Monday

ukongwe na usasa wa fasihi simulizi PDF

0 comments

 

FASIHI SIMULIZI INAO UKONGWE NA PIA USASA. JADILI.

a.     Ukongwe katika fasihi simulizi.

Fasihi simulizi ni aina ya fasihi ambayo inaaminika kuwa kongwe zaidi kuliko fasihi andishi. Fasihi hii ilizuka tu pindi mwanadamu alipoanza kuongea. Hata hivyo upo wakati ambapo fasihi simulizi ilidharauliwa mno. Hali hii ilitokea tangu kutawala kwa fasihi andishi Ulaya, Asia na kutumiwa na wenye nguvu za kisiasa na kiuchumi, fasihi simulizi ilidharauliwa ikatwezwa, ikadunishwa na kushushwa hadhi huku fasihi andishi ikitukuzwa na kuendelezwa.

Taaluma ya fasihi simulizi hivi leo inashughulikiwa kwa nguvu nyingi ili kuondokana na fikra duni zilizorithiwa toka kwa wataalamu wa kigeni kuwa sanaa kongwe ya fasihi simulizi ni ya kishenzi. Pamoja na dharau juu ya fasihi simulizi bado ukweli unabaki kuwa sanaa hii ndiyo ghala halisi la fasihi andishi.

Hata sasa imebainika kuwa tenzi za Kigiriki zinazodaiwa kutungwa na manju aitwaye “Home” hazikuwa zimeandikwa kwa zaidi ya miaka mia tano (500) ndipo baadaye zikaja kuhifadhiwa katika maandishi. Hivi majuzi pia wanateknolojia wameanza kukubali kuwa sehemu kubwa ya Biblia ni fasihi simulizi ya Wayahudi walioishi zama mbalimbali. Wanazidi kueleza kuwa imebainika kuwa fasihi hiyo haikutoka mbinguni bali mizizi yake ni katika jamii ya Wasumuri (Mesopotamia), Waajemi na Wagiriki. Hoja ya msingi ni kuwa fasihi andishi haijaibua dhamira mpya, zote ni zile zile ambazo zilijitokeza katika masimulizi. Mfano: Mapenzi, siasa, unyonge wa wanawake, ukombozi, uchawi na ushirikina, uzazi, ndoa na migogoro ya kitabaka. Misemo ya fasihi simulizi haijapitwa na fasihi andishi wala fani yake haijabadilika mpaka leo.

Kwa yakini ukongwe wa fasihi simulizi unaanzia pale sanaa hii  ilikuwa ni sanaa ambayo imejengwa katika mfumo uliozoeleka wa kufikisha ujumbe kwa hadhira, mfumo uliolenga zaidi katika kurithishana mila, desturi na utamaduni kutoka kizazi kimoja hadi kingine.

Hii ina maana kurithishana mila, desturi na tamaduni kutoka kizazi cha kale (babu, bibi na wengineo wa umri wao) kwa kukifundisha kwa kukirithisha kizazi kipya (ambacho ni watoto na wajukuu zao). Katika utoaji wa sanaa hii ni lazima pande zote mbili ziwepo.Hili lina maana kuwa ukale na utamaduni bado umo na utazidi kujitikeza katika fasihi simulizi.

Fasihi hii ilirithishwa kutoka kizazi kimoja kwenda kingine kupitia katika nyimbo, hadithi, ngoma, mashairi ya zamani (malenga), na hata michezo ya ujasiri na majigambo.Tanzu hizi bado zipo hadi sasa ishara kuwa usuli wake wa ukongwe bado unahimilika.

Katika kuiwasilisha fasihi hii ni lazima kuwepo na pande mbili za mawasiliano (majadiliano) yaani fanani (anayerithisha, msimuliaji) na Hadhira (anayerithishwa, msimuliwaji). Fanani hujitahidi kutumia mbinu mbalimbali kuijenga kazi yake ili iweze kuvutia hadhira.  

Uhusiano wake hujitokeza anapotumia viungo vyake vya mwili katika kujenga kazi yake.Lengo la fanani kutumia viungo hivyo ni kuwa anataka kuyakamilisha maadili yatokanayo na kazi yake. Msimuliaji anapochukua nafasi ya wahusika, mfano endapo kuna wimbo ndani ya hadithi na makofi, au ishara fulani ya kutumia viungo vya mwili; msimuliaji anapoimba na kupiga ma- kofi, hapo anakuwa msimuliaji wa wakati huohuo pia ni mhusika mshiriki. Lazima ikumbukwe kwamba, fanani siku zote huanzisha majadiliano au mafundisho na Hadhira lazima iwe na uwezo wa kupokea na kuihifadhi majadiliano au mafundisho.

Ukongwe wa fasihi simulizi waaidha imo katika mbinu za kuhifadhi. Hapo zama za zama fasihi simulizi ilikuwa ikihifadhiwa kichwani. Ilihifadhiwa humo kwa muda mrefu kiasi kwamba baada ya muda ilibidi ipatiwe kizazi kingine na kingine. Ingawaje katika kukipatia kizazi kingine yale yaliyokuwapo sio yote ambayo yalifikishwa kwa kizazi kipya, bali yaliyofikishwa yalikiwezesha kizazi kipya kufahamu yaliyotokea na kutendeka hapo zamani.Hii pia ipo hadi sana ingawa kwa kiasi fulani, maendeleo na maenezi ya sayansi na teknolojia yameivamia fasihi hii katika viwango mbalimbali.  

Urathi vile vile eni swala ambalo lina mashiko makubwa katika fasihi simulizi. Hivyo basi, mmiliki wa fasihi simulizi katika kipindi na wakati huo wazama alikuwa ni mwana jamii na fasihi hii ilikuwa ni mali ya jamii. Fasihi simulizi ya zamani ilikuwa na mvuto wa aina yake, ambapo kukosea au kwenda kinyume na maadili ya jamii ilikuwa si rahisi kwa sababu jamii ilikuwa pamoja kwa muda mwingi. Kupitia kwa huyo mwana jamii mmoja aneweza kufahamu mengi mno kuhusiana na jamii husika.

Baada ya mwingilio wa wageni toka pande mbalimbali za dunia, fasihi simulizi ilianza kubadilika kutokana na kuingizwa kwa mila, desturi na tamaduni toka kwa wageni hawa. Ama kwa hakika wageni hawa walifanikiwa kwa kiasi kikubwa kuathiri fasihi simulizi na kuipa mkondo mpya. Jamii iliyapokea mafanikio ya wakoloni yaliyodhihirika wakati wanajamii wenyewe walipoamini kwamba amali walizokuwa nazo hazikuwa na maana kama zile walizoletewa na wageni au wakoloni hawa. Jamii iliamini kwamba amali hizo hawakuwa nazo, na kama walikuwa nazo, basi hazikuwa na maana kama zile walizoletewa.

Kwa mfano wakati jamii ilifurahia kuburudishwa na kuburudika kwa kutumia simulizi zilizotolewa jioni kwa pamoja mbele ya nuru ya mbalamwezi, kuingia kwa wageni hawa kumesababisha kuwepo kwa fasihi simulizi nyingine ambayo kwa kiasi kikubwa kumeadhiri starehe hiyo. Kadhalika wageni hawa wamechangia sana kuingia kwa maendeleo ya kisayansi na teknolojia ambayo yameanza kuiingiza jamii yetu katika fasihi ya televisheni, kompyuta redio na video ambayo kwa kiasi kikubwa imefifisha starehe iliyokuwa ikipatikana hapo awali. Amali hizi mpya kama televisheni, kompyuta, redio na video ndizo zinazotumika kuiwasilisha fasihi simulizi ya kisasa na ambazo tutaziangalia uwepo wake na athari zake katika jamii.

b.     Usasa wa fasihi simulizi.

Usasa ama uleo wa fasihi simulizi unagubikwa na swala zima la makuzi na maendeleo ya Teknolojia. Tunapozungumzia juu ya Teknolojia ni lazima tuhusishe na Sayansi, ambapo tunapozungumzia juu ya teknolojia tunayazungumzia maendeleo ya Kisayansi. Kwa hivyo basi Sayansi na Teknolojia ni vitu viwili vinavyokwenda sambamba na pamoja bila ya kuachana. Bali, teknolojia ni maendeleo ya kisayansi katika hatua ya mwisho kabisa ambayo inaonekana. Historia inaonyesha kwamba nchi zote ambazo zimeendelea, maendeleo yake yametokana na Sayansi na Teknolojia.

 

Tunatumia teknolojia katika maisha yetu ya kila siku; mfano nyumba, mawasiliano,   mwanga n.k. Halikadhalika tunatumia teknolojia kwa matumizi mengi ya kila siku, kupikia, kuwasilia- na, kutembeleana na mambo mengine yanayofanana na hayo.

 

Tunapozungumzia juu ya Teknolojia mpya, tunamaanisha maendeleo zaidi katika Sayansi na Teknolojia. Na tunapozungumzia juu ya Usasa katika fasihi simulizi, tunazungumzia jinsi ambavyo tunaweza kuitumia teknolojia mpya katika kuihifadhi, kuiwakilisha, kuikosoa, kuburudisha na hata kuichangia mada fasihi simulizi. Na hayo yote yanawezekana kupitia televisheni, kompyuta, mikanda ya video, mikanda ya CD, barua pepe, simu za mkononi, setelaiti n.k. Labda hapa niweke wazi ya kuwa nitakachokieleza manufaa ya teknolojia mpya kwa fasihi simulizi na kwa jamii nzima kwa ujumla.

Kwanza, katika kuiwakilisha fasihi simulizi kwa watu wengi walio mbali na fanani, kwani hii ni fasihi ambayo uwasilishaji wake si lazima wahusika wote wawili wawepo yaani fanani na Hadhira. Hadhira inaweza kuwepo lakini fanani asiwepo na nafasi yake ikachukuliwa na utaalamu wa kisasa unaotokana na teknolojia mpya. Hili hufanyika kupitia mikanda ya video na ya CD, kupitia tarakilishi, barua pepe, radio, setelaiti,vipata-ninga n.k. Kwa ujumla hapa teknolojia mpya inatumika kama kihifadhi cha fasihi simulizi ili kuweza kufikisha ujumbe.

 

Pili, katika kuihifadhi fasihi simulizi ili vizazi vingine viweze kuirithi, nyanja hii ya fasihi hu- tumia vyombo vya kisasa kabisa vya kuhifadhia kama mikanda ya video, DVD, tepurekoda na utepe wake, tarakilishi,vipakatalishi,tarakiba(tab) ,rununu za kisasa(Smart phones)  kadi sakima (memory card), diski mweko(flash disk), CD mtandao wa You tube n.k. Hivi vyote vimeirahisisha shughuli nzima ya kuhifadhi kazi mbalimbali za fasihi simulizi. Kwa kweli mbinu asilia ya kuhifadhi fasihi simulizi inao udhaifu wake chungu nzima. Baadhi ya udhaifu huu ni pamoja na  swala la kusahau baadhi ya sehemu za tanzu husika kwa kuwa binadamu katika kusahau si ajabu,baadhi ya tanzu hubadilika badilika wakati hasa fanani anapowasilisha kwa kutumia maneno mbadala na cha ajabu mno ni kule kufariki kwa aliyehifadhi fasihi hii kwa kichwa ishara kuwa yale yote yaliyokuwa kichwani mwake nayo pia hayapo.

Tatu, katika kuchangia mada, teknolojia mpya inatumika kama kiunganishi kati ya fanani na hadhira, ambapo mfano mzuri katika eneo hili ni matumizi ya setelaiti. Aidha setelaiti yaweza kutumika kuiwasilisha kazi ya fasihi simulizi kwa hadhira iliyo mbali na fanani kama alivyofanya aliyekuwa raisi wa Marekani Bill Clinton alipokuwa akichangia mawazo yake ili kuwezesha kupatikana kwa suluhisho la mgogoro baina ya nchi za Rwanda na Burundi. Raisi huyu alichangia moja kwa moja akiwa Marekani wakati mkutano wa suluhu ulikuwa ukifanyikia Arusha. Rais huyu alionekana kwenye setelaiti akizungumzia mtazamo wake kuhusu mgogoro huo. Vile vile vyombo vya habari huwa na sehemu fulani ambapo vituo hivi huweza kutumia mtandao maarufu wa SKYPE kuwasiliana moja kwa moja na mtangazaji aliye kwenye studio. Hii hujitokeza katika idhaa ya KTN, Citizen, NTV, K24 n.k.

 

Nne, katika kukosoa jamii  hii hufanyika kupitia televisheni, video hasa kwenye michezo ya kuigiza (Tamthilia) kupitia video na televisheni wasanii huikosoa jamii pale inapokuwa aidha imekosea au imepotoka, hivyo jamii inapata mafunzo kupitia teknolojia mpya. Tamthilia inaweza kuwa inachezwa na watu kutoka nchi nyingine kwa mfano Nigeria,Tanzania, Uingereza lakini kwa kuwa matatizo ya kijamii hufanana basi mchezo huo unaweza kutoa mafunzo kwa jamii mbalimbali duniani.Mifano mizuri ya idhaa hizi ni TeleMundo, Zee World,Holly wood n.k Idhaa hizi zimeiteka jamii bakunja kuhusiana na vipindi vyake babu-kubwa vilivyo na maudhui pana ya jamii.Hii ni pamoja na kikosi maarufu nchini Kenya ambacho kimejitokeza kuigiza michezo mabalimbali ikiwa pamoja na tamthilia teule zinazotahiniwa katika shule za upili nchini.

Tano, katika kuburudisha, hapa jamii inaburudishwa na vipindi mbalimbali vya kijamii katika tamthilia, muziki ngoma n.k. kupitia runinga, video, tarakilishi, pata-ninga-DVD n.k. Hapa Kenya vipo vipindi ainati vya burudani kama Kipindi cha muziki kiitwacho “Roga roga” kwenye Radio Citizen kila wikendi na Fred Obachi Machoka, “Mseto East Afrika” kwenye runinga ya Citizen na Mzazi Willy M. Tuva,kipindi cha Mzooka kwenye Maisha Magic Swahili ambacho hucheza miziki hasa ya kizazi kipya ya kuruka majoka(ngoma za rapu).

 

Sita, katika kuipa jamii tumaini la maisha. Aghalabu hii hujitokeza katika vipindi mbalimbali vya kidini (kikristo na kiislamu) ambavyo vimezagaa katika idhaa mbalimbali ima redio runinga au setilaiti. Mifano mizuri ni vipindi chungu nzima  vya wahubiri mashuhuri hapa nchini Kenya: James Maina ng’ang’a(Neno Everngelism Centre), Mark Kariuki(Life Celebration Centre), Pius Muiru(Kuna Nuru Gizani),  Mhubiri. Peter Manyuru (JTM), Dr. Prophet Owuor (Ministry of Repentance and Holiness) na wengine wengi ambapo wana vipindi chekwa katika idhaa mbalimbali za hapa nchini Kenya. Mbali na hawa pia kuna wale wa kimataifa ambao pia jamii huwapata moja kwa moja kupitia vitandazi tofauti tofauti. Bila kusahau kipindi maalumu cha Ukumbi wa Kiislamu katika runinga ya KBC pamoja na idhaa maalum ya kiislamu kwenye ving’amuzi mbalimbali.

 

Aidha kwa upande mwingine mabadiliko haya ambayo yameigeuza dunia kuwa ndogo na ndogo kila kukicha, yameonesha kwamba udogo huu wa dunia unaotokana na teknolojia mpya ya mawasiliano, ambayo imekuwa ya kisasa zaidi. Teknolojia hii ndiyo iliyozaa dhana mpya ya fasihi simulizi ya kileo iliyochukua nafasi ya dhana iliyoitangulia ya fasihi   simulizi ya zamani. Kwa mtazamo wa juu zaidi twaweza kusema kuwa ni fasihi ambayo watu wa kizazi hiki wanaiita kuwa ni fasihi inayokwenda na wakati, fasihi ya kisasa au fasihi iliyokwenda shule.

 

Wataalamu wengi wa intaneti wamefungua tovuti mama kwa nia ya kuharakisha mawasiliano duniani. Wanafunzi wengi sana wamejifunza kutumia kompyuta na kwa kupitia teknolojia hii wamekuwa wakipata elimu ya mbali kwa gharama nafuu. Teknolojia ya setelaiti, intaneti imekuwa ikitumika ili kuboresha elimu ya juu na kupiga hatua ya maendeleo ya sayansi na teknolojia. Aidha televisheni, video, mitambo ya setelaiti na ving’amuzi vimekuwa vikitoa misaada inayojumuisha mafunzo makini ya kuwasaidia walimu kuboresha taaluma zao. Walimu na wanafunzi waliokuwa katika hali ya kukata tamaa juu ya namna ya kuimarisha ufundishaji, wameanza kubaini matunda ya mpango huu wa kutoa elimu kwa kutumia teknolojia hii. Japo kuwa katika mpango huu vifaa ni haba, shule na vyuo vinaendelea kujitahidi kuongeza ufanisi wa ufundishaji wake pamoja na kuimarisha jamii watokako wasomaji. Hatua hii hapana shaka itasaidia sana katika kuongeza viwango vya wanafunzi kufaulu.

 

Kwa upande mwingine tumeona kwamba maendeleo haya ya programu za tarakilishi yameikuza elimu ya sayansi na teknolojia kwa kiasi kwamba hata madaktari bingwa wa upasuaji wa magonjwa ya moyo wamekiri kuwa inafaa. Aidha kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na mwandishi wa gazeti la Mtanzania la tarehe 13.06.03 ukurasa wa 9 ambapo mwandishi ambaye jina lake halikutajwa aliinukuu makala iliyochapishwa katika gazeti la Uingereza Sunday Times Kwa mujibu wa makala hiyo, mwandishi ametuelezea jinsi elimu ya sayansi na teknolojia inavyotufikisha mbali akiwa anatumia mfano wa programu ya kompyuta iliyovumbuliwa na wataalamu huko Uingereza inayoweza kuwaamba mabingwa wa upasuaji iwapo inafaa kumfanyia upasuaji mgonjwa wa moyo.

Kwa kuangalia maendeleo hayo ya kasi ya teknolojia ya mawasiliano na kuzingatia ukweli uliojitokeza kwamba dunia ni mahali pa ujirani, kuna aina fulani ya kukaribiana kwa watu kupitia hizo njia mpya na za kisasa zaidi za mawasiliano.

Kama tulivyokwishaona, hivi sasa dunia hususan, nchi za dunia ya tatu kama Kenya, Uganda, Tanzania na nyingine nyingi tumeikubali kwa hiari yetu wenyewe na kuipokea aina hii mpya ya fasihi simulizi. Aidha katika kuikubali huku, kumetokea na kumekuwepo na vituo vingi vya mitandao ya kielektroniki ambapo vijana wanapoteza muda mwingi sana kuwasiliana na vijana wenzao duniani, wanabadilishana mawazo  na kuelimishana mambo mengi sana yanayowahusu vijana hao.

c)     Athari hasi  za teknolojia mpya katika  fasihi simulizi

Hakuna jambo zuri linalotokea duniani bila ya kupatikana kwa ubaya wake.Hoja hii ina mshabaha na methali isemayo: “Hakuna masika yasiyokuwa na mbu” Mafanikio haya ya kisayansi na teknolojia mpya, yameleta athari kubwa sana katika fasihi simulizi, hususan katika utamaduni, mila na desturi zetu. Amali hii ambayo ni utajiri mkubwa wa taifa lolote  lile ni muhimu sana katika nchi.

Teknolojia mpya ni utamaduni mpya kutoka nchi za Ulaya na Marekani zilizoendelea, ambazo zina utamaduni wenye nguvu ukilinganisha na tamaduni za Kiafrika ambazo ni dhaifu kimataifa. Kwa hivyo, kutokana na utandawazi tunalazimika kuonyesha vipindi vingi vya Tamthilia vya nje ya nchi kuliko vya ndani ya nchi. Mfano tamthilia nyingi za kigeni kama Egoli, The Bold & The Beautiful, Days of Our Life, La Mujer de mi Vida (Woman of My Life), Isindingo, n.k. zinaonyeshwa na Televisheni zetu za hapa nyumbani kama KTN,CITIZEN,K24 n.k

Teknolojia mpya inaenda sambamba na utandawazi ambao ndani yake kuna udhalilishwaji wa nchi za ulimwengu wa tatu kama Tanzania, Uganda, Kenya na nchi nyingi nyingine zipatikanazo hasa katika bara la Afrika. Kwa hali hiyo utakuta kuwa nafasi ya fasihi simulizi ya nchi zinazoendelea kama Tanzania katika teknolojia ni finyu sana katika kujitangaza.

 

Matumizi ya zana za kisasa katika muziki wa dansi, hususan Bongo Flava yanachangia kwa kiasi kikubwa kupunguza ladha halisi ya kitamaduni ambayo ingepatikana kama ngoma, marimba, vinubi, matoazi na ala nyingine zingetumika. Aidha kwa kutumia fasihi simulizi ya kileo kumezuka lugha za namna nyingi katika jamii zetu. Lugha hizi zimetokana aidha na filamu jamii inazoziangalia katika vipindi vyetu vya televisheni. Kumekuwepo na misuguano kadhaa kati ya watu wa bara na watu wa pwani hususan wa Mombasa hapa Kenya kuhusu lugha za mitaani zinazotumika katika televisheni zetu ambazo wakenya wenzao wa bara wanashindwa kukubali kwani baadhi ya misamiati hiyo haipo katika misamiati ya Wakenya wenzao. Kwa mfano baadhi ya msamiati anaoutumiwa na watangazaji kama Baya Kitsao wa Radio Rahma Mombasa: filfi-nyange. au msamiati aliokuwa akitumia mwendazake Profesa Ahmed Sheikh Nabahany  na wengine wengi

 

 

Halikadhalika kumekuwa na wimbi kubwa la wanajamii pamoja na mashabiki wanaoshabikia filamu na maonyesho mengi yanayoonyeshwa katika televisheni na kumbi zetu za starehe. Filamu hizi na maonyesho haya yanatuonyesha mila, desturi na itikadi za jamii husika. Kwa mfano maonyesho ya Filamu za Zee Word, Telemondo,Televisa na nyinginezo nyingi za Kimarekani, Kinaijiria, Kighana, Kikongo, Kihindi na nyinginezo nyingi. Mapokeo ya filamu hizi kwa jamii ya Kikenya ni yale ya kupata na kujua tamaduni za wenzetu hawa. Katika kupata na kuiga tamaduni hizo za wenzetu, ni dhahiri kwamba kunabadilisha mwenendo na mwelekeo wa taifa kisiasa, kijamii, kiutamaduni, kisaikolojia na kiitikadi. Mabadiliko haya yanaweza kuibadilisha jamii hususan vijana wa marika yote katika kuiga tamaduni, mila na desturi za mataifa mbalimbali.

 

Aidha maneno yanayotumika katika nyimbo zinazoimbwa na wasanii wanaoshiriki kucheza filamu mbalimbali hayasikiki vizuri, lugha wanayoitumia haiendani na maadili ya mila na desturi za Kikenya. Nyimbo nyingine hazina mafunzo mazuri katika muktadha wa jamii ya Kenya. Wengi wa wanamuziki wanajitangazia tu umaarufu wao pasipokujua kuwa wanatakiwa kuutangaza utamaduni wa Kiafrika. Midundo wanayoipiga na mitindo wanayoicheza haionyeshi utamaduni wa Mwafrika bali inamdhalilisha Mwafrika kwa kuonyesha namna jinsia moja inavyodhalilishwa.

 

Hii ina maana kwamba mdhalilishwaji wa kwanza katika nyimbo, filamu au maigizo tunayoyaonyeshwa aidha katika runinga zetu au tunazozisikia katika vipindi vya redio daima ni mwanamke. Zaidi ya hayo, yote tusikiayo na tuonyeshwayo yanalengwa katika utamaduni wa magharibi zaidi kuliko utamaduni wa Kikenya au wa Kiafrika kwa ujumla. Matamasha yanayotumiwa na wasanii wetu sio yale ya kuinua vipaji vyao kisanii bali ni ya kuiga mila na desturi za Mataifa ya wenzetu na wala sio za kwetu. Hii imewasababisha wasanii

wengi kudumaa na kuona kuwa hakuna haja ya kubuni na kujifunza dhana nyingine.

 

Fasihi simulizi ya kileo si mali ya jamii. Hii ni mali ya wachache kwani inapotolewa kupitia vikundi vya sanaa na utamaduni ni lazima watu walipe ili waweze kuishuhudia. Kwa hiyo imekuwa ni biashara kuliko hali halisi.Mfano mzuri ni kile kipindi maarufu hapa Kenya cha vichekesho cha Churchill Show ambapo lazima watu walipe ndipo wachekeshwe. Mbali na hapo pia wapo wanamuziki chungu nzima ambao huwa na tabia ya kuchapa muziki kwa malipo katika sehemu mbalimbali. Ifahamike kuwa wasanii hawa wana hati-miliki ya kazi yao na iwapo yeyote amgependa kuitumia, hana budi kupewa ruhusa nao kwa maandishi la sivyo kuna uwezekano wake mkubwa wa kujikita taabani.

 

d)    Athari chanya  za teknolojia mpya katika  fasihi simulizi.

Teknolojia mpya ni njia ya kisasa zaidi katika kuhifadhi fasihi simulizi ili kutunza kumbukumbu. Kwa mfano historia ya zamani ya jamii  kabla ya ukoloni kuhusu maisha ya mababu na mabibi zetu inaweza ikarekodiwa kwenye mikanda na kusikilizwa na hadhira. Mfano mzuri ni Filamu inayoonyesha juhudi za mapiganaji wa MAU MAU walipokuwa wakitafuta kuikomboa Kenya kutoka mikononi mwa mkoloni.

Kwa utashi huo ina maana kuwa teknolojia mpya ni utaalamu wa hali ya juu, hivyo kazi zimekuwa za ubora wa hali ya juu. Teknolojia mpya ina faida nyingine nyingi katika kukuza fasihi simulizi ya Kiswahili. Mfano katika jamii ya leo  hasa taifa la Kenya kwa ujumla kuna vituo vingi vya redio na televisheni ambavyo hurusha matangazo yake sehemu mbalimbali hapa  nchini Kenya  na nje ya mipaka yake.

 

Kwa kupitia vituo hivyo fasihi simulizi imeweza kuwafikia watu wengi ambao wako mbali ambako matangazo hayo  ya redio na televisheni yanafika. Katika vituo mbalimbali vya runinga hapa  nchini kuna vipindi mbalimbali vya watoto ambapo hadithi, vitendawili, methali, mafumbo husimuliwa kwa watoto walioko pale studio na wengineo ambao huyapata matangazo hayo kupitia sehemu walizopo. Katika idhaa ya redio ya Radio Salaam   kuna kipindi cha watoto kila siku ya Jumamosi saa tatu asubuhi.

Kule nchini Tanzania  siku ya Jumapili saa tisa alasiri kuna kipindi cha mgongano wa mawazo ambapo fasihi ya Kiswahili husimuliwa kwa jamii hasa fasihi ya vitabu ambapo huwa kuna mjadala kuhusu mada mbalimbali za kifasihi na huendeshwa na wanafunzi chini ya usimamizi wa walimu wao.

Hapa nchini Kenya kulikuwa na kipindi cha Kamusi ya Changamka kwenye NTV kikiongozwa na Nuhu Bakari na Mnene Nyaga, katika runinga ya KBC kuna kipindi cha mashindano ya mijadala kwa shule za upili ambacho hukuza vipawa vya ulumbi kati ya wanafunzi wa shue za upili. 

Kwa upande wa redio nchini Tanzania vipo vipindi kadhaa katika Radio One Stereo, ambapo baadhi yake ni kile cha watoto ambacho hurushwa kila siku ya Jumamosi asubuhi, na kimekwishadumu kwa muda mrefu kikiwa kikiendeshwa na mtangazaji wa muda mrefu wa redio nchini Tanzania, Julius Nyaisanga, ambaye katika kipindi hicho cha watoto hujulikana kama Babu wa Kimanzichana. Kimanzichana ni moja ya sehemu maarufu katika mkoa wa Pwani ambayo ipo kijijini. Radio Tanzania na Televisheni ya Taifa nao hawako nyuma katika hilo. Nao pia wana vipindi mbalimbali kama zilivyo redio na televisheni nyingine. Mfano mzuri redio Tanzania wana vipindi kama “cheichei Shangazi” na “mama na mwana”, ambapo hadithi mbalimbali zenye semi, mafumbo, methali na vitendawili husimuliwa.

Hapa nchini Kenya idhaa mbalimbali za redio nazo zina vipindi mbalimbali ambavyo huangazia maswala ya Kiswahili.Radio Maisha kuna kipindi cha Bahari ya Lugha chini ya nahodha wake Hassan Mwana wa Ali (Mtoto wa Nyumbani) kila Jumamosi asubuhi ambaye huwashirikisha wataalam mbalimbali wa Kiswahili wakiwa pamoja na Ustadhi Guru Wallah bin Wallah, mwalimu Tsalwa na wengine wengi. Kwenye kipindi hiki Mashairi hughaniwa, wanafunzi wakahojiwa na uchambuzi mbalimbali ukafanywa pamoja na chemshabongo mbalimbali hasa kutoka kwa Guru Ustadh Wallah bin Wallah ambaye pia huwa na hadithi za kuibua hisia za kutafakari ambazo huionya, kuisifu na kuielekeza jamii ifaavyo.

Waaidha  jijini Mombasa kuna idhaa ya Radio Rahma ambayo huangazia kipindi cha Ndimi za Malenga kila Jumamosi saa nane hadi saa kumi alasiri. Kipindi hiki huongozwa na Baya Kitsao pamoja na mwalimu Newton Omukabe. Kwenye kipindi hiki, mambo mbalimbali huangaziwa yakiwa pamoja na ughani na uchambuzi wa mashairi, uchambuzi wa vitabu mbalimbali vinavyotahiniwa katika kidato cha nne  na mengine mengi.Radio rahma kwa upande wake jijini Mombasa, ina kipindi cha Ukwasi wa Lugha ambacho pia huangazia fani mbalimbali za lugha huku wakishirikisha wataalamu mbalimbali kutoka mwambao.

 

e)     Hitimisho

Fasihi simulizi hapo  zamani ilikuwa imekitwa katika misingi mikuu miwili; moja, mila na de- sturi. Mbili, fasihi simulizi ya kale ililenga kutoa huduma zaidi na si biashara. Fasihi hii inafikisha ujumbe katika jamii ikiwa na lengo la kuelimisha, kuonya, kuburudisha na kukosoa.

Teknolojia mpya katika fasihi simulizi ina faida na hasara kama tulivyobainisha. Fasihi simulizi hii imekitwa katika misingi mikuu miwili. Moja, sayansi na teknolojia; mbili, ni biashara. Fasihi hii inaua utamaduni wa jamii. Mfano watoto na vijana wengi hivi sasa wanafurahia na kufahamu mambo mengi ya Ulaya, Amerika na tamaduni zao kuliko tamaduni za jamii zetu za kiasili. Haya wanayafahamu kupitia televisheni, video na intaneti. Fasihi simulizi ya kileo imekuwa ni biashara zaidi kuliko kutoa elimu kwa jamii kama huduma ya kawaida. Hivyo kwa kadri tunavyozidi kuwa karibu zaidi utandawazi na matumizi ya teknolojia mpya katika maisha yetu ya kila siku, nchi za Kiafrika ni lazima ziwe bunifu kwa tamaduni zao wenyewe ili kuepukana na hasara zinazopatikana kutokana na kuwepo kwa teknolojia mpya.

Aidha kwa upande wa vifaa, nchi nyingi za Kiafrika zimeshindwa kuagiza vifaa na kutumia teknolojia mpya kutokana na sababu kwamba ni ghali sana. Hii inahatarisha uchumi wa nchi hizi kwa kuzifanya ziwe tegemezi katika kuipata teknolojia mpya. Teknolojia mpya ni nguzo muhimu sana katika maendeleo ya fasihi simulizi si katika jamii ya Wakenya  tu, bali ulimwenguni kwa ujumla. Hii ni kwa sababu inawawezesha watu wengi zaidi kupata matangazo ya moja kwa na wakati mwingine wao kushiriki kwa kupiga simu na kuchangia wanachopaswa kama ni kusimulia hadithi, vitendawili, nyimbo, ngonjera n.k.

Lakini wengi wanaofaidi huduma hii ni wale walioko mijini na katika vijiji vichache ambapo matangazo ya redio na runinga yanafika na kwa bahati nzuri katika dunia  ya leo sehemu nyingi sana za mijini na vijijini wanapata matangazo ya redio mbalimbali zilizopo nchini. Kwa upande wa runinga zaidi ni mijini kuliko vijijini ndio wanaofaidi huduma hii kwa kiwango kikubwa. Teknolojia mpya ina faida nyingine nyingi katika kukuza fasihi simulizi ya Kiswahili. Mfano katika jamii hasa hapa nchini Kenya tuna vituo vingi vya redio na televisheni ambavyo hurusha matangazo yake sehemu mbalimbali nchini. Kupitia vituo hivi fasihi simulizi imeweza kuwafikia watu wengi ambao wako mbali ambako matangazo hayo ya redio na televisheni yanawafikia.

 

Marejeleo

 

·        Gazeti la Mtanzania la tarehe 13.06.03.

·        Kimani N. 2006. Fasihi Simulizi na Nadharia ya Fasihi ya Kiafrika, katika Fasihi ya Kiswahili. Nairo- bi: Twaweza Communications. Uk. 1 – 10.

·        Kirumbi, P. S. 1975. Misingi ya Fasihi Simulizi. Nairobi: Shungwaya Publishers.

·        Matteru, M. D. 1983. Fasihi Simulizi na Uandishi wa Kiswahili, katika Fasihi: Makala za Semina ya Kimataifa ya Waandishi wa Kiswahili. Dar es Salaam: TUKI. Uk. 26 – 37.

·        Mlacha, S. A. K. 1995. Fasihi Simulizi na Usuli wa Historia ya Pemba. Katika: Lugha, Utamaduni na Fasihi Simulizi ya Kiswahili. Dar es Salaam: TUKI/ITAA. Uk. 16-26.

·        Msokile, M. 1992. Kunga za Fasihi na Lugha. Kibaha: EPD.

·        Wamitila K. W. 2003. Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi, Kenya: Focus Publications. Wamitila, K. W. 2003. Kichocheo cha Fasihi: Simulizi na Fasihi. Nairobi, Kenya: Focus Publications.

 

No comments:

Post a Comment