Friday

Mzee baba! Ili kutimiza malengo yake, mpenzi wako anahitaji haya

0 comments

  • Kati ya mambo ya kufanya ni pamoja na kumpatia mpenzi wako mtaji pale akitaka kufungua biashara au kuanzisha kitu chochote.
  • Usimpatie mawazo ya kubomoa. Toa mawazo yanayomjenga ili afanikiwe.
  • Hakikisha unaonyesha kujali mambo ambayo anayafanya.

Dar es Salaam. Wiki iliyopita tumeongelea nini wanawake wafanye ili malengo ya wapenzi wao yatimie. Meza zimegeuka wiki hii na kama nilivyoahidi, ni wakati wa kufahamu pia wakina kaka wana mengi ya kufanya kuwasaidia wapenzi wao watimize malengo yao.
Wakati kina baba wakihitaji kuonyesha uwezo wao, msaada wa kutunza fedha, na moyo pale wanapokata tamaa, haya ndiyo wanaume wanashauriwa kuyafanya ili malengo ya wapenzi wao yatimie.
  1. Mpatie mpenzi wako mtaji
Kama mwanaume, wewe ni nguzo ya familia na ni jukumu lako kuhakikisha kuwa familia yako unaijali na kuilinda. Hauwezi ukawa na pesa siku zote lakini kama unazo mpatie mtaji mpenzi wako wa kuanzisha biashara aipendayo ili asikusumbue na pesa za kusuka.
Siyo pesa za kusuka tu, mtaji utakaompa utasaidia familia hasa kwenye mambo madogo madogo hasa pale unapokuwa mbali au hata pale yeye anapohitaji kufanya jambo fulani. Kweli unataka hadi pesa ya zawadi ya mama yake akuombe? Fikiria.
  1. Kuwepo, shiriki, mpatie mawazo
Kuna haja gani ukampatia mtaji halafu ukatokomea? Unahitaji kuonyesha kuwa unafuatilia kile ambacho mpenzi wako anafanya.
Mpatie mawazo na ushauri katika kile anachokifanya. Itamtia moyo mpenzi wako na kuonyesha kuwa unamjali. Hata atakapofanikiwa, atautambua mchango wako kama kweli fadhila imo ndani yake.
Uwepo wako kwenye harakati zake zitakupatia wewe faraja kumuona akifanikiwa. Picha| Pinterest.
  1. Shiriki katika shughuli za nyumbani
Kuna mzee baba kaguna hapa! Hahaha! Wapo wanaowafokea wapenzi wao pale wanaposhindwa kutimiza majukumu fulani fulani nyumbani.
Kama wewe unavyochoka na kazi, yeye pia anachoka. Msaidie baadhi ya kazi zikiwemo kuwasaidia watoto “homework”, kama unaona msosi umechelewa, kapike naye. 
Msaidie hata kumenya karoti au hata kumsogezea kijiko anapokihitaji. Ni vitu vidogo vidogo mzee baba.
  1. Mkosoe kwa nia ya kumjenga
“Utasikia mimi nilijua tu biashara yako hiyo lazima ikusumbue” amesema mdau mmoja. 
Maneno kama hayo hayafai kwani yanakatisha tamaa. Badala yake, unapoona anaenda mwelekeo ambao siyo, hakikisha unamuita na kuongea naye ili kuyajenga. Mpatie ushauri na mwache yeye aamue kuufanyia kazi. 
  1. Mpatie nafasi
Kama wewe unavyohitaji nafasi ya kuangalia mpira bila usumbufu wake, yeye pia pale anapofanya kazi za kiofisi akiwa nyumbani, haina haja ya kumsumbua kama hauna jambo la msingi. Mpatie nafasi akamilishe kazi zake kama wewe ambavyo ungeihitaji nafasi hiyo.
Mpende, mlinde na kuwa bega la kuegemea kwake. Mafanikio yake, ni mafanikio yako.
Nitakachokuandikia wiki ijayo, ni “suprise” usikose.

No comments:

Post a Comment