- Wanachuana kubaki katika orodha 10 bora ya wasanii wanaofuatiliwa zaidi Youtube.
- Ndani ya mwezi mmoja, wote wawili wametoa nyimbo mbili kila mmoja.
- Diamond anashika nafasi ya kwanza akifuatiwa na Harmonise katika nafasi ya pili.
Dar es Salaam. Kuteka masikio ya mashabiki wa muziki, kila wimbo unapotoka, ni ndoto ya kila msanii wa muziki.
Wanamuziki wamekuwa wakitumia mtandao wa YouTube kama jukwaa muhimu la kuwafikia mashabiki wao maeneo mbalimbali duniani kwa nyimbo zilizo kwenye mfumo wa sauti na video.
Mtandao huo, una kipengele cha “YouTube Charts” ambacho kinawapanga wanamuziki kwa umaarufu wa kazi zao kulingana na kasi ya kutafutwa na watu kwa kipindi husika.
Hadi kufikia mchana wa leo (Desemba 3, 2019), chati ya mtandao huo kwa wasanii wa Tanzania, inaongozwa na Naseeb Abdul maarufu kama Diamond Platnumz katika nafasi ya kwanza akichuana na vikali na Rajab Kahali anayefahamika zaidi kama Harmonize ambaye anashika nafasi ya pili.
Wasanii hao wawili wote kwa pamoja wanaunda orodha ya dhahabu ya 10 bora ya wasanii wa muziki wanaofuatiliwa zaidi katika mtandao wa Youtube akiwemo Rayvanny katika nafasi ya tatu, Aslay (4), Jux (5) na InnosB katika nafasi ya sita.
Wengine wanaofunga 10 bora ni Ali kiba aliyeshika nafasi ya saba, Mbosso (8), Lava Lava (9) na Nandy ambaye ameshika nafasi ya kumi.

Kwa nini Diamond Platnumz na Harmonize?
Ushindani wa wawili hao katika nafasi za juu ambao awali walikuwa katika lebo moja ya Wasafi kabla ya kutengena, huenda ni matokeo ya kuachilia nyimbo zao hivi karibuni.
Diamond amefanikiwa kuingiza nyimbo mbili Youtube zenye maudhui ya video ambazo zote ziko kwenye orodha ya nyimbo 10 zilizotazamwa zaidi.
Wimbo wake wa Sound unashikilia nafasi ya kwanza ukiwa umejizolea watazamaji 1.9 milioni hadi kufikia Disemba 3, 2019 saa 9:40 alasiri.
Wimbo wa pili ni Baba Lao ambao umeshika nafasi ya nne kwenye orodha hiyo ya nyimbo zinazowika zaidi nchini Tanzania baada ya kuutoa Novemba 8, 2019 huku ukijizolea watazamaji 6.5 milioni hadi kufikia leo mchana.
Wakati Diamond akiingiza nyimbo mbili, mwenzake Harmonize ameingiza nyimbo mbili pia zote zina maudhui ya video. Wimbo wake wa Kushoto kulia wenye watazamaji 462,828 uliotolewa jana Disemba 2, 2019 umeshika nafasi ya tano.
Audio (sauti) ya wimbo huo huo uliotolewa Novemba 20, umejizolea wasikilizaji 860,810 na kushika nafasi ya saba kwenye nyimbo za sauti 10 bora zilizosikilizwa zaidi.
Wimbo wake mwingine wa Uno alioutoa Novemba 4, 2019 nao umeingia kwenye orodha ya video 10 zilizotazamwa zaidi YouTube.
Mbali na Diamond na harmonize, wasanii wengine wenye nyimbo zenye mfumo wa video zilizotazamwa zaidi ni pamoja na Sugua yake Jux, I love You ya Rayvanny na Moyo Kiburi ya Aslay
Zaidi, video zingine zinazofanya vizuri ni pamoja na mshumaa ya Ali Kiba na wimbo wa injili wa Mkono wa bwana yao Zabron singers.
Kasi ya Diamond na Harmonize kutoa nyimbo mfululizo na kutengana kwao huenda kumezidi kuwaweka kileleni kila wakati, kwa sababu watu wengi wanawafuatili kujua kitu gani kinaendelea kati yao.