KWA mujibu wa tovuti ya WhatsApp, hadi kufikia Februari 1, 2020, programu ya WhatsApp itakuwa inafanya kazi kwenye simu za iPhone zenye mfumo wa iOS kuanzia iOS 9 na kuendelea. Simu zote za Apple zenye kutumia mfumo wa iOS 8 na kushuka chini zote hazitokuwa na uwezo wa kutumia programu hiyo hadi kufika kipindi hicho.
Mbali na hayo, watumiaji wenye simu zenye mfumo wa iOS ambao umebadilishwa kwa namna yoyote yaani (jailbroken), nao pia hawatoweza kutumia programu ya WhatsApp kwa asilimia 100 kama hapo awali.
WhatsApp imebainisha kuwa haizuii simu za namna hiyo kutumia programu yake bali programu hiyo haitoweza kufanya kazi kwa asilimia 100 au kwa maneno mengine ni kwamba inaweza kufanya kazi au inaweza isifanye kazi.
Kwa watumiaji wa mfumo wa Android na mifumo mengine kama Window Phone, WhatsApp imebainisha kuwa hadi kufikia mwezi wa kumi na mbili mwaka huu 2019, WhatsApp itasitisha kabisa upatikanaji wa programu yake kwenye simu za Windows Phone na pia kwenye simu zenye mfumo wa Android 2.3 (Gingerbread) nazo hazitoweza kufanya kazi kufikia wakati kipindi hicho.