Monday

UHAKIKI WA FUMO LYONGO KWA KUTUMIA NADHARIA YA VIKALE

0 comments

 

UHAKIKI WA HADITHI YA  FUMO LYONGO KWA KUTUMIA NADHARIA YA VIKALE.

Nadharia ya vikale ni mojawapo wa nadharia critical theory.Hii ni nadharia ambayo kuchanganua maandishi hasa visa vya kikale kwa kuelekeza makali yake kwenye ngano za kimiujiza.Mifano ya ngano hizi za kimiujiza ni mighani.

Nadharia hii imeelekeza mizizi yake katika miaka ya 1934 wakati Maud Bodkin alipokichapisha kitabu chake, Archetypal Patterns in Poetry. Nadharia hii ina Mihimili yake miwili mikuu katika vitengo viwili vya kiakademia. Vitengo hivi ni Anthropolojia na saikolojia Kila mhimili huchangia nadharia hii katika njia tofauti teule. Saikolojia hujitokeza kama tawi dogo la nadharia hii ya vikale. Nadharia ya vikale ilitia fora mno katika miaka ya 1940 na 1950 kutokana na kazi ya mchanganuzi wa vikale kutoka Kanada, Northrop Frye. Ingawa nadharia hii ya vikale haijatamba na kutaratamba pakubwa, bado inashikilia nafasi kubwa muhimu katika jamii zetu za kiutamaduni. .

Usuli wa athropolojia ya vikale unaupiku usuli wa saikolojia kwa zaidi ya miaka thelathini(30) Maandishi The Golden Bough (1890-1915) ya mwana-anthropojia kutoka Uskoti , Sir James George Frazer ndiyo yaliyokuwa makala ya kwanza ambayo yaliangazia hadithi kama hizi za kimila. Frazer alikuwa mmoja wa wanaathropolojia wachanganuzi waliokuwa katika chuo kikuu cha Cambridge ambao walifanya kwa jino na ukucha kwenye makala : The Golden Bough.

Frazer alipokuwa akifanya haya yupo mwenziwe Carl Gustay Jung, na Frye. Wapo wana-lugha ambao vilevile  walitoa mchango wao wa kuunga mkono wazo hili ni pamoja na Maud Bodkin. Kutokana na maelezo ya awali basi vikale vina usuli wa ukongwe katika jamii za wanadamu.

Ili kuthibitisha hili ,wapo watafiti wa nadharia ambao vilevile wamekita kambi katika fani hii ya vikale.

Makumbo yote mawili haya ya anthropolojia na kisaikolojia katika swala zima la vikale yana umuhimu mkubwa. Katika upande wa Anthropolojia masomo ya nadharia ya vikale huhamasisha akili zetu kuhusu vikale ambapo imani ya wasomi kama vile Joseph Campell ni msingi wa ujumbe kwa msomi yeyote na hutupa wakati mwafaka wa kujadili na wenzetu katika vitengo mbalimbali.

Swala la kuwepo kwa mashujaa halina mipaka kiasi kwamba inavuka mipaka ya Utamaduni na kiwakati kwa kuaonyesha wazi kuwa binadamu ni mmoja tu. Kwa upande wa kisaikolojia, nadharia ya vikale huangazia maisha yetu namna yalivyo hasa tunapochanganua maswala kuhusu mashujaa na ushujaa wao mbalimbali katika jamii. Tunapotazama mashujaa hawa wakipambana na maisha, kwa kuanguka, kujifunza, kuvumilia na kupitia katika hali za faraja na hofu, ni taswira kabambe inayodhihirisha wazi hali halisi ya maisha yetu jinsi yalivyo. Hivi ni kusema kuwa kujifunza maswala ya vikale hutuweza kujitambua na kujijua jinsi tulivyo.Kwa hivyo tunapodadavua maswala ya nadharia ya ukale sio tu ati tunarejeshwa kuhusu ukale wa mambo namna yalivyokuwa bali hutuwezasha Kujua ukale wetu binafsi.

Kwa mujibu wa Wafula R.M na N. K. (2007:106), Vikale ni picha kongwe zinazotokea mara kwa mara katika kazi za fasihi. Vikale hivi vinaweza kuwa taswira, wahusika, miundo ya usimuliaji na fani zingine zinazopatikana katika fasihi yoyote.

Abrahams (1971:11-12), alieleza nadharia ya uhakiki wa vikale kwa mitazamo miwili. Alieleza kuwa chimbuko la nadharia hii ni kutokana na kazi ya James G.Frazer katika kitabu cha “The Golden Bough” (1890-1915) kilichotolewa na katika idara ya Antropolojia Linganishi, Chuo Kikuu cha Cambridge. Abrahams (1971:11-12) aneleza kuwa kitabu hiki kilifuatilia ruwaza za kimsingi za visaasili na za kitambiko ambazo alidai hujirudiarudia katika visakale na taratibu nyingi katika tamaduni anuwai.

 Kwa upande mwingine alieleza kuwa, nadharia ya vikale ilitokana na maelezo ya Carl G. Jung kuhusai na na akili-laza. Jung alikuwa mwanafunzi wa Sigmund Freud, mtaalamu aliyeasisi taaluma ya uchanganuzi nafsia. Lakini walitofautiana kimawazo. Wakati ambapo Freud alisisitiza akili-laza ya kibinafsi, naye Jung alisisitiza kuhusu akili-laza jumuishi. Jung alitumia istilahi ya vikale kwenye taswira za asili za Kumbukumbu zinazorudiwarudiwa kutokana na tajiriba katika maisha ya tangu mababu zetu wa kale.

Alisisitiza kuwa, taswira hizi hurithiwa na kutiwa kwenye akili-laza jumuishi ya jamii ya watu na ambazo hudhihirika katika visaasili, ndoto, mawazo ya binadamu mathalan, katika vipengele vyote katika maisha ya binadamu wote duniani na pia katika kazi za kifasihi. Katika uhakiki wa kifasihi, vikale hutumiwa katika ruwaza ya aina za wahusika au taswira ambazo zinafanana katika tungo mbalimbal za kifasihi na pia katika visasili na mitindo anuwai ya kijamii. Kufanana katika maswala haya anuwai huchukuliwa kuakisi seti ya ruwaza bia ambazo zimekuwepo tangu jadi. Nadharia ya uhakiki wa vikale kwa hivyo inaeleza kuwa binadamu wote ni sawa popote walipo. Tofauti ni kidogo za kufikirika ambazo husababishwa na tofauti za kihistoria na za kimazingira.

Kwa mujibu wa Mutiso (1999:2). Kwa jumla, vikale hurejelea ruwaza za kimsingi. Ruwaza za jumla au bia za aina moja au nyingine ambazo aghalabu hudhihirika katika jamii za watu mbalimbali duniani. Anashikilia kuwa vikale humvuta msomaji vikitumiwa vizuri katika kazi ya fasihi.


Waitifaki wa nadharia ya vikale wanashikilia kwamba umaarufu wa kazi ya sanaa unatokana na wahusika, maudhui na taswira zinazorudiwarudiwa katika kazi husika. Baadhi ya wahusika wanaotumiwa kudhihirisha vikale ni kama: jaribosi au nguli anayeandaa safari ambayo mara nyingi huanzia utotoni hadi anapofika utu uzima ambapo safari hii inaweza kuwa ya kikweli pale nguli anajizatiti kukisaka kitu au kujisaka mwenyewe.

Katika nadharia ya vikale, mkinzani wa nguli huwa ni mhusika wa kikale ambaye hujifunga kibwebwe kuiharibu mipango ya nguli kwa kujaribu kumwangamiza. Aghalabu mhusika huyu huwa mzinzi, mlafi na wakati mwingine huwa tajiri. Hii inaafikiana na sifa za Fomo Lyongo mhusika mkuu katika mighani ya Fumo Lyongo.

Fomo Lyongo alizaliwa katika mji wa Shanga kwenye himaya ya ufalme wa Pate uliokuwa chini ya utawala wa Mfalme Mringwari. Katika ubarobaro  wake Fomo Lyongo alionekana kuwa na sifa za nguvu zake, ushujaa wake katika vita, uhodari wake katika kufuma kwa mishale, umalenga wake katika kuimba na uashairi, na umanju wake katika kucheza ngoma na kutumbuiza watu. Kwa hakika sifa hizi zilienea kama moto kwenye kituka kikavu swala ambalo lilimtia tumbo joto mfalme wa Pate ambaye alianza kupinga njama ya kumwondoa uhai.

Katika vikale hutokea vishawishi chungu nzima ambavyo hujengwa vizingiti ili nguli lengwa asiweze kutekeleza wajibu wake kikamilifu. kwa hivyo katika hadithi ya Fumo Lyongo, wapo wengi waliodhihirisha hili ili kumfanya Fumo Lyongo kutotimiza na kutekeleza mradi wake. Fomo Lyongo alipohama mji wa Pate, alisakini kwenye mji wa Ozi ambao kwa wakati huo,Waozi walikuwa wakishambuliwa na makabila mbalimbali. Kwa sababu ya nguvu zake, Fomo Lyongo alifanywa Kiongozi wao. Hili lilimzidishia jakamoyo mfalme wa Pate.

Mfalme Mringwari alifanya njama ya kumuua Fumo Lyongo akitumia mashujaa wakali wa kabila la Wagala.Wagala walifululiza hadi mji wa Ozi wakiwa na nia ya kumwangamiza Fumo Lyongo ingawa walipowasili walifahamishwa kuwa hakuwepo wakati huo kwa vile huwa yeye huenda mawindoni na kurudi siku ya pili baadaye. Hata hivyo mashujaa wa Wagala walitulia na kumsubiri hadi wampate na kumwangamiza. Kwa kweli vikale huwa na nguli mbao huyatenda mambo yasiyo ya kawaida.Fumo Lyongo alipotoka mawindoni, alipuliza panda yake.Kwa mshangao Wagala hao walitanabahi kuwa zile panda zote mbili alizozipulizwa, zilipasuka.Hali hii iliwaingiza mugma wa hali ya juu kwa kuhofu namna Fumo Lyongo alivyokuwa na nguvu kiasi hicho. Hofu iliwaingia na kuondoka bila kwaheri jinsi walivyoingia bila hodi wala karibu.

Kwa kweli vikale kwa ujenzi wake huwa na mhusika mmoja ambaye huiongoza njama ya kuyawekea mitego na viunzi matendo ya wahusika wakuu ambao huwa nguli. Kwa hivyo mfalme wa Pate hakufa moyo.Aliwakabidhi Wasanye na Wadahalo wanamoishi msituni kumwuua pindi aendapo kuwinda.

Njama yao iliteguka. Mahasidi hawa walimwita Fumo Lyongo kwenye karamu ya kikao. Kila mmoja alihitajika  kuchuma makoma ambayo yataliwa kwenye kikoa. Mtego wao ulikuwa  eti pindi tu Fumo Lyongo apandapo kuchuma makoma, ndipo wangemwangamiza. Hata hivyo Fumo Lyongo kwa weledi na uhodari wake, kwa kutumia weledi wake wa kufuma, alifuma na kuangusha fungu zima la makoma. Hilo liliwafanya Wasanye kuwa na hofu na kukosa tumaini la kumwangamiza.

Ila za mfalme wa Pate hazikukoma kama koma zilizokoma kurudi kwenye mkoma.Aliwaarifu Wasenye wamwalike Fumo Lyongo kwenye ngoma ya mdundo wa gungu ambayo aliipenda sana. Hii ndiyo hila iliyofaulu kwa kuwa Fumo Lyongo hakuweza kustahimili mawimbi ya mdundo huo. Hii ilikuwa nafasi murua na mwafaka  ya kutekeleza unyama wao ambapo walimtia nguvuni kwa Kufungwa kwa pingu na silisili hadi gerezani Pate.

Katika nadharia hii ya vikale , hutokea mhusika mmoja mwenye hekima ambaye hutumiwa kumwasa nguli.Katika hadithi hii, kuna binti mjakazi kwa jina Saada ambaye kila mara alitayarishiwa mkate na kumpelekea Fumo Lyongo akiwa gerezani. Alipopata habari kuwa angeuawa ingawa kabla ya hapo aombe lolote ambalo angetaka.Kwake aliomba apewe nafasi ya kuwatumbuiza wageni katika harusi ya nduguye.

Kwa ujanja wake, Fumo Lyongo alimpa mjakazi ujumbe kwa wimbo wa kuandaliwa mkate kisha awekewe ndani tupa ya kukerezea minyororo. Alipofanya hivyo akiwa kwenye gungu watu walishangaa kuona kuwa Fumo Lyongo akiwa huru Huria. Alitoroka kutoka hapo hadi akafika Ozi.

Katika nadharia ya vikale hutokea mhusika mmoja ambaye huwa na ukuruba wa karibu na nguli na yuyo huyo ndiye atumiwaye kumwangamiza. Mhusika huyu huwa mwenye wingi wa ubinafsi wa kujitakia makuu. Hata hivyo wanaomhadaa huelekea kwenye mtindo wake wa maisha huku wakimpa ahadi chungu nzima kwa kutekeleza maangamizi ya nguli.

Kwenye hadithi hii mwanawe Fumo Lyongo aliyekuwa na usuhuba na binti mmoja kutoka Pate ndiye aliyetumiwa kutia babaye hatarini. Alipewa ahadi kuwa iwapo angemwua babaye basi angeozwa yule binti kutoka Pate ambaye alimtaka. Kijana huyo aliwatobolea siri ya ushujaa wa Fumo Lyongo kuwa akitiwa tu sindano kwenye kitovu, basi huo huwa mwisho wake wa kuishi.

Kijana huyo kwa ujanja na hila zake alimdunga Fumo Lyongo kitovuni. Fumo Lyongo aliondoka na maumivu hadi mtoni ambapo alifia. Kikawa kilio mjini Ozi huku mfalme wa Pate akiwa na sherehe kisirisiri.

Katika kazi hii nitatumia mtazamo wa mtaalamu Gustav Jung kwa kumuonyesha hadithi hii  anavyomsawiri Fumo Lyongo katika safari ya kuijenga jamii adilifu kuonyesha maudhui ya wema na uovu na jinsi mhusika huyu anavyopambana na vipingamizi kutoka kwa wakinzani wake, Mfalme Mringwari  wa Pate. Haya yote ni katika kudhihirisha kuwa fasihi simulizi ni picha kongwe za fasihi zinazotokea mara kwa mara katika jamii zetu.

Hitimisho

Kazi hii inatalii kwa muhtasari maisha na wasifu Fumo Lyongo wa Ozi. Ni muhimu kutaja kuwa makala haya yametuwezesha kumulika na kuelewa wasifu wa Kiongozi huyu aliyekuwa mashuhuri. Kupitia kazi hii, tumedhihirisha kwamba vikale  ni tukio la kihistoria. Hadithi ya Fumo Lyongo ni dhihirisho tosha kuwa nguli na majagina ni wahusika ambao kwa njia moja ama nyingine hupimana nguvu, maarifa na uwezo katika jamii zetu.Waaidha makala haya yanadhihirisha kuwa  ni muhali kuitenga jamii na historia.

Kwa hivyo ili kuyaelewa haya fika si jingine ilakuzama katika nadharia ya vikale inayotupa mwongozo na kioo thabiti cha kuyachanganua haya yote.

Marejeleo

 Kiswahili kwa kidato cha pili(Toleo Jipya)-2005-Uk.60-64, KLB, Nairobi

Aristotle(1965).“Poetics”,Classical Literary Criticism.  Harmondsworth: Penguin.

Bakhtin, Mikhail (1989).  The Dialogic Imagination.  Austin: University of Texas Press.

Blamires, Harry (1995).A History of Literary Criticism.London: Macmillan.

Cuddon, J.A. (1977). A Dictionary of Literary Terms.Oxford: Blackwell.

Daiches, David (1981). Critical Approaches to Literature.London: Longman..

Dundes, Alan (1965).  The Study of Folklore.  NJ: Prentice Hall, Inc.

Eagleton, Terry (1983).  Literary Theory: An Introduction.  Oxford: Blackwell.

Esslin, Martin.  The Theatre of the Absurd.  London: Methuen.

Feud, Sigmund (1950).  The Interpretation of Dreams.

Harland, Richard (1999).  Literary Theory: From Plato to Barthes.  New York: St. Martins.

Kimani Njogu et.al. (1999).  Ufundishaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu.  Nairobi: Jomo Kenyatta.

Lord, Albert (1960).  The Singer of Tales.  Cambridge: Harvard University Press.

Murfin, Ross ed. (1991).  The Case Studies in Contemporary Criticism.  New York: St. Martins Press.

Musau, Paul (1985).  Kezilahabi: Mwandishi Aliyekata Tamaa.  Tasnifu, M.A.  Chuo Kikuu cha Nairobi.

Ngugi wa Thiong’o (1986).  Decolonising The Mind.  London: HEB.

Scholes, Robert (1974).  Structuralism in Literature.  New Haven: Yale University Press.

Wafula, R.M.& Kimani Njogu (2007).  Nadharia za Uhakiki wa Fasihi.  Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

Wafula, R.M. (1999).  Uhakiki wa Tamthilia: Historia na Maendeleo Yake.  Nairobi:  Jomo Kenyatta Foundation.

Wamitila, K.W. (2003).  Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia.  Nairobi: Focus Books.

Wamitila, K.W.  (2002).  Uhakiki wa Fasihi.  Nairobi: Phoenix.

Zirimu, Pio ed.(1971).  Black Aesthetics.  Nairobi: Kenya Literature Bureau.

 Abrams, M.H. "Archetypal Criticism. (1999)" A Glossary of Literary Terms. 7th ed. Fort Worth: Harcourt Brace College Publishers.

 Biddle, Arthur W., and Toby Fulwiler(1989). Reading, Writing, and the Study of Literature. NY: Random House.

Lynn, Steven(1998). Texts and Contexts: Writing About Literature with Critical Theory. 2nd ed. NY: Longman.

Murfin, Ross, and Supryia M. Ray.(1997) The Bedford Glossary of Critical and Literary Terms. Boston: Bedford Books.

Walker, Steven F. Jung and the Jungians on Myth. NY(2002): Routledge.

 

No comments:

Post a Comment