Tuesday

UHAKIKI DIWANI YA MAPENZI BORA

0 comments

Katika uhakiki wa diwani ya Mapenzi Bora, utaangazia utangulizi na kiini. Ambapo katika utangulizi utaangazia shabaha ya kitabu hiki na kiini utaangazia vipengele vya fani na maudhui.

Utangulizi.

Mapenzi Bora ni diwani iliyoandikwa na Shaaban Robert mwaka 1958. Diwani hii yenye beti 700, dhumuni ni kuiadili jamii juu ya maana, faida na hasara za kukosa mapenzi bora. Kusudi la kitabu hiki ni kuandalia mahitaji ya watu waliofikia fahamu ya kuwaza na kuhoji neno au kitu au tendo kwa akili ingawa haitakuwa vibaya kama kitasomwa na watu wowote ambao hawajafikia upeo kama huo wakipenda kujiweka tayari kwa zamu yao.

Fani na Maudhui ya kitabu hiki.

Kipengele cha Maudhui, kipengele hiki kinahusisha dhamira, ujumbe, falsafa ya mwandishi na msimamo wake.

DHAMIRA

Samwel na wenzake (2013) wanaeleza kuwa dhamira ni mada, lengo, kusudi, wazo kuu linalozungumzwa na shairi au kazi ya sanaa. Wanaongeza kuwa katika mashairi huweza kuwa na dhamira ya kiuchumi, kijamii, kisiasa na hata kiutamaduni. Pia, katika kazi ya fasihi kunaweza kuwa na dhamira kuu na dhamira ndogondogo.

DHAMIRA KUU

Mapenzi yaliyo bora, katika diwani hii dhamira ya mapenzi yaliyo bora ndiyo dhamira kuu. Katika kueleza suala hili la mapenzi bora mtunzi amefafanua kwa namna tofautitofauti.

Mosi, mtunzi ameonesha maana ya mapenzi bora ni yapi, mwandishi anaona kuwa mapenzi bora ni mapenzi ya kumcha Mungu. Mungu ndiye muumba wa Ulimwengu na ndiye anayeamua jaala za wanadamu. Hivyo basi, ni muhimu kupenda na kumjali Mungu. Mathalani ubeti wa  122, mtunzi anasema:-

“Tusihini walimwengu,

 Mapenzi tumpe Mungu,

Naye atatupafungu,

Katika wake wenezi.”

Kwa mantiki hii, inaonesha kuwa mapenzi yaliyo bora kwa wanadamu ni kumtii muumba wa ulimwengu.

 Pili, mtunzi anaona kuwa mapenzi yaliyo bora ni yale ya kuthaminiana wenyewe kwa wenyewe bila kubaguana au kutengana na kuangalia tofauti zetu kama vile rangi, dini, kabila na hali ya ukiuchumi. Kwa mfano, katika ubeti wa 123, mtunzi anasema:-

“Tupendane wenyewe,

                                                            Tofauti tuondoe,

                                                            Amani iyushukie,

           Mapenzi tufanye ngazi.”

Vilevile, mtunzi katika kuelezea suala la mapenzi bora mtunzi amebainisha sifa mbalimbali za mapenzi bora kama ifuatavyo;

Mtunzi anasema mapenzi bora ni kama pambo la moyo, anaona mapenzi bora ni jambo zuri linaupendezesha moyo na haliishi uzuri wake. Kwa mfano, katika ubeti 467, mtunzi anasema;

“Mapenzi pambo la moyo,

                                                           Nifuraha kuwa nayo,

Mapenzi hushinda cheo,

            Hata pato la ghawazi.”

Kwahiyo, mtunzi anaona kuwa mapenzi ni muhimu kushinda hata cheo alichonacho mtu.

Pia, mapenzi bora ni kitu cha thamani na endapo yatatoweka itakuwa gharama kubwa sana kuyarejesha. Mathalani, katika ubeti 103- 104, mtunzi anasema;

“Wote wapige mayowe,

                                                            Mapenzi wayalilie,

                                                            Kwa kutaka yarejee,

      Na kurudi hayawezi.”

“Watayataka kwa pesa,

                                                             Yawape tena fursa,

                                                             Kitu walichokifyosa,

        Huwaje tena kipenzi!”

Vilevile, mapenzi bora hayaendani na aina yoyote ya chuki na ni dawa ya kuondokana na chuki. Kwa mfano, katika ubeti wa 471, mtunzi anasema;

“Kitu hiki ni mithaki,

   Kwa waelewa wa haki,

         Mapenzi ni dawa ya chuki,

        Kwa watu wavumilizi.”



Pia, mtunzi ameonesha faida ya kuwa na mapenzi bora kwa jamii kamaifuatavyo;

Endapo watu watakuwa na mapenzi bora wote hujiona wa namna moja pia, hawataona tofauti zao za mambo kama ubaguzi na rangi. Kwa mfano, katika ubeti wa 147, mtunzi anasema;

“Mapenzi wanayo wengi,

                                                           Wanadamu kila rangi,

                                                            Lakini hayawaungi,

   Kwa sera ya ubaguzi.”

Pakiwa na mapenzi bora dhuluma itatoweka na haki itatawala katika jamii. Mtunzi anaona kuwa haki usawiri sehemu penye mapenzi bora. Mathalani katika ubeti wa 627, 628, 630- 631, mtunzi anasema;

“Wanadamu kwa wanyama,

                                                         Na wadudu wa kuuma,

                                                         Walisafiri salama,

                Kwa imani na mapenzi.”UK. 628

Mapenzi bora huepusha majanga mbalimbali yaliyo katika jamii kama vile, chuki na uchoyo. Kwa mfano katika ubeti wa 66 mtunzi anasema;

“Ulimwengu  kama huu,

 Wenye mashaka makuu,

                                                            Kimbilio na nafuu,

         Ni palipo na mapenzi.”

Aidha, mtunzi ameonesha hasara ya kutokuwa na mapenzi bora katika jamii kama ifuatavyo;

Mapenzi yakisawiri na chuki husababisha kupotewa kwa amani katika jamii. Pia, anaongeza kuwa chuki ikisawiri katika jamii ni kitu hatari kama moto. Mtunzi anasema kwenye ubeti 333;

“Chuki inashinda moto,

                                                             Ikisadifu mateto,

                                                              Chuki ni kitu kizito,

        Kuweka hatukiwezi.”

Kukosekana kwa mapenzi bora katika jamii, hufanya watu wadhulumiane na wabaguane katika jamii. Mtunzi anasema katika ubeti wa 126;

“Ubaguzi ni husuda,

Wala hauna faida,

   Unadhuru kila muda,

           Katika kila kizazi.”

DHAMIRA NDOGONDOGO

Suala la chuki, mtunzi ameonesha kuwa chuki ni jambo mbaya sana na ina madhara pia ameifananisha na laana, huleta maudhi na husababisha athari kwa muda mfupi. Mfano ubeti 335, 336 na 345;

“Chuki madhara ya dhati,

                                                           Afadhali ya mauti,

Ni faradhi kwa umati,

                          Chuki inanyong’onyezi.”UK. 335

Suala la matabaka, mtunzi amejaribu kuweka wazi namna jamii yetu ilivyo na matabaka hasa tabaka la wenye nacho na tabaka la wale wasonacho ikiwa na maana ya masikini. Mfano katika ubeti wa 95 mtunzi anasema;

“Masikini na tajiri,

  Watu wa kila umri,

Kulia watakithiri,

           Kama hili hubarizi.”

Suala la uchoyo, mtunzi ameonesha kuwa uchoyo ni tatizo kubwa, humfanya mtu asiwe na mapenzi kwa wenzake pia usababisha uhasama na upumbavu. Kwa mfano, mtunzi anasema ubeti 378;

“Choyo kikishika mila,

                                                              Hakimpi mtu kula,

Wala nafasi kulala,

               Hurukwa na usingizi.”

Suala la ulevi, mtunzi amejaribu kuonesha kuwa ulevi wa pombe na mihadarati humfanya mtu asiwe na mawazo na fikra njema, hawe bwege na akili zisimtoshe. Kwa mfano, katika ubeti 50-52, mtunzi anasema;

   “Nahofu kanywa kangara,

 Kileo chenye madhara,

                                                            Na fikra zimegura.

    Kuzingatia hawezi.”





“Nahisi kalewa mbege,

                                                             Na sawa na mtu bwege,

     Mapenzi tunda za ndege,

        Wanyama na sisimizi.”

UJUMBE

Samwel na wenzake (2013) wanasema ujumbe ni yale mambo ambayo mshairi angependa hadhira yake ijifunze ili kuweza kufanikisha misimamo iliyojengwa na mshairi huyo.

Mtunzi amebainisha ujumbe wa aina mbalimbali katika diwani hii kama ifuatavyo;

Mosi, Binadamu wote bila kujali tajiri ama masikini anahitaji mapenzi ya dhati na yaliyo bora, kwa sababu mapenzi yanatija kwa matabaka yote. Kwa mfano katika ubeti 95.

Pili, mapenzi ya kweli ni muhimu katika mzungumzo wa maisha, kwa kuwa mapenzi ni uguzo kwa wagonjwa na ni faraja kwa yatima. Mfano, ubeti 251- 252

FALSAFA

Wamitila (2003) anasema falsafa ya mwandishi ni mawazo au wazo alilo nalo juu ya kile anachokiamini kuwa kina msingi unaotawala maisha.

Mtunzi wa diwani hii, anaamini kuwa dunia au nchi itakuwa na utulivu na amani endapo jamii bila kujali kabila, dini, rangi na matabaka watakapo na mapenzi bora wenyewe kwa wenyewe na mapenzi kwa mwenyezi Mungu muumba wa ulimwengu na Mungu atatupatia thawabu.

MSIMAMO WA MTUNZI

Mtunzi anaamini kuwa mapenzi ya kweli ni muhimu kwa maendeleo ya Nyanja zote za maisha ya binadamu.







FANI

Katika kipengele cha fani kinahusisha muundo na mtindo wa mtunzi.

MUUNDO

Senkoro (2011) anasema muundo wa kazi ya fasihi ni mpangilio na mtiririko wa kazi hiyo kwa upande  wa visa na matukio. Kwahiyo, mtunzi ana namna yake ya kusuka, kufuma, kuunda na kuunganisha tukio moja na lingine.

Mtunzi ametumia muundo wa tarbia ambao kila ubeti wa shairi una mishororo mine. Na mshororo wane ni kituo.

MTINDO

Njogu na chimerah (1999) wanasema kuwa hakuna njia moja ya kuelezea mtindo. Lakini kwa ujumla twaweza kusema kwamba mtindo ni tabia ya utungaji inayopambanua mtunzi mmoja na mwingine.

Katika diwani hii  mtunzi ametumia mtindo unaofuata kanuni za ushairi wa kamapokeo, yenye vina, ulinganifu wa mizani na mpangilio wa beti. Kila ubeti una vina vya mwisho ambavyo ni “nzi” na “zi” na kila mstari una mizani 8.

MATUMIZI YA LUGHA

Tamathali za semi

Senkoro (k. h. j) anasema ni maneno, nahau au sentensi ambazo hutumiwa na wasanii wa fasihi ili kutia nguvu katika maana, mtindo na hata sauti katika maandishi ama usemi. Wakati mwingine hutumiwa kama njia ya kuipamba kazi ya fasihi na kuongeza utamu wa lugha. Katika diwani hii tamathali za semi zilizojitokeza ni kama zifuatazo;

Sitiari, Senkoro (2011) anasema sitiari ni kama tashibiha hulinganisha vitu ama watu bila kutumia viunganishi-linganishi.

Sitiari zilizoibuka ni mapenzi ua la moyo, mfano ubeti 161. Kwahiyo, mtunzi alimaanisha kuwa mapenzi hufurahisha na kupendezesha moyo kwa mwenye nayo.

Pia, sitiari nyingine ni chuki mwanawe ni kondo.  Ubeti 280

Maisha ni utelezi, katika ubeti 641. Mtunzi akiwa na maana maisha muda wowote yanaweza kukatika.

Tashihisi, Senkoro (k. h. j) anasema kuwa tamathali hii wakati mwingine huitwa fasili ya binadamu, kuvipa sifa ya kibinadamu vitu visivyo na si hizo. Tashihisi zilizojitokeza katika diwani hii kama vile;

Tunachekwa na wadudu wajinga wa kuabudu, kwa mfano, ubeti 201. Mtunzi anawapa sifa ya kucheka wadudu kama binadamu. Pia, chuki ilie kwa wivu,  mfano ubeti 583. Kondoo na mbwa mwitu hawakuteta kwa kitu, mfano ubeti 630.

Tashibiha, Gibbe (1980) anasema kuwa ni tamathali ambayo hulinganisha vitu viwili kwa kutumia viunganishi linganishi mbalimbali kama vile, mithili ya na kama kwamba. Tashibiha zilizoibuka katika diwani hii ni;

Mapenzi kwa mwanadamu, kama mshipa na damu, mfano ubeti 86. Akiwa na maana ya utegemezi wa vitu hivi viwili.

Twanuka kama kutuzi, mfano ubeti 298. Mtunzi anaona wasio na mapenzi bora wananuka kama kutuzi.

Mubaalagha, Mulokozi na Kahigi (1979) wnasema kuwa dhima ya mubaalagha ni kuongeza utamu na kuleta athari fulani. Kwa mfano katika diwani hii mubaalagha kadhaa imejitokeza;

Nyuso zikifanya mito, ya machozi ya fukuto, katika ubeti 94

Nyuso zete zitatota kwa bahari ya machozi, katika ubeti wa 93

MBINU NYINGINE ZA KISANAA.

Takriri, Msokile (1993 ) anasema takriri ni moja kati ya vipengele vya matumizi ya lugha katika kazi ya fasihi ambapo kuna kuwa na marudirudio ya herufi, silabi, neno kirai, sentensi na wakati mwingine hata aya nzima. Katika diwani hii takriri zilizoibuka ni kama zifuatavyo;





“Chuki” katika beti ya 330- 336, kuna “choyo” katika ubeti wa 364- 385, kuna “tata na tatizi” katika ubeti wa 296-297.

Mazida, ni mbinu ya kisanaa ambayo mtunzi hurefusha neno kwa lengo la kupata vina ama idadi ya mizani, kwa mfano;

Neno, “zamani” katika mshororo usemao “watu wa zamani hizi” akimaanisha “zama hizi” ubeti wa 98. Pia, “wataalumuzi” katika ubeti wa 648 akimaanisha “wataalamu”

KUFAULU KWA MTUNZI

KIFANI

Mtunzi ametumia Kiswahili fasaha kilichojaa tamathali za semi kama vile, tashihisi, sitiari mbaalagha, tashibiha na mbinu nyingine za kisanaa kwa lengo la kuipamba kazi yake na kuongeza utamu wa lugha.

KIMAUDHUI

Mtunzi ameonesha umuhimu wa kudumisha mapenzi bora kwa jamii, pia ameonesha mapenzi bora ni yapi na kujaribu kuonesha mambo ambayo jamii inaweza kukumbananayo wasipo zingatia kuwa na mapenzi bora. Wamitila, K. W. (2003). Kichocheo cha Fasihi: Simulizi na Andishi. Nairobi: focus publications Ltd.















                                                                  MAREJELEO

Gibbe, A. G. ( 1980). Shaaban Robert: Mashairi. Dar es Salaam, Tanzania Publishing House.

Mulokozi, M. M. na Kahigi, K. K. (1979). Kunga ya Ushairi na Diwani Yetu. Dar es Salaam.   

                                                                    Tanzania Publishing House.

Njogu, K. na R. Chimerah (1999). Ufundishaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu. Nairobi.                                              

                                                       Kiswahili Tertiary Publishing Project.

 Robert, S, (1958). Mapenzi Bora. Dar es Salaam. Mkuki na Nyota publishers Limited.

Samwel, M na wenzake, (2013). Ushairi wa Kiswahili, Mwongozo kwa Walimu wa Kiswahili na

                                                    diwani ya MEA. Dar es Salaam. Mevelli Publishers.

Senkoro, F. E. M. K.(2011). Fasihi. Dar es Salaam,  KAUTU Limited.






No comments:

Post a Comment