“Ni heri kudungwa na mwiba kuliko aibu hii.
Sikutaki tena maishani mwangu”
Hakutia mzaha akatoweka zake………
Zake na kuutupia moyo wangu gizani.
Sasa nalia na moyo!
Nitamuita nani Mahabibi?
Ataniita nani Mahabuba?
Bodaboda amelitia shubiri pendo letu
Amechochea moto penzi letu likateketea
Sina la kumlipa ila namwambia ‘Ahsante’
Wito na rai yangu ni tahadhari
Kinga ni njema tiba usiozee
Usijigambe leo kesho haina jina
Bodaboda ziepukeni japo ni rahisi
Wengi roho zimewatia kapuni
189
Huko kilio kule msiba
Hospitalini walemavu wamiminika
Yote ni kosa la bodaboda
Wilayani kwetu
Wahanga wa pikipiki wamekithiri
Wodi zimefurika wahanga wa bodaboda
Mji unatishika
Taifa linayeyuka nguvu kazi inapotea
Pikipiki inaua kuliko ugonjwa sasa
Tahadhari chukueni vizazi vyote
Kumbukeni usalama kwanza
Mengi tuyape baadaye
Nani atakulindia nyumba ukiondoka?
Nani atamlinda mwanao ukimpa uyatima
Nani atamfariji mkeo ukimuacha mjane?
Nani atamfariji mumeo ukimuacha mgane?
Bodaboda si salama!
Vunjeni chupa ya ukimya mseme!!
NDEGE SI NDEGE,MNYAMA SI MNYAMA.
Enyi wanadamu!
Hamueleweki mnataka nini
Mkipata mnachokitaka
Mwakana mnataka kingine.
Unaitwa kuwa mwalimu
Unafundisha uzalendo toka moyoni
Nasi twakuamini twakuiga
Muda kadhaa twasikia umesaidia kudonoa keki yetu
Sasa tukueleweje?
Unaimba na kughani amani
Unatia mfano unaongoza matembezi marefu
Siku chache jua halijatua
Unakuruta askari wanaingia msituni
Amani unaiua,msiba unabaki kwetu
Sasa tukueleweje?
Twapendana na dunia inajua hilo
Twawekeana viapo kupendana hata kwenye shida
Tunaponda raha pamoja,shida ikijivinjari
Unaruka kimanga,na kuanzisha pendo pengine
Nako unaweka nadhiri
Shida ikiwasili mfumo ni uleule
Unarukaruka kama chura
Sasa tukueleweje?
Kitu kidogo unachukua usiku86
Mchana kweupe waikemea
Tukikuuliza huna la kujibu
190
Unaahidi kuacha kesho unarudia
Sasa tukueleweje?
KIZUNGUMKUTI
Hatari!
Kizungumkuti kwa lidikteta
Alama za nyakati zikitimia
Mvua ya masika ya mabadiliko ikinyesha
Madarakani lafurushwa.
Nchi inazizima.Dunia inafunguka.
Tawala za haki na usawa zinaposimama.
Simanzi!
Jua linapopatwa
Taifa linatikisika,linafifia na linapotea kabisa.
Mfalme anapokufa
Anakufa na utukufu wa taifa lake!
Jaribu!
Umaskini unapokithiri
Maovu hujizalisha
Tufani hutawala nyumbani na mtaani
Wizi unachipuka
Elimu yazalisha wasomi tasa
Ukengeufu unakithiri
Magonjwa yanajitanda majumbani
Jaribu likikomaa laashiria kutoweka.
Furaha!
Miale inapopenyeza
Mabadiliko ya hewa yanaposimama
Upepo unakomba kifusi chote
Taifa jipya linazaliwa
Changa toka tumboni mwa……
Mwa mkulima mnyonge
Mwalimu mla vumbi la chaki
Mstaafu atangishwaye mafao yake
Ni taifa jipya la wazawa!
TUSIRUDI TULIPOTOKA.
Zamani kabla dunia haijaumbwa
Kulikuwa na ombwe kubwa
Hakukua na maisha
Ndipo.
Ndipo dunia ikaumbwa.
Amani ilitawala kila ncha ya nchi
Ustaarabu ulitawala hadi chini ya chupa
Miaka siyohesabika mbele
Tamaa ikatawala
Sisimizi akaingia na kulamba amani yote
Ukoloni ukazaliwa
191
Utumwa ukazaliwa.
Waafrika tukatumikishwa
Tukauzwa kama nyanya sokoni
Tukafungwa minyororo mizito
Mateso yakazidi kikomo
Harakati zikaanza uhuru wetu tukaupigania
Tukapata taifa letu
Leo ni miongo kadhaa imepita
Sisimizi aliyekufa amerudi tena
Anailamba amani taratibu
Matabaka yanajenga tena
Ukoloni umerudi na sura mpya
Ya wenye na wasio nacho
Daraja linakua!
Ukiwa nacho unatawala dunia
Usipokuwa nacho unakoma kuringa
Unamtegemea akuokoe
Anatumia hitaji lako kukukamua
Hali inazidi na mwisho tunarudi dunia ile
Jamani,tusirudi tulipotoka.
BUNGE LA WAHUNI.
Lugha yangu ni Kiswahili
Yataifa yaniunganisha popote niendapo
Lakini hivi majuzi nikajikuta taabani
Mawazoni nikiogelea
Maswali bila majibu
Lugha hii siijui au ni bunge la wahuni?
Bunge la wahuni na wachafuzi wa lugha
Si akaja kijana
Wenzie watano wamekusanyika
Si hapo maajabu nilipoyaona
Akaanza
Masela mishe vipi?
Leo na mchongo mzito nawashushia
Pande zile nazo dozi mimi si msala wa kufa mtu
Shoka likabriki mpini ukastick
Njemba mtoto wa majalala
Si kamlia mingo kinda la kidosi
Madini kamtemea si manzi akaitika.
Huwezi amini,mshua wa demu akazidaka nyeti
Kinda wake anazodolewa na mjalala mmoja hivi
Daaa! Jogoo hajafanya mambo yake
Dingi si akatua geto na mguu wa kuku
Akamsalia mchizi na kumwagia woning’
“Nisikuone wala kusikia unatembea na mwanangu.
Lasivyo nitaitumbukiza risasi moyoni mwako!”
Usiombe mdosho akasepa na kuacha nongwa kitaa!
192
Nikajiuliza alikuwa anongea nini
Si mwenzake akasikika akisema
Chili,chili,nikupe data hizo hizo za mademu
Si unamdaka demu wangu Salome?
Wenzake wakajibu“Sana tu!”
Nikabaki najiuliza ‘sana tu’ nini?
Akaendelea!
Hivi majuzi aliniletea swaga za kijingajinga
Anadai eti nilimpiga upepo
Kitumbo kinamuuma,samaki hawamaindi tena
So anahisi ana kijazuzito
Nikahisi ananichawia tu
Palepale nikabriki karilesheni
Nikamwambia“Kama hutakitoa kijusi hicho.
Sipo tayari kuitwa baba”
Si akatia nyodo na mimi ndiye nguli wake
Nimempiga chini!
Ghafla vicheko vikaripuka
Kila mmoja akamgongea mwenzie mkono
Najikuta naduwaa na kamchezo hako!
Mwingine naye anatema yake
Mazito kuliko hata zege lililolala
Hivi majuzi basi soo likanipenda
Nimedamka mida ya jogoo mfukoni sina kitu
Nikaona isiwe nongwa
Si nikajitupia viwalo hadi mtaa wa kati
Huko kuna kibosile mishe zake si za kuajiri mayanki kupora
Nikafunga mkataba akanipa misheni
Nimuibukie na mguu wa kuku manzi mmoja
Yasemekana alikuwa kipoozeo chake
Nami si nikafanya hivyo
Duu! Manzi mwenyewe wa ukweli
Huwezi amini.Nilipomuona nilipagawa
Nikamdetail eksi wake ameniagiza nimtoe roho
Kusikia hayo Manzi akabwaga chozi
Naye akanijibu“Sema unachotaka nitakupa.
Napenda kuishi.Niachie maisha yangu!”
Akatulia,si akawauliza wenzake swali
Swali ambalo wote walijibu kwa mpigo
“Unajua nilidisaidi nini?
“Kula nyapu!”
Sikutaka kuendelea kukaa hapo tena
Nikaondoka!
Sijui lugha gani haswa waliyokuwa wakitumia
Ni Pijini? Krioli? Au Vizalia?
Haieleweki!
193
Vijana mnafanya nini?
Lugha gani hizo?
Kweli hilo ni bunge la wahuni.
KARIBU MWANANGU!
Karibu sana
Ndani ya ulimwengu huu
Ni chereko nyumbani na moyoni
Twamshukuru Jalali umezaliwa salama
Mimi ndiye baba yako
Huyu ndiye mama yako
Sote tunafuraha isopimika
Twakukaribisha tena nyumbani.
Mwanangu!
Dunia hii ni jino mfupa
Ukiwa tumboni mwa mama yako
Ulikuwa safi
Lakini unapotoka tumboni
Na kuja dunia nyingine
Unatunukiwa hatia usoiona
Tambua hilo.
Yapo mengi mwanangu
Yasikitisha na kuchosha moyo
Duniani tunaishi na majirani wa kutegemewa
Magonjwa,chuki,dharau na masimango
Fitina,uongo,unyonyaji na makandamizo
Lakini!
Unapokuja duniani jua vita tunayo haijaisha
Kila siku twavaa magwanda na silaha mkononi
Amani kuipigania
Usishangae!
Karibu mwanangu.
Chonde chonde mwanangu!
Nje ya nyumba yetu kuna lijinamizi
Linalonyonya na kuacha vipele
Linalolowanisha nywele na kuzipukutisha
Linalonyanyua kenchi za begani
Linalokomba mwili hata damu
Limezalisha wajane kila limvamiaye
Laacha uyatima wazazi wapukutika
Jihadhari!
Halionekani lakini lipo kati yetu
Tiba yake ni moja
Badili tabia na mwenendo!
Mwanangu!
Chapa ya hatia ulotunukiwa unapozaliwa
Haitokutoka hadi mwisho wa dahali
Usijeshangaa ukatupwa jela bila kosa
Kuna wengi twawajua wapo huko
Hawana makosa wanaozea gerezani
194
Wenye hatia warandaranda kama popo
Nikutajie?
Subiri ukue utayaona
Picha zao za udhalimu wao ninazo
Ukiziona na kusihi usiseme kitu
Ila
Chukua hatua thabiti
Chukua mabadiliko ya kujenga
Tafadhari yajue hayo!
TWENDE TUKAWINDE
Tukawinde mbu arukaye kwa roketi
Apigaye mbawa zake kila uwio
Na kutoa mahadhi ya kifu arukapo
Maghorofani azidi kujining’iniza pembeni
Sakafuni ajitundika kutani.Oneni
Ofisini ajibanza kati ya karatasi nzito
Na nyepesi zilizorowa chai ya machozi
Njooni kote tukamwinde.
Huko
Msife moyo!
Milima ni mizito upepo ni kitanzi
Shikeni moyo marungu kuyafumua
Fimbo nzito ziwe mikwaju
Yakujikongojea bahari ya uonevu kuivuka
Jinamizi nyonya jasho na damu yenu
Lipo linajineemesha kwa keki na siagi
Tukilifuma!
Msihoji.Pigieni lipigeni
Life
Lifanyeni mshikaki wa ungaunga
Majivu yake ndo ushindi wetu
Tukirudi salama nyumbani
Silaha msizitupe koridoni
Kesho napo
Kuna lindo la toa roho,fakiri apone
Twendeni tukaliwinde
Dume la nyani lilokubuhu
Kupokonya mahindi yetu shambani
Likicheka pasua kichwa chake
Likinuna kata shingo lake
Likiomba msamaha piga mishale
Onyo na fundisho
Matoto na mate yake yatahama msitu
Ikiwa hivyo
Lindo limefanikiwa!
KWA JIRANI YETU!
Baba amka! Amka!
Mama amka! Amka!
Kaka amka! Amka!
Dada amka! Amka!
Jamani amkeni nawasihi.Amkeni!
195
Kwa jirani kuna balaa limeshika hatamu
Amkeni msikilalie kifo.
Jongeeni dirishani mjionee.
Katikati ya ufinyu huu wa pazia
Kule! Kule kwa Mzee Owadwa
Moshi unarandaranda juu angani
Nyumbani pake pana moto unapikika
Yowee apiga.
Msaada wa moto kuuzima,aomba.
Lakini
Msiende.Mzee Osito sijumuona
Akienda toa msaada nao ni majirani
Wasiwasi wanizonga,begani na mzigo
Mkienda nawaambia:
Mzee Owadwa atafaidika na uingilio wenu
Lawama,shutuma na lalamishi
Atazisukuma kwenu
Mmeenda kumendea mali zake amana
Si kumsaidia moto kuuzima
Unajua kwanini?
Chokochoko za moto kaziwasha mwenyewe
Hamjaona?
Angalieni tu dirishani msiende.
Amkeni!
Kwa Mama Sikitu
Kuna uvamizi wa silaha unafanyika
Msilale sasa vaeni gwanda
Mjomba shika upinde na mshale
Kaka chukua sime
Baba ile bunduki usisahau
Mama nawe chukua kisu
Tunyatie polepole nje tutoke
Majizi ya mali tuyaangamize hadi kifo
Mama Sikutu tumsaidie
Leo Mama Sikitu,kesho kwetu.
Tumlinde mwenzetu lakini
Tusisahau na nyumbani giza ni zito
Macho yetu yasimame
Huku na huko tusijevamiwa.
Jirani ameuguliwa dawa peleka
Jirani amefurukiwa hema peleka
Jirani ana njaa chakula tumpe
Jirani ana kiu maji safi tumpe
Jirani ni jirani mtu wako wa pili
Jirani ni mimi na wewe
Jirani ni nchi nyenzako!
NI LINI NA WAPI?
Najiuliza safari ndefu nendayo
Yenye dhoruba na vingi vijaruba
196
Vunja moyo na simanzi begani
Isoisha kila safari nayopiga
Kutoka hapa kwenda pale
Asipopajua binadamu awaye nani
Ila yeye aliyeziumba na kuzimiliki
Nchi na mbingu na kutia vidole vyake
Ajua fumbo hili
Ni lini na wapi?
Ntafika mimi.
Nainua mikono juu mja wako
Najisalimisha unione kama ulivowaona wale
Unipe leo mkate wangu wa maisha
Tufani ijapo nivuta huko na huku
Mawimbi ya bahari yajapo kisuka chombo
Kwa karima zako utaniweka imara
Nami hujiuliza bila kukoma
Kwani mi ni nani uniangalie?
Kwani mi ni nani nikusahau?
Kwani mi ni nani nijisifu?
Ni we wajua maana uliniumba
Safari ulonianzishia ni we pekee wajua
Ni lini na wapi itaishia!
Kilio changu ni kimoja
Maisha haya ni mazito mno
Kuliko kontena bandarini
Kila kukicha wahesabu tarehe ya maisha
Kila kukicha majanga yazidi niandama
Kila kukicha vilio ni vilevile
Kona yote duniani
Kila kukicha sijui jioni itakuaje
Nipe moyo wa ujasiri
Mapito haya kushinda
Ewe Mola wangu mmiliki wa vyote
Mmiliki wa maisha na kifo cha mwanadamu
Mmiliki wa amani na mfariji mkuu duniani
Nakusifu na kukuheshimu,Amina
Ni we pekee wajua ni lini na wapi
Mimi Akech nitakuwa kesho ikigonga hodiHaleluya!
NYAKO MA ERO AINYA (Msichana Nnayempenda sana)Ni msichana aliyeshushwa toka mbinguni
Mwana wa Adamu aliyetunukiwa shada ya uzuri
Mvuto wa sura na umbo kama la malaika
Atembeapo.Waume kwa wake macho kwake
Mwenye sauti nyororo kama ya kasuku
Anipoozaye moyo maji ya kiu yangu
Ni msichana ninayempenda sana!
Ni msichana anayejua ndugu na wageni
Mkarimu na pambo la nyumba yangu
Aing’arishaye nyota ya uaminifu
197
Machoni nikimuona hana mafamba
Mkweli hata ibilisi anatetemeka akimuona
Ni msichana niyempenda sana.
Ni msichana anayeimiliki dunia
Rafiki yake mkubwa ni amani
Shoga yake mkubwa ni upendo
Shosti yake mkubwa ni uvumilivu
Ajue nilichonacho asinakili nisichonacho
Nalala chini ajue ni mpito tu
Tunakula ugali na dagaa,ajue
Twashiba na bado tunaishi
Ni msichana niyempenda sana.
Ni msichana mwenye macho ya mduara
Madogo mazuri yakuibia hisia
Shingo ndefu kidogo ya pingilipingili
Ngozi laini ya kuishinda sufi
Mwenye pumzi ya moyo wangu
Uwapo jirani nami
Moyo wangu uogelee kwenye maji ya sura yako
Ni msichana ninayempenda sana!
WIMBO ULIO BORA
Wimbo ulio bora
Huimbwa baada ya kazi
Hudunduliza hisia za kweli
Hukonga nyoyo za ushujaa
Ni ule unaochochea badiliko la kweli.
Wimbo ulio bora
Si wa nyokonyoko wala ugeugeu
Si wa kupumbaza wala kughadhabisha
Ni ule unaoparara puya!
Wimbo ulio bora kuimbika
Si ule unaoabudu rushwa na hongo
Si ule unaazima mawazo ya wanyang’anyi
Ni ule unaokidhi shauku ya tahadhari.
Wimbo ulio bora
Haunyofoi furaha ya mafakiri
Walimu,wanafunzi kutandazwa nao barabarani
Kumuimbia mwenye hazina apitaye na gari kwa kasi
Kunakucha,lakini Mheshimiwa akatiza jioni
Ni ule utakaokemea vikali dharau hizo.
Wimbo ulio bora
Si ule unaotukuza taifa kuparaganyika
Si ule unaotukuza maasi barani
Si ule unaosifu ujinga wa watawala
Si ule unaokiuka na kutetea unyanyasaji
Ni ulotukuka kwa tashtiti ya uzalendo,utu na ukemi!
198
Wimbo ulio bora
Si wa kuimbwa na mdomo,bali moyo
Si wa kusemwa na maneno,bali matendo
Si wa kusujudu utumwa,bali uhuru
Si wa sukuma twende,bali wa msimamo kina
Ni ule unaofikia haja ya ndani ya hadhira yake.
MAFAMBA
Wewe ni bosi wa idara
Umepewa dhamana ya rasirimali watu
Unapaswa kuandaa vocha za malipo
Vocha ya malipo ya wafanyakazi wako
Unazilisha majina mengi yasokuwepo
Malipo yanatoka unakula cha hila yako
Hiyo ni mafamba.Acha!
Wewe ni waziri wa nchi
Unaruka na mamilioni yetu kwenda ulaya
Unakunywa chai ya kikombe kidogo hotelini
Unalewa.Unasinzia unasaini mkataba kandamizi
Wazawa wanapokonywa chao
Mwekezaji ananyonya malighafi zetu
Unalijua hilo.Unanyamaza kimya
Unaogopa kuaziliwa kwa chai ulokunywa
Hiyo ni mafamba.Acha!
Wewe ni mzee wa ukoo
Unakosea kama binadamu
Kijana anakurekebisha kiungwana
Unaitisha baraza la wazee
Unatishia kumwagia razi kijana huyo
Eti hana nidhamu kwa wakubwa.
Hiyo ni mafamba.Acha!
Wewe ni kiongozi wa kimila
Unaitisha mjadala wa kimila
Unaamuru kila ukoo ukuletee mfugo mmoja
Unaletwa unachinja
Unakula we na mke wako
Ndugu wakija juu
Unatishia laana itawatandika
Nasaba zao za pili hazitoishi abadani
Hiyo ni mafamba.Jiangalie!
Wewe ni kijana mdogo
Unakaa kijiweni ukivuta bangi
Jua lachomoza,lazama,we na bangi
Kesho unashutumu umerogwa
Unawaona walojituma wakapata,
Ndio wachawi wa maendeleo yako
Hiyo ni mafamba.Acha!
199
Wewe ni mpenzi wangu
Nakupenda sana nawe wajua
Watembea na rafiki yangu mi sijui
Wanisaliti usiku na mchana
Ukiwa nami wajichora kunipenda
Hiyo ni mafamba.Acha!
Wewe ni mke wa mtu
Ndoa ni heshima ya mume na mke
Unarukaruka na vijana wadogowadogo.
Wadogo rika la mdogo wako
Umekosa muhamana wa penzi lenu
Mumeo unampumbaza kumpenda
Hiyo ni mafambo.Acha!
Wewe ni mwanasiasa
Unaporoja jukwaani:Tumaini jema kwa wote
Tunakuchagua ututumikie.
Unatumia vyetu ovyo kutunisha tumbo lako
Tukihoji unapuuza madai yetu
Unatujibu utakavyo.
Hiyo nayo mafamba.Acha!
Wewe ni mwanafunzi
Unakosea unarekebishwa unafyumu
Unachonga kinyongo kikali dhidi ya mwalimu wako
Unamvizia njiani unampiga
Unamuumiza kesho unarudi shule
Hiyo ni mafamba.Acha!
Wewe ni kiongozi wa dini
Una waumini waadilifu
Wanatoa sadaka kujenga hekalu
Usiku unaiba sadaka
Mchana unarudi kuhubiri tena michango
Unawanyonya maskini na wizi wako
Hiyo ni mafamba.Acha!
Wewe ni mwalimu
Unadhamana ya kutoa maarifa
Unatumia chaki yako kupotosha jamii
Uongo unaupaka rangi uwe ukweli
Ukweli unaudidimiza
Unamlindia fulani maslahi
Hiyo mafamba.Acha!
Wewe ni baba mwenye nyumba
Nakulipa kodi yako ipasavyo
Unanipandishia kodi nje ya mkataba
Shutuma ni nyingi zisizo na msingi
Kidogo unajilia familia haijui
Hiyo ni mafamba.Jiangalie!
200
Wewe ni daktari mhodhi wa afya zetu
Dawa zipo hospitalini twajua
Twagonjeka twaja kwako kutibiwa
Unatuandikia vidonge unajua ziliporwa muda
Unatusihi kuzipata duka la tatu
Lenye muamala na wewe
Unadhani hatujui
Hiyo ni mafambo.Badilika!
RAMLI YA TAIFA (Nalipita pembezoni mwa mji)
Moyoni nimechoka kadhia yanilemea
Naliona bango chakavu limetundikwa
Katikati ya miti miwili mikubwa
Najaribu kulisoma!
Mganga wa Jadi mashuhuri yu nchini
Ametua nchini kutatua matatizo yako
Tabu na adha zikupatazo.
Magonjwa anayotibu:
1.Kisukari
2.Kifua kikuu
3.Ukimwi
4.Miguu kujaa maji
5.Surua na pepopunda
6.Magonjwa ya zinaa.
Nafinya macho sielewi kinachotibiwa hapo
Navuta pumzi huenda kadhia yangu
Yanizibia uhuru wa kufahamu tangazo hilo.
Naendelea kusoma.
Matatizo anayotatua
1.Kupendwa
2.Kurudisha mpenzi aliyepotea
3.Kupata pesa haraka
4.Kuondoa mkosi kwenye biashara
6.Kuzindika nyumba.
Najikuta natabasamu sasa
Tabasamu la kusikitikia tangazo hilo
Lenye mvuto lakini la kilaghai
La kuwaibia wazawa hadi kidogo chao!
Mwishoni navutiwa na maneno haya
TUNAPIGA RAMLI UKITAKA!
Navuta usukani najiondoa eneo hilo
Narandaranda barabarani nikiwaza kwa kina
Nawaza.
Kwanini taifa letu tusilipigie ramli?
Ramli isiyo msujudu sangoma
Ramli ya kutatua matatizo majanga nchini
Ramli ya kuvunja visasi
Ramli ya kuagua gonjwa la rushwa
Ramli ya kutokomeza usaliti
201
Ramli ya kusambaratisha matabaka
Ya akina hohehae na ya akina hohihai
Ramli ya kukemea uongo wa viongozi
Ramli ya kuleta umoja wa kitaifa.
Ramli! Ramli! Ramli ya taifa!
Nashtuka!
Nipo katikati ya mji
Natanabahi ramli nayo ni ulaghai
Ulaghai ulosukwa kiustadi na mganga mwenyewe
Daaa! Nang’aka kusadiki nimeokoka
Kutoka kwenye domo la utumwa wa kifikra
Tiba ya taifa langu siyo ramli
Ni umoja wa taifa ndani na nje
Ni mshikamano ndani na nje
Ni uadilifu kazini
Ni ukweli wa tutendayo
Ni kuchukia dhambi ya mirungura toka moyoni
Ni uzalendo wa kufa na kufia nchi
Ni usawa wa watu nchini
Na hizo ndizo ramli aminifu kwa taifa letu.
INAPOTOKEA
De
Degedege likimvagaa mtoto
Wazazi hofu huwatanda
Hospitalini watangatanga
Tiba thabiti kumtafutia
Uchungu mwana kumpoteza,furaha gonjwa likikoma.
Lakini.
Degedege likipenyeza taifani
Wazalendo roho juu juu
Machozi mazito kuwatoka
Watoto huomboleza amani imekufa
Wamama huangua viilo vikali
Wazee hujikunyata.
Lo! Wanasiasa uchwara macho huwatoka
Huajiri hadi ughaibuni,usalama kujiongezea
Familia zao salimini,wazalendo kizaazaa
Tufani ikipumzika,nchini hurejea
Mabavu hutumia madaraka kujitwalia
Degedege lajipenyeza tena taifani!
Mo
Moshi ukifuka,nyumba imeungua
Majirani hujikusanya,maji kumwagia
Mitikisiko ikiendelea,maisha’po rehani
Uchumi gizani,umaskini usukanini
Taifa likisinzia tu
Wazawa kekundu wameshaliwa
Moto ukionekana,amani ishatoweka!
Ila.
202
Moja ikizidi moja,mbili hutokea
Maisha ukiyaanza leo,kesho uwe mwendelezo
Nyuma usigeuke,dahari kuna furaha
Tamaa siisikilize ni mjomba wa poromoko
Bidii ipe mashiko,mafanikio yakujie pekee
Moja ikizidi moja,idadi yaongezeka!
Ki
Kichinjaudhia ikikwama kuponya kichwa
Fikra hugonga mwamba kubaini
Mvua ikishuka bila kikomo kichwa hupoa
Adha za maisha zikitulia loa mafanikio
Ngalawa ya maisha ikusukwasukwa
Kichwa huwanga bila kikomo
La kheri ni kuvaa boya
Mbizi kuipiga hadi pensula ya heri
Lakini.
Kichinjaudhia ikithubutu kuponya kichwa
Kidurango huwa mrefu tena
Mbele hutambua jitihada huamua
Maisha kuyavalia njuga kazi kuifanya
Pepo za kusi zikiyumbisha ngalawa
Machafuko ya bahari hupoa
Kichinjaudhia ikitia nguvu,maisha yanarudia ahueni.
Ra
Radi ikipiga,kifo kimeacha
Tanzia itasikika mtaani kuna msiba
Tukahani kilioni wafiwa tuwafariji
Vurumai yachipuka.Matusi yavurumushwa
Ndugu,majirani washuku radi ni mkono wa mtu
Amani ikitoweka mtaani hapakaliki
Niwinde nikuwinde.Nipe nikupe!
Mfumo mpya wa visasi utatawala,
Ardhi itanyonya damu zisizo na hatia
Radi ikipiga tena.Mvua ya mawe itanyesha
Damu ikichujika udongo utanuka vifo.
Jema ni.
Radi ikipiga,dunia itakoma kuringa
Ngurumo zikitetema ndege watarudi ardhini
Vitoweo bwerere manati haitumiki
Wazalendo watacheka chaguzi zitatii amani
Viongozi watatii jina la demokrasi
Uchumi ukilegea,bolt watakaza
Radi ikitandika.Ukweli utajulikana.
Si
Sibu ya umaskini ikikithiri
Nchi itayumba na kujifia
Mdororo ukizidi kukua
Wenye nacho watageuka miungu watu
Mafukara watalamba michuzi ya chini
Mbwa watagombania kidogo alichotupiwa fakiri
203
Tifu lake litaleta chachu ya maamuzi
Hatimaye.
Sibu ya ukombozi itashika hatamu
Taifa talipigania ili lisipotee
Miungu-watu tutayatwanga shoka ya kichwa
Yakifa huo ukombozi wa kweli
Shuka la tabaka taliteketeza moto
Sote tajifunika blanketi la usawa na undugu
Sibu ya ukombozi ni kuwa na taifa jipya.
MWANZO MWISHO
Unazaliwa
Unakua
Unabalehe/unavunja ungo
Unaoa/unaolewa
Huoi/huolewi
Unazaa/huzai
unazeeka
Unakufa
Unasoma/husomi
Unahitimu/huhimu
Unaajiriwa/huajiriwi
Unastaafu/unaacha kazi
Unaranda mtaani/unapumzika nyumbani
Yote yamekwisha
Unagombea/hugombei
Unachaguliwa/huchaguliwi
Unatimiza wajibu/hutimizi wajibu
Unang’atuka/unavurumshwa
Mageuzi kamili yatokea
Unapenda/hupendwi
Unasaliti/husalitiwi
Unatengana/wasamehe
Unaishi kikapera/unaishi kiseja
Mwakutana tena
Mwasahau na kusameheana
Unacheka/unalia
Unatabasamu/unanuna
Unafurahi/unasikitika
Unalumbana/Una patana
Changamoto za maisha.
DINI
Dini hueleweki! Una matatizo gani hasa?
Dini husitiriki! Umekuwa tuzo duni tasa
Dini hukumbukiki! Umeteta watoto wako!
Dini huchukuliki! Walokuleta wamekukimbia
Dini hukumbuki! Walokupata umewaharibia
Dini hubabaiki! Unatupepeta unatuchafua
204
Dini maaskofu! Wamekutetea umewazingua
Dini waongofu! Wamekulea umewaibia
Dini mashehe! Wamekupigania mama
Dini wahehe! Walikutambua zama
Dini balehe! Umeikosea hama
Dini wazee! Mitini walikuhifadhi
Dini amani! Mjini uligawa ardhi
Dini wa leo! Chupa sawa
Dini kileo! umetupa dawa?
Dini wanasiasa wamekutumia
Dini walimu wamekubabaikia
Dini wakulima wamekupapatikia
Dini madreva wamekupakia
Dini chakula tumekupikia
Dini kijiji umekichafua
Dini wanakijiji umetutifua!
NGAO
Ni ngao vitani vita nyumbani
Vita ya hapa mjini
Vita ya ukapa
Vita iso mipaka
Panya na paka
Wote wanataka
Kukaa jikoni
Kupaa angani
Kukaa kitini
Kiti kile kimoja
Kinamtosha mmoja
Paka anangoja
Panya anangoja
Wanajifanya wana hoja
Wote wakosa
TAMATI!
Tamati!
Kila kitu tamati
Machungu ya maisha tamati
Madhila ya mapenzi tamati
Tamati! Tamati!
Tamati!
Kila kitu chatamatishika
Uongo wa wanasiasa tamati
Dharau na chuki tamati
Maisha yanasimama
Giza linashuka
Kifo! Kifo kila kiumbe duniani
Tamati! Tamati! Tamati
205
MAREJELEO
Abby, C. na Billy Seba (2011) “Kashfa Nzito Part. 2: ni ile ya wasanii wa Bongofleva Kukosa nauli,”
Ijumaa Weekenda, Julai 04, 2011, Dar es Salaam: Global Publishers, uk.9
Abdalla, A. (1973) Sauti ya Dhiki, Nairobi: Oxford University Press.
Abedi, K. A. (1954) Sheria za Kutunga Mashairi na Diwani ya Amri, Nairobi: Kenya Literature
Bureau.
Abrams, M. H. (1981) A Glossary of Literary Terms (4 th Ed.), USA: Holt Rinhart na Winston.
Adejeji, J. (1969) "Traditional Yoruba Theatre," African Arts 3.1 (Spring): 60-63
Ajayi, J.F.A. (1999) Historia Kuu ya Afrika: Afrika kwenye Karne ya Kumi na Tisa hadi Miaka ya
1880, Dar es Salaam: TUKI.
Akilimali, K. H. A. (1971) Diwani ya Akilimali, Dar es Salaam, Nairobi na Kampala: East
African Literature Bureau
Akivaga, S. K. na Odaga, A. B. (1998) Oral Literature, Nairobi: Sunlitho Limited.
Alembi, E. B. (2000) Understanding Poetry, Nairobi:Acacia Publishers.
Alipo, J. (2011) “Mitulinga Basi’ Prof. Jay” katika FEMA, July-September, 2011, Dar es Salaam:
FEMINA HIP, Uk. 4 – 6.
Ally, S. (2003) “Wasanii wa Hip hop Wanakaribia Kukitia Mchanga Kitumbua Chao, Nyimbo
Za Mipasho, Majungu Yamezidi, Uwezo Mdogo Roho Mbaya Ndio Chanzo,” Bingwa,
Juni, 3, 2003, Dar es Salaam: Bingwa Newspaper Limited. Uk. 9.
Ayisi, E.O. (1972) An Introduction to the Study of African Culture, Nairobi: East African Educational
Publishers.
Bongo Celebrity (2011) http://www.wahapahapa.com iliyopakuliwa tarehe 22/08/2011
Bowra, C.M. (1952) Heroic Poetry, London: Clarendon Press.
315 – 354.
Bukenya, A. S. na Wenzake (2000) Understanding Oral Literature, Nairobi: Longhorn
Publishers (K) Limited.
Bynoe, Y. (2006) Encyclopedia of Rap and Hip Hop Culture, London: Greenwood Press.
Campbell, L. (1993) Michael Jackson: The King of Pop, New York: Branden.
Chachage, C. S. L. (2002) “Ndani ya Bongo: Utamaduni na Migogoro ya Utamaduni,”
Paper presented at the Tenth Conference on the Political Environment in
Tanzania, 17TH – 18th September, Dar es Salaam.
Chiraghdin, S. (mh.) (1977) Malenga wa Mrima: Tungo za Mwinyi Mohamed, OUP: Nairobi.
Cohen, N. (1993) “Worksongs: A Demonstration Collection of Examples,” katika Archie Green (mh.),
Song About Work: Essays in Occupational Culture, 332 -356, Bloomington: Indiana
University.
Coupland, R. (1938) East Africa and Its Invaders, Oxford: Clarendon Press.
Cuddon, J.A. (1998) Dictionary of Literarry Terms and Literary Theory, Great Britain: Andre
Deutsch.
Curran, J. (2000) Pagan City and Christian Capital, Oxford: Oxford University Press.
Dunleavy, D. (1992) The Language Beat, Ontario: Pembroke Publishing House.
El Kaiim, M. F. S. (1985) Ufasaha wa Ushairi, Nairobi: Kenya Literature Bureau.
Fiesta (2011a) “Vumilia Abrahamu Braham: Matarajio Yangu ni Kuwa Mwanamuziki Bora Afrika
Nzima,” Aprili – Mei, 2011, Dar es Salaam: Jamana Printers Ltd, Uk. 25 – 27.
________ (2011b) “Mr. Ebbo Alia na Wasanii Wanaopenda Kuiga,” Aprili – Mei, 2011, Dar es
salaam: Jamana Printers Ltd, Uk. 27.
________ (2011c) “H-Baba Aponda,” Aprili – Mei, 2011, Dar es Salaam: Jamana Printers Ltd,
Uk. 27.
Finnegan, R. (1970) Oral Literrature in Africa, Nairobi: Oxford University Press.
________ (1977) Oral Poetry, Its Nature, Significance and Social Context, New
York/Melbourne: Cambridge University Press.
_______(2007) The Oral and Beyond: Doing Things with Words in Africa, Chicago: The University of
Chicago Press
George, V. (2010) “Wamasai Watakiwa Kuacha Ukeketaji,” Mwananchi, Tarehe 24 Novemba,
206
2010, Dar es Salaam: Mwananchi Communicatins Ltd.
Gibbons, B. (1980) Romeo and Juliet. The Arden Shakespeare Second Series, London: Thomson
Learning.
___________ (1993) Shakespeare and Multiplicity, Cambridge: Cambridge University Press.
Goldstein, J. (2005) The Real Price of War: How You Pay for the War on Terror, New York: NYU
Press.
Grady, H. (2001a) "Modernity, Modernism and Postmodernism in the Twentieth Century's
Shakespeare," katika Bristol, Michael; McLuskie, Kathleen, Shakespeare and Modern
Theatre: The Performance of Modernity, New York: Routledge.
___________ (2001b) "Shakespeare Criticism 1600–1900", katika de Grazia, Margreta; Wells,
Stanley, The Cambridge Companion to Shakespeare, Cambridge: Cambridge University Press.
Gunderson, F. (2010) Sukuma Labour Songs from Western Tanzania: We Never Sleep We
Dream of Farming, Leiden/Boston: Brill.
Haggard, H. (1885) King Solomon’s Mines, London: Good Cause.
Harries, L. (1962) Swahili Poetry, London: Oxford University Press.
Haskins, J. (2000) One Nation Under a Groove: Rap Music and its Roots, New York: Hyperion
Books.
Heidegger, M. (1971) Poetry, Language, Thought, New York: Harper & Row Publishers.
Innes, G. (1974) Sunjata: Three Mandinka Versions, Londo: SOAS.
Itandala, A. B. (1983) “A History of the Bazinza of Usukuma, Tanzania,” PhD. Dissertation
(Haijachapishwa), Dalhousie University.
Jamieson, K. M. (1975) "Antecedent Genre as Rhetorical Constraint," Quarterly Journal of
Speech, London: Taylor and Francis Group, 61: 406-415.
Johnson, J.W. (1978) “The Epic of Sunjata: An Attempt to Define the Model for African Epic
Poetry,” PhD Dissertation, in 3 vols., Bloomington: I.U Press
__________(1986) The Epic of Son-Jara, Bloomington: I.U. Press.
Kabuta, N.S. (1997) “Isimu-Ushairi: Muundo wa Majigambo,” katika Nordic Journal of African
Studies 6 (1): 36-60.
Kahigi, K.K & M. M. Mulokozi (1973) Mashairi ya Kisasa, Dar es Salaam: Tanzania Publishing
House.
__________ (1979) Kunga za Ushairi na Diwani Yetu, Dar es Salaam: Tanzania Publishing
House.
Kanuri, J. na wenzake (2008) Mwongozo wa Mayai Waziri wa Maradhi na Hadithi Nyingine,
Nairobi: NES.
Keyes, C. L. (2002) Rap Music and Street Consciousness, Urbana: University of Illinois Press.
Kezilahabi, E. (1988) Karibu Ndani, Dar es Salaam: DUP.
Kimani, N. na Wenzake (wah.) (2006) Fasihi Simulizi ya Kiswahili, Nairobi: Twaweza
Communications.
King’ei, K. na Catherine Kisovi (2005) Msingi wa Fasihi Simulizi, Nairobi: Kenya Literature
Bureau.
Kisanda, H. (2010) “Wasanii Bongo na Thamani ya Big,” http://www.globalpublishers.info
Iliyopakuliwa tarehe 13/07/2010.
Kisanda, H. na Gladness Mallya (2011) “Bob Junior, Diamond, Wema Vita Nzito,” Amani,
Tarehe 14 April 2011, Dar es Salam: Global Publishers, UK. 9.
Kitangoma (2011a) “Sanaa Imegeuzwa Chombo cha Starehe na Kutukuza Anasa,” Aprili - Mei, 2011,
Dar es Salaam: PrimeTime Promotions Co. Ltd., Uk. 7
___________ (2011b) “20% Sipendi Sifa Bila Ushahidi,” Aprili - Mei, 2011, Dar es Salaam:
PrimeTime Promotions Co. Ltd., Uk. 20-21.
__________ (2011c) “Lugha Yetu ya Taifa ina Vionjo Vingi Wasanii Tuitangaze,” Aprili – Mei,
2011, Dar es Salaam: PrimeTime Promotions Co. Ltd., Uk. 22-23.
__________ (2011d) “Ombaomba ya Wasanii Inatia Kinyaa,” Aprili - Mei, 2011, Dar es
Salaam: PrimeTime Promotions Co. Ltd., Uk. 31.
Koponen, P. (1988) People and Production in Late Pre-colonial Tanzania: History and Structures,
207
Helsinki: Finnish Society for Development Studies.
________ (1995) Development for Exploitation: German Colonial Policies in Mainland Tanzania
1884 – 1914, Helsinki: Finnish Historical Society.
Kineene wa Mutiso (2005) Utenzi wa Hamziyya, Dar es Salaam: TUKI
Lenski, G. (1974) Human Societies: An Introduction to Macrosociology. New York: McGraw- Hill,
Inc.
Little, M. (1987) “Native Development” and Chronic Malnutrition in Sukumaland, Tanganyika 1925
– 1945, PhD Dissertation (Haijachapishwa), University of Minnesota.
Lissah, C. (2007) “Najuta Kuacha Shule-Mr. Blue”, Uwazi, Tarehe 24-30 Aprili 2007, Dar es
Salaam: Global Publishers.
Lo Liyong, T. (1972) Popular Culture of East Africa, Nairobi: Longman Kenya
Lord, A. (1981a) The Singer of Tales, Cambridge: Harvard University Press
____________(1981b) “Memory, Fixty, and Genre in Oral Traditional Literature,” in Foley (mh.):
451 – 61.
Mahenge, E. (2009) “Bongo Fleva ni Uasi au Sanaa za Maonyesho?” Makala Iliyowasilishwa katika
Tamasha la Elimika na Bongo Fleva, Januari 16 – 17, 2010, Chuo Kikuu cha Dar es salaam.
Mair, L. (1964) Primitive Government, London: Penguine Books.
_______(1965) An Introduction to Social Anthropology, Oxford: Clarendon Press.
________(1979) African Societies, Cambridge: Cambridge University Press.
Majembe, A. K. (1998) “Language Use in the Tanzanian Hip hop Scene” Unpublished Research
Paper, UDSM.
Mangesho, P. (2003) “Global Cultural Trends: The Case of Hip hop Music in Dar es Salaam,”
MA Dissertation (Haijachapishwa), University of Dar es Saalam.
Masalu, B. (2011) “Bob Junior: Sitamsamehe Wema”, Ijumaa, Tarehe 4 Mei 2011, Dar es
Salaam: Global Publishers, Uk. 11.
Massamba, D.P.B. (1996) Historia ya Kiswahili: 50 B.K. hadi 1500 B.K., Nairobi: Jomo Kenyatta
Foundation.
_______________(2009) Kiswahili Origins and the Bantu Divergence-Convergence Theory, TUKI:
Dar es Salaam.
Massamba, D. P. B na Wenzake (1999) Sarufi Maumbo ya Kiswahili Sanifu (SAMIKISA),
Dar es Salaam: TUKI
____________________ (2002) Historia ya Kiswahili: 50 BK Hadi 1500 BK, Nairobi: The Jomo
Kenyatta Foundation.
Mayoka, J. M. (1984) Mgogoro wa Ushairi na Diwani ya Mayoka, Dar es Salaam:
Tanzania Publishing House
Mbaga, N.O. (2004) “Ngonjera: Historia yake tangu Simulizi hadi Andishi,” katika Kiswahili Na. 67
Juzuu 67:43-48, Dar es Salaam: TUKI.
Mbarwa, H. (2000) Mashairi Boriti, Nairobi: Eagle H. Publishers.
Mbilinyi, J. (2011) Sugu: The Autobiography, Muziki na Maisha From the Streets to Parliament,
Deiwaka: Dar es Salaam.
Mbunda, M. (1993) Misingi ya Uhakiki wa Fasihi, Nairobi: East African Educational Publishers.
McCall, J. (1995) “Rethinking Ancestors in Africa,” Africa 65 (2), 256 – 270.
Melvin, L.D.F. (1975) Theories of Mass Communication, New York: Longman
Mhando, P. na Ndayanao Balisidya (1976) Fasihi na Sanaa za Maonyesho, Dar es Salaam:
Tanzania Publishing House.
Michuzi, I. (2010) “Mzee Yusufu Ndiye Mwanzilishi wa Kiduku?” katika
http://issamichuzi.blogspot.com/2010/07/mzee-yusuf-ndiye-mwanzilishi-wa-kiduku.html
iliyoangaliwa tarehe 7/10/2010.
Mickys, P. (2010) “Sugu na Ruge Malizeni Tofauti Zenu Kimyakimya,” Spoti Starehe, Tarehe 30,
Juni 2010, Dar es Salaam: Mwananchi Co. Ltd, Uk. 14.
Mihangwa, J. (2009) “Imani za Kishirikina Zinapogubika Chaguzi na Uongozi,” Raia Mwema,
Tarehe 11-17, Septemba, 2009, Uk. 3.
208
Miller, C. (1984) "Genre as Social Action," Quarterly Journal of Speech, 70: 151- 67, London:
Taylor and Francis Group,.
Miller, F, Agnes F. Vandome, John McBrewster (Eds.) (2009) Tanzanian Music, New York:
Amazon Press.
Mnyampala, M. (1970) Diwani ya Mnyampala, Dar es Salaam, Nairobi na Kampala: East
African Literature Bureau.
Msuya, M. (2011), “Maisha Bora kwa Mtanzania Bado,” Sir George Kahama, Mwananchi,
Tarehe 17 Julai, 2011 Uk. 1.
Msongo, B. (2011) “Hata Hicho Kidogo Wananyang’anywa,” Habari Leo, Tarehe 29 Agosti,
2011, Uk. 4.
Mtemwa, I. (2011) “Mastaa 10 Waliosahau Majina Yao,” katika Risasi Jumamosi, Tarehe 20-22,
Agosti, 2011, Dar es Salaam: Imprint Limited, Uk. 17.
Mulokozi, M. M. (1986) “The Nanga Epocs of the Bahaya: A Case Study in African Epic
Characteristics,” PhD Thesis (Unpublished), Dar es Salaam: University of Dar es Salaam.
__________(1996) “Fasihi ya Kiswahili,” Dar es Salaam: OUT.
__________ (1997) Utenzi wa Nyakiiru Kibi, Morogoro: ICOL Publications.
____________(Mh.) (1999) Tenzi Tatu za Kale, Dar es Salaam: TUKI.
__________ (2002) The African Epic Controversy: Historic, Philosophical and Aesthetic
Perspectives on Epic Poetry and Performance, Dar es Salaam: Mkuki na Nyota Publishers.
Mulokozi, M.M. na T.S.Y Sengo (1995) History of Kiswahili Poetry A.D. 1000-2000,
Dar es Salaam: Institute of Kiswahili Research.
Musa, M. (2010a) “Keisha Ajitoa Tip Top Connection,” Habari Leo, Tarehe 17 Septemba, 2010,
Dar es Salaam: TSN Publishers, Uk. 16.
______(2010b) “Kiduku Itumike kwenye Dansi,” Tanzania Daima, Tarehe 16, Aprili
2010, Dar es Salaam: Freemedia, Uk. 15.
______(2011) “Nyota wa Bongo Fleva `Aliyeteketea’ kwa Cocaine,” Habari Leo, Tarehe 31,
Julai, 2011, Dar es Salaam: TSN Publishers, Uk. 14.
Musoma Press (1968) Tenzi za Rohoni, Musoma: Musoma Press.
Mutembei, A. (2012) Korasi katika Fasihi: Nadharia Mpya ya Uhakiki wa Fasihi, Dar es Salaam:
TUKI
Mutua, B. F. (2006) Kioo cha Ushairi, Eldoret: Taaluma Publishers
Muzale, H.R.T. (2006) Ikaningabo ya Oruhaya, Dar es Salaam: Mradi wa Lugha Tanzania
_____________ (2009) Diwani ya Nakuomba, Dar es Salaam: Mradi wa Lugha Tanzania.
______________(2011) Kamusi ya Majina na Matumizi ya Mimea kwa Kihaya, Dar es Salaam:
Mradi wa Lugha Tanzania (LOT).
Mwanjoka, G. (2011) Harakati za Bongo Fleva na Mapinduzi, Dodoma: H.M.
Mwaruka, R. (1968) Utenzi wa Jamhuri ya Tanzania, Dar es Salaam, Nairobi na Kampala: East
African Literature Bureau.
Nagler, M.N. (1974) Spontaneity and Tradition: A Study in the Oral Art of Homer, Berkeley:
University of California Press
Nandwa, J. na A. Bukenya (1983) African Oral Literature for Schools. Nairobi: Longman.
Ngure, A. (2003) Fasihi Simulizi kwa Shule za Sekondari, Nairobi: Phonex Publishers.
Njogu, K. na R. Chimerah (2008) Ufundishaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu, Nairobi: Jomo
Kenyatta Foundation.
Nketia, J.H.K. (1963) Drumming in Akan Communities of Ghana, Accra: Edinburgh: Thomas Nelson.
____________ (1974) The Music of Africa, New York: W.W. Norton Company
Nkwera, F. (1979) Sarufi na Fasihi: Sekondari na Vyuo, Dar es Salaam: Tanzania Publishing
House.
Okpewho, I. (1979) The Epic in Africa, New York: Columbia University Press.
___________(1990) The Oral Performance in Africa, Ibadan: Spectrum Books.
___________ (1992) African Oral Litearature: Backgrounds, Character and Continuity,
Bloomington and Indianapolis: Indiana University Press.
Omari, S. (2006) “Mtindo wa Matumizi ya Lugha katika Muziki wa Kizazi Kipya Tanzania,”
209
Kiswahili vol. 69, Dar es Salaam: Institute of Kiswahili Research, 73 – 92.
________ (2009) “Tanzanian Hip hop Poetry as Popular Literature,” PhD Thesis
(Haijachapishwa), Dar es Salaam: University of Dar es Salaam.
_________ (2010) “Call Me Shakespeare: Aliases and Self-Praise in Tanzanian Hip hop
Music,” Unpublished paper.
__________ (2011) “Call Me ‘Top in Dar:’ The Role of Pseudonyms in Bongo Fleva Music,”
Swahili Forum 18 (2011): 69-86.
Parry, M. (1930) “Studies in Epic Techniques of Oral Verse Making II,” HSCP 41:70 – 71.
_______ (1932) “Studies in the Epic Techniques of Oral Verse Making II,” HSCP 43:1 – 50.
Parry, A. (mh.) (1971) The Making of Homeric Verse: The Collected Papers of Milman Parry,
Oxford: Clarendon.
Peek, P. M. na K. Yankah (wah.) (2004) African Folklore: An Encyclopedia, London na
New York: Routledge Taylor and Francis Group.
Perullo, A. (2003) “The Life that I Live: Popular Music, Urban Practises, and Agency in Dar es
Salaam, Tanzania,” Ph. D Dissertation, Indian University.
Posnansky, M. (1966) “Kingship, Archaeology and Historical Myth,” Uganda Journal, 30,1: 1- 12.
___________ (1969) “Bigo Bya Mugenyi,” Uganda Journal, 33, 2:125 – 150.
Raglan, Lord (1956) The Hero, New York: American Library.
1 – 69
Robert, S. (1967) Wasifu wa Siti Binti Saad, Nairobi: Nelson Publishers.
_________(1990) Kusadikika, Nairobi: Evans Africa.
________ (2008) Kufikirika, Dar es Salaam: Mkuki na Nyota Publishers.
Rodney, W. (1974) How Europe Underdeveloped Africa, Washington, D.C.:Howard University Press.
Roy-Campbell, Z.M. and M.A.S. Qorro (1997) Language Crisis in Tanzania: the Myth of
English vs Education, Dar es Salaam: Mkuki na Nyota Publishers.
Rubanza, Y. I. (1981) “Dhima ya Fasihi katika Majigambo ya Wahaya,” Makala ya Semina ya
Idara, Idara ya Kiswahili, Cho Kikuu cha Dar es Salaam.
____________(1994) Fasihi Simulizi: Majigambo (Ebyebugo), Dar es Salaam: DUP
Samwel, M. (2010) “Nafasi ya Nyimbo za Mapenzi katika Siasa: Mtazamo wa KiBongo Fleva,”
Makala Iliyowasilishwa katika Tamasha la Elimika na Bongo Fleva, Januari 16 – 17, 2010,
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Samwel, M. (2012a) “Mabadiliko katika Majigambo: Uchunguzi wa Majigambo ya Jadi na Bongo
Fleva,” Tasnifu ya Uzamivu (Haijachapishwa), Dar es Salaam: Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
Samwel, M. (2012b) Hadithi Fupi: Nadharia, Mbinu na Mifano, Iringa: Kasenyenda Tanzania.
Samwel, M. (2013) “‘Bongo Fleva Inapotosha Jamii’: Je, ni Dai Jipya katika Maendeleo ya Fasihi ya
Kiswahili?” katika Kioo cha Lugha, Na. 10 Juz. 10, Dar es Salaam: TUKI
Samwel, M. na Wenzake (2012a) Mwongozo wa Mstahiki Meya, Nairobi: NES
_____________ (2012b) Mwongozo wa Damu Nyeusi na Hadithi Nyingine, Nairobi: NES.
_____________ (2012c) Hadithi Fupi: Nadharia, Mbinu na Mifano, Iringa: Kasenyenda
Tanzania.
Shabaya M. J. na wenzake (2009) Demstifying Poetry, Nairobi: NES
Senkoro, F.E.M.K. (1988) Ushairi: Nadharia na Tahakiki, DUP: Dar es salaa.
______________(2011) Fasihi, Dar es Salaam: KAUTTU LTD.
Shitemi, N.L. (2010), Ushairi wa Kiswahili Kabla ya Karne ya Ishirini, Moi University Press:
Eldoret.
Shija, F. (2009) “Wanandoa Wauawa kwa Mapanga,” Mwananchi, Tarehe 08 November 2010, Uk. 7.
Smith, A. (1776) The Wealth of Nations, Glasglow: Gsm.
Smith, E. W. na A. M. Dale (1920) The Ila Speaking Peoples of Northern Rhodesia, 2 vols,
London: Clarendon
Songoyi, E.M. (2005) “The Form and Content of the Wigashe Dance Songs of the Sukuma,”
Tasnifu ya Uzamivu (Haijachapishwa), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
_________ (1988) “The Artist and the State in Tanzania: Study of Two Singers: Kalikali and
Mwinamila,” Tasnifu ya Uzamili (Haijachapishwa), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
210
Sunkuli, L. O & Miruka, S. O. (1990) A Dictionary of Oral Literature, Nairobi: East Africa
Educational Publishers.
Suriano, M. (2006) “Hip hop and Bongo Flavour music in Contemporary Tanzania: Youths’
Experiences, Agency, Aspirations and Contradictions”, Paper submitted for the conference,
“Youth and the Global South: Religion, Politics and the Making of Youth in Africa, Asia and
the Middle East”, Dakar, 13–15 October 2006.
__________ (2007) “Mimi ni Msanii, Kioo cha Jamii, Urban Youth Culture in Tanzania as Seen
Through Bongo Fleva and Hip- Hop,” Swahili Forum 14 (2007): 207-223.
Tanzania Bible Society (1997) Biblia Takatifu, Dodoma: Tanzania Bible Society.
TUKI (1981) Kamusi ya Kiswahili Sanifu, Dar es Salaam: TUKI.
Ushe, M.U. (2007) Kpor of Tiv Culture, Enugu: Sam Press.
Ushe, M.U. (2010) The Mortgage Culture of Tiv Death and Burial Rites, Lagos: Vast Publishers.
Ushe, M.U. (2012) “The talking drum: An Inquiry into the Reach of a Traditional Mode of
Communication,” Katika International Journal of Educational Research and Development
Juzuu. 1(2), Uk. 023-028.
Uvetie, E. A. (1976) Utamu wa Lugha, Dar es Salaam, Nairobi na Kampala: East African
Literature Bureau
Vansina, J. (1965) Oral Traditions, Harmondsworth: Penguin.
Wade, M. na Almir Maljevic (Wah.) (2011) A War on Terror?: The European Stance on a New Threat,
Changing Laws and Human Rights Implications, New York: Springer.
Wafula, R.M. na Kimani, N. (2007) Nadharia za Uhakiki wa Fasihi, Nairobi: Jomo Kenyatta
Foundation.
Wamitila, K. (2005) Tamthilia ya Maisha, Nairobi: Vide Muwa.
__________(2008) Kazi ya Fasihi, Nairobi: Vide Muwa Publishers
__________ (2010) Kichocheo cha Fasihi: Simulizi na Andishi, Nairobi: Focus Books
Wolf, F.A. (1795), Prolegomena (Maelezo mengine ya uchapaji hayapo).
Wood, R. (1767) An Essay on the Origin Genius of and Writings of Homer, New York: Garland
Publishing Inc.
http://en.wikipedia.org/wiki/Clan ilipakuliwa tarehe 12/07/2011
http://spotistarehe.wordpress.com/page/50/
DISKOGRAFIA
Afande Sele (2003) Darubini Kali, Dar es Salaam: GMC Wasanii Promoters.
Bob Junior Ft Nuru (2011) “Muhogo Andazi,” Dar es Salaam: Sharobaro Records.
Dogo Janja (2009) Ngarenaro, Dar es Salaam: GMC Wasanii Promoters.
Lady Jaydee (2007) Shukrani, Dar es Salaam: FKW
Mr. Ebbo (2002) Fahari Yako, Dar es Salaam: FKW
Mr. 2 a.k.a Sugu (2009) Veto, Dar es Salaam: DEIWAKA Entertainment.
Professor Jay (2001) Machozi Jasho na Damu, Dar es Salaam: FKW.
___________ (2003) Mapinduzi Halisi, Dar es Salaam: GMC Wasanii Promoters.
Sister P. (2001) Marekebisho, Dar es Salaam: GMC Wasanii Promoters.
Wagosi wa Kaya (2003) Ripoti Kamili, Dar es Salaam: GMC Wasanii Promoters.
Zay B. (2002) Mama Afrika, Dar es Salaam: GMC Wasanii Promoters.
211
FAHARASA
Abedi, 25, 26, 28, 60, 63, 64, 205
Afrika, 4, 10, 14, 17, 18, 19, 23, 41, 42, 45, 58,
59, 60, 61, 65, 66, 70, 71, 79, 80, 90, 97, 99,
114, 132, 133, 134, 143, 148, 159, 160, 161,
165, 177, 186, 205, 210
Afrika Mashariki, 18, 23, 41, 79, 132, 133, 134
Akilimali, 26, 62, 185, 205
Akivaga na Odaga, 12, 95
Albert Lord, 72, 73
Amri Abedi, 24, 25, 42, 43, 60, 63, 84, 112
Andalio la Somo, 134
Ashton, 24
Azimio la Arusha, 61, 62
Azimio la Kazi, 134, 135
BAHARI ZA USHAIRI WA KIMAPOKEO,
113, 120
Balagha, 130
Bantundi, 121
Bembelezo, 15
Beti, 85, 104, 107, 120, 128
Bongo Fleva, 14, 15, 26, 46, 47, 48, 49, 50, 51,
52, 53, 54, 55, 56, 59, 65, 66, 67, 68, 69, 70,
71, 72, 74, 77, 78, 79, 80, 81, 82, 83, 84, 85,
87, 88, 89, 90, 91, 92, 93, 94, 95, 96, 97, 98,
99, 100, 101, 102, 103, 104, 105, 106, 107,
108, 109, 110, 126, 128, 142, 207, 208, 209,
210
Bowra, 14, 205
Bukenya na wenzake, 13
Chapuzo, 15, 21
CHIMBUKO LA USHAIRI, 41, 45
Chiraghdin, 45, 46, 63, 64, 205
Chuku, 95, 105, 130
Coupland, 41, 43, 205
Dhamira, 42, 126
dhima za ushairi, 52
DHIMA ZA USHAIRI, 29, 35
DRAMA SIMULIZI, 17
Ebeze, 19
Falsafa, 10, 90, 95, 126
fanani, 12, 17, 20, 22, 23, 53, 54, 73, 77, 78, 79,
101, 103, 110, 115, 124
fani, 12, 14, 26, 28, 41, 46, 61, 64, 65, 72, 77,
98, 99, 100, 101, 107, 109, 115, 126, 127,
128, 130, 133, 137, 148
FANI, 72, 127, 137
fasihi, 12, 13, 14, 15, 16, 17, 18, 19, 20, 22, 23,
24, 25, 26, 27, 28, 41, 42, 43, 44, 46, 54, 57,
58, 62, 63, 64, 72, 73, 74, 80, 81, 82, 83, 85,
89, 94, 95, 102, 104, 109, 110, 111, 115, 126,
127, 129, 130, 131, 132, 134, 137, 144, 145,
146, 147
FASIHI ANDISHI, 23, 137
FASIHI NGOMA, 18
fasihi simulizi, 12, 13, 14, 15, 17, 18, 19, 23,
25, 54, 74, 82, 83, 85
Finnegan, 13, 54, 74, 83, 114, 205
Fuji, 19
Fundisho, 127
Githuma, 24
Gunderson, 48, 52, 54, 206
Gungu, 121
Guni, 123
hadhira, 12, 13, 14, 15, 20, 22, 25, 26, 27, 28,
53, 54, 55, 77, 79, 80, 81, 84, 87, 100, 101,
103, 106, 107, 112, 116, 126, 127, 129, 130,
198
Hamziya, 118
Hamziyya, 42, 57, 59, 113, 118, 207
Harries, 41, 42, 57, 144, 206
hati za Kiarabu, 41, 42, 43, 44, 58
Hekaya, 16
Hip hop, 66, 67, 69, 70, 78, 80, 81, 82, 84, 88,
89, 93, 96, 100, 108, 205, 207, 209, 210
Homer, 72, 208, 210
Hotuba, 17
Hurafa/ khurafa, 16
Inksari, 130
Innes, 29, 30, 206
ishara, 16, 27, 28, 55, 56, 91, 93, 106, 128, 168
Istiara, 16
Jamieson, 13, 206
Jando, 17
Johnson, 29, 30, 73, 104, 206
Jùjú, 19
Kahigi, 3, 26, 27, 28, 58, 62, 63, 105, 110, 129,
130, 206
Kanuri na wenzake, 27
Kejeli, 105
Kezilahabi, 27, 62, 63, 127, 186, 206
Kibwagizo, 85, 87, 128
kiduku, 82, 83, 207
kikai, 113
Kikai, 119, 123
kikwamba, 113, 118, 119, 123
Kikwamba, 116, 123
kimai, 21, 113, 119, 122
Kimai, 15, 119, 122
Kimani na wenzake, 13
King’ei na Kisovi, 13, 119
Kisarambe, 123
Kituo/kimalizio, 128
Knappert, 46, 57
Komedia/Futuhi, 17
212
KUALIKA MGENI, 141
Kumbukumbu, 16, 178
Kwabena Nketia, 18
Lakabu, 16, 92
LENGO KUU, 145
lugha ya mkato, 24, 27, 28, 120, 130
Lugha ya mkato, 131
maandishi, 12, 13, 24, 27, 42, 44, 54, 57, 58,
111
Macgoye, 26, 28
MADHUMUNI MAHSUSI, 145
Mafumbo, 16
Maghani, 15, 16, 21, 22, 23
Mahenge, 15, 109, 207
Maigizo ya kidini, 17
Maigizo ya msibani, 17
Maigizo ya sherehe, 17
maigizo ya watoto, 17
MAJADILIANO, 141
Majigambo ya Majibizano, 96
Majigambo ya Majina, 88, 91, 92, 93, 94, 95
majigambo ya wanawake, 14
malenga, 27, 44, 104, 107, 115
Mandhari, 55, 84, 131
Mandhuma, 113, 118, 124
Maombi, 17
Mapisi, 16
mashairi ya kikasuku, 61
Masivina, 123
Massamba, 3, 27, 44, 45, 63, 207
Masuluhisho, 127
Matambiko, 17
Matumizi ya Lugha, 100, 101, 128, 130, 208
Matumizi ya Mapigo, 56, 108
Matumizi ya Nahau, 130
maudhui, 18, 20, 22, 26, 27, 28, 41, 42, 43, 46,
48, 49, 50, 51, 52, 58, 62, 66, 67, 68, 69, 70,
71, 87, 89, 90, 91, 103, 104, 105, 106, 109,
111, 112, 114, 119, 124, 126, 127, 128, 129,
130, 131, 133, 135, 137
MAUDHUI, 67, 126, 137
Mavazi na Vifaa, 54
Mawaidha, 17, 186
Mazda, 130
MAZUNGUMZO, 16
Mbalaksi, 19
Mbazi, 16
Mbinu ya kufundishia, 139
Mbolezo, 15
Mchongoano, 17
MDAHALO, 142
Melvin, 18, 207
methali, 14, 18, 61, 90, 106, 109, 128, 129, 130
Methali, 14, 16, 109, 130
Mgogoro, 63, 127, 207
MGOGORO WA USHAIRI, 63
Mhando na Balisidya, 18
Michapo, 16
Michezo ya Kuigiza, 17
Mighani (Visakale), 16
Miller, 13, 208
Milman Parry, 72, 209
Misemo, 16, 91
Misimu, 109, 110, 130
Mivigha, 17
Mizaha, 17
Mizani, 128
mkabala wa Kimaksi, 29, 30
Mkarara, 128
Mmbaga, 46, 115
Mnyampala, 3, 25, 28, 31, 33, 42, 45, 60, 61,
62, 63, 111, 116, 208
Mochiwa, 62, 63
Mshororo, 121, 128
Msimamo, 127
msuko, 113, 114, 118, 119
Msuko, 118, 121
Mtindo, 55, 74, 82, 88, 93, 128, 208
Mtiririko, 122
Mugasha, 50, 114
MUHTASARI, 133, 134
muktadha, 12, 14, 15, 20, 22, 23, 28, 43, 74, 94,
115, 119, 131
Mulokozi, 3, 12, 13, 14, 18, 24, 26, 27, 28, 41,
42, 43, 45, 46, 53, 54, 57, 58, 59, 60, 62, 63,
73, 74, 81, 83, 85, 89, 91, 92, 93, 97, 104,
105, 109, 110, 113, 114, 115, 118, 119, 129,
130, 137, 206, 208
Mulokozi na Kahigi, 28
Mulokozi na Sengo, 57, 58, 59, 60
Muundo, 84, 85, 87, 88, 92, 117, 120, 124, 127,
206
Mwanjoka, 54, 67, 69, 70, 77, 79, 81, 83, 84,
89, 90, 92, 208
Mwaruka, 25, 27, 31, 33, 61, 208
Mwindo, 114
Nagler, 73, 208
nanga, 14, 30, 31, 32, 34, 36, 54, 73
NATHARI, 16
Nathari za Kibunifu, 16
Nathari za Kihistoria, 16
Naudia, 113
ngano, 13, 105
Ngano, 16
Ngoma, 18
ngoma za ishara, 18
213
ngoma za kifasihi/ngomezi, 18
ngoma za kuchezwa, 18
Ngomezi, 18
ngonjera, 46, 61, 113, 115, 116, 142
Ngonjera, 31, 33, 46, 61, 62, 115, 116, 124, 207
Nketia, 18, 208
NUDHUMU, 15, 20
nudhumu simulizi, 20
nyimbo, 14, 15, 17, 19, 20, 21, 22, 25, 44, 45,
47, 54, 55, 56, 57, 58, 59, 66, 67, 68, 69, 70,
74, 76, 77, 78, 81, 82, 84, 87, 88, 89, 91, 92,
93, 99, 100, 101, 103, 109, 111, 112, 115,
119, 122, 132, 139, 140
NYIMBO, 20
Okpewho, 73, 208
Omari, 3, 51, 54, 60, 65, 66, 67, 68, 71, 72, 76,
79, 80, 81, 82, 88, 89, 90, 93, 94, 96, 97, 98,
99, 100, 102, 103, 104, 106, 107, 108, 109,
110, 208
Peek na Kwesi, 14, 53, 54, 56, 81, 94
Philip na Kwesi, 54, 55
Picha na Taswira, 106
Pindu, 123
Posnansky, 30, 209
Raglan, 29, 30, 209
Ritifaa, 131
Robert, 3, 24, 26, 27, 42, 43, 60, 63, 73, 140,
209
Rubanza, 3, 13, 14, 49, 50, 51, 53, 54, 55, 56,
81, 83, 93, 97, 209
Sabilia, 121
Sakarani, 118
Samwel, 1, 13, 14, 15, 19, 26, 43, 45, 46, 47,
48, 49, 50, 51, 52, 53, 54, 55, 56, 65, 66, 67,
73, 74, 92, 93, 95, 112, 126, 129, 130, 131,
135, 137, 146, 209
sanaa za maonyesho, 14, 109
sarakani, 113
Sarakani, 124
sayansi na teknolojia, 13, 54
Senkoro, 3, 20, 23, 24, 27, 28, 45, 57, 58, 62,
63, 94, 105, 106, 129, 130, 209
Shabaya na wenzake, 24, 111
shairi, 24, 25, 26, 27, 28, 44, 45, 49, 56, 59, 60,
61, 62, 63, 65, 71, 85, 87, 98, 104, 105, 107,
108, 110, 111, 112, 113, 114, 116, 117, 118,
119, 120, 121, 122, 123, 124, 126, 127, 128,
130, 131, 170
Shairi, 25, 85, 112, 113, 118, 120, 123
Sherehe za kutolea majina, 17
Shirikina, 16
sifo, 16, 22, 53
silabasi, 133, 134, 143, 144, 147, 148, 215
Simango, 15, 21
Simo/Misimu, 16
sitiari, 27, 47, 55, 56, 93, 94, 95, 102, 103, 104,
129
Sitiari, 55, 94, 103, 129
Soga, 17
Songoyi, 48, 49, 54, 55, 104, 209
Sundiata, 114
Suriano, 54, 66, 79, 84, 109, 210
Tabdili, 130
Tabuka, 42, 57, 59
Takhmisa, 58, 113, 117, 121, 122
Takriri, 106, 129
tamathali za semi, 28, 88, 93, 94, 102, 128, 129,
137
Tamathali za Semi, 102, 129
Tanakali Sauti, 131
Tanzu, 12, 14, 15, 20
TANZU FUPIFUPI, 16
tanzu kongwe, 18
Tarbia, 113
Tarihi, 16
Tasadia, 113
Tasdisa, 113
Tashbiha, 102, 129
Tashihisi, 95, 104, 129
Tasifida, 129
Tathlitha, 113
Tathmina, 113
Tathnia, 113
Telemania, 113
Tiyani Fatiha, 124
Tukuzo, 15, 20
Tumbuizo, 15, 19, 20, 120, 124
Uainishaji wa maghani, 15, 16, 22, 23
Uainishaji wa tanzu, 13, 23
UAINISHAJI WA USHAIRI, 111
Ucheshi, 106, 130
Udokezi, 104, 105, 130
UFUNDISHAJI WA USHAIRI, 132
uhakiki wa mashairi, 126
uhifadhi, 12
Uhifadhi wa Historia, 29
Ujumbe, 126
ukara, 113, 117
Ukara, 117, 122
Ukawafi au kawafi, 116, 121
ukawafi/kawafi, 113
ukoloni, 43, 57, 59, 60, 62, 64, 97, 101, 102,
165
UKOLONI WA WAINGEREZA, 60
UKOLONI WA WAJERUMANI, 60
Ukumi, 113
214
Ukuraguni, 122
ukweli wa kihistoria, 29, 31
Umbea, 16
Unyago, 17
Upeo, 123
Usambamba, 110
ushairi simulizi, 12, 20, 25, 27, 41, 42, 45, 46,
47, 48, 49, 50, 51, 52, 53, 54, 56, 57, 58, 61,
64, 85, 110, 111, 112, 132, 140
Ushairisimulizi wa Kibantu, 45, 46
Ushairi wa Bongo Fleva, 66, 67, 72
ushairi wa kazi, 48, 57
USHAIRI WA KISASA, 62
ushairi wa kizazi kipya, 106
Ushe, 18, 19, 210
UTANDAWAZI, 65
Utani, 17
Utendaji, 53, 77, 80, 81, 83, 84
Utendi wa Rukiza, 36, 46, 47
Utendi/utenzi, 114, 120
Utenzi wa Adamu na Hawaa, 114, 131
Utenzi wa al-Inkishafi, 58, 124
Utenzi wa Fumo Liyongo, 58, 114
Utenzi wa Jamhuri ya Tanganyika, 31, 33, 61
Utenzi wa Jamhuri ya Zanzibar., 31, 33, 61
Utenzi wa Mwanakupona, 42, 43, 58, 59, 185
Utenzi wa Nyakiiru Kibi, 114, 208
Utenzi wa Uhuru wa Kenya, 31, 33, 61
Utenzi wa Uhuru wa Tanganyika, 31, 33, 61
Utenzi wa Vita vya Maji Maji, 114
Utenzi wa Vita vya Mau Mau, 114
utenzi/utendi, 113
utoaji wa somo, 143, 144, 145
utungaji, 12, 25, 53, 72, 73, 74, 76, 77, 91, 115,
120, 123
Utungaji wa Kabla ya Tukio, 77
Utungaji wa Papo kwa Papo, 72
Uvetie, 25, 210
uwasilishaji, 12, 13, 14, 54, 73, 76, 77, 81, 111,
115, 141
Vansina, 29, 30, 210
Vichekesho, 16
vigezo, 12, 13, 20, 22, 44, 66, 104, 111, 114,
119, 120, 180
Vina na Mizani, 56, 107, 120, 121, 142
Vipande, 120, 121, 128
vipera vya fasihi, 13
Visasili, 16
Visaviini, 16
Vitabu vya kiada, 144
Vitanza-Ndimi/ Kauli Tauria, 16
Vitendawili, 16
Waarabu, 41, 42, 43, 44, 57, 58, 59, 60, 64, 112
Wafula na Njogu, 13
Wahusika, 55, 95, 96, 110, 131
wajiwaji, 113
Wamitila, 3, 12, 27, 116, 118, 119, 131, 210
wanamapokeo, 24, 25, 26, 27, 28, 45, 63, 64,
112, 114
Wanausasa, 27, 64, 112
Wareno, 41, 57, 59, 60
wawe, 15, 21, 113, 118, 122
Wawe/ Vave, 118, 122
Wimbo, 21, 52, 59, 69, 105, 106, 114, 120, 132,
197, 198
Zana za kufundishia, 144
Ziara, 140
zivindo, 113, 116
Zivindo, 116, 124
215
Ushairi wa Kiswahili umekuwa ukifundishwa katika vyuo mbalimbali katika mahali pengi duniani.
Mbali na kufundishwa huko, hapajakuwa na kitabu kinachofafanua masuala ya kidhana na kinadharia
yanayohusiana na ushairi wa Kiswahili na kuyahusisha na mbinu za ufundishaji wa ushairi na Kiswahili
kwa ujumla. Kitabu hiki kinauvamia mfupa huo. Hivyo, kitabu hiki kinafafanua kwa kina masuala ya
kidhana na kinadharia yanayohusiana na ushairi wa Kiswahili. Kinaelezea, kwa mfano, ushairi ni nini,
ulianzaje, unaainishwaje na unachambuliwaje miongoni mwa mambo mengine. Aidha, kitabu hiki,
tofauti na vingi vilivyotangulia, kinatoa mwongozo kwa walimu juu ya namna ya kufundisha ushairi na
Kiswahili kwa ujumla. Kinafafanua dhana nzima ya ufundishaji wa ushairi na Kiswahili, silabasi ya
Kiswahili ilivyo na nafasi ya ushairi katika silabasi hiyo. Aidha, kinafafanua hatua za kufuata katika
utiaji wa silabasi katika vitendo, uaandaji wa azimio la kazi na andalio la somo pamoja na uteuzi wa
mbinu za kufundishia. Vilevile, kitabu hiki kinafafanua hatua za kufuata katika ufundishaji wa ushairi
darasani na namna ya kutunga mitihani na mazoezi ya ushairi wa Kiswahili na Kiswahili kwa ujumla.
Sehemu ya mwisho ya kitabu hiki inaundwa na Diwani ya MEA ambayo ni kusanyiko wa mashairi
yenye mvuto wa hali ya juu.
Method Samwel ni Mhadhiri wa Isimu na Fasihi katika Idara ya Kiswahili ya Chuo Kikuu Kishiri cha
Elimu Dar es Salaam (DUCE). Ana digrii za BA (Ed.), MA (Linguistics) na PhD (Fasihi ya Kiswahili)
alizozipata katika miaka ya 2006, 2008 na 2012 mtawalia katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,
Tanzania. Mwandishi huyu ameshaandika sana katika uwanda wa isimu na fasihi ya Kiswahili na lugha
nyingine za Kibantu. Miongoni mwa vitabu vyake maarufu ni Hadithi Fupi: Nadharia, Mbinu na
Mifano, Mwongozo wa Tamthilia ya Mstahiki Meya na Mwongozo wa Damu Nyeusi na Hadithi
Nyingine. Mbali na uandishi wa vitabu, ameshaandika pia makala mbalimbali katika majarida ya kitaifa
na kimataifa kuhusu lugha, fasihi, muziki na utamaduni.
Amina J. Seleman ni mkufunzi msaidizi katika Idara ya Misingi ya Elimu katika Chuo Kikuu Kishiriki
cha Elimu Dar es Salaam (DUCE). Ana digrii ya BA (Ed.) (Hons.) (Daraja la Kwanza) kutoka katika
Chuo hichohicho aliyoipata mwaka 2011 akibobea katika Kiswahili na Ualimu. Mwandishi huyu ni
mwanataaluma anayechipukia aliye na utayari wa kujifunza na mwenye bidii kubwa sana katika
kujaribu. Kwa sasa anaendelea na masomo ya digrii ya MA (Ed.) katika Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam. Mbali na kufundisha katika Chuo Kikuu cha Elimu Dar es Salaam ameshafundisha kwenye
shule mbalimbali za sekondari nchini Tanzania. Hivyo, ni mwalimu mzoefu sana.
Akech Kabiero ni mwandishi maarufu sana wa kazi mbalimbali za fasihi. Yeye huandika mashairi,
riwaya, tamthilia na hadithi fupi. Mpaka sasa ana hazina kubwa ya miswada ya kazi hizo za fasihi
ambazo bado angali anatafuta mchapishaji. Ni mwanafasihi mwenye kipajai cha hali juu. Kabiero
alihitimu digrii ya BA (Ed.) mwaka 2012 katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambako alibobea
katika somo la Kiswahili. Mwandishi huyu zaidi ya kipaji cha utunzi ni mwalimu wa sekondari
aliyebobea.
MEVELI Publishers, Dar es Salaam-Tanzania.
ISBN: 978-9987-9735-0-7
MEVELI PUBLISHERS (MVP)